HOTUBA YA WAZIRI WA AFYA MHESHIMIWA ANNA MARGARETH ABDALLAH, MBUNGE, KUHUSU MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2002/2003

 

 

UTANGULIZI

 

1.     Mheshimiwa Spika, kutokana na taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kisekta inayohusu Wizara yangu, naomba kutoa hoja kwamba sasa Bunge likubali kupitisha makadirio ya matumizi ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha wa 2002/2003.

 

2.     Mheshimiwa Spika, naomba nianze hotuba yangu kwa kutoa pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa, kwa kusimamia vizuri na kwa ushupavu mkubwa, hatua mbalimbali zilizowezesha vyama vya CCM na CUF kufikia muafaka. Mfarakano mkubwa baina ya vyama hivyo, uliojitokeza baada ya uchaguzi wa mwezi Oktoba 2000, ulikuwa ni tishio kwa amani na mustakabali wa taifa letu. Hivyo Watanzania wote tuna kila sababu ya kujivunia makubaliano ya muafaka kati ya CCM na CUF.

 

3.     Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii pia kuwapongeza kwa dhati wale wote ambao katika kipindi cha kuanzia mwezi Agosti 2001 hadi leo wameteuliwa kushika nafasi mbalimbali za uongozi wa juu wa taifa letu. Hao ni Mheshimiwa Dr. Ali Mohamed Shein, aliyeteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Mheshimiwa Dk. Juma Ngasongwa, Mb. Waziri wa Biashara na Viwanda na Mheshimiwa Ritha Mlaki, Mb. Naibu Waziri wa Biashara na Viwanda. Hali kadhalika nawapongeza  Mheshimiwa Masumbuko Lamwai na Mheshimiwa Hamad Rashid Mohamed, kwa kuteuliwa kwao na Mheshimiwa Rais kuwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano la Tanzania.

 

4.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/2002, Bunge lako Tukufu limewapoteza Wabunge wafuatao; Mhe. John Mangwangwa - Mbunge wa Mpanda Kati na Mhe. Sebastian Kinyondo - Mbunge wa Bukoba Vijijini. Mwenyezi Mungu aziweke roho zao mahali pema peponi.  Amin. Hali kadhalika katika kipindi hiki taifa lilipata majanga makuu mbalimbali; ajali mbaya ya gari moshi (treni) iliyotokea tarehe 24/6/02 kati ya vituo vya reli vya Igandu na Msagani ambapo Watanzania zaidi ya 286 walipoteza maisha na wengine zaidi 800 walijeruhiwa.   Pia ajali mbaya ya basi lililopinduka katika barabara ya Iringa ambapo watu takribani 38 walipoteza maisha, ajali ya basi katika barabara ya Songea Makambako iliyosababisha vifo vya watu 37,  ajali ya kuzama kwa kivuko cha mto Kilombero ambapo inahofiwa kuwa watu zaidi ya 30 walipoteza maisha yao, ajali ya wanamichezo iliyotokea huko Kikatiti - Arusha ambapo watu kumi walipoteza maisha na ajali iliyotokea katika machimbo ya madini huko Mererani ambapo inakadiriwa kuwa watu 40 wamepoteza maisha yao. Tunamwomba Mwenyezi Mungu aziweke mahali pema peponi roho za marehemu wote. Natoa pole nyingi kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu hao.

 

Kwa niaba ya serikali na kwa niaba yangu mwenyewe natoa shukrani za dhati kwa wale wote walioshiriki katika uokoaji wa majeruhi, uopoaji  na uhifadhi wa maiti katika ajali zote zilizotokea hapa nchini. Hatua makini na za haraka katika ajali zinasaidia sana kuponya maisha. Napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza waganga na wauguzi katika hospitali zote zinazopokea majeruhi wa ajali kwa kufanya kazi nzuri sana, pia wapiganaji wa Majeshi yetu yote ya Ulinzi na Usalama, pamoja na wananchi ambao walijitokeza kuwaokoa majeruhi, na kuwasitiri marehemu, pia waliojitolea damu, chakula, maji, mavazi na dawa kwa waliopatwa na ajali.  Nawashukuru wote kwa niaba ya Serikali kwa upendo mkubwa waliouonyesha kwa wenzetu waliofikwa na majanga haya.

 

5.     Mheshimiwa Spika, niruhusu nitoe shukrani zangu kwa Kamati ya Kisekta ya Huduma za Jamii ya Bunge lako Tukufu chini ya uenyekiti wake Mheshimiwa  Omar S. Kwaang, Mbunge wa Babati Mashariki kwa maelekezo yao na kwa ushauri mbali mbali walioutoa ambao ulisadia sana kukamilisha bajeti ya Wizara ya Afya.  Ushauri na maelekezo ya Kamati hii yamekuwa dira muhimu iliyowezesha kutoa mwelekeo sahihi.

 

6.     Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Bima ya Afya ni jambo lililozua mjadala miongoni mwa watumishi na vyombo vya habari kuanzia makato yalipoanza kufanyika katika mishahara ya watumishi wa Serikali mwezi Julai 2001, kwa mujibu wa Sheria Na.8 ya mwaka 1999. Wako walioshangilia kuwa Mfuko ni hatua muhimu ya kimaendeleo na wale walioona kuwa haiwasaidii kuwemo katika utaratibu huu.  Kwa sehemu kubwa hali hii ilisababishwa na matatizo makuu mawili. Tatizo la kwanza lilikuwa ni kukosekana kwa elimu ya kutosha miongoni mwa wadau juu ya dhana, umuhimu na madhumuni ya Bima na la pili ni kutokamilishwa kwa usajili wa hospitali, vituo vya afya na zahanati za kutoa huduma kwa wanachama. Mapungufu haya sasa yamerekebishwa. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei 2002 watendaji wakuu wa Mfuko wa Bima ya Afya walikuwa wametembelea mikoa yote kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu Bima na wamechukua hatua madhubuti kukamilisha usajili wa hospitali, na vituo vya matibabu vyenye sifa ya kutoa huduma kwa wanachama wa Mfuko. Baada ya kufanikisha hatua hizo watumishi wa Serikali wameanza kutambua manufaa makubwa ya Mfuko ambayo ni pamoja na:

 

·        Familia kupata huduma bora za matibabu bila kuzilipia papo kwa papo.

 

·        Serikali kuchangia asilimia tatu ya mshahara wa mtumishi kila mwezi kwa matibabu ya kila mwanachama na familia yake ya watu wasiozidi 6.

 

·        Huduma za vituo vya matibabu kuimarika kutokana na malipo ya Bima baada ya kuwahudumia wanachama.

 

     Wizara ya Afya inapenda kurudia wito wake kwa viongozi wa sehemu za kazi, wanachama na vyama huru vya wafanyakazi kuwa Bima ya Afya kwa hakika ni ukombozi kwa watumishi wa Serikali.

 

7.     Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2001/2002 viongozi wa Wizara ya Afya wameendeleza kwa nguvu vita dhidi ya rushwa katika vituo vya kutolea huduma za matibabu na sehemu nyingine za kazi. Hatua muhimu zilizochukuliwa ni pamoja na:

·        Kuwaagiza wakuu wa sehemu za kazi wasimamie kikamilifu watumishi kuvaa vitambulisho wakati wote wawapo kazini.

 

·        Kuendelea kuwakumbusha wananchi kupitia vyombo vya habari kuhusu haki zao na jinsi haki hizo zinavyoweza kuathirika kutokana na kutoa au kupokea rushwa.

 

·         Kuendelea kuwakumbusha wataalam na watumishi wengine wa afya, kwa njia za mikutano, mabango na vipeperushi, kuwa kudai rushwa ni tabia mbaya ya mtu binafsi na kamwe haihusiani na udogo wa mishahara au upungufu wa vitendea kazi. Walikumbushwa pia kwamba  Serikali haitasita kutoa adhabu kali kwa yeyote atakayedhihirika kuvunja maadili kwa njia hiyo.

 

     Ni matumaini yetu kwamba juhudi hizi zikiendelezwa bila kupunguza msisitizo au kasi yake wananchi wataanza kuona mabadiliko katika sekta hii nyeti hivi karibuni.

 

8.     Mheshimiwa Spika, ugonjwa wa malaria umeendelea kuwa tishio kwa maisha. Ningependa kurudia kuwakumbusha wananchi na Bunge lako Tukufu kuwa  inakadiriwa Watanzania takribani 100,000 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na ugonjwa wa malaria. Hali kadhalika, takwimu zinaonyesha kuwa malaria inaongoza kwa wagonjwa wa kulazwa, katika vituo vya matibabu ikiwa ni asilimia 54 kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano na asilimia 35 kwa watu wazima. Kinachosikitisha ni kuwa ugonjwa huu unaweza kuzuilika iwapo mambo muhimu yafuatayo yatazingatiwa:

 

·        Kila kaya itasafisha maeneo ya makazi yake na kufukia au kuondoa maji  yaliyotuama katika mifereji na karo.

 

·        Kila familia itatumia vyandarua vilivyotiwa dawa ya kuua mbu.

 

·        Kila Jiji, mji na manispaa itahakikisha kuwa nyumba zinajengwa kulingana na mpango uliotayarishwa ili kuepuka misongamano ya nyumba zisizofikika kwa huduma (squatter homes) na pia inakarabati mifereji yote ya maji taka.

 

Serikali kwa upande wake inaendelea kuchukua hatua madhubuti zikiwa ni pamoja na kuukamilisha Mpango Kamambe wa Udhibiti wa Malaria ambao utaanza kutekelezwa mwaka 2002/03, kuondoa kodi katika vyandarua na kutoa elimu ya afya kwa wananchi juu ya kutambua dalili za malaria na tiba sahihi.

 

MAPITIO YA MWAKA 2001/2002

MIPANGO YA MAENDELEO

 

9.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/2002 Wizara ya Afya ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 40.505 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika sekta ya afya.   Kati ya fedha hiyo, jumla ya shilingi bilioni 3.245  ilitolewa na Serikali ya Tanzania shilingi bilioni 37.260 ilitoka Mfuko wa Pamoja (Health Basket Fund) unaochangiwa na wahisani kutoka nchi marafiki.  Fedha hiyo ilitumika kutekeleza miradi ifuatayo:-

 

·        Kuimarisha uendeshaji wa upangaji mipango katika Sekta ya Afya.

·        Programu ya Kuimarishaa Afya (HSPS II).

·        Kuimarisha Hospitali za Taifa.

·        Kuimarisha Huduma za X-ray.

·        Ukarabati wa vyuo 17 vya afya.

·        Ukarabati na Ujenzi wa Hospitali za Muhimbili, Taasisi ya Mifupa (MOI) na Taasisi ya Saratani (Ocean Road Cancer Institute).

·        Ukarabati wa Majengo ya Mkemia Mkuu wa Serikali.

·        Udhibiti wa Magonjwa ya Kumabukiza.

·        Ukarabati wa majengo yaTaasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu.

·        Mpango wa Maendeleo wa Kisekta (HSDP).

·        Ukarabati wa majengo ya Taasisi ya Chakula na Lishe.

·        Ukarabati wa majengo ya Tume ya Udhibiti wa Vyakula (TUKUTA).

·        Kuimarisha utendaji katika vyuo vya afya.

 

UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU 2001/2002

 

HUDUMA ZA KINGA

 

Udhibiti wa Magonjwa ya Kuambukiza (Epidemiologia).

 

10. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2001/2002 tatizo la magonjwa ya milipuko limeendelea kuwepo ingawaje takwimu zimeonyesha unafuu wa kiasi, kwa mfano, kwa upande wa ugonjwa wa kipindupindu mwaka 2000/2001 wagonjwa walikuwa 4,637 ikilinganishwa na mwaka 2001/2002 ambapo wagonjwa walikuwa 2,154.  Hii inaonyesha nafuu ya takribani asilimia 53.5.  Hali kadhalika, kwa upande wa vifo vilivyotokana na kipindupindu, mwaka juzi kulikuwa na vifo 153 wakati mwaka jana vifo vilikuwa 87, ambayo ni nafuu ya karibu asilimia 43.  Hata hivyo Wizara inarudia kusisitiza kuwa juhudi kubwa zinahitajika ili kutokomeza tatizo la milipuko ya magonjwa.

 

11. Mheshimiwa Spika, kuhusu ugonjwa wa tauni bado milipuko imeendelea kutokea wilayani Lushoto.  Katika kipindi cha mwaka 2001/2002 jumla ya watu 21 waliugua ugonjwa huu na kati yao 5 walifariki dunia. Uchunguzi wa kitaalam uliofanyika umeonyesha kuwa mlipuko uliotokea 2001/2002 uliwaathiri zaidi watoto wa umri kati ya miaka mitano hadi kumi.  Hii inaonyesha kuwa juhudi za ziada zinahitajika kukabili tatizo hilo.

 

12.Mheshimiwa  Spika,   Wizara    ya   Afya   imeendelea

kuchukua tahadhari kuhakikisha kuwa ugonjwa wa Ebola, ulioathiri nchi jirani, hauingii hapa kwetu.  Vituo vyote vya mipakani vilihimizwa kufuatilia magonjwa yote ya kuambukiza kama tahadhari ya kuzuia kuzuka kwa ugonjwa wa Ebola.  Hali kadhalika Elimu ya Afya juu ya kinga ya kuenea magonjwa ya milipuko ilipewa umuhimu mkubwa katika maeneo ya mpakani.

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Malaria

 

13.Mheshimiwa   Spika, Wizara   yangu   imekuwa

ikifanya  jitihada mbalimbali dhidi ya ugonjwa wa malaria ambao bado ni tishio kubwa kwa afya na maisha ya Watanzania.  Katika kipindi cha mwaka 2001/2002, Wizara ya Afya ilitekeleza majukumu yafuatayo:-.

 

·        Tiba sahihi kwa Wagonjwa wa Malaria

 

Kuanzia mwezi Agosti 2001 Wizara ilianza utekelezaji wa Mwongozo mpya wa matibabu ya ugonjwa wa Malaria.  Katika mwongozo huu mpya, dawa ya Sulphadoxine – Pyrimethamine (SP) ilianza kutumika rasmi kama dawa ya safu ya kwanza ya kutibu malaria badala ya dawa ya Klorokwini.  Kwa takribani mwaka mmoja sasa tangu dawa hii ianze kutumika kwa wingi, kulingana na taarifa tunazopokea kutoka kwa watoa huduma na wagonjwa, kuwa dawa hii imeonyesha kuwadhuru baadhi ya wagonjwa. Wagonjwa hao ni wale wanaodhurika na kemikali ya sulphur ambayo ipo katika dawa hiyo. Wizara inafanya uchunguzi wa kiwango cha madhara hayo iwapo yapo katika kiwango cha kawaida cha madhara yanayotokana na matumizi ya dawa za aina nyingine. Iwapo itathibitika kuwa kiwango hicho ni kikubwa kuliko ilivyo kwa dawa nyinginezo, Wizara itachukua uamuzi wa kuibadilisha dawa hiyo.  Aidha matumizi ya dawa hii yamewasaidia wagonjwa wa malaria kupona mapema kuliko hapo awali wakati dawa ya Klorokwini ilipokuwa ikitumika.

 

·        Mafunzo

 

Katika kipindi hicho, Wizara yangu imetoa mafunzo ya rejea kwa Waganga, Wauguzi na Mafundi Sanifu Maabara kuhusu tiba sahihi ya malaria.  Jumla ya Watumishi wa Afya 176 kutoka Wilaya zote nchini walipata mafunzo hayo. Watumishi hawa wanategemewa kuwa walimu wa kuwafundisha wataalam wengine wanaotoka katika wilaya zao.

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma

 

14.Mheshimiwa  Spika,      pamoja   na    kuongezeka   kwa

ufanisi  wa utekelezaji  wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu bado idadi ya wagonjwa inaendelea kuongezeka kutoka wagonjwa 54,000 mwaka 2000 hadi kufikia wagonjwa 60,000 mwaka 2001.  Hili ni ongezeko la karibu asilimia 10.  Hii inaashiria kwamba bado kuna idadi kubwa ya wagonjwa wa Kifua Kikuu katika jamii. Kwa upande mwingine ongezeko hilo lina uhusiano mkubwa na kuenea kwa ugonjwa wa UKIMWI.

 

15.Mheshimiwa  Spika,    katika    kikao   cha   Bunge     la 

bajeti  mwaka 2001/2002, Wizara ya Afya iliahidi kutekeleza mpango maalum wa kudhibiti Kifua Kikuu hususan katika miji mikubwa ikiwemo Dar es salaam,  Mwanza na Mbeya.  Katika jiji la Dar es salaam, vituo vipya 7 vya kuchunguza wagonjwa wa Kifua Kikuu vimefunguliwa na hivyo kuongeza uwezo wa jiji wa kuchunguza wagonjwa wa Kifua Kikuu na kupunguza msongamano wa wagonjwa.   Kwa upande wa Mwanza tayari jiji hilo limeshagawanywa katika sehemu tatu na waratibu wapya wawili waliteuliwa kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma na tayari wameshaanza kazi.  Tathimini ya kuongeza vituo vipya vitakavyotoa huduma ya kudhibiti Kifua Kikuu imefanyika. Mategemeo ni kuongeza angalau vituo vipya vinane.  Hii itaongeza uwezo wa serikali wa kutoa huduma hii muhimu na hivyo kupunguza usumbufu kwa wananchi ikiwemo kusafiri mwendo mrefu kupata huduma hizo.  Aidha mawasiliano ya awali katika kupanua huduma hizo yameanza katika mikoa ya Arusha na Mbeya.

