HOTUBA YA WAZIRI WA USALAMA WA RAIA, MHESHIMIWA H. BAKARI MWAPACHU (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2006/07

 

HOJA

 

1.     Mheshimiwa Spika,   kutokana    na   taarifa  iliyowasilishwa Bungeni mapema leo na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ulinzi na Usalama, Mheshimiwa William Kusila, Mbunge wa Bahi, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu sasa likae kama Kamati ya Matumizi ili liweze kujadili na kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Usalama wa Raia kwa mwaka wa fedha wa 2006/07.

 

UTANGULIZI

 

2.     Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza kwa dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi za kishindo, za asilimia 80.2 katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi Desemba 2005.  Napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Dr. Ali Mohamed Shein aliyekuwa Mgombea Mwenza, kwa ushindi mkubwa walioupata.

 

3.     Mheshimiwa Spika, nampongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Amani Abeid Karume kwa ushindi mkubwa alioupata katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, ambao katika mazingira ya Zanzibar ni ushindi wa kishindo. Aidha, nampongeza Waziri Mkuu Mheshimiwa Edward Ngoyai Lowassa kwa kuteuliwa kushika wadhifa huo.  Kuteuliwa kwake na kuthibitishwa kwa kura nyingi na bunge hili ni ishara ya imani kubwa aliyonayo Mheshimiwa Rais na Waheshimiwa Wabunge juu ya utendaji wake wa kazi. 

 

4.  Mheshimiwa Spika, nakupongeza kwa dhati wewe binafsi Mheshimiwa Samuel Sitta na Naibu Spika Mheshimiwa Anne Makinda kwa kuchaguliwa kutuongoza. Vile vile nampongeza Spika Mstaafu, Mhe. Pius Msekwa kwa usimamizi madhubuti wa shughuli za Bunge ambao umetuwezesha kupata jengo jipya na la kisasa. Nawapongeza pia Wenyeviti, Mheshimiwa Jenista Mhagama Mbunge wa Peramiho na Mheshimiwa Job Ndugai, Mbunge wa Kongwa kwa kuteuliwa kuwa wenyeviti.  Aidha, nawapongeza Wenyeviti wote na Makamu Wenyeviti wa Kamati zote za Kudumu za Bunge kwa kuchaguliwa kuongoza kamati hizo.

 

5.  Mheshimiwa Spika,    napenda     pia     kutoa pongezi nyingi za dhati kwa Chama changu cha CCM kwa kupata viongozi wapya wa kitaifa.  Nampongeza sana Mwenyekiti wa CCM Taifa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuchaguliwa kwa kishindo kushika wadhifa huo.  Ushindi wa kura 1,812 kati ya kura 1,813 zilizopigwa ni ushindi wa kihistoria.

 

6.     Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kumpongeza Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa na Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Frederick Tulway Sumaye kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kuendeleza amani na utulivu nchini.  Aidha, nawapongeza kwa kusimamia utungaji mzuri wa sera za kiuchumi zilizoweza kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi na hivyo kuufanya uchumi wetu uwe wenye ushindani na endelevu.

 

7.     Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Yusuph Rajab Makamba kwa kuteuliwa na baadaye kuthibitishwa na NEC kuwa Katibu Mkuu wa CCM.  Nampongeza Mheshimiwa Jaka Mwambi kwa kuteuliwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara).  Nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa nyadhifa walizopata, Mheshimiwa Aggrey Mwanri, Mheshimiwa Dr. Asha Rose Migiro, Mheshimiwa Kidawa Salehe na Mheshimiwa Rostam Aziz.

 

8.     Mheshimiwa Spika, wote hawa tunawaombea kheri, afya njema na baraka tele za Mwenyezi Mungu katika kutekeleza majukumu yao mapya.  Napenda kuwathibitishia kuwa, mimi binafsi pamoja na wananchi wa Jimbo la Tanga tunawaahidi kuwapa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yao.

 

9. Mheshimiwa Spika, natoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waziri wa Fedha na Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji kwa hotuba zao nzuri ambazo zimetoa mwelekeo wa bajeti ya Serikali, hali ya uchumi wa nchi kwa jumla na masuala ya msingi yanayopaswa kutekelezwa mwaka ujao wa fedha wa 2006/07.

 

10.  Mheshimiwa Spika, natoa shukrani zangu za dhati kwa Kamati ya Bunge ya Ulinzi na Usalama kwa kuyapitia na kuyachambua makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yangu tarehe 30 Mei 2006, pamoja na kuchambua  masuala mbalimbali ya Wizara ya Usalama wa Raia na kuyatolea maoni na ushauri. Michango iliyotolewa na kamati kwa ujumla imetusaidia kwa kiwango kikubwa kuiboresha hotuba yangu.

 

11.   Mheshimiwa Spika, napenda pia kutoa shukrani kwa ushirikiano wa karibu, ushauri na maelekezo fasaha ambayo nimekuwa nikiyapata kutoka Kamati ya Bunge ya Ulinzi na Usalama. Ushauri na maelekezo yao unasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha utendaji kazi katika Wizara yangu.

 

12.   Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mhe. Rais kwa kuniteua kuwa Waziri wa kwanza wa Wizara mpya ya Usalama wa Raia na kunipatia Naibu Waziri wa Usalama wa Raia Mheshimiwa Mohamed Aboud Mohamed, ambaye ameonesha umahiri na uwezo mkubwa katika kunisaidia kusimamia shughuli za Wizara na za Bunge. 

 

13.   Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii pia kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara Bw. Bakari Mahiza ambaye ni hazina kubwa kwa Wizara yetu kutokana na uzoefu alioupata akiwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambayo wakati huo Jeshi la Polisi lilikuwa chini yake. 

 

14. Mheshimiwa Spika, aidha, napenda kumshukuru Inspekta Jenerali Mstaafu, Alhaj Omar Iddi Mahita, ambaye yeye pamoja na Makamishna wake wote walifanya kazi nzuri na walijitahidi sana kuboresha mazingira ya utendaji kazi wa Polisi.  Ninawashukuru na kuwapongeza sana.

 

15.   Mheshimiwa Spika, namshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa uteuzi wa  Inspekta Jenerali mpya Ndugu Said Mwema, pamoja na Makamishna wapya ambao kwa kipindi kifupi wameweza kuleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji na kukabiliana na uhalifu nchini, na hivyo kurejesha heshima ya Serikali na kuwapa imani wananchi, wageni na wawekezaji, kwamba nchi yetu bado ina amani na utulivu.

 

16.   Mheshimiwa Spika, napenda kutoa pongezi nyingi kwa Makamanda wote wa Polisi wa Mikoa, Vikosi na Wilaya; Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa, Vikosi na Wilaya na askari wote kwa ujumla kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya ya kulinda amani na usalama nchini.  Juhudi zao tunazitambua na kuzithamini.

 

17.   Mheshimiwa Spika, Wizara ya Usalama wa Raia ilianzishwa na  Mheshimiwa Rais kwa Tangazo la Serikali Na. 1 la mwezi Januari 2006 kwa lengo la kusimamia usalama wa raia na mali zao wakiwemo wageni na wawekezaji.  Kuundwa   kwa Wizara hii ni kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2005, kama ilivyoainishwa kwenye Ibara ya 111 inayozungumzia Ulinzi na Usalama. Ilani ya Uchaguzi inataka uwezo wa Taifa wa kupambana na ujambazi na uhalifu kwa ujumla wake uongezwe na pia kuwahamasisha wananchi kushiriki katika ulinzi wa maeneo yao ili kuhakikisha usalama wao na wa mali zao.

 

18.  Mheshimiwa Spika, wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu Mheshimiwa Rais alisisitiza umuhimu wa kuendeleza amani na utulivu uliopo nchini ili kuimarisha uchumi wa nchi na kuongeza kasi ya maendeleo, na hivyo kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania.   Kunapokuwa na amani na utulivu wananchi wanaweza kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa ili kujiletea maendeleo yao. 

 

19.   Mheshimiwa Spika, hali ya amani na utulivu pia itawavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza kwenye maeneo mbali mbali nchini na hivyo kuongeza nafasi za ajira na Pato la Taifa.  Ni katika mazingira hayo ya amani na utulivu, mipango na mikakati ya Kitaifa kama vile Mipango ya Muda wa Kati na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA), inaweza kutekelezwa na malengo ya Millenia 2015 na hatimaye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 inaweza kufanikiwa.

 

20.  Mheshimiwa Spika,    wakati    Mheshimiwa    Rais alipotembelea Wizara hii mara baada ya kuunda Baraza la Mawaziri, alizitaja sababu kuu za kuundwa kwa Wizara hii kama ifuatavyo:

 

a.    Ongezeko  la  idadi ya watu  kutoka  milioni   10.3 wakati wa Uhuru mwaka 1961 hadi milioni 35 hivi sasa.

 

b.     Kuongezeka kwa uhalifu na maarifa ya uhalifu, ikiwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika kufanya uhalifu.

 

c.     Kukua kwa Jeshi la Polisi na shughuli za Polisi kuongezeka.

 

d.     Kupunguza ukubwa wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwani ilikuwa kubwa mno, kiasi cha kupunguza umakini wa kazi.

 

e.     Kumpa   nafasi    Waziri kushughulikia masuala yanayohusu Polisi tu ili kukabiliana na ongezeko la vitendo vya uhalifu, hasa uhalifu wa kutumia silaha. 

 

MAJUKUMU YA WIZARA

 

21.  Mheshimiwa   Spika,   muundo wa Wizara uliidhinishwa na Mheshimiwa Rais tarehe 18 Aprili 2006. Baadhi ya majukumu ya Wizara ya Usalama wa Raia kulingana na muundo huo ni kama ifuatavyo:

 

a.     Kusimamia  na kufuatilia  masuala    yote   yanayohusu usalama wa raia na mali zao   ikiwa ni pamoja na wageni kama vile  watalii na wawekezaji kutoka nje.

 

b.      Kuandaa   Sera   ya   Usalama   wa   Raia  

        na kusimamia  utekelezaji wake.

 

c.          Kuandaa mikakati ya muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu ya kukabiliana na uhalifu nchini.

 

d.    Kushirikisha jamii katika kuweka mikakati ya kuzuia uhalifu kupitia utaratibu wa Polisi Jamii.

 

e.               Kushughulikia malalamiko mbali mbali ya wananchi na kuyapatia ufumbuzi.

f.                Kusimamia maendeleo ya watumishi wa Wizara.

 

g.       Kuzuia uhalifu wa kimataifa kwa kushirikiana na nchi jirani pamoja na Mashirika ya Kimataifa na kikanda kama vile Shirikisho la Polisi la Kimataifa (INTERPOL), Shirikisho la Polisi la Nchi za SADC (SARPCCO), na Shirikisho la Polisi la Nchi za Afrika Mashariki na Pembe ya Afrika (EAPCCO).

