HOTUBA YA WAZIRI WA UJENZI, MHESHIMIWA JOHN P. MAGUFULI (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MPANGO WA MAENDELEO NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2004/05

 

UTANGULIZI

 

1.                 Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha makadirio ya matumizi ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka wa fedha wa 2004/2005.

 

2.                 Mheshimiwa Spika, Kwanza kabisa napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa Kamati ya Bunge ya Miundombinu kwa kukamilisha kazi ya kupitia, kujadili na kutoa ushauri kuhusu Bajeti ya Wizara yangu na hatimaye kuidhinisha Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2004/2005. Wizara yangu imejitahidi kuzingatia ushauri uliotolewa na Kamati ya Bunge ya Miundombinu katika Bajeti hii na tutaendelea kuyafanyia kazi maelekezo ya Kamati yaliyobaki na yale yatakayotolewa na Bunge lako Tukufu wakati wa kujadili Bajeti hii.

 

DIRA YA WIZARA

 

3.                 Mheshimiwa Spika, Dira ya Wizara ya Ujenzi ni kuendeleza Sekta ya Ujenzi ili iwe endelevu, yenye ufanisi na inayotoa huduma bora na nafuu katika mazingira ya ushindani ili kuchochea na kuleta ufanisi katika maendeleo ya jamii na kiuchumi na hivyo kuchangia kikamilifu katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

 

Aidha, katika kuendeleza Sekta ya Ujenzi, ili kutumia kikamilifu faida ya Kijiografia iliyonayo Tanzania katika kuziunganisha nchi kadhaa tunazopakana nazo na Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mwanza, Kigoma, Bukoba na Mtwara, Wizara yangu inaendelea kutekeleza ukarabati na ujenzi wa Barabara Kuu kwa kiwango cha lami katika Kanda Kuu Tisa za Usafirishaji kwa kadri hali ya uchumi wetu na bajeti inavyoruhusu.

 

    MAJUKUMU YA WIZARA

 

4.  Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika uanzishwaji wa Wakala wa Barabara (TANROADS) na Wakala wa Majengo (TBA), Taasisi hizi sasa ndizo zenye majukumu ya utekelezaji wa kazi za barabara na majengo na nyumba za Serikali. Kazi hizi zilikuwa zinafanywa na Wizara moja kwa moja hapo awali. Majukumu yaliyobaki yanayoendelea kutekelezwa na Wizara yanahusu:

 

·        Kuandaa Sera, kubuni Mikakati na kupanga Mipango inayolenga katika ukuzaji, uimarishaji na uendelezaji wa sekta ya ujenzi nchini katika muda mfupi, wa kati na mrefu.

·        Kusimamia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Ujenzi kwa kuzingatia mikakati iliyowekwa.

·        Kusimamia uendeshaji wa shughuli za Bodi ya Mfuko wa Barabara, Wakala wa Barabara, Wakala wa Majengo pamoja na Wakala nyingine zinazotarajiwa kuundwa chini ya Wizara kama vile Wakala wa Ufundi na Umeme (Tanzania Electrical, Mechanical and Electronics Services Agency - TEMESA) na Wakala wa Bohari Kuu ya Serikali (Government Stores Agency – GSA).

·        Kuratibu shughuli za Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi ambazo ni Baraza la Taifa la Ujenzi na Bodi za Usajili wa Makandarasi, Wahandisi, Wasanifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi na Usimamizi wa Vifaa.

·        Kutafuta fedha za nje na za ndani za kugharamia miradi ya barabara, madaraja, vivuko n.k.

·        Kuandaa na kusimamia viwango vya ubora wa kazi za ujenzi, ukarabati pamoja na matengenezo ya barabara; ujenzi nyumba na majengo ya Serikali; vifaa vya kawaida vitumiwavyo na Serikali; mitambo; magari na vifaa vya umeme.

·        Kusimamia shughuli za Usalama wa Barabara (Road Safety)

·        Kusimamia shughuli za ununuzi, ukarabati na matengenezo ya magari, viyoyozi na vifaa vya elektroniki; kuendesha vivuko na ukodishaji wa magari, mitambo ya kokoto na mitambo ya barabara ambavyo ni mali ya Serikali.

·        Kusimamia Maendeleo ya Watumishi wa Wizara.

 

Aidha, majukumu mengine ya Wizara yanayotekelezwa kupitia Wakala, Baraza la Ujenzi, Bodi na Vituo/Vyuo vilivyo chini ya Wizara ni kama yalivyofafanuliwa kwa kirefu katika aya ya 38 hadi 69.

 

Mikakati ya Utekelezaji 

 

5.   Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha majukumu yaliyotajwa hapo juu Wizara imejiwekea mikakati ifuatayo:-

 

·     Kutafuta vyanzo vya ziada vya fedha za Mfuko wa Barabara ili kukidhi mahitaji ya matengenezo ya mtandao mzima wa barabara.

·     Kutoa kipaumbele katika ukarabati na ujenzi wa barabara kwa kufuata Kanda Kuu za Usafirishaji, Barabara za Mikoa na za Wilaya ambazo ni muhimu kwa huduma za usafirishaji wa mazao ya kilimo na huduma nyingine muhimu za kitaifa.

·        Ili kuimarisha mabadiliko yanayofanyika katika sekta ya Ujenzi, Wizara itaendelea kuboresha uwezo (capacity building) wa Wakala wa Barabara na Majengo ili kuongeza ufanisi zaidi katika matengenezo na ukarabati wa barabara, nyumba na majengo ya Serikali.

·     Kuweka mazingira mazuri ya upatikanaji wa mitambo ya ujenzi kwa kuimarisha karakana za Serikali na kuhamasisha watu binafsi kuanzisha kampuni za kukodisha mitambo.

·     Kukaribisha Sekta binafsi kushiriki katika ujenzi wa miradi ya barabara na majengo ya Serikali. Aidha, Wizara yangu inakamilisha Mwongozo rasmi utakaoweka wazi utaratibu wa Ushiriki wa Sekta Binafsi katika shughuli za ujenzi wa barabara, majengo na madaraja.

·     Kuendeleza mafunzo kwa Wahandisi Washauri na Makandarasi wa kizalendo ili wasimamie na kutekeleza vizuri mikataba ya ujenzi na matengenezo ya barabara.

·     Kusimamia Sheria ya Udhibiti wa Uzito wa Magari na matumizi bora ya barabara kwa kuwashirikisha wadau wote.

·     Kuimarisha huduma za vivuko nchini kwa kununua vivuko vingine vipya vyenye uwezo mkubwa na kuvifanyia ukarabati vivuko vilivyopo hivi sasa.

·     Kuwaelimisha wananchi ili waweze kutambua mipaka ya maeneo ya barabara (Road Reserve) na kutayarisha ramani za barabara zitakazoonyesha mipaka ya miliki ya barabara zote nchini. Aidha uwekaji wa alama za kuonyesha mipaka ya maeneo ya barabara nao sasa umepewa umuhimu katika miradi yote inayotekelezwa.

·     Kuendeleza teknolojia ya nguvu kazi ili kuwapa uwezo wananchi wengi zaidi kushiriki katika kazi za matengenezo ya barabara katika maeneo yao bila kusubiri msaada kutoka Serikalini.

·     Kuimarisha uwezo wa kiutendaji wa Bodi na Taasisi zilizo chini ya Wizara ili ziweze kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi.

·     Kuendesha mafunzo kwa Wafanyakazi wa Wizara ili kuwajengea uwezo wao wa kufanya kazi.

·     Kukamilisha uanzishwaji wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) na Wakala wa Bohari Kuu ya Serikali (GSA).

 

USHIRIKIANO WA KIKANDA

 

Mtandao wa Barabara za Jumuiya ya Afrika Mashariki na NEPAD

6.       Mheshimiwa Spika, Nchi za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC) zimepanga kutekeleza miradi ya barabara katika Kanda tano (5). Miradi inayohusika ni ile iliyokubaliwa katika Mkutano wa mwaka 1998 (Kiambatanisho Na. 11) na pia miradi mipya ambayo ilikubaliwa iongezwe kwenye mtandao wa miradi ya barabara ya Jumuiya ya Afrika Mashariki katika Mkutano wa mashauriano kati ya Wahisani na Nchi Wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki uliofanyika tarehe 29 – 30 Aprili, 2003 (Kiambatanisho Na. 11A).  Wahisani walikubaliana na utekelezaji wa miradi iliyokuwepo toka mwaka 1998 na miradi mipya iliyoongezwa. Nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki kwa kushirikiana na Sekretariati ya Jumuiya hiyo tunaendelea kuwasiliana na Wahisani kwa lengo la kufanikisha ahadi hiyo. Hali halisi ya maendeleo ya upatikanaji fedha ama utekelezaji wa kila mradi ni kama ilivyofafanuliwa katika Viambatanisho Na. 11 na 11A vilivyoko ukurasa wa 92 hadi 95.

 

7.       Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba mwaka 2003 kilifanyika kikao cha Wakuu wa Nchi na Serikali za nchi za Mashariki mwa Afrika (Eastern Africa Sub-region Summit) mjini NairobiKenya.  Pamoja na mambo mengine, Wakuu wa Nchi walikubaliana msisitizo uwekwe kwenye miradi ya barabara iliyoko kwenye kanda tano za barabara za Afrika Mashariki zilizokwisha ainishwa. Aidha, Wizara yangu imeainisha miradi ya barabara itakayoingizwa katika Mkakati Mpya wa Kuondoa Umaskini yaani “The New Partnership for Africa’s Development – NEPAD”.  Miradi hiyo ni pamoja na barabara zenye urefu wa kilomita 7,499 (Kiambatanisho 12 – ukurasa wa 96 hadi 97) na Daraja la Umoja kati ya Tanzania na Msumbiji. Miradi hii inakadiriwa kugharimu Dola za Marekani 2,414.4 milioni.

 

Ukanda wa Maendeleo wa Mtwara (Mtwara Development Corridor – MtDC)

 

8.       Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa Programu ya uendelezaji wa Ukanda wa Maendeleo wa Mtwara unaendelea kwa miradi mikubwa (anchor projects) mitatu.  Hatua zilizofikiwa kwa sasa ni kama ifuatavyo:-

 

i)       Barabara ya Mtwara – Masasi – Songea – Mbamba Bay

 Kazi ya upembuzi yakinifu (Feasibility Study) ilimalizika mwezi Januari 2004. Kazi ya usanifu wa kilomita 200 kati ya Songea na Matemanga itafanyika katika mwaka wa fedha 2004/05 kwa kugharamiwa na fedha zilizobaki baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu.

 

ii)                Daraja la Umoja kati ya Tanzania na Msumbiji

Juhudi za kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Daraja hili zinaendelea. Serikali ya Japan imekubali kimsingi tangu mwezi Oktoba 2003 kuwa itasaidia ujenzi wa daraja hili na imeahidi kuleta ujumbe Tanzania kabla ya mwisho wa mwaka huu 2004 ili kufanya uchunguzi wa kitaalam.  Katika mwaka wa fedha wa 2004/05 Serikali ya Tanzania imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuanza kufanya Upembuzi Yakinifu (Feasibility Study). 

 

iii)              Mradi wa uzalishaji umeme kwa kutumia makaa ya mawe ya Mchuchuma – Katewaka

 

Serikali imeendelea kufanya majadiliano na wawekezaji wa mradi huu kwa lengo la kuhakikisha kuwa mradi utakapotekelezwa utakuwa na manufaa kwa uchumi wa nchi hususan sekta ya umeme. Serikali iliona ni vema kwanza ijiridhishe na matokeo ya awali ya utafiti uliofanywa na wawekezaji kwa kuzingatia vigezo vya kiuchumi, kiufundi, kifedha na pia masuala ya mazingira. Mnamo mwezi wa Mei 2004 Serikali imewaelekeza NDC na Wizara ya Nishati na Madini kufanya majadiliano na wawekezaji wa mradi kwa kuzingatia vigezo vilivyotajwa hapo juu.

 

9.       Mheshimiwa Spika, Mwezi Mei 2004 ulifanyika mkutano huko Maputo – Msumbiji uliojumuisha nchi zinazotekeleza Mkakati wa Maendeleo ya Kikanda (Spatial Development Initiative).  Nchi zilizowakilishwa ni Msumbiji, Afrika ya Kusini, Zimbabwe, Malawi, Namibia, Angola na Tanzania.  Kimsingi, mkutano ulisisitiza umuhimu wa kanda za maendeleo. Mkutano ujao wa pamoja kwa nchi hizi utafanyika Tanzania kabla ya mwisho wa mwaka 2004.  Mkutano huu utasaidia kuutangaza Mpango wa Maendeleo na miradi iliyomo katika Ukanda wa Mtwara kwa wawekezaji wa nje ya nchi.