 

16.Mheshimiwa  Spika,     Kuhusu   ugonjwa   wa   Ukoma,  

takwimu zinaonyesha kwamba ugonjwa huu unazidi kupungua.  Kwa mfano mwaka 2000 kulikuwa na wagonjwa wapya 5,200 na mwaka 2001 kulikuwa  na wagonjwa wapya 4,743.  Hii inaonyesha kupungua kwa wagonjwa wapya kwa asilimia 9.  Licha ya kuwa  ugonjwa huu unapungua, lakini karibu asilimia 15 ya wagonjwa  hao wana ulemavu wa kudumu.  Ulemavu huo unajionesha katika upotevu wa baadhi ya viungo vikiwemo vidole vya miguu, mikono au sehemu nyingine za mwili.  Hivyo basi wagonjwa  hawa wanahitaji msaada wa matibabu na huduma nyingine za kijamii kwa maisha yao yote.  Pamoja na mafanikio hayo, takwimu zinadhihirisha wazi kuwa Tanzania haitaweza kufikia kiwango cha kimataifa cha kutokomeza ugonjwa wa Ukoma duniani ifikapo mwaka 2005.  Jitihada zaidi zitaongezwa za kuhamasisha wananchi wenye dalili za ugonjwa wa Ukoma wajitokeze haraka ili kupata matibabu ambayo hutolewa bila malipo katika vituo vya kutolea huduma.

 

17.Mheshimiwa  Spika,   katika   kipindi   cha   2001/2002

Wizara iliahidi kutekeleza Kampeni maalum ya kutokomeza Ukoma katika mikoa ya Tanga na Pwani.  Napenda kulieleza  Bunge lako tukufu kuwa kampeni hizo zimeanza kutekelezwa katika mikoa hiyo na kupanuliwa  katika mikoa mingine miwili zaidi ya Lindi na Kagera.  Matokeo ya kampeni hizo yatatolewa hapa Bungeni katika kipndi cha 2003/2004.

 

 

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI

 

18. Mheshimiwa Spika, ugonjwa wa UKIMWI ni miongoni mwa magonjwa yanayoongoza kwa kusababisha vifo vingi.   Wakati takwimu kwa ujumla zinaonyesha kuwepo viwango vya juu vya maambukizi ya virusi vya UKIMWI, kuna dalili kuwa katika baadhi ya mikoa hapa nchini ishara za awali za mafanikio zimeanza kuonekana.

 

19. Mheshimiwa Spika, katika ufuatiliaji wa idadi ya wagonjwa wa UKIMWI, Mkoani Mbeya kwa kipindi cha Oktoba hadi Desemba 2001, takwimu zifuatazo zimejitokeza.  Matokeo ya tafiti kwa rika zote kwa mwaka 2001/02 yalionesha kuwa asilimia 11.9 wameambukizwa virusi vya UKIMWI ukilinganisha na asilimia 20.3 mwaka 1994/95.  Mchanganuo zaidi wa vipimo hivi ni kama ifuatavyo:

 

a.       Sehemu za mijini – Asilimia 17.0 kwa mwaka

2001 ikilinganishwa na asilimia 20.7 mwaka 1994/95.

 

b.     Sehemu za kando kando ya barabara kuu – Asilimia 9.8 mwaka 2001 ikilinganishwa na 25.6 mwaka 1994/95.

 

c.     Sehemu za mipakani – Asilimia 18.3 mwaka 2001 ikilinganishwa na asilimia 33.8 mwaka 1994/95.

 

20. Mheshimiwa Spika, hali ya maambukizi kwa vijana wenye umri wa miaka 15 –24 yanatoa matumaini zaidi.  Kwa ujumla viwango katika kundi hili vimeshuka hadi wastani wa asilimia 11.75 mwaka 2001 kutoka asilimia 20.6 mwaka 1994/95.  Mabadiliko ya kushuka kwa viwango miongoni mwa vijana sehemu za vijijini, kando kando ya barabara kuu na sehemu za mipakani ni kama ifuatavyo:-

 

·        Vijijini – Asilimia 4.7 mwaka 2001 ikilinganishwa na asilimia 15.6 mwaka 1994/95.

 

·        Kando kando ya barabara kuu – Asilimia 7.5 mwaka 2001 ikilinganishwa na asilimia 26.5 mwaka 1994/95.

 

·        Vituo vya mipakani – Asilimia 19.5 mwaka 2001 ikilinganishwa na 36.1 mwaka 1994/95.

 

21. Mheshimiwa Spika, nimetoa takwimu hizi kwa nia ya kusisitiza jambo moja kwamba UKIMWI unaweza kudhibitiwa.  Mambo yaliyopelekea kushuka kwa viwango hivyo nilivyovitaja mkoani Mbeya ni wananchi kutumia kikamilifu huduma zitolewazo kwa ajili ya udhibiti wa ugonjwa wa UKIMWI.  Huduma hizo ni pamoja na upimaji, tiba ya magonjwa ya zinaa, matumizi ya kondomu, dawa za kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, usalama wa damu na elimu ya kubadili tabia za vijana kutofanya ngono mpaka wakati wanapooa au kuolewa na kuwa mwaminifu kwa mwenza.  Changamoto kwa taifa letu sasa ni kuinua upatikanaji wa huduma hizi nchini kote na kuwashawishi wananchi kuzitumia kwa ukamilifu.   Kutokana na mwelekeo huu, ninapenda kuwahakikishia Watanzania wote kuwa tukiamua tunaweza kudhibiti janga la kuenea kwa UKIMWI ikiwa kila Mtanzania atachukua hatua za dhati za kujikinga.

 

22. Mheshimiwa Spika,   upatikanaji  wa dawa za kurefusha

maisha ya waathirika wa virusi vya UKIMWI ni mkakati sahihi kabisa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI. Kwa mantiki hiyo, Wizara ya Afya sasa  imesajili madawa aina kumi yanayoongezea maisha watu wenye virusi vya UKIMWI.  Madawa yaliyosajiliwa ni: Nevirapine Stavudine, Lamivudine, Efavirenz, Nelfinavir, Zakitabine, proguanil HCL, Zidovudine, Abacavir na Delavirdine mesylate.  Madawa haya yamesajiliwa na Kampuni sita za Madawa ambazo ni Baehriinger Ingelhein Pharma KG, Bristol Myers Squibb, Cipla, Dupont,  Merck na Haffman, la Roche na Glaxo- Smithkline.  Aidha, katika jitihada za kuimarisha utaratibu huu, shughuli zifuatazo zimefanyika:

 

·        Wizara imeandaa utaratibu utakaowezesha waathirika wa virusi vya UKIMWI kupata taarifa juu ya matumizi ya madawa ya kurefusha maisha.

 

·        Hospitali zote za rufaa zimepatiwa machine za kupima chembechembe hai za CD4 ambacho ni kipimo muhimu katika matumizi ya madawa ya UKIMWI.  Kipimo cha CD4 ni lazima kifanyike kuweza kufahamu wakati wa kuanza matibabu na baadaye hutoa dira ya maendeleo ya matibabu.

 

·        Mwongozo wa kuwahudumia wagonjwa wa UKIMWI, hususan matumizi ya madawa ya UKIMWI umeandaliwa na utasambazwa kwa watumishi wa afya nchini kote.

 

 

 

Mpango wa Taifa wa Kuzuia ugonjwa wa vikope

(trachoma) na usubi (River blindness or onchocerciasis)

 

23. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/2002 Wizara ya Afya imeweza kutoa tiba ya ugonjwa wa vikope ( trachoma), katika mikoa yenye ugonjwa huo, kwa kutumia dawa ya zithromax.  Dawa hizo zilitolewa katika  wilaya 9  za mikoa ya Dodoma, Singida, Morogoro, Iringa na Kilimanjaro ambapo watu 310,671 walitibiwa.  Hii ni moja ya juhudi za kitaifa na kimataifa za kutokomeza ugonjwa wa vikope ulimwenguni ifikapo mwaka 2020. Aidha Mpango wa kudhibiti ugonjwa wa usubi kitaifa ulizindua miradi mipya ambayo ni Kilosa Focus na Tunduru Focus katika kipindi cha mwaka 2001/2002 na kufanya idadi ya watu waliyopewa dawa ya Mectizan kufikia 624,290 katika vijiji 468, ikilinganishwa na watu 338,886 waliotibiwa mwaka 2000/2001.

 

Huduma za Afya ya Uzazi Mama na Mtoto

 

24. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2001/2002 Wizara iliendesha mafunzo kwa walengwa wafuatao:

 

·        Watoa Huduma za Afya ya Uzazi na Mtoto 52 kutoka wilaya za Rukwa Singida na Lindi.

 

·        Wakufunzi wa Wakunga wa Jadi 18 toka katika wilaya za Tabora na Kigoma.

 

·        Timu za utoaji huduma za afya ngazi ya mkoa na wilaya toka Wilaya zote za mikoa ya Dodoma, Singida, Mwanza na Mara.

 

Sambamba na mafunzo hayo Wizara pia ilisambaza kadi za Huduma za Mama na Mtoto (MCH 1, 4 na 5), dawa na vifaa vya uzazi wa mpango katika vituo vyote vya kutolea huduma.

 

Mpango wa Taifa wa Chanjo

 

25. Mheshimiwa Spika, Mpango wa Taifa wa Chanjo umeendelea kutoa chanjo kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano na mama wajawazito. Mwaka 2001/2002 Wizara ya Afya iliendesha zoezi maalum la chanjo ya Polio kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano katika wilaya 16 na kupata mafanikio ya asilimia 100 kwa mzunguko wa awamu ya kwanza na ya pili.  Sambamba na zoezi hilo maalum la chanjo ya Polio, Wizara pia iliendesha Kampeni ya chanjo ya Surua kwa watoto wenye umri kati ya miezi tisa hadi miaka 15 katika wilaya 31 na kupata pia mafanikio kwa asilimia 100.  Ninachukua nafasi hii kutoa shukrani za dhati kwa Halmashauri, Wahisani, Taasisi na Mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali, Mashirika ya kimataifa, na Waheshimiwa Wabunge kwa kushiriki kikamilifu katika kufanikisha kampeni hizi.Wakati huo huo shughuli za kawaida za chanjo ziliendelea katika vituo vyote nchini ambapo wastani wa asilimia 87  ya walengwa walichanjwa.

 

26. Mheshimiwa Spika katika  mwaka 2001 Wizara yangu iliweza kufunga majokofu yatumiayo mionzi ya jua 29 Mkoa wa Tabora na 51 Mkoa wa Kigoma.  Pia imefanikiwa kubadilisha majokofu yanayotumia mafuta ya taa na kuanza kutumia gesi katika mikoa sita ya Tanga, Mtwara, Dodoma, Morogoro, Pwani na Lindi. Hali kadhalika, kuanzia mwezi Januari 2002 tulipozindua chanjo ya ugonjwa wa homa ya ini (Hepatitis B), tulizindua mpango wa kutumia mabomba ya sindano maalum yanayotumika mara moja tu, kwa ajili ya kuimarisha na kuboresha utoaji sindano salama wa chanjo zote nchini. Aidha Vituo vyote vinatumia vikasha maalum (safety boxes) kwa ajili ya kukusanyia mabomba na sindano zilizotumika.  Wizara yangu pia imejenga matanuru nane ya kuchomea taka (medical incinerators) katika Hospitali za Rufaa za Muhimbili na Mbeya, Hospitali za Wilaya za Bagamoyo, Korogwe, Kilombero,  na Kondoa, na vituo vya afya vya Morogoro Mjini na Ngerengere. Wizara ina mpango wa kujenga matanuru haya katika Hospitali zote za Wilaya, Vituo vya Afya na Zahanati zote nchini.

 

Huduma za Elimu ya Afya kwa Umma.

 

27.  Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya imeendelea kutoa elimu ya afya kwa wananchi kuhusu kubadilisha mitindo ya maisha na mienendo ili kujenga jamii yenye siha nzuri na uwezo wa kuchangia kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii.   Wizara ya Afya imeendelea kutayarisha vipindi mbalimbali vinavyotangazwa katika magazeti, redio na televisheni.  Mwaka uliopita niliahidi kuwa Wizara yangu itaandaa mpango wa miaka mitano wa mawasiliano ya Elimu ya afya na mwongozo wa utoaji huduma hizo hapa nchini.  Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa mpango huo umekamilika na mwongozo utasambazwa kwa wahusika katika kipindi cha mwaka 2002/03.

 

Afya ya Mazingira

 

28. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya inatilia maanani umuhimu wa usafi wa mazingira katika uimarishaji wa afya ya jamii.  Katika kipindi cha 2001/2002 Wizara imetayarisha miongozo miwili inayotoa dira ya uimarishaji wa afya ya mazingira nchini.  Miongozo hiyo ni Mwongozo wa Udhibiti wa Taka na Mwongozo wa Sera ya Afya na Usafi wa Mazingira (Policy Guidelines on Environmental Health and Sanitation). Aidha Wizara kwa kutambua umuhimu wa afya bora ya wafanyakazi hasa viwandani na kwenye mashamba, iliendesha mafunzo kwa waganga wa mikoa ya Shinyanga na Mwanza.  Mafunzo hayo yalilenga katika upimaji wa afya za wafanyakazi na udhibiti wa magonjwa yatokanayo na kazi.  Mafunzo hayo yalishirikisha waganga wa mikoa ya Mwanza na Shinyanga kwa kuzingatia kuwepo kwa kazi za uzalishaji wa pamba mashambani,  viwanda vya kuchambua pamba, viwanda vya samaki na migodi katika mikoa hiyo.

 

29.     Mheshimiwa Spika, napenda kulifahamisha Bunge lako kwamba tarehe 22 – 28 Novemba 2001, Wizara ya Afya ilikuwa mwenyeji wa Kongamano la Kimataifa la Afya ya Mazingira (International Conference on Environmental Health) lililofanyika Bagamoyo.  Sambamba na Kongamano hilo, ulifanyika uzinduzi wa maktaba kubwa katika chuo cha Maafisa Afya – Muhimbili.

 

Huduma ya Bandarini, Vituo vya Mipakani na Viwanja vya Ndege.

 

30. Mheshimiwa Spika, moja ya kazi za Wizara ya Afya ni udhibiti wa afya sehemu za bandarini, viwanja vya ndege na vituo vya mipakani, ili kuhakikisha kwamba watu na bidhaa zitokazo na kuingia nchini zipo katika hali bora.  Katika kipindi cha 2001/2002 jumla ya tani 439,453 za vyakula zilikaguliwa na kuruhusiwa kuingia nchini baada ya kuonekana zinafaa kuliwa na binadamu.  Tani 487 zilionekana kuwa hazifai na hivyo ziliteketezwa.

             

Mradi wa Uimarishaji wa Huduma za Afya (MUHUMA)

(Tanzania Essential Health Interventions Project – TEHIP)

 

31. Mheshimiwa  Spika, Mradi wa Uimarishaji Huduma Muhimu za Afya (MUHUMA) ambao ni ushirikiano kati ya kituo cha kimataifa cha utafiti cha Canada (IDRC) pamoja na Wizara ya Afya unaendelea kusaidia Timu za Uendeshaji Huduma za Afya na Halmashauri za Wilaya za Morogoro Vijijini na Rufiji katika kupanga mpango wa Afya wa Wilaya, kuandaa makadirio na kutoa huduma muhimu  za afya kwa kupitia  mfumo wa Afya ya Jamii. Katika kipindi cha mwaka 2001/2002 mradi ulitumia shilingi billioni 1.6 kwa kugharamia huduma katika vituo vya afya na zahanati, kufanya utafiti na kusadia katika uimarishaji wa mipango ya afya ya halmashauri za wilaya za Rufiji na Morogoro Vijijini na kutoa mafunzo kwa watumishi wa afya.

 

HUDUMA ZA TIBA

 

Huduma ya Dawa na Vifaa vya Hospitali

 

32.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2001/2002, shilingi bilioni 14.7 zilitumika kununua na kusambaza dawa na vifaa katika zahanati, vituo vya afya na hospitali za Serikali pamoja na Hospitali Teule za Wilaya. Kati ya fedha hizo Serikali ilitoa shilingi bilioni 10.6. Mfuko wa pamoja wa Sekta ya Afya (Health Basket Fund) unaochangiwa na wahisani ulitoa shilingi bilioni 2.0. Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA) kupitia Mradi wa Kuimarisha Sekta ya Afya (Health Sector Programme Support) lilitoa shilingi bilioni 2.1. Aidha, Wizara iliendeleza mfuko wa dawa katika hospitali za wilaya, mikoa na rufaa kupitia uchangiaji wa huduma ya afya ambapo wananchi walipata unafuu wa bei katika kuzinunua dawa hizo kwa vile wanalipia nusu tu ya bei halisi ya dawa hizo (Drug Revolving Fund).

 

33.     Mheshimiwa Spika, zahanati na vituo vya afya vya Serikali viliendelea kupelekewa masanduku ya dawa (Essential Drug Kits) kila mwezi. Aidha, orodha ya dawa na vifaa iliongezeka kutoka 54 hadi 67 ili kukidhi mabadiliko ya tiba ya malaria na kukabiliana na maradhi ambayo husababisha vifo kwa watoto chini ya miaka mitano.  Ili kuboresha upatikanaji wa dawa katika zahanati na vituo vya afya,  Halmashauri zilizoanzisha Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ziliandaliwa kutekeleza mfumo wa uagizaji na usimamizi wa matumizi ya dawa na vifaa (Indent System). Halmashauri hizo ni Hanang, Igunga, Nzega, Iramba, Singida Vijijini, Iringa Vijijini, Songea Vijijini, Songea Mjini, Kilosa na Mbinga.

 

Huduma za Uchunguzi wa Magonjwa

 

34.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/2002 Wizara ya Afya ilianza maandalizi ya mkakati wa uanzishaji wa mpango wa kitaifa wa upatikanaji wa damu salama na ya kutosha kwa wagonjwa.  Maandalizi ya kuunda taasisi ya kitaifa itakayoshughulikia huduma ya upatikanaji wa damu salama yaani, National Blood Transfusion Services, yameanza kwa kufanya upembuzi yakinifu wa mahitaji ya vifaa, watumishi, miongozo na mafunzo kwa ajili ya shughuli hiyo.  Taasisi hiyo itakuwa na ofisi za kanda kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili, Hospitali za Rufaa za KCMC, Bugando na Mbeya.  Mpango wa utekelezaji wa kuanzisha huduma hii kwenye hospitali ya Rufaa ya Mbeya kwa ajili ya Kanda ya Nyanda za juu Kusini umeandaliwa.  Aidha, mwongozo wa matumizi ya damu katika utoaji huduma umeandaliwa.

