HOTUBA YA WAZIRI WA MIPANGO, UCHUMI  NA UWEZESHAJI  MHE. DKT. JUMA  NGASONGWA (MB), AKIWASILISHA  BUNGENI  MUHTASARI WA HALI YA UCHUMI WA TAIFA KWA MWAKA 2005 NA MAPENDEKEZO YA MPANGO WA MUDA WA KATI NA MFUMO WA MATUMIZI YA SERIKALI KWA KIPINDI CHA

MWAKA 2006/07–2008/09

UTANGULIZI                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                 

 

1.                  Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu sasa likae kama kamati ili liweze kupokea na kujadili Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2005 na mapendekezo ya Mpango wa Muda wa Kati na Mfumo wa Matumizi ya Serikali kwa kipindi cha mwaka 2006/07–2008/09. Pamoja na hotuba hii nawasilisha kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2005 na kitabu cha Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2006/07.

 

2.                  Mheshimiwa Spika, Awali ya yote napenda kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja na Makamu wake Dkt. Ali Mohamed Shein kwa kuchaguliwa kwao kwa ushindi mkubwa wa kishindo. Aidha, ninapenda kumpongeza Mhe. Amani Abeid Karume kwa kuchaguliwa kwake kwa kipindi cha pili kuwa Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar. Vilevile, nampongeza Mhe. Edward Ngoyai Lowassa (Mb.), kwa kuchaguliwa kwake kuwa Mbunge na kuteuliwa kuwa Waziri Mkuu katika Serikali ya Awamu ya Nne.

 

3.                  Aidha, napenda kukupongeza wewe Mhe. Samwel John Sitta (Mb.) na Naibu wako Mhe. Anna Makinda (Mb.) kwa kuchaguliwa kushika nyadhifa hizo za juu katika Bunge la Awamu ya Nne. Nawapongeza pia Mawaziri wenzangu wote pamoja na Naibu Mawaziri wote kwa kuteuliwa kwao na Mhe. Rais. Mwisho napenda niwapongeze wabunge wote kwa kuchaguliwa au kuteuliwa kwao kuingia katika Bunge hili Tukufu. Aidha, nawashukuru kipekee wapiga kura wangu wa Jimbo la Ulanga Magharibi kwa kunichagua kwa mara ya tatu kuwa mbunge wao.  Tutaendelea kushirikiana katika kuliletea maendeleo jimbo letu.

 

4.                  Mheshimiwa Spika, Napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa Kamati ya Bunge ya Fedha na Uchumi ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Dkt. Abdallah Omari Kigoda (Mb), kwa kutupatia ushauri na maelekezo wakati wa kujadili muhtasari wa hotuba hii. Aidha, ninawashukuru wale wote tulioshirikiana nao katika maandalizi ya Taarifa hii na Mpango ninaouwasilisha leo. Kwanza kabisa ninamshukuru Naibu Waziri, Mhe. Salome Joseph Mbatia (Mb.), timu yote ya wataalam wa Wizara ya Mipango, Uchumi na Uwezeshaji ikiongozwa na Katibu Mkuu, Dkt. Enos Bukuku na Naibu wake Dkt. Stegomena Tax Bamwenda pamoja na wataalam wa wizara na taasisi mbalimbali kwa michango yao.

 

5.                  Mheshimiwa Spika, Baada ya kusema hayo, sasa naomba nianze kutoa muhtasari wa mapitio ya hali ya uchumi na maendeleo kwa mwaka 2005, ikiwa ni mapitio ya mwaka wa kwanza wa utekelezaji wa Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA) wenye mwelekeo na azma ya kutufikisha kwenye malengo ya jumla ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025. Kwa kipindi cha mwaka 2005/06, bajeti iliendelea kujikita zaidi katika kuendeleza mageuzi ya kiuchumi na kijamii yaliyolenga katika kukuza na kutengemaza uchumi, kwa kutekeleza sera, mipango, programu na mikakati mbali mbali ya kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Taifa letu. Aidha, ikumbukwe kwamba taarifa hii ni ya kipindi cha kuanzia Januari hadi Desemba 2005 na sehemu chache zimegusia robo ya kwanza ya mwaka 2006.

