Hotuba ya Waziri wa Elimu na Utamaduni

Mhe Joseph J Mungai MB Kuhusu Makadirio

ya Matumizi ya Fedha Kwa Mwaka 2005/06

 

I.       UTANGULIZI

1.   Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu baada ya kuzingatia taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii likae kama kamati ya matumizi kuyapitisha makadirio ya matumizi ya kawaida na ya maendeleo ya Wizara yangu kwa mwaka wa fedha 2005/2006.

 

2.   Mheshimiwa Spika nawashukuru; (a) Mheshimiwa, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Ubinafsishaji kwa hotuba yake iliyotoa tathmini ya hali na mwelekeo wa Uchumi; na (b) Mheshimiwa, Waziri wa Fedha, kwa hotuba yake iliyofafanua kwa ufasaha Bajeti ya Serikali ya mwaka 2005/06 pamoja na MKUKUTA.  Aidha namshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kwa taarifa nzuri ya maendeleo ya miaka kumi ya Serikali ya Awamu ya Tatu.

 

3.         Mheshimiwa Spika, Aidha, naishukuru Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, kwa ushauri wao mahili na kwa kupendekeza Bajeti ya Wizara yangu ipitishwe na Bunge hili heshimika.

 

Majukumu ya Wizara

4.   Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza majukumu yake Wizara inaongozwa na (a) Sheria ya Elimu Na. 25 ya 1978; (b) Taarifa ya Mfumo wa Elimu ya Tanzania kwa Karne ya 21; (c) Sera ya Elimu na Mafunzo; (d) Sera ya Utamaduni; (e) Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2025; (f) Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA); na (g) Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2000 ya Chama Tawala cha CCM. 

 

II.          MAENDELEO YA ELIMU NA UTAMADUNI YA MIAKA KUMI YA SERIKALI YA AWAMU YA TATU  1995 – 2005

 

5.   Mheshimiwa Spika, kwa kuwa huu ni mwaka wa mwisho wa Serikali ya Awamu ya Tatu inayoongozwa na Rais Benjamin William Mkapa, ningependa kulitaarifu Bunge kuhusu maendeleo makubwa ya Elimu na Utamaduni yaliyopatikana katika kipindi hicho cha miaka kumi (1995 – 2005).  Serikali ya Awamu ya Tatu ilianza kwa kuchukua hatua mbili muhimu:

(i)               Kwanza: Iliandaa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (Education Sector Development Programme) iliyokamilika 1997 kama hatua muhimu ya kupanga utekelezaji wa Taarifa ya Mfumo wa Elimu ya Tanzania Karne ya 21 (The Tanzania Education System for the 21st Century) iliyozaa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995

(ii)            Pili: Ilihakikisha inatimiza masharti magumu ya HIPC ili tuweze tena kukopesheka na kupewa misaada ya maendeleo.  MMEM na MMES ni matokeo ya hatua hii muhimu.

 

(a) Elimu ya Msingi

6.   Mheshimiwa Spika ,mafanikio ya Elimu ya Msingi yamekuwa:

·       Shule za Msingi zimeongezeka 3,330 sawa na asilimia 30 kutoka 10,927 mwaka 1995 hadi 14,257 mwaka 2005.

·       Watoto wa Rika la Elimu ya Msingi (miaka 7–13) walioko shuleni wameongezeka kutoka asilimia 55 mwaka 1995 hadi asilimia 95 mwaka 2005.

·       Kwa hiyo Watoto wa rika hilo walio nje ya shule wamepungua kutoka asilimia 45 mwaka 1995 hadi asilimia 5 mwaka 2005; na.

·       Wanafunzi wa umri wa juu kuliko rika lengwa la miaka 7–13 wamepungua kutoka asilimia 22 mwaka 1995 hadi asilimia 15 mwaka 2005.

