HOTUBA YA WAZIRI WA FEDHA

MHESHIMIWA BASIL P. MRAMBA (MB.),

AKIWASILISHA KATIKA BUNGE MAPENDEKEZO YA SERIKALI KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI

KWA MWAKA 2004/05

 

UTANGULIZI:

 

1.      Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba, Bunge likubali kujadili na kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali katika mwaka wa fedha wa 2004/05.  Takwimu zinazoelezea kwa undani Bajeti hii ziko kwenye vitabu vinne (4) ambavyo ni sehemu ya Bajeti hii.  Kitabu cha kwanza kinahusu makisio ya mapato, Kitabu cha pili na cha tatu vinahusu makisio ya matumizi ya kawaida kwa Wizara, Idara, Mikoa pamoja na Halmashauri za Miji na Wilaya.  Kitabu cha nne kinaelezea makadirio ya matumizi ya maendeleo kwa Wizara, Idara, Mikoa, na Halmashauri.  Aidha, upo Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2004/05.

 

2.      Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine kufanikisha matayarisho ya bajeti, hususan Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge na Kamati za Kisekta; kwa kazi zao nzuri za kuchambua makisio yote kwa kina.  Ushauri uliotolewa na Kamati hizo umesaidia sana kuboresha bajeti ninayowasilisha leo.

 

3.      Mheshimiwa Spika, maandalizi ya bajeti hii yamehusisha wadau wengi ndani na nje ya Serikali. Napenda kuwashukuru wote waliochangia ambao ni pamoja na wafanyakazi wa Wizara mbalimbali, Idara zinazojitegemea, Mikoa na Halmashauri zote za Wilaya, Miji, Manispaa na Jiji, Asasi zisizo za Kiserikali pamoja na sekta binafsi, kwa michango yao iliyosaidia kufanikisha utayarishaji wa bajeti hii.  Aidha, napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutayarisha Miswada na Nyaraka mbalimbali za Sheria ambazo ni sehemu ya bajeti hii.  Nawashukuru pia wenzangu wa Wizara ya Fedha, Manaibu Waziri, Mheshimiwa Abdisalaam Issa Khatibu (Mb.) na Mheshimiwa Dr. Festus Limbu (Mb.); Makatibu Wakuu Bw. Gray S. Mgonja na Bw. Peniel M. Lyimo,  Manaibu Katibu Mkuu Bw. Ramadhani Khijjah na Bw. Wilfred Nyachia, Wakuu wa Idara, na wafanyakazi wengine wote kwa michango yao iliyowezesha bajeti hii kukamilika.  Vile vile, namshukuru Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kwa kuchapisha kwa wakati hotuba hii, vitabu vya bajeti pamoja na nyaraka nyingine zinazohusu bajeti hii. Mwisho, nawashukuru wale wote waliowasilisha kwangu mapendekezo yao ya kodi mpya au ya kurekebisha kodi zilizopo na pia wataalam wote waliotoa ushauri kuhusu sera na namna ya kutoza kodi mbali mbali nchini, pamoja na matumizi ya mapato yetu ambapo mengi yamezingatiwa katika kuandaa bajeti hii.

 

4.      Mheshimiwa Spika, mwaka huu wa fedha tumeshuhudia kuundwa rasmi kwa Bunge la Afrika.  Napenda kuchukua fursa hii kuwapongeza Wabunge wote waliochaguliwa kutuwakilisha katika Bunge hilo ambao ni Mhe. Gertrude Mongella, Mbunge wa Ukerewe, Mhe. Dr. William F. Shija, Mbunge wa Sengerema, Mhe. Dr. Amani W. A. Kabourou, Mbunge wa Kigoma Mjini,     Mhe. Dr. Remigius Edington Kissassi, Mbunge wa Dimani Zanzibar, na Mhe. Athumani Janguo, Mbunge wa Kisarawe.  Aidha, pongezi za pekee nazitoa kwa Mhe. Mongella kwa kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Kwanza wa Bunge hilo.  Uchaguzi wake unaonyesha imani kubwa waliyo nayo Wabunge wa Bunge la Afrika kwake binafsi na kwa Tanzania kwa ujumla.  Sina shaka kwamba Mhe. Mongella ataifanya kazi hiyo kwa umakini mkubwa ili kufanikisha malengo ya Bunge hilo na hivyo kuiletea heshima nchi yetu. 

 

5.      Napenda kuchukua fursa hii pia kumpongeza Mhe. Arcado Ntagazwa, Mbunge wa Muhambwe, kwa kuteuliwa kwake kuwa Rais wa Baraza la Kimataifa la Mazingira.   Naamini kwamba uteuzi huo si wa kubahatisha bali unaonyesha imani waliyo nayo Wajumbe wa Baraza hilo kwa Mhe. Ntagazwa na kwa nchi yetu.  Vile vile, ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Sophia Simba, Mbunge Viti Maalum na pia Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Maendeleo ya Jamii kwa kuteuliwa kuiwakilisha Tanzania katika Baraza la Wabunge wa SADC, yaani “SADC Parliamentary Forum”. Narudia tena kuwapongeza wote na ninawatakia kazi njema katika majukumu hayo mapya.

 

6.      Mheshimiwa Spika, tunakumbuka kwamba, tarehe 30 Mei, mwaka huu kulifanyika uchaguzi mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Bariadi Mashariki, Mkoa wa Shinyanga, ambao umemrudisha Bungeni Mheshimiwa Danhi Makanga kwa kishindo na kwa tiketi ya CCM.  Uchaguzi huo ulifuatia mtafaruku baina yake na chama chake cha UDP ambapo ilibidi akihame chama hicho na kurejea tena kwenye Chama cha Mapinduzi.  Nampongeza Mheshimiwa Makanga kwa ushindi wake katika uchaguzi huo, na pia wananchi wa Bariadi Mashariki kwa kutorudia kosa la kutokiri umaarufu wa CCM na kukubalika kwa Mheshimiwa Makanga miongoni mwa wapiga kura wa Bariadi Mashariki. Aidha, Waheshimiwa Wabunge watakumbuka kwamba katika mwaka huu wa fedha, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, alimteua Mhe. Makongoro Nyerere kuwa Mbunge.  Napenda pia kumpongeza Mhe. Makongoro Nyerere kwa uteuzi huo na kwa kurejea kwenye Chama alicho asisi hayati baba yake ambaye ni Baba wa CCM na wa Taifa letu.

 

7.      Mheshimiwa Spika, matukio mengine muhimu yaliyotokea mwaka huu wa fedha ni pamoja na kuteuliwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa na pia Mtanzania mwenzetu, Profesa Anna Tibaijuka, kuwa Makamishna katika Kamisheni ya Afrika iliyoundwa na Waziri Mkuu wa Uingereza, Mhe. Tony Blair.  Kamisheni hii ina jukumu la kutathmini vikwazo ambavyo vimekuwa vikirudisha nyuma maendeleo ya Bara la Afrika na kupendekeza nini kifanywe kuondokana navyo.  Uteuzi wa Rais Mkapa umetokana na juhudi zake za kuyapa kipaumbele matatizo ya Bara la Afrika, hususan matatizo ya maendeleo na umaskini uliokithiri pamoja na ufahamu wa Rais Mkapa wa masuala ya utandawazi. Uzoefu wake kama Rais wa nchi ya Kiafrika inayojizatiti kupiga vita umaskini na kuleta maendeleo ya wananchi wake unatambulika duniani.  Sote tunajivunia uteuzi huo wa Rais Mkapa na wa Profesa Tibaijuka ambae ni Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Makazi duniani.  Tunawapongeza Watanzania hao kwa kazi nzito wanazoufanyia ulimwengu na heshima kubwa wanayo iletea nchi yetu katika kutekeleza majukumu hayo mazito mazito.   

UTEKELEZAJI WA SERA ZA BAJETI YA MWAKA 2003/04:

 

Hali ya Uchumi

8.      Mheshimiwa Spika, tathmini ya hali ya uchumi katika mwaka 2003/04 inaonyesha maendeleo ya kuridhisha, licha ya ukame ulioikumba nchi yetu.  Takwimu za awali zinaonyesha kwamba uchumi ulikua kwa asilimia 5.6 mwaka 2003 badala ya lengo letu la asilimia 6.3.  Kasi ya mfumuko wa bei iliongezeka kidogo kutoka asilimia 4.0 mwezi Julai 2003 hadi asilimia 4.6 mwezi Machi 2004.  Mfumuko wa bei ulitokana na upungufu wa chakula kutokana na ukame, pamoja na ongezeko kubwa la bei ya mafuta ya petroli.  Akiba ya fedha za kigeni mwishoni mwa Machi, 2004 ilifikia uwezo wa kugharamia mahitaji muhimu kutoka nje kwa kipindi cha zaidi ya miezi minane ambayo ni zaidi ya lengo la miezi sita. 

 

9.      Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Bajeti ya Serikali ya mwaka 2003/04, umekuwa wa kuridhisha, licha ya dharura iliyoletwa na ukame, hasa katika kuongeza mahitaji ya fedha ya bajeti kwa ajili ya kununua na kusambaza chakula, pamoja na kulazimika kutoa ruzuku kwa TANESCO kwa ajili ya kununulia mafuta ya kuendesha mitambo ya kuzalisha umeme, na kununua umeme wa mtambo wa IPTL.

10.    Katika bajeti ya mwaka 2003/04 Serikali ililenga kukusanya mapato ya ndani yasiyopungua asilimia 13.3 ya Pato la Taifa.  Ili kufanikisha lengo hili, Serikali ilikusudia kutekeleza hatua kadhaa za kurekebisha mfumo na utawala wa kodi.  Marekebisho hayo yalilenga kupanua wigo wa kodi, kuongeza uwajibikaji kwa watoza kodi na walipa kodi, kuondoa kodi za kero, kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kuongeza ufanisi wa utendaji katika Mamlaka ya Mapato Tanzania.  Aidha Sheria mpya ya Kodi ya Mapato iliwasilishwa na kupitishwa Bungeni mwezi Aprili mwaka huu wa fedha.

 

11.    Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya mwaka huu wa fedha yaani kuanzia Julai, 2003 hadi Aprili, 2004 ukusanyaji wa mapato ya ndani umevuka lengo kwa kila mwezi.  Aidha, misaada ya bajeti kutoka kwa Nchi Wafadhili, Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika na Umoja wa Ulaya, ilivuka lengo.  Sehemu kubwa ya misaada hiyo ilipatikana katika nusu ya kwanza ya mwaka huu wa fedha na hivyo kutupa uwezo zaidi wa kumiliki bajeti hiyo.  Inatarajiwa kwamba malengo ya mapato ya ndani na misaada ya bajeti kwa mwaka huu yatafikiwa ifikapo mwisho wa mwaka huu wa fedha.