 

DIRA YA WIZARA

 

22.   Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imejizatiti kutekeleza majukumu niliyoainisha hapo juu kwa kuongozwa na Dira ya “Kuwa na Wizara yenye uwezo endelevu wa kuhakikisha kuwa usalama wa raia na mali zao unakuwepo”. Lengo la dira hii ni kuhakikisha usalama wa raia na mali zao wakiwemo wageni kama vile watalii na wawekezaji.

HALI YA UHALIFU NCHINI

 

23.   Mheshimiwa Spika, kwa ujumla idadi ya matukio ya uhalifu nchini, Tanzania Bara na Visiwani, hasa makosa makubwa ya jinai kitakwimu imeendelea kushuka kuanzia mwaka 2000 hadi kufikia Desemba 2005.  Mfano, kipindi cha Januari hadi Desemba 2000, jumla ya matukio 87,973 yaliripotiwa katika vituo vya Polisi nchini, ikilinganishwa na jumla ya matukio 73,555 yaliyoripotiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2001. 

 

24.   Mheshimiwa Spika, idadi hiyo ilishuka zaidi mwaka 2002 ambapo jumla ya matukio 67,371 yaliripotiwa.  Takwimu zinaonyesha pia kwamba, idadi ya matukio hayo yalipungua zaidi mwaka 2003 na kufikia matukio 58,516.  Mwaka 2004 kulikuwepo na ongezeko kidogo la idadi ya matukio yaliyoripotiwa Polisi ambapo jumla ya matukio 61,376 yaliripotiwa.  Hata hivyo, idadi hiyo ya matukio kwa kipindi kilichoishia mwezi Desemba 2005 ilishuka sana hadi kufikia matukio 46,650, ikiwa ni upungufu wa matukio 14,726 ambao ni sawa na asilimia 24.

 

25. Mheshimiwa Spika, makosa makubwa ya jinai yaliyotolewa taarifa katika vituo vya Polisi kuanzia Julai 2005 hadi Aprili 2006 katika mikoa yote nchini yalikuwa 48,265 ikilinganishwa na matukio 51,820 kipindi cha Julai 2004 hadi Aprili 2005.  Kuna upungufu wa matukio 3,555 sawa na asilimia 6.8.  Hata hivyo, bado juhudi zaidi zinahitajika  kupambana na uhalifu kote nchini, Bara na Visiwani.

 

26. Mheshimiwa Spika, makosa ya Usalama Barabarani yaliyosababisha ajali ambayo yaliripotiwa Polisi kati ya Julai 2005 hadi Aprili 2006 yalikuwa 17,062 ikilinganishwa na 14,710 katika kipindi cha Julai 2004 hadi Aprili 2005. Kuna ongezeko la makosa 2,352 sawa na asilimia 16. Kati ya Julai 2005 hadi Aprili 2006 watu waliofariki kutokana na ajali za barabarani walikuwa 1,896 na wengine 12,349 walijeruhiwa ikilinganishwa na kipindi kama hiki mwaka 2004/05 ambapo watu 2,159 walifariki na wengine 16,523 walijeruhiwa.

 

27.   Mheshimiwa Spika, idadi ya watu waliofariki ilipungua kwa watu 263 sawa na asilimia 12.2 na waliojeruhiwa walipungua kwa watu  4,174 sawa na asilimia 25.3 kama inavyoonyesha katika Jedwali Na. 1. Pamoja na takwimu hizo kuonyesha kupungua, lakini bado tatizo la ajali za barabarani ni kubwa, hivyo jitihada zaidi za Jeshi la Polisi katika kukabiliana na makosa ya usalama barabarani zinahitajika.

 

28. Mheshimiwa Spika, sababu za kuwepo  ajali nyingi za barabarani ni pamoja na uzembe wa madereva, ubovu wa  magari, ubovu wa barabara, magari kujaza kupita  kiasi, uendeshaji mbaya na wa hatari, ulevi, mwendo wa kasi, kulegeza vidhibiti mwendo, utembeaji mbaya wa waenda kwa miguu, upandaji mbaya wa pikipiki na baiskeli, ukosefu wa alama za barabarani, n.k.

 

29. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza hapo awali, tatizo la ajali za barabarani bado ni kubwa na linahitaji mikakati thabiti ya pamoja ya wadau wote wa sekta hii. Ajali za barabarani zinasababisha vifo kwa abiria na waenda kwa miguu, zinaacha majeruhi, vilema na wengine kubaki yatima.  Ajali pia husababisha upotevu na uharibifu wa mali.

 

30.   Mheshimiwa Spika, kulingana na takwimu za mwaka 2005, mikoa inayoongoza kwa kuwa na ajali nyingi za barabarani ni  Dar es Salaam,  Mwanza,  Mjini Magharibi, Pwani, Iringa, Arusha, Tanga, Mbeya, Morogoro na Kilimanjaro kama inavyoonyesha kwenye Jedwali Na. 2(f).

 

31.   Mheshimiwa Spika, matukio ya ajali mbaya za barabarani ya hivi karibuni ni yale yaliyotokea Mkoani Kagera na kuua watu 28 na Mkoani Arusha, ambapo watu 54 walipoteza maisha yao. Nachukua fursa hii kuwapa pole familia, ndugu na jamaa za marehemu, na kuwatakia wapone haraka majeruhi wote ambao bado wamelazwa. Aidha, narudia kutoa wito kwa madereva wote, kuwa waangalifu na kufuata  sheria zote za barabarani.  Abiria kwa upande wao, wasikubali kabisa kupanda magari yaliyojaa na yanayokwenda mwendo wa kasi kwani ni hatari kwa maisha yao wenyewe.   

 

32 Mheshimiwa Spika, kama ilivyo kwenye matukio mengine ya uhalifu ambapo wananchi hutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi, Wizara yangu inaomba ushirikiano kutoka kwa abiria kwa kutoa taarifa Polisi kuhusu magari ya abiria yanayokiuka sheria za Usalama Barabarani.

 

33. Mheshimiwa Spika, Majedwali Na. 2(a) hadi 2(e) na 2(g) yanatoa mchanganuo wa makosa ya jinai kimkoa kwa kipindi cha Januari hadi Desemba, 2005. Kwa muhtasari kwa makosa dhidi ya binadamu mikoa inayoongoza ni  Dar es Salaam, Tanga, Mbeya, Kagera, Mwanza,  Shinyanga na Arusha. Makosa dhidi ya mali, mikoa inayoongoza ni Dar es salaam, Kagera, Tanga, Morogoro, Mwanza, Mbeya, Kilimanjaro, Mara na Kigoma. Aidha kwa upande wa makosa dhidi ya maadili ya jamii, mikoa inayoongoza ni   Dar es  Salaam, Mwanza, Mara, Kilimanjaro, Arusha, Morogoro, Shinyanga, na Kagera.

 

BAADHI YA MATUKIO MAKUBWA YA UHALIFU YALIYOTOKEA NCHINI

 

34.   Mheshimiwa Spika, ufuatao ni muhtasari wa baadhi ya matukio makubwa ya uhalifu yaliyotokea katika kipindi cha Januari hadi Julai, 2006.  Matukio hayo yalileta hofu kubwa kwa wananchi kiasi cha kujenga hisia kwamba Jeshi la Polisi limeshindwa kukabiliana na wimbi la ujambazi hapa nchini na wengine walithubutu hata kusema kwamba kazi hii wapewe Jeshi la Wananchi wa Tanzania.

 

35.   Mheshimiwa Spika, kazi ya kulinda usalama wa raia na mali zao ni yenye taaluma maalum na wenye taaluma hiyo ni Jeshi la Polisi. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa jumla kuwa Jeshi la Polisi lina uwezo wa kuwalinda wananchi na mali zao.

 

36.  Mheshimiwa Spika, tarehe 7 Januari 2006 majambazi yakiwa na silaha yalivamia Benki ya NBC (T) LTD Tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kupora Tsh. 8,762,915, mali ya benki hiyo na kutoweka.

 

37.   Mheshimiwa Spika, tarehe 14 Januari 2006 ilisemekana majambazi manne yakiwa na silaha yalivamia gari la Kampuni ya BIDCO lililokuwa na makusanyo ya fedha za mauzo Tsh. 5,775,000 na kupora kisha kutoweka.  Hata hivyo, ilisemekana wakati huo kwamba majambazi hayo yalikamatwa na Polisi muda mfupi baadaye na kuuawa wakati wakirushiana risasi.  Tukio hili la kuuawa watu hao lilisababisha hisia tofauti miongoni mwa wananchi ambapo yalikuwepo madai kwamba waliouawa hawakuwa majambazi bali raia wema.  Malalamiko hayo yalisababisha Mheshimiwa Rais kuunda Tume ya Jaji Kipenka Mussa ili kufanya uchunguzi. 

 

38.   Mheshimiwa Spika, tayari Tume imewasilisha ripoti yake Serikalini, na katika uchunguzi wake ilibaini kwamba waliouawa hawakuwa majambazi bali raia wema na kupendekeza askari 15 waliohusika katika tukio hilo washtakiwe kwa mauaji.  Askari 12 wamekwishakamatwa na kufikishwa mahakamani ambapo kesi yao bado inaendelea.  Askari waliobakia bado wanasakwa na Jeshi la Polisi.

 

39. Mheshimiwa Spika, tarehe 2 Februari, 2006 majambazi yanayokadiriwa kufikia 10 yakiwa na silaha yalivamia Benki ya NBC Tawi la Ubungo na kufanikiwa kupora Tsh. 123,000,000, Dola za Kimarekani 16,128 na EURO 50 mali ya benki hiyo na kisha kutoweka.

 

40.   Mheshimiwa Spika,  tarehe 6 Machi 2006 majambazi yakiwa na silaha yalivamia benki ya Standard Chartered Tawi la Life House na kufanikiwa kupora fedha taslimu Shilingi Milioni 300 kutoka kwa mteja ambaye alikuwa anataka kuweka fedha hizo benki.

 

41. Mheshimiwa Spika, tarehe 20 Aprili, 2006  katika makutano ya barabara za Morogoro, Sam Nujoma na Nelson Mandela, majambazi kadhaa yaliyokuwa na silaha nzito za kivita yalishambulia msafara wa magari ya benki ya NMB Tawi la Bank House ambayo yalikuwa yanasafirisha fedha Shilingi bilioni 1 kutoka tawi la  NMB Bank House Dar es Salaam kwenda Tawi la NMB Wami Morogoro. Katika tukio hilo askari mmoja kati ya askari wanne waliokuwa wanasindikiza fedha hizo pamoja na mfanyakazi mmoja wa benki ya NMB waliuawa na majambazi hayo.

 

42.   Mheshimiwa Spika, askari wengine watatu, dereva na wananchi wengine wapita njia walijeruhiwa kwa risasi zilizopigwa na majambazi hayo. Fedha shilingi milioni 150 ziliporwa na majambazi hayo na Polisi waliweza kuokoa shilingi milioni 850. 