 

(b)  Elimu ya Sekondari

7.   Mheshimiwa Spika, Mafanikio ya Elimu ya Sekondari yamekuwa:

·       Shule za Sekondari zimeongezeka kwa asilimia 195 kutoka 595 mwaka 1995 hadi 1,755 mwaka 2005, zikiwemo 1,206 za Serikali na 549 Zisizo za Serikali sawa na asilimia 31.

·       Wanafunzi wa Shule za Sekondari Kidato cha 1-6 wameongezeka zaidi ya maradufu kutoka 196,375 wakiwemo asilimia 5.5 (NER) ya rika husika mwaka 1995, hadi 524,325 wakiwemo asilimia 11.7 (NER) ya rika husika mwaka 2005.

·       Aidha, Huu ni mwaka wa pili wa utekelezaji wa  MMES, mpango ambao utaongeza wanafunzi Kidato cha 1 hadi 4 kufikia 2,000,000, sawa na asilimia 50 ya rika hilo, na Kidato cha 5 na 6 hadi 250,000 sawa na asilimia 25 ya rika hilo ifikapo mwaka 2010; na

 

·       Umeanzishwa Mtaala Mpya ambamo masomo ya sekondari yamepunguzwa kutoka 13 hadi 8 kwa kuunganisha masomo ya mchepuo na ya kawaida. Mtaala huo mpya utampatia mwanafunzi elimu bora zaidi ya Sekondari yenye msingi imara wa kuendelea na elimu ya juu au kujifunza ufundi au kujiajiri.  Hatua hii ni utekelezaji wa taarifa maalumu iitwayo: The Tanzania Education System for the 21st Century iliyoandaliwa na Tume Maalumu ya Wataalamu iliyoteuliwa na Serikali mwaka 1990 ambayo ilizaa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 1995 (The Education and Training Policy 1995) na Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu (Education Sector Development Programme – ESDP) ya mwaka 1997.

 

 

(c) Elimu ya Ualimu

8.   Mheshimiwa Spika, mafanikio ya Elimu ya Ualimu yamekuwa:

·       Walimu Tarajali katika Vyuo vya Ualimu wameongezeka kutoka 12,417 mwaka 1995 hadi 29,952 mwaka 2004, ambalo ni ongezeko la 17,535 sawa na asilimia 141

·       Vyuo vya Ualimu, vimeongezeka kutoka 34 mwaka 1995 hadi 52 mwaka 2005 vikiwemo 18 vizivyo vya Serikali sawa na asilimia 35

·       Kuanzia mwaka huu, Shule ya Sekondari ya Mkwawa, na Chuo cha Ualimu cha Dar es Salaam, vinakuwa Vyuo Vikuu vya Elimu Vishiriki vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha Chuo cha Ualimu cha Mtwara kitakuwa Chuo cha Elimu Ambata cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na kitaanza kutoa Stashahada ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

·       Mafunzo ya Kompyuta na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yanaanzishwa katika Vyuo vyote vya Ualimu.  Somo hilo litakuwa ni la lazima kwa kila Mwalimu Tarajali.

 

 

 

(d) Ubora wa Elimu

9.   Mheshimiwa Spika, katika miaka hii kumi kumekuwepo pia ongezeko la ubora wa Elimu itolewayo katika shule kwa vipimo vya mitihani ya Baraza la Mitihani Tanzania kama ifuatavyo:

·       Asilimia ya kufaulu (Pass Rate) Darasa la VII imeongezeka kutoka 15 mwaka 1995 hadi 49 mwaka 2004.

 

·       Asilimia ya kufaulu (Pass Rate) Kidato cha 4 katika Daraja la I–III imeongezeka kutoka 25 mwaka 1995 hadi 39 mwaka 2004 kwa shule zote kwa pamoja na 53 kwa Sekondari za Serikali peke yake.

 

·       Asilimia ya kufaulu Kidato cha 6 katika Daraja la I–III imeongezeka kutoka 71 mwaka 1995 hadi  94 mwaka 2005.