12.    Mheshimiwa Spika, mapato halisi ya ndani kwa kipindi cha Julai, 2003 hadi Machi, 2004 yalifikia shilingi trilioni moja, bilioni themanini na tisa, milioni mia mbili sitini na mbili (1,089,262 milioni) sawa na asilimia 3.7 au shilingi milioni 38,396 zaidi ya makisio ya bajeti ya shilingi trilioni moja, bilioni hamsini, mia nane sitini na sita milioni (1,050,866 milioni).  Kodi ya VAT kwenye mauzo ya ndani ya nchi ilikadiriwa kuwa shilingi milioni 142,242 katika kipindi hicho, lakini makusanyo halisi yalifikia shilingi milioni 148,632, ambayo ni ziada ya shilingi milioni 6,390 au asilimia 4.5 juu ya makisio kwa kipindi hicho.  Kwa upande wa Kodi ya Mapato, makusanyo halisi yalifikia shilingi milioni 256,888 ikilinganishwa na makisio ya shilingi 227,382 milioni, sawa na ziada ya shilingi milioni 29,506 au asilimia 13 juu ya makadirio.  Ukusanyaji wa Ushuru wa Forodha ulifikia shilingi milioni 95,239 ukilinganishwa na makadirio ya shilingi milioni 93,562, na hivyo kuwa na ziada ya shilingi milioni 1,677 sawa na asilimia 1.8 juu ya makadirio.  Aidha, mapato yasiyo ya kodi (non-tax revenue) yakijumuisha mapato ya Wizara, Idara mbali mbali na Mikoa, yalifikia shilingi milioni 87,368 ikiwa ni chini ya lengo la shilingi milioni 96,951.

 

13.  Mheshimiwa Spika, sababu kuu zilizochangia kuongezeka kwa Mapato ya Serikali ni pamoja na usimamizi na utawala bora wa ukusanyaji wa kodi, hasa Kodi ya Mapato na Kodi ya Ongezeko la Thamani, (VAT).  La muhimu zaidi ni zile hatua tulizochukua kudhibiti ukwepaji wa kodi katika biashara ya mafuta ya petroli. 

 

14.    Kwa muhtasari matokeo mazuri ya hatua zilizochukuliwa na Serikali kwa lengo la kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali ni pamoja na haya yafuatayo:-

 

Kwanza:

Marekebisho ya viwango vya ushuru wa forodha ambayo yameipatia Serikali mapato ya shilingi milioni 1,717 kwa kipindi cha Julai 2003 hadi Machi 2004 ikilinganishwa na lengo la shilingi milioni 133.8 kwa mwaka 2003/04.  Hii ni sawa na ziada ya asilimia 1,183.

 

Pili:

Marekebisho ya Ushuru wa bidhaa katika bidhaa mbali mbali, yaliyoipatia Serikali mapato ya ziada ya shilingi milioni 758.5 katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2003.

 

Tatu:

          Kupunguzwa kwa ushuru wa bidhaa kwa gesi ya kupikia (LPG) kutoka shilingi 228 hadi shilingi 114 kwa kilo, kulikoongeza uagizaji wa gesi hiyo kwa asilimia 52.6 kama ilivyotarajiwa.

Nne:

          Msamaha wa kodi uliotolewa kwa mitambo ya kuchimbia Visima vya Maji ambao umeonyesha matokeo mazuri.  Mitambo ya aina hii iliyoagizwa imeongezeka kwa asilimia 68 kutoka shilingi milioni 12,602.1 mwaka 2002 hadi shilingi milioni 21,187.8 mwaka 2003.

 

Tano:

Nafurahi kuliarifu Bunge hili tukufu kwamba hatua zilizochukuliwa kudhibiti ukwepaji wa kodi katika biashara ya mafuta ya petroli zimezaa matunda yaliyotarajiwa.  Jumla ya shilingi milioni 226,036 zimekusanywa kwa kipindi cha Julai 2003 hadi Aprili 2004, kulinganisha na lengo la shilingi milioni 208,002.  Kiasi hiki ni asilimia 25 zaidi ya kodi za mafuta zilizokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka uliotangulia.

 

Sita:

          Nasikitika kwamba kodi ya mauzo ya nje ya asilimia 15 kwa ngozi ghafi iliyoanzishwa mwaka huu wa fedha ili kuvutia usindikaji wa bidhaa hiyo hapa nchini, haijawa na matokeo yaliyo kusudiwa, kwani mapato yaliyopatikana katika nusu mwaka ya kwanza ni shilingi milioni 413 kulinganisha na lengo la shilingi milioni 1,080 katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2003.  Eneo hili litachunguzwa zaidi mwaka huu kwa lengo la kuwezesha kusindika ngozi zote hapa nchini, kwa manufaa ya wafugaji na uchumi wa taifa kwa ujumla.

 

15.    Mheshimiwa Spika, matokeo kamili ya hatua mbali mbali zilizochukuliwa na Serikali kuongeza mapato yatafahamika baada ya mwisho wa mwezi huu, lakini mifano michache niliyoielezea ni ushahidi tosha kwamba sera nzuri, utawala bora na usimamizi imara katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali, huongeza mapato.  Serikali itaendelea kusimamia mambo haya na mengine mapya ambayo nitaelezea hivi punde.  Aidha, Sheria mpya ya Kodi ya Mapato iliyotungwa na Bunge hili tukufu mwezi Aprili mwaka huu itaanza kutumika mwezi Julai 2004 kama ilivyo pangwa.  Zoezi la kutayarisha Kanuni za Sheria hii pamoja na maelezo ya kina ya vifungu mbali mbali vya sheria hiyo linaendelea vizuri.  Sheria hiyo inatarajiwa kupanua wigo wa kodi na kuanzisha utaratibu mpya wa walipa kodi kujikadiria kodi wenyewe.  Aidha, Idara ya Walipa Kodi Wakubwa katika Mamlaka ya Mapato Tanzania imeimarishwa na malalamiko yaliyokuwepo ya walipa kodi hao yamepungua kwa kiwango kikubwa.

 

16.    Mheshimiwa Spika, kama nilivyo kwisha elezea hapo awali, mwenendo wa upatikanaji wa misaada na mikopo nafuu umekuwa wa kuridhisha kwa mwaka huu wa fedha wa 2003/04.  Katika kipindi cha Julai 2003 hadi Mei 2004 jumla ya misaada na mikopo kwa ajili ya bajeti ya kawaida ilifikia shilingi milioni 490,253 sawa na asilimia 121 ya makisio tuliyojiwekea ya shilingi milioni 405,047.  Fedha hizi pia zilitolewa mapema ikilinganishwa na miaka ya nyuma ambapo hadi kufikia Desemba 2003, asilimia 90 ya fedha hizo ilikwisha patikana na hivyo kutoa mchango mkubwa kwa Serikali katika kukabiliana na matatizo ya kibajeti yaliyotishia kujitokeza, kutokana na ukame.  Mafanikio yote haya ni matokeo ya utekelezaji wa mkakati wetu wa kupokea misaada na mikopo (Tanzania Assistance Strategy – TAS) na wa kurahisisha utawala wa misaada (aid harmonisation) ili kupunguza urasimu na umimi kama ilivyo kuwa huko nyuma.  Utaratibu huu pamoja na ule wa kujadiliana na Wafadhili katika vikao vya pamoja na pia kujadili matumizi ya bajeti hadharani kila mwaka umeimarisha sana imani ya Wafadhili kwa Tanzania kuliko nchi nyingi Afrika.

 

17.    Pamoja na uhusiano huo unaoivumisha Tanzania katika duru za Wafadhili, bado tunalo tatizo la kuimarisha zaidi uhuru wa Tanzania kuelekeza misaada hiyo kikamilifu na bado liko tatizo kubwa zaidi kuwa nchi karibu zote zingali bado kutimiza ahadi zao za kuongeza misaada chini ya makubaliano ya Monterrey, Mexico ili ifikie asilimia 0.7 au zaidi ya Pato la Taifa la nchi tajiri katika kutekeleza mkakati wa kuondoa umaskini duniani karne hii (Millenium Development Goals).  Tunazipongeza hasa Serikali za Uingereza na Ufaransa kwa kuongoza mijadala ya suala hili kwenye vikao vya kimataifa na hata kupendekeza kuanzishwe mfuko maalum wa kimataifa wa kuziwezesha nchi maskini sana duniani kupata misaada zaidi ya kupambana na umaskini, jambo ambalo baadhi ya wakubwa wenzao wanalichenga au wanalikwepa kwa kuanzisha mifuko yao ya aina isiyo lenga kikamilifu kukabiliana na umaskini kwa misingi iliyo kubalika tayari duniani.

 

18.    Mheshimiwa Spika, Serikali itaendeleza majadiliano na Wafadhili mwaka ujao wa fedha kuhakikisha kuwa misaada na mikopo nafuu inaelekezwa katika maeneo yanayolenga kutekeleza dira na matakwa ya nchi (complete ownership of aid utilization) ili kukuza uchumi, hususan kwenye kilimo, elimu, viwanda, na miundo mbinu, hasa madaraja na barabara za lami za kuunganisha wilaya, mikoa, mikoa na mikoa, maeneo ya uzalishaji mkubwa na baina yetu na nchi majirani.  Maeneo haya ndiyo yatatuondoa kwenye ujinga na umaskini kwa haraka zaidi kuliko mengineyo ambayo ni ya ulaji (consumption) kuliko uzalishaji (production). Kupanga ni kuchagua pale panapo weza kulivusha taifa letu haraka haraka.  Tutaweza kulima kwa wingi, kusindika mazao hayo kwa wingi na kusafirisha mazao ya kilimo na viwanda hadi nchi jirani, za kanda na ng’ambo kwa barabara za kuaminika hadi bandarini au nchi majirani, hasa kaskazini, magharibi na kusini mwa Tanzania.  Na hatuwezi kufanya hayo na mengineyo bila kuwa na wasomi wa nyanja zinazo endana na ulimwengu huu wa elimu ya juu, sayansi, na utandawazi.

 

19.    Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Serikali napenda kuchukua nafasi hii kushukuru nchi Wafadhili, Jumuiya ya Ulaya, pamoja na Mashirika yote ya Kimataifa yaliyotoa fedha kusaidia bajeti yetu kwa mwaka huu wa fedha.  Nchi na mashirika hayo ni Australia, Austria, Canada, China, Denmark, Finland, Hispania, Ireland, Italia, Japan, Marekani, Norway, Sweden, Ubeligiji, Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani na Uswisi Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), BADEA, Benki ya Dunia, EIB,  Jumuiya ya Ulaya, Kuwait Fund, NDF, OPEC Fund na Taasisi za Umoja wa Mataifa.

 

20.    Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kudhibiti ukuaji holela wa madeni chini ya Mkakati wa Madeni wa Taifa. Sheria ya Madeni, Dhamana na Misaada ya Mwaka 1974 pamoja na marekebisho ya mwaka 2003 inaendelea kutekelezwa kikamilifu. Kwa sasa, mikopo inatafutwa kutoka vianzio vyenye masharti nafuu sana na kuelekezwa kwenye maeneo muhimu ya kukuza uchumi na kuondoa umaskini.  Aidha, udhamini wa Serikali kwa mikopo ya nje umesitishwa na hakuna ruksa kwa mtumishi au mamlaka yoyote kukopa kwa niaba ya Serikali au kufikia mapatano yanayo husu fedha bila idhini rasmi ya Waziri wa Fedha ambaye naye lazima ashauriwe kwanza na Kamati iliyoundwa chini ya sheria hiyo.