 

43.   Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kisiwani Zanzibar mwanzoni mwa mwezi Julai, yametokea matukio ya ujambazi wa kutumia silaha ambapo kiasi kikubwa cha fedha kimeibiwa na mtu mmoja kuuawa.  Hali hii imesababisha hofu kubwa kwa wafanyabiashara  na wananchi wa Visiwani kwa sababu siyo kawaida matukio ya aina hii kutokea huko.

 

44.   Mheshimiwa Spika, tarehe 4 Julai, 2006  eneo la Darajani Mjini Unguja, majambazi yakiwa na silaha yalivamia dukani kwa Ndugu Mohamed Nassoro na kupora fedha taslimu Sh.12,000,000 na kadi za simu zenye thamani ya Sh.5,000,000.  Majambazi hayo yalifyatua risasi na kumpiga kichwani Ndugu Mohamed Bakari Mrisho na kufariki.

 

45.   Mheshimiwa Spika, tarehe 6 Julai, 2006 eneo la Kisiwandui, majambazi yenye silaha yalivamia duka la Al-Habbys na kufanikiwa kupora fedha taslimu Sh.30,000,000 baada ya kutishia kwa silaha.

 

46.   Mheshimiwa Spika, kufuatia matukio haya ya ujambazi kutokea kwa mfululizo, Jeshi la Polisi lilijipanga upya kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama na kukamata idadi kubwa ya majambazi yaliyohusika kwenye matukio haya pamoja na silaha walizotumia.   Miongoni mwa majambazi yaliyokamatwa wapo raia wa nchi jirani na raia wa humu humu nchini. Watuhumiwa wamekwishafikishwa mahakamani.  Majambazi hayo yaliweza kukamatwa kutokana na ushirikiano wa wananchi.  Kwa kupitia Waheshimiwa Wabunge, napenda kuwashukuru wananchi waliotoa ushirikiano wao uliowezesha majambazi kukamatwa.  Aidha napenda kuwapongeza askari wote walioshiriki kupambana na majambazi na kufanikisha kuokolewa kwa mali na kukamatwa kwa majambazi.

 

SABABU ZA KUWEPO KWA UHALIFU NCHINI

 

47.   Mheshimiwa Spika, zipo sababu nyingi zinazosababisha kutokea kwa uhalifu nchini.  Sababu za jumla ni kama vile kuongezeka kwa idadi ya watu nchini, tatizo la wimbi la watu kuhamia mijini  toka vijijini, kupanda kwa gharama za maisha na ukosefu wa ajira, na  kuongezeka kwa wakimbizi ambao baadhi yao huingia na silaha kinyume cha sheria.  Sababu hizo za jumla kwa namna moja au nyingine zimechangia ongezeko la vitendo vya uhalifu nchini na hasa uhalifu wa kutumia silaha.

 

48.   Mheshimiwa Spika, uchambuzi umeonyesha kwamba zipo sababu nyingine zinazochangia kuwepo kwa vitendo vya uhalifu kama ifuatavyo:-

 

a.               Utandawazi na Mageuzi katika Mfumo wa Mawasiliano

 

Sera ya Utandawazi imesababisha na kurahisisha mwingiliano wa watu wa mataifa mbali mbali. Wahalifu wa Kimataifa nao wametumia mwanya huu na kuweza kufanya uhalifu nje ya mipaka ya nchi zao.  Aidha, mageuzi katika mfumo wa mawasiliano yamerahisisha sana na kuongeza kasi ya utendaji makosa.  Wahalifu hivi sasa wanaweza kuwasiliana kwa haraka na kwa mawasiliano bora zaidi popote wanapokuwa, wakati mwingine kupita yale waliyonayo Polisi kwa sasa.  Mfano, matumizi ya Computer, Internet na simu za mkononi za kisasa.

Aidha, pale ambapo Polisi wanahitaji kufuata utaratibu wa kisheria na Kidiplomasia wa kuvuka mipaka kufuatilia wahalifu, wahalifu hao hawalazimiki kufanya hivyo wanapokwepa mkono wa sheria.

 

b.              Uchache wa askari na nyenzo za kutendea kazi

 

Upo uhaba mkubwa wa askari ikilinganishwa na idadi ya wananchi wanaohitaji huduma ya Polisi.  Kwa upande mwingine, upo uhaba wa vitendea kazi muhimu kwa ajili ya doria za miguu, magari, vifaa vya majini na vifaa vya mawasiliano.  Kukosekana kwa vitendea kazi hivi kumeathiri sana uwezo wa Idara kukabiliana kikamilifu na tishio la uhalifu nchini.  Mfano, imekuwa ni vigumu kuwahi kwenye baadhi ya matukio ya uhalifu kwa sababu ya ama kukosekana gari au gari kutokuwa na mafuta.

 

Aidha, imekuwa vigumu kukabiliana na uhalifu wa kuteka nyara magari kwenye barabara kuu kutokana na kutokuwa na magari ya kufanyia doria kwenye barabara hizo (Highway Patrol).

 

c.               Kutokuwa na Mfumo wa Kisasa wa Uwekaji Kumbukumbu na Upashanaji Taarifa

 

Upo umuhimu wa kuwa na njia za kisasa za uwekaji kumbukumbu, mawasiliano kwa njia ya mtandao wa ‘Computer’ na umuhimu wa kuwa na ‘Electronic Surveillance System’ kama ‘Closed Circuit Televisions (CCTV), ambayo hunakili matukio yote ya uhalifu.  Kukosekana kwa mfumo  huo  wa kisasa wa uwekaji kumbukumbu na mawasiliano  kwa Jeshi letu kumedhoofisha kwa kiasi kikubwa jitihada za kukabiliana na uhalifu.

 

d.              Uhaba wa Elimu na Taaluma za Upelelezi

 

Uhaba wa askari wenye taaluma ya upelelezi umechangia kwa kiasi fulani kupunguza kiwango cha mafanikio ya kudhibiti uhalifu kwa baadhi ya maeneo.  Ukweli ni kwamba aina, muundo na mbinu za makosa ya jinai kwa jumla hubadilika siku hadi siku. 

 

Mbinu hizo ni matumizi ya teknolojia ya kisasa kama vile matumizi ya mifumo ya kisasa na ya haraka ya kusafirisha fedha pamoja na kujenga mtandao wa magenge ya wahalifu ambao unahusisha wahalifu wa nchi za jirani.  Hali hii inahitaji kupata askari ambao wamepata taaluma kuhusu mabadiliko hayo ili kuweza kukabiliana kikamilifu na matishio ya uhalifu wa kisasa na yenye sura ya Kimataifa.

 

e.               Udhibiti hafifu wa Mipaka yetu

 

Upo upungufu wa nyenzo na watendaji wa kutosha katika maeneo muhimu ya mipaka yetu.  Matukio yaliyotokea hivi karibuni hasa ya unyang’anyi wa kutumia silaha, wizi wa magari, madawa ya kulevya, n.k. yametudhihirishia kwamba wahalifu kutoka nchi jirani wamehusika katika matukio hayo. 

 

Hali hii inaashiria kwamba kumekuwepo na udhaifu katika kuwachunguza wageni mbalimbali wanaoingia nchini mwetu.  Udhaifu huu umetokana na ama ukosefu wa vifaa muhimu na vya kisasa kama vile detecting/screening machines, kumbukumbu sahihi za wahalifu wa Kimataifa na upungufu wa watendaji wenye taaluma inayostahili kwenye vituo vya mipakani.

 

f.                Ukosefu wa Vyumba/Ofisi Maalumu za Upelelezi

 

Tatizo la uhaba wa ofisi kwa ajili ya askari wa Upelelezi na hasa vyumba maalum vya kufanyia mahojiano (Interview Rooms) pia linaathiri kwa kiasi kikubwa ufanisi katika upelelezi hasa wa kesi kubwa.  Hali hii inachangia kuharibika au kuchelewa na hatimaye kushindwa mahakamani katika baadhi ya kesi.

 

g.               Mabenki na Taasisi za Fedha  Kutojikinga kwa Njia za Kisasa

 

Kukataa ushauri wa Polisi wa kuweka  mifumo mizuri ya ulinzi inayotumia teknolojia ya kisasa katika Benki na Taasisi nyingine za fedha hapa nchini,  kumechangia sana wahalifu wa ndani na nje ya nchi kufanya vitendo vya uporaji kwenye taasisi hizo kwa urahisi na kuondoka bila kugundulika na hivyo kufanya kazi ya upelelezi kuwa ngumu zaidi.

 

HATUA ZINAZOCHUKULIWA KUIMARISHA UTENDAJI

 

49.   Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka 2002/03 Serikali imekuwa ikichukua hatua za kuboresha Bajeti ya Jeshi la Polisi.  Bajeti hiyo imewezesha upatikanaji wa baadhi ya vitendea kazi kama vile magari, vifaa vya mawasiliano, mashua za doria n.k na upatikanaji wa makazi ya askari.

 

50.   Mheshimiwa Spika, bajeti ya Jeshi la Polisi imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka kama ifuatavyo: Mwaka 2006/07 bajeti ya matumizi ya kawaida ya Jeshi la Polisi imeongezeka kwa asilimia 40.1 na ile ya maendeleo imeongezeka kwa asilimia 36.2 ukilinganisha na mwaka 2005/06 ambapo bajeti ya matumizi ya kawaida iliongezeka kwa asilimia 18.7 na ile ya maendeleo iliongezeka kwa asilimia 1.9. Kwa mwaka 2006/07 bajeti ya matumizi ya kawaida na ya maendeleo kwa pamoja imeongezeka kwa asilimia 39.8 ukilinganisha na asilimia 17.6 mwaka 2005/06 kama inavyoonyesha kwenye Jedwali Na. 4(a).  Hata hivyo kutokana na matatizo ya Jeshi la Polisi kuwa makubwa, kama yalivyotajwa bado juhudi zaidi zinahitajika kuboresha bajeti yake.

 

51.   Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais kwa kuiangalia Wizara hii kwa jicho la huruma.  Mheshimiwa Rais akiwa ndiye Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama ameona umuhimu wa kuisaidia Wizara hii ili iweze  kukabiliana na vitendo vyote vya uhalifu.  Pamoja na ukweli kuwa safari bado ni ndefu, lakini namshukuru sana kwa hatua zinazochukuliwa.  Aidha, namshukuru Waziri wa Fedha na Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji kwa kuyaelewa matatizo ya Wizara yangu na kuendelea kuyapatia ufumbuzi kulingana na uwezo uliopo.

 

52. Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kufanya mabadiliko ya uongozi wa juu wa Jeshi la Polisi, ambapo aliteuliwa Inspekta Jenerali mpya na Makamishna, hatua mbali mbali zimechukuliwa kwa lengo la kuimarisha utendaji kama ifuatavyo:-

 

a.               Kufanya mabadiliko ya Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa.  Aidha, baadhi ya Wakuu wa Polisi Usalama Barabarani wa Mikoa na Wakuu wa Polisi wa Wilaya pia wamebadilishwa.