 

(e) Maendeleo ya Utamaduni

10.         Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza Utamaduni:

·       Sera ya Utamaduni ilipitishwa mwaka1997;

·       Vikundi vya burudani vilivyosajiliwa vimeongezeka kwa asilimia 377 kutoka 133 mwaka 1995 hadi 634 mwaka 2005; na

·       Wanafunzi wa Stashahada ya Sanaa wa Chuo cha Sanaa Bagamoyo wameongezeka kwa asilimia 180 kutoka 30 mwaka 1995 hadi 84 mwaka 2005.

 

III.                                MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM YA MWAKA 2000

 

11.   Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2000, Serikali ya CCM ilichukua hatua tatu muhimu:

(i)      Kwanza imeifanya elimu ya msingi kuwa ya bure na ya lazima.

(ii)            Pili kwa ushirikiano na wabia na wadau wetu wote wa maendeleo ya elimu imeandaa MMEM 2002-2006 na MMES 2004-2009 inayotoa Ruzuku za Maendeleo na Uendeshaji kwa wananchi wanaojenga shule.

(iii)          Tatu imepunguza ada ya Sekondari za kutwa kwa asilimia 50 kutoka shs.40,000 kuwa shs.20,000 na kuongeza maradufu ruzuku ya kuwasomesha watoto wa familia zisizo na uwezo ili nao wajikomboe kwa elimu ya Sekondari.

 

Baada ya hatua hizo utekelezaji wa Ilani umekuwa na mafanikio makubwa yafuatayo katika kipindi cha miaka mitano ya Bunge hili la 2000-2005:

 

(a) Elimu ya Msingi

12.   Mheshimiwa spika, kuhusu Elimu ya msingi:

(i)           Shule za msingi zimeongezeka 2,603 kutoka 11,608 kufikia 14,257  sawa na asilimia 23.

(ii)        Wanafunzi wameongezeka kwa asilimia 72 kutoka 4,382,410 wakiwemo asilimia 59 (NER) wa rika lengwa hadi 7,541,208 wakiwemo asilimia 95 (NER) wa rika lengwa.

(iii)      Ruzuku ya Maendeleo ya Shs.Bn 147.733 imetolewa kukamilishia ujenzi wa madarasa 32,539 na Nyumba za Walimu 9,664, Madawati 566,664, na Maliwato 14,417.

(iv)     Ruzuku ya Uendeshaji ya Shs.Bn 136.336 imetolewa kwa ajili ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia.  Hali ya vitabu imeboreka kutoka Kitabu 1 au 2 kwa Darasa hadi Kitabu 1 kwa wanafunzi 3.

(v)        Walimu wapya 45,451 wameajiriwa wakiwemo 37,261 wa Daraja A, na 7,152 wa Stashahada.

(vi)     Waliofaulu Mtihani wa DVII wameongezeka kutoka asilimia 19 mwaka 1999 hadi 49 mwaka 2004.

 

(b)  Elimu ya Sekondari

13.   Mheshimiwa spika, Kuhusu Elimu ya Sekondari katika miaka mitano ya Bunge hili:

(i)    Zimeongezeka Sekondari 828 sawa na asilimia 89 kufikia Sekondari 1,755.

(ii)   Wanafunzi wameongezeka maradufu kutoka 266,896 hadi 524,325.

(iii)     Jumla ya Shs.Bn 43.100 zimetumwa shuleni kwa ajili ya utekelezaji wa MMES ikiwemo:

(a) Ruzuku ya Maendeleo ya:

·       Shs.Bn 10.500 za ujenzi wa madarasa 1,499: na

·       Shs.Bn 7.600 za ujenzi wa Nyumba za Walimu 848: na

(b) Ruzuku ya Uendeshaji ya Shilingi Bn 11.900 za vifaa vya kufundishia na kujifunzia.