 

MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA WIZARA KWA MWAKA 2003/04.

 

10.     Mheshimiwa Spika, Baada ya kutoa maelezo kuhusu Dira, Majukumu na Mikakati ya Wizara yangu, naomba sasa kulieleza Bunge lako Tukufu hali ya utekelezaji wa malengo ya Wizara kwa mwaka wa fedha wa 2003/04.

 

Ukusanyaji wa Mapato kwa mwaka 2003/04

 

11.     Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2003/2004, Wizara ilipanga kukusanya jumla ya shilingi 3,724,943,000.00 kupitia Idara zake zinazokusanya Mapato ambazo ni Ufundi na Umeme, Ugavi na Huduma na Utawala. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei, 2004, jumla ya shilingi 3,072,020,781.58 zilikusanywa ambazo ni asilimia 82.5 ya malengo yaliyowekwa. Mchanganuo wa mapato hayo kwa kila idara umeonyeshwa kwenye Kiambatanisho Na. 1 kilichoko ukurasa wa 58.

 

 

 

 

Matumizi ya Kawaida Mwaka 2003/04

 

12.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2003/04 Wizara ilitengewa jumla ya shilingi 59,689,799,900 za Matumizi ya Kawaida. Kati ya fedha hizi shilingi 45,156,999,600 zilikuwa fedha za Mfuko wa Barabara na shilingi 14,522,800,300 zilikuwa za Matumizi Mengineyo na Mishahara.

 

13.     Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei, 2004 jumla ya shilingi 11,381,802,114 za Matumizi ya Kawaida zilikuwa zimetumika ambazo ni sawa na asilimia 78.4 ya fedha zote zilizotengwa kwa mwaka huu.  Pia hadi Mei, 2004 jumla ya shilingi milioni 43,940 za Mfuko wa Barabara sawa na asilimia 97 ya fedha zilizotengwa kwa mwaka huu zilikuwa zimetolewa kwa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi.

 

Muhtasari wa Matumizi ya Kawaida kwa mwaka 2003/04, umeonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 2 kilichoko ukurasa wa 59.

         

          Mpango wa Matengenezo ya Barabara Kuu na za Mikoa kwa Mwaka 2003/04

 

14.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2003/04, matengenezo ya Barabara Kuu na zile za Mikoa yaliyopangwa yalilenga kuhudumia kilomita 16,274 na madaraja 1,809 kwa kutumia jumla ya shilingi 61,399,954,000 ambapo shilingi 40,234,901,000 ni kutoka Mfuko wa Barabara na shilingi 21,165,063,000 zilikuwa fedha za kigeni.

 

15.            Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei 2004, kazi zilizokuwa zimeanza na zinaendelea kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara zinahusisha mikataba 705 ya makandarasi yenye thamani ya shilingi 31,024,700,000 na kazi zinazofanywa na TANROADS moja kwa moja (Force Account) zenye thamani ya shilingi 2,861,210,000 kama inavyoonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 10 kilichoko ukurasa wa 91.

 

          Aidha, hadi mwishoni mwa mwezi Mei 2004, jumla ya barabara zenye kilomita 10,898 na madaraja 1,119 vilifanyiwa matengenezo ya aina mbalimbali.

 

Matengenezo ya Miundo Mbinu iliyoharibiwa na Mvua za El-Nino

 

16.     Mheshimiwa Spika, mradi huu unahusisha Ukarabati na Matengenezo ya Barabara Kuu katika Kanda nne zenye urefu wa km 2,643 zilizoharibiwa na mvua za El Nino za Mwaka 1997/98. Kazi zinazofanywa kwenye Barabara za Kanda hizi ni pamoja na ukarabati/matengenezo ya madaraja madogo na makalavati, kutengeneza matuta ya barabara na kuweka changarawe kwenye sehemu zilizoharibika.

 

17.     Mheshimiwa Spika, urefu halisi unaohusika na Ukarabati/Matengenezo haya kwenye Kanda zote nne ni Km 845 ambazo zimegawanywa kama ifuatavyo:

 

·        Ukanda wa Ziwa (Mwanza na Mara) km 128; barabara za Usagara-Katoro, Nyamswa-Ikoma na Nyanguge-Musoma. Sehemu kubwa ya matengenezo zaidi ya asilimia 90 imekamilika.

·        Ukanda wa Kati –Magharibi (Tabora, Rukwa na Singida) km 325; Barabara za Tabora-Nzega, Tabora-Ipole-Koga, Ipole-Rungwa, Manyoni-Rungwa na Mpanda-Koga. Kazi zinatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba 2004.

·        Ukanda wa Kusini (Iringa, Ruvuma na Mtwara) km 203; barabara za Songea-Masasi, Songea-Mbamba Bay na Itoni-Manda. Mkandarasi anaendelea na kazi.

·        Ukanda wa Magharibi (Kigoma na Rukwa) km 189, barabara za Sumbawanga-Kasesya, Mpanda-Uvinza, Uvinza-Kanyani na Mwandiga-Manyovu. Mkandarasi anaendelea na kazi.

 

Mradi huu unafadhiliwa kwa pamoja kati ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na Serikali ya Tanzania kwa gharama ya jumla ya Shilingi bilioni 14.56 ambapo ADB itatoa kiasi cha Shilingi bilioni 13.08 na Serikali ya Tanzania itachangia kiasi cha shilingi bilioni 1.48.

 

Matengenezo ya Barabara chini ya RUSIRM

 

18.     Mheshimiwa Spika, mradi wa RUSIRM ni wa muda wa Miaka 5 ya matengenezo ya barabara kwa mikoa ya Iringa Kusini na Ruvuma.  Mradi ulibuniwa mwaka 1995 na kuanza rasmi Julai 2000 na utaisha Juni 2005.

 

Mradi unagharamiwa kwa pamoja kati ya Jumuiya ya nchi za Ulaya (EU) na Serikali ya Tanzania kwa gharama ya EURO 34.17 milioni.  EU itachangia EURO 21.8 milioni na Serikali ya Tanzania EURO 12.37 milioni.   Kwa sasa hivi (2003/04) mradi uko mwaka wa 4 wa utekelezaji.

Hadi kufikia Machi 2004 zaidi ya km 600 kati ya km 898 zimefanyiwa ukarabati mkubwa kwa mikoa ya Iringa na Ruvuma.  Aidha matengenezo ya sehemu korofi na matengenezo ya kawaida (Routine and Recurrent Maintenance) yamekuwa yakiendelea kwa barabara zote chini ya mradi zenye jumla ya km 2,716 na kufanya ziendelee kupitika bila matatizo kwa mwaka mzima.  Mpaka sasa Serikali ya Tanzania imechangia EURO 7,455,410 na EU imechangia EURO 15,581,375.52.

 

Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo ya Barabara Kuu na za Mikoa kwa mwaka 2003/04     

 

19.  Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2003/2004 Wizara ilitengewa jumla ya shilingi milioni 157,180.04 kwa Miradi ya Maendeleo ambapo shilingi milioni 48,989.47 zilikuwa fedha za hapa na shilingi milioni 108,191.57 zilikuwa fedha za nje. Kati ya fedha za hapa shilingi milioni 4,470.47 zilikuwa fedha za Mfuko wa Barabara na shilingi milioni 44,519.00 zilikuwa fedha za Maendeleo kutoka Hazina.

Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Mei 2004, shilingi milioni 43,340.95 sawa na 97.4% ya fedha zote za Maendeleo kutoka HAZINA na shilingi milioni 3,994 sawa na asilimia 89 ya fedha za Mfuko wa Barabara zilizopangwa kwa mwaka 2003/04 zilikwishatolewa.  Aidha, katika kipindi hiki Bajeti ya Maendeleo ilipunguzwa kwa shilingi bilioni 1.178 ili kuchangia dharura za ununuzi na usambazaji wa chakula cha njaa na kusaidia gharama za uzalishaji umeme.

 

Taarifa ya utekelezaji ya mradi kwa mradi zimeonyeshwa kwenye Kiambatanisho Na. 3 ukurasa wa 60 hadi 62 kwa miradi ya Barabara Kuu na Kiambatanisho Na. 4 ukurasa wa 63 kwa miradi ya Barabara za Mikoa.

Utelelezaji wa mwaka 2003/04 wa Wakala, Bodi, Baraza la Ujenzi, Vituo na Vyuo vilivyo chini ya Wizara

 

20.     Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Taasisi zilizo chini ya Wizara kwa mwaka 2003/04 ni kama ulivyofafanuliwa katika maelezo ya Taasisi husika katika aya ya 38 hadi 69.

 

Mafanikio na Matatizo yaliyojitokeza Wakati wa Utekelezaji wa Malengo ya mwaka 2003/04

 

21.     Mheshimiwa Spika, Kwa ujumla Wizara imepata mafanikio mengi katika utekelezaji wa mipango ya mwaka 2003/04, kama ilivyofafanuliwa katika taarifa ya utekelezaji wa mradi kwa mradi. Aidha mafanikio mengine yaliyopatikana ni kama ifuatavyo:

 

i)                   Kukamilika na kufunguliwa rasmi kwa Daraja la Mkapa katika Mto Rufiji tarehe 2.8.2003. Aidha, madaraja mengine 23 kati ya Tunduma – Sumbawanga, Tanga – Horohoro na barabara ya TANZAM yamekamilika.

ii)                Kuweka Mawe ya Msingi kwa ajili ya ujenzi unaoendelea wa kiwango cha lami wa barabara zifuatazo:

·        Mbwemkulu-Mingoyo (km 95)

·        Dodoma-Manyoni-Singida (km 246)

·        Ilula-Tinde/Isaka-Nzega (km 168)

·        Songwe – Tunduma (km 70)

Aidha, barabara nyingi zinaendelea kukarabatiwa kwa kiwango cha lami na changarawe ili nchi yote iendelee kupitika. Pia, madaraja yanaendelea kutengenezwa katika barabara mbalimbali.

 

iii)              Daraja la Umoja: Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alizungumza na Serikali ya Japani alipokwenda Japani kuhudhuria Mkutano wa TICAD III mwezi Oktoba 2003. Katika mazungumzo hayo, Serikali ya Japani ilikubali kimsingi kuwa itasaidia ujenzi wa Daraja la Umoja. Serikali ya Japani imeahidi kuleta ujumbe Tanzania kabla ya mwisho wa mwaka huu ili kufanya uchunguzi wa kitaalamu. Pia, ili kuhakikisha kuwa Daraja hili linapata fedha za ujenzi, Serikali ya Tanzania imeamua kuanza kutenga fedha za ndani katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2004/2005 ili kuanza kufanya upembuzi yakinifu (Feasibility Study).

 

iv)              Daraja la Kigamboni: Katika mwaka huu 2004 Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) wameonyesha nia ya kuwekeza katika daraja la Kigamboni. Serikali na NSSF tumeingia katika Mkataba wa Maelewano ambapo katika kipindi cha miezi sita, NSSF watawasilisha Serikalini mpango wao madhubuti wa kujenga daraja hili.  Baada ya hapo mapendekezo yao yakikubalika na Serikali kazi za ujenzi zitaanza.

 

v)       Kivuko cha Ukara: Kivuko hiki kimeshanunuliwa na kazi ya kukifunga itakamilika mwezi Juni mwaka 2004. Aidha, Kivuko cha Kilombero ambacho kilinunuliwa mwaka 2002/03 kinaendelea kufanya kazi vizuri.

 

vi)      Usajili wa magari kwa namba za Serikali: Usajili wa magari   ya Serikali na ya miradi uliendelea kufanyika ili kupunguza matumizi mabaya ya magari, pikipiki na mitambo ya Serikali. Kuanzia mwezi Januari 2002 hadi kufikia Mei 2004, usajili umefanyika kama ifuatavyo: - magari 3,204 yamesajiliwa kwa namba za ST, magari 2,834 kwa namba za SU, magari 477 kwa namba za SM, magari 4,301 kwa namba za DFP na magari 105 kwa namba za PT. Aidha pikipiki 1207 zilisajiliwa kwa namba za ST, 338 kwa namba za SU, 215 kwa namba za SM, 1,487 kwa namba za DFP na 3 kwa namba za PT. Halikadhalika ilisajiliwa mitambo 199 kwa namba za CW, 93 kwa namba za SU, 21 kwa namba za SM na 81 kwa namba za DFP. Hivyo kwa kipindi hicho jumla ya magari 11,026, pikipiki 3,250 na mitambo 394 imesajiliwa kwa namba za Serikali na kufanya jumla ya vifaa vilivyosajiliwa tangu zoezi lianze kuwa 15,064.