 

35.     Mheshimiwa Spika, kupitia mradi wa kuimarisha huduma za uchunguzi wa wagonjwa unaogharamiwa na serikali za Tanzania na Uholanzi (ORET), Wizara ya Afya imefunga mitambo mipya ya X-ray na Ultrasound katika hospitali zilizoko katika mikoa ya Rukwa, Mbeya, Singida, Dodoma, Kilimanjaro na Arusha, hii ni awamu ya pili ya ufungaji wa vifaa hivi.  Aidha, katika awamu hii, nasikitika kuliarifu Bunge lako kuwa mitambo ya X-ray na Ultrasound ambayo imekwisha wasili, haikufungwa katika hospitali za mikoa ya Mbeya, Singida na Arusha na Hospitali za wilaya za Hanang, Babati na Chunya kwa kuwa hazikuwa na vyumba au nyumba ya x-ray, au hali ya vyumba haikukidhi viwango vinavyotakiwa ili kufungwa mashine hizo.  Viongozi wa huduma za afya katika mikoa na wilaya hizo wanahimizwa kukamilisha matayarisho hayo ili mitambo ifungwe na huduma ianze kutolewa.

 

36.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2001/2002, Wizara ya Afya imekamilisha mwongozo wa kisera juu ya vifaa vya kitaalam vya kutolea huduma za afya (Policy Guidelines for Health Care Technology).  Kupitia mwongozo huu, utaratibu wa kuchagua, kununua, kusimika na kutumia vifaa vya kitaalaam vya kutolea huduma za afya umeainishwa.  Pia mwongozo huu una lengo la kuimarisha mpango wa kuvifanyia matengenezo ya kinga (Planned Preventive Maintenance) vifaa hivi katika hospitali zote. Aidha, karakana za kanda za kutengeneza vifaa vya kitaalam vya kutolea huduma za afya zilizopo kwenye hospitali za Muhimbili, Mtwara, Mbeya, KCMC na Bugando zimeimarishwa kwa kupatiwa vifaa vya kufanyia kazi na mafunzo.  Wahandisi na mafundi 15 kutoka kwenye hospitali hizo walipewa mafunzo hayo na vifaa kupitia Mradi wa ORET.

 

Huduma ya Afya ya Kinywa na  Meno

 

37.     Mheshimiwa Spika kwa upande wa huduma za afya ya kinywa, mwaka 2001/2002 Wizara yangu imefanikiwa kuagiza vifaa kwa ajili  ya tiba ya meno kwa hospitali zifuatazo; Monduli, Kasulu, Ilala, Lindi, Mwanza, Musoma, Bukoba, Shinyanga, Magu, Dodoma na Ulanga.  Pia, madawa muhimu kwa ajili ya tiba ya meno yamenunuliwa kwa kushirikiana na Idara ya Bohari Kuu ya Dawa.  Hali kadhalika mtaala kwa ajili ya kufundishia Madaktari wa Meno Wasaidizi umefanyiwa marekebisho.

 

Huduma za Afya ya Akili na Madawa ya Kulevya

 

38.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2001/2002 Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Sheria na Mambo ya Katiba imekuwa ikiandaa mapendekezo ya muswada wa sheria ya kuboresha huduma za afya ya akili nchini. Wizara inakusudia kuwasilisha muswada huo wa sheria Bungeni katika mwaka wa fedha 2002/2003.  Aidha Wizara imeandaa vitabu vya elimu ya msingi juu ya afya ya akili kwa wafanyakazi wa afya, ambavyo vikichapishwa vitasambazwa nchi nzima.  Vitabu hivi vitasaidia kuboresha ustadi wa wataalam wa ngazi ya msingi katika kukabiliana na maradhi ya akili.

 

Hospitali za Rufaa na Taasisi za Matibabu Maalum

 

39.     Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya inasimamia utoaji huduma katika hospitali nane zinazotoa huduma za rufaa na huduma maalum za tiba.  Hospitali za rufaa ni Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Bugando, Hospitali ya KCMC na Hospitali ya Rufaa Mbeya.  Hospitali zinazotoa huduma maalumu ni Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili (Mifupa na Ajali), Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (Saratani), Hospitali ya Mirembe na Isanga (Afya ya Akili) na Hospitali ya Kibong'oto (Kifua Kikuu).  Katika mwaka wa fedha wa 2001/2002, Wizara ya Afya imezipatia hospitali hizi fedha kwa ajili ya mishahara na matumizi ya kawaida, vifaa vya kutolea huduma za afya na dawa kwa ajili ya kutoa huduma za rufaa.  Jumla ya shilingi bilioni 11.9 zilitumika katika utoaji huduma katika hospitali za rufaa na hospitali za huduma maalum.  Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 11.2 zilitolewa na Serikali na shilingi bilioni 0.7 zilitolewa na mfuko wa pamoja wa Sekta ya Afya (Health Basket Fund)  Pia Wizara ya Afya iliingia mkataba mpya wa matengenezo ya kinga kwa ajili ya mashine za CT scanner zilizopo kwenye hospitali ya Muhimbili na KCMC.  Gharama ya mkataba huo ni shilingi milioni 472.0.  Hospitali za KCMC na Muhimbili zilichangia jumla ya shilingi milioni 140.0 katika malipo ya mkataba huo.  Fedha hiyo ilitokana na matumizi ya mashine hizo, na Wizara ya Afya ililipa shilingi milioni 332.0. Aidha hospitali za watu binafsi  za Regency Medical Centre, Mikocheni Mission Hospital na Agha Khan pia zimeanza kutoa huduma hii.

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili

 

40.     Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Taifa Muhimbili imeundwa upya baada ya Bunge lako Tukufu kupitisha Sheria Na 5 ya mwaka 2000. Sheria hiyo ilitenganisha uendeshaji wa taasisi mbili zilizokuwa chini ya Shirika la Afya Muhimbili, yaani Hospitali ya Taifa na Chuo Kikuu Kishiriki cha Sayansi ya Afya.  Katika utekelezaji wa sheria hiyo Wizara iliendelea kusimamia mabadiliko ya Hospitali kwa kuunda Kamati ya Mpito (Transition Management Committee) na Baraza la Wadhamini la Hospitali.  Kamati ya Mpito imekuwa ikisimamia utekelezaji wa mgawanyo wa rasilimali na wafanyakazi kati ya Hospitali ya Taifa na Chuo Kikuu Kishiriki cha Sayansi ya Afya Muhimbili.  Kazi hii imekamilika na hivi sasa Kamati inakamilisha taarifa na mapendekezo yake ili yawasilishwe Serikalini kwa ajili ya maamuzi ya mwisho juu ya mgawanyo huo.  Napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Milton Makongoro Mahanga, Mbunge wa Ukonga, kwa kazi nzuri inayofanywa na kamati hiyo. Hali kadhalika, Baraza la Wadhamini la Hospitali ya Taifa Muhimbili chini ya Mweyekiti wake Mheshimiwa Abdulrahman Kinana, Spika wa Bunge la Afrika Mashariki limeshaanza kazi ya kushughulikia mabadiliko ya Muundo wa Hospitali pamoja na uteuzi wa Menejimenti mpya ya Hospitali.

 

41.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2000/2001 hospitali ya Taifa Muhimbili ilitumia shilingi milioni 600.0 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa ghorofa ya kwanza ya jengo la wodi ya watoto.  Pia hospitali ilifanya ukarabati wa baadhi ya majengo ya hospitali kwa kutumia fedha zitokanazo na mifuko ya kujitegemea. 

 

Hospitali ya Rufaa ya KCMC

 

42.   Mheshimiwa spika, katika mwaka 2001/2002 hospitali

ya KCMC iliendelea kutekeleza mipango yake ya utoaji wa huduma ya tiba, utoaji wa elimu na uendeshaji wa utafiti.  Wagonjwa wa kulazwa 17,421 na wagonjwa wa nje 99,747  walitibiwa katika mwaka 2001. Katika mwaka 2001/2002 Hospitali ya KCMC ilikamilisha ukarabati wa kitengo cha wagonjwa mahututi waliofanyiwa upasuaji (Surgical Intensive Care Unit) kwa gharama ya shilingi milioni 16.0 zilizotolewa na Shirika la Msamaria Mwema.  Aidha, ujenzi wa ofisi na madarasa ya Chuo Kikuu kishiriki cha Tiba cha KCMC ulikamilika mwezi wa Agosti 2001. Fedha za kugaharmia ujenzi wa jengo hilo zilitolewa na wadau wa Shirika la Msamaria Mwema.  Sambamba na ujenzi uliofanyika, hospitali ilifanya ukarabati wa bweni la wanafunzi wanaochukua mafunzo ya Madaktari Wasaidizi (Assistant Medical Officers) na Wazoesha Viungo (Physiotherapists).

 

 

 

Hospitali ya Rufaa ya Mbeya

 

43.     Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Rufaa ya Mbeya inayotoa huduma za rufaa kwa hospitali za mikoa ya Kanda ya Nyanda za juu Kusini ilipatwa na msiba mkubwa baada ya kufariki aliyekuwa Mganga Mkuu wa Hospitali Dr. Titus Nkulila.  Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi.  Amin.

 

44.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2001/2002 ufanisi wa kazi katika hospitali ya Rufaa ya Mbeya uliongezeka baada ya watumishi kutiwa moyo na Wizara kwa kukamilisha zoezi la kuwapandisha madaraja watumishi wengi kuliko miaka ya nyuma.  Pia Wizara ilitoa fedha za kulipia deni la posho za zamu ya kuitwa kazini wakati wa mapumziko (on call allowance) na posho za sare kwa maafisa wauguzi.  Aidha, ubora wa huduma za hospitali uliimarika kwa upatikanaji mzuri wa dawa kutokana na ruzuku ya serikali inayopitia Idara ya Bohari Kuu ya Dawa, mfuko wa dawa wa hospitali (Drug Revolving Fund) na mpango wa uchangiaji wa huduma za Afya (Cost Sharing Fund).  Kuanzia Machi 2002, hospitali ilianza kutoa huduma kwa watumishi wote wa idara za serikali kupitia mpango wa Bima ya Afya.  Uongozi wa hospitali umeamua kusimamia kikamilifu zoezi hili ili kuhakikisha kuwa wateja wanapata huduma bora na kwa haraka.  Aidha, hospitali imekamilisha ukarabati wa wodi mbili, mitambo ya hospitali na vifaa vya kitaalam. Ukarabati huo ulifanikiwa kutokana na kutenga shilingi milioni 38 kutoka kwenye bajeti ya serikali.  Pia, hospitali imetumia shilingi milioni 67.0 kukamilisha ukarabati wa mabweni ya madaktari walio mazoezini (Interns Hostel) na imeanza ukarabati wa hospitali ya wazazi Meta utakaogharimu shilingi milioni 53.0 na ukarabati wa wodi ya wagonjwa wa akili kwa shilingi milioni 30.0

 

45.     Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Rufaa Mbeya imekuwa mstari wa mbele katika shughuli za utafiti.  Katika mwaka 2001/2002 hospitali ya Rufaa ya Mbeya ilinufaika kwa ushirikiano wake na Chuo Kikuu cha Munich, Ujerumani, Chuo Kikuu cha Johannesburg, Afrika Kusini na Walter Reed Foundation ya Washington, Marekani.  Kupitia ushirikiano huo, hospitali ya Rufaa Mbeya iliweza kujenga ofisi na kliniki ya kufuatilia utafiti wa chanjo ya kinga ya maambukizo ya UKIMWI kwa gharama ya shilingi milioni 75.0

 

Hospitali ya Bugando

 

46.     Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Bugando yenye vitanda 820 inatoa huduma za rufaa katika Kanda ya Ziwa.  Katika mwaka uliopita hospitali hiyo imetoa huduma kwa wagonjwa 109,317.  Kati ya wagonjwa hao 83,749 walikuwa wagonjwa wa nje, hii ni sawa na wagonjwa 247 kwa kila siku. Jumla ya wagonjwa 25,568 walilazwa, hii ni sawa na wagonjwa 71 wa kulazwa kila siku.  Hospitali ya Bugando inatoa matibabu maalum ya upasuaji wa akina mama waliopata matatizo wakati wa kujifungua na kupata madhara ya njia ya mkojo (V.V.F).  Matibabu haya huendeshwa kwa msaada wa shirika la Maryknol kutoka Marekani na AMREF Tanzania, hivyo wagonjwa hawa hutibiwa bila malipo.  Huduma hii inawafikia wagonjwa wengi kutoka sehemu mbalimbali za Kanda ya Ziwa Victoria.  Mwaka uliopita walitibiwa wagonjwa wa V.V.F 220  na kupona.

 

47.     Mheshimiwa spika, Hospitali ya Bugando imeweza kuanzisha kliniki za huduma binafsi za kulipia (Private Clinics) ambazo hutoa huduma baada ya saa za kazi za kawaida.  Hii imesaidia kwa sehemu kubwa ya wataalam kubaki katika kliniki za Bugando baada ya saa za kazi kwisha, kwani kabla ya hapo madaktari na wauguzi walikuwa wakienda kutafuta au kufanya kazi mjini kwenye hospitali binafsi.

 

48.     Mheshimiwa spika, pamoja na kutoa huduma za tiba, taasisi hii vile vile inatoa mafunzo kwa wataalam wa afya katika fani zifuatazo:

 

·        Madaktari wasaidizi (AMO).

·        Wauguzi daraja la kwanza.

·        Wafamasia Wasaidizi.     

·        Fundi sanifu maabara.

·        Fundi sanifu mionzi (Radiographers).

·        Watoa dawa za usingizi.

·        Ushauri Nasaha     

 

Wizara imekubali vyuo vitoavyo mafunzo ya Famasia, Radiolojia na Maabara vianze kutoa mafunzo ya Stashahada kuanzia mwaka huu.  Pamoja na mafunzo haya ya vyuoni, Hospitali ya Bugando ina kitengo ambacho hutoa elimu kwa njia ya kujiendeleza kwa wafanyakazi wa fani mbalimbali za uganga.  Huduma hii imelenga zaidi kwa wafanyakazi ambao wako katika Kanda ya Ziwa. Masomo haya yanalengo la kuinua elimu ya wafanyakazi na vile vile ni motisha kwa wale ambao wamekaa kazini bila kujiendeleza kwa muda mrefu.

 

49      Mheshimiwa Spika,  Ili kupunguza tatizo la nyumba kwa wafanyakazi, Hospitali ya Bugando ilifanikiwa kununua nyumba 10 za ghorofa zinazoweza kukaa familia 40 zilizokuwa zinamilikiwa na kiwanda cha nguo cha Mwanza (Mwatex).  Pia taasisi ilinunua basi moja kwa ajili ya usafiri wa wafanyakazi.  Magari mawili ya huduma, yaani lori na pickup, yamefanyiwa ukarabati.

 

Taasisi ya Saratani ya Ocean Road

 

50.     Mheshimiwa Spika, Taasisi ya Saratani ya Ocean Road pamoja na ongezeko la wagonjwa na hali ngumu ya kifedha imezidi kuboresha huduma kwa wagonjwa wa Saratani nchini.  Pamoja na sera ya wananchi kuchangia huduma za afya, wagonjwa wa Saratani wamesamehewa kulipia gharama za matibabu.  Katika mwaka wa fedha uliopita, Taasisi ya Saratani ilipata mashine ya kuhakiki matibabu ya mionzi inayoitwa Simulator yenye thamani ya dola 400,000 ukiwa ni msaada kutoka Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (International Atomic Energy Agency -IAEA).  Mashine hii imeipa Taasisi uwezo wa kuhakikisha kwamba sehemu ya mwili inayotibiwa na mionzi ni ile iliyoathirika tu na hivyo kuzuia uwezekano wa kuziathiri sehemu ambazo hazina maradhi.  Pia, katika mwaka wa fedha uliopita Taasisi ilipata msaada wa vifaa vya kuboresha huduma za tiba ya mionzi (Nuclear Medicine) kutoka Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA) vyenye thamani ya dola 200,000. Vile vile, Taasisi ya Saratani imekamilsha kazi ya ukarabati wa majengo yenye vyumba vya matibabu, X-ray, Ultrasound, Nuclear Medicine, Maabara na Mapumziko ya Wagonjwa kwa kutumia shilingi milioni 100.0 ambazo zilitokana na bajeti ya Serikali.

 

Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili – MOI – (Mifupa na Ajali)

 

51. Mheshimiwa Spika katika mwaka wa fedha wa 2001/2002 , Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili iliendelea kutoa huduma za matibabu ya mifupa na magonjwa yatokanayo na ajali, kufundisha na kutafiti kuhusu matibabu ya magonjwa ya mifupa, majeruhi, mifumo ya fahamu na ubongo. Kwa kushirikiana na Chuo Kikuu Kishiriki cha Tiba, Taasisi imefanikiwa kuanzisha mafunzo ya shahada ya uzamili katika fani ya mifupa na ajali. Kozi hii ilianza oktoba 2001 ikiwa na wanachuo wanne. Imefanikiwa pia kuandaa kitabu cha Mwongozo wa Matibabu ya Magonjwa ya Mifupa, majeruhi, mfumo wa fahamu na ubongo.

 

Hospitali ya Mirembe na Taasisi ya wagonjwa wa akili ya Isanga

 

52. Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Mirembe na Taasisi ya

Isanga ni Hospitali maalum za kutoa huduma za tiba na ukarabati wa mienendo ya wagonjwa wa akili nchini.  Hospitali ya Mirembe inatoa huduma za afya ya akili kwa wagonjwa wa kawaida  na Taasisi ya Isanga inatoa huduma za afya ya akili kwa Wagonjwa waliotenda makosa ya jinai.

 

Kwa mwaka wa fedha 2001/2002 hospitali ilihudumia jumla ya wagonjwa 20,397 kati ya hao wagonjwa 2,209 walilazwa, wagonjwa 18,188 walikuwa ni wagonjwa wa nje.  Wagonjwa waliolazwa walikuwa wanashumbuliwa na magonjwa yafuatayo:-

 

·        Kuchanganyikiwa kwa kushindwa kumiliki na kutawala fikra (Schizophrenia) kwa asilimia 15 na marudio kwa asilimia 77,

·        Madawa ya kulevya asilimia 15 marudio asilimia 3,

·        Kifafa cha kuchanganyikiwa asilimia 14 marudio 11.