(iv)         Wanafunzi 24,000 wa familia zisizo na uwezo wanapewa Ruzuku ya Sekondari ya Shs. Bn 1.600 katika Vidato vya 1 na 2.

(v)            Watahiniwa wa shuleni waliofaulu KIV katika DI-III wameongezeka kutoka asilimia 26 mwaka 2000 hadi 39 mwaka 2004.

(vi)         Watahiniwa wa shuleni waliofaulu K6 katika DI-III wameongezeka kutoka asilimia 82 mwaka 2000 hadi 94 mwaka 2005.

 

IV.                           MALENGO YA MWAKA 2005/06

A.          Idara ya Elimu ya Msingi

14.   Meshimiwa Spika, Kupitia Idara ya Elimu ya Msingi mwaka 2005/06         unakuwa wa tano wa utekelezaji wa MMEM  wenye malengo   yafuatayo:

(a)             Kutoa Ruzuku ya Maendeleo ya shilingi Bilioni 5.556 ya kukamilishia ujenzi wa madarasa 1,792.

(b)    Kutoa Ruzuku ya Maendeleo ya shilingi Bilioni 3.312 kukamilishia ujenzi wa Nyumba za Walimu 920.

(c)    Kuajiri Walimu wapya 7,286 ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wa Shule za Msingi.

(d)            Kutoa mafunzo kwa Walimu tarajali 9,000 wa Daraja A.

(e)           Kuendelea kutekeleza MEMKWA na MUKEJA.

(f)              Kutoa Ruzuku ya Uendeshaji wa Shule ya Shilingi Bilioni 62.145 ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia ili pia kufikia uwiano wa kitabu kimoja kwa mwanafunzi (1:1)

(g)            Kuimarisha ubora wa elimu kwa kutekeleza mtaala mpya wa Elimu ya Msingi; na kuboresha mfumo wa mitihani na upimaji wa Elimu ya Msingi na Ualimu ngazi ya Cheti.

(h)            Kufuatilia na kuratibu utekelezaji wa MMEM katika kila ngazi; na ukaguzi wa hesabu za MMEM katika ngazi hizo na asasi za Wizara za TET na NECTA.

(i)               Kuendelea kuimarisha utoaji wa elimu maalumu kwa watoto wenye ulemavu katika ngazi ya elimu ya msingi.

 

15.   Mheshimiwa Spika, Bajeti ya Sekta ya Elimu ya mwaka huu ya jumla ya shilingi Bn 384.189  inaombwa kama ifuatavyo:

·       Kupitia Fungu 56 la TAMISEMI               Shs.Bn   44.999

·       HAZINA moja kwa moja Halmashauri        Shs.Bn 307.322 ; na

·       Kupitia Fungu 46 la Wizara yangu           Shs.Bn  31.868

                                                    Jumla Shs.Bn.384.189

                                                               =============

 

B.       Idara ya Elimu ya Sekondari

16.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu Idara ya Elimu ya Sekondari imepangiwa malengo yafuatayo ya MMES:

(a)         Kutoa Ruzuku ya Maendeleo ya Shs.Bn12.355 za kukamilishia ujenzi wa madarasa zikiwemo:

·   Shilingi Bn 2.989 za madarasa mapya 427 katika Sekondari zilizopo.

·   Shs.Bn 8.470 za madarasa 1,210 ya Sekondari mpya za ngazi ya kawaida; na

·   Shs.Milioni 896.0 za madarasa mengine 128 ya Sekondari zilizopo za ngazi ya juu K5 na K6.

(b)        Kutoa Ruzuku ya Maendeleo Shs.Bilioni 9.0 za kukamilishia ujenzi wa Nyumba za Walimu zikiwemo :

·   Shs.Bn 3.843 za Nyumba 427 za Sekondari zilizopo.

·   Shs.Bn 5.157 za Nyumba za Walimu 573 za Sekondari mpya za kawaida.