 

MAPITIO YA HALI YA UCHUMI JUMLA

Pato la Taifa

6.                  Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, Pato la Taifa lilikua kwa asilimia 6.8[1] ikilinganishwa na lengo la ukuaji wa asilimia 6.9, na ukuaji halisi wa asilimia 6.7 mwaka 2004. Ukuaji huu ulichangiwa zaidi na ukuaji wa sekta za uuzaji wa jumla, rejareja na mahoteli, ikijumuisha utalii; bidhaa za viwandani; ujenzi; madini na uchimbaji mawe na mawasiliano na uchukuzi. Vile vile, mchango mwingine ulitokana na ongezeko la viwango vya ukuaji wa sekta za umeme na maji; huduma za kibiashara na fedha; na uendeshaji wa serikali na huduma nyingine. Pamoja na mambo mengine, ukuaji huu haukufikia lengo kutokana na ukame uliotokea katika maeneo mengi nchini, hasa katika kipindi cha robo ya nne ya mwaka 2005.

 

7.                  Mheshimiwa Spika, Pato la wastani kwa kila mtu liliongezeka hadi sh. 360,865 mwaka 2005 kutoka sh. 319,754 mwaka 2004 kwa bei za miaka husika, sawa na ongezeko la asilimia 12.9.  Aidha, kwa bei za mwaka 1992, wastani ulikuwa sh. 61,798 mwaka 2005 ikilinganishwa na sh. 59,335 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 4.2.

8.                  Mheshimiwa Spika, Mchango wa sekta ya kilimo katika Pato la Taifa uliendelea kupungua kidogo kidogo ambapo mchango wa sekta nyingine hasa bidhaa za viwandani; uuzaji wa jumla, reja reja na mahoteli, ikijumuisha utalii; madini; na ujenzi uliendelea kuongezeka. Hali hii inaonyesha kubadilika kwa muundo wa uchumi ambao sasa hautegemei kuchangiwa kwa kiasi kikubwa na kilimo pekee. Hata hivyo, mchango wa sekta ya kilimo katika Pato la Taifa uliendelea kuwa mkubwa ikilinganishwa na sekta nyingine. Katika mwaka 2005, sekta ya kilimo ilichangia asilimia 45.6 ya Pato la Taifa ikilinganishwa na asilimia 46.3 mwaka 2004.

 

9.                  Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, sekta ya kilimo ilikua kwa asilimia 5.2 ikilinganishwa na asilimia 5.8 mwaka 2004. Kupungua kwa ukuaji wa sekta hii kulitokana hasa na kushuka kwa uzalishaji katika sekta ndogo za mazao na mifugo. Ukuaji wa sekta hizi ndogo ulishuka kutoka asilimia 6.0 na 4.8 mwaka 2004 hadi  asilimia 5.2 na 4.2 mwaka 2005 kwa mtiririko huo. Hata hivyo, viwango vya ukuaji vya sekta ndogo za uvuvi; na misitu na uwindaji viliongezeka kutoka asilimia 6.7 na 3.8 mwaka 2004 hadi asilimia 7.3 na 4.5 mwaka 2005, kwa mtiririko huo.

 

10.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya bidhaa za viwandani ilikua kwa asilimia 9.0 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 8.6 mwaka 2004. Ukuaji huo ulitokana na kuongezeka kwa uzalishaji bidhaa katika baadhi ya viwanda hususan saruji, aluminiamu na bati. Mchango wa sekta ya uzalishaji bidhaa viwandani uliongezeka hadi kufikia asilimia 9.0 mwaka 2005 kutoka asilimia 8.8 mwaka 2004.

 

11.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya mahoteli, uuzaji jumla na reja reja ikijumuisha utalii, ilikua kwa asilimia 8.2 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 7.8 mwaka 2004. Mchango wa sekta hii katika Pato la Taifa ulikuwa asilimia 17.2 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 16.9 mwaka 2004.

 

12.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya madini na uchimbaji mawe ilikua kwa asilimia 15.7 mwaka 2005, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 15.4 mwaka 2004. Kuongezeka kwa ukuaji wa sekta hii kulitokana hasa na uwekezaji mpya katika machimbo ya dhahabu ya Tulawaka yaliyoko wilaya ya Biharamulo. Mchango wa sekta ya madini na uchimbaji mawe katika Pato la Taifa uliongezeka hadi asilimia 3.5 mwaka 2005 kutoka asilimia 3.2 mwaka 2004.