 

vii) Uuzaji na Ujenzi wa Nyumba za Watumishi:

 

Wakala wa Majengo umewauzia watumishi wa Serikali na wa Mashirika ya Umma nyumba zipatazo 5,248 kuanzia mwaka 2002 hadi sasa na fedha zinazopatikana zinatumika kujenga nyumba nyingine. Jumla ya shilingi 41,567,805,337.00 zinatarajiwa kukusanywa kutokana na mauzo ya nyumba hizi. Katika nyumba 5,248 zilizouzwa, nyumba 4,234 wameuziwa Wafanyakazi wa Serikali na nyumba 1,188 zimeuzwa kwa Wafanyakazi wa Mamlaka ya Bandari (THA). Aidha nyumba zipatazo 2,580 za Shirika la Reli (TRC) zitauzwa kwa Watumishi wanaoishi katika nyumba hizo.

 

Wakala pia umejenga nyumba 173 Dar es Salaam, Dodoma na Arusha na umetiliana mkataba na Jeshi la Kujenga Taifa na Jeshi la Magereza kujenga nyumba nyingine 300 za Watumishi wa Serikali katika Manispaa ya Dodoma ili kuharakisha uhamishaji wa Makao Makuu kwenda Dodoma.

 

Aidha, Wakala kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu hivi karibuni umekamilisha kuandaa mwongozo wa utaratibu wa kuingia ubia wa wawekezaji binafsi kwa ajili ya kuendeleza “Prime Areas” zilizo chini ya Wakala. Mwongozo huo utaanza kutumika mwaka 2004/05.

 

viii)    Kupungua kwa Tatizo la Kuzidisha Uzito wa Magari katika Barabara zetu: Tatizo la kuzidisha uzito katika barabara zetu linaendelea kupungua ambapo mpaka sasa magari yanayozidisha uzito ni chini ya asilimia 10 ukilinganisha na asilimia 30 kwa mwaka 1998. Mafanikio haya yote yanatokana na Wizara kuchukua hatua zifuatazo:

·        Kuendesha kampeni za kuwaelimisha wadau wetu kuhusu suala la Usalama Barabarani kupitia vipindi vya Radio na Televisheni pia makala katika magazeti.

·        Kufunga mizani ya kisasa na kununua mizani 18 inayohamishika (mobile).

·        Kufukuza wafanyakazi 140 katika vituo vya mizani baada ya kutuhumiwa kujihusisha na rushwa.

 

22.     Mheshimiwa Spika, baadhi ya matatizo yaliyoathiri utekelezaji wa kazi zilizopangwa kwa mwaka 2003/04 ni pamoja na:

 

·        Ufanisi duni wa baadhi ya makandarasi katika kutekeleza kazi za barabara.

·        Upungufu wa mitambo ya kuwawezesha makandarasi wazalendo kumudu utekelezaji wa kazi za barabara.

·        Baadhi ya wahisani kuchelewa kutoa fedha kufuatana na ratiba iliyowekwa hivyo kuchelewesha miradi kuanza ama malipo kwa makandarasi kwa muda uliokubaliwa katika mikataba.

·        Upungufu wa fedha kulinganisha na mahitaji halisi ya miradi ya maendeleo na kazi za ujenzi na matengenezo ya barabara pamoja na ujenzi wa nyumba za kuwauzia wafanyakazi wa Serikali.

·        Utaratibu mrefu wa kutoa zabuni (hasa kwa miradi ya Wahisani) umechelewesha kuanza kwa utekelezaji wa baadhi ya miradi.

 

KAZI ZILIZOPANGWA KUFANYIKA KATIKA MWAKA WA FEDHA 2004/05

 

          Mpango wa Matengenezo ya Barabara Kuu na za Mikoa 2004/05

 

23.     Mheshimiwa Spika, malengo ya mwaka wa 2004/05 ni kufanyia matengenezo Barabara Kuu na Barabara za Mikoa zenye urefu wa kilomita 13,328 na madaraja 1,692. Fedha zilizopangwa kutumika ni shilingi 56,784,146,000 ambapo shilingi 45,788,352,000 ni za Mfuko wa Barabara na shilingi 10,995,794,000 ni fedha za kigeni.

 

Mchanganuo kamili wa Mpango wa Matengenezo ya Barabara Kuu na za Mikoa kwa mwaka 2004/05 ni kama unavyoonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 7 kilichoko ukurasa wa 77 hadi 88.

 

Mpango wa Ukarabati wa Barabara Kuu na za Mikoa kwa mwaka 2004/05

 

24.     Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi inakadiria kutumia jumla ya shilingi milioni 89,606.6 fedha za ndani na shilingi milioni 129,623.4 fedha za kigeni katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya upembuzi yakinifu, usanifu, ukarabati na ujenzi wa Barabara Kuu na za Mikoa. Kati ya fedha za ndani, shilingi milioni 5,087.6 ni fedha za Mfuko wa Barabara na shilingi milioni 84,519 ni fedha za Maendeleo kutoka Hazina.

 

25.     Mheshimiwa Spika, mgawanyo wa fedha za ndani kwa mwaka 2004/05 umezingatia mambo yafuatayo:

 

(i)                            Utekelezaji wa Mpango Maalum wa ujenzi wa barabara za Somanga-Lindi-Mingoyo na Dodoma-Manyoni-Singida kwa kutumia fedha za ndani. Jumla ya shilingi 49,950,000,000.00 fedha za hapa zimetengwa kwa mradi huu.

 

(ii)                          Kuelekeza mgawanyo wa rasilimali kwenye miradi ya Barabara Kuu na za Mikoa inayoendelea. Jumla ya shilingi zipatazo 29,334,000,000.00 fedha za hapa kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali na shilingi 5,087,600,000.00 kutoka Mfuko wa Barabara zimetengwa kwa miradi hii.

 

(iii)                        Kutenga rasilimali za kutosha kwenye miradi mipya yenye fedha za kigeni na miradi mipya ya upembuzi yakinifu na usanifu wa barabara mbalimbali zinazotarajiwa kujengwa. Jumla ya shilingi zipatazo milioni 5,235,000,000.00 fedha za ndani zimetengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hii.

Muhtasari wa Mpango wa Ujenzi/Ukarabati wa Barabara Kuu umeonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 5 kilichoko ukurasa wa 64 hadi 70 na ule wa Barabara za Mikoa katika Kiambatanisho Na. 6 kilichoko ukurasa wa 71 hadi 76.

USALAMA BARABARANI NA UDHIBITI WA UZITO WA MAGARI

26.     Mheshimiwa Spika, ajali za barabarani ni tatizo kubwa hapa nchini. Tathmini ya hasara zitokanazo na ajali za barabarani inaonyesha kuwa ajali huchangia hasara ya kati ya asilimia 1 na 2 katika pato la Taifa kwa mwaka. Wizara ya Ujenzi imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kupunguza ajali na uharibifu wa barabara. Hatua hizo ni pamoja na:-

·        Kuanzisha mfumo wa kisasa wa uwekaji wa takwimu za ajali kwenye Kompyuta ili kurahisisha upatikanaji na uchambuzi wa takwimu, kufahamu sehemu sugu za ajali na kuzifanyia utafiti na kuzirekebisha ili kuondoa vyanzo vya ajali. Mafunzo yametolewa kwa Askari wa usalama barabarani na Wahandisi kuhusu uwekaji na uchambuzi wa Takwimu za ajali kwa kutumia Kompyuta. Aidha, tafiti za vyanzo vya ajali zinaendelea kufanyika na kuchukua hatua za kuzuia ajali.

·        Kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TIE) iliyoko chini ya Wizara ya Elimu tumeandaa mitaala kwa ajili ya somo la elimu ya usalama barabarani katika Shule za Msingi, Sekondari na Vyuo vya Walimu nchini. Majaribio ya kufundisha somo hili katika baadhi ya Shule za Msingi na Sekondari katika mikoa ya Pwani, Dar es Salaam na Morogoro yanendelea. Aidha, tathimini ya somo hili inafanyika ili liweze kufundishwa katika shule nyingine.

·        Kufanya Utafiti na kupendekeza mifumo bora ya ukaguzi wa magari, shule za udereva na utoaji wa leseni za udereva.

·        Kutoa elimu ya usalama barabarani kwa njia ya redio, televisheni, magazeti, vipeperushi n.k. kwa watumiaji wa barabara wa aina zote.

·        Kudhibiti uzito wa magari makubwa katika barabara zetu kwa kutumia mizani pamoja na kuwaelemisha wasafirishaji kuhusu ufungaji wa mizigo na athari za uzidishaji uzito. Aidha, mzani mmoja unaohamishika umenunuliwa, Ujenzi wa Mizani ya Mwendakulima (Shinyanga) na Mikumi (Morogoro) umekamilika na Mzani wa Mikese (Morogoro) uko katika hatua za mwisho kukamilika.

·        Kuandaa mfumo wa usalama barabarani utakaozingatiwa katika kila hatua ya ujenzi wa barabara, yaani ‘Road Safety Audit System’.

·        Kuandaa rasimu za kanuni za barabara, miongozo ya uendeshaji magari na ya kufundishia wakaguzi wa magari.

·        Ili kuondoa tatizo la rushwa, Wizara kupitia Wakala wa Barabara imekuwa ikiwashirikisha wadau wote kuanzia wanaoagiza, wanaosafirisha mizigo, Mamlaka ya Bandari, Mamlaka ya Mapato (TRA) ili kuhakikisha kwamba mizigo inayoagizwa na kusafirishwa katika barabara zetu inakuwa katika viwango vinavyoruhusiwa na hivyo kupunguza mianya ya rushwa.

·        Kukamilisha Mpango Kabambe kuhusu masuala ya usalama barabarani (Road Safety Master Plan) mnamo Juni, 2004.

          Malengo ya Mwaka 2004/2005

 

27.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2004/2005 kazi zifuatazo zimepangwa kutekelezwa:

·                    Kuendelea kuwaelemisha Wananchi juu ya utumiaji salama wa barabara zetu kupitia vyombo mbalimbali vya habari.

·                    Kujenga mzani wa kisasa katika eneo la Mpemba (Tunduma) na kuanza maandalizi ya ujenzi wa mizani mingine maeneo ya Nangurukuru na Mingoyo mkoani Lindi na mwigine mkoani Dodoma. Mizani hii itajengwa sambamba na ujenzi wa barabara unaoendelea kati ya Nangurukuru – Mingoyo na Dodoma - Manyoni.

·                    Kuendelea kudhibiti uzito wa magari katika barabara zetu.

·                    Kuendelea kuendesha mafunzo ya uwekaji wa takwimu za ajali kwenye kompyuta na uchambuzi wake.

·                    Kuendelea na tathimini ya mpango wa kufundisha somo la elimu ya usalama barabarani katika Shule za Msingi na Sekondari.

MATUMIZI YA TEKNOLOJIA YA NGUVU KAZI KATIKA UJENZI NA MATENGENEZO YA BARABARA

 

28.     Mheshimiwa Spika, Nia ya Serikali ni kuondoa umaskini ifikapo mwaka 2025.  Katika kutekeleza azma hii, Wizara yangu imeweza kuwaongezea wananchi kipato kwa kuwapatia ajira za matengenezo ya barabara kwa kutumia nguvu kazi ambapo sio tu wanapata kipato, bali pia huboresha barabara zetu kwa kuzikarabati na kuzitengeneza.

Katika mwaka wa fedha wa 2003/04 Wizara yangu imeendelea kuratibu na kutoa miongozo ya matumizi ya teknolojia hii, kufuatilia utendaji na kutathmini ubora wa kazi katika miradi ya barabara. Aidha, Wizara imeendelea kukiwezesha Chuo chake cha “ Appropriate Technology Trainining Institute”(ATTI) - Mbeya kutoa mafunzo ya teknolojia sahihi ya nguvu kazi kwa kazi za barabara kwa mafundi wasimamizi wa kazi za barabara wapatao 85 kutoka Halmashauri za Wilaya mbalimbali nchini.