·        Kuchanganyikiwa kutokana na maradhi ya ubongo (Organic Brain Sydrome), asilimia 11 marudio asilimia moja (1%).

·        Kuchanganyikiwa au kusononeka kupita kiasi kunakotokana na mabadiliko makubwa ya hisia (Mania) asilimia 4, marudio asilimia 7.

·        Ugonjwa wa kifafa uliongoza kwa asilimia 70 kwa wagonjwa wa nje.

 

Mwelekeo wa magonjwa ya akili

 

Magonjwa ya akili yanakaribia kufikia kiwango cha mlipuko kwa sababu zifuatazo:

 

·        Ongezeko la matumizi ya madawa ya kulevya nchini.

·        Kutopewa uzito unaostahili katika Huduma za Afya ya Msingi kwa wagonjwa wa afya ya akili.  Wagonjwa wengi hurudiwa na ugonjwa mara baada ya matibabu na kuruhusiwa kurudi nyumbani kwa kukosa huduma inayostahili hasa upendo toka kwa ndungu na jamii inayowazunguka.

·        Ongezeko la Ugonjwa wa UKIMWI ambao sasa unaathiri afya ya akili.

·        Jamii kutojua dalili za mwanzo za magonjwa ya akili na kuyapatia tafsiri potofu, hasa imani za kishirikina.

 

Huduma kwa wagonjwa wa kawaida.

 

Pamoja na kutibu wagonjwa wenye matatizo ya afya ya akili, hospitali ya Mirembe inahudumia pia wakazi wa Manispaa ya Dodoma wanaoumwa magonjwa ya kawaida.  Ugonjwa wa malaria uliongoza kwa idadi ya wagonjwa waliolazwa kwa asilimia 52 na kwa wagonjwa wa nje kwa asilimia 40.

 

53. Mheshimiwa Spika, Katika  mwaka  2001/2002  Wizara

ilianza kufanya ukarabati wa mifumo ya maji machafu ya hospitali na kuiunganisha na mfumo wa maji machafu wa mji wa Dodoma. Aidha mfumo wa maji safi wa Taasisi ya Isanga nao ulifanyiwa pia ukarabati kwa kurekebisha mabomba na tanki la maji. Ukamilishaji wa kazi hizi unatarajiwa katika mwaka huu wa fedha 2002/2003.

 

Hospitali ya Kibong’oto

 

54. Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Kibong’oto ambayo ilikuwa inatumika kama kituo cha kuwatenga wagonjwa na kuwaweka mahali penye mazingira mazuri ya matibabu, hivi sasa bado inatoa mchango mkubwa katika tiba na utafiti wa ugonjwa wa Kifua Kikuu. Aidha hospitali hiyo pia  inahudumia wagonjwa wa kawaida. Takwimu zinaonyesha kuwa mwaka 2001/2002, Hospitali ya Kibong’oto ilitibu wagonjwa wa kifua kikuu 6,961, wakiwemo wagonjwa 810 wakulazwa na wagonjwa 6,151 wa nje. Vile vile hospitali ilitoa huduma kwa wagonjwa 3,566 wa kawaida. Kati yao wagonjwa 494 walilazwa na wagonjwa 3,072 walitibiwa na kurudi nyunbani.

 

Huduma ya Kuzuia Maambukizi ya UKIMWI Katika Hospitali za Rufaa

 

55. Mheshimiwa Spika, Hospitali zote za Rufaa hazikubaki nyuma katika kupiga vita UKIMWI na kutafuta njia za kuwasaidia waaathirika wa janga hili.  Hospitali za Rufaa za Muhimbili, KCMC, Bugando na Mbeya, na Hospitali ya Mkoa wa Kagera zilishiriki katika kuanzisha kwa majaribio ya mpango wa kuzuia maambukizi ya virusi vya UKIMWI kutoka kwa mama wajawazito walioathirika na virusi vya UKIMWI kwenda kwa watoto watakaozaliwa.  Mpango huo unagharamiwa na serikali ya Tanzania, Shirika la Umoja wa Mataifa Linalohudumia Watoto (UNICEF), Shirika la Medicins du Monde la Ufaransa na Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GTZ).  Katika mpango huo mama wajawazito hupewa ushauri nasaha juu ya UKIMWI na chaguo la kupima kama wameambukizwa virusi vya UKIMWI au la.  Wale walioambukizwa hupewa dawa za kuzuia maambukizi kwa mtoto akiwa tumboni.  Aidha huduma makini hutolewa wakati wa kujifungua ili mtoto asiambukizwe.  Kabla ya kuruhusiwa kwenda nyumbani, wazazi hupewa ushauri nasaha juu ya njia salama za kumlisha mtoto mchanga ili asiambukizwe wakati wa kunyonyesha.  Kuanzia Julai 2000 hadi Juni 2001, mpango huu umefanikiwa kuwafikia mama wajawazito 24,000. 

 

56. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio mazuri ya mpango huu, kumekuwa na matatizo katika utekelezaji wake.  Matatizo hayo ni pamoja na ushiriki mdogo wa wanaume, upungufu wa wataalam wa kutoa ushauri nasaha na wasiwasi wa kujulikana walioathirika kutokana na unyanyapaaji (stigma) ulioenea katika jamii.  Pia mpango huu unaonekana kujali kuzuia maambukizi ya mtoto lakini hauwafikii vyema akina mama baada ya kujifungua.  Vilevile, wanaonufaika na mpango huu ni mama wanaopata huduma kwenye hospitali za rufaa.  Ili kukabili matatizo haya na kurekebisha mapungufu, mpango huu utafanyiwa tathmini katika mwaka wa fedha wa 2002/2003 kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Afya, UNICEF, Axios International na Shirika la kudhibiti magonjwa (Center for Disease Control-CDC) la Marekani. Kwa madhumuni ya kurekebisha mapungufu hayo na kisha kuusambaza katika hospitali za Mikoa.

 

57. Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya serikali, napenda kutoa shukurani za dhati kwa mashirika na makampuni mbalimbali yaliyotuwezesha kutekeleza mpango huu.  Kampuni ya Abbot Laboratories kupitia shirika la Axios International ilitoa msaada wa vifaa vya kisasa vya maabara kwa hospitali ya Mkoa wa Mbeya na Hospitali ya Taifa Muhimbili.  Pamoja na msaada wa vifaa hivyo, kampuni ya Abbot Laboratories imetoa msaada wa kiufundi katika kuandaa mwongozo wa kutoa huduma kwa walioathirika na virusi vya UKIMWI.

 

Mabadiliko ya Uendeshaji wa Huduma za Hospitali

 

58. Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya imekamilisha hadidu za rejea kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalamu (consultancy) wa kufanya mapitio ya mahitaji ya ukarabati na utoaji huduma katika hospitali za wilaya na mikoa kulingana na mahitaji ya mabadiliko ya hospitali (Hospital Reforms).  Taratibu za kumpata mtaalam mshauri wa kufanya mapitio hayo zimeanza na zitakamilika mwanzoni mwa mwaka wa fedha wa 2002/2003.  Matokeo ya mapitio hayo yatasaidia katika kukamilisha mpango wa miaka 10 wa maendeleo ya hospitali na mwongozo wa kuanzisha vituo vipya vya huduma za afya kulingana na mahitaji na uwezo wa nchi.  Vile vile, Wizara ya Afya imeandaa mwongozo wa utekelezaji wa mabadiliko ya huduma za hospitali ambao utazisadia hospitali mbalimbali katika kupanga na kutathmini mabadiliko yanayoendeshwa katika hospitali zao.

 

HUDUMA ZA UTAWALA NA UTUMISHI

 

Huduma ya Utawala

Ununuzi wa magari

 

59. Mheshimiwa   Spika,    katika    kipindi    cha   mwaka

2001/2002. Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ilinunua magari 11 kwa gharama ya shilingi milioni 239.93.  Magari hayo yaligawanywa kwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza na Halmashauri za wilaya za Shinyanga, Kahama, Maswa, Meatu, Bukombe, Newala, Kongwa, Bunda, Muleba na Ngara.

 

Huduma za Utumishi

 

60. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2001/2002 Wizara

ya Afya ilihuisha miundo ya Utumishi (Scheme of Service) ya watumishi chini ya Wizara kutoka miundo 30 hadi kufikia 20.  Baada ya zoezi hilo wataalam wa Wizara ya Afya waliichambua miundo hiyo na kufanya marekebisho; kuunganisha ile iliyokuwa na kazi zinazofanana; kupunguza au kuongeza upeo wa ngazi ya mishahara, kuboresha sifa za kuingilia kazini na kuongeza muundo mpya wa Medical Entomologist ambao  awali uliunganishwa na ule wa Maafisa Afya.

 

61.     Mheshimiwa Spika, mapendekezo ya miundo hiyo mipya iliwasilishwa mbele ya kikao cha kwanza cha Baraza la Wafanyakazi wa Wizara (TUGHE) tarehe 4 na 5 Oktoba, 2001.  Katika kikao hicho iliamuliwa kuwa miundo ya Mafundi Sanifu iunganishwe.   Kutokana na hatua hiyo, miundo ilipungua tena kutoka 20 hadi 17 baada ya kuunganishwa miundo ya Mafundi Sanifu.   Miundo hiyo baada ya kupitishwa katika Baraza la Wafanyakazi la Wizara; iliwasilishwa katika Baraza Kuu la Taifa katika kikao chake kilichofanyika tarehe 19 na 20 Novemba 2001 hapa Dodoma.   Ni matumaini yangu kuwa miundo hiyo itakapoanza kutumika watumishi wa Sekta ya Afya watanufaika.

 

62.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2001/2002 Wizara ya Afya iliendeleza jitihada za kuwapandisha vyeo watumishi katika ngazi mbalimbali.  Ninayo furaha kulifahamisha Bunge lako tukufu kwamba watumishi wa kada mbalimbali 6,029 walipandishwa vyeo.  Aidha mapendenezo ya kuwapandisha vyeo watumishi wengine 3,545 yamekamilishwa na kuwasilishwa kwenye mamlaka husika.  Zoezi hili bado litapewa kipaumbele katika mwaka huu wa fedha.

 

 

 

 

HUDUMA ZA MAFUNZO YA WATUMISHI WA AFYA

 

UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU MWAKA 2001/2002

 

63.     Mheshimiwa Spika, Mafunzo ya kuimarisha utendaji wa watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri na kuzipa uwezo wa kupanga na kusimamia uendeshaji na utoaji wa huduma za Afya, yanaendelea kutolewa  na Wizara nchini kote. Jumla ya halmashauri 73 zimekwishapata mafunzo hayo. Aidha uendeshaji wa mafunzo hayo umefanyiwa tathmini ya kati (Mid-Term Evaluation) na kuonyesha kuwa na mafanikio hususan katika kuongeza uwezo wa Kamati za Uendeshaji wa Huduma za Afya za Wilaya (Council Health Management Team) kupanga na kutekeleza mipango ya afya, ukilinganisha na Halmashuri ambazo bado hazijapata mafunzo hayo.

 

64.     Mheshimiwa Spika, ili kuinua ubora wa mafunzo, Wizara yangu inashirikiana na Baraza la Elimu ya Ufundi (National Council for Technical Education) kuhakiki viwango vya ufundishaji katika vyuo vya afya. Aidha, kwa kushirikiana na Chuo Kikuu Kishiriki Muhimbili, Chuo Kikuu Cha Johns Hopkins na Taasisi ya Magonjwa ya Kuambukiza ya Atlanta Marekani (Center for Disease Control, Atlanta) sehemu kubwa ya mitaala inayotumika kufundishia wataalam wa kada mbalimbali imepitiwa na kufanyiwa marekebisho ikiwa ni pamoja na mtaala wa Tiba ya Dharura kwa ajili ya wanafunzi wa udaktari na uuguzi.

 

 

 

65.     Mheshimiwa Spika, ninafurahi kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba Mafunzo ya Shahada ya Afya ya Mazingira (BSc. Enviromental Health) yameaanza katika chuo Kikuu Kishiriki cha Sayansi ya Afya (MUCHS). Katika mwaka 2001/2002. Jumla ya wanafunzi 23 wamejiunga na kozi hiyo. Matarajio yetu ni kwamba wataalam watakaofuzu kozi hiyo watatuwezesha kukabiliana kikamilifu zaidi na magonjwa yanayotokana na mazingira duni.

 

66.     Mheshimiwa Spika, kutokana na kuchakaa kwa majengo ya vyuo vya afya, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2001/2002 wizara yangu imekamilisha ukarabati wa majengo ya vyuo 17 kwa kutumia gharama ya shilingi millioni 226.04

 

67.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa masomo uliopita wanafunzi katika fani mbalimbali za vyuo vya afya wamehitimu kama ifuatavyo; waliopata vyeti ni 1,290 waliopata stashahada ni 638 na waliopata stashahada ya juu 195.  Jumla ya wahitimu wote ni 2,123. Aidha idadi ya madaktari imeongezeka na kufikia wahitimu 100 kwa mwaka kutoka vyuo vya Muhimbili , KCMC, na kutoka vyuo vya nje. 

 

OFISI YA  MGANGA MKUU KIONGOZI

 

Huduma za Uuguzi

 

68. Mheshimiwa  Spika,   katika   kuimarisha  huduma   za

Wauguzi nchini, Wizara imefanya mapitio ya mwongozo wa kisera wa Uuguzi na Ukunga ili uweze kukidhi mahitaji ya maadili mapya ya Uuguzi na mabadiliko ya utendaji wa huduma za afya pia imeandaa rasimu ya mwongozo wa maadili ya Uuguzi na Ukunga. Rasimu hiyo imesambazwa katika Mikoa yote kwa ajili ya kupata maoni na mapendekezo zaidi. Wizara imefanya ukaguzi wa huduma za Uuguzi katika mikoa mitano. Ilikuendeleza huduma za uuguzi nchini Wizara imeandaa mpango wa kuendeleza huduma hizo kwa kipindi cha mwaka 2002-2004. Aidha Wauguzi viongozi wa wodi wamefundishwa mbinu za kufanya utafiti wa kutatua matatizo ya utoaji huduma katika sehemu zao za kazi. Mafunzo hayo yamefanyika kwa Wauguzi wa mikoa ifuatayo:- Ruvuma, Mtwara, Tanga, Morogoro, Iringa, Pwani, Dodoma, Tabora, Rukwa na Mbeya.

 

Ukaguzi wa Huduma za Afya

 

69.     Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha 2001/02, Wizara ya Afya, iliandaa na kusambaza Mwongozo wa Viwango vya Huduma za Afya (National Norms, Guidelines and Standards on Cross Cutting Issues in Health Care Practice in Tanzania). Aidha, Kitengo kimeandaa na kusambaza mwongozo wa uoanishaji wa huduma za afya (Integration of Health Services). Kitengo pia kilifanya ukaguzi wa utoaji wa huduma za afya katika mikoa 8 ikijumuisha wilaya 17 yaani wilaya 2 kila mkoa kwa mikoa 7 na wilaya 3 katika mkoa mmoja na kilitoa maelekezo juu ya marekebisho yaliyopasa kufanyika katika maeneo ambayo matatizo yalijitokeza.

 

Huduma za Dharura na Maafa

 

70.     Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Dharura na Maafa cha Wizara ya Afya kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2001/2002, kilitembelea hospitali za mikoa ya Ruvuma, Lindi, Mtwara, Mara, Kagera na Mwanza ili kutoa ushauri na maelekezo ya kitaalamu kwa ajili ya kuboresha huduma za dharura na maafa. Hali kadhalika, mafunzo ya huduma za dharura na maafa, yalitolewa kwa madaktari na wauguzi wa hospitali za rufaa na hospitali za mikoa ya Morogoro, Pwani, Dodoma,  Iringa, Tanga, Kilimanjaro, pamoja na hospitali za Wilaya za Jiji la Dar-es-Salaam. Kazi nyingine muhimu zilizokamilshwa ni kama ifutavyo:

 

·        Watumishi 2 walishiriki katika warsha ya mafunzo ya utoaji huduma za Dharura na Maafa nchini Msumbiji.

·        Mwongozo wa Utoaji huduma za Dharura na Maafa ulikamilika (Health Sector Guideline and Protocol on Emergency and Disaster Management).

·        Upembuzi yakinifu (Situation Analysis) katika hospitali, kuhusu hali halisi ya kukabiliana na Dharura na Maafa hapa nchini ulifanyika kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) na Shirika la Misaada la Marekani (USAID) katika hospitali zote za rufaa na za mikoa ya Tanga, Iringa Pwani , Dodoma na Morogoro.

 

TAASISI, TUME NA BODI ZILIZOPO CHINI YA WIZARA YA AFYA

 

Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu

(National Institute for Medical Research –NIMR)

 

71.     Mheshimiwa Spika, Taasisi imefanya utafiti kupima uwezo wa dawa ya  Amodiaquine   katika kutoa tiba ya muda mfupi kwa watoto wachanga wanaogua ugonjwa wa Malaria kupitia  Mpango wa Taifa wa Chanjo.  Utafiti huu umeendeshwa chini ya mradi wa Presumptive Malaria Intermittent Treatment in Infants.  Matokeo ya Utafiti huu yameonyesha mafanikio mazuri kwa asilimia kati ya 60 na 70.  Hali kadhalika, utafiti juu ya  matumizi ya vyandarua vyenye kutiwa dawa ili kupunguza ugonjwa wa malaria uliendeshwa katika maeneo ya nyanda  za juu na vijiji vya Muheza.  Matokeo ya utafiti huo yameonyesha kwamba kiasi cha maambukizo ya vimelea ya malaria kwa watoto wadogo vimepungua kwa asilimia 16.4 kwa watoto wanaotumia vyandarua hivi.