 

13.             Mheshimiwa Spika, Mchango wa sekta ya ujenzi katika Pato la Taifa ulikuwa asilimia 5.7 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 5.4 mwaka 2004. Sekta ilikua kwa asilimia 11.9 mwaka 2005, kutoka asilimia 10.8 mwaka 2004.  Ukuaji huu ulitokana hasa na ujenzi wa majengo yasiyo ya kuishi na nyumba za kuishi, ujenzi wa barabara na madaraja, pamoja na uendelezaji wa ardhi.

 

14.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya mawasiliano na uchukuzi ilikua kwa asilimia 6.4 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 6.0 mwaka 2004. Ukuaji huu ulitokana na kuboreshwa kwa miundombinu ya usafirishaji na kuongezeka kwa huduma za mawasiliano hasa kwa njia ya simu. Hata hivyo, mchango wa sekta ya mawasiliano na uchukuzi katika Pato la Taifa ulibakia kuwa asilimia 5.4 mwaka 2005 kama ilivyokuwa mwaka 2004.

 

15.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya umeme na maji ilikua kwa asilimia 5.1 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 4.5 mwaka 2004. Kuongezeka kwa ukuaji huu kulitokana na kukua kwa sekta ndogo za umeme na maji kutoka asilimia 4.7 na 2.8 mwaka 2004 hadi asilimia 5.3 na 3.4 mwaka 2005 kwa mtiririko huo. Mchango wa sekta ya umeme na maji katika Pato la Taifa ulibakia kuwa asilimia 1.6 kama ilivyokuwa mwaka 2004.

 

16.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya huduma za fedha na kibiashara ilikua kwa asilimia 5.3 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 4.4 mwaka 2004. Ukuaji huu ulitokana na kuongezeka katika ukuaji wa sekta ndogo za fedha na bima, upangishaji majengo na huduma za kibiashara wa asilimia 5.7, 5.0 na 6.1 mwaka 2005, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 4.4, 4.3 na 5.5 mwaka 2004, kwa mtiririko huo. Sekta hii ilichangia asilimia 9.6 katika Pato la Taifa mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 9.7 mwaka 2004.

 

17.             Mheshimiwa Spika, Sekta ya uendeshaji serikali na huduma nyingine ilikua kwa asilimia 5.1 mwaka 2005, kutoka asilimia 4.3 mwaka 2004. Ukuaji huu ulichangiwa na sekta ndogo ya utawala kwa asilimia 4.7 mwaka 2005, kutoka asilimia 2.8 mwaka 2004. Sekta ndogo za elimu, afya na huduma nyinginezo zilikua kwa asilimia 6.3, 5.7 na 4.9, viwango ambavyo ni pungufu ya vile vilivyofikiwa katika mwaka 2004 vya asilimia 6.6, 6.0 na 5.8, kwa mtiririko huo. Mchango wa sekta ya uendeshaji serikali na huduma nyingine katika Pato la Taifa ulikuwa asilimia 7.0 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 7.1 mwaka 2004.

 

Kasi ya Upandaji Bei

18.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, wastani wa kasi ya upandaji bei ulikuwa asilimia 4.3 ikilinganishwa na lengo la asilimia 4.0 na kasi halisi ya asilimia 4.2 mwaka 2004. Kuongezeka kwa kasi ya upandaji bei kulitokana na kupanda kwa bei ya bidhaa za chakula kutokana na hali ya ukame na kupanda kwa wastani wa bei za bidhaa za mafuta ya petroli zilizosababisha kuongezeka kwa gharama za usafirishaji na umeme. Aidha kwa mwezi Machi 2006 kasi ya upandaji bei ilifikia asilimia 6.9 kupanda huku kulitokana na ukame uliopandisha bei ya vyakula na gharama za umeme.

 

BAJETI YA SERIKALI

Mapato

19.             Mheshimiwa Spika, Katika nusu ya kwanza ya mwaka 2005/06, mapato ya ndani yalifikia sh. 1,013.8 bilioni, ikilinganishwa na sh. 869.9 bilioni katika kipindi kama hicho mwaka 2004/05. Mapato hayo ni sawa na wastani wa sh.169 bilioni kwa mwezi ikilinganishwa na sh.145 bilioni kwa mwezi katika kipindi kama hicho mwaka 2004/05 sawa na ongezeko la asilimia 16.6. Kuongezeka kwa mapato kulitokana hasa na kuendelea kuimarika kwa usimamizi wa ukusanyaji wa kodi, hususan, kodi ya mapato na ya ongezeko la thamani kwa bidhaa za ndani na nje. Kufikia Machi, 2006 mapato ya ndani yalikuwa sh. 1,544.4 bilioni, sawa na asilimia 100.5 ya lengo katika kipindi hicho.