 

Katika kutoa umuhimu wa matumizi ya teknolojia hii, Wizara yangu kwa kushirikiana na TAMISEMI, imeandaa na kukamilisha Mwongozo wa Kitaifa wa kuratibu shughuli zote zinazohusiana na matumizi ya teknolojia ya nguvu kazi. Utekelezaji wa Mpango huu utaanza mwaka wa fedha wa 2004/05. Aidha, Wizara yangu kwa kushirikiana na Shirika la kazi Duniani (ILO) iliandaa na kuwa mwenyeji wa semina ya kimataifa ya wadau wa nguvu kazi (Labour Based Practitioners) ambayo iliwashirikisha washiriki 210 kutoka nchi mbalimbali 24 duniani.  Semina hii ilifanyika Arusha mnamo Mwezi Oktoba 2003 na ilitoa changamoto kubwa katika kuboresha na kudumisha matumizi ya nguvu kazi katika kazi za barabara.

 

29.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2004/05, Wizara yangu itatekeleza Mpango wa Kitaifa wa matumizi ya nguvukazi katika matengenezo ya barabara ambao utaratibu shughuli zote za matumizi ya teknolojia ya nguvu kazi katika kazi za barabara nchini kwa kuzingatia ushirikishwaji wa sekta binafsi. Vilevile, Wizara itakiendeleza na kukipatia nyenzo, miundo mbinu na vitendea kazi Chuo cha ATTI-Mbeya ili kiweze kujitegemea na kufanya kazi kwa ufanisi zaidi. Aidha, Wizara itaimarisha maktaba (Labour Based Documentation Centre) ambapo nyaraka mbalimbali za shughuli za teknolojia ya nguvu kazi na rejea mbalimbali zinazohusiana nayo zinahifadhiwa. Wizara itashiriki na kuratibu shughuli za utafiti kwa lengo la kutathimini ubora wa kazi za barabara zinazojengwa na kutunzwa kwa kutumia teknolojia hii.

 

USHIRIKISHWAJI WA WANAWAKE KATIKA KAZI ZA

BARABARA NCHINI

 

30.     Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kwa kipindi cha 2003/04 imeendelea kuhamasisha na kuelimisha wanawake na jamii kwa ujumla ili wanawake waweze kushiriki kwa wingi zaidi katika kazi za barabara.  Ushirikishwaji huu unatofautiana mkoa kwa mkoa kulingana na mila na desturi, jitihada za wataalam walioko kwenye mikoa za kuhamasisha na kushirikisha na uelewa wa jamii husika. Wizara yangu imeendelea kuchapisha na kusambaza kwa wadau makala mbalimbali kama vile vipeperushi na mabegi yenye ujumbe wa uhamasishaji wa kuelimisha jamii, wadau, vikundi vya wanawake na wanaume ili washiriki katika shughuli za sekta ya ujenzi. Aidha, Wizara imeendelea kufuatilia utekelezaji wa ushirikishwaji wa wanawake katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Morogoro, Kagera, Mtwara na Pwani na ukusanyaji wa takwimu katika maeneo ambayo yanatekeleza mpango huu. Vilevile, Wizara imeshirikiana na Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD) kuhamasisha shule zenye michepuo ya sayansi ili ziweze kuhamasisha wanafunzi wa kike kwenye shule zao kuyapenda masomo ya sayansi.  Walimu 50 kutoka shule mbalimbali wamepatiwa mafunzo, na wanawake wataalam 25 wamepatiwa mafunzo ya uongozi na mabadiliko katika uongozi na wengine 12 wamepatiwa mafunzo ya juu ya “computer”

31.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/05 Wizara imepanga:

·        Kuhamasisha na kuendeleza vikundi vya wanawake vinavyofanya kazi za barabara ili vifikie ngazi ya kujiandikisha daraja la VII la Ukandarasi wa nguvu kazi au zaidi, kuendelea kuhamasisha wanafunzi na walimu wa shule za sekondari zenye michepuo ya sayansi ili kuongeza idadi ya wataalam wanawake wa uhandisi na teknnolojia nyingine zinazohusiana na ujenzi,

·        Kuandaa makala mbalimbali zitakazotumika kuelimisha jamii, washika dau, vikundi mbalimbali katika sekta ya ujenzi kuhusu ushirikishwaji wanawake na faida zake,

·        Kufuatilia utekelezaji wa mpango wa ushirikishwaji wa wanawake katika kazi za barabara kwenye mikoa na miradi mbalimbali ya barabara,

·        Kutoa mafunzo na semina za masuala ya ushirikishwaji wanawake, uongozi na matengenezo ya barabara.

 

IDARA YA UGAVI NA HUDUMA

 

32.     Mheshimiwa Spika, Idara ya Ugavi na Huduma ina majukumu ya kusimamia Ununuzi, Utunzaji Usambazaji wa vifaa na upatikanaji wa huduma mbalimbali kwa ajili ya shughuli za Serikali (Procurement and Supply Management).  Aidha Idara ya Ugavi na Huduma inasimamia Taratibu za Ugomboaji na usafirishaji wa shehena za Serikali (Clearing and Forwarding Agent) pamoja na shughuli za uendeshaji wa Bohari Kuu ya Serikali.

 

Takwimu kutoka vyanzo mbali mbali zinaonyesha kwamba kati ya asilimia 60 hadi 70 ya matumizi ya Serikali hutumika katika ununuzi wa vifaa, kazi na huduma (Goods, Works and Services). Serikali pia hutumia fedha nyingi katika kugomboa shehena zake kutoka nje ya nchi zinazoletwa kupitia bandari, viwanja vya ndege na mipakani.

 

Malengo ya mwaka 2003/2004 na utekelezaji wake.

 

33.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2003/2004 Idara ilipanga kutekeleza yafuatayo:-

·                    Kuongeza utoaji na usambazaji wa vifaa na huduma kwa Wizara, Idara, Taasisi za Serikali na Bohari za Mikoa kufikia Shilingi bilioni 18.

 

·                    Kuimarisha uwezo wa kiutendaji wa Maafisa Ugavi katika shughuli za ununuzi na utunzaji wa vifaa vya Serikali kwa kuwapa mafunzo ya muda mrefu na mfupi.

 

·                    Kuongeza usimamizi wa ukaguzi wa vifaa na huduma kwa mikoa yote kwa kutembelea na kukagua vituo hivyo.

 

Utekelezaji wa malengo haya ni kama ifuatavyo:

·                    Hadi Mei 2004 bidhaa zenye thamani ya Shilingi bilioni 13.568 zimeuzwa kwa wateja,

·                    Wafanyakazi 28 walipelekwa kusoma Shahada ya juu ya Biashara inayohusu masuala ya Manunuzi. Aidha, wafanyakazi 37 walipelekwa kusomea kozi mbalimbali hapa nchini.

·                    Ukaguzi umefanyika Bohari 10 za Mikoa ya Tanga, Arusha, Moshi, Kigoma, Singida, Kagera, Mara, Shinyanga, Dodoma na Morogoro.

·                    Bohari za Mikoa ya Mara, Kigoma, Morogoro na Singida zimekarabatiwa.

 

Malengo ya Mwaka 2004/2005

 

34.            Mheshimiwa Spika, malengo ya mwaka 2004/05 ni:

·                    Kuongeza vitendea kazi kama magari na “computer” kwa ajili ya utunzaji wa kumbukumbu.

·                    Kuhakikisha kwamba taratibu zinaendelea kufanyika ili kukamilisha uanzishaji wa Wakala wa Bohari Kuu ya Serikali ifikapo Juni, 2006.

 

·                    Kuandaa orodha ya viwango vya vifaa ambavyo vinatumika Serikalini kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali.

 

·                    Kutoa mafunzo kwa Watumishi wa Ugavi Serikalini kuhusu sheria, kanuni na taratibu kama zilivyoainishwa na Sheria ya Ununuzi ya Umma Na. 3 ya mwaka 2001.

 

·                    Kuhakikisha kwamba Watumishi wa Ugavi Serikalini wanaendelea kupewa mafunzo ya muda mrefu na mfupi katika taaluma yao ili wafanye kazi zao kwa upeo mkubwa na ufanisi.

·                    Kuimarisha shughuli za Kitengo cha Wakala wa Ugomboaji na Usafirishaji wa Shehena za Serikali kwa kukiongezea vitendea kazi ili kiweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwa gharama nafuu.

 

·                    Kuongeza vitendea kazi ikiwa ni pamoja na kununua magari ya kusambaza vifaa mikoani.

 

IDARA YA UFUNDI NA UMEME

 

          Utekelezaji wa mwaka 2003/04

 

35.     Mheshimiwa Spika, Idara ya Ufundi na Umeme kwa kutumia vitengo vyake mbalimbali imeweza kutekeleza majukumu yake ya kuratibu, kutathmini, kusajili, kufuta, kukodisha na kufanya matengenezo ya magari na mitambo ya Serikali, uendeshaji wa Vivuko na Mitambo ya kusaga mawe, ushauri, usimamizi wa miradi, usimikaji na matengenezo ya mitambo ya umeme, mabarafu, viyoyozi na vifaa vya Electoniki. Aidha, Idara imeendelea na zoezi la kusajili magari, mitambo na pikipiki za Serikali kwa kwa namba za Serikali kama nilivyokwishaeleza katika aya ya 21 kipengere cha (vi).

 

Katika kuboresha huduma kwa Wananchi, Wizara   yangu katika mwaka 2003/04 imenunua kivuko kimoja cha Bugolora-Ukerewe mkoani Mwanza kwa Shilingi 1,000,000,000 kitakachofanya kazi kati ya Mwanza na Ukerewe, na hivyo kupunguza kero kubwa iliyokuwa inawakabili wananchi wa maeneo hayo.

 

Pia, mkataba wa ununuzi wa Boti mbili (2) za uokoaji umesainiwa na boti hizo zinategemewa kupatikana mwishoni mwa mwezi Agosti, 2004 na zitatumika katika kivuko cha Magogoni Dar es Salaam na Kigongo – Busisi Mkoani Mwanza. Pia zimenunuliwa “Life Jackets” 345 kwa ajili ya matumizi ya mikoa ya Mwanza na Dar es Salaam.

 

Magari 5 yamenunuliwa kwa ajili ya kuimarisha karakana katika Mikoa ya Dodoma, Kigoma, Mtwara, Manyara na Ruvuma. Aidha, katika kuimarisha kitengo cha ukodishaji wa magari ya Serikali (G.T.A.) magari mawili aina ya Mercedes Benz yamenunuliwa.

 

Pia, Idara imeendelea kutoa ushauri kuhusu utekelezaji wa miradi ya umeme. Miradi 17 kati ya 58 imekamilika na iliyobaki 41 inaendelea. Jumla ya Shilingi 110,000,000 zimepatikana.

 

36.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2004/05, malengo yafuatayo yamepangwa:

·                    Kununua kivuko kipya cha Kigongo - Busisi mkoani Mwanza,

·                    Kununua kivuko kilichokuwa kinamilikiwa na TAMOFA katika mto Ruvuma eneo la Kilambo- Mtwara.

·                    Kununua “Vending Machine” ya kukatia tiketi katika Kivuko cha Magogoni kwa lengo la kuongeza ufanisi na kuimarisha ukusanyaji wa mapato.

·                    Kukarabati vivuko vya Mv. Kigamboni, Mv. Rufiji, Mv. Sengerema, Mv. Pangani, Mv. Kilombero na kile cha Kyanyabasa kilichopo Mkoani Kagera.

·                    Kubadilisha mfumo wa uendeshaji kutoka uvutaji wa kamba unaofanywa na watu na badala yake kutumia winchi katika kivuko cha mto Ruhuhu Mkoa wa Ruvuma.

·                    Kununua Boti 2 za uokoaji, magari 3 (4WD) na Vifaa vya karakana (Workshop tools).

 

37.     Mheshimiwa Spika, taratibu za kuifanya Idara ya Ufundi na Umeme kuwa Wakala utakaojulikana kama “Tanzania Electrical, Mechanical and Electronics Services Agency” (TEMESA), zinaendelea na utekelezaji wake umefikia asilimia 60. Inatarajiwa kuwa, Wakala utaanza kufanya kazi rasmi mwezi Januari 2005.