 

72.   Mheshimiwa  Spika  milipuko ya  Malaria  inayotokea

mara kwa mara katika Wilaya za Babati, Hanang, Dodoma, Mpwapwa, Muleba na Lushoto inaleta athari kubwa kwa wananchi.  Utafiti wa milipuko hiyo katika mkoa wa Dodoma umebaini kuwa milipuko  hiyo imekuwa ikiandamana na mvua baada ya kipindi kirefu cha kiangazi pamoja na ongezeko la hali ya joto.  Hii imekuwa dhahiri hasa katika wilaya ya  Mpwapwa. Utafiti umeonyesha pia kuwa  kutokana na takwimu za hali ya hewa inawezekana kabisa  kutabiri lini milipuko ya malaria inategemewa kutokea ili matayarisho ya kudhibiti milipuko hiyo yaweze kufanyika.  Kufuatia utafiti huu taasisi ilitumia jedwali maalum la kutabiri milipuko ya Malaria katika tarafa ya Kibakwe Wilayani Mpwapwa na imeonekana kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kutumia takwimu za hali ya hewa kutabiri milipuko hiyo.

 

73.     Mheshimiwa Spika, mfuko wa utafiti wa Afya (Health Research User Trust Fund) umeendelea kupata fedha toka Serikalini na kwa Wahisani.  Katika mwaka wa fedha 2001/2002  mfuko  uliweza kulipia mada za utafiti zenye thamani ya shilingi milioni 47.7  Mfuko pia ulitoa  tangazo la kuomba miradi mipya ili uweze  kuichambua na hatimaye kuipatia fedha.  Kufuatia tangazo hilo mada za utafiti 18 zilipokelewa na bado zinaendelea kuchambuliwa.

 

Taasisi ya Chakula na Lishe

 

74      Mheshimiwa Spika, Taasisi ya Chakula na Lishe kwa kushirikiana na Taasisi nyingine, imeendelea na juhudi za kudhibiti tatizo la upungufu wa madini joto mwilini na athari zake. Taasisi iligawa vidonge vya madini joto katika Wilaya 9 ambazo bado zimeonekana kuwa na tatizo kubwa la upungufu wa madini hayo. Jumla ya vidonge millioni 3.5 vilivyotolewa kama msaada kutoka Serikali ya Japani vimekwisha sambazwa katika Wilaya za Ulanga, Songea, na Mufindi. Wilaya nyingine ni Mbeya vijijini, Sumbawanga, Kibondo, Kigoma, Biharamulo na Ngara. Gharama za usambazaji wa vidonge hivyo zilifadhiliwa na Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF). Aidha uhamasishaji wa viongozi na watendaji mbalimbali katika ngazi ya Wilaya juu ya tatizo la upungufu wa madini joto na njia ya kukabiliana nalo ulifanyika katika wilaya 15 zenye matatizo makubwa ya upungufu wa madini joto.  Wilaya zilizohamasishwa ni Monduli, Arumeru, Rombo, Mpwapwa, Kigoma, Kasulu na Kibondo. Nyingine ni Biharamulo, Ngara, Karagwe, Bukoka Vijijini, Songea, Mbinga, Makete na Ludewa. Jumla ya viongozi 131 na Maafisa wa Afya 151 walipata mafunzo hayo.

 

75.     Mheshimiwa Spika, Taasisi pia ilifuatilia upatikanaji wa chumvi yenye madini joto katika ngazi ya kaya. Mpango huu huwashirikisha walimu na wanafunzi wa shule za msingi katika kila wilaya. Walimu wote katika shule zilizoteuliwa hupatiwa mafunzo ya kupima chumvi kama ina madini joto au la. Taarifa za upatikanaji wa chumvi yenye madini joto zinawasilishwa Wilayani na ngazi ya kitaifa ili kufanyiwa kazi. Katika kipindi cha 2001/2002. Mpango huu ulianza kutekelezwa katika wilaya za Rombo, Arumeru, Monduli na Mpwapwa. Nyingine ni Songea, Mbinga, Ludewa na Makete. Upimaji wa chumvi uliofanyika katika wilaya hizo ulionyesha kuwa wastani wa asilimia 79 ya kaya katika maeneo hayo zilikuwa zikitumia chumvi yenye madini joto.  Haya ni mafanikio mazuri, lakini bado kuna kazi ya kuhamasisha matumizi ya chumvi yenye madini joto.

 

76.Mheshimiwa Spika, Taasisi pia iliendelea na juhudi

za kudhibiti tatizo la upungufu wa damu ambalo bado ni kubwa nchini mwetu hasa kwa akina mama na watoto. Watoto wote wenye umri chini ya miaka mitano wilayani Bagamoyo, walipewa dawa ya kuongeza damu (ferrous sulphate syrup) pamoja na vidonge vya kutibu minyoo (mebendazole tablets). Katika kipindi hicho cha mwaka 2001/2002, Taasisi pia ilisambaza vidonge 65,000,000 vya kuongeza damu (ferrous sulphate/Folic acid) kwa ajili ya akina mama wajawazito katika hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa nchini kote. Dawa hizo zilitolewa na Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF).

 

77.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho, Taasisi

ilipokea mashine 76 za kupimia kiwango cha damu “colorimeters” kutoka serikali ya Japan. Wataalamu wa maabara 71 kutoka katika hospitali za wilaya 67 walipata mafunzo kuhusu namna ya kutumia mashine hizo. Jumla ya hospitali 17 zimekwishapokea mashine hizo nazo ni  Tumbi, Kongwa, Hospital ya Rufaa Mbeya, Tukuyu, Igogwe, Rujewa, Iringa, Makete. Hospitali nyingine ni Ndanda, Mkomaindo, Lugarawa, Ludewa, Kolandoto, Mwadui, Mugana, Nkinga, na St Francis ya Ifakara. Hospitali nyingine 59 zilizobaki za wilaya zitapatiwa mashine hizo katika mwaka wa fedha wa 2002/2003.

 

78.     Mheshimiwa Spika, Taasisi kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Shirika la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF)  na Halmashauri za Wilaya saba nchini imeanza  maandalizi ya mpango wa kuzuia watoto kuzaliwa na uzito pungufu. Wilaya zinazoshiriki katika mpango huu ni Hai, Magu, Kibaha, Kilosa, Mbarali, Mtwara vijijini na Masasi.

 

79.     Katika kutekeleza mpango huo, mafunzo yametolewa kwa viongozi 197 wa Wilaya, wajumbe 104 wa kamati za utekelezaji wa mpango wa wilaya na wafanyakazi 339 wa sekta ya afya kutoka vituo vinavyotoa huduma ya mama na mtoto katika wilaya hizo.  Mafunzo hayo yalihusu lengo la mpango, jinsi mpango utakavyotekelezwa na uhamasishaji wananchi ili kushiriki kikamilifu katika utekelezaji mpango. Vile vile, vifaa na dawa kwa ajili ya mpango zimekwishanunuliwa na tayari usambazaji umeanza.

 

80.     Mheshimiwa Spika, Taasisi kwa kushirikiana na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na Hospitali za Manispaa ya Ilala, Temeke na Kinondoni imekuwa ikitoa ushauri na ushauri nasaha na elimu ya lishe bora kwa wagonjwa wa kisukari na shinikizo la damu. Jumla ya wagonjwa 155 walipata ushauri huo.

 

81.     Mheshimiwa Spika, katika kuboresha lishe ya wananchi, mradi wa majaribio wa kuongeza virutubisho kwenye unga wa mahindi umeanzishwa katika tarafa ya Mazombe, wilaya ya Iringa vijijini. Kupitia mradi huu, virutubisho vya madini na vitamini mbali mbali vitachanganywa katika unga wa mahindi kwenye mashine za kusagia mahindi zilizopo kwenye jamii. Mradi huu utasaidia kuboresha afya za wananchi kwenye eneo hilo, hasa za mama na watoto ambao ni waathirika wakuu wa tatizo la utapiamlo.

 

82.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki suala la lishe na afya bora kwa watoto wachanga limezidi kupewa kipaumbele kwa kuendeleza mikakati ya kuimarisha unyonyeshaji wa ziwa la mama na ulishaji wa mtoto. Juhudi zimefanyika kutafsiri maandiko ya kiingereza kwa kiswahili ya kufundishia stadi za utoaji wa ushauri nasaha juu ya unyonyeshaji na ulishaji wa watoto kwa wakati huu tunapopambana na gonjwa la UKIMWI.  Mafunzo haya yatatolewa kwa watoa huduma za msingi, wakiwemo wahudumu wa afya na wafanyakazi wengine wa ugani.  Aidha, vipeperushi, vijitabu, vijarida na mabango vimeandaliwa kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma kuhusu unyonyeshaji na ulishaji wa watoto na UKIMWI, Lishe na UKIMWI na ushauri nasaha juu ya kupima UKIMWI.

 

83.     Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya bado inasisitiza kuwa unyonyeshaji wa ziwa la mama pekee bado ndio njia bora ya kumlisha mtoto kwa mama ambaye hana maambukizo ya UKIMWI.  Kwa mama ambaye amepata maambukizo awasiliane na wahudumu wa afya kwa ushauri zaidi.

 

84.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2001/2002, Taasisi katika kuendeleza makuzi bora ya mtoto, ilikuwa iongeze idadi ya hospitali zilizo na sifa ya huduma bora kwa watoto (Hospitali rafiki wa mtoto) nchini kutoka hospitali za sasa 55 hadi 65. Kutokana na uhaba wa fedha wa kuthathimini hospitali hizo, lengo hilo halikufikiwa. Kazi hiyo itafanyika katika kipindi cha 2002/2003 kwenye mikoa ya Arusha, Mwanza na Kagera.

 

85.     Mheshimiwa Spika, katika mpango wa kuboresha lishe na afya ya watoto kwa mwaka 2001/2002, Taasisi iliendelea kuelimisha na kutoa mafunzo kwa vikundi na watu mbali mbali juu ya uboreshaji wa vyakula vya kulikiza kwa kutumia mchanganyiko wa mazao ya nafaka na mikunde. Aidha kwa kushirikiana na Taasisi mbalimbali, Taasisi iliendelea na utafiti kuhusu uboreshaji na upatikanaji wa virutubisho katika vyakula vya kulikiza kwa kutumia njia zilizo sahihi na rahisi. Lengo la tafiti hizo ni kubaini mbinu za kuinua kiwango cha hali ya lishe ya watoto ikiwa ni pamoja na kuongeza upatikanaji wa madini ya chuma na hivyo kuchangia kupunguza tatizo la upungufu wa damu kwa watoto. 

86.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/2002 Wizara ya Afya kupitia Taasisi yake ya Chakula na Lishe iliendesha kampeni ya kitaifa ya utoaji matone ya vitamini A kwa watoto wote wenye umri kati ya miezi 6 na miaka 5 katika mikoa yote ya Tanzania Bara. Kampeni hii ilifanyika kwa awamu mbili zilizopishana kwa miezi 6 ambapo awamu ya kwanza ilifanyika sambamba na Siku ya Mtoto wa Afrika tarehe 16 Juni 2001, na awamu ya pili ilifanyika sambamba na Siku ya Ukimwi Duniani tarehe 1 Desemba 2001. Katika awamu ya kwanza watoto 4,645,568,  sawa na asilimia 80 ya watoto walengwa  5,842,953  walipatiwa matone ya vitamini A katika mikoa yote ya Tanzania Bara.  Katika awamu ya pili, watoto 5,285,641, sawa na asilimia 91 ya watoto walengwa  5,870,822 walipatiwa matone ya vitamini A katika mikoa yote ya Tanzania Bara.

 

Tume ya kudhibiti vyakula ya Taifa (TUKUTA)

 

87.     Mheshimiwa   Spika,    katika    mwaka   2001/2002

TUKUTA iliendesha mafunzo kwa Maafisa Afya na Wenye Viwanda kuhusu mfumo makini wa utengenezaji wa vyakula salama katika wilaya 74 za Tanzania Bara. Maafisa wa Forodha wa vituo vya mipakani walipewa mafunzo kuhusu taratibu za uagizaji na uingizaji wa vyakula nchini. Aidha Tume iliandaa rasimu za sheria ndogo za uhifadhi wa vyakula kwa kutumia mionzi ( Food Irradiation). Ilitoa mafunzo kwa Maafisa Afya wa mikoa ya kanda ya ziwa kuhusu usimamizi na utekelezaji wa Sheria ndogo ya Unyonyeshaji na Vyakula vya Kulikiza watoto ya mwaka 1994 katika mikoa yao. Aidha ilitoa pia mafunzo kwa Maafisa Afya na Madaktari kuhusu uchunguzi na uratibu wa magonjwa yaeneayo kwa njia ya chakula. Pia Tume iliendesha mafunzo kwa wazalishaji wa vyakula 92 wenye viwanda vidogo vidogo (Small Scale Food Producers/Entrepreneurs) kuhusu utengenezaji wa vyakula bora na salama katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Iringa, Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Mwanza na Shinyanga. Kuendesha warsha juu ya usimamizi na utekelezaji wa sheria ya madini joto.  Katika kipindi hiki TUKUTA ilitoa leseni 163 kwa viwanda vinavyotengeneza vyakula hapa nchini na ilisajili waagizaji wa vyakula 115.

 

Bohari Kuu ya dawa

 

88.     Mheshimiwa Spika,   zoezi   la   kuteketeza  dawa za

Medical Stores zilizoharibika kati ya mwaka 1994 hadi 2000 limekamilika. Dawa zenye uzito wa kilo 193,925 za thamani ya Tshs. 2,734,922,910 ziliteketezwa kwa awamu kuanzia Juni 2001 hadi Mei 2002.  Ili kudhibiti uharibifu huu usitokee tena, hatua zifuatazo zinachukuliwa; tunafunga mashine za computer katika Bohari Kuu ya Dawa ambazo zitarahisisha kufahamu mwenendo wa kiasi na aina ya dawa pamoja na kujua tarehe zake za muda wa kumaliza uwezo wa kutibu. Aidha tumebadilisha utaratibu wa kuagiza dawa kwa kuwataka wazabuni kutuletea dawa katika awamu mbili tofauti zinazopishana kwa kipindi cha miezi sita badala ya kuzileta zote kwa mara moja kama ilivyokuwa hapo awali. Hatua hizi zitapunguza mlundikano wa dawa na pia kuwezesha Bohari Kuu ya Dawa kuuza dawa mapema iwezekanavyo kabla ya kwisha muda wake wa uwezo wa kutibu.

 

Mkemia Mkuu wa Serikali

 

89.Mheshimiwa  Spika,     katika    kipindi    cha   mwaka

2001/2002 Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ilipata kiasi cha Tshs 1,183,000,000 kutoka serikalini, nchi wahisani na mikopo kutoka Benki ya Dunia. Fedha hiyo zilitumika kununulia kemikali, mitambo ya kisasa na vitendea kazi muhimu vya kufanyia uchunguzi wa kimaabara pamoja na ukarabati wa majengo. Vitendea kazi hivyo vimewezesha jumla ya sampuli 2849 za dawa, maji, makosa ya jinai, ubora wa malighafi na bidhaa kufanyiwa uchunguzi.

 

Bodi ya Madawa

 

90.Mheshimiwa Spika, Bodi ya Madawa katika kipindi cha

2001/2002 iliendelea kutekeleza wajibu wake wa kisheria wa kudhibiti shughuli za dawa ikiwa ni pamoja na usajili wa wafamasia, usajili wa dawa, ukaguzi wa viwanda vya madawa na sehemu mbalimbali zitoazo huduma za dawa, uchunguzi wa viwango vya ubora wa dawa yanayoingia na kutumika nchini na pia kutoa ushauri kuhusiana na masuala ya dawa. Hadi kufikia mwezi Desemba 2001 jumla ya dawa 347 zilisajiliwa. Kiasi hiki ni asilimia 65% ya dawa zote zilizo katika orodha ya dawa muhimu nchini. Maabra imeweza kufanya uchunguzi wa dawa aina 308 kati ya hizo asilimia 18.5 ya dawa haikufikia viwango.

 

MATARAJIO YA MWAKA 2002/2003

MIPANGO YA MAENDELEO

 

91.Mheshimiwa  Spika,   Katika   kipindi  cha  2002/2003

Wizara    ya   Afya   imetengewa   kiasi   cha    shilingi

51,096,671,000 kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo.  Kati ya fedha hii kiasi cha shilingi 3,552,448,200 ni kutoka Serikali ya Tanzania na kiasi cha shilingi 47,544,222,800 ni mchango kutoka nchi na taasisi za kimataifa zinazochangia Mfuko wa Pamoja wa Afya. Taasisi na nchi hizo ni Benki ya Dunia, Serikali za Uingereza, Uholanzi, Ujerumani, Uswisi, Denmark, Ireland na Norway. Wahisani hawa wote wanachangia katika Mfuko wa Pamoja ili  kuiwezesha Wizara kutekeleza majukumu muhimu yaliyopangwa  katika matumizi  ya kawaida  na miradi ya maendeleo.

 

92. Mheshimiwa Spika, fedha hii imepangiwa kutekeleza shughuli na miradi ambayo ni kipaumbele kwa Wizara ambayo kwa mwaka 2002/03 inalenga maeneo makuu yafuatayo: 

 

·        Tathmini na usimamizi wa miradi ya maendeleo, ukusanyaji takwimu sahihi na mafunzo ya muda mfupi kwa timu za wilaya kuhusu mbinu za utafiti wenye malengo thabiti (Action Oriented Research Methods), shillingi millioni 79.6.

 

·        Kutoa msaada wa utaalam na uendeshaji wilayani ikiwa ni pamoja na dawa za chanjo na vifaa vya hospitali, fedha hizi zitatolewa na DANIDA, shillingi billioni 1.9.

 

·        Wizara katika kuhakikisha kuwa ukarabati wa majengo ya serikali ya kutolea huduma za afya unafanyika, Mpango wa Maendeleo wa Miaka 10 wa Kukarabati Hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa utaandaliwa.  Sambamba na mpango huu, Wizara, kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), itafanya upembuzi yakinifu wa ukarabati wa hospitali za mikoa mitatu ambayo ni Mara, Tabora na Mtwara.  Matokeo ya utafiti huu yatatumika katika mikoa mingine.  Pia Hospitali ya Rufaa ya Taifa ya Muhimbili itaanza kufanyiwa ukarabati kwa kutumia fedha za mkopo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na za Serikali ya Tanzania.  Jumla ya shillingi billioni 4.3 zinapendekezwa kutumika.