 

Matumizi

20.             Mheshimiwa Spika, Katika nusu ya kwanza ya mwaka 2005/06, matumizi yalifikia sh. 2,122.9 bilioni, ikilinganishwa na sh. 1,641.3 bilioni katika kipindi kama hicho mwaka 2004/05. Hadi Machi 2006, matumizi yalifikia sh. 3,180.5 bilioni ikilinganishwa na makisio ya sh. 3,171.1 bilioni sawa na ziada ya asilimia 0.3. Kati ya fedha hizo, sh. 2,199.6 bilioni zilitumika kwa matumizi ya kawaida na sh. 980.9 bilioni kwa miradi ya maendeleo. Ongezeko la matumizi lilitokana na kuongezeka kwa gharama za uchaguzi kufuatia kuahirishwa kwa Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba na kufanyika tarehe 15 Desemba 2005; kutoa ruzuku kwa TANESCO kwa ajili ya kununua ‘‘transformer’’ ya kituo cha Ilala, Jijini Dar es Salaam baada ya iliyokuwepo kuungua; na gharama za kulikwamua Shirika la Ndege Tanzania. Aidha, mahitaji mengine yaliyochangia katika ongezeko la matumizi yalitokana na maamuzi ya serikali yaliyofanywa baada ya bajeti kupitishwa, kama vile, marekebisho ya viwango vya posho za askari (ration allowances), pamoja na marekebisho ya mishahara ya watumishi wa afya.

 

Ujazi wa Fedha na Karadha

21.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, ujazi wa fedha kwa tafsiri pana (M2) uliongezeka kwa asilimia 36.2, ikilinganishwa na asilimia 19.2 mwaka 2004, ambapo ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi (M3)[2] uliongezeka kwa asilimia 38.2 mwaka ulioshia Desemba 2005, kutoka asilimia 19.3 Desemba 2004. Ongezeko hilo lilikuwa zaidi ya lengo la asilimia 24 kwa M2 na lengo la wigo wa asilimia 23-24 kwa M3 katika mwaka 2005/06. Ongezeko hilo lilichangiwa zaidi na ongezeko la amana za hundi, amana za akiba katika benki na kuongezeka kwa mikopo iliyotolewa na benki kwa sekta binafsi. Aidha, wastani wa viwango vya riba uliongezeka kidogo kutoka asilimia 14.8 mwaka 2004 hadi asilimia 15.0 mwaka 2005.

 

Ukuzaji Rasilimali

22.             Mheshimiwa Spika, Ukuzaji rasilimali uliongezeka kufikia sh. 735,180 milioni mwaka 2005 kutoka sh. 624,371 milioni mwaka 2004 kwa bei za mwaka 1992, sawa na ongezeko la asilimia 17.7. Ukuzaji rasilimali kwa bei za miaka husika uliongezeka kutoka sh. 2,598,974 milioni mwaka 2004 hadi sh. 3,149,402 milioni mwaka 2005 sawa na ongezeko la asilimia 21.2. Kuongezeka kwa ukuzaji rasilimali kulitokana hasa na ujenzi wa majengo; uagizaji wa vifaa; na kuongezeka kwa shughuli nyinginezo za ukuzaji rasilimali zikiwemo uendelezaji ardhi, barabara na madaraja, pamoja na maji. Aidha, uwiano wa ukuzaji rasilimali na Pato la Taifa ulikuwa asilimia 32.9 ikilinganishwa na asilimia 29.8 mwaka 2004, kwa bei za mwaka 1992. 

 

23.             Mheshimiwa Spika, Mchango wa sekta binafsi katika ukuzaji rasilimali ulikuwa asilimia 65.1 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 62.4 mwaka 2004. Kwa upande wa sekta ya umma, ukuzaji rasilimali uliongezeka hadi sh. 1,068,171 milioni kutoka sh. 950,077 milioni mwaka 2004 kwa bei za miaka husika, sawa na ongezeko la asilimia 12.4. Mchango wa sekta ya umma katika ukuzaji rasilimali kwa jumla ulikuwa asilimia 33.9 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 36.6 mwaka 2004.