 

BODI YA MFUKO WA BARABARA (RFB)

 

38.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2003/2004 Bodi ya Mfuko wa Barabara imezidi kujiimarisha kwa kuongeza ufanisi katika ukusanyaji na usimamizi wa fedha za Mfuko wa Barabara. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika mwaka wa fedha 2003/2004 Bodi ilitarajia kukusanya shilingi milioni 64,510 kwa ajili ya kazi za barabara. Hadi Mei 2004, shilingi milioni 61,616 (96%) ya lengo, zilikuwa zimekusanywa.  Kati ya kiasi hicho Bodi ilipokea na kugawa jumla ya shilingi milioni 57,675 kama ifuatavyo: TANROADS shilingi milioni 39,946, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa shilingi milioni 17,117, Wizara ya Ujenzi shilingi milioni 3,944 na shilingi milioni 618 kwa ajili ya uendeshaji wa Mfuko.  Mwelekeo unaonyesha kwamba, ifikapo mwishoni mwa mwezi Juni 2004 Bodi ya Mfuko itafikisha lengo lake la kukusanya shilingi 64,510 milioni.

 

Aidha, Bodi imeshiriki katika semina mbalimbali zinazoendeshwa na Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB) na TAMISEMI kwa Watendaji wa Halmashauri na Makandarasi ili kutumia nafasi hiyo katika kuwaelimisha washiriki umuhimu wa matumizi bora ya fedha za Mfuko.  Bodi ya Mfuko itaendeleza juhudi hizi katika mwaka ujao wa fedha.

 

Vilevile, Bodi kwa kutumia ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali, imeendelea kufanya ukaguzi wa kawaida pamoja na ukaguzi maalum wa kuhakiki mapato yake kutoka kwa wakala wa ukusanyaji.

 

Katika juhudi za kuongeza mapato ya Mfuko, Bodi imeandaa mapendekezo ya kuongeza vyanzo vya mapato ambayo yanafanyiwa kazi na Serikali. Bodi imeweza pia kutoa mafunzo ya usimamizi wa Mfuko kwa watumishi na wajumbe wa Bodi.  Pia Bodi imechapisha Kijarida kinachotoa mwongozo juu ya matumizi ya fedha za Mfuko ambacho kimegawiwa kwa wadau mbalimbali.

 

39.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/2005 Serikali inategemea kukusanya jumla ya shilingi 71,443 milioni kwa ajili ya Mfuko wa Barabara. Kati ya fedha hizi shilingi 50.01 milioni (70%) zitapelekwa Wizara ya Ujenzi na shilingi 21.433 milioni (30%) zitapelekwa TAMISEMI.

 

Aidha mfuko unatarajia kupata kiasi cha shilingi 8,000 milioni kutoka Jumuia ya Ulaya ikiwa ni msaada kwa ajili ya matengenezo ya barabara katika mwaka wa fedha wa 2004/2005. Katika fedha hizi, Wizara ya Ujenzi itapata Shilingi bilioni 5.6 na TAMISEMI Shilingi bilioni 2.4. 

 

40.     Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2004/05, Bodi ya Mfuko wa Barabara inategemea kuendelea kuboresha makubaliano ya utendaji (Performance Agreements) na taasisi zinazotekeleza kazi za barabara na kutoa ushauri wa kuboresha utendaji kwa kuzingatia uzoefu wa nchi nyingine ili kuhakikisha kwamba ubora wa kazi unalingana na fedha zinazotolewa. Aidha, Bodi kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, itaendelea kuimarisha ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya Mfuko kutoka vyanzo mbalimbali na kusimamia vizuri matumizi ya fedha hizo kwa kuimarisha ukaguzi wa ubora wa kazi na Fedha.

 

Katika kufanikisha malengo na majukumu yake, Bodi itaandaa Mpango wa muda mrefu (Strategic Plan) uwe dira ya kuiongoza na katika kuongeza ufanisi wa utunzaji wa kumbukumbu za fedha na itaanza kutumia mfumo mpya wa kompyuta wa kudhibiti matumizi ya fedha (Computerized Financial Management System).

 

WAKALA WA BARABARA (TANROADS)

 

41.     Mheshimiwa Spika, Wakala wa Barabara una miaka minne tangu ulipoanzishwa. Katika kipindi hicho, umeendelea kutekeleza vizuri majukumu yake ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya Barabara Kuu na za Mikoa zenye jumla ya kilometa 35,000. Aidha muundo wa TANROADS umepitishwa rasmi na ofisi za kanda sasa zimeondolewa Mikoani na zimehamishiwa Makao Makuu ya Wakala. Katika kipindi hiki cha miaka minne Wakala umefanikiwa kuweka mifumo ya kisasa ya menejimenti na mawasiliano Makao Makuu na Ofisi zote za mikoa.

 

42.     Mheshimiwa Spika, kutokana na kuimarika kwa Wakala na ukweli kwamba fedha za matengenezo zimekuwa zinapatikana kwa wakati na kwa kiasi kilichopangwa, Wakala umejitahidi kuongeza ufanisi na kuongeza uzuri wa hali ya barabara zetu.

 

43.     Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kupitia TANROADS itaendelea kutunza barabara zetu kwa kusisitiza pamoja na mambo mengine masuala yafuatayo:

 

·                    Samani za barabara

Wenye magari wanatakiwa kuwa waangalifu ili wasizigonge alama za barabarani. Baadhi ya wananchi wamekuwa waking’oa alama na samani nyingine za barabara. Ukosefu wa alama na samani unachangia kuwepo kwa ajali. Wananchi wanaombwa kulinda na kutunza alama za barabarani.

 

·                    Usalama barabarani

Mwendo wa kasi ni kichocheo kikubwa cha ajali. Madereva na wenye magari wanatahadharishwa kuhusu jambo hili. Pamoja na kuhakikisha kunakuwepo na alama za tahadhari barabarani, ukaguzi wa mwendo wa magari na ubora wa magari vitafanyika mara kwa mara.

 

·              Uzito wa magari

Shughuli ya upimaji wa uzito wa magari itaendelea kuboreshwa ili kuhakikisha magari yanazingatia sheria na taratibu zilizowekwa.

 

·              Hifadhi ya barabara (Road Reserve)

Wananchi wanaojenga au wanaofanyia shughuli zao kando ya barabara katika eneo la mita 22.5 kila upande wa Barabara Kuu na zile za Mikoa, wanatakiwa kuzingatia sheria ya barabara inayowataka kuheshimu eneo hilo na kuliacha wazi. Serikali itaendelea kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa hifadhi ya barabara, jukumu lao la kutunza barabara na itaendelea kuwachukulia hatua kali ikiwa ni pamoja na kubomoa au kuwaondoa wote walio katika eneo la hifadhi ya barabara pindi maeneo hayo yatakapohitajika kwa miradi ya barabara.

 

·                    Waheshimiwa Wabunge, Viongozi wa Mikoa na Wilaya wanaombwa kutoa ushirikiano kwa Wizara/Wakala kwa kutoa ushauri na kujadili kwa makini taarifa za matengenezo na matumizi ya fedha wakati wa vikao vya Bodi za Barabara.

 

Aidha, ni vema ieleweke kwamba kazi nyingi za matengenezo zinafanywa na makandarasi wazalendo hivyo zinachangia kutoa ajira kwa wananchi walio wengi na hivyo kuboresha hali zao za maisha.

 

WAKALA WA MAJENGO YA SERIKALI (TBA)

 

44.     Mheshimiwa Spika, Wakala wa Majengo ya Serikali (TBA) umeanzishwa chini ya Sheria Na 30 ya mwaka 1997 ya Wakala wa Serikali na kuzinduliwa rasmi mwezi Mei, 2002. Madhumuni ya kuanzishwa Wakala huu ni pamoja na kuweka utaratibu na kanuni zitakazowawezesha wafanyakazi wa Serikali kumudu kugharamia makazi bora wakiwa bado kazini na baada ya kustaafu.

 

Kwa kuzingatia hayo, majukumu ya Wakala ni kama ifuatavyo:

·        Kujenga majengo ya Serikali kwa viwango vinavyotakiwa na kuyatunza.

·        Kutoa ushauri wa kitaalam na kusimamia miradi ya ujenzi wa nyumba na majengo ya Serikali.

·        Kuuza nyumba za serikali kwa kuwakopesha wafanyakazi wa ngazi zote ili waweze kuzimiliki kabla ya kustaafu

·        Kuendelea kujenga nyumba mpya na kuwauzia wafanyakazi.

 

 

Mapitio ya Utekelezaji wa 2003/04

 

45.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2003/04, Wakala ulipanga kufanya kazi zifuatazo:

·                    Kuzifanyia matengenezo nyumba za Serikali 262 katika mikoa yote ya Tanzania Bara.

·                    Kuuza pamoja na kujenga nyumba 500 za gharama nafuu.

·                    Kufanya kazi za ushauri zitakazoingiza kiasi cha Shilingi 372,086,700

 

Hadi Aprili, 2004, jumla ya nyumba 177 zimefanyiwa matengenezo katika mikoa mbalimbali. Aidha, Wakala umeanza ujenzi wa nyumba 300 kwa ajili ya viongozi wa Serikali katika Manispaa ya Dodoma na zabuni ya ujenzi wa nyumba 10 za gharama nafuu mjini Babati Mkoani Manyara zimeshatangazwa. Jumla ya nyumba 5,248 zimeuzwa kwa watumishi wa Umma hadi sasa na kiasi cha fedha kilichokusanya kutokana na mauzo ya nyumba kwa mwaka 2003/04 hadi kufikia mwezi Mei 2004 ni Shilingi 3,511,318,753.

 

Malengo ya mwaka 2004/05

 

46.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2004/05 Wakala umepanga kukusanya jumla ya shilingi 9,284,134,361 kutokana na mauzo ya nyumba kwa watumishi wa Serikali, upangishaji wa nyumba za kibiashara, huduma za ushauri na ruzuku kutoka Serikalini kwa ajili ya kulipia mishahara ya watumishi. Mapato haya yataelekezwa kwanza katika kukamilisha nyumba 300, ambazo ujenzi wake unaendelea pamoja na kujenga nyumba nyingine. Aidha, Wakala utaendelea na matengenezo ya kawaida ya nyumba za Serikali.

BODI YA USAJILI WA MAKANDARASI (CRB)

 

47.     Mheshimiwa Spika, Bodi ya Usajili wa Makandarasi (Contractors Registration Board) ilianzishwa kwa sheria ya Bunge Namba 17 ya mwaka 1997, na kupewa majukumu yafuatayo:

(i)                Kusajili makandarasi wa aina zote

(ii)              Kuratibu shughuli na mwenendo wa makandarasi wote, na

(iii)            Kujenga uwezo wa makandarasi wa Kitanzania.

 

Bodi imetayarisha Dira ya Miaka Mitano ya 2004-08 kwa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi. Dira hii inalenga katika maeneo makuu sita ambayo ni:

·                    Kuboresha uwezo, ujuzi na maadili ya Makandarasi

·                    Kuhakikisha kwamba makandarasi wa kizalendo wanatumika ndani na nje ya nchi.

·                    Kuongeza ubora wa kazi za ujenzi

·                    Kuhakikisha kwamba afya na usalama kazini unazingatiwa

·                    Kuongeza ufanisi wa shughuli za Bodi

 

48.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa 2003/04, Bodi imepata mafanikio yafuatayo:

(i)                Kusajili jumla ya makandarasi 968. Hii inafanya jumla ya makandarasi waliosajiliwa hadi Mei, 2004 kuwa 3,094.

(ii)              Bodi imefuta usajili wa makandarasi 135 mwezi Januari 2004 kwa kushindwa kutimiza masharti ya Sheria ya Usajili wa Makandarasi Na. 17 ya 1997 ikiwa ni pamoja na utendaji mbaya wa kazi. Hii imefanya jumla ya makandarasi waliofutwa tangu mwaka 1999 kufikia 1,448.

(iii)            Bodi imefanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi 946 katika kipindi cha 1999 – Mei 2004. Kati ya hiyo, miradi 414 ilikuwa na mapungufu mbali mbali ya uvunjaji wa sheria ambapo wahusika walichukuliwa hatua za kisheria. Hadi Mei, 2004 jumla ya kesi 25 zipo Polisi na kati ya hizo kesi 15 ziko mahakamani.

(iv)            Hadi Mei, 2004, Bodi imeshaendesha kozi 12 chini ya Mpango Endelevu wa Mafunzo ya Makandarasi (Sustainable Structured Training Program) ambapo Makandarasi 300 walihudhuria. Tangu Mpango huu uzinduliwe mwaka 2001, jumla ya kozi 29 zimeshaendeshwa na kuhudhuriwa na makandarasi 900.