 

·        Katika kuimarisha Hospitali za Taifa, fedha zimetengwa ili kukarabati Wodi za Wazazi hospitali ya Meta/ Mbeya, Jengo la Maabara, Jengo la utawala na wagonjwa wa nje katika hospitali ya Rufaa Mbeya.  Pia ukarabati wa wodi tatu, uzio wa Taasisi  maalumu ya Isanga na ukarabati wa majengo ya kijiji cha wagonjwa wa Akili, pamoja na mfumo wa maji safi hospitali ya Mirembe utafanyika. Jumla ya shillingi millioni 367.02 zinapendekezwa kutumika kwa kazi hii.

 

·        Kukamilisha ujenzi wa wodi ya watoto Muhimbili ambayo ni Awamu ya  kwanza inayojumuisha ujenzi wa sakafu iliyo chini  ya usawa wa ardhi (Basement floor), sakafu iliyo usawa  wa ardhi (Ground floor) na sakafu ya kwanza (First Floor). Jumla ya shillingi millioni 720 zinapendekezwa kutumika kwa kazi hii. Ujenzi wa awamu ya pili ambayo ni sakafu ya pili na ya tatu utaanza kufanyika katika mwaka 2003/2004.

 

·        Hospitali ya Mifupa – Muhimbili Orthopaedic Institute (MOI) imetengewa jumla ya shillingi millioni 850 ikiwa ni mchango wa Serikali ya Tanzania katika kukamilisha ujenzi wa Chumba cha Wagonjwa Mahututi (ICU), Maabara ya Benki ya Damu, vyumba vya Xray na upasuaji wa moyo  (Open Heart Surgery).

.

·        Taasisi   ya Saratani (Ocean Road Cancer Institute) imetengewa jumla ya shillingi millioni 900  kwa ajili ya kubadilisha na kufanya matengenezo makubwa ya mashine ya uchunguzi wa magonjwa ya saratani, pamoja na ununuzi wa mashine nyingine mpya.

 

·        Wakala wa Mkemia Mkuu wa Serikali imetengewa jumla ya shillingi millioni 590.5 kwa ajili ya kununua na kufunga vifaa vya maabara, kuendeleza ujenzi wa maabara ya kudhibiti ubora wa dawa nchini (Drug Quality Control Laboratory) na kufanya upembuzi yakinifu ili kuweza kuanzisha maabara ya Kanda Mwanza.

 

·        Uzuiaji wa magonjwa ya kuambukiza umetengewa jumla ya shillingi billioni 8.3 kwa ajili ya kugomboa toka bandarini na kusambaza dawa za Kifua Kikuu na Ukoma, kampeni za kitaifa juu ya taarifa, elimu na mawasiliano kuhusu malaria, kununua dawa ya kuzuia mazalio ya mbu pamoja na kujenga uzio kuzunguka majengo ya Mpango wa Taifa wa Chanjo na ukarabati wa ofisi na mfumo wa umeme majengo ya Elimu ya Afya kwa Umma.

 

·        Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) imetengewa jumla ya shillingi millioni 387.4 kwa ajili ya kuanzisha kituo kipya cha ugunduzi na uendelezaji wa dawa za asili Mabibo, ukarabati wa majengo ya vituo vya utafiti Mwanza, Gonja, Amani, Bombo, Muheza pamoja na mchango wa Serikali katika Mfuko wa Utafiti (Research Users Trust Fund).

 

·        Kuendelea na uanzishwaji wa Mfuko wa Afya ya Jamii katika wilaya nyingine 20 na kufanya majaribio ya Mfuko wa Afya ya Jamii Mijini, ujulikanao kama Tiba kwa Kadi (TIKA), Jumla ya shillingi billioni 1.9 zinapendekezwa kutumika kwa kazi hii.

 

·        Kuendelea kuupatia fedha Mfuko wa Bima ya Afya ili uweze kuelimisha wadau wote kuhusu mfuko huo, kuhamasisha watoa huduma za afya, kulipia pango la ofisi, kuanzisha ofisi za kanda na kununua vitendea kazi kwa ajili ya kutunza   takwimu za mfuko, Jumla ya shillingi billioni 1.3 zinapendekezwa kutumika katika kazi hii.

 

·        Kuendelea kuhamasisha umma wa Tanzania kuhusu mabadiliko yanayofanyika katika sekta ya Afya katika ngazi zote pamoja na kuimarisha huduma za afya Wilayani kwa kuzipatia zana, dawa na vifaa mbalimbali vya hospitali shillingi billioni 28.8 zinapendekezwa kutumika kwa kazi hii.

 

·        Katika kuimarisha utoaji wa mafunzo ya Afya, vyuo vya afya 26 vilivyo katika hali mbaya vitafanyiwa ukarabati wa majengo, Jumla ya shillingi millioni 730.8 zinapendekezwa kutumika kwa kazi hii..

 

HUDUMA ZA KINGA

 

Udhibiti wa magonjwa ya kuambukiza

 

93.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki Wizara yangu itaendelea kupambana na magonjwa yanayoenezwa na wadudu wanaoruka, wasioruka, pamoja na wanyama (vectors and vector borne diseases) kwa kutoa kozi fupi  zinazohusu njia mbalimbali za kudhibiti magonjwa haya kwa wafanyakazi wa afya wapatao 40 kutoka mikoa inayoathirika mara kwa mara. Aidha ufuatiliaji wa ugonjwa wa kichaa cha mbwa pamoja na matumizi ya chanjo ya kichaa cha mbwa utafanyika katika mikoa  kumi na moja ya Tanzania Bara.

 

Mpango wa chanjo wa Taifa

 

94.     Mheshimiwa Spika, kampeni ya chanjo ya Polio na Surua itaendelea tena mwaka huu 2002/2003 katika baadhi ya wilaya. Kwa chanjo ya Polio, Wilaya 16 zitakuwemo katika kampeni na kwa chanjo ya Surua Wilaya 82 zenye wagonjwa wengi zitahusishwa.  Kutokana na zoezi la kuhesabu idadi ya watu (Sensa) litakalofanyika nchi nzima mwezi Agosti, kampeni za chanjo zitafanyika mwezi wa Oktoba kwa chanjo ya kwanza ya Polio na mwezi Novemba kwa chanjo ya pili ya Polio pamoja na Surua.

 

95.     Mheshimiwa Spika, mwaka huu wa fedha Wizara yangu itafunga majokofu 720 yanayotumia gesi katika Mikoa ya Ruvuma, Iringa, Mbeya, Kilimanjaro, Arusha, Mwanza, Mara na Kagera kwa kutegemea upatikanaji wa fedha za kununulia majokofu toka fedha za Wizara zilizotengwa kwa ununuzi huo pamoja na msaada toka Serikali ya Japan.

 

 Mradi wa Taifa wa Kudhibiti Malaria

 

96.     Mheshimiwa spika, mtazamo wa sasa wa kutibu magonjwa kama malaria, TB na UKIMWI ni kutumia dawa zaidi ya moja (dawa mseto) Faida ya dawa mseto ni kwamba huboresha tiba na pia hupunguza kuzuka kwa vimelea sugu. Wizara yangu imeanza kutafiti mseto wa dawa utakaofaa kutibu malaria ambao katika miaka michache ijayo utaanza kutumika rasmi badala ya dawa za sasa za mstari wa kwanza. Katika mpango wa utekelezaji wa mwaka 2002/2003 Wizara yangu inakusudia kuendelea kutoa mafunzo kwa wataalamu mabalimbali wa afya juu ya udhibiti sahihi wa malaria katika wilaya zote 32 zilizo katika awamu ya tatu ya utekelezaji wa mpango wa mabadiliko wa utoaji huduma za afya nchini. Aidha uhamasishaji juu ya utumiaji wa vyandarua vilivyo tiwa dawa utafanyika nchi nzima. Utafiti wa usugu wa vimelea vya malaria na tiba mseto utaendelea kufanyika.

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma

 

97.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2002/03, Wizara  itaendelea kuimarisha utafiti katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani ili kubaini kiwango cha uambukizo wa Kifua Kikuu katika jamii. Tayari mikoa 11 imeshafanyiwa utafiti huu. Matarajio ni kukamilisha mikoa yote ya Tanzania ifikapo mwaka 2004. Kwa upande wa ugonjwa wa Ukoma, mikoa mingine miwili itaingizwa katika kampeni za kutokomeza ugonjwa huu ambayo ni Dar es Salaam na Rukwa.  Matarajio ni kupanua kampeni hizi katika mikoa yote hapa nchini kwa awamu. Aidha wananchi na watumishi wa afya katika mikoa hiyo watapewa elimu zaidi ya kutambua dalili za ukoma katika jitihada ya kutokomeza ugonjwa huu.

 

Huduma ya Afya ya Uzazi  Mama na Mtoto

 

98.     Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha huduma za Afya ya Mama na Mtoto, Wizara imepanga kutoa mafunzo ya huduma za dharura kwa wazazi (emergency obstetric care) kwa kufundisha waalimu wa waalimu 12 kitaifa, na waalimu 84 (kila mkoa waalimu wanne). Hawa watatumika kufundisha wafanyakazi katika hospitali, vituo vya Afya na Zahanati njia bora za kutoa huduma ya dharura wakati wa uzazi.  Vile vile wafanyakazi wa afya wanotoa huduma za mama na mtoto 234 katika mikoa ya Kagera, Ruvuma, Tabora, Shinyanga, Rukwa, Singida na Kigoma, watapata mafunzo rejea kuhusu uzazi wa mpango na uzazi salama ili kuboresha huduma hizo. Aidha, Wizara itaendelea kununua na kusambaza dawa na vifaa vya  uzazi wa mpango nchi nzima kwa kushirikiana na wahisani.  Pia vipeperushi, vielelezo na mabango mbali mbali yanayotoa ushauri kuhusu maswala ya Afya ya uzazi mama na mtoto yatachapishwa na kusambazwa katika vituo vya kutolea huduma za afya na ofisi mbalimbali za serikali za mitaa nchi nzima ili kuwaelimisha wananchi na kuwahamasisha kutumia hudumia hizi. Sambamba na mipango hii, Wizara ya Afya itaandaa Mkakati wa Kitaifa wa Kuboresha Afya ya Uzazi na Mtoto awamu ya pili 2003 – 2007.

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI 

 

99.     Mheshimiwa Spika, Mkakati wa Kitaifa wa Kudhibiti UKIMWI wa mwaka 1998-2002 ( MTP III) umemaliza muda wake wa utekelezaji. Mkakati huo ulikuwa umetoa dira kwa   wadau wote kuhusu vipaumbele na mikakati ya kuzingatia katika mapambano ya UKIMWI kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita. Wizara yangu sasa imeanza maadalizi ya  kuandaa mpango mpya wa miaka mitatu utakaoendeleza mapambano katika sekta ya afya.  Mpango huu utakuwa wa kwanza tangu ianzishwe Tume ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI (TACAIDS) na utazingatia majukumu mapya ya sekta ya afya kama tulivyokubaliana na TACAIDS.  Mkazo mkubwa utaelekezwa kwenye suala la kuongeza huduma zilizothibitika kuwa ni bora kwa kudhibiti UKIMWI na kujenga uwezo wa sekta katika kumudu majukumu yake katika udhibiti wa UKIMWI.  Mkakati huu utaweka vile vile utaratibu wa kutoa ushauri kwa sekta nyingine pamoja na kuziwezesha halmashauri za wilaya kutekeleza majukumu yao.

 

Huduma ya Elimu ya Afya kwa Umma

 

100.   Mheshimiwa Spika, shabaha ya kuelimisha na kuhamasisha jamii itambue matatizo yake ya kiafya iko palepale. Wizara yangu inalenga katika kuwapa wananchi mbinu mbali mbali za kubadili tabia na mitindo ya maisha inayoathiri afya zao. Aidha lengo lingine ni kuiwezesha jamii kupanga, kutekeleza na kutathmini mipango ya kuzuia na kudhibiti magonjwa. Katika kipindi cha 2002/2003 Kitengo cha Elimu ya Afya kitaweka mkazo katika kuimarisha  kamati na bodi za Wilaya katika kubuni na kutayarisha vielelezo bora vya afya kulingana na sehemu zao. Kitengo pia kitalenga katika kuziwezesha wilaya katika kupanga na kutathimini utoaji wa elimu ya afya.

 

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Ugonjwa wa vikope (trachoma)  na Usubi (onchocerciasis)

 

101.Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2002/2003, Wizara ya Afya inatarajia kutibu watu 700,000 wanaosumbuliwa na ugonjwa wa usubi. Ukilinganisha na idadi ya wagonjwa 338,886 waliotibiwa mwaka 2000/2001 na wagonjwa 624,290 waliotibiwa mwaka 2001/2002. Gharama za kutibu wagonjwa hao zinakadiriwa kuwa shillingi millioni105.7. Aidha kuhusu ugonjwa wa vikope katika kipindi hiki Wizara inatarajia kuongeza juhudi za kudhibiti ugonjwa huu kwa kutumia mbinu ijulikanayo kama SAFI  yaani (Sawazisha kope, Anza matibabu mapema, Fanya usafi wa mwili, na Imarisha mazingira) kutoka vijiji 150 vya sasa hadi kufikia vijiji 204.

 

Mradi wa Uimarishaji wa Huduma Muhimu za Afya

 

102.          Mheshimiwa Spika, Mradi wa Uimarishaji wa Huduma Muhimu za Afya, umekuwa chombo cha kutusaidia kufanya majaribio ya matumizi ya rasilimali mbalimbali katika sekta ya afya na jinsi rasilimali hizo zinavyoweza kuongeza ufanisi na ubora wa huduma za afya .Matokeo ya majaribio hayo yaliyofanyika kuanzia mwaka 1995 yamepatikana. Matokeo hayo yamewezesha kuandaa miongozo ya jinsi ya kupata viwango vya magonjwa vya wilaya, hali ya matumzi ya afya ya wilaya, hali ya huduma za afya wilayani na mfumo wa taarifa za afya wilayani.  Katika mwaka wa fedha wa 2002/2003 mradi utashughulikia kuandaa utaratibu utakaowezesha miongozo hiyo kutumika katika wilaya nyingine.

 

HUDUMA ZA TIBA

 

Huduma ya Dawa na Vifaa vya Hospitali

 

103    Mheshimiwa Spika, Jumla ya fedha zilizotengwa kwa ununuzi na usambazaji wa dawa na vifaa katika mwaka wa fedha wa 2002/2003 ni shilingi bilioni 16.2. Ingawa kuna ongezeko la shilingi bilioni 1.5 ikilinganishwa na Shilingi bilioni 14.7 za mwaka uliopita, bado ongezeko hilo halikidhi mahitaji halisi ya vituo vya kutolea huduma. Hii inatokana na kupanda kwa bei ya dawa na vifaa kwani asilimia 80 ya dawa na vifaa vinanunuliwa kutoka nje na gharama yake inategemea thamani ya shilingi kwa fedha za kigeni.

 

104.   Mheshimiwa Spika, zahanati na vituo vya afya vitaendelea kupewa kipaumbele kupata dawa kwa kuzingatia kwamba vituo hivyo vipo vijijini ambapo wananchi hawana sehemu nyingine za kupata huduma ya afya kama ilivyo mijini. Hivyo, zahanati na vituo vya afya vitapelekewa masanduku ya dawa (drug kits) kila mwezi. Ili kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa katika zahanati na vituo vya afya, mfumo wa uagizaji kulingana na mahitaji (Indent System) utatumika katika halmashauri 16 ambazo zimeanzisha Mfuko wa Afya wa Jamii (Community Health Fund). Chini ya mfumo huo, Serikali itatoa fedha sawa na thamani ya makasha ya dawa (drug kits) na Mfuko wa Afya wa Jamii utatoa fedha kugharimia dawa na vifaa vya ziada kukidhi mahitaji halisi vya vituo hivyo.  Halmashauri 6 ambazo ni Monduli, Mbulu, Karatu, Masasi, Mtwara Mjini na Vijijini zitaanza kutekeleza mfumo huo wakati Halmashauri nyingine 10 zitaandaliwa katika mwaka wa fedha 2002/2003.

 

105.        Mheshimiwa Spika, katika kuboresha upatikanaji wa

dawa katika hospitali za wilaya, teule, mikoa na rufaa, mfumo wa mfuko wa dawa, unaowezesha hospitali hizo kununua dawa kulingana na fedha zinazopatikana na mauzo ya dawa hizo (Capitalization of Hospital Pharmacies) utaimarishwa kwa kuzipatia hospitali hizo vitendea kazi vya kudhibiti matumizi ya dawa na makusanyo ya fedha kutokana na uchangiaji wa huduma ya afya. Pia watumishi katika hospitali hizo watapewa mafunzo ili kufanikisha udhibiti wa dawa na makusanyo ya fedha. Fedha itakazokusanywa chini ya mfumo huo itatumika kununua dawa na vifaa vya ziada.

 

106.   Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID) chini ya Mpango wa Ushirikiano wa Japani na Marekani (Japan – USA Common Agenda) itandaa mfumo wa ugavi (Integrated Logistics System) ambao utatumika kufuatilia uagizaji na usambazaji wa dawa na vifaa katika Sekta ya Afya ili kupima uwiano wa uagizaji na matumizi halisi. Mfumo huo utakapokamilika utaunganishwa na Mfumo wa Taarifa za Dawa  (Medical Stores Management Information System). Chini ya mfumo huo, zahanati, vituo vya afya na hospitali zitatakiwa kuonyesha salio la dawa na vifaa vilivyopo, wakati wa kuagiza vitu hivyo kutoka Bohari Kuu ya Dawa.  Salio la kila dawa na kifaa vitaingizwa kwenye mtandao wa kompyuta kubaini kama uagizaji wa dawa na vifaa unaendana na matumizi halisi katika vituo vya kutolea huduma ya afya. Mfumo huo unatarajiwa kurahisisha ukusanyaji wa takwimu za uagizaji, usambazaji na matumizi ya dawa na vifaa na hivyo kuboresha mfumo wa upatikanaji wa dawa na vifaa nchini na vilivile kudhibiti wizi na ubadhirifu.