 

Mikopo Kutoka Benki za Biashara kwa Sekta Mbalimbali

24.             Mheshimiwa Spika, Mikopo iliyotolewa na benki za biashara kwa sekta mbalimbali iliongezeka kutoka sh. 965,985.9 milioni mwaka 2003/04 hadi sh.1,219,305.6 milioni mwaka 2004/05, sawa na ongezeko la asilimia 26.2. Kufikia mwishoni mwa Desemba 2005, mikopo kwa sekta binafsi iliongezeka hadi sh. 1,425,062.3 milioni ikilinganishwa na sh. 1,060,077.3 milioni mwishoni mwa Desemba 2004. Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 34.4 ikilinganishwa na asilimia 30.0 mwishoni mwa Desemba 2004.

 

Mauzo na Uagizaji Bidhaa Nje

25.             Mheshimiwa Spika, Thamani ya mauzo ya bidhaa nje iliongezeka kufikia dola za Kimarekani 1,676.3 milioni mwaka 2005 kutoka dola za Kimarekani 1,473.1 milioni mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 13.8. Thamani ya mauzo ya bidhaa asilia iliongezeka na kufikia dola za Kimarekani 354.4 milioni mwaka 2005 kutoka dola za Kimarekani 297.8  milioni mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 19.0. Ongezeko hilo lilitokana na kuongezeka kwa mauzo ya mazao ya kahawa, tumbaku na pamba. Thamani ya mauzo ya bidhaa zisizo asilia iliongezeka na kufikia dola za Kimarekani 1,321.8 milioni mwaka 2005 kutoka dola za Kimarekani 1,175.3 milioni mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 12.5. Bidhaa zisizo asilia zilichangia asilimia 78.8 ya mauzo yote, wakati bidhaa asilia zilichangia asilimia 21.2. Pamoja na mafanikio hayo, mapato yatokanayo na mauzo nje yamekuwa na uwezo wa kugharamia asilimia 63.0 tu ya uagizaji nje. Changamoto iliyopo ni kuongeza mauzo nje na kuhamasisha uzalishaji na uuzaji wa bidhaa zenye viwango vya kuweza kuhimili ushindani kama kahawa ya ‘Kilicafe’ ya Kilimanjaro na mboga mboga za ‘Gomba Estate’ ya Arusha zinazouzwa katika masoko yenye bei nzuri nje ya nchi.

 

26.             Mheshimiwa Spika, Thamani ya bidhaa zilizoagizwa kutoka nje (f.o.b) iliongezeka kutoka dola za Kimarekani 2,339.7 milioni mwaka 2004, hadi dola za Kimarekani 2,661.8 milioni mwaka 2005 sawa na ongezeko la asilimia 13.8. Thamani ya bidhaa zilizoagizwa kutoka nje ilikuwa kubwa kuliko thamani ya bidhaa zilizouzwa nje na hivyo kuleta nakisi kubwa katika urari wa biashara ya bidhaa. Thamani ya bidhaa za matumizi ya kawaida ilipungua kwa asilimia 1.8 kutokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya chakula hususan mahindi. Uagizaji wa bidhaa nyingine za matumizi ya kawaida uliongezeka kutoka dola za Kimarekani 515.9 milioni mwaka 2004 hadi dola za Kimarekani 583.0 milioni mwaka 2005 sawa na ongezeko la asilimia 13.0.

 

27.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, urari wa malipo yote ulikuwa na nakisi ya dola za Kimarekani 437.5 milioni ikilinganishwa na ziada ya dola za Kimarekani 43.4 milioni mwaka 2004. Nakisi hii ilitokana na kuongezeka kwa nakisi ya urari wa biashara ya bidhaa, ambapo mwaka 2005, urari wa biashara ya bidhaa ulikuwa na nakisi ya dola za Kimarekani 985.5, sawa na asilimia 13.7, ikilinganishwa na nakisi ya dola za Kimarekani 866.6 mwaka 2004.

Akiba ya Fedha za Kigeni

28.             Mheshimiwa Spika, Akiba ya fedha za kigeni ilipungua hadi dola za Kimarekani 2,048.4 milioni mwaka 2005, kutoka dola za Kimarekani 2,296.1 milioni mwaka 2004, sawa na upungufu wa asilimia 10.8. Kiasi cha akiba ya fedha za kigeni mwaka 2005, kilikuwa na uwezo wa kuagiza bidhaa na kulipia huduma miezi 6.4 ikilinganishwa na kiasi cha mwaka 2004 kilichokuwa na uwezo wa miezi 8.2. Kiasi hiki ni chini ya lengo lilokusudiwa la uwezo wa kuagiza bidhaa na kulipia huduma kwa zaidi ya miezi 7.