 

21.    Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na juhudi za kupata misamaha ya madeni toka nchi wanachama na zile zisizokuwa wanachama wa Kundi la Paris kwa mujibu wa makubaliano yaliyofikiwa katika mpango wa kuzipunguzia madeni nchi masikini. Nchi za Kundi la Paris, isipokuwa Brazil, zimefuta sehemu kubwa ya madeni yetu kwao, na nyingine zimeyafuta kabisa madeni hayo.  Juhudi za kufanya majadiliano na Brazil zitaendelea mwaka ujao wa fedha.  Aidha, katika mwaka huu wa fedha, tumepata msamaha wa deni kiasi cha dola za Marekani milioni 15.1 toka Bulgaria na mazungumzo ya awali yamekamilika kwa Iran na karibu kukamilika kwa Mfuko wa Abu Dhabi na mashirika ya kibiashara ya India ambayo tayari imetufutia madeni ya kiserikali.  Juhudi zitaendelea kuwa na mazungumzo na nchi nyingine zinazotudai ili zitufutie madeni kwa mujibu wa makubaliano ya kimataifa kwa nchi maskini sana duniani.  Majadiliano na nchi na mashirika yasiyo ya Kundi la Paris yamekuwa magumu kwa wao kutokubali kutii makubaliano ya Paris, suala linalo zua mijadala katika mikutano ya kimataifa ambapo baadhi ya nchi zimeshitakiwa na mali zao kufilisiwa.

 

22.    Mheshimiwa Spika, mwenendo wa utekelezaji wa Bajeti ya mwaka huu wa fedha unaonyesha kwamba kwa kiasi fulani kumekuwa na ongezako la ufanisi na udhibiti wa matumizi, hasa katika Serikali Kuu, kama ilivyo kwenye ukusanyaji wa mapato.  Hii inamaanisha kwamba Serikali inaanza kuona matunda (ingawa ya awali) ya hatua ilizochukua kwa kipindi cha miaka nane iliyopita za kupanga na kusimamia bajeti, kuondoa matumizi yasiyo ya lazima, na kujifunza kutumia kile tulicho nacho.  Ni ishara nzuri pia kwamba sasa taratibu na kanuni za ununuzi kwa mujibu wa Sheria ya Ununuzi wa Umma (Na. 3 ya 2001) zinaeleweka.  Aidha, licha ya matumizi makubwa yaliyosababishwa na ukame katika maeneo ya chakula na umeme, matumizi ya Serikali kwa ujumla yamedhibitiwa na hakuna athari kwenye bajeti ya mwaka huu.  Serikali imehakikisha kwamba sekta za kuondoa umaskini yaani afya, elimu, maji, barabara, kilimo, mahakama na sheria zimepata fedha kulingana na bajeti zao, hata pamoja na kwamba kumekuwa na matumizi makubwa kwa ajili ya TANESCO na chakula.  Kigezo kikubwa cha uimara wa utekelezaji wa bajeti ya mwaka huu ni kwamba, Serikali haikukopa kutoka Benki Kuu nje ya lengo.  Badala yake, hata kiwango cha kukopa Benki Kuu kilichowekwa katika makubaliano na IMF chini ya mpango wa PRGF, hakikuvukwa.  Hili limewezekana kutokana na ukusanyaji mzuri wa mapato ya ndani, misaada ya bajeti kutoka kwa Nchi Wafadhili ambayo pia imepita lengo kidogo, udhibiti wa matumizi ya Serikali, na kasi ndogo ya utekelezaji wa miradi.

 

23.    Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha Julai 2003 hadi Machi 2004, matumizi kwa ujumla yalifikia shilingi trilioni moja, bilioni mia saba ishirini na mbili na mia sita kumi na mbili milioni (1,722,612 milioni) ikilinganishwa na makisio ya shilingi trilioni moja, bilioni mia nane themanini na tisa na milioni mia mbili na saba (1,889,207 milioni) katika kipindi hicho.  Kati ya fedha hizo, shilingi milioni 422,559 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo na shilingi trilioni moja, bilioni mia tatu na milioni hamsini na tatu (1,300,053 milioni) ni kwa matumizi ya kawaida. 

 

24.    Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba kutokana na hali ya ukame ulioikumba nchi yetu mwaka 2003, Serikali ililazimika kuandaa Bajeti ya Ziada na kupata kibali cha Bunge cha kutumia fedha kiasi cha shilingi milioni 176,784 zaidi ya zilizoidhinishwa awali katika bajeti ya 2003/04. Mahitaji ya nyongeza ya shilingi milioni 176,784 yalikuwa ni pamoja na ununuzi na usambazaji wa chakula cha njaa, msaada kwa TANESCO kuiwezesha kumudu gharama za uzalishaji wa umeme kwa kutumia mafuta badala ya nguvu za maji, fidia kwa Halmashauri za Wilaya na Miji kufuatia kufutwa kwa kodi zenye kero, mchango katika Mfuko wa Pensheni ya Watumishi wa Serikali pamoja na malipo kwa  Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PPF), kufidia michango ambayo haikuwa imewasilishwa na mashirika hayo kabla ya kubinafsishwa.  Mahitaji mengine ya ziada yalihusu maandalizi ya Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, ukaguzi wa dhahabu, na ununuzi wa ndege mpya ya Serikali.  Mahitaji haya yaligharamiwa kwa njia mbili; kwanza shilingi 87,250 milioni zilitokana na mapato mapya, na pili, shilingi 89,534 milioni zilitokana na uhamisho wa fedha ambazo zilikuwa ndani ya bajeti iliyoidhinishwa.  Matumizi hayo ya nyongeza yalifanyika na yanaendelea kufanyika kama yalivyopangwa. 

 

25.    Mheshimiwa Spika, kulingana na mwenendo wa mapato na matumizi hadi sasa inatarajiwa kwamba kwa mwaka wote wa fedha mapato yatavuka lengo kwa shilingi bilioni 74 na milioni 210 (74,210 milioni) sawa na asilimia 5.3 zaidi ya lengo.  Inategemewa pia kwamba misaada na mikopo ya masharti nafuu kwa ajili ya bajeti nayo itazidi lengo.  Mapato kutokana na ubinafsishaji ambayo yalikadiriwa kufikia shilingi bilioni 17 (17,000 milioni), yaelekea hayatapatikana yote. 

 

Kuhusu malengo ya matumizi, mwelekeo ni kwamba, maeneo mengi ya matumizi ya maendeleo na ya kawaida hususan Matumizi Mengine (OC) hayatafikia malengo kwa sababu zilizoelezwa awali.  Aidha, kuna mwelekeo wa malengo kufikiwa katika sekta za kipaumbele za kupunguza umaskini na kukuza uchumi.

 

26.    Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuboresha usimamizi wa fedha za umma, Serikali imechukua hatua mbalimbali ambazo ni pamoja na kuanzisha kamati za ukaguzi wa ndani wa hesabu za Serikali katika Wizara, Idara na Wakala zote za Serikali.  Mafunzo hivi sasa yanaendelea ya kuelimisha Wakaguzi hao kuhusu kazi za kamati hizo.  Kanuni na taratibu za ukaguzi wa ndani wa hesabu zimekamilishwa na zitachapishwa hivi punde na kutangazwa kwa wadau wote.  Aidha, Ofisi ya Ukaguzi ya Taifa (NAO) inaimarishwa kwa kupatiwa makao mapya ya ofisi, na sasa inakamilisha mpango wa kurekebisha muundo wake wa ndani na kujaza nafasi za kazi zilizo wazi ili kuongeza tija katika utendaji wake.  Vile vile, maandalizi yamekamilika ya kuifanyia marekebisho Sheria ya Ununuzi wa Umma Na. 3 ya 2001 ili kuongeza ufanisi na tija katika utekelezaji wa bajeti ya Serikali, hasa kuhusu miradi ya maendeleo.  Marekebisho hayo yatawasilishwa katika Kikao hiki cha Bunge kwa kusomwa kwa mara ya kwanza.

 

27.    Mheshimiwa Spika, katika sekta ya huduma za kibenki, kuna maendeleo ya kuridhisha pia.  Ujazi wa fedha ulidhibitiwa na kuongezeka kwa asilimia 18.7 kati ya Julai 2003 na Machi 2004 kulinganisha na asilimia 22.7 mwaka uliotangulia.  Mwenendo huu wa ujazi wa fedha unathibitisha kwamba tumeweza kweli kuweka msingi thabiti wa kuzuia mfumuko wa bei.  Mikopo ya benki za biashara kwa sekta binafsi iliongezeka kwa kiwango kikubwa cha asilimia 41.8 kati ya Julai 2003 na Machi 2004.  Ongezeko hili limetokana hasa na kampuni kubwa hapa nchini kuacha kukopa kutoka benki za nje ya Tanzania, badala yake sasa zinakopa kutoka benki za hapa nchini.  Hali hii inatokana na sababu kadhaa, kubwa zikiwa, kwanza kuepuka hasara inayotokana na kubadilika kwa bei ya fedha za kigeni (exchange rate); na pili kushuka kwa gharama za kukopa hapa Tanzania hasa kutokana na ongezeko la ushindani katika sekta ya kibenki.  Kwa hiyo riba ya mikopo sasa imeshuka na kufikia wastani wa asilimia 13.5.  Riba ya amana kwa upande mwingine imepanda na kufikia wastani wa asilimia 4.1.  Sasa tofauti kati ya riba ya mikopo na riba ya amana imeshuka kutoka kiwango cha 10.6 mwezi Juni 2003 hadi 9.4 mwezi Machi 2004.  Ingawa riba ya amana bado ni ndogo na ile ya mikopo bado ni kubwa, mwenendo huu unatia moyo, na ni dalili nzuri kwamba benki sasa zimepata uelewa mkubwa wa soko la Tanzania, hasa mahitaji ya huduma za benki, na kwamba riba zitaendelea kubadilika kulingana na mahitaji ya soko.  Serikali inaamini kwamba hili litatokea kwa kuzingatia mabadiliko ambayo Serikali imefanya ili kuboresha mazingira yanayotoa motisha kwa benki kama vile kurekebisha Sheria ya Ardhi, kuimarisha Kitengo cha Mahakama Kuu kinacho shughulikia Mashauri ya Biashara, kuanzisha mifuko ya kudhamini mikopo (credit guarantee schemes), na maendeleo yanayotokea katika miundo mbinu.