 

b.              Kuanzishwa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, ambapo Wilaya za Kinondoni, Ilala na Temeke zimepewa hadhi ya Mikoa Kipolisi ili kuongeza ufanisi, kwani Jiji la Dar es Salaam lilikuwa linaongoza kwa matukio ya uhalifu.

 

c.     Kutangazwa hadharani namba za simu za IGP, Makamanda wa Polisi wa Mikoa, Wakuu wa Upelelezi wa Mikoa na Wakuu wa Upelelezi wa Wilaya kumewezesha upatikanaji wa taarifa nyingi za uhalifu kutoka kwa wananchi.  Matukio mengi ya uhalifu yalizuiwa kutokea kutokana na Polisi kupata taarifa mapema.

d.     Uwekaji wa masanduku ya maoni nje ya Vituo vya Polisi umewezesha upatikanaji wa taarifa muhimu za uhalifu.

 

e. Uhamasishaji wa wananchi kwa njia ya mazungumzo na viongozi wa Serikali za Mitaa, wananchi na vikundi binafsi vya ulinzi ili kuwaelimisha juu ya utoaji taarifa za uhalifu.

 

f.     Kufanya misako ya kushtukiza na yenye malengo maalum baada ya kupata taarifa za uhalifu ili kuzuia uhalifu usitokee.

 

g.     Kuwasaka wafadhili wa uhalifu, ambapo baadhi yao wanaotuhumiwa wameshafikishwa mahakamani na zoezi linaendelea.

 

h.     Kila Mkoa unaendelea kuimarisha kitengo cha Intelijensia ambacho kazi yake ni kutafuta na kukusanya taarifa za uhalifu kwa nia ya kuzuia, kufuatilia, kuwatambua na kuwakamata watu wanaofanya uhalifu huo.

 

i.      Kuimarisha ulinzi katika Mabenki na Maduka ya fedha nchini.

 

j.      Kuwahamasisha wananchi wanaosafirisha fedha nyingi kutumia huduma ya Polisi ya kusindikiza fedha.

 

k.      Kuongeza juhudi katika upelelezi wa matukio ya uhalifu yaliyotokea hasa ya ujambazi wa kutumia silaha.  Jitihada hizo ambazo ziliwezesha Polisi kufika hata nchi za jirani kuwafuatilia wahalifu, zimeleta mafanikio makubwa ambapo wahalifu wengi wamekamatwa na mitandao yao kuvunjwa.

 

 l.     Kuimarisha doria za miguu, magari, pikipiki na operesheni mbalimbali.

 

m.    Kufanya ukaguzi mara kwa mara kwenye nyumba za kulala wageni na maeneo yanayohisiwa kuwa maficho ya wahalifu.

 

n.   Kuwapa askari, hasa wa Upelelezi, mafunzo  ya  ndani  na  nje ya nchi kwa lengo la kuwaongezea ujuzi.

 

o.      Kufanya   uchunguzi   wa   kuwabaini askari wote wa Polisi na wa vyombo vingine vya ulinzi na usalama wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu kwa lengo la kuwachukulia hatua za kisheria.

 

p.     Kusindikiza    magari    ya    abiria     kwenye

maeneo ambayo ni hatari kama vile Milima ya Kitonga Mkoani Iringa,  Mapori ya Biharamulo Mkoani Kagera na Mlima wa Koro (Kondoa) Mkoani Dodoma.

 

q.      Kuimarisha ushirikiano wa vyombo vya dola vyote nchini na kupanga mikakati ya pamoja ya kupambana na uhalifu nchini.

 

r.    Kuimarisha    ushirikiano    wa    Kimataifa na kikanda  wa  Kipolisi   kwa kupitia INTERPOL,   SARPCCO, EAPCCO, EAC na kuimarisha ushirikiano na nchi nyingine kwenye ukanda wetu na hata duniani kote.

 

MATARAJIO YA WANANCHI KWA JESHI LA POLISI

 

53.   Mheshimiwa Spika, baada ya mabadiliko ya uongozi wa juu wa Jeshi la Polisi, wananchi na wadau wengine wamejenga imani na kuwa na matarajio makubwa kwa Jeshi la Polisi.  Kutokana na hali hiyo, Jeshi la Polisi linajitahidi kufanya yafuatayo:

 

  a. Kuboresha Huduma ya Polisi Kwa Wananchi

 

54.   Mheshimiwa Spika, utendaji kazi wa Polisi usiojali na kuheshimu haki za raia, Polisi kushindwa kushughulikia kero za wananchi kikamilifu na ukiukwaji wa haki za binadamu ni miongoni mwa sababu zinazowafanya wananchi kukosa imani na Jeshi hilo na hivyo kuacha kutoa ushirikiano. Kufuatia hatua mbali mbali zinazochukuliwa na Jeshi hivi sasa kupambana na uhalifu nchini, wananchi na wadau wengine wanatarajia huduma ya Polisi kwao itaboreshwa. Hivyo, kazi kubwa ya Jeshi la Polisi itakuwa ni kuboresha huduma kwa wananchi.

 

 b. Jeshi la Polisi Kuwa Karibu Zaidi na Wananchi

 

55.   Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia kwamba wahalifu ni watu waishio miongoni mwa wananchi, na kwamba waathirika wakubwa ni wananchi wenyewe, raia wapenda amani na watiifu wa sheria wanatarajia kwamba Jeshi la Polisi litashirikiana nao kwa karibu zaidi katika kukabiliana na uhalifu.  Katika ushirikiano huo, Jeshi la Polisi litazingatia utunzaji wa siri za raia wema wanaotoa taarifa za kuisaidia Polisi.  Askari watakaobainika kuvujisha siri za raia hao watachukuliwa hatua kali za kinidhamu.

 

c.     Kufanya Kazi kwa Kuzingatia Sheria na Haki za   Binadamu

 

56.   Mheshimiwa Spika, wananchi wanatarajia Jeshi la Polisi kufanya kazi kwa ukweli, uwazi na kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo. Pia wananchi wanatarajia Polisi kujiepusha  na vitendo vyovyote vya ukiukaji wa haki za binadamu, kama vile kutumia nguvu ya ziada kwa mtuhumiwa, kuwabambikiza watu kesi, kuchelewesha upelelezi wa kesi, kuwanyima watu dhamana ya Polisi hata kwa kesi ndogo na kuepuka itikadi na ushabiki wa vyama vya siasa.  Aidha, askari Polisi wanatakiwa kujiepusha na kuwakamata wananchi siku za mwisho wa wiki bila ya sababu za msingi na kuwashikilia watu hasa wafanyabiashara hata pale wanapoonyesha vielelezo vyote vya biashara zao. 

 

57.   Mheshimiwa Spika, napenda kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara yangu kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi imeanza kuchukua hatua madhubuti za kuwasimamia  askari kwa lengo la  kupunguza  vitendo hivi na wale watakaobainika kukiuka, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao, ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi.

 

d.     Polisi Kujiepusha na Vitendo Vyote vya Rushwa

 

58.   Mheshimiwa Spika, wananchi wanawatarajia askari Polisi wa ngazi zote kujiepusha na vitendo vyote vya rushwa, hasa askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani na askari wa upelelezi. Polisi wanatarajiwa kuwa mstari wa mbele kupambana na vitendo vya rushwa, na siyo kuonekana wanashiriki kwa namna moja au nyingine.

 

e.     Askari Kufika Mapema Eneo la Tukio

 

59.   Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa ya Wizara hii ni kuwahakikishia Watanzania usalama wao pamoja na mali zao. Katika hili, matarajio ya wananchi ni Polisi kufika mapema eneo la tukio. Sanjari na hili, wananchi wanatarajia kwamba Polisi watayashughulikia matukio yote ya uhalifu kwa ufanisi kwa kuwakamata na kuwafikisha mahakamani wahalifu wote wanaohusika. Inapotokea askari wamechelewa kufika kwenye tukio na hakuna wahalifu wanaokamatwa kuhusiana na tukio hilo, wananchi hubaki na tafsiri tofauti, ikiwa ni pamoja na tafsiri kwamba Polisi imeshindwa kazi au Polisi nayo inashiriki katika vitendo  vya uhalifu.

 

 

MATARAJIO YA WIZARA

 

60.   Mheshimiwa Spika, ili Jeshi la Polisi liweze kukidhi matarajio ya Serikali na ya wananchi, lazima liwezeshwe. Serikali kwa upande wake, italipatia Jeshi la Polisi vitendea kazi vya kutosha na kuboresha mazingira ya utendaji kazi.  Wananchi kwa upande wao, wanatarajiwa kulipatia Jeshi la Polisi ushirikiano mkubwa, hasa wa kuwapatia taarifa sahihi na kamilifu za uhalifu na wahalifu zitakazotumika kukabiliana na uhalifu. Wananchi  pia wanatarajiwa kushiriki kikamilifu katika kutafuta mbinu za kukabiliana na uhalifu katika maeneo yao.  Pande zote mbili ni lazima sio tu zinapaswa kuwa na mawasiliano mazuri bali pia zinapaswa kuaminiana kwa kiwango kikubwa katika kufanikisha azma hii.  Aidha, mambo yafuatayo yanatarajiwa kufanywa na Wizara:-

 

 

 

a.     Kuandaa Sera ya Usalama wa Raia

 

61.   Mheshimiwa Spika, Wizara ya Usalama wa Raia inatarajia kuanza mchakato wa kuandaa Sera ya Usalama wa Raia ambayo itaongoza pamoja na mambo mengine, mahusiano ya kiutendaji kati ya Wizara na Jeshi la Polisi, wananchi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Mahakama, Magereza, Usalama wa Taifa, Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Taasisi ya Kuzuia Rushwa, Uhamiaji, Idara ya Forodha, Taasisi zisizo za Kiserikali, Vyuo, Sekta Binafsi, Makampuni Binafsi ya Ulinzi, pamoja na mashirikisho ya Kipolisi ya Kikanda na Kimataifa.

 

b. Kuangalia Upya Mfumo wa Jeshi la Polisi

 

62. Mheshimiwa Spika, baada ya muundo wa Wizara ya Usalama wa Raia kuidhinishwa, hatua inayofuata ni kuangalia upya muundo na mfumo wa Jeshi la Polisi. Lengo ni kuuboresha mfumo wa Jeshi la Polisi ili kuliwezesha kukabiliana  na uhalifu wa sasa kulingana na  mabadiliko ya hali ya uchumi, jamii na utamaduni nchini na duniani kwa jumla ambapo sasa sera za utandawazi zinatawala dunia. 