 

Thamani ya Shilingi

29.             Mheshimiwa Spika, Thamani ya shilingi imeendelea kufuata mabadiliko ya hali ya soko. Mwaka 2005, thamani ya shilingi ya Tanzania ilikuwa na wastani wa sh.1,128.8 kwa dola moja ya Kimarekani, ikilinganishwa na wastani wa sh.1,089.3 kwa dola moja ya Kimarekani mwaka 2004. Hali hii inaonyesha kushuka kwa thamani ya shilingi kwa asilimia 3.6 ikilinganishwa na asilimia 5.0 mwaka 2004. Aidha, hadi mwishoni mwa Desemba 2005, thamani ya shilingi kwa dola moja ya Kimarekani ilikuwa sh.1,165.5 ikilinganishwa na sh.1,043.0 mwishoni mwa Desemba 2004.

 

Misaada na Mikopo ya Nje

30.             Mheshimiwa Spika, Misaada na mikopo imeendelea kupatikana kwa kiwango cha kuridhisha kutokana na kwamba wahisani wengi wameonyesha kuitikia mwito wa kuisaidia nchi yetu katika kutekeleza Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini. Misaada na mikopo ya bajeti ya kawaida ilifikia sh. 576,956 milioni mwezi Machi 2006 ikilinganishwa na makadirio ya sh. 589,913 milioni,sawa na asilimia 97.8. Pungufu hiyo ilitokana na baadhi ya nchi wahisani pamoja na Benki ya Dunia kupunguza misaada na mikopo pamoja na wengine kuchelewesha utoaji wa misaada na mikopo yao hasa ile ya ‘‘Basket Funding’’. Hata hivyo idadi kubwa ya wahisani walitoa misaada waliyoahidi. Kwa upande wa misaada na mikopo kwa ajili ya bajeti ya maendeleo, sh. 731,711 milioni, zilipatikana ikilinganishwa na sh. 783,467 milioni zilizoahidiwa sawa na asilimia 80.7.

 

Deni la Taifa

31.             Mheshimiwa Spika, Hadi Desemba 2005, deni la Taifa lilifikia dola za Kimarekani 9,961.3[3] milioni ikilinganishwa na dola za Kimarekani 9,726.9 milioni, Desemba 2004, sawa na ongezeko la asilimia 2.4.  Kati ya deni hilo, dola za Kimarekani 7,934.4 milioni ni deni la nje, sawa na asilimia 79.6 ya deni lote, na dola za Kimarekani 2,026.9 milioni ni deni la ndani.  Deni la nje lilipungua kwa asilimia 1.1, ikilinganishwa na mwaka 2004 ambapo lilikuwa dola za Kimarekani 8,022.9 milioni. Kiasi hicho cha deni la nje kinahimilika, licha ya kuwa kikubwa kutokana na malimbikizo ya riba kwa madeni ambayo hayajasamehewa na nchi zisizo wanachama wa Paris Club.

 

32.             Pamoja na kuzingatia tahadhari ya mzigo wa madeni, hatuwezi kusita kukopa mikopo nafuu na stahimilivu, ambayo itaelekezwa katika kuchangia kujenga uwezo wa uchumi na kuongeza uwekezaji hatimaye kuibua ongezeko la ajira, mauzo nje, mapato ya serikali, kuboresha miundombinu, na maendeleo ya rasilimali watu.

 

33.             Mheshimiwa Spika, Ulipaji wa deni la nje uliongezeka kutoka dola za Kimarekani 77.8 milioni mwaka 2004 hadi dola za Kimarekani 91.1 milioni mwaka 2005. Deni hilo lilijumuisha mkopo wa dola za Kimarekani 53.4 milioni na riba ya dola za Kimarekani 37.7 milioni. Kuongezeka huko kulitokana na ulipaji wa madeni ambayo hayajasamehewa na nchi sisizo wanachama wa Paris Club.