 

28.    Mheshimiwa Spika, kwa upande wa urari wa malipo ya nje (balance of payments), kumekua na ongezeko la uagizaji wa bidhaa kutoka nje, na pia ongezeko la mauzo ya nje, hasa ya bidhaa zisizo asilia.  Uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi umeongezeka kwa asilimia 26.6 katika mwaka wa 2003, kutokana na mafuta ya petroli na chakula na hasa mchele.  Uagizaji wa mafuta ya petroli umeongezeka kutokana na mahitaji makubwa ya TANESCO kwa ajili ya kuzalisha umeme kwa kutumia mitambo ya mafuta badala ya maji.  Usafirishaji nje wa bidhaa uliongezeka kwa asilimia 16 ukitokana hasa na dhahabu, na bidhaa za viwandani.  Usafirishaji wa mazao asilia uliendelea kuzorota ingawa kuna dalili za kupanda tena kwa bei za kahawa, pamba, chai, na korosho katika soko la dunia.  Mapato yatokanayo na utalii yaliongezeka katika mwaka huu.  Kwa ujumla, kwa mara ya kwanza, urari wa malipo ya nje ulikuwa na ziada (surplus) ya dola za Marekani 243.9 milioni.  Kwa kuzingatia misamaha ya Madeni na ongezeko la misaada na mikopo ya bajeti, akiba ya fedha za kigeni ilikuwa dola za Marekani 1,973.2 milioni (dola bilioni moja, milioni mia tisa sabini na tatu, laki mbili) sawa na shilingi trilioni 2.2.

 

Mambo Mengine Muhimu Yaliyojitokeza Katika Utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka 2003/04:

 

29.    Mheshimiwa Spika,  ingawa tunapata mafanikio makubwa kutokana na marekebisho ya sera na utawala, bado tuna kazi kubwa ya kufanya kuweza kujitegemea, na la muhimu zaidi kuondoa umaskini.  Baadhi ya mambo mengine muhimu yaliyo jitokeza katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka huu wa fedha unaoisha ni:-

 

La kwanza:

Bajeti ya Serikali bado ni tegemezi kwa kiasi kikubwa, ingawa kiwango cha utegemezi kinapungua.  Katika mwaka 2003/04, Wafadhili pamoja na Mashirika ya Fedha ya Kimataifa wamechangia asilimia 45 ya Bajeti ya Serikali ikilinganishwa na asilimia 47 mwaka 2002/03.  Hivyo, ingawa mapato ya  ndani yanaongezeka, pengo la kujitegemea bado ni kubwa.

 

La pili:

Pamoja na kupewa upendeleo maalum, fedha zinazotengwa kwa sekta za kuondoa umaskini bado hazitoshelezi mahitaji; na

 

La tatu:

Ingawa ufanisi na nidhamu Serikalini vimeongezeka kiasi, uwezo wa utendaji hasa katika maeneo ya uhasibu, mawasiliano, utibabu n.k. bado ni duni, na ndio sababu miradi ya maendeleo haitekelezwi kwa wakati na hata hesabu za Serikali haziko sahihi wakati wote.

 

MISINGI, SERA, NA MALENGO YA BAJETI YA MWAKA 2004/05

 

30.    Mheshimiwa Spika, mfumo wa bajeti ya mwaka 2004/05 unazingatia malengo muhimu ya uchumi ambayo ni pamoja na:-

 

(i)                 Uchumi kukua kwa asilimia 6.3 mwaka 2004 na asilimia 6.5 mwaka 2005.  Kukua huku kutatokana na kilimo, uzalishaji viwandani na uzalishaji kwa mauzo ya nje.

 

(ii)              Mapato ya ndani yanalengwa kufikia shilingi trilioni moja, bilioni mia saba thelathini na tisa, na milioni mia mbili themanini na nane (1,739,288 milioni) sawa na asilimia 13.8 ya Pato la Taifa.

 

(iii)            Mfumuko wa bei utakuwa katika kiwango cha asilimia 4 ifikapo Juni 2005 na baadaye kulingana na viwango vya wastani katika nchi tunazofanya nazo biashara na zile tunazoshindana nazo katika biashara ya nje.

 

(iv)            Akiba ya fedha za kigeni inalengwa iwe katika kiwango ambacho kinatosha kulipia mahitaji muhimu ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa muda usiopungua miezi sita.

 

(v)               Kupunguza kiwango cha utegemezi wa bajeti ya Serikali hadi asilimia 41 mwaka 2004/05.

 

(vi)            Kusimamia utekelezaji wa sera ya mikopo midogo midogo (micro-finance) na mpango wa dhamana kwa wawekezaji wadogo wadogo (SMEs) na miradi mikubwa ili kuwezesha wananchi walio wengi kujiendeleza kiuchumi kwa kujipatia mikopo zaidi ya kibenki.

 

31.    Mheshimiwa Spika, muhula wa kwanza wa Mkakati wa Kupunguza Umaskini umemalizika, na taarifa ya tatu ya utekelezaji wa Mkakati huo imechapishwa.  Taarifa hiyo imeainisha matokeo ya tafiti mbalimbali zilizofanywa kuhusu hali ya umaskini nchini.  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais anayesimamia Mkakati wa kuondoa umaskini ataelezea kwa kina maudhui ya taarifa hiyo.  Taarifa hiyo imebainisha, pamoja na mambo mengine, kwamba maendeleo ya kilimo ambayo ni sekta muhimu kuliko zote Tanzania yanakwamishwa na mambo mengi.  Vikwazo hivyo ni pamoja na ukosefu wa mikopo ya pembejeo na mitaji, ukosefu wa huduma za ugani, mazingira mabaya ya uwekezaji, ubovu wa miundombinu, na mengine mengi.  Wakati huo huo, sekta ya kilimo bado inabakia kuwa sekta kuu katika uchumi wa Tanzania.  Udogo wa mashamba, teknolojia duni na utegemezi kwa mvua ni baadhi ya orodha ya matatizo yanayokwamisha maendeleo ya kilimo na pia maendeleo ya wananchi wanao kitegemea.  Serikali imekua ikichukua hatua mbali mbali kila mwaka katika jitihada za kuondoa matatizo haya lakini hayaja tokomezwa bado. 

 

32.    Mheshimiwa Spika, ili kuinua kilimo, Serikali imechukua hatua za ziada zenye lengo la kuvutia uwekezaji katika sekta hii, na papo hapo kuwezesha wakulima wadogo kuongeza tija ya jasho lao, na kujiondolea umaskini.  Hatua hizo ni pamoja na hizi zifuatazo:-

 

Moja:  Chini ya Sheria ya Kodi ya Mapato ya 2004

(a)              Kuna punguzo la mara moja (100% expensing) la gharama za kusafisha pori, ujenzi wa mifereji ya umwagiliaji, kupanda mazao ya kudumu na kutunza mazingira au kudhibiti mmomonyoko katika ardhi inayotumika kwa kilimo.  Kwa taratibu za kawaida za kiuhasibu, gharama hizi ni za rasilimali (capital expenditures) na zingepunguzwa kwa kipindi kirefu sana.

 

(b)              Gharama ambazo mtu ametumia kuhifadhi mazingira kwenye ardhi inayotumiwa kwa kilimo, ufugaji wa wanyama au samaki, au kuirejeshea ardhi hiyo hali yake baada ya kuharibiwa, zinapunguzwa katika kukadiria mapato ya mhusika kwa minajili ya kodi ya mapato.

 

(c)               Gharama za utafiti na uendelezaji wa mashamba ya kilimo na mifugo zinapatiwa punguzo hilo kwa ajili ya kodi ya mapato.

 

(d)              Vifaa vya umwagiliaji maji mashambani vimeingizwa katika kundi moja na magari makubwa ili kupata punguzo la uchakavu kwa kiwango cha juu zaidi cha asilimia 25 kwa mwaka.

 

(e)              Matrekta na mitambo mingine inayotumiwa katika kilimo, ufugaji na uvuvi imeingizwa katika kundi la mitambo ya viwandani na kupatiwa punguzo la uchakavu la asilimia 50 katika mwaka wa kwanza na asilimia 25 miaka inayofuata.

 

(f)                 Wafanyabiashara wa mazao ya kilimo hawatakiwi kulipa kodi ya awali kwa awamu sawa (equal quarterly instalments), bali mwisho wa robo ya tatu ya mwaka baada ya kuvuna.

 

 

 

Mbili:    Chini ya Sheria ya Ushuru wa Forodha:

Zana na pembejeo za kilimo kama vile matrekta, madawa ya kuua wadudu na mbolea hivi sasa hazitozwi Ushuru wa Forodha.  Ikiwa kuna kodi zilizosalia bado katika maeneo haya zitafutwa.

 

Tatu:    Chini ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani  (VAT)

(a)        Mazao ghafi ya kilimo na mifugo yanapata msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), ikiwa ni pamoja na nyama isiyosindikwa, mazao ya mifugo ambayo hayajasindikwa, samaki zisizosi-ndikwa, na mazao mengine yote ya kilimo ambayo hayajasindikwa.

 

(b)        Hakuna Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye pembejeo za kilimo na uvuvi kama vile madawa ya kuua wadudu, mbolea, madawa na vifaa vya mifugo, vifaa vya kilimo kama matrekta, majembe, sururu, nyavu, mashine na vifaa vya uvuvi.

 

(c)         Kuna unafuu wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) pia kwa mazao ya kilimo yanayouzwa nje na wakulima waliojiunga kwenye Vyama Vya Ushirika au Umoja wa wazalishaji (Associations) na kujisajili chini ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani.

 

Nne:     Chini ya Sheria ya Ushuru wa Stempu

 

Mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi yamesamehewa ushuru wa stempu.  Aidha, ushuru wa stempu haukusanywi katika magulio, ambapo mazao haya huuzwa kwa wingi.

 

Tano:      Chini ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa

 

(a)        Bado sheria inakataza Serikali za Mitaa kutoza kodi inayozidi asilimia tano (5%) ya bei ya shambani au chama cha msingi au cha wakulima kwenye mazao  ya kilimo. Aidha, kodi hiyo inatakiwa kutozwa pale ambapo mazao husika yamelimwa au yanaponunuliwa kwa mara ya kwanza kutoka kwa wakulima na siyo katika Wilaya yanakopitia yakielekea sokoni au Wilaya nyingine au nchi jirani.

 

(b)        Kodi  na ada zinazoruhusiwa kutozwa ni zile tu zilizo orodheshwa katika Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa na Sheria ya Fedha ya Taifa ya mwaka 2003.

 

Sita:   Katika Bajeti ya Matumizi ya Serikali

(a)        Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya mipango ya maendeleo ya kilimo katika ngazi ya Wilaya.

 

(b)        Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufidia gharama za usafirishaji wa mbolea kwa ajili ya Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na mikoa mingine yenye mvua za uhakika itakayo tangazwa na Waziri wa Kilimo na Chakula.

 

(c)         Mfuko wa Dhamana ya Mikopo kwa vyama vya ushirika na vyombo vingine vinavyonunua mazao ya wakulima utaimarishwa kwa kuongezewa fedha katika bajeti hii.  Mfuko huu umekuwa na mafanikio makubwa.

 

33.       Mheshimiwa Spika, Hatua hizi za kufuta kodi au kutoa unafuu mkubwa wa kodi na fidia ya mbolea iliyotangazwa mwaka tunao malizia kwa wakulima, wafugaji na wavuvi, hasa wadogo na wa kati ambao wengi ni wananchi, zikiunganishwa na mpango wa Serikali wa kudhamini wakulima wadogo wadogo ili waweze kukopa kutoka mabenki kibiashara na mipango inayoendelea ya kuchimba na kuimarisha barabara vijijini hadi taifani, na pia hatua za kuondoa kero za kodi za leseni, ni ushahidi imara wa utekelezaji wa sera na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.  Ni hatua madhubuti za kuwawezesha Watanzania vijijini kuzalisha mali na kujitajirisha kwa kujituma na kuwa wabunifu; ni msumari muhimu kwenye jeneza la kuuzika umaskini kisayansi.  Atakayesema kwamba bajeti hii haimsaidii maskini au mkulima, mfugaji na mvuvi atakuwa anapotosha tu ukweli.  Aliye na macho haonyeshwi njia!