(c)         Kujenga kwa tenda ya Serikali maabara 88 katika shule zilizopo za ngazi za kawaida na ya juu wakati mahitaji ni Maabara 1,278.

(d) Kujenga Maliwato, Hosteli, Mabweni, Maktaba na Kumbi za Mikutano kwa Shs.Bn 12.468.

(e) Kufanya ukarabati wa shule za zamani kwa Shs. Bn 3.280.

 

(f)  Kutoa Ruzuku ya elimu ya Sekondari kwa wanafunzi 36,000 wa kidato cha 1 - 3 wa familia zisizo na uwezo:Shs.6.480.

 

C.      Idara ya Elimu ya Ualimu

17.   Mheshimiwa Spika, mwaka huu Idara ya Elimu ya Ualimu imepangiwa majukumu yafuatayo :

(a)     Kuanzisha miundo mbinu na mtandao wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika Vyuo vya Ualimu vyote kwa ajili ya Kufundishia na Kujifunzia.  Somo hili litakuwa la lazima kwa kila Mwalimu Tarajali.  Nawashukuru sana SIDA Sweden kwa msaada wa Shs.Bn 4.168 pamoja na huduma za kiufundi.

(b)     Kutenganisha Vyuo vya Stashahada viwe 14; na vya cheti Daraja A viwe 18.

(c)      Kufuatilia uandaaji wa muhtasari wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHEMA) kwa ajili ya Vyuo vya Ualimu.

(d)     Kuandaa Mkakati wa Kuboresha Menejimenti na Elimu ya Ualimu.

 

D.   Idara ya Ukaguzi wa Shule

18.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu Idara ya Ukaguzi wa Shule itafanya ukaguzi wa asasi mbalimbali za Elimu 19,905, na itanunua magari 18 na kutoa mafunzo ya awali kwa Wakaguzi wa shule wapya 127.

 

19.   Mheshimiwa Spika, Idara pia itaendesha mafunzo ya mbinu shirikishi za ufundishaji kwa Wakaguzi wa masomo ya English, Kiswahili, Physics, Chemistry, Biology na Ualimu. 

 

E.       Idara ya Maendeleo ya Utamaduni

20.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu, Idara ya Maendeleo ya Utamaduni itaendesha Tamasha Maalumu la kuimarisha umoja, amani, mshikamano na upendo miongoni mwa Watanzania.  Aidha itaendesha katika Mikoa 10 utafiti wa kubaini mila na desturi nzuri za kuimarisha ufanisi katika vita dhidi ya umaskini, rushwa, ubaguzi wa kijinsia, VVU na UKIMWI.

 

F.                     Idara ya Utawala na Utumishi

21.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu Idara ya Utawala na Utumishi itaajiri watumishi 795 wa kada mbalimbali ; na walimu 3,094 wa Shule za Sekondari.  Aidha, Watumishi 150 watapelekwa kwenye mafunzo ya muda mrefu na  mfupi ndani na nje ya nchi.

 

22.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu, ADEM itatoa mafunzo mbalimbali kwa : Viongozi Watendaji wa Elimu  21,294, na ya Stashahada ya Uongozi wa Elimu kwa Wanachuo 100.

 

G.      Idara ya Sera na Mipango

23.   Mheshimiwa Spika, Mwaka huu Idara ya Sera na Mipango itatekeleza majukumu kumi na mbili yaliyoainishwa ndani ya Hotuba ya Bajeti.

 

H.       Ofisi ya Afisa Elimu Kiongozi

24.   Mheshimiwa Spika, Afisa Elimu Kiongozi ataendelea kutoa miongozo ya kuboresha Elimu na Utamaduni, na kuongoza vitengo maalumu vilivyo katika ofisi yake.  Aidha, ataendelea  kusimamia mambo ya uhusiano wa kielimu wa kimataifa ukiwemo na SADC na EAC

 

I   TAASISI NA MABARAZA YALIYO CHINI YA WIZARA

 

25.         Mheshimiwa Spika, Wizara itaendelea kusimamia Taasisi, Mabaraza na Mashirika yake Saba katika ukurasa wa 78-90.