 

Deni la Ndani

34.             Mheshimiwa Spika, Hadi Desemba 2005, deni la ndani lilifikia sh. 2,362.5 bilioni, ikilinganishwa na deni la sh. 1,813.1 bilioni, katika kipindi kama hicho mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 30.3. Ongezeko hilo lilitokana na kuongezeka kwa matumizi ya serikali.  Kiasi cha sh. 716.8 bilioni za deni la ndani zililipwa katika mwaka 2005. Kati ya fedha hizo, sh. 616.4 bilioni zilikuwa ni mkopo na sh. 100.4 bilioni ilikuwa ni riba.

 

HALI YA UCHUMI DUNIANI NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA

Hali ya Uchumi Duniani

35.             Mheshimiwa Spika, Pato la dunia lilikua kwa asilimia 4.8 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 5.3 mwaka 2004. Kushuka kwa ukuaji wa pato la dunia kulichangiwa kwa kiasi kikubwa na kuyumba kwa uchumi wa nchi zilizoendelea hasa katika Bara la Ulaya hususan Ufaransa, Ujerumani, Italia na Uingereza; pamoja na ongezeko kubwa la bei ya mafuta na majanga mbali mbali yaliyoikumba dunia. Pamoja na kushuka kwa kasi ya ukuaji wa uchumi wa dunia, baadhi ya nchi za Asia zinazochipukia kiviwanda zilikuwa na ukuaji wa haraka wa uchumi, kwa mfano ukuaji wa uchumi wa China ulifikia asilimia 9.9 mwaka 2005.

 

36.             Mheshimiwa Spika, Pato la nchi zilizoendelea lilikua kwa asilimia 2.7 mwaka 2005, ikilinganishwa na asilimia 3.4 mwaka 2004. Kushuka kwa ukuaji wa pato la nchi zilizoendelea kulichangiwa hasa na kupanda kwa bei za mafuta na kupungua kwa mauzo nje. Kwa upande wa nchi zinazoendelea na nchi za Asia zinazoinukia kiviwanda wastani wa pato lilipungua hadi asilimia 7.2 na 8.6 kwa mwaka 2005 ikilinganishwa na asilimia 7.6 na 8.8 mwaka 2004, kwa mtiririko huo. Ukuaji wa pato la nchi zinazoendelea, ikilinganishwa na ukuaji wa pato la dunia, umeendelea kuimarika kutokana na kukua kwa biashara na shughuli za uzalishaji viwandani na utekelezaji mzuri wa sera za kurekebisha uchumi.

 

37.             Mheshimiwa Spika, Pato la nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara lilikua kwa wastani wa asilimia 5.5 mwaka 2005, ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.6 mwaka 2004. Mwaka 2005, ukuaji wa pato la Bara la Afrika ulishuka hadi wastani wa asilimia 5.2 kutoka wastani wa asilimia 5.5 mwaka 2004. Ukuaji wa pato la Bara la Afrika ulitokana na kuongezeka kwa mauzo ya mafuta, madini na ongezeko la bei kwa baadhi ya bidhaa za kilimo. Aidha, utekelezaji wa sera na mageuzi ya kiuchumi kwa baadhi ya nchi barani Afrika kulichangia katika ukuaji huo. Hata hivyo, ukuaji ulipungua kutokana na matatizo ya ukame na migogoro ya kisiasa iliyozikumba baadhi ya nchi za Kiafrika.

 

38.             Mheshimiwa Spika, Kwa nchi za maziwa makuu ikiwemo Tanzania pato lilikua kwa wastani wa asilimia 5.6 mwaka 2005, sawa na kiwango cha mwaka 2004.  Kwa nchi za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki pato lilikua kwa wastani wa asilimia 5.7 mwaka 2005, ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.5 mwaka 2004. Ukuaji huu ulitokana na kuongezeka kwa mauzo ya madini na ongezeko la bei kwa baadhi ya bidhaa za kilimo. Kwa upande wa nchi za Afrika ya Kati na Magharibi, pato lilikua kwa wastani wa asilimia 5.4 mwaka 2005, ikilinganishwa na wastani wa asilimia 6.6 mwaka 2004.

 

39.             Hivyo, ukuaji waasilimia 6.8 wa pato la taifa letu kwa mwaka 2005 ni hatua nzuri zaidi siyo tu katika kanda hii ya Afrika Mashariki na kati, bali pia katika Kanda yote ya Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Hii siyo kujipigia debe ingawa hili siyo baya; ni suala la kuwa na mikakati mizuri ya kukuza uchumi na maendeleo ya jamii ikijumuisha juhudi kubwa za kuvutia wawekezaji kwa kujenga na kuboresha kuboresha mazingira a biashara nchini. Juhudi zitaendelezwa kwa kasi na nguvu zaidi katika miaka ijayo.