 

34. Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2004/05, hatua za kuimarisha na kuboresha vyanzo vya akiba za pamoja za wananchi zitachukuliwa, ambapo “Unit Trust of Tanzania”  (UTT) itauza hisa (Units) kwa wananchi.  Uanzishwaji wa ‘Collective Investment Schemes’ ambapo wananchi watashirikiana kuweka akiba kwa pamoja na hivyo kushiriki katika masoko ya mitaji nchini litakuwa jambo geni sana. 

 

UTT itashirikiana pia na benki za biashara katika kuanzisha chombo cha kuweka kumbukumbu za wakopaji (credit reference bureau) ili kuboresha mazingira ya benki kukopesha.  Aidha, hatua zinazochukuliwa kuimarisha mifuko ya dhamana ya mikopo na mitaji zinalenga pia kuwawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika uendeshaji wa uchumi wa Taifa.

 

MWELEKEO WA BAJETI YA MWAKA 2004/05

 

Mapato

35.    Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2004/05, Serikali inalenga kukusanya mapato ya ndani yasiyopungua shilingi trilioni moja, bilioni mia saba thelathini na tisa na milioni mia mbili themanini na nane (milioni 1,739,288) sawa na asilimia 13.8 ya Pato la Taifa.  Kiwango hiki ni ongezeko la asilimia 20 ikilinganishwa na mapato yanayotarajiwa kukusanywa mwaka huu wa 2003/04.  Azma ya Serikali kwa mwaka 2004/05 na muda wa kati ujao itaendelea kuwa ya kuongeza mapato, kupunguza utegemezi, kugharamia mpango wa kuondoa umaskini, na kuhakikisha kwamba hatubebi tena mzigo tusiouweza wa madeni.  Hatua kuu zitakazochukuliwa katika kuongeza mapato ni pamoja na:-

 

Moja:     Kuimarisha usimamizi na utawala wa Mamlaka ya Mapato, hasa kwa kupanua Idara ya Walipa Kodi Wakubwa.

 

Mbili:    Kutekeleza Sheria Mpya ya Kodi ya Mapato, 2004 na kukamilisha mapitio ya sheria nyingine za kodi kwa lengo la kuziboresha.

 

Tatu:     Kuanza utekelezaji wa Mkataba wa Kuanzishwa Umoja wa Forodha wa Afrika Mashariki.

 

Nne:      Kuingiza mapato yatakayotokana na mauzo ya gesi ya Songo Songo katika maduhuli ya Serikali.  Mategemeo ni kwamba gesi hii itaanza kupatikana kunako mwezi Julai 2004.

 

Tano:     Kufanya marekebisho ya mfumo wa kodi katika baadhi ya maeneo ili kuuboresha zaidi pamoja na kuweka vivutio kwa baadhi ya sekta ili kukuza Pato la Taifa.

 

Sita:      Kuimarisha makusanyo ya mapato kutoka Wizara na Idara, hasa zile zilizo kwenye utaratibu wa “retention”.

 

Saba:     Kusimamia kikamilifu biashara ya bidhaa ya mafuta ya petroli ikiwemo kufungwa kwa “Flow Meter” bandarini ili kudhibiti ukwepaji kodi.  “Flow Meter” inategemewa kufungwa mwezi Julai 2004.

 

Nane:    Kuendeleza utaratibu wa utawala wa misamaha ya kodi kwa njia ya “Treasury Voucher” na kuangalia uwezekano wa kuingiza katika utaratibu huu vifaa vinavyoingizwa nchini kwa miradi inayogharamiwa na Wafadhili.

 

Tisa:      Kuimarisha utendaji wa TRA kwa kuongeza matumizi ya teknolojia, tija ya watumishi, mafunzo, na huduma bora kwa walipa kodi.

 

Kumi:    Kuanzia Julai 2004 ukaguzi wa mizigo utafanywa baada ya kuwasili nchini (destination inspection) badala ya utaratibu wa sasa wa kabla ya kuwasili (preshipment inspection).  Utaratibu huu utaboresha mazingira ya biashara, utaondoa kero kwa waagizaji wa bidhaa, na utaboresha mazingira ya uwekezaji.

 

Kumi na moja: Kuongeza saa za kazi za shughuli za forodha ili kuondoa msongamano wa mizigo bandarini.  Vyombo vyote vinavyotoa huduma katika maeneo ya Forodha vitatakiwa kushirikiana kwa karibu zaidi na Idara ya Forodha ili kufanikisha azma hii.

 

Kumi na mbili: Zoezi limeanza la kuainisha maeneo ya Sheria ya Uwekezaji ya mwaka 1997 ambayo yanahitaji kurekebishwa ili kuondoa mianya ya ufujaji wa mapato ya Serikali.

 

Kumi na tatu: Imeundwa Kamati ya kutathmini sheria na kanuni zinazotawala uwekezaji katika sekta ya madini kwa lengo la kutoa mapendekezo ya kuziboresha ili Serikali isipoteze yale mapato ambayo ni halali yake.

 

36.    Mheshimiwa Spika, inaeleweka wazi kuwa misaada kutoka nje sio njia nzuri ya kuendeleza uchumi imara na wa kudumu (sustainable).  Hata hivyo katika kipindi hiki ambacho tunafufua uchumi wetu na Kuondoa Umaskini, michango ya Wafadhili ni muhimu katika kusaidia Serikali yetu.  Sera safi tulizo nazo pamoja na usimamizi imara wa uchumi vimewezesha Wafadhili na Mashirika ya Fedha ya Kimataifa kupenda kuendelea kutoa misaada yao kuchangia bajeti ya taifa.  Kama nilivyosema awali, ni muhimu kutumia nafasi hii vizuri na kuhakikisha kuwa michango hii inatumika vizuri kutuwezesha kuondoa umaskini na kuleta maendeleo kama ilivyokuwa kwa nchi nyingi za Bara la Asia.  Mkakati wetu wa Kusimamia Misaada (TAS) utazidi kutuongoza ili kuhakikisha misaada na mikopo ya masharti nafuu inatumika vizuri kukuza uchumi wa taifa.

37.    Mheshimiwa Spika, kutokana na majadiliano tuliyofanya na nchi Wafadhili na Mashirika ya Fedha ya Kimataifa, katika mwaka wa fedha 2004/05 tunatarajia kupata misaada na mikopo ya masharti nafuu kiasi cha shilingi trilioni moja, bilioni mia tatu sitini na saba na milioni ishirini na tano (shilingi 1,367,025 milioni) ambacho kitakuwa asilimia 41 ya matumizi yote ya Serikali.  Kati ya fedha hizo, shilingi 509,140 milioni ni misaada ya bajeti, na shilingi 857,885 milioni ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.  Kiwango hiki cha misaada na mikopo kinaonyesha ongezeko la shilingi 191,204 milioni au asilimia 16 ikilinganishwa na matarajio ya misaada na mikopo kwa mwaka huu wa fedha wa 2003/04.  Ni mategemeo yetu kwamba Nchi Wafadhili zitaendelea kuongeza misaada yao kwa Tanzania na kutekeleza kikamilifu ahadi za Monterrey (Monterrey Consensus), ya kuhakikisha kuwa tunawezeshwa kufikia malengo ya Maendeleo ya Milenia Mpya ( “Millenium Development Goals” - MDG).

 

38.    Mheshimiwa Spika, Serikali imepanga kutumia akiba yake Benki Kuu pamoja na kukopa katika vyanzo vya ndani kiasi cha shilingi 231,110 milioni kwa kutumia dhamana za muda mfupi na mrefu.  Sehemu kubwa ya mikopo hiyo itatumika kulipia madeni yaliyoiva (rollover) na madeni mengine yanayotokana na mikataba.  Kiasi kingine kitatumika kuchangia mfuko wa dhamana ya mikopo kwa bidhaa za kuuza nje.

 

Matumizi

39.    Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/05, Serikali imedhamiria kuendelea kusimamia vyema nidhamu katika matumizi ya fedha za umma. Aidha, Serikali itaendelea kuimarisha mtandao wa kompyuta wa kutayarisha na kutekeleza bajeti ya Serikali. Hatua hii ni pamoja na kupanua teknolojia hii ili ifike kwenye Serikali za Mitaa.

 

40.    Mheshimiwa Spika, mgao wa fedha kwa mwaka 2004/05 umezingatia mambo yafuatayo:-

 

Kwanza: Sekta za kipaumbele katika Mkakati wa Kupunguza Umasikini zimeendelea kupewa upendeleo.  Hata hivyo kwa kuzingatia mahitaji mapya ya fedha kugharamia matayarisho ya Uchaguzi Mkuu, na pia mahitaji ya sekta ya nishati, hasa kuhusu umeme, nyongeza katika sekta hizo za kuondoa umaskini haitakuwa kubwa, isipokuwa kwa zile ambazo zinapata misaada mikubwa ya Wafadhili.

 

Pili:     Utaratibu wa kutoa ruzuku kupunguza gharama za usafirishaji wa mbolea kwenda Mikoa iliyoteuliwa utaendelezwa mwaka wa 2004/05.

 

Tatu:  Utaratibu wa kutoa fedha kulingana na mapato yaliyopo (cash budget) utaendelea.

 

Nne:    Fedha zaidi zimetengwa kwa ajili ya Mfuko wa Dhamana ya Mikopo kwa Wauzaji wa bidhaa nchi za nje (ECGS) na Mfuko wa Dhamana kwa Biashara ndogo na za kati (SME Credit Guarantee Scheme).

 

Tano: Mipango ya kuendeleza kilimo katika ngazi ya Wilaya kwa utaratibu wa angalao Zao moja la Chakula na zao moja la biashara utaendelezwa.

 

Sita:    Mheshimiwa spika, katika miaka ya hivi karibuni tumeshuhudia juhudi za Serikali za kutumia mapato yake ya ndani katika ujenzi wa barabara muhimu. Mwaka 2004/05, Serikali itaendelea na utaratibu huo ambapo fedha zaidi ya zile zilizotolewa mwaka huu zimetengwa, kama atakavyoeleza zaidi Waziri wa Ujenzi atakapo-wasilisha bajeti ya Wizara yake.

 

Saba:   Serikali itaendelea kutekeleza mpango wa kuboresha mishahara ya watumishi wake, ili kufikia asilimia 4.8 ya Pato la Taifa kama ilivyodhamiriwa katika mpango huo.  Aidha, Serikali inaandaa utaratibu maalum wa kushughulikia kwa haraka malimbikizo ya mishahara ya watumishi wa Serikali wakiwemo walimu. Malipo ya malimbikizo hayo yalisitishwa kutokana na matukio ya wizi wa kalamu wa mishahara ulio fanywa na watumishi wachache wasioaminika ambao sasa umefanyiwa uchunguzi na hatua za kisheria zinachukuliwa kwa wanaohusika.