 

63.   Mheshimiwa Spika, upo mpango wa kupunguza zaidi watendaji wanaoripoti moja kwa moja kwa Inspekta Jenerali ili kutawanya madaraka katika kanda kwa ajili ya kupunguza urasimu, kuharakisha maamuzi na kubwa zaidi ni kumpa muda wa kutosha Inspekta Jenerali wa Polisi  kufikiria maandalizi ya mipango ya mikakati ya kuboresha utendaji wa Jeshi la Polisi.  Kanda ya Dar es Salaam ni kama kanda ya majaribio; itakapofanya vizuri, zitaanzishwa Kanda nyingine na Makamanda wa Mikoa wa Kanda husika wataripoti kwa Kamishna wa Kanda.

 

64.   Mheshimiwa Spika, hivi sasa idadi ya Makamanda wanaoripoti moja kwa moja kwa Inspekta Jenerali ni 35, ikijumuisha Makamanda wa Mikoa na Vikosi.  Huu sio mfumo mzuri wa kiutendaji. Watateuliwa Wataalamu (Consultants) kuchambua masuala haya yote na kutupa mapendekezo ya muundo na mfumo mpya wa Jeshi la Polisi.

 

65.   Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inakusudia pia kulifanyia maboresho Jeshi la Polisi ili muundo na mfumo wake uwe imara kutoka ngazi ya Makao Makuu hadi ngazi ya Kituo cha Polisi.  Hii ni pamoja na kugawa madaraka na raslimali husika Mikoani, Wilayani na Vituoni na kukasimu madaraka ya uongozi kwa watendaji bila kuathiri udhibiti ili kuongeza ufanisi zaidi.

 

c.     Kuzipitia Upya Sheria na Kanuni za Jeshi la Polisi

 

66. Mheshimiwa Spika, baadhi ya sheria zinazoongoza Jeshi la Polisi zilitungwa wakati wa ukoloni. Sheria hizo zilitungwa kukidhi mahitaji ya ulinzi na usalama wa wakoloni.   Baadhi ya sheria na kanuni hizo hivi sasa zimepitwa na wakati na kuhitaji marekebisho kwani hazijazingatia kikamilifu Haki za Binadamu na hata za askari wa kawaida ndani ya Jeshi lenyewe. Lengo ni kuziboresha ili ziendane na wakati na zisikwamishe kwa namna moja au nyingine utekelezaji wa majukumu ya Polisi.

 

67.   Mheshimiwa Spika, taratibu, kanuni na sheria zinazokusudiwa kupitiwa upya ni Taratibu za Kudumu za Polisi (Police General Orders (PGO), Kanuni za Utumishi za Jeshi la Polisi (Police Force Service Regulations), Muundo wa Utumishi (Scheme of Service), Muundo wa Kamisheni ya Polisi. Aidha, utawasilishwa Bungeni muswada wa Sheria kwa lengo la kuibadilisha sheria ya sasa ya Jeshi la Polisi yaani Police & Auxilliary Services Act na kutengeneza sheria ya Polisi yaani ‘Police Act’.

 

68. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imekuwa ikipokea malalamiko mengi kutoka kwa askari wanaostaafu wakilalamikia utaratibu wa malipo ya Bakshishi (Gratuity).  Pamoja na ukweli kwamba askari huchagua kwa hiari yake kuingia utaratibu wa Pensheni au Bakshishi, inaelekea askari hapati elimu ya kutosha ili kumwezesha kuchagua vizuri utaratibu unaomfaa. Kwa utaratibu uliopo ukishachagua kuingia katika Pensheni au Bakshishi huruhusiwi tena kubadilisha.  Hivyo, kanuni zinazoongoza taratibu za malipo ya Bakshishi na Pensheni zitapitiwa upya ili kuona uwezekano wa kuweka utaratibu mmoja

 

d. Kuifanyia Maboresho Idara ya Upelelezi

 

69. Mheshimiwa Spika, Serikali ipo kwenye mchakato wa kuhamisha shughuli za uendeshaji mashtaka kutoka Jeshi la Polisi na taasisi nyingine zilizokuwa zinafanya kazi hiyo na kuzipeleka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini. Ili kuweza kufanikisha mchakato huo, Idara ya Upelelezi inahitaji kufanyiwa maboresho ili iweze kuhimili mabadiliko hayo.  Maboresho hayo yatakuwa na lengo la kuweka mahusiano mazuri ya kiutendaji kati ya ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini.

 

70.   Mheshimiwa Spika, maboresho hayo pia yatalenga kumpatia Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini uwezo wa kuratibu shughuli zote za upelelezi wa makosa ya jinai zinazofanywa na taasisi mbali mbali ili hatimaye iweze kuwa rahisi kupata takwimu zote na kumbukumbu sahihi za makosa ya jinai nchini.  Aidha, utaratibu huu utamwezesha Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai kuandaa taratibu zinazofanana za upelelezi zitakazotumiwa na taasisi zote (Standard Operating Procedure).

 

71.   Mheshimiwa Spika, sanjari na hayo, Wizara yangu inatarajia kuigawa Idara ya Upelelezi katika vitengo kulingana na utaalamu wa makosa mbali mbali ya jinai.  Kwa mfano, vitaundwa vitengo vya Makosa dhidi ya Binadamu, Makosa dhidi ya Mali, Uhalifu wa Kimataifa (Transnational/Cross Border Crimes), Makosa ya Uhujumu Uchumi (Serious Economic Crimes).   Kitengo cha Intelijensia pia kitaimarishwa ili kiweze kutoa mchango mkubwa katika uzuiaji wa uhalifu.

 

e.     Kuboresha Utendaji Kazi wa  Askari wa  Kikosi cha Usalama   Barabarani

 

72. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia kwamba ajali za barabarani bado ni kero kubwa na tishio kwa maisha ya wananchi, na kwa kuelewa madhara ya malalamiko ya vitendo vya rushwa dhidi ya askari wa usalama barabarani, Jeshi la Polisi limeanzisha utaratibu wa usimamizi madhubuti wa askari wa usalama barabarani. Kwa sasa Wakuu wa Polisi wa Vituo na Wilaya wanakofanya kazi askari hawa watawajibika kuwasimamia moja kwa moja tofauti na zamani ambapo usimamizi ulikuwa unafanywa na Makamanda wa Kikosi hicho.

 

73.   Mheshimiwa Spika, vile vile Kikosi cha Usalama Barabarani hivi sasa kinafanyiwa mageuzi makubwa.  Sehemu ya mageuzi hayo inahusu maandalizi ya mtaala mpya, ambapo askari watakapoenda chuoni siku zijazo, watakuwa wanajifunza pia Sheria ya Usalama Barabarani na hivyo kila askari atakuwa na elimu hiyo.  Lengo ni  kuwafanya askari wote kufahamu kazi za Usalama Barabarani ili pale inapolazimu kuweza kuwabadilisha bila kulazimika kuwapeleka kwanza chuoni. 

 

74.   Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Makamanda wa Polisi wa Mikoa wamepewa mamlaka ya kuwabadili askari wa Usalama Barabarani wakati wowote watakapoona inafaa bila kulazimika kuwasiliana  kwanza na Makao Makuu.  Hivyo, hakutakuwa na askari wa kukaa katika kikosi hicho mpaka anastaafu, bali askari hao watakuwa wakibadilishwa mara kwa mara kulingana na mahitaji.

75.   Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatarajia kupendekeza marekebisho ya baadhi ya Sheria za Usalama Barabarani, ikiwemo Sheria ya kutoa leseni, ambapo sasa madereva wa magari makubwa, hasa magari ya abiria watalazimika kujaribiwa upya ili kupima uwezo wao wa kuendelea  kubeba roho za watu.  Aidha, sifa zinazotakiwa ili mtu aruhusiwe kuendesha magari ya abiria zimepitiwa upya na leseni daraja C inayoruhusu madereva kuendesha magari yote, sasa itatumika kwa kuendesha magari ya abiria tu. Aidha, tunatarajia pia kubadili leseni za udereva ili zifanane na za nchi za SADC zenye mfano wa kadi za Benki ambazo siyo rahisi kughushiwa.

 

76.   Mheshimiwa Spika,  maandalizi ya kutunga sheria ya ukaguzi wa lazima wa magari (Mandatory Vehicle Inspection) yanaendelea. Vile vile, faini na adhabu kwa makosa ya usalama barabarani zinatazamwa upya kwa lengo la kuziongeza ili kuwadhibiti madereva wasio waangalifu.  Aidha Wizara inatarajia kupendekeza kutungwa kwa sheria zifuatazo :  Sheria ya kuwashitaki wamiliki wa magari, madereva, makondakta na abiria wanaozidi kwenye magari ya abiria ; Sheria ya kuwaadhibu madereva na makondakta wanaonyanyasa wanafunzi na watu wengine wasio na uwezo; Sheria ya kuzuia magari kuweka vioo vya giza (tinted) ; Sheria ya kuwazuia madereva kuendesha magari wakati wanaongea na simu za mkononi na Sheria ya kuruhusu taasisi za Serikali, Makampuni binafsi na magereji yenye uwezo kukagua magari kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kudhibiti magari mabovu.

 

f.     Kuanzisha Kikosi Maalum kwa Ajili ya Ulinzi na     Usalama Kwenye Vituo Vya Kuingilia Nchini

 

77.  Mheshimiwa Spika, kwa kutambua kuongezeka kwa kasi kwa tatizo la wahamiaji haramu nchini na hali ya vitendo vya uhalifu vinavyofanywa na wahamiaji hao, na vile vile kwa kuelewa kwamba upo uwezekano wa biashara haramu ya watu (Human Trafficking) kushamiri hapa nchini, Wizara inaangalia uwezekano wa kuanzisha Kikosi Maalum ndani ya Jeshi la Polisi kwa ajili  ya kuboresha ulinzi na usalama kwenye vituo vyote vya kuingilia nchini.  Aidha Wizara inaangalia sababu zilizofanya Jeshi la Polisi kujiondoa kwenye ulinzi wa bandari zetu na kuachia Mamlaka ya Bandari jukumu hilo.  Lengo ni kurudisha ulinzi wa Bandari kwa Jeshi la Polisi kwa vile huo ni mlango wa kuingilia nchini kama ilivyo Viwanja vya Ndege na Mipaka ya nchi kavu.

 

g.     Kuanzisha Kikosi Maalum kwa Ajili ya Ulinzi wa Watalii

 

78.   Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa sekta ya utalii  katika kuchangia Pato la Taifa na kwa kuzingatia hali ya kuongezeka kwa vitendo vya uhalifu dhidi ya watalii, Wizara inaangalia uwezekano wa  kuanzisha Kikosi Maalum ndani ya Jeshi la Polisi ambacho jukumu lake kubwa  litakuwa ni kuimarisha  ulinzi na usalama wa watalii, wanaotembelea nchi yetu, Bara na Visiwani. Mawasiliano yanaendelea hivi sasa baina ya Wizara yangu na Wizara ya Maliasili na Utalii na wadau wengine muhimu katika suala hili.  Kwa upande wa Zanzibar, Wizara yangu inaendelea na mazungumzo na Wizara ya Biashara, Uwekezaji na Utalii kuhusu suala hili.