 

V.               MATATIZO KATIKA UTEKELEZAJI

26.         Mheshimiwa Spika, Katika uendeshaji wa elimu na programu za MMEM na MMES yamejitokeza matatizo yafuatayo:

(a)             Kutokusoma au kutokuelewa kwa usahihi Sheria na maamuzi yaliyomo katika maandiko muhimu ya Serikali kumesababisha baadhi ya wadau, na watendaji kutokujua na hata kudiriki kupinga mabadiliko yanayoendana na wakati likiwemo badiliko maalumu la mtaala wa elimu ya Sekondari !!

(b)            Kuchelewa kuzibwa pengo la fedha la MMEM kutokana na kumalizika utumiaji wa mkopo wa USD 150 milioni kutoka Benki ya Dunia na wahisani wengine kuwa katika mchakato wa badiliko kutoka “Pooled Fund” kuingia “Budget Support” ambao haujakamilika.

(c)             Kuwepo kwa pengo kubwa la fedha katika programu ya MMES kutokana na kuwa na chanzo kimoja tu cha uhakika ambacho ni mkopo nafuu wa Benki ya Dunia, wa USD 150 Milioni wakati bado tunasubiri ahadi za wabia wetu wengine ambao nawaomba wafanye upesi.

(d)            Kuwepo kwa tatizo la uelewa juu ya uendelevu wa programu ya MMEM baada ya 2006.  Inafaa kila mdau, aelewe kwamba Elimu ya Msingi ni jambo la kudumu kwa sababu watoto wataendelea kuwepo na kuongezeka.  Kipindi cha miaka mitano ya MMEM ni cha mpango kwa lengo la kufikia Elimu ya Msingi kwa wote; na ilihitajika kujenga majengo mengi ya shule kukidhi ongezeko kubwa la wanafunzi na walimu.  Baada ya mpango kukamilika ongezeko la miundo mbinu ya shule litakuwa la kawaida kuendana na ongezeko la idadi ya watu na watoto ambalo hatimaye litabebeka katika Bajeti ya ndani.

 

VI.            MAAMUZI MUHIMU

27.         Mheshimiwa Spika, Mwaka huu Wizara yangu itatekeleza maamuzi muhimu yafuatayo:

(a)    Kuboresha utekelezaji wa Programu ya MMES kwa kuziimarisha Shule za Sekondari kupokea, na kusimamia fedha za Ruzuku za Uendeshaji na Maendeleo bila kupitia Hazina Ndogo.

(b)   Kuendelea kuimarisha mtaala wa Elimu ya Sekondari ili kukidhi changamoto za utandawazi, soko huria na ushindani wa kielimu wa kimataifa. Nimetoa pamoja na Hotuba ya Bajeti makala maalumu ya Maelezo ya Mtaala Mpya wa Sekondari niliyoyatoa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii.  Wale ambao mpaka sasa bado hawajauelewa mtaala mpya wanashauriwa wayasome kwa makini maelezo hayo, na maandiko niliyoyataja ambayo ndiyo chimbuko la mtaala huo.

(c)    Kuedelea kutoa Ruzuku ya Maendeleo na Uendeshaji kwa wananchi wanaojenga shule za Msingi na Sekondari.

(d)   Kuendelea na sera sahihi za CCM za kupunguza ada ya Sekondari za kutwa kuwa shs.20,000/=; na kutoa elimu ya msingi ya bure na ya lazima. Mheshimiwa spika nachukua fursa hii kulitaarifu Bunge lako heshimika kuwa katika Azimio la Algiers la tarehe 11 April 2005 la Mawaziri wa Elimu wa Africa kutokana na uzoefu na ushauri wetu kifungu cha 7 kinasomeka "TAKE all necessary measures to make primary education free and compulsory for all children of Africa"  Huo ndio ushauri wetu Mawaziri wa Elimu wa Afrika utakaofikishwa kwa Wakuu wa Nchi za AU katika kikao chao cha mapema mwaka kesho.