 

Nane:  Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza miradi mikubwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Umuhimu wa kwanza unawekwa kwa miradi ambayo tayari ina mikataba.

 

Tisa:   Bajeti imeendelea kutenga asilimia 4.5 ya mapato yatokanayo na misaada (grants) isiyo ya miradi kwa ajili ya bajeti ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ).  Utaratibu huu utaendelea hadi hapo mapendekezo ya Tume ya Pamoja ya Fedha (Joint Finance Commission) yatakapopa-tikana.

 

Kumi: Katika mwaka wa fedha 2004/05, Serikali itawarejesha katika daftari la Pensheni wastaafu waliokuwa wamepokea mafao yao kwa mkupuo. Wastaafu hawa wanategemewa kuanza kupokea malipo yao mwezi Januari, 2005, ili kujipa muda wa matayarisho baada ya sheria husika kurekebishwa.

 

Kumi na moja:        Kutokana na ongezeko la matukio ya ujambazi nchini, maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka ujao, na vitendo vingine vya uhalifu, bajeti ya mwaka 2004/05 imeongeza mgao wa fedha kwa vyombo vya ulinzi na usalama.

 

Kumi na mbili:       Katika mwaka 2004/05, Serikali imetenga fedha zaidi kwa ajili ya chakula cha dharura endapo hali ya hewa itakuwa mbaya pamoja na kugharamia Mfuko wa Hifadhi ya Chakula (SGR).

 

Kumi na tatu:         Kama ilivyokuwa katika mwaka 2003/04, bajeti ya 2004/05 imetenga fedha kwa ajili ya kulipia mahitaji ya sekta ya Nishati na hasa TANESCO kuisaidia katika mpango wake wa dharura, pamoja na malipo ya “capacity charge” kwa IPTL na Songas.

 

Kumi na nne:          Kwa kuzingatia ukweli kuwa idadi ya Wabunge inategemea kuongezeka baada ya uchaguzi mkuu wa mwakani, Mifuko ya Hifadhi za Jamii imekubali kwa ridhaa yao wenyewe, kujenga Ukumbi mpya kwa utaratibu wa kujenga, kukodisha na hatimaye kuikabidhi Serikali.  Kwa sababu hii, mradi huu hauko kwenye bajeti ya Serikali ya mwaka huu.     Serikali pia inafikiria kutumia utaratibu kama huu kwa miradi mingine mikubwa ya ujenzi ikiwemo miradi ya barabara.

 

Kumi na tano:        Kwa kuzingatia umuhimu wa michezo, bajeti ya mwaka 2004/05 imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa michezo wa kisasa.  Sehemu kubwa ya fedha hiyo ni msaada wa Serikali ya China.

 

Kumi na sita:          Mgao wa Ruzuku kwa Halmashauri za Wilaya kwa mwaka 2004/05 umezingatia utaratibu mpya ambao umebuniwa kufuatia zoezi la kina lililoshirikisha wadau wa aina zote.  Utaratibu mpya umetumika katika kutenga fedha za bajeti ya kawaida kwa sekta za afya na elimu kwa Halmashauri, na umetumika kwa sekta zote katika fedha za bajeti ya maendeleo.  Utaratibu huu mpya unajibu hoja za Waheshimiwa Wabunge kuhusu usawa wa mgao wa bajeti Kimkoa na Kiwilaya.  Maelezo zaidi yatatolewa na Waziri wa TAMISEMI atakapowasilisha bajeti ya Wizara yake. 

 

MFUMO WA MAKISIO YA BAJETI YA MWAKA 2004/05

 

41.    Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza hapo awali, Serikali imelenga kukusanya mapato ya ndani ya jumla ya shilingi trilioni moja, bilioni 739 na milioni 288 (1, 739, 288 milioni) mwaka wa fedha wa 2004/05 kwa msingi wa mfumo wa kodi wa sasa, pamoja na marekebisho yanayopendekezwa katika eneo la kodi. Kiwango hiki cha mapato ni sawa na asilimia 13.8 ya Pato la Taifa.  Serikali inakusudia pia kuingiza katika mapato yake shilingi 10,115 milioni mapato yatakayotokana na uuzaji wa hisa za Serikali katika baadhi ya Mashirika ambapo Serikali ni mbia.

 

42.    Mheshimiwa Spika, Serikali imepanga kutumia jumla ya shilingi trilioni tatu, bilioni mia tatu arobaini na saba, milioni mia tano thelathini na nane (shs. 3,347,538, milioni) katika mwaka wa fedha wa 2004/05.  Kwa kuzingatia mapato ya shilingi trilioni moja, bilioni mia saba thelathini na tisa, milioni mia mbili themanini na nane (shs. 1,739,288 milioni) na yale ya kuuza hisa za shilingi bilioni kumi, milioni mia moja kumi na tano (shs. 10,115 milioni), bajeti inakuwa na pengo la shilingi trilioni moja, bilioni mia tano tisini na nane, na milioni mia moja thelathini na tano (shs. 1,598,135 milioni).  Sehemu kubwa ya pengo hili itajazwa na misaada ya Nchi Wafadhili, Jumuiya ya Ulaya, mikopo yenye masharti nafuu kutoka kwa Mashirika ya Fedha ya Kimataifa, hususan Benki ya Dunia na Benki ya Maendeleo ya Afrika.  Kwa mujibu wa makubaliano tuliyofikia kati ya Serikali ya Tanzania na hawa Wafadhili na Mashirika kwa pamoja, tumekadiria kupata misaada na mikopo ya masharti nafuu, jumla ya shilingi trilioni moja, bilioni mia tatu sitini na saba, milioni ishirini na tano (shs. 1,367,025 milioni) mwaka wa 2004/05.  Kwa hiyo pengo linapungua hadi shilingi bilioni mia mbili thelathini na moja, milioni mia moja na kumi (shs. 231,110 milioni).  Pengo hili litazibwa kwa njia ya kupunguza akiba ya Serikali katika Benki Kuu na kukopa kutoka soko la fedha la ndani kama nilivyosema hapo awali.

 

MAREKEBISHO YA MFUMO WA KODI, ADA MBALIMBALI NA HATUA NYINGINE ZA MAPATO

 

43.    Mheshimiwa Spika, hapo mwanzo nimetoa maelezo kuhusu matokeo mazuri ya hatua zilizochukuliwa na Serikali mwaka huu wa fedha unaoisha za kuongeza tija na kuziba mianya katika ukusanyaji wa mapato ya Serikali.  Aidha,    kama nilivyoeleza awali, Serikali ina dhamira ya dhati ya kuona kuwa tija katika sekta ya kilimo inaongezeka ili kupanua ajira, kujitosheleza kwa chakula, kupunguza umaskini, na kuongeza mauzo yetu nje ya nchi. Pamoja na hatua mbalimbali zilizokwishachukuliwa, Serikali itachukua hatua za ziada mwaka wa fedha ujao.  Serikali imeona kuna haja ya kutoa vivutio zaidi ili kuhamasisha uwekezaji wa miradi mikubwa na ya kati katika sekta hii ili kutumia ardhi kubwa ambayo hivi sasa haitumiki ipasavyo na kuongeza nafasi za ajira vijijini.  Aidha, tunalenga kuongeza tija kwa viwanda vinavyozalisha pembejeo au kusindika mazao ya kilimo.  Hatua hizo ambazo ni nyongeza ya zile nilizoelezea awali ni pamoja na hizi zifuatazo:-

 

(a)              Kwa Wakulima na Wafugaji Wakubwa:

Kwanza:     Katika Mfumo wa Kodi ya Mapato, utatolewa unafuu wa asilimia mia moja (100% expensing) ya gharama za mtaji katika mwaka wa kwanza wa kutumia rasilimali inayotokana na gharama hizo.  Unafuu huu pia utahusu mitambo ya usindikaji wa mazao ghafi ya kilimo mashambani au uvuvi.  Nia ni kuongeza uwekezaji katika teknolojia ya kilimo.

 

Pili:   Katika Mfumo wa Ushuru wa Stempu, utawekwa ukomo wa Shilingi 500 kwa kiwango cha ushuru unaolipwa wakati wa kuhamisha milki (conveyance) ya ardhi ya kilimo. Nia ni kupunguza gharama za kubadilisha milki ya ardhi ya kilimo.

 

Tatu: Katika Mfumo wa Tozo ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (Skills Development Levy), tozo hiyo kwa ajira za mashambani itafutwa.

 

(b)              Kwa Wakulima na Wafugaji Wadogo Wadogo:

Hatua zilizotangazwa mwaka jana  za kuboresha mazingira na mapato ya wakulima na wafugaji wadogo wadogo zinapaswa kutekelezwa kwa ukamilifu.  Napenda kukumbusha kwamba Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Jiji zina fursa ya kutoza kodi na tozo zilizoorodheshwa katika Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa kufuatia marekebisho yaliyofanywa mwaka jana. Aidha, Halmashauri zinakumbushwa kuzingatia ukomo wa asilimia 5 ya bei ya mazao kwa mkulima kwa ajili ya Ushuru wa Mazao unaotozwa, na iwapo tu mazao husika yamezalishwa katika eneo la Halmashauri hiyo. Aidha, imedhihirika kwamba Halmashauri nyingi bado zinatoza michango mabalimbali kwenye mazao kwa maelezo kuwa ni ya hiari!  Inasisitizwa kwamba michango ya namna hiyo inakubalika tu pale ambapo wanakijiji wameshirikishwa na michango iwe kwa ajili ya miradi maalumu inayotekelezwa ndani ya kijiji husika au kwa ushirikiano wa vijiji kadhaa.

 

(c)              Kwa Viwanda vya Pembejeo za Kilimo na Uvuvi:

Kwa kuwa pembejeo za kilimo na uvuvi hazitozwi VAT, wazalishaji wa ndani wa bidhaa hizo wanapata ushindani usio wa haki kutoka kwa bidhaa za namna hiyo zinazotoka nje.  Ili kuondoa kasoro hii, inapendekezwa kuwa bidhaa husika zijumuishwe kwenye kundi la kutozwa VAT kwa kiwango cha sifuri (zero rate) zinapouzwa na wazalishaji wa ndani ili kuwezesha wazalishaji hao kurejeshewa kodi wanayolipa kwenye nyenzo na malighafi. Aidha, hatua hii itaboresha mazingira ya uwekezaji kwa ajili ya kuzalisha pembejeo.

 

(d)              Kwa Viwanda vya Mazao ya Kilimo na Uvuvi:

 

Pamoja na hatua zilizotangazwa chini ya Sheria ya Kodi ya Mapato, inapendekezwa kuwa:

 

Kwanza:   Mvinyo na brandi vitakavyo-tengenezwa kutokana na zabibu za hapa nchini visitozwe Ushuru wa Bidhaa.  Lengo ni kupanua soko la zabibu hapa nchini, ili kupanua kilimo cha zao hilo, hasa Mkoani Dodoma.