(v)              Mfuko wa kusaidia Makandarasi (Contractors Assistance Fund) umeboreshwa kwa kuongeza fedha na sasa Mfuko huo una zaidi ya Shilingi milioni 600. Aidha, wanachama wa mfuko huo maalum wa kusaidia makandarasi kupata dhamana za malipo ya awali (Advance Payment Guarantee) na dhamana za zabuni (Bid Bond), waliongezeka hadi kufikia 251. Hadi Mei, 2004 jumla ya wanachama 198 wa Mfuko huo walikuwa wamefaidika. Mfuko unalenga kuwasaidia makandarasi wadogowadogo wazalendo.

(vi)            Bodi ilifanya marekebisho ya sheria yake ndogo ili kuboresha mazingira katika sekta hii, na kutoa uwezo zaidi wa kuendeleza makandarasi wazalendo. Mabadiliko haya yanahusu: -

 

§        Kuongeza thamani ya viwango vya juu vya kazi katika kila daraja la Ukandarasi kwa kuzingatia thamani ya fedha za Tanzania katika soko la dunia.

§        Kuweka sifa za chini (minimum qualifications) za nafasi ya Mkurugenzi Mmiliki wa kampuni ya Ukandarasi ili kuhakikisha kwamba biashara ya ukandarasi inafanywa na wenye fani zinazotakiwa.

§        Ili kuongeza nafasi za kazi kwa makandarasi wazalendo, Bodi imesajili Makandarasi wageni katika daraja la kwanza peke yake ili kuhakikisha kwamba ni wageni wenye uwezo mkubwa tu ndio wanaoruhusiwa kufanya kazi Tanzania. Aidha Bodi imeweka utaratibu wa Makandarasi kusajili miradi na kupata nembo maalum kwa kila mradi wanaotekeleza ili kuondoa udanganyifu wa watu kununua majina ya makandarasi waliosajiliwa na kufanya kazi kinyume cha sheria. Vilevile hatua hii inalenga katika kuiwezesha Bodi kudhibiti ukiukwaji wa viwango vya kazi kwa kila daraja na kukusanya takwimu zinazotakiwa katika Sekta ya Ujenzi.

 

49.     Mheshimiwa Spika, matatizo makubwa yanayowakabili makandarasi nchini ni pamoja na : -

·        Mitaji midogo na masharti magumu ya kupata mikopo ya kufanyia kazi kutoka mabenki na taasisi zingine za fedha.

·        Udhaifu wa uendeshaji na usimamizi wa miradi miongoni mwa makandarasi.

·        Ukosefu wa vifaa na mitambo ya ujenzi kwa makandarasi wenyewe, hii ni pamoja na kutokuwa na uwezo wa kuimiliki, bei kubwa za kukodisha mitambo na uchache wa sehemu za kuikodisha.

 

50.     Mheshimiwa Spika, malengo ya mwaka 2004/05 ni pamoja na haya yafuatayo:

·        Kuendelea na zoezi la kusajili makandarasi wa ngazi zote

·        Kuendelea kusimamia Mfuko wa Kusaidia Makandarasi nchini

·        Kutoa mafunzo chini ya Mpango Endelevu wa Mafunzo ya Makandarasi (Sustainable Structured Training Program)

·        Kufanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi katika sehemu mbali mbali

·        Kuendelea na zoezi la usimamizi wa Sheria ya usajili wa makandarasi

 

BODI YA TAIFA YA USIMAMIZI WA VIFAA (NBMM)

 

51.     Mheshimiwa Spika, Bodi ya Taifa ya Usimamizi wa Vifaa (National Board for Materials Management – NBMM) ni Taasisi ya Serikali iliyoanzishwa mwaka 1981 kwa Sheria ya Bunge Na. 9.  Bodi ina majukumu ya kusimamia, kuratibu na kuendeleza fani ya Ununuzi na Ugavi. Bodi pia huendesha mitihani, kudhibiti mienendo ya wanataaluma na kusajili wataalamu.

 

Katika mwaka wa fedha wa 2003/04 Bodi imetekeleza yafuatayo:

·                    Imesajili wataalamu 112 hivyo kufanya idadi ya wataalamu waliosajiliwa kufikia 1,609.

·                    Imetahini Wanataaluma 1,967 kwenye ngazi mbalimbali

·                    Bodi imeweza kutembelea na kukagua sehemu za kazi mkoani Dodoma na kubaini watendaji wasio na sifa. Wafanyakazi 11 tu kati ya waliokaguliwa 58 ndio waliokuwa wamesajiliwa na kutambulika kisheria.

·                    Mafunzo endelevu (Continued Professional Development) yameendelea kutolewa ambapo warsha na semina 24 ziliendeshwa kwa watendaji wa ngazi zote za Serikali Kuu, Wilaya, Miji, Manispaa n.k. Mafunzo haya, yalihusu pia sheria ya Manunuzi ya Umma.

·                    Utaratibu wa kutoa mafunzo kwa vitendo (Internship) yameanzishwa kwa wanataaluma wanaotoka vyuoni ili wapate uzoefu katika kazi.

·                    Bodi ikishirikiana na Crown Agents – UK iliendesha semina ya uhamasishaji kwenye Sheria Na.3 ya Ununuzi. Lengo la semina lilikuwa ni kuboresha mbinu za ufundishaji, uandaaji machapisho ya masomo (manuals) na pia utoaji wa mafunzo ya muda mfupi na mrefu.

·                    Mafunzo mengine yaliyotolewa ni pamoja na namna ya kupambana na janga la UKIMWI, kuondoa kero za rushwa na kudumisha maadili ya kazi.

·                    Katika kuboresha mfumo wa mafunzo, Bodi imebadili mitaala ili ikidhi mabadiliko yanayoletwa na ukuaji wa utaalamu ulimwenguni, teknolojia na sheria za ununuzi.

·                    Bodi imetoa ushauri wa kitaalamu kwenye Serikali na Asasi zake, pia imeandaa miongozo ya kazi (operations manuals), mfumo wa kazi na utunzaji wa kumbukumbu kwenye shughuli za ununuzi na ugavi.

 

52.     Mheshimiwa Spika, Baadhi ya matatizo ambayo Bodi inakumbana nayo katika utekelezaji ni pamoja na:

·        Upungufu wa vitendea kazi, nyenzo muhimu za kufanyia kazi na usafiri.

·        Uhaba wa fedha za kutoa elimu kwa vitendo. 

·        Waajiri wengi kushindwa kuajiri wanataaluma wanaotoka vyuoni moja kwa moja kwa kuwa hawana uzoefu kazini kutokana na ama kutojua sheria ama kuidharau na kufanya utekelezaji kuwa mgumu hasa kuhusu suala la kuajiri wataalamu wasio na sifa. Ili kukabiliana na tatizo hili, Bodi itaendelea kutoa elimu kwa umma kuhusiana na Sheria Na.9 na hali hii itaondoa tatizo la uvamizi kwenye fani na pia kuongeza ajira kwa wahitimu wenye sifa.

 

53.     Mheshimiwa Spika, malengo ya Bodi kwa mwaka wa fedha 2004/2005 ni pamoja na:

·                    Kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria Na. 9 ya 1981.

·                    Kuongeza idadi na kiwango cha wanaofaulu mitihani toka wastani wa asilimia 39.5 ya sasa hadi kufikia asilimia 50,

·                    Kuboresha uwezo wa maktaba na kupata wakufunzi wenye upeo mkubwa zaidi na kuboresha mafunzo kwa wakufunzi.

·                    Kufungua vituo vya kutahini katika mikoa ambayo huduma za Bodi hazijafika.

·                    Kuimarisha usimamizi wa sheria Na.9 ili waajiri wengi waweze kuitii sheria na kupata fursa ya kutumia wataalamu waliopo ipasavyo.

·                    Bodi itatoa huduma zaidi kwa njia ya warsha, semina na ushauri wa kitaalamu kama mbinu mbadala ya kuongeza kipato.

·                    Bodi itaendelea kushirikiana na taasisi nyingine zikiwemo Bodi za kitaaluma na vyuo mbalimbali ili kuweza kupata ufumbuzi wa matizo yanayoathiri ukuaji wa taaluma. Kwa kushirikiana na vyombo husika, itakamilisha muswada wa marekebisho ya Sheria Na.9 na kuuwakilisha Bungeni. 

·                    Katika kuleta ufanisi zaidi na kukuza uwezo wao kitaaluma, Bodi itaendelea kuwapatia wafanyakazi mafunzo ya muda mrefu na mfupi.

 

BODI YA USAJILI WA WAHANDISI (ERB)

 

54.     Mheshimiwa Spika, Bodi ya usajili ya wahandisi ilianzishwa na Serikali kwa sheria Na. 15 ya mwaka 1997 na imepewa madaraka ya kusimamia mienendo na shughuli za kihandisi zinazofanywa na wahandisi pamoja na kampuni za ushauri wa kihandisi.

Jukumu kubwa la bodi ni kulinda masilahi ya taifa na watumiaji wa huduma za kihandisi kwa kuhakikisha kuwa shughuli zote za kihandisi zinafanywa na wahandisi waliosajiliwa au na makampuni ya ushauri wa kihandisi yaliyosajiliwa kwa kuzingatia viwango na maadili ya kihandisi ili kuhakikisha usalama wa maisha, mali na mazingira. Katika kutekeleza jukumu hili, bodi inafanya yafuatayo:

·                    Kusajili wahandisi pamoja na makampuni yanayotoa ushauri wa kihandisi,

·                    Kupitia na kutoa maamuzi juu ya maombi ya kusajiliwa,

·                    Kuwaendeleza wahandisi kitaaluma, ikiwa pamoja na kusimamia programu ya mafunzo kwa wahandisi wahitimu (internship),

·                    Kuratibu mienendo na shughuli za kihandisi za wahandisi na makampuni ya ushauri wa kihandisi,

·                    Kujenga uwezo (capacity building) wa wahandisi na makampuni ya ushauri wa kihandisi, na

·                    Kuandaa machapisho mbalimbali yanayohusu shughuli za Bodi.

 

Mafanikio na Matatizo katika mwaka wa fedha 2003/04.

 

55.     Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Mei, 2004 Bodi imefanikiwa kutekeleza yafuatayo:

 

·                    Kusajili Wahandisi – 909 ikiwa ni asilimia 152 ya lengo la mwaka

·                    Kusajili Kampuni za Ushauri – 9, ikiwa ni asilimia 81.8 ya lengo la mwaka.

·                    Ziara za kanda – 4 zimefanyika ikiwa ni asilimia 57.1 ya lengo la mwaka.

·                    Kuendesha mihadhara 4 ikiwa ni asilimia 66.7 ya lengo la mwaka,

·                    Kuendesha kozi fupifupi – 4 ikiwa ni asilimia 200 ya lengo la mwaka.

·                    Kuandaa na kuendesha mtihani wa kitaaluma –1 ikiwa ni asilimia 50 ya lengo la mwaka.

·                    Kuendesha na kusimamia mafunzo kwa vitendo kwa wahandisi - 250 ikiwa ni asilimia 48 ya lengo la mwaka.

·                    Kuratibu Siku ya Wahandisi – 1 ikiwa ni asilimia 100 ya lengo la mwaka.

 

56.     Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio haya, Bodi ilikabiliwa na changamoto zifuatazo:

·                    Ufinyu wa Bajeti:  Shughuli za Bodi zimepanuka hivyo ada kama chanzo pekee cha mapato haiwezi kukidhi shughuli zote.  Tatizo hili limesababisha kuahirishwa au kufutwa utekelezaji wa baadhi ya mipango yake.

·                    Ukosefu wa ajira kwa wahandisi wahitimu. Wahandisi wahitimu wazalendo hukosa ajira kwa kutokuwa na uzoefu wa kufanya kazi na hivyo kusababisha waajiri kuajiri wahandisi wa kigeni.  Hata hivyo, tatizo hili linatazamiwa kupungua baada ya kuanzishwa kwa utaratibu wa mafunzo ya vitendo kwa wahandisi wahitimu.

·                    Idadi ndogo ya kampuni za Ushauri wa kihandisi mikoani.

 

Ni azma ya Bodi kuendelea kuyatafutia ufumbuzi matatizo haya ili kuimarisha ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake.