 

Mheshimiwa Spika, kwa wale wanaopenda kusema mafanikio ya Rais Mkapa hayana ‘‘TRICKLE DOWN’’ naomba kuwapasha kuwa (i) ada ya Sekondari iiliyopunguzwa kuwa shs.20,000/= ;  na (ii) elimu ya msingi ya bure inaingia karibu KILA KAYA ya Tanzania nzima kupitia mlangoni, na umasikini umeanza kutokea madirishani!  Kwa mipango hii tumeanza kuandaa Rika Jipya la Watanzania ambao asilimia 100 watakuwa na elimu ya Msimi na asilimia 50 watakuwa na elimu ya Sekondari.

 

VII    SHUKRANI NA PONGEZI

 

28.   Mheshimiwa spika, nawashukuru na nawapongeza wanachi wa Mikoa yote na Halmashauri zao kwa moyo wao wa kujitolea kujenga na kuendesha Shule za Msingi na za Sekondari.  Aidha, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge na viongozi wote wa Mikoa, Wilaya, na Vijiji kwa ushirikiano wao kuhimiza na kufanikisha ujenzi na uendeshaji wa Shule katika maeneo yao.

 

29.   Mheshimiwa spika, naliomba Bunge hili liniunge mkono kuwashukuru nchi rafiki, mashirika ya fedha ya kimataifa, wadau wote na wabia wetu wa maendeleo ya elimu kwa misaada na ushirikiano wao kama nilivyowataja ukurasa 94 wa Hotuba ya Bajeti.

 

 

 

 

30.   Mheshimiwa spika, nawashukuru sana wafuatao :

·       Naibu Waziri wangu Mheshimiwa Bujiku Sakila, Mbunge wa Kwimba, kwa kunisaidia kwa uaminifu na bidii yake yote.

 

·       Katibu Mkuu wa Wizara yetu Dr. Naomi Katunzi kwa ushauri wa kitaalam na kitaaluma ; na

 

·       Aidha, Afisaelimu Kiongozi, Wakurugenzi wa Idara wote, Wakuu wa Shule na Vyuo, Walimu Wakuu, Walimu wote ; na Wafanyakazi wengine wote wa Wizara yangu ; kwa ushirikiano wao katika kutekeleza majukumu ya wizara na pia katika kuandaa Bajeti hii.

 

31.   Mheshimiwa spika, nawashukuru pia Viongozi na Wafanyakazi wote wa Mabaraza na Taasisi zote zilizo chini ya Wizara yangu.  Aidha, nawashukuru CWT na tawi la TUGHE la Makao Makuu ya Wizara kwa ushirikiano na ushauri wao unaoepusha migogoro kazini.

 

VIII   MWAKA WA MWISHO

32.   Mheshimiwa Spika, kwa kuwa huu ndio mwaka wa mwisho wa Serikali ya Awamu ya Tatu na wa Bunge hili ; nachukua nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa wafutao :

·       Kwanza kwa Mheshimiwa Rais Benjamin Mkapa kwa kuniteua na kunipa fursa ya kuitumikia nchi yangu kama Waziri wa Elimu na Utamaduni wa kipindi hiki cha mwanzoni mwa Karne ya 21 yenye changamoto za Dunia ya Utandawazi na Soko Huria.

·       Pili Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ushiriki wake wa kikatiba katika uteuzi wangu na kwa uongozi wake mzuri ; na Waheshimiwa Mawaziri na Wabunge wenzangu wote kwa uashirikiano wao mzuri sana.  Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuwa katika Timu nzuri ya Serikali ya Awamu ya Tatu iliyofunga mabao mengi ya maendeleo.