 

Pili:   Inapendekezwa kusamehe kodi ya VAT kwa chai iliyosindikwa (black tea) na iliyofungashwa (packaged tea) ili kuhimili ushindani baada ya soko la chai kufunguliwa. Lengo kubwa hapa ni kulinda pato la wakulima wadogo wa chai.

 

 

 

 

Uwezeshaji Wananchi katika Biashara Ndogo na za Kati

 

44.    Mheshimiwa Spika,   eneo jingine litakalo patiwa msukumo maalum katika bajeti hii ni la biashara ndogo na za kati (SMEs).  Baada ya sekta ya kilimo, inafuata sekta ya biashara ndogo na kati kuwa tegemeo kubwa la ajira kwa wananchi wengi.  Aidha, sekta hii ni muhimu sana katika juhudi za Serikali za kuwawezesha wananchi kujiondolea umaskini.  Kwa hiyo mkazo mwingine wa bajeti hii ni kuboresha mazingira kwa ajili ya kukua kwa sekta ya biashara ndogo na za kati.

 

45.    Mheshimiwa Spika,   hivi sasa biashara ndogo na za kati zenye mauzo (turnover) isiyozidi shilingi milioni 20 kwa mwaka hulipa aina mbili kubwa za kodi kwa TRA, ambazo ni Ushuru wa Stempu na Kodi ya Mapato kwa utaratibu wa kodi ya makadirio (presumptive tax). Kodi hizo mbili zinakadiriwa kwa msingi wa thamani ya mauzo ya biashara husika.  Ili kupunguza gharama kwa biashara hizi, inapendekezwa kufuta Ushuru wa Stempu na kufidia sehemu ya mapato yatakayopungua kwa kuongeza kidogo  viwango vya kodi ya makadirio (presumptive tax rates).  Viwango vipya vya kodi ya makadirio vitakuwa kama ifuatavyo:

 

Thamani ya Mauzo

(Shilingi)

Kodi iwapo kuna kumbukumbu za kuridhisha

Kodi iwapo hakuna kumbukumbu za kuridhisha

0      -      3,000,000

1.2% ya mauzo kwa mwaka

35,000 kwa mwaka

3,000,001 - 7,000,000

Tshs.35,000 na 1.5% ya mauzo yanayozidi Tshs3,000,000 kwa mwaka.

95,000 kwa mwaka

7,000,001 - 14,000,000

Tshs.95,000 na 2.8% ya mauzo yanayozidi Tshs7,000,000 mwaka.

291,000 kwa mwaka

14,000,001 - 20,000,000

Tshs.291,000 na 5.0% ya mauzo yanayozidi Tshs.14,000,000 kwa mwaka.

589,000 kwa mwaka

 

Pamoja na kuwapunguzia mzigo wa kodi, utaratibu huu utatoa hamasa kwa wenye biashara hizi kutayarisha na kutunza kumbukumbu na hivyo kuongeza uwezekano wa kujenga mahusiano mazuri na wakopeshaji.  Aidha, viwango vya kawaida vya Kodi ya Mapato kwa msingi wa faida halisi vitatumika pale ambapo hesabu kamili zitakuwa zimeandaliwa na kuwasilishwa TRA.

 

46.    Mheshimiwa Spika, vile vile inapendekezwa kuongeza kiwango cha chini (threshhold) cha mauzo kwa ajili ya usajili wa VAT kutoka shilingi milioni 20 hadi milioni 40 kwa mwaka.  Lengo la hatua hii ni kuondoa biashara ndogo ndogo katika wigo wa VAT kwa kuzingatia gharama za kutunza mahesabu na pia gharama za kusimamia na kutawala ukusanyaji wa kodi hii. Hata hivyo, biashara zenye kiwango hiki cha mapato zitaweza kujisajili kama zikipenda kukusanya VAT lakini zitalazimika kufuata masharti ya TRA kuhusu uwajibikaji (compliance). Hatua hii itaongeza tija ya TRA ya kusimamia ukusanyaji wa kodi hii kwa kuwa itaachana na utitiri wa walipa kodi wenye mchango mdogo kimapato.  Hatua hii ikifanikiwa uamuzi kuhusu kiwango cha chini cha VAT utafanywa.  Kushusha kiwango hicho kwa asilimia 2 tu kutailetea Serikali hasara ya shilingi bilioni 59 na kuathiri sana mapato ya kodi hiyo katika bajeti.

 

47.    Mheshimiwa Spika, pendekezo la tatu linalolenga kuboresha mazingira na kuondoa kero kwa biashara, hasa ndogo na za kati linahusu ada za leseni za biashara chini ya Sheria ya Leseni za Biashara ya mwaka 1972. Kwa kuwa nia ya leseni za biashara ni kusimamia tu kanuni za biashara kwa kutoa leseni (regulatory) na wala siyo chanzo cha mapato, hatua zifuatazo zinapendekezwa:

 

Kwanza:  Kufuta ada za leseni kwa hospitali, zahanati na vituo vya afya vinavyoendeshwa na asasi za dini ili kupanua huduma za afya zinazotolewa na asasi hizo.

 

Pili:          Kufuta ada ya leseni inayotozwa chini ya Sheria ya Leseni za Biashara ya 1972 kwa  biashara zenye mauzo yasiyozidi shilingi milioni 20 kwa mwaka ili kupunguza gharama na kuwezesha vijana na wafanyabiashara wadogo kuanzisha biashara kwa njia halali.  Biashara hizi zitapewa leseni bila kulipia ada.

 

Tatu:       Biashara zenye mauzo yanayozidi Shilingi milioni 20 kwa mwaka zitozwe ada ya leseni ya shilingi 20,000/= tu ili kupunguza gharama zinazoambatana na kuanza biashara, na kuweka mazingira mazuri ya kuingiza biashara nyingi katika Uchumi Rasmi.

 

Nne:         Kufuta ada za leseni zinazotozwa chini ya Sheria ya Leseni za Biashara, pale ambapo biashara husika inasimamiwa chini ya Sheria nyingine ya kisekta ambapo leseni nyingine hutolewa chini ya sheria hizo.  Mfano ni biashara ya kibenki, bima, hoteli n.k. 

 

Tano:       Leseni ya biashara chini ya Sheria ya Leseni za Biashara itolewe mara moja tu wakati biashara inapo-anzishwa.  Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa, na Jiji zitakiwe kutayarisha na kutoa takwimu sahihi za leseni za biashara kwa mamlaka husika ili kuwa na takwimu pale zinapotakiwa kufanya hivyo.  Kwa kuwa wenye biashara wanasajiliwa pia na TRA kupitia Namba ya Utambulisho ya Kodi (TIN), hakuna haja ya kukata leseni ya biashara kila mwaka.

 

Sita:         Pamoja na hatua hizi zinazohusu kodi na tozo nyingine mbalimbali, ningependa kueleza kwamba Mfuko wa Dhamana ya Mikopo kwa ajili ya Biashara Ndogo na za Kati ulioanzishwa mwaka huu wa fedha umeongezewa fedha katika bajeti hii.  Kanuni na taratibu za kutawala mfuko huo zimeshakamilika.

 

48.    Mheshimiwa Spika,  pamoja na hatua hizi za kuboresha sekta za kilimo na biashara ndogo na za kati, marekebisho mengine mapya katika kodi mbalimbali yanapendekezwa kama ifuatavyo:

 

(i)                Mfumo wa Kodi ya Mapato

Sheria ya Kodi ya Mapato ya mwaka 2004 iliyopitishwa katika kikao cha Bunge cha mwezi Aprili itaanza kutumika kuanzia Julai 2004.  Inapendekezwa kwamba uandishi wa Sheria hiyo urekebishwe ili kufafanua kwamba Sheria hii itatumika kuanzia Julai 2004 kwa walipa kodi wote isipokuwa wale ambao wanatengeneza mahesabu na ambao mwaka wao wa mapato ulianza kabla ya Julai 2004.

 

(ii)             Mfumo wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT)

 

(a)  Ili kuwezesha wazalishaji wa ndani kurejeshewa VAT wanayolipa kwa malighafi, inapendekezwa kujumuisha madawa ya binadamu na mifugo, vyandarua, na vifaa maalum vya walemavu katika Jedwali la I ili zisilipiwe kodi kwa kuwa kwenye kiwango cha sifuri (zero rate).

 

(b)  Kurekebisha msamaha wa kodi kwa magari kwa wale wenye msamaha huo, ili kujumuisha magari yaliyomo kwenye HS Code 8703, 8702.10.20 na 8702.90.20 yenye injini zenye uwezo zaidi ya CC 3000.

 

Pamoja na hatua nilizoeleza awali, marekebisho haya katika mfumo wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) yatapunguza mapato ya Serikali kwa shilingi 4,954 milioni.

 

Hatua mpya nilizozitaja zina lengo la kuimarisha kilimo na biashara na kuwezesha wananchi, hasa wale wa kipato kidogo kuingia katika uchumi rasmi na kujitafutia riziki ili wajiondolee umaskini.  Aidha, marekebisho katika ada za leseni yanajibu pia hoja za wawekezaji na Wafadhili wetu ambao ni pamoja na taasisi za dini zinazotoa huduma ya jamii Nchini mwetu.

 

(iii)          Mfumo wa Ushuru wa Bidhaa

Mheshimiwa Spika, inapendekezwa kufanya marekebisho kadhaa katika eneo la ushuru wa bidhaa kama ifuatavyo:

 

Kwanza, kurekebisha viwango vya Ushuru wa Bidhaa  kulingana na  mfumuko wa bei kwa bidhaa zifuatazo:

 

Moja:   Vinywaji baridi. Ushuru unaongezwa kutoka shilingi 37.50 kwa lita hadi shilingi 40.0 kwa lita.

 

Mbili:   Bia. Ushuru unaongezwa kutoka shilingi 232.0 kwa lita hadi shilingi 243.0 kwa lita.

 

Tatu:   Mvinyo.  Unaotengenezwa kwa kiwango kisichozidi asilimia 75 ya zabibu inayozalishwa hapa nchini.  Ushuru unaongezwa kutoka shilingi 743.40 kwa lita hadi shilingi 780.00 kwa lita.

 

Nne:    Vinywaji vikali.  Ushuru unapanda kutoka shilingi 1,102.50 kwa lita hadi shilingi 1,158 kwa lita.

 

Tano:   Sigara zenye urefu usiozidi milimita 70 na zinazotengenezwa kwa tumbaku inayozalishwa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 75.  Ushuru unaongezwa kutoka shilingi 3,781.05 kwa sigara 1000, hadi shilingi 3,970 kwa sigara 1000.

 

Sita:     Kwa sigara zenye urefu wa milimita 70 au zaidi zilizotengenezwa kwa kiwango cha tumbaku inayozalishwa nchini inayozidi asilimia 75.  Ushuru unaongezwa kutoka shilingi 8,920.30 kwa sigara 1000 hadi shilingi 9,367 kwa sigara 1000.

 

Saba:   Sigara nyingine zenye sifa tofauti na nilizozitaja katika vifungu vya (tano) na (sita) hapo juu, ushuru utaongezeka kutoka shilingi 16,206.75 kwa sigara 1000 hadi shilingi 17,017 kwa sigara 1000

 

Nane:  Tumbaku ambayo iko tayari kutengeneza sigara “cut rug/filler” ushuru wake unaongezeka kutoka shilingi 8,183.70 kwa kilo hadi shilingi 8,593.