 

h.     Kuanzisha Utaratibu wa Polisi Jamii

 

79.   Mheshimiwa Spika,  kwa kuzingatia ukweli kwamba wahalifu wa kila namna, yakiwemo majambazi yanayotumia silaha ni watu waishio miongoni mwa jamii, utaanzishwa utaratibu wa Polisi Jamii (Community Policing).  Polisi Jamii  ni utaratibu wenye lengo la kuweka mazingira ya ushirikiano wa dhati baina ya Polisi na wananchi.  Katika utaratibu huu Jeshi la Polisi litasambaza huduma zake kwa jamii kwa kutumia askari Polisi wa Kata au Shehia kwa upande wa Zanzibar.  Askari huyu atapangwa katika kata/shehia kwa utaratibu wa kudumu na atakuwa kichocheo cha mabadiliko ndani ya kata/shehia hiyo.

 

80.   Mheshimiwa Spika, kwa kumpanga askari  Polisi katika kata/shehia kama sehemu yake ya kazi, Jeshi la Polisi litakuwa na mtazamo wa muda mrefu wa kutatua matatizo ya uhalifu katika kata/shehia hiyo badala ya kusubiri kutatua tatizo moja moja  kila linapojitokeza.  Aidha, kwa utaratibu huu, raia wa kawaida atakuwa na kauli katika uwekaji wa malengo ya Polisi badala ya kuwa mpokeaji tu wa maelekezo kutoka Polisi juu ya namna ya kuzuia uhalifu.

 

81.   Mheshimiwa Spika,  lengo  ni kuondoa dhana iliyokuwepo kuwa Jeshi la Polisi ni chombo cha mabavu, badala yake kuwa chombo rafiki na  cha utoaji huduma.  Hili litawezekana kwa kuwa na taratibu zilizobuniwa makusudi kuruhusu mashauriano  baina ya Polisi na wananchi. Taratibu hizi zitawawezesha wananchi kuwaarifu Polisi kuhusu kuridhika au kutoridhika kwao na huduma ya Polisi.  Kwa njia hii uwajibikaji wa Polisi kwa wananchi utaongezeka.  Aidha, utaratibu huu utasaidia sana kupunguza kero ya rushwa ya Polisi kwa sababu Polisi Kata/Shehia ambaye ni sehemu ya jamii ya Kata/Shehia husika inatarajiwa hataweza kuwadai rushwa wanajamii wenzake ili atoe huduma ya Polisi maana mipango yenyewe ya kazi wanapanga wote. 

 

82.   Mheshimiwa Spika, ili utekelezaji wa utaratibu wa Polisi Jamii (Community Policing) uweze kufanyika kwa mafanikio, Wizara yangu inaandaa mkakati maalum kwa lengo hilo.  Mkakati huo pia utaelekeza namna ambavyo Polisi Kata atashirikiana na Vikundi vya Ulinzi wa Jadi katika utekelezaji wa utaratibu wa Polisi Jamii.  Suala la kutoa elimu ya Polisi Jamii kwa wananchi na Polisi wenyewe nalo litapewa kipaumbele.  Elimu hii ni muhimu sana ili kuondoa migongano baina ya wananchi na Polisi ambayo inaweza kujitokeza wakati wa utekelezaji.  

 

i.      Kushirikiana na Idara Nyingine za Serikali

 

83. Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mchango wa vyombo vingine vya dola katika suala zima la ulinzi na usalama wa raia na mali zao. Hivyo,  Wizara inakusudia  kukuza na kuendeleza ushirikiano uliopo hivi sasa baina ya Jeshi la Polisi na vyombo vingine vikiwemo Idara ya Usalama wa Taifa, Taasisi ya Kuzuia Rushwa, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Jeshi la Magereza, Idara ya Uhamiaji, Mamlaka ya Mapato Tanzania,  pamoja na wadau wengine muhimu, hasa katika ubadilishanaji wa taarifa za kiintelijensia na kufanya operesheni za pamoja.

 

 

 

 

j.     Kutoa Ushauri wa Kiusalama Kwa Taasisi za

Fedha

 

84. Mheshimiwa Spika, ni jukumu la Jeshi la Polisi kutoa ushauri wa kiusalama kwa taasisi mbalimbali za kibiashara kama vile mabenki juu ya namna bora ya kuimarisha mifumo ya ulinzi katika maeneo yao.  Kwa  hivi sasa Jeshi la Polisi linaendelea kuwasiliana na Benki Kuu kuhusu kuweka utaratibu wa kisheria wenye lengo la kuwalazimisha wamiliki wa benki na taasisi za fedha nchini kuweka mifumo ya kisasa ya  ulinzi katika benki zao kama CCTV Cameras kwa lengo la kudhibiti uporaji wa fedha katika taasisi hizo.

 

k.     Taratibu za Ajira

 

85.  Mheshimiwa Spika, kwa kutambua kuwepo kwa mapungufu katika zoezi la ajira ya askari Polisi, Wizara kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi inachambua taratibu za ajira zinazotumika sasa ili  kubuni utaratibu bora zaidi wa ajira.

 

l.      Upandishwaji Vyeo

 

86.  Mheshimiwa Spika, upandishwaji vyeo ndani ya Jeshi la Polisi unapaswa kufanyika kwa mujibu wa maelekezo yaliyopo kwenye Taratibu za Kudumu za Polisi (Police General Orders).  Hata hivyo, kwa kuwa yamejitokeza malalamiko miaka ya hivi karibuni kuhusiana na  upandishwaji vyeo hasa kwa askari wa vyeo vya chini, Wizara kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi inaangalia upya utaratibu uliopo, iwapo bado unafaa au umepitwa na wakati ili askari wapandishwe vyeo kulingana na sifa na utendaji kazi.

 

m.    Msongamano wa Wafungwa na Mahabusu

 

87. Mheshimiwa Spika, kwa kuelewa tatizo la msongamano wa mahabusu katika magereza yetu na kwa kutambua kwamba msongamano huo wakati mwingine unasababishwa na utendaji usioridhisha wa baadhi ya askari wa Jeshi la Polisi, Makamanda wa Polisi wa Mikoa wameelekezwa kushirikiana na wenzao wa Jeshi la Magereza katika kuendesha zoezi la kukagua magereza kwa lengo la kuelewa sababu za  watuhumiwa kuendelea kukaa ndani na ucheleweshaji wa kesi zao.

 

88.   Mheshimiwa Spika, itakapodhihirika hakuna sababu za msingi za kuendelea kukaa magerezani, taratibu za kisheria zitafuatwa  ili mahabusu hao waachiwe ama kwa dhamana au kwa kesi zao kumalizika haraka iwezekanavyo. Zoezi hili litaenda sanjari na uendeshaji wa mara kwa mara wa vikao vya Kamati za Kusukuma Kesi Nchini. 

 

89.   Mheshimiwa Spika, Wizara yangu itawasiliana na Wizara za Katiba na Sheria, na Mambo ya Ndani ya Nchi kwa lengo la kuweka utaratibu ambao Maafisa wa Polisi, Mawakili wa Serikali wakiongozwa na Majaji Wafawidhi wa Kanda husika na Mahakimu Wakazi wataenda magerezani kuwasikiliza mahabusu na kufanya uamuzi wa haraka kwa mujibu wa sheria.  Lengo ni kushirikiana na wizara hizo kupunguza msongamano wa mahabusu  magerezani, hasa kwa kesi ndogo ndogo. 

 

n.     Udhibiti wa Silaha Ndogo Ndogo

 

90.     Mheshimiwa Spika, ujambazi wa kutumia silaha nchini bado ni tatizo kubwa ambalo linachangiwa kwa kiasi kikubwa na tatizo la kuzagaa silaha. Hivyo, pamoja na juhudi na mikakati mingine, Jeshi la Polisi  litazikagua, kuziorodhesha na kuzisajili upya silaha zote za kiraia nchini ili kuhakiki umiliki na matumizi yake.   Zoezi kama hili pia litafanyika kwa silaha ndogo ndogo zinazomilikiwa na Taasisi/Idara za Serikali ili hatimaye ziwepo kumbukumbu za silaha zote ndogo ndogo nchini na udhibiti wake uweze kuwa rahisi. 

91.     Mheshimiwa Spika,  sanjari na uhakiki huu wa miliki ya silaha na risasi, yanafanyika mapitio ya Sheria ya umiliki wa silaha  ili hatimaye ifanyiwe marekebisho kwa lengo la kuongeza udhibiti wa silaha na risasi.   Katika marekebisho hayo, suala la utengenezaji na miliki ya Magobore litaangaliwa kwa lengo la kuyapiga marufuku. Uzoefu umeonyesha kwamba watengenezaji na wamiliki wanakiuka taratibu za utengenezaji, umiliki na matumizi ya silaha hizo.  Kwa mfano, sasa hivi Magobore mengi yanayotengenezwa yanatumia risasi za kisasa kitu ambacho ni kinyume cha sheria.  Vile vile sheria za Kimataifa zimekwishapiga marufuku utengenezaji na umiliki wa silaha  za aina hii.

 

92.     Mheshimiwa Spika, udhibiti na utaratibu wa magobore unafanywa na Halmashauri za Wilaya/Manispaa chini ya sheria ndogo ya ‘Arms and Ammunition Native Authorities Regulations’ iliyo chini ya Sheria za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.   Chini ya sheria hii, Halmashauri za Wilaya ndizo zinazotoa leseni za kutengeneza magobore, kuweka alama au namba kwenye magobore yanayotengenezwa na kuwatoza kodi watengenezaji na wamiliki wa magobore. 

 

93.     Mheshimiwa Spika, kazi hii itaenda pamoja na juhudi za makusudi za kuendesha misako ya mara kwa mara kuhakikisha kuwa silaha zinazomilikiwa kinyume cha sheria zinakamatwa pamoja na wamiliki wa silaha hizo kama moja ya mikakati ya kupunguza ujambazi nchini.

 

o.     Ushirikishwaji wa Sekta Binafsi

 

94. Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuzuia uhalifu nchini, Jeshi la Polisi linatarajia kujenga ubia na sekta binafsi. Lengo ni kuwahamasisha wafanya biashara wakubwa, makampuni binafsi, taasisi na mashirika mbalimbali kuchangia na kutunisha mfuko wa Ulinzi wa Umma ambao tayari umeshaanzishwa na Jeshi la Polisi. Hili limeanza kufanyika kwa Benki ya CRDB kuchangia fedha kwa ajili ya kufungua akaunti Makao Makuu ya Polisi pamoja na Mikoani kwa ajili hiyo.

 

95. Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Jeshi la Polisi limepokea michango mbalimbali ya vitendea kazi na fedha taslimu toka kwa Kampuni za Ulinzi za Ultimate Security Ltd, Vodacom, Kampuni ya Simu ya Alphatel, Umoja wa Kampuni za Ulinzi Nchini, Riki Hill Hotel, Kampuni ya CMC Motors, Kampuni ya Sigara nchini (TCC)  pamoja na wafanyabiashara mbalimbali.   Napenda kutumia fursa hii kuyashukuru makampuni haya na watu wote waliochangia.  Ninatoa wito kwa sekta binafsi kwa ujumla, kuchangia mfuko huo kwa lengo la  kuunganisha nguvu za Serikali pamoja na za sekta binafsi katika kukabiliana na uhalifu nchini.