 

Huduma za Uchunguzi wa Magonjwa

 

107.   Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2002/2003, Wizara ya Afya itaendelea na uimarishaji wa upatikanaji wa damu salama na ya kutosha kwa wagonjwa kwa kukamilisha taratibu za uanzishaji wa Huduma ya Kitaifa ya Damu Salama (National Blood Transfusion Services).  Aidha, huduma ya damu salama itaanzishwa katika Kanda ya Nyanda za juu Kusini chini ya hospitali ya Rufaa Mbeya kwa kutoa mafunzo ya wataalamu wa kutoa ushauri nasaha na kuhamasisha wananchi kujitolea damu.  Mafunzo hayo yatagharamiwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa  (UNDP).  Mpango huo utatekelezwa sambamba na ukarabati wa majengo na ununuzi wa vifaa vya kutolea huduma ya damu salama katika kanda zote nne zinazosimamiwa na hospitali za rufaa za Muhimbili, Mbeya, KCMC na Bugando. Taasisi ya Kudhibiti Magonjwa ya Marekani (CDC) imetenga jumla ya dola za marekani milioni 2.0 kwa ajili ya ukarabati na ununuzi wa vifaa hivyo.

.

108.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha, Wizara ya Afya itaendelea kukamilisha ufungaji wa mashine za X-ray na Ultrasound katika hospitali za wilaya na mikoa  iliyokuwa bado kuwekewa mitambo hiyo. Mikoa hiyo ni Mwanza, Mara, Shinyanga, Kagera, Kigoma na Tabora.  Aidha, karakana za kutengeneza vifaa vya kutolea huduma za afya zilizoko kwenye hospitali za  KCMC, Bugando, Muhimbili, Mbeya na Mtwara zitaimarishwa kwa kupatiwa vifaa na magari (Mobile Maintenance Workshop Vehicles) ili viwe na uwezo wa kutengeneza mashine za X-Ray na Ultrasound.

 

109.   Mheshimiwa Spika, Mwongozo wa kisera wa Vifaa vya Kitaalamu vya Kutolea Huduma za Afya “Policy Guidelines for Heath Care Technology” ulioandaliwa mwaka 2001/2002 utaanza kutekelezwa kwa majaribio katika hospitali nne za Rufaa (Muhimbili, Bugando, KCMC na Mbeya) na katika hospitali mbili za Mkoa (Kagera na Tanga). Aidha, mpango ya kufanya na kufuatilia matengenzo ya kinga (Planned Preventive Maintenance) kwa kutumia utaalamu wa kompyuta utaanzishwa katika hospitali hizi.  Wizara inatarajia kujifunza kutokana na uzoefu utakaopatikana katika hospital hizi ili uenezwe katika hospitali zote za mikoa na wilaya.  Aidha, kwa kushirikiana na Kamisheni ya Huduma za Jamii za Kikristo na Baraza kuu la Waislam Tanzania, huduma hizi zitaenezwa pia katika hospitali zinazomilikiwa na mashirika ya dini.

Huduma za Afya ya Kinywa

 

110.   Katika kipindi cha 2002/2003 Wizara yangu inakusudia kununua vifaa vya tiba ya meno kwa ajili ya hospitali za Halmashauri zifuatazo; Arumeru, Rombo, Manyoni, Kibaha, Bagamoyo, Kilosa, Makete, Mufindi, Mpanda, na Tunduru.  Pia madawa muhimu kwa ajili ya tiba ya meno yatanunuliwa na kusambazwa katika kliniki za meno mikoani na wilayani.  Aidha, katika kuimarisha kinga ya magonjwa ya kinywa, vijitabu, mabango na vipeperushi vitatayarishwa kwa ajili ya kufundishia afya ya kinywa kwenye kliniki za mama wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano nchini.

 

Huduma za Afya ya Akili na Madawa ya Kulevya

 

111.   Mheshimiwa Spika, Wizara imekusanya taarifa zinazohusu masuala ya afya ya Akili kutoka mikoa ya Kigoma, Mbeya, Morogoro, Mtwara, Pwani, Shinyanga Singida na Tabora. Taarifa hizo zitachambuliwa na kutolewa ripoti katika mwaka wa fedha 2002/2003. Tunategemea kuwa mchanganuo wa taarifa hizo utasaidia katika kufanya mapitio na Miongozo ya Sera ya afya ya akili nchini. Pia shughuli za kusimamia na kuendeleza mafunzo ya stadi za kukabiliana na maradhi ya akili zitaimarishwa katika mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Dodoma, Mbeya, Mwanza, Mtwara na Dar es Salaam

 

Huduma ya Tiba za Asili

 

112.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa 2002/2003 Wizara ya Afya itaandaa mkakakati na mpango wa muda mrefu wa kuimarisha na kufanya utafiti wa huduma za tiba za asili na tiba mbadala.  Wadau mbalimbali watahamasishwa na kutakiwa kuchangia maendeleo ya sekta hii. Aidha rasimu ya muswada wa sheria itakayosimamia masuala ya dawa na tiba ya asili imekamilika na inatarajiwa kuwasilishwa katika Bunge lako tukufu katika mwaka wa fedha wa 2002/2003.

 

Hospitali za Rufaa

 

113.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa 2002/2003 Wizara ya Afya imetenga shilingi bilioni 15.0 kwa ajili ya ruzuku kwa hospitali za rufaa, hospitali teule za wilaya na hospitali za mashirika ya dini.  Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 13.8 zitatolewa na serikali wakati shilingi  bilioni 1.6  zitatolewa na mfuko wa pamoja wa sekta ya afya. Aidha, hospitali za rufaa, na hospitali za mikoa zimetengewa shilingi  milioni 198.0 kwa ajili ya kupanua mpango wa kuzuia maambukizi ya virusi vya ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Aidha shilingi bilioni 1.4 zimetengwa kwa kuendeleza mabadiliko ya uendeshaji wa huduma za hospitali na shilingi milioni 996.0 kwa ajili ya ukarabati na ununuzi wa vifaa vya kutolea huduma za afya.

 

Hospitali ya Taifa Muhimbili

 

114.   Mheshimiwa Spika, uimarishaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kipindi cha mwaka 2002/2003 utalingana na mwelekeo mpya wa uendeshaji wa hospitali. Hata hivyo mipango iliyokuwepo kabla ya mabadiliko inatarajiwa kuendelezwa. Kati ya mipango hii ni pamoja na kuendeleza ujenzi wa wodi ya watoto kufikia ghorofa ya pili.  Pia utekelzaji wa awamu ya kwanza ya ukarabati mkubwa wa majengo ya hospitali, njia za umeme na njia za mawasiliano unaogharamiwa na mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika utaanza mapema katika mwaka wa fedha 2002/2003.

 

Hospitali ya Rufaa ya KCMC

 

115.   Mheshimiwa spika, sambamba na mabadiliko yanayoendelea katika sekta ya afya hospitali ya KCMC imefanya mabadiliko yenye lengo la kuongeza ufanisi. Katika mabadiliko haya hospitali inatarajia kuweka viwango vya utekelezaji wa wafanyakazi ili kila mmoja apimwe utendaji wake kufuatana na viwango hivyo. Hospitali pia inatarajia kuajiri mafundi sanifu wa maaabara wa kutosha ili kuleta ufanisi katika huduma inayo tolewa na maabara.  Kwa upande wa menejimenti hospitali inatarajia kuendesha warsha kwa ajili ya viongozi katika ngazi mbalimbali ili kuongeza uwezo wa watumishi na kuwezesha utawala bora.  

 

Taasisi ya Saratani ya Ocean Road

 

116    Mheshimiwa Spika,  Ili Taasisi ya Saratani iweze kuyamudu majukumu yake ya kutibu wagonjwa wa Saratani ambao wamekuwa wakiongezeka mwaka hadi mwaka, katika mwaka huu wa fedha Taasisi itanunua mitambo mipya ya mionzi ambayo thamani yake ni shilingi milioni  250.0 na mashine mpya ya matibabu ya  saratani ya thamani ya shilingi milioni 400.0.

 

 

Hospitali ya Bugando

 

117    Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Bugando imeazimia kupunguza matatizo ya nyumba na usafiri yanayo wakabili watumishi wake.  Hivo, hospitali imeazimia kujenga nyumba mbili kila mwaka kwa ajili ya wafanyakazi katika maeneo ya Hospitali.  Pia katika mwaka 2002/2003 hospitali itanunua basi moja kwa ajili ya wafanyakazi.  Kwa upande wa huduma za wagonjwa, hospitali itajenga wodi maalum kwa ajili ya matatizo ya uzazi (V.V.F) kwa kuwa wagonjwa wa tatizo hili wamekuwa wengi na hakuna wodi maalum ya kuwalaza wagonjwa wa aina hii.  Pia Hospitali ya Bugando itaanzisha sehemu ya wagonjwa mahututi ambao wanahitaji uangalizi wa karibu sana kama vile wagonjwa wanaotoka upasuaji mkubwa. Katika eneo la mafunzo hospitali ya Bugando inatarajia mwezi septemba mwaka huu kufungua mafunzo ya shahada ya udaktari wa matibabu chini ya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino.

 

Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili (Muhimbili Orthoaepadics Institute)/MOI

 

118.        Katika kipindi cha mwaka 2002/2003, MOI inatarajia kukamilisha ujenzi wa awamu ya pili ya MOI na inatarajiwa kufunguliwa rasmi mwezi Septemba 2002. Kukamilika kwa awamu hii kutaifanya MOI kuwa Taasisi na hospitali yenye hadhi ya kipekee hapa nchini na hata Afrika Mashariki na Kati katika kutoa huduma kwa kutumia teknolojia ya kisasa. Ujenzi wa awamu ya pili unajumuisha huduma zifuatazo:

 

·        Chumba cha upasuaji kwa dharura (Emergency Theatre).

·        Vyumba vinne vya upasuaji (theatres) vyenye teknolojia ya kisasa.

·        Vyumba viwili kwa ajili ya wagonjwa mahututi (Intensive Care Unit), vyenye vitanda nane.

·        Chumba cha upasuaji wa moyo (open heart surgery theatre) chenye teknolojia ya kisasa.

·        Maabara, Chumba cha kutunzia damu , X-ray na sterilization.

·        Wodi ya vitanda 17 kwa ajili ya wagonjwa binafsi (private patients).

·        Vyumba vya Ofisi za wafanyakazi.

·        Karakana ya umeme na mitambo mingine ya hospitali.

 

Hospitali ya Mirembe na Taasisi ya Isanga

 

119.        Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2002/2003, Hospitali itaendelea kutoa huduma zake kwa wagonjwa wa afya ya akili pia Wizara inakusudia kuendeleza ukarabati wa hospitali ya Mirembe na Taasisi ya Isanga kwa kukarabati wodi tatu za hospitali ya Mirembe na kujenga uzio wa ukuta katika Taasisi ya Isanga. Na kumalizia ukarabati wa mfumo wa Safi na maji taka.

 

Hospitali ya Kibong’oto

 

120.        Mheshimiwa   Spika,    katika    mwaka    2002/2003

Hospitali ya Kifua Kikuu itafanya tathmini ili kulinganisha mahitaji, gharama na faida itakayopatikana kwa kubadili muundo na mfumo wa utoaji huduma kulingana na mpango wa mabadiliko ya sekta ya Afya.  Aidha Hospitli ya Kibong’oto itatekeleza mpango wa kuinua ubora wa huduma zinazotolewa kwa kutoa mafunzo kwa watumishi, kukarabati majengo, kununua vifaa vya kutolea huduma na kuimarisha mkakati dhidi ya ukimwi.  Wizara ya Afya imetenga Jumla ya Shs. 357 milioni kwa ajili ya shughuli hizi, ambapo Shs. 220 milioni ni kutoka bajeti ya Serikali na Shs. 137 milioni ni kutoka mfuko wa pamoja wa wahisani.

 

Huduma za hospitali, Vituo vya Afya, Zahanati na Maduka ya dawa ya watu binafsi

 

121.        Mheshimiwa Spika, Wizara inathamini mchango wa hospitali, Vituo vya Afya, Zahanati na maduka ya dawa ya watu binafsi katika kutoa huduma kwa wananchi. Hadi sasa kuna jumla ya hospitali 125 Vituo vya Afya 137 Zahanati 1537 na maduka ya dawa ya Part I 520 yaliyosajiliwa na Msajili wa Hospitali Binafsi pamoja na Msajili wa Bodi ya Madawa. Katika kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Sekta Binafsi na Wizara,Wizara imekuwa ikiwaalika wawakilishi wa Chama Cha Wenye Kumiliki Hospitali binafsi katika mikutano mbalimbali ya kujadili maendeleo ya sekta hii kama vile mapitio ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya sekta ya afya yanayofanyika kila mwaka pamoja na kumteua mwakilishi wa Chama hicho katika Bodi ya Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa. Wizara inakusudia pia kupunguza muda wa kutoa leseni baada ya kupokelewa maombi kutoka wastani wa siku zaidi 120 hadi 30. Aidha Wizara itaongeza idadi ya ukaguzi wa huduma hizi ili kuzifanya ziwe bora zaidi.Wizara inatoa shukurani nyingi kwa watu binafsi ambao wamesaidia kusogeza huduma za afya kwa wananchi. Tunawaomba wananchi katika siku zijazo kuendelea kufungua huduma hasa zile za matibabu maalumu kama vile ya upasuaji wa moyo, ubadilishaji wa figo na kadhalika. Ili watu waweze kutibiwa ndani ya nchi. Serikali inaahidi kuimarisha na kuongeza ushirikiano uliopo baina yake na sekta ya watoa huduma za matibabu binafsi.

 

HUDUMA ZA UTAWALA NA UTUMISHI

 

122.Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya imetenga fedha

kiasi cha shilingi milioni 897.5 za kununua magari kwa

ajili ya usimamizi ambayo yatagawanywa katika halmashauri zifuatazo; Arumeru , Korogwe, Handeni, Kwimba, Mtwara, Nzega, Musoma, Rungwe, Mbarali, Ukerewe, Pangani, Kilosa, Kibaha, Arusha, Mbinga, Bukoba, Same, Mbeya, Mwanga, Dodoma, Mafia, Kisarawe, Mufindi, Tarime, Morogoro, Mbozi, Geita, Nachingwea, Misungwi, Kinondoni, Igunga, Makete, Kibondo, Temeke, Sikonge na Ilala. .Magari hayo yatasaidia kuongeza usimamizi na ufuatiliaji wa huduma za afya wilayani Aidha, Wizara itaendelea na zoezi la kuwapandisha vyeo watumishi wa sekta ya Afya. Katika mwaka wa fedha wa 2002/2003, Wizara inatarajia  kuwapandisha vyeo watumishi 10,000.

 

 

HUDUMA YA MAFUNZO YA WATUMISHI WA AFYA

 

123.        Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002/2003 huduma ya mafunzo ya watumishi wa sekta ya afya imepanga kutekeleza mambo muhimu yafuatayo;_

 

·        Kuendelea kukarabati vyuo vingine 20 ilikuboresha majengo ya kufundishia.

 

 

·        Kuendesha mafunzo ya menejimenti kwa wilaya arobaini na moja zilizobali (41) ili kuzipa uwezo wa wa kiutendaji na utekelezaji wa huduma zinazotolewa.

·        Kununua magari matano mengine kwa ajili ya vyuo ilikuboresha mafunzo kwa vitendo kwa kuwawezesha wanafunzi kufika sehemu za mazoezi.

·        Kuendesha kozi mbili za mafunzo ya menejimenti kwa madaktari wanaohitimu  inter doctors) kabla ya kupangiwa vituo.

·        Kununua vitabu na vijarida kwa ajili ya maktaba vyuo thelasini (30).

·        Kutoa mafunzo ya kujiendeleza kwa walimu 48 ilikuinua uwezo wao wa ufundishaji katika vyuo.

·        Kuendelea kupitia upya mitaala minane zaidi ili iendane na mahitaji ya wakati uliopo na mabadiliko ya kisekta yanayoendelea.

 

OFISI YA MGANGA MKUU KIONGOZI

 

Huduma za Uuguzi

 

124.Mheshimiwa Spika,   katika  kipindi cha  mwaka wa

fedha wa 2002/2003, Wizara inatarajia kufanya usimamizi wa huduma za uuguzi katika mikoa tisa. Pia Wizara, itafanya utafiti wa jinsi huduma za uuguzi zinavyopokelewa na wananchi na ubora wa huduma za uuguzi. Utafiti huu utafanyika katika mikoa mitatu itakayochaguliwa hapo baadaye, kufuatana na miongozo ya uchaguzi wa sampuli za utafiti. Wizara pia imekubali kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa wauguzi wa nchi kumi na nne ambao ni wanachama wa Chuo Kikuu cha Wauguzi wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini (ECSACON).

Ukaguzi wa Huduma za Afya

 

125.Mheshimiwa Spika,   katika   kipindi  cha  fedha  cha 

2002/2003 Wizara imepanga kutekeleza  kazi zifuatazo; kufanya ukaguzi wa utoaji huduma za afya katika mikoa 8 ikiwa inajumuisha wilaya 16 yaani wilaya 2 kila mkoa, kutathmini ubora wa huduma  za afya zinazotolewa katika jamii ya Tanzania na kuendelea kusambaza mwongozo wa viwango vya utendaji kazi katika huduma za afya nchini.

 

Huduma za Dharura na Maafa

 

126. Mheshimiwa  Spika,     katika    kipindi   cha   mwaka

2002/2003,     Kitengo    kinakusudia     kufanya     kazi

zifuatazo; kutembelea mikoa 12 ya Tanzania Bara na baadhi ya wilaya zake kwa lengo la kufanya ufuatiliaji na usimamizi wa huduma za afya za maafa, ili kutoa ushauri na maelekezo ya kitaalam katika kuboresha huduma hizo nchini. Vilevile,kitakamilisha mwongozo wa utoaji huduma za Dharura na Maafa (Health Sector Guideline and Protocol on Emergency and Disaster Management) na kuusambaza katika vituo vyote vya huduma nchini. Kitengo pia kitatoa mafunzo ya Tiba ya Dharura na Maafa kwa wanafunzi Madaktari na Wauguzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Muhimbili, kwa kutumia mitaala maalumu iliyoandaliwa kwa ushirikiano na Taasisi ya Magonjwa ya kuambukiza cha CDC (USA), Chuo Kikuu cha John Hopkins (USA) na Chuo Kikuu cha Muhmbili.