 

Malengo ya Mwaka wa Fedha wa 2004/2005

 

57.     Mheshimiwa Spika, Malengo ya mwaka wa fedha 2004/05 ni kutekeleza kazi zifuatazo:

·                    Usajili wa Wahandisi - 1,030

·                    Usajili wa Kampuni za Ushauri wa Kihandisi - 15

·                    Kufanya ukaguzi mikoani kwa kutembelea kanda 5 zenye mikoa 16.

·                    Kuandaa mihadhara ya kitaalamu

·                    Mafunzo ya vitendo kwa Wahandisi wahitimu na kozi fupi

·                    Kuratibu Siku ya Wahandisi

·                    Mtihani wa Kitaaluma

·                    Kushughulikia uanzishwaji wa Kampuni za Ushauri wa Kihandisi mikoani ili kusogeza huduma hii karibu na watumiaji

·                    Kukamilisha maandalizi ya programu ya mafunzo ya kujiendeleza kwa wahandisi.

 

58.     Mheshimiwa Spika, nafurahi kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Bodi imeanzisha utaratibu wa kusherehekea – Annual Engineers’ Day. Siku hii maalum ina lengo la kuwatambua wahandisi na makampuni ya kihandisi yaliyotoa michango mikubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini na kuwahamasisha Wahandisi kuwa wabunifu na hivyo kuharakisha maendeleo ya taifa.  Sherehe kama hizi zitakuwa zinafanyika kila mwaka.

 

BODI YA WABUNIFU MAJENGO NA WAKADIRIAJI MAJENZI (AQSRB)

 

59.     Mheshimiwa Spika, Bodi ya Usajili wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi ilianzishwa kwa Sheria Na. 16 ya mwaka 1997. Majukumu makubwa ya Bodi ni pamoja na: -

·                    Kusajili, kusimamia, kuangalia na kuratibu mwenendo wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi na kampuni za kitaalamu na za ushauri zinazohusiana na kuhusika na fani hizo. Lengo la Bodi ni kuhakikisha kuwa wataalam hawa, wanatoa huduma za kitaalamu zinazokidhi mahitaji ya wananchi na mazingira yao.

·                    Kulinda utaalamu (Professionalism).

·                    Kuhamasisha umma na wataalamu, kushirikiana na wadau wengine kama vile Bodi mbalimbali chini ya Wizara.

 

Katika mwaka wa fedha 2003 /2004, Bodi ilifanikisha kutekeleza yafuatayo:

·                    Kusajili Wabunifu na Wakadiriaji Majenzi wa ndani 22 na wa nje 5. Aidha, Bodi ilisajili kampuni za ndani 9 na za nje 2 na kufikisha jumla ya wataalam wa ndani na nje waliosajiliwa tangu Bodi ianze kuwa 293 na kampuni za ndani na za nje kuwa 123.

·                    Kutembelea na kukagua sehemu za majenzi katika mikoa 12 ya Tanzania. Sehemu 182 za majenzi zilikaguliwa na kufikisha jumla ya sehemu za majenzi zilizokaguliwa tangu Bodi kuanza kufanya kazi hiyo kufikia 1,841.

·                    Kukamilisha Mapendekezo ya Marekebisho ya Sheria Na. 16 ya mwaka 1997

·                    Kuandaa na kuendesha makongamano mawili ya taaluma hizi mbili katika kuwanoa wana taaluma chini ya Mpango wa Taaluma ya Elimu Endelevu (Continued Professional Development).

·                    Kutayarisha na kutahini wana taaluma wanaoomba kusajiliwa na Bodi.

·                    Katika kuhakikisha Sheria Na. 16 ya 1997 na sheria ndogondogo GN No.168/2000 za Bodi zinafuatwa, Bodi iliweza kutoa adhabu, maonyo na kuwapeleka mahakamani wale walioonekana kukaidi sheria.

·                    Kukamilisha matayarisho ya Rasimu ya Sheria ya Taifa ya Majengo- (National Building Control Act) kwa kuwashirikisha wadau. Mapendekezo yake yaliwasilishwa kwenye vyombo vya juu kwa hatua zaidi.

·                    Kuzindua Mpango wa Mihadhara ya Kitaaluma yenye lengo la kutambua michango ya wana taaluma wa Ubunifu Majengo na Ukadiriaji Majenzi, kuhamasisha kizazi kipya kujiunga na fani hizi mbili na kubadilishana uzoefu.

·                    Kutayarisha na kuwasilisha kwenye vyombo husika taarifa ya utendaji ya mwaka 2002 kwa mujibu wa sheria Na. 16 ya 1997.

·                    Kutayarisha “Standard Documents” kwa ajili ya kurahisisha usimamiaji wa Sheria Na. 16ya mwaka 1997 na Sheria ndogondogo namba 168 ya 2000 kwenye sehemu za majenzi.

·                    Kuhusu mitihani ya Bodi, maombi 76 ya wataalamu yalipokelewa. Wataalam 57 waliotimiza masharti waliruhusiwa kufanya mitihani na kati ya hao 17 walifaulu na 11 walisajiliwa na Bodi. Aidha wataalam 4 na kampuni 3 za Ubunifu Majengo na Ukadiriaji Majenzi zilifutiwa usajili kwa kukiuka Sheria Na.16 ya 1997 na kufanya jumla ya wataalam waliofutiwa usajili tangu Bodi ianze kuwa 272 na makampuni 8.

 

60.     Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio haya Bodi ilikabiliana na changamoto zifuatazo: -

·        Upungufu wa fedha uliathiri kwa kiwango kikubwa utekelezaji wa malengo yaliwekwa na Bodi

·        Kutojitokeza kwa wana taaluma wa sifa za kati kutahiniwa kwa ajili ya usajili kunashusha idadi ya watahiniwa na hivyo kuathiri mpango wa usajili.

·        Mapato ni kidogo, hayakidhi mahitaji ya Bodi.  Kwa hiyo Bodi inakabiliwa na matatizo ya upatikanaji wa vitendea kazi, utekelezaji wa mipango mizuri, kutoa elimu kwa umma n.k. Hii inatokana na kutokuwa na vyanzo vya kutosha vya mapato.

 

61.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2004/2005, Bodi inatarajia kutekeleza yafuatayo:

·        Kusajili wataalam 50

·        Kuimarisha taratibu za usajili,

·        Kuimarisha sera na mfumo wa sheria wa Bodi.

·        Kuendelea na ukaguzi wa sehemu za majenzi katika mikoa yenye shughuli nyingi za ujenzi ikiwemo Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, Iringa, Mbeya, Mwanza, Shinyanga, Arusha, Kilimanjaro na Tanga.

·        Bodi inaandaa mafunzo maalum ya vitendo kwa ajili ya kuwasaidia wahitimu wa taaluma husika ili waweze kutimiza masharti ya kuweza kusajiliwa kwa mujibu wa sheria.

·        Vilevile, Bodi itaendelea kupiga vita rushwa kwa kuwaelimisha wataalam wake kuhusu kufuata sheria na imetayarisha “practice note” itakayowataka watekelezaji miradi yenye maslahi kitaifa km. hospitali, shule, nyumba za wageni, hoteli, nyumba za kupangisha na maofisi kuwatumia wataalam waliosajiliwa na wasimike mabango yanayoonyesha hivyo.

 

BARAZA LA TAIFA LA UJENZI (NCC)

 

62.     Mheshimiwa Spika, Baraza la Taifa la Ujenzi limeanzishwa kwa Sheria ya Bunge Na. 20 ya mwaka 1979. Majukumu makuu ya Baraza ni pamoja na:

·                    Kusimamia na kuratibu maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini na kushauri kuhusu Sera, Mipango na mikakati ya kukuza sekta,

·                    Kutoa ushauri wa kiufundi (“technical audit”),

·                    Kutoa mafunzo kwa washauri wazalendo

·                    Ukusanyaji wa takwimu za ujenzi na kufanya utafiti

·                    Kuchapisha na kusambaza habari kuhusu shughuli za sekta,

·                    Utoaji wa miongozo ya kiufundi ikiwa ni pamoja na kanuni za zabuni.

 

63.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2003/2004 Baraza lilipanga kutekeleza yafuatayo:

 

·                    Kutoa msukumo katika utekelezaji wa Sera ya Ujenzi,

 

·                    Kutoa mafunzo kwa makandarasi, wahandisi washauri, watendaji wakuu hasa wa Serikali za Mitaa kuhusu masuala mbalimbali ya sekta ikiwemo sheria ya Manunuzi ya Umma (Public Procurement Act No.3 of 2001), usimamizi wa mikataba ya ujenzi,

 

·                    Kuboresha upatikanaji wa takwimu za shughuli za ujenzi,

 

·                    Kutoa huduma za ushauri kuhusu ukaguzi wa miradi, ujenzi wa barabara, ukadiriaji wa gharama za ujenzi,

 

·                    Kutoa mafunzo ya utekelezaji wa miradi ya miundo mbinu kwa njia ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (Public Private Partnerships - PPPs) na usuluhishi wa migogoro. 

 

·                    Kufuatilia kukamilishwa kwa uundwaji wa Mfuko wa Fedha wa Maendeleo ya Sekta ya Ujenzi (Construction Industry Develoment Fund -CIDF).

 

64.     Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Mei 2004 kazi zifuatazo zilitekelezwa:

 

·                    Baraza lilikamilisha utayarishaji wa Mikakati ya utekelezaji wa Sera ya Ujenzi na kuisambaza kwa wadau mbalimbali ili kutolewa maoni.

·                    Mfuko wa Fedha wa Maendeleo ya Sekta ya Ujenzi (Construction Industry Develoment Fund -CIDF) una mtaji wa Shilingi bilioni 5 na utatoa mitaji ya kufanyia kazi kwa wadau wa sekta ya ujenzi kwa masharti nafuu kuliko benki.  Mitaji hii ni pamoja na dhamana, mikopo ya kufanyia kazi (working capital) na mikopo ya kununulia vifaa na mitambo ya ujenzi. 

 

·                    Kwa kushirikiana na “Tanzania Investment Centre” na wadau wengine, Baraza limekuwa likishughulikia upatikanaji wa mapendekezo ya kuboresha mazingira bora ya utekelezaji wa miradi ya miundo mbinu ya kiuchumi kwa njia ya “(Public Private Partnerships -PPPs).”

 

·                    Baraza pia limeandaa mapendekezo ya marekebisho ya Sheria Na.20 iliyounda Baraza ambayo yanashughulikiwa na Serikali ili iendane na Sera ya Taifa ya Ujenzi ya mwaka 2003.

 

65.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/2005, Baraza litatoa msukumo wa utekelezaji wa Sera ya Ujenzi. Kipaumbele kitatolewa kwa malengo na mikakati inayolenga kuondoa matatizo makuu ya sekta ya ujenzi ambayo ni uwezo mdogo, tija ndogo na ubora hafifu wa kazi.  Aidha, Baraza litaendelea kusimamia Mfuko wa CIDF, kutoa huduma za ushauri wa kiufundi kwa Wadau mbalimbali kuhusiana na tathmini za zabuni, uteuzi wa Washauri, utayarishaji wa makabrasha ya Zabuni, madai, usuluhishi wa migogoro, usimamizi wa miradi na uchapishaji wa majarida.

 

 

 

CHUO CHA UJENZI - MOROGORO

 

66.     Mheshimiwa Spika, Chuo cha Ujenzi - Morogoro kilianzishwa kwa lengo la kufundisha Mafundi Sanifu, Mchundo na Wahandisi wa Wizara ya Ujenzi na Halmashauri za wilaya. Kwa sasa, chuo kinatoa pia mafunzo kwa mafundi Sanifu na Stadi wa fani mbalimbali wanaoshiriki kazi za ujenzi kwenye sekta za umma na binafsi. Katika mwaka wa fedha 2003/04, Chuo kilipanga kufundisha mafundi Sanifu150 katika fani za matengenezo ya barabara, majengo na ufundi, mafundi stadi 60 katika stadi mbalimbali, madereva wapya 120 na kuendeleza madereva wa umma 90, kukarabati majengo mawili na kununua samani na pia kununua gari 1 mini – bus.

 

Hadi kufikia Mei, 2004 Chuo kimefanikiwa kufundisha mafundi Sanifu 124 wa fani mbalimbali, madereva wapya 142, kuendesha mafunzo ya mafundi stadi mbalimbali 60 na kuendesha mafunzo kwa madereva wa umma – 26.