 

96.   Mheshimiwa Spika, vitendea kazi vilivyopokelewa ni pamoja na magari, pikipiki, simu za mkononi na simu za upepo. Mawasiliano yatafanyika na taasisi zinazohusika ili kuandaa taratibu madhubuti za matumizi ya fedha zinazopatikana kwenye mfuko huu.

 

97.   Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu imekuwepo dhana kwamba kazi ya kudhibiti uhalifu na ujambazi ni jukumu la Serikali au Jeshi la Polisi peke yake.  Mtazamo huu siyo sahihi.  Kudhibiti uhalifu, na hasa wakati huu wa utandawazi ni lazima kuishirikisha sekta binafsi, wafanyabiashara na wananchi wote kwa ujumla wao. 

 

98.   Mheshimiwa Spika, Mzee Nelson Mandela alipokuwa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Afrika Kusini aliwahi kusema, na ninamnukuu :

 

 

 

«The business sector could make a valuable contribution in supporting Government in combating crime and the causes of crime by transfer of knowledge and the development of skills and capacity through a public - private partnership »  mwisho wa kunukuu.

 

 

99.   Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi limefungua milango kwa sekta binafsi na wananchi na kuwa wazi katika kuandaa mikakati ya ushirikiano wa hali na mali baina yao ili kwa pamoja watokomeze vitendo vya uhalifu. Tayari baadhi ya Mikoa kama vile Dar es Salaam, Arusha na Mbeya imekwishajitokeza kuchangia juhudi za Polisi.  Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Mikoa hiyo.   Natoa wito kwa Wakuu wa Mikoa mingine kushirikiana na sekta binafsi kuanzisha programu ya kupambana na wahalifu na hivyo kuwa karibu na Wakuu wa Polisi wa Mikoa yao katika kubuni mikakati na kuitekeleza.

 

100. Mheshimiwa Spika, ili kuufanya utaratibu huu wa sekta binafsi kuchangia shughuli za Polisi uwe endelevu na wa kisheria, Wizara yangu kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi inawasiliana na Wataalamu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili waweze kushauri namna ya kuufanya mfuko huu kuwa endelevu na wa kisheria.  

 

p.     Udhibiti wa Simu za Mkononi

 

101.  Mheshimiwa Spika, mawasiliano ya simu za mkononi yanachangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la matukio ya uhalifu nchini, kwa kuwa simu hizo zimerahisisha mawasiliano kufanyika wakati wowote, mahali popote na kwa haraka zaidi. Wahalifu wameweza kutumia njia hii ya mawasiliano na kufanikiwa kufanya uhalifu bila kugundulika kwa urahisi.

 

102. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imekwishaanza kushauriana na Mamlaka ya Mawasiliano Nchini pamoja na makampuni yote ya simu za mkononi, ili kuhakikisha unakuwepo udhibiti wa simu zote za mkononi, ambapo wamiliki wote wa simu watasajiliwa na kuondokana na utaratibu wa sasa wa kuuza namba za simu (line) kiholela. Utaratibu huu una lengo la kuweka kumbukumbu za wamiliki wote wa simu ili iwe rahisi kuwapata pindi wanapohitajika.

 

q.     Askari Polisi Kutokaa Katika Kituo Kimoja Muda Mrefu

 

103. Mheshimiwa Spika,  kazi za kupambana na  uhalifu na wahalifu zinahitaji kufanywa kwa  uadilifu mkubwa ili kuepuka uvujaji wa taarifa. Ili lengo hili lifanikiwe unahitajika mkakati utakaohakikisha kwamba askari Polisi hawakai kituo kimoja muda mrefu na kuzoeleka. Jeshi la Polisi litaendelea kufanya uhamisho mara kwa mara wa askari wote, ili kudumisha nidhamu na kuboresha utendaji kazi.

 

 

 

r.      Kuboresha Maslahi ya Askari

 

104. Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge na wananchi ni mashahidi wa juhudi kubwa zinazochukuliwa na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete katika kuboresha maslahi ya askari na kuwapatia vitendea kazi.  Kupitia Bunge lako Tukufu, napenda nimshukuru pia Mhe. Hawa Ghasia, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa kuliangalia suala la mishahara ya watumishi wa umma pamoja na Askari Polisi ambapo  mishahara yao imeongezwa.

 

105. Mheshimiwa Spika, kutokana na kipato kidogo cha askari Polisi, inawawia vigumu kukopa katika mabenki nchini kutokana na  riba kuwa  kubwa na kukosa dhamana za uhakika. Hivyo, askari Polisi hawana mahali popote wanapoweza kupata fedha za kujiendeleza kiuchumi. Aidha, mishahara na posho wanayolipwa askari bado haikidhi hali halisi ya mahitaji yao na familia zao.

 

106. Mheshimiwa Spika, ili kupunguza ukali wa maisha kwa askari, Maduka ya Polisi yenye utaratibu wa kuwakopesha askari mahitaji muhimu (Kantini) yatafufuliwa na kusimamiwa kwa karibu ili yaweze kutoa mikopo midogo midogo na huduma nyingine muhimu kwa askari na familia zao.  Aidha, Serikali itaendelea kuwadhamini askari na watumishi wengine wa Wizara kupata mikopo kutoka Benki kama vile CRDB, NMB, AZANIA BANCOP, BENKI YA POSTA  na makampuni binafsi, kama vile  TUNAKOPESHA Limited n.k.

 

107. Mheshimiwa Spika, ili kujenga utamaduni wa askari kujiwekea akiba kwa njia ya kuweka na kukopa, inatarajiwa kuanzishwa Chama cha Kuweka na Kukopa  (SACCOS) cha Wizara ambacho  askari Polisi watajumuika na watumishi wengine kukopa kwa masharti nafuu. Mikopo hii  itawasaidia askari kustaafu kwa heshima wakiwa na makazi yao na hali nzuri ya maisha.

 

108. Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuboresha maslahi ya askari, Serikali ilipandisha kiwango cha posho ya resheni kutoka Sh.28,000 kwa mwezi kuwa Sh.50,000.  Aidha, askari wanaidai Serikali Sh. bilioni 8.5 zikiwa ni stahili mbali mbali kama posho za safari nk. Baada ya mazungumzo kati yangu na Wizara ya Fedha, deni hili litalipwa  katika mwaka huu wa fedha ili kuondoa kero hiyo ya muda mrefu na askari hao kupata stahili zao.

 

109. Mheshimiwa Spika, zaidi ya askari 18,000 wa Jeshi la Polisi wanaishi nje au ndani ya makambi katika mazingira ya makazi yasiyofaa.  Baadhi ya askari wanaishi katika nyumba za kupanga uraiani.  Hali hii huathiri utendaji wao wa kazi kwa kiasi kikubwa. Jitihada zinafanyika ili kuhakikisha kwamba askari Polisi wote wanaishi kambini katika mazingira ya kuridhisha.  Wizara yangu inafanya mazungumzo na Mifuko ya  Fedha ya NSSF na PPF na Wizara ya Fedha  kwa lengo la kuanzisha mradi wa ujenzi wa nyumba za Polisi nchini kote.  Kwa kuanzia ujenzi utafanyika Dar es Salaam na Zanzibar.

 

110. Mheshimiwa Spika, katika kujali afya za askari, hivi sasa yanafanyika mazungumzo na Bima ya Afya ili askari Polisi nao wajumuishwe katika mpango huo.  Awali askari  Polisi hawakuwa wamejumuishwa katika Bima ya Afya kama ilivyo kwa watumishi wengine.  Mawasiliano na Mfuko wa Bima ya Afya tayari yameshaanza na mweleko ni mzuri.  Baada ya taratibu zote kukamilika, askari Polisi na familia zao watanufaika kutokana na kupata matibabu wakati wote.

 

111. Mheshimiwa Spika, Mabaraza ya Askari ni mahali ambapo askari hupata fursa ya kueleza kwa viongozi wao, matatizo  mbali mbali yanayowakabili.  Hivyo, Makamanda wote wa Mikoa, Vikosi na Wilaya wameelekezwa kuhakikisha kwamba Mabaraza hayo yanafanyika ipasavyo kwa malengo yaliyokusudiwa.  Kila Kamanda wa Mkoa, Kikosi na Wilaya ahakikishe kwamba Baraza la Askari linafanyika walau mara moja kwa mwezi, na askari wanapata fursa kamili ya kueleza matatizo yao.

 

s.     Kuwapatia Mafunzo askari wa Vyeo vya Chini na Maofisa

 

112. Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imeandaa mpango wa mafunzo kazini ambapo askari watapatiwa mafunzo na mbinu mbali mbali za utendaji kazi.  Hivi sasa walimu wa mafunzo hayo wako chuoni CCP Moshi wakipata mafunzo ili nao waweze kuwafundisha askari wenzao waliopo kazini.  Aidha, unaandaliwa utaratibu ili walimu kutoka nje ya nchi waje kuwafundisha askari hapa  nchini ili kupata askari wengi zaidi wenye ujuzi.  Aidha, Wizara yangu imeandaa mpango wa mafunzo ya uongozi wa askari wa vyeo vya juu wakiwemo Makamanda wa Mikoa ili kuwaongezea ujuzi kuhusu dhana ya menejimenti na ufahamu wa sera za maboresho mbalimbali yanayofanyika hapa nchini.

 

113. Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha maendeleo ya Jeshi la Polisi Mikoani, Makamanda wa Mikoa watashirikishwa kikamilifu katika kupanga mipango na maboresho ya Mikoa yao na kushirikishwa katika mipango ya maboresho.  Matarajio ni kwamba, kila  Kamanda wa Mkoa ataweza kuandaa na kuitetea bajeti yake, ikiwa ni pamoja na kusimamia matumizi mazuri ya raslimali.

 

UTEKELEZAJI WA BAJETI YA 2005/06

 

114. Mheshimiwa Spika, naomba sasa kutoa tathmini ya utekelezaji wa malengo ya Jeshi la Polisi  katika kipindi cha mwaka 2005/06. Kwa ujumla utekelezaji wa malengo ya mwaka 2005/06 ulikuwa wa mafanikio. Hali halisi ya utekelezaji kwa maeneo muhimu ilikuwa kama ifuatavyo:

MAPATO

 

115. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi lilikadiria kukusanya mapato ya Serikali ya jumla ya Sh.4,247,940,000 kwa mwaka 2005/06.  Hadi kufikia Aprili, 2006, Jeshi lilikuwa limekusanya jumla ya Sh. 3,825,584,105 sawa na asilimia 90 ya lengo la mwaka mzima.  Hadi tarehe 31 Mei, 2006 Wizara ilivuka lengo lililowekwa kwa kiasi cha Shilingi 10,563,419.21. 