 

Tisa:    Ushuru wa “Cigar” unabaki kuwa asilimia thelathini (30%).

 

Pili, kuweka  ushuru wa bidhaa (excise) kwenye huduma ya televisheni kupitia satelaiti (DSTV) kwa kiwango cha asilimia 5 kwa mauzo  ya huduma hiyo.

         

Mwisho, kurekebisha msamaha wa ushuru wa bidhaa kwa magari ili kuingiza magari yaliyomo kwenye HS Code 8703, 8702.10.20, na 8702.90.20 yenye injini zenye uwezo zaidi ya CC 3000.

 

Marekebisho haya ya Ushuru wa Bidhaa yataiongezea Serikali mapato ya shilingi milioni 6,143.

 

(iv)           Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa

Mheshimiwa Spika, inapendekezwa kufanya marekebisho ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa ili kuzipa uwezo Halmashauri kukusanya mrahaba kwenye madini ya Jasi (Gypsum), Pozzolana,  na Chokaa, ambayo yanatumiwa na viwanda kama malighafi.

 

(v)              Ada ya Leseni za Biashara zinazokusanywa na Wizara na Vyombo Vingine vya Serikali.

Mheshimiwa Spika, hatua nilizoainisha awali katika eneo hili kwa pamoja zitaipunguzia Serikali mapato kwa  kiasi cha shilingi milioni 14,000, ambazo zimegawanyika kama ifuatavyo:-

 

q       shilingi milioni 11,200 kwa Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Jiji, na

 

q       shilingi milioni 2,800 kwa Wizara ya Viwanda na Biashara.  Bajeti hii imetenga fedha hizo kufidia Halmashauri na Wizara hiyo.

 

(vi)           Ada ya Viza na Utaratibu wa kutoa Viza

 

Mheshimiwa Spika, hivi sasa wageni wanaoingia Tanzania kama wafanya-biashara wanalipa ada ya viza ya dola za Marekani 200, na wale wanaoingia kama Watalii au wasafiri wa kawaida wanalipa ada ya viza ya dola za Marekani 50.  Kwa kuwa dola 200 ni nyingi na kwa kuzingatia tofauti kubwa kati ya dola 200 na 50, wageni wengi waingiapo nchini wanajitambulisha kama wasafiri au watalii wa kawaida.  Hivyo ni wachache sana wanaolipa ada hiyo ya dola za Marekani 200.  Aidha, kuna ufujaji mkubwa wa mapato yatokanayo na ada ya viza unaosababishwa na utaratibu unaotumika wa kutoa viza kwa wageni wanaokuja nchini kwetu.  Utaratibu unaotumika ni wa kupiga mhuri kwenye pasi ya kusafiria, ambao imedhihirika hauna udhibiti, na ni wa kizamani.  Kwa sababu hizi, inapendekezwa kama ifuatavyo:-

 

(i)                 Ada ya “viza ya biashara” ya dola za Marekani 200 ipunguzwe hadi dola za Marekani 50 ili kuondoa tofauti hiyo ambayo haina faida kwa Nchi yetu ambayo inataka itembelewe na wawekezaji wengi, wafanyabiashara wengi na watalii kemkem.

 

(ii)              Utaratibu mpya wa kutumia “visa stickers” uanzishwe badala ya huu wa sasa wa mihuri, ili kudhibiti mapato yatokanayo na viza nchini na katika Balozi zetu.

 

Hatua hizi mbili kwa pamoja zitaipatia Serikali mapato mapya ya shilingi milioni 19,823.

 

(vii)        Mfumo wa Ushuru wa Forodha

 

 

Lengo la Marekebisho ya Mfumo wa Kodi mwaka 2004/05

 

49.    Mheshimiwa Spika, Lengo la marekebisho yote yanayo pendekezwa ni kuboresha mazingira ya kukuza uchumi wetu, kuwawezesha wananchi kufanya shughuli mbali mbali za kujiendeleza na kujiondolea umaskini, na kupanua wigo wa ajira na kodi.  Aidha, baadhi ya hatua hizi zitaongeza na nyingine zitapunguza mapato ya Serikali katika mwaka ujao wa fedha, kama ifuatavyo:

 

Eneo la Hatua

Nyongeza/Punguzo la Mapato (shilingi milioni)

(i)

Mfumo wa Kodi ya Ongezeko la Thamani

          (4,954)

(ii)

Mfumo wa Ushuru wa Bidhaa

           6,143

(iii)

Mfumo wa Kodi ya Mapato

          13,189

(iv)

Mfumo wa Ushuru wa Forodha

            1,138

(v)

Mfumo wa Ushuru wa Stempu

         (19,263)

(vi)

Mfumo wa Tozo ya Ufundi Stadi

           (2,076)

(vii)

Mfumo wa Leseni za Biashara

         (14,000)

(viii)

Mfumo wa Viza

           19,823

 

JUMLA

                0

 

SURA YA BAJEI YA MWAKA 2004/05

 

50.    Mheshimiwa Spika,   kwa kuzingatia mfumo wa bajeti nilioueleza hapo juu, sura ya bajeti kwa mwaka 2004/05 inakuwa kama ifuatavyo:

 

Sura ya Bajeti

Mapato

                                                             Shilingi Milioni

A.   Mapato ya Ndani                                                   1,739,288

 (i)  Mapato ya Kodi                 1,603,886  

 (ii) Mapato yasiyo ya Kodi       135,402 

 

B.   Mikopo na Misaada ya Nje

      ikijumuisha HIPC                                                 1,367,025

 

C.   Mapato kutokana na uuzaji Hisa                             10,115

 

D.   Kupunguza akiba (reserve) pamoja na

      mikopo ya ndani                                                     231,110

 

      Jumla ya Mapato Yote                                       3,347,538

 

Matumizi

E.   Matumizi ya Kawaida                                         2,239,000

(i)            Deni la Taifa                              481,175

(ii)          Wizara (sekta mbali mbali)    1,293,467

(iii)         Mikoa                                         33,473

(iv)         Serikali za Mitaa                      386,768

(v)          Matumizi Maalum                       44,117

a)   Mishahara (taasisi)                6,000

b)   Mishahara (Serikali Kuu)   32,699

c)   Tansort escrow account            561

d)   Vita Dhidi ya Rushwa                857

e)   Mafao ya Watumishi              4,000

 

F.   Matumizi ya Maendeleo                                       1,091,590

a)   Fedha za Ndani                    233,705

b)   Fedha za Nje                                    857,885

           

G.   Dharura                                                                     16,948

            JUMLA YA MATUMIZI YOTE                       3,347,538

 

MWISHO

 

51.    Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali, bajeti ya mwaka 2004/05 imeandaliwa kwa msingi wa kuendeleza juhudi za Serikali katika kutekeleza:

 

(i)                 Shabaha za Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000 ya Chama Cha Mapinduzi;

 

(ii)              Dira ya Taifa ya Maendeleo hadi 2025;

 

(iii)            Mkakati wa Kupunguza Umaskini;

 

(iv)            Sera za Kijumla za Kiuchumi kwa mwaka 2004/05.

 

52.    Mheshimiwa Spika, Kama nilivyosema, sekta ya kilimo ina uwezo mkubwa wa kutoa ajira kwa wananchi wengi iwapo yatafanyika mapinduzi zaidi katika sekta hii.  Serikali imejitahidi kufanya yale yanayowezekana kwa uwezo uliopo.   Sasa ni juu ya wananchi, pamoja na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi, kutumia fursa hizi ili kuinua sekta hii.  Aidha, sekta ya Viwanda pia ina uwezo wa kuongeza Pato la Taifa na ajira kwa haraka kama itapewa msukumo wa kutosha.   Ili kupata mafanikio ya wazi, msukumo katika ukuzaji wa uchumi lazima uwe wa dhati kabisa.  Bajeti hii inalenga kuweka misingi mizuri kwa sekta ya biashara ndogo na za kati ili iweze kuibuka na kujaza pengo dhahiri katika uchumi.

 

53.    Mheshimiwa Spika, katika yote haya, mafanikio halisi ya kukuza uchumi na kuondoa umaskini yatapatikana pindi tutakapoweza kuunganisha Nchi yetu kwa njia ya miundo mbinu ya barabara, reli, mawasiliano na nishati.  Pili tunahitaji kujenga uwezo wa utaalam ambao ni lazima katika dunia hii ya utandawazi.  Tatu, kwa kuwa wananchi wengi wanaishi vijijini na wanategemea kilimo kwa chakula na ajira, ni lazima mkakati wetu wa kuinua kilimo uwe imara zaidi – na uunganishe kilimo, viwanda na biashara, ndipo tutaweza kugeuza sekta hiyo iwe ya kisasa.  Pengine tuna haja ya kuangalia tena vipaumbele vyetu ili tupate tija ya uhakika kwa kutumia uwezo mdogo tulio nao wa fedha kwa maeneo machache kwanza kuliko kugawa kidogo kidogo bila mafanikio ya maana.  Nitafurahi kupata ushauri wa Waheshimiwa Wabunge juu ya wazo hili wakati wa mjadala wa hoja hii.

 

54.    Mheshimiwa Spika, Bajeti hii ni mfululizo wa jitihada za Serikali ya awamu ya tatu za kurekebisha uchumi na kupambana na umaskini.  Inaendeleza matakwa ya uchumi tulivu, endelevu na unaokua hatua kwa hatua, mwaka hadi mwaka.  Inaweka mazingira mazuri ya kujiajiri, kuwekeza, na kujiendeleza.  Inatoa fursa kwa kila mtu kufanya kazi kwa tija, hasa za kilimo na shughuli ndogo ndogo.  Inawezesha Wananchi walio kwisha anza safari ya kujiajiri na kujitegemea kiuchumi kupiga hatua zaidi, kwa kuwaondolea urasimu, kuwadhamini wakikopa benki, kuwapunguzia kodi, leseni na ushuru wa aina aina na kuwaondolea kero ya kufukuzana na wakata leseni, hasa wa mijini.  Naamini kuwa hotuba zifuatazo za Mawaziri wa kisekta zitatangaza hatua zaidi za kuwawezesha Watanzania kujiendeleza kiuchumi na kijamii katika sekta zao kwa mujibu wa sera iliyo wekwa.

 

Pamoja na hayo Mheshimiwa Spika, hakuna Serikali inayo weza kumlisha au kumtajirisha mwana kaya ambaye hachukii umaskini na kufanya kazi kwa bidii.  Uchumi wa kaya na wa taifa unakuzwa na wanakaya na wananchi kwa ujumla wao.  Serikali itaendelea kuweka mazingira bora ya kumwezesha mwenye nia na dhamira ya kupiga hatua ya maendeleo ya kaya yake na ya taifa lake.  Naamini kabisa kwamba Waheshimiwa Wabunge wanaelewa sana ninachosema na hivyo natumaini watakuwa radhi kuniunga mkono kwa kura zao moja moja.

 

55.    Mheshimiwa Spika,  naomba kutoa hoja.

 

                                    Bonyeza hapa kuona majedwali