·       Tatu Nawashukuru sana wananchi wenzangu wa Jimbo la Mufindi Kaskazini kwa fursa hii waliyonipa, na nawaomba iwe Tena ! Tena ! Octoba mwaka huu !  Na ikiwa hivyo naahidi kuendelea kuwatumikia kama Mbunge wao KWA LUHALA NA UPIFU; KWA BUSARA NA USHUJAA kama isemavyo motto ya Hehe Council iliyobuniwa na Hayati Mtwa Adamu Sapi Mkwawa:  ‘Lidege Lingi Siliwhana amayago’.

·       Nne Nakushukuru sana Mheshimiwa Spika, kwa uongozi wako uliotulizana wa ‘‘Nyumba ya Malumbano’’ kama wanavyoliita Bunge kule Malawi !!  Kwa uongozi wako uliotulizana tumelumbana kwa utulivu sana.

 

IX     USHAURI

33.   Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa na jukumu la kusimamia na kuongoza maendeleo ya elimu kwa miaka hii mitano ya mwisho ya Serikali ya Awamu ya Tatu na ya mwanzo ya Karne ya 21 najipa uhuru wa kutoa ushauri ufuatao kwa Serikali ya Awamu ya Nne.

(i)  Kwanza Kukamilisha bila kuchelewa uandaaji ambao tayari unaendelea wa:   (a)        Mpango wa Maendeleo ya Mafunzo ya Ufundi (Vocational Education Development Plan – VEDP) ili kupanua mafunzo ya ufundi kwa ajili ya asilimia 50 ya wanafunzi ambao hawataendelea ngazi inayofuata ya elimu ya kawaida baada ya DVII, Kidato cha 4 na Kidato cha 6; na (b)      Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Juu (Higher Education Development Plan – HEDP) ili kumudu ongezeko kubwa la wahitimu  wa Kidato cha 6 kutokana na upanuaji wa Elimu ya Sekondari ya Juu uanoendelea. Wakati mwaka huu jumla ya wanafunzi wa sekondari K1-6 ni 524,325; ifikapo mwaka 2010 wanaohitimu Kidato cha 4 na Kidato cha 6 watakuwa zaidi ya 600,000 kwa mwaka.

 

(ii) Pili Inahitajika mapema iwezekanavyo kuanza kuandaa na kukamilisha Awamu ya Pili ya SEDP kwa lengo la kufikia Elimu ya Sekondari kwa Wote (Universal Secondary Education – USE) ifikapo mwaka 2015 au mapema zaidi kwa sababu nusu USE iliyomo katika mpango wa sasa haitoshi.

 

34.  Mheshimiwa spika, mimi naamini hatua hizo mbili za (i) kukamilisha      VEDP na HEDP na (ii) kuanzisha USE zitakuwa ni kichocheo muhimu cha kusukuma gurudumu la maendeleo ‘kwa kasi mpya, nguvu mpya na ari mpya’.

 

 

 

X  MAKADIRIO YA BAJETI YA WIZARA

35.  Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yote hayo, ninaliomba sasa Bunge lako heshimika lipitishe makadirio ya matumizi ya Shilingi 175,434,506,800 ili kuiwezesha Wizara yangu kutekeleza majukumu yake ya mwaka 2005/06. Kati ya fedha hizo:

(a)     Shilingi 66,070,411,000 zinaombwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya Wizara ya Elimu na Utamaduni; na

(b)    Shilingi 109,364,095,800 zinaombwa kwa ajili ya Mipango ya Maendeleo ya Wizara ya Elimu na Utamaduni.

 

36.   Mheshimiwa Spika, Hotuba hii ; na Hotuba ya Bajeti inapatikana pia katika Tovuti ya Wizara yangu : www.moec.go.tz

 

 

37.   Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.