 

MATUMIZI

 

116. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi liliidhinishiwa jumla ya Sh. 102,161,080,300 kwa matumizi  ya kawaida na ya  maendeleo. Hadi kufikia Aprili, 2006, jumla ya Sh. 91,860,947,158 zilikwishatumika ikiwa ni sawa na asilimia 90 ya lengo la mwaka. Kati ya fedha hizo Tsh. 58,449,119,797 ni Matumizi Mengineyo, Tsh. 30,782,827,361 ni Mishahara na Tsh. 2,629,000,000 ni za Matumizi ya Bajeti ya Maendeleo.

 

117. Mheshimiwa Spika, hatua mbalimbali zimefikiwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na uendeshaji wa ofisi kutokana na fedha zilizotengwa katika bajeti ya 2005/06. Baadhi ya kazi zilizotekelezwa ni pamoja na:

       

a.           Ujenzi   wa   nyumba   124  kati ya 131   katika   Kambi ya   Kunduchi umekamilika.

 

        b.   Awamu ya kwanza ya ujenzi wa maabara ya kisasa ya uchunguzi (Forensic Laboratory) imekamilika.  Ujenzi wa awamu ya pili ulikwishaanza na bado unaendelea.

 

 c.   Ujenzi wa Kituo cha Polisi Katesh – Hanang

       upo katika hatua za mwisho.

 

d.    Ujenzi   wa   mabweni   mawili Kambi ya FFU

       Finya Pemba umekamilika.

 

        e.    Ukarabati  wa   mabweni  mawili  Chuo   cha     

Polisi Dar es Salaam umekamilika.

 

f       Mashua mbili za doria zimenunuliwa kwa ajili ya ukanda wa Bahari ya Hindi. Mashua moja iko Unguja na nyingine iko Dar es Salaam.

 

g.     Ujenzi    wa  Ofisi  za  Makamanda  wa  Polisi

wa Mikoa uko katika hatua mbali mbali  katika  mikoa ya Tabora, Ruvuma, Mwanza na Iringa.

 

h.    Ujenzi  wa  Kituo  cha  Polisi  Morogoro upo

hatua za mwisho.

 

         i.     Ukarabati   wa   Chuo   cha   Polisi   Zanzibar  

      unaendelea.

 

j.     Mafunzo ya askari wapya 2000 yameendeshwa na yalimalizika tarehe 21 Aprili, 2006. Mafunzo kazini yanaendelea kufanyika.

k.    Doria  na  Operesheni  mbalimbali  za  Polisi

       zilifanyika Kiwilaya, Kimkoa, Kitaifa na Kimataifa ambapo nchi tatu za Afrika Mashariki zilishiriki.

 

l.        Mawasiliano ndani ya Jeshi la Polisi yaliendelea kuimarishwa kwa ununuzi wa mitambo, simu n.k.

m.            Mkutano wa Maofisa wa Polisi ulifanyika       CCP Mjini Moshi kwa mafanikio makubwa, ambapo mikakati mbali mbali ya utendaji iliwekwa na sasa inaendelea kutekelezwa .

n.Kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola, Jeshi la Polisi lilifanikisha Uchaguzi Mkuu mwezi Desemba, 2005 kwa amani na utulivu.

VITA DHIDI YA UKIMWI

 

118. Mheshimiwa Spika, juhudi za kupambana na janga la ukimwi ndani ya Jeshi la Polisi zimeendelea kwa mwaka uliopita ikiwa ni pamoja na kuendesha semina tatu za uelimishaji zilizohusisha Maofisa, askari na wakufunzi. Juhudi hizi zitaendelezwa mwaka wa fedha wa 2006/07.

 

MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA

 

119. Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi limeendeleza  vita dhidi ya rushwa ndani na nje ya Jeshi.    Mafunzo mbali mbali kwa maafisa na askari wa kawaida yameendeshwa nchi nzima ambapo wadau mbali mbali wa mapambano dhidi ya rushwa walishirikishwa.  Hatua za kinidhamu zimeendelea kuchukuliwa dhidi ya askari/maofisa wanaojiingiza katika vitendo vya rushwa au kuvunja maadili ya kazi zao. 

 

120. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio yaliyotajwa, baadhi ya matatizo yaliyoathiri utekelezaji ni pamoja na haya yafuatayo:

 

a.     Ufinyu wa bajeti kwa kiasi kikubwa umeathiri utekelezaji wa mipango mbali mbali ya Jeshi  na hivyo kutofanya kazi kwa ufanisi na tija kama inavyotarajiwa.

 

       b.      Upungufu wa vitendea kazi kama vile magari, pikipiki, vifaa vya mawasiliano, mbwa, farasi, karatasi, vifaa vya kunasia sauti, Fomu mbali mbali, mfano PF.3 n.k.

 

c.     Upo upungufu mkubwa wa nyumba za kuishi askari. Zaidi ya askari 18,000 wanaishi nje ya Makambi katika nyumba za kupanga uraiani na wengine wanaishi katika mazingira magumu sana makambini.

 

       d.      Upo upungufu mkubwa wa vituo vya Polisi katika wilaya mbali mbali nchini, ambapo Wilaya 24 hazina kabisa vituo vya Polisi. Aidha, katika wilaya 73 Vituo vya Polisi vipo kwenye majengo chakavu, ambapo baadhi yalirithiwa  kutoka kwa  wakoloni.

 

e.     Upo upungufu wa askari unaochangiwa na askari kustaafu, kuacha kazi, kufukuzwa kazi, kufariki n.k.

 

121. Mheshimiwa Spika, changamoto zinazolikabili Jeshi la Polisi ni nyingi. Ni azma ya Serikali kuendelea hatua kwa hatua kulipunguzia matatizo na kulipatia mahitaji Jeshi la Polisi ili kulijengea uwezo wa kukabiliana na uhalifu nchini.

 

 

MALENGO YA MWAKA 2006/07

 

122. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2006/07, Wizara inatarajia kutekeleza majukumu yake kama ifuatavyo:-

 

a.                   Kuandaa Sera ya Usalama wa Raia na kusimamia utekelezaji wake.

 

b.                  Kuandaa Muundo mpya wa Jeshi la Polisi ikiwa ni pamoja na kutazama upya Sheria na Kanuni za Jeshi hilo.

 

c.                   Upatikanaji wa Ofisi na Makazi kwa Kanda Maalum ya Polisi Dar es Salaam.

 

d.                  Kuboresha maslahi ya askari

 

e.                   Kuboresha mazingira ya kufanyia kazi, upatikanaji wa vitendea kazi na miundombinu.

 

f.                    Kuwapatia askari mafunzo mbali mbali ya taaluma zao na ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Kuimarisha Vyuo vya Polisi vya Moshi, Dar es Salaam na Zanzibar na kuanza maandalizi ya ujenzi wa chuo cha CID Dodoma.

 

g.                   Kwa kushirikiana na Mifuko ya Fedha nchini na Makampuni kutoka nje ya nchi, itaanzishwa Programu ya ujenzi wa Makambi nchini kote, kwa kuanzia nyumba za Kambi ya Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam na Ziwani Zanzibar.

 

h.                   Jeshi la Polisi kuendelea kushiriki kikamilifu katika maboresho ya Sekta ya Sheria (Legal Sector Reform Programme).

 

i.                     Kuharakisha upelelezi wa kesi ili kuhakikisha kuwa haki inatendeka na hivyo kupunguza msongamano wa mahabusu katika magereza.

 

j.                    Kupambana na uhalifu kwa kubuni mbinu na mikakati ya kisasa maeneo ya mijini, vijijini, mipakani na katika maeneo ya kitalii.

 

k.                   Kuendeleza miradi ya maendeleo katika mikoa na Wilaya na ukarabati wa majengo ya Ofisi.

 

MWISHO

 

123. Mheshimiwa Spika, kabla ya kumalizia hotuba yangu naomba kutoa shukrani za pekee kwa Naibu Waziri wa Usalama wa Raia, Mheshimiwa Mohamed Aboud Mohamed, Katibu Mkuu wa Wizara ya Usalama wa Raia Bwana Bakari A. Mahiza, Inspekta Jenerali wa Polisi Bwana Said A. Mwema, Wakuu wa Idara, Makamanda wa Polisi wa Mikoa, Askari na wafanyakazi wa Wizara ambao kwa ushirikiano wao wamewezesha hotuba hii kuandaliwa na kukamilika katika wakati unaotakiwa. Aidha, napenda kumshukuru Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali Bw. Cassian Chibogoyo kwa kufanikisha uchapaji wa hotuba hii.

 

124. Mheshimiwa Spika, napenda pia kutoa shukrani zangu za dhati kwa wahisani wote ambao misaada yao imeiongezea nguvu Wizara yangu katika kutekeleza baadhi ya majukumu yake.  Wahisani hao ni pamoja na Serikali za Jamhuri ya Watu wa China, Marekani, Afrika Kusini,  Misri na Uingereza.

 

125. Mheshimiwa Spika, napenda pia kuyashukuru Mashirika ya Kimataifa ya  INTERPOL, SAFER AFRICA, UNDP na  EU na wafadhili wa  hapa nchini  ikiwa ni pamoja na Kampuni ya Ulinzi ya Ultimate Security Ltd, Kampuni ya Simu ya Alphatel, Vodacom, Umoja wa Kampuni za Ulinzi hapa nchini, Riki Hill Hotel, CMC Motors, Kampuni ya Sigara (TCC) wafanyabiashara pamoja na wote ambao kwa njia moja au nyingine wanaendelea kuisaidia Wizara ya Usalama wa Raia.

 

126. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa shukrani za pekee kwa nchi wahisani za Canada, Sweden, Denmark na Belgium na Mashirika ya UNDP na WB ambao wamechangia fedha kwenye mfuko ( Basket Funding)  wa kutekeleza programu ya maboresho ya  Sekta ya Sheria  (Legal Sector Reform Programme) ambapo Wizara yangu ni mdau katika sekta hiyo. Jeshi la Polisi litanufaika na programu hii katika maeneo ya mafunzo, kuimarisha upelelezi, marekebisho ya sheria, uboreshaji mazingira ya kazi n.k.

 

127. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo haya, sasa naliomba kwa heshima na taadhima Bunge lako Tukufu likubali kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Usalama wa Raia ya jumla ya shilingi 142,908,007,300 kwa mwaka wa fedha wa 2006/07 kama ifuatavyo:-.

 

FUNGU 28: WIZARA YA USALAMA WA RAIA

 

 

SH.

Mishahara (PE)

52,728,751,000

Matumizi Mengineyo (OC)

82,826,000,000

Matumizi ya Maendeleo

7,353,256,300

Jumla

Sh. 142,908,007,300

                       

128. Mheshimiwa Spika, nakushukuru wewe binafsi pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunisikiliza.

 

129.  Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

Majedwali