 

67.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/05, chuo kimepanga kutoa mafunzo kwa mafundi Sanifu 75, madereva mahiri 30, wanafunzi wa udereva wa awali 80 na mafundi stadi mbalimbali 60.

 

KITUO CHA USAMBAZAJI TEKNOLOJIA

 

68.     Mheshimiwa Spika, kituo hiki kilianzishwa mwaka 1997 kwa madhumuni ya kuimarisha/kuboresha sekta ya usafirishaji kwa kutumia mbinu ya usambazaji wa teknolojia kwa wadau wa sekta nzima ya usafirishaji.

 

Katika mwaka wa fedha wa 2003/04 kituo kilipanga kuimarisha na kuboresha huduma ya maktaba ya kituo, kutekeleza kwa majaribio mradi wa TRAC katika shule za sekondari za Azania, Jangwani na Mzizima jijini Dar Es Salaam, kuandaa, kuchapisha na kusambaza kwa wadau makala na majarida kuhusu kituo, kuanzisha tovuti ya kituo na takwimu mbalimbali. Aidha kituo kilipanga kuandaa kozi 4 na warsha 2 kwa wadau, kuendelea kutangaza/kunadi kwa wadau huduma zinazotolewa na kituo ili kuongeza matumizi ya huduma zinazotolewa, na kushiriki katika mikutano ya kimataifa ya utafiti na usambazaji wa teknolojia katika sekta ya barabara na usafirishaji kwa ujumla.

Hadi Mei, 2004 kituo kilisambaza kwa wadau 668 makala na taarifa zinazoelezea teknolojia mbalimbali katika sekta ya usafirishaji. Kwa kushirikiana na Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi, Baraza la Taifa la Ujenzi, Taasisi ya Barabara ya Marekani (US FHWA) na Tanzania Global Development Learning Centre, kituo kimeendesha warsha ya “Public-Private Partnerships in Transport Sector: Reforms, Development and Management”. Kituo, kimeshiriki katika makongamano 3 ya kimataifa na kongamano, mikutano na semina 12 nchini ili kujifunza, kubadilishana uzoefu na kubaini teknolojia zinazofaa kutumika hapa nchini. Wadau 141 walitumia huduma ya Maktaba ya kituo na kwa kushirikiana na taasisi nyingine 20 za wadau mbalimbali wa sekta ya ujenzi hapa nchini, kimeendelea kuratibu uandaaji wa mradi unaolenga kujenga uwezo wa sekta nzima ya ujenzi hapa nchini. Ripoti yenye mapendekezo ya mradi huo imekamilika na inafanyiwa kazi. Ili kuboresha utendaji wa kazi za Kituo, shughuli za utendaji zimehamishiwa kwa Wakala wa Barabara.

 

 

 

69.    Mheshimiwa Spika, Malengo ya Kituo kwa mwaka 2004/05 ni kama ifuatavyo:

·                   Kuandaa, kuchapisha na kusambaza kwa wadau makala na majarida kuhusu kituo,

 

·                   Kuandaa na kuendesha kozi na warsha kwa wadau,

 

·                   Kuendelea kutangaza/kunadi kwa wadau huduma zinazotolewa na kituo ili kuongeza matumizi ya huduma zinazotolewa,

 

·                   Kushiriki katika mikutano ya kimataifa ya utafiti na usambazaji wa teknolojia katika sekta ya barabara na usafirishaji.

 

MAENDELEO YA WATUMISHI

 

70.     Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2003/2004 watumishi wapya 38 waliajiriwa, 1,412 wa kada mbali mbali walipandishwa vyeo na 138 walithibitishwa kazini. Aidha, katika mwaka wa fedha 2003/2004 watumishi 26 walihudhuria mafunzo ya muda mrefu na 935 walihudhuria mafunzo ya muda mfupi katika fani mbalimbali.  Lengo la mafunzo hayo ni kuwaongezea ujuzi na ufanisi katika kazi zao.  Wizara yangu itaendelea na juhudi za kuwapatia mafunzo zaidi wafanyakazi wake katika mwaka wa fedha 2004/2005.

 

Uboreshaji wa Utumishi wa Umma Serikalini

 

71.     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2003/2004 Wizara ya Ujenzi, iliendelea kutekeleza Mpango wa Uboreshaji Utumishi wa Umma Serikalini. Mradi wa kuanzishwa Mfumo wa Uendeshaji na Usimamizi (Performance Management System) katika Wizara hii ulianzishwa Januari, 2003. Wizara imeshiriki hatua kwa hatua katika kutayarisha na kuandika Mpango Mkakati (Strategic Plan) kwa kipindi cha mwaka 2003/2004 hadi 2005/2006 na Mkataba wa Huduma kwa Mteja.  Aidha utaratibu mpya wa kupima Utendaji Kazi kwa Watumishi wa Umma umeanza kwa kuwahusisha kwanza Watendaji Wakuu wa Wizara.

 

Mikakati ya kupambana na UKIMWI

 

72.     Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2003/04 Wizara kupitia Kamati ya Ukimwi imeendesha Warsha za kuhamasisha Wafanyakazi wa ngazi zote kupambana na ukimwi.  Aidha Warsha kama hizo zimeendeshwa kwa Wafanyakazi wa baadhi ya Miradi ya Ujenzi wa Barabara kama vile miradi ya barabara za Makuyuni-Ngorongoro, Chalinze-Melela n.k.

 

Halikadhalika, Kamati ya ukimwi ya Wizara kwa kushirikiana na Mtaalam Mshauri (Consultant) imeandaa Mpango Mkakati (Strategic Plan) ya utekelezaji wa shughuli za kupambana na UKIMWI Wizarani kwa kipindi cha kuanzia 2004 – 2007.

 

Maadili kwa Watumishi wa Umma

 

73.     Mheshimiwa Spika, ili kukabiliana na mmomonyoko wa maadili, Wizara ya Ujenzi imeunda Kamati ya Maadili kama ilivyoelekezwa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.  Kamati hii itahakikisha inashirikiana na taasisi nyingine za Serikali kama vile PCB na Tume ya Uchunguzi katika utekelezaji wa kazi zake. Aidha itafuatilia kwa karibu uwajibikaji wa watumishi wa wizara katika kutoa huduma kwa wananchi na katika kutekeleza majukumu yao kwa ujumla. Aidha, Wizara inaendelea kutoa mafunzo ya maadili kwa watumishi wake.

 

Vita dhidi ya Rushwa

 

74.     Mheshimiwa Spika, mikakati ya kupiga vita rushwa katika Sekta ya Ujenzi ambayo Wizara yangu inaendelea kuitekeleza ni pamoja na kuendelea kutekeleza kikamilifu Sheria Na. 3 ya mwaka 2001 (Public Procurement Act No.3) ambayo inapunguza sana mianya ya rushwa katika utoaji zabuni za ujenzi, ushauri na ununuzi wa vifaa.  Vile vile katika kupunguza rushwa kwenye vituo vya mizani, Wizara inapunguza mizani ya kizamani na kuweka mipya ambayo inatumia kompyuta na imeongeza mizani inayohamishika (portable weighbridges). Aidha, Wizara imefukuza watumishi 140 waliotuhumiwa kujihusisha na rushwa katika vituo vya mizani.

 

Makusanyo ya Mapato kwa Mwaka 2004/05

 

75.    Mheshimiwa Spika, Wizara ya Ujenzi inatarajia kukusanya jumla ya shilingi 3,109,483,490 kutokana na vianzio vyake mbalimbali. Idara zinazokusanya maduhuli ni Utawala, Ugavi na Huduma pamoja na Ufundi na Umeme. Idara za Ufundi na Umeme pamoja na Ugavi na Huduma ziko chini ya “Retention Scheme” hivyo huruhusiwa kutumia kiasi fulani cha makusanyo yao kugharamia matumizi ya kawaida na kiasi kingine kinachobakia hupelekwa HAZINA. Muhtasari wa Makusanyo ya Mapato kwa mwaka 2004/05 ni kama ulivyoonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 8 kilichoko ukurasa wa 89.

Matumizi ya Kawaida mwaka 2004/05

 

76.    Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2004/05, Wizara ya Ujenzi imetengewa jumla ya shilingi 62,099,569,100.00 fedha za hapa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida.  Fedha hizi zinajumuisha:

·        Mfuko wa Barabara – Shs. 50,010,100,000.00

·        Mishahara ya Wizara - Shs. 2,552,525,400.00

·        Mishahara ya Taasisi nyingine zilizo chini ya Wizara - Shs. 4,634,749,400.00

·        Ruzuku kwa Taasisi nyingine zilizo chini ya Wizara - Shs. 533,262,900.00

·        Retention - Shs. 2,329,623,840.00

·        Matumizi Mengineyo kwa Wizara - Shs. 1,760,212,060.00

 

Muhtasari wa makisio ya Matumizi ya Kawaida kwa mwaka 2004/05 umeonyeshwa katika Kiambatanisho Na 9 kilichoko ukurasa wa 90.

 

HITIMISHO

 

77.     Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mchango mkubwa na muhimu wa Wahisani katika kufanikisha malengo ya sekta hii. Napenda nitumie nafasi hii kuwashukuru wahisani wote kutoka nchi mbalimbali, kwa moyo wao wa kusaidia nchi hii. Wahisani hao ni pamoja na Serikali za nchi za Denmark, Finland, Italia, Japan, Marekani, Norway, Saudi Arabia, Switzerland na Uingereza ambazo kwa kiasi kikubwa zimeisaidia sana sekta ya Ujenzi. Pia nayashukuru mashirika ya kimataifa ya ADB, EU, IDA na Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait na OPEC kwa kuendelea kusaidia sekta hii. 

78.     Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kuishukuru kwa mara nyingine Kamati ya Bunge ya Miundo Mbinu chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Prof. Henry Mgombelo, Mbunge wa Tabora Mjini, kwa ushauri mzuri waliotupa katika kuandaa bajeti hii.  Nawashukuru pia viongozi wa ngazi mbalimbali katika Wizara ya Ujenzi ambao ni Naibu Waziri, Mheshimiwa Hamza Mwenegoha (Mb), Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Katibu Mkuu Eng. John Kijazi, Wenyeviti wa Bodi za RFB, NCC, CRB, ERB, AQSRB na NBMM.  Aidha, nawashukuru Wakurugenzi na Watendaji Wakuu wa Taasisi na Wakala zote zilizo chini ya Wizara yangu pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara kwa kuonyesha utendaji mzuri wa kazi na uwajibikaji.

Vile vile napenda kuwashukuru wananchi wa Jimbo langu la Uchaguzi la Biharamulo Mashariki kwa ushirikiano walionipa katika kipindi hiki na kwa kunivumilia pale niliposhindwa kuwa nao kutokana na majukumu mengine ya kitaifa yaliyonikabili.  Kwa pamoja ninawashukuru sana.

         

79.     Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua umuhimu wa Miundombinu, hususan barabara katika kukuza uchumi. Lengo la Wizara yangu ni kuhakikisha Barabara Kuu zote Tanzania Bara zenye urefu wa kilomita 10,300 ziwe zimekamilika kujengwa kwa kiwango cha lami ifikapo mwaka 2012. Hivyo hatua mbalimbali tunazochukua ndani ya Wizara ni katika kufanikisha lengo hili. Tunatambua tatizo la upatikanaji wa fedha lakini siku zote tutaendelea kujitahidi ili fedha kidogo inayopatikana itumike katika ujenzi wa barabara. Siku zote penye nia pana njia. Naamini lengo letu litafanikiwa kutokana na kasi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami unaoendelea sasa katika nchi nzima.

 

Makadirio ya Bajeti ya Wizara 2004/05

 

80.     Mheshimiwa Spika, ili Wizara yangu iweze kutekeleza majukumu na malengo yake ya mwaka 2004/05, naomba Bunge lako Tukufu liidhinishe bajeti ya jumla ya Shilingi 287,237,763,100 ambapo kati ya hizo, Shilingi 146,618,569,100 ni za hapa na Shilingi 140,619,194,000 ni za nje.

 

Fedha za hapa zinajumuisha:

 

·        Fedha za Matumizi ya Kawaida shilingi 62,099,569,100

·        Fedha za Maendeleo Shilingi 84,519,000,000

 

Fedha za nje zinajumuisha:

 

·        Shilingi 129,623,400,000 kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo ya Barabara Kuu na za Mikoa.

·        Shilingi 10,995,794,000 za matengenezo ya Barabara Kuu na za Mikoa.

 

81.     Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.