 

 

 

 

TAASISI, TUME NA BODI ZILIZOPO CHINI YA WIZARA YA AFYA

 

Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania

 

127. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2002/2003,

Taasisi  ya  Chakula   na   Lishe itaendelea   kuratibu

kampeni za utoaji wa matone ya vitamini A kwa watoto wote wenye umri wa miezi 6 hadi miaka 5 katika mikoa yote ya Tanzania bara.  Sambamba na utoaji wa matone ya vitamini A, Taasisi itaendelea na kuhamasisha viongozi na jamii kuhusu umuhimu wa uzalishaji na ulaji wa vyakula vyenye vitamini A kwa wingi ikiwa ni hatua ya kudumu ya kuzuia na kudhibiti matatizo yatokanayo na upungufu wa vitamini A kwa jamii yote ya Tanzania.

 

128.Mheshimiwa Spika, Taasisi vilevile, itaendelea na

usambazaji wa machine za kupimia damu katika Wilaya 59 zilizobaki na kusimamia utoaji wa dawa za kuongeza damu na kutibu minyoo kwa watoto wenye umri  chini ya miaka mitano wilayani Bagamoyo. Aidha, Taasisi itaendelea na mikakati ya kuboresha vyakula vya kulikiza pamoja na vile vya watoto walioathirika na ukimwi na makundi mengine maalum. Taasisi pia itaendelea kutoa mafunzo na kuelimisha vikundi na watu mbalimbali juu ya uboreshaji wa vyakula vya kulikiza kwa kutumia teknolojia rahisi na kuandaa  mwongozo wa utengenezaji wa vyakula kwa makundi maalum.

 

129.Mheshimiwa  Spika,   Taasisi  itaelekeza  juhudi  zake

katika kueneza teknolojia rahisi ya usindikaji na hifadhi

ya mhogo, viazi vitamu, mboga na matunda na  kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kutumia chakula kwa uangalifu ili kuhakikisha upatikanaji katika ngazi ya kaya kwa mwaka mzima. Vile vile Taasisi kwa kushirikiana na Taasisi husika itaendelea kufuatilia usalama na ubora wa vyakula vinavyotumika humu nchini.

 

Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu

 

130.Mheshimiwa   Spika,     katika    kipindi   cha   mwaka

2002/2003  Taasisi  imepanga   kutoa  dawa  za  kuzuia

ugonjwa wa matende na ngiri maji kwa wananchi wa wilaya zote ili kuhakikisha kuwa hakuna mwananchi atakaye athirika kwa ugonjwa wa matende na  ngiri maji ifikapo mwaka 2020.  Hali kadhalika,  ili kuimarisha shughuli za utafiti taasisi itapatiwa msaada wa kujenga majengo mapya ya ofisi na kuyavunja yale ya zamani.  Msaada huu utatolewa na Center for Disease Control ya Marekani na Serikali imepanga kuchangia shilingi milioni 10.0 kwa ajili ya ujenzi wa maabara na ofisi za taasisi  tawi la Tukuyu. Aidha, Taasisi imetayarisha mradi utakaochangia ujenzi wa kituo cha Centre for Enhancement of Malaria Intervention (CEEMI), Joint Malaria Programme na ofisi za National Malaria Control Program.  Mradi unafadhaliwa na Bill and Melinda Gates Foundation kupitia London School of Hygine and Tropical Medicine.  Mfadhili ametoa ahadi kutoa msaada zaidi kwa ajili ya ujenzi wa Malaria Reference Laboratory katika hospitali ya Bombo, Tanga.

 

 

 

Bodi ya Madawa

131.Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002/2003, Bodi ya

Madawa itaendelea na ufuatiliaji wa usalama wa dawa

kwenye soko kwa kuzingatia utaratibu wa usajili wa dawa ambao umekuwepo kuanzia mwaka 1998.  Katika zoezi hili dawa za malaria, Kifua Kikuu na zile zinazosaidia kupunguza makali kwa wagonjwa wenye virusi vya ukimwi zitapewa kipaumbele.  Bodi ya Madawa inalenga kukabiliana na tatizo la uingizaji nchini wa dawa zisizofikia viwango na dawa bandia ambazo zinaaminika kuingizwa kwa kupitia njia za zisizohalali au kwa udanganyifu. Bodi pia ina malengo ya kuelimisha wananchi juu ya matumizi sahihi ya dawa na jinsi ya kuweza kupata huduma ya uhakika ya dawa.

 

132.Mheshimiwa  Spika,      ili   Bodi   ya   Madawa  iweze

kukabiliana na matatizo haya, Bodi imejiwekea mkakati wa kutimiza malengo muhimu yafuatayo:

 

·        Kuongeza idadi ya wakaguzi katika ngazi mbalimbali hususan katika mipaka na  kanda zake za ukaguzi .

·        Kufanyia ukaguzi wa mara kwa mara wa maduka ya dawa.

·        Kuimarisha maabara ya uchunguzi wa dawa kwa kuongezea vifaa vya kisasa na wataalam.

·        Kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali, Bodi ya Madawa itaimarisha mikakati ya kukabiliana na tatizo la madawa ya kulevya:

 

133.Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya iko katika hatua

za mwisho za kuunganisha Bodi ya Madawa na Tume

ya Taifa ya Kudhibiti Ubora wa Vyakula ili kuunda chombo madhubuti cha kudhibiti biashara ya dawa, chakula na vipodozi.  Ili kutimiza azma hiyo, Sheria Na. 9 ya Dawa na Sumu na Sheria Na. 10 ya Kudhibiti Ubora wa vyakula zote za mwaka 1978, zitafutwa na kuunda sheria mpya itakayosimamia udhibiti wa vyakula, dawa na vipodozi. Muswada wa sheria hiyo umekwishasomwa kwa mara ya kwanza Bungeni.   Aidha masuala ya usimamizi wa maadili ya fani ya famasia yatasimamiwa na Baraza la Famasia ambalo litafanya kazi zake chini ya Sheria mpya ya Famasia ya mwaka 2002.

 

Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali:

 

134.        Mheshimiwa Spika Ofisi ya Maabara ya Mkemia  Mkuu wa Serikali ni mojawapo ya wakala za serikali zilizo chini ya Wizara ya Afya. Katika mwaka wa fedha wa 2002/2003, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali itaendelea na kazi za uchunguzi wa sampuli mbalimbali kwa nia ya kutoa vidhibiti mahakamani na kuhakikisha usalama wa bidhaa mbalimbali zinazotumiwa na binadamu. Ilikuwezesha wakala hii kufanya kazi zake vizuri ipasavyo. Wizara imepanga kujenga chumba cha kuteketezea kemikali zilizoharibika na kufunga mashine itakayofanya kazi hiyo (Incinerator). Kununua mashine ya kuzalisha umeme pamoja na kujenga chumba cha kuifunga mashine hiyo. Kuweka mfumo wa kuzuia moto. Kuweka mfumo wa mashine za kupoza hewa katika ofisi zote. Kufanya utafiti wa jinsi ya kuanzisha maabara za kanda.

 

 

 

 

Tume ya kudhibiti vyakula ya Taifa (TUKUTA)

 

135.        Mheshimiwa Spika, hata baada ya TUKUTA kuunganishwa na Bodi ya Madawa kazi zilizopangwa kutekelezwa mwaka huu zitaendelea kutekelezwa chini ya Taasisi mpya kama ifuatavyo:- Kuendelea kutoa mafunzo kwa Maafisa Afya na wenye viwanda kuhusu mfumo makini wa utengenezaji vyakula salama na bora katika wilaya zote za Tanzania Bara. Kutoa mafunzo kwa Maafisa Afya kuhusu namna ya kutumia mwongozo wa kitaifa wa ukaguzi wa viwanda vya chakula. Kutayarisha miongozo kuhusu mfumo wa usajili wa majengo ya kuuzia na kutengenezea vyakula na utoaji wa leseni. Kufanya ukaguzi wa vyakula katika mikoa 21 ya Tanzania Bara. Kuchunguza kiwango cha masalio ya madawa na kemikali nyingine mbalimbali katika vyakula. Kuendelea kufanya utafiti juu ya athari zinazoweza kumpata mlaji kutokana na vifaa mbalimbali vya kufungia vyakula, ikiwemo mifuko ya plastiki. Kukusanya na kutafiti viwango vya madawa katika nyama na mazao yatokanayo na maziwa.

 

Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya

 

136.        Mheshiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha Wizara yangu inakusudia kuimarisha Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kuupatia fedha za kutoa elimu kwa wanaonufaika na Mfuko huo. Kuwawezesha kuanzisha Ofisi za Kanda. Kuwapatia vitendea kazi iliwaweze kushughulikia madai ya hospitali kwa haraka iwezekanavyo. Aidha, Wizara inaandaa mapendekezo ya marekebisho ya sheria iliyounda Mfuko huo iliiweze kutatua matatizo yaliyojitokeza wakati wa utekelezaji wa Mfuko huo.

 

USHIRIKIANO WA NDANI NA NJE YA NCHI YETU

 

Nchi na Mashirika kutoka nje

 

137.         Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/ 2002 sekta ya afya imeendelea kupata ushirikiano mkubwa kutoka nchi za nje na mashirika ya kimataifa. Ushirikiano huo ulilenga zaidi katika maeneo ya mabadiliko ya sekta ya afya, uboreshaji huduma, ununuzi wa dawa na vifaa, ukarabati wa majengo na masomo ya nchi za nje. Nchi hizo na mashirika mbalimbali tuliyoshirikiana nayo ni:- China, Cuba, Canada, Denmark, Hispania, India, Ireland,  Italia, Japan, Korea ya Kusini, Marekani, Misri, Norway, Switzerland, Sweden, Uholanzi, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, , Benki ya Dunia , Benki ya Maendeleo ya Afrika, Benki ya Nchi za Kiarabu kwa ajili ya Maendeleo ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika ( BADEA), OPEC, Jumuia ya Nchi za Ulaya (EU), Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO), Shirika la kuhudumia Watoto  (UNICEF), Shirika la Kimataifa la Uzazi wa Mpango (UNFPA), UNAIDS, Shirika la Kimataifa la kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) na Madaktari Wasio na Mipaka,  (Medicins Sans Frontieres), MISERIOR, African Programme for Onchorcerciasis Control, Hellen Keller Foundation na International Trachoma Initiatives, Bill & Melinda Gates Foundation, Abott Laboratories, Axios International, Merck, Pfizer Inc. Wizara ya Afya inatoa shukrani za dhati kwa nchi na mashirika yote yanayoendelea kushirikina nasi katika kuinua afya ya Watanzania.

 

 

 

 

Taasisi na Mashirika ya Hapa Nchini

 

138.   Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya ina furaha kulifahamisha Bunge lako Tukufu  kuwa hapa nchini sekta ya afya inayo pia washiriki wengi.Ingawaje sitaweza kuataja washiriki wote, napenda kutoa shukrani za dhati kwa mashirika yafuatayo:- Shirika la Aga Khan, AMREF, BAKWATA, CCBRT, TAC AIDS, CCT, CSSC, ELCT, TEC, Msalaba Mwekundu, Shree Hindu Mandal na TANESA na mashirika yote yasiyo ya kiserikali yanayoshirikiana na Wizara. Kwa ushirikiano wao katika kukuza sekta ya afya.

 

MWISHO

 

139.Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie hotuba yangu kwa kutoa shukrani zangu za dhati kwa viongozi wa Wizara ya Afya, Mheshimiwa Dk. Hussein Alli Mwinyi, Mb. Naibu Waziri wa Afya, Mbunge wa Mkuranga, Ndugu Mariam Joy Mwaffisi, Katibu Mkuu, Dk. Gabriel Upunda, Mganga Mkuu Kiongozi, Wakurugenzi wa Idara Wizara ya Afya, Wakurugenzi wa Hospitali za Rufaa na Taasisi za Afya na Waganga Wakuu wa Mikoa Wilaya na wafanyakazi wote wa sekta ya Afya popote walipo. Ushirikiano wao wa karibu ndiyo ulioiwezesha Wizara kupiga hatua kubwa ya maendeleo katika kipindi chote cha mwaka uliopita. Vilevile nawashukuru na kuwapongeza wafanyakazi wote wa sekta ya afya popote pale walipo kwa kuendelea na moyo wa uadilifu katika kuwatumikia wananchi. Nina waomba waendelee kuzingatia maadili yao ya kazi hii nyeti. Nachukua pia nafasi hii kuwashukuru wananchi wa jimbo la Lulindi walioniwezesha kupata nafasi hii ya kulitumikia taifa.

 

140.   Mheshimiwa Spika, ili kuiwezesha Wizara ya Afya kutekeleza hayo niliyoyaeleza naliomba Bunge lako Tukufu litafakari, lijadili na kuidhinisha Makadirio ya Wizara ya Afya ya jumla ya shillingi 103,100,021,600 kati ya hizo shillingi 52,003,350,600, ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi 51,096,671,000 kwa ajili ya Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2002/2003.  Kati ya fedha ya maendeleo shilingi 3,552,448,200 ni fedha ya ndani na shilingi 47,544,222,800 ikiwa ni fedha kutoka nje ya nchi.

 

141.        Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Kiambatanisho Na.1

 

KIREFU CHA MAJINA YA MASHIRIKA YA KITAIFA NA KIMATAIFA YANAYOSAIDIA HUDUMA ZA AFYA.

 

ADB                =         African Development Bank

AMREF          =         African Medical and Research Foundation

BADEA          =         Bangue Arabe pour Développement

Enonomique en Afrique

BAKWATA    =         Baraza Kuu la Waislam Tanzania

CBM               =         Christoffel Blinden Mission

CCT                =         Christian Council of Tanzania

CSSC              =         Christian Social Services Commission

CUAMM         =         International College for Health Cooperation

in Developing Countries

DANIDA        =         Danish International Development Agency

DFID              =         Department For International Development

DSE                =         Deutsche Stiftung fur Internationale

Entwicklung

ELCT              =         Evangelical Lutheran Church of Tanzania

EU                  =         European Union

FINNIDA       =         Finnish International Development Agency

GSF                =         Good Samaritan Foundation

GTZ                =         Gesellschaft fuer Technische Zusammenarbeit

IDRC              =         International Development Research Centre of

Canada

JICA               =         Japan International Cooperation Agency

NBC                =         National bank of Commerce

NIMR              =         National Institute of Medical Research

NORAD          =         Norwegian Agency for Development

NSSF              =         National Social Security Fund

SAREC           =         Swedish Agency for Research Cooperation in

Developing Countries

SDC                =         Swiss Agency for Development and

Cooperation

SIDA               =         Swedish International Development Authority

TAMWA         =         Tanzania Media Women Association

TANESA        =         Tanzania Netherlands Support to AIDS control

TANESCO     =         Tanzania Electric Supply Company

TBL                =         Tanzania Breweries Limited

TEC                =         Tanzania Episcopal Conference

TPDC             =         Tanzania Petroleum Development

Corporation

TRA                =         Tanzania Revenue Authority

TTCL              =         Tanzania Telecommunication Company

Limited

UNDP             =         United Nations Development Programme

UNFPA          =         United Nations Fund for Population Activities

UNHCR          =         United Nations High Commission for Refugees

UNICEF        =         United Nations Children Fund

USADEFU     =         Usambara Development Fund

USAID            =         United State Agency for International

Development

WHO               =         World Health Organisation

 

 

 


Kiambatanisho Na. 2

 

Wanafunzi waliohitimu katika Vyuo vya Wizara ya Afya kwa Mwaka 2001

 

 

Na.

KADA

IDADI

1.

Stashahada ya Juu Uuguzi (Afya ya Jamii)

20

2.

Stashahada ya Uuguzi

403

3.

Cheti cha Uuguzi

522

4.

Cheti cha Uuguzi/Ukunga

408

5.

Uuguzi Afya ya Jamii (B)

197

6.

Maafisa kumbukumbu za Afya

15

7.

Mafundi Sanifu Maabara Wasaidizi

108

8.

Mafundi Dawa Wasaidizi

18

9.

Mafundi wa Eksrei Wasaidizi

10

10

Tabibu

235

11.

Wazoeza Viungo (Physiotherapists)

9

12.

Fundi Mewani (Optometry)

12

13.

Madaktari Wasaidizi (AMO)

165

14.

Madaktari Wasaidizi (Meno)

8

 

JUMLA

2,130

 

 

 

 

Kiambatanisho Na. 4

 

Orodha ya Wilaya ambazo zitaanza mpango wa kuagiza dawa na vifaa vya hospitali kulingana na Mahitaji (indent  system).

 

1.      Igunga+

2.      Nzega+

3.      Iramba+

4.      Singida(V)+

5.      Hanang+

6.      Kilosa+

7.      Iringa(V)+

8.      Songea(M)+

9.      Songea(V)+

10.  Mbinga+

11.  Babati*

12.  Monduli*

13.  Simanjiro*

14.  Kiteto

15.  Masasi*

16.  Ulanga

17.  Hai*

18.   Karatu*

19.  Mufindi

20.  Njombe

21.  Mtwara(V)*

22.  Kisarawe

23.  Kasulu

24.  Mbulu*

25.  Mwanga

26.  Sumbawanga(V)

27.  Tandahimba*

28.  Arusha Munispaa*

29. Rombo*

 


 


Kiambatanisho Na. 3

 

Mtiririko wa wagonjwa wa Ukoma, Tanzania:2000 - 2001

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Mkoa

 

2000

 

 

2001

 

 

2002 January - March

 

 

 

Wapya

Waza

mani

Jumla

Wapya

Waza

mani

Jumla

Wapya

Waza

mani

Jumla

 

Arusha

PB + MB

17

2

19

3

2

5

2

0

2

 

Dar es salaam

PB + MB

370

43

413

385

46

431

117

6

123

 

Dodoma

PB + MB

144

18

162

206

29

235

41

8

49

 

Iringa

PB + MB

28

5