 

USHIRIKIANO WA KIKANDA NA KIMATAIFA

40.             Mheshimiwa Spika, Uhusiano wa nchi yetu na mataifa mengine duniani pamoja na mashirika ya kimataifa na ushirikiano wa kikanda umeendelea kuimarika kwa kiwango kikubwa na hivyo kuendelea kulijengea Taifa letu mazingira mazuri ya shughuli za kiuchumi na kijamii.

 

Jumuiya ya Afrika Mashariki

41.             Mheshimiwa Spika, Itifaki ya Ushuru wa Pamoja wa Forodha kwa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ilianza kutumika tarehe 1 Januari  2005 baada ya kusainiwa na Marais wa nchi wanachama wa Jumuiya na kuridhiwa na Mabunge ya nchi hizo. Aidha, Jumuiya iliendelea kuandaa Mkakati wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Mkakati huo unafuatia kukamilika kwa kipindi cha mkakati wa awali wa mwaka 2001-2005 ambao kwa kiasi kikubwa ulifanikisha kuanzishwa kwa Ushirikiano wa Ushuru wa Pamoja wa Forodha, pamoja na kuweka misingi ya kuanzishwa kwa Soko la Pamoja la Afrika ya Mashariki.

 

42.             Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa miradi ya maendeleo, Jumuiya iliendelea kutekeleza shughuli za Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Ziwa Victoria kama ifuatavyo; mradi wa Ushirikiano wa Uvuvi katika Ziwa Victoria; matayarisho ya miradi ya miundombinu ikijumuisha barabara, reli, usafiri wa majini, uzalishaji na usambazaji wa nishati; na miradi ya kilimo. Aidha, katika kutimiza azma ya kuwa na majengo ya kudumu, maandalizi ya ujenzi wa makao makuu ya Jumuiya yalifikia hatua nzuri baada ya Tanzania kutoa eneo, pamoja na mshauri mwelekezi wa ujenzi kupatikana.

 

43.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, mkutano wa Kamati ya Mawaziri wa Mkutano wa Kimataifa kuhusu Eneo la Maziwa Makuu ulifanyika Lusaka Zambia chini ya uenyekiti wa Tanzania. Mkutano huo ulijadili itifaki ya mpango na programu za muda mfupi, kati na mrefu na kupitisha miradi inayokusudiwa kutekelezwa kwenye maeneo makubwa manne yafuatayo ni: Amani na Usalama; Demokrasia na Utawala Bora; Maendeleo ya kiuchumi na ushirikiano kikanda; na Haki za Binadamu na Masuala ya Kijamii. Aidha, katika mkutano huo nchi ya Misri ilikubaliwa kuwa mwanachama wa nchi za eneo la Maziwa Makuu.

 

 

Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC)

44.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, SADC ilifikisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwake. Mambo yaliyofanyika katika kipindi cha 2005/06 ni pamoja na: kupitisha azimio la kuongeza lengo la chini la  ushiriki wa wanawake katika maamuzi ya kisiasa na uongozi wa ngazi za juu kutoka asilimia 30 hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2010 ikiwa ni sambamba na malengo ya Jumuiya ya Afrika; kupitisha uamuzi wa kujenga Makao Makuu ya SADC  Gaborone, Botswana katika kipindi cha miaka kumi na mitano; na kukubaliana juu ya taratibu zinazohusu utatuzi wa migogoro ya kibiashara kwa lengo la kurekebisha na kuboresha itifaki ya biashara ya SADC.

 

45.             Aidha, taratibu za kuunganisha njia za umeme kati ya Tanzania na Zambia (Zambia–Tanzania Inter connector) ziliendelea kukamilishwa na Sekretariati ya SADC baada ya fedha za kutekeleza mradi kupatikana ili Tanzania iweze kuunganishwa rasmi kwenye mradi wa “Southern African Power Pool (SAPP)” kama nchi nyingine za SADC.

 

Mpango Mpya wa Ushirikiano Ili Kuleta Maendeleo Afrika (NEPAD)

46.             Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa mwaliko kwa sekretariati ya African Peer Review Mechanism (APRM) kuja nchini kuhakiki ni kwa jinsi gani Tanzania inatekeleza makubaliano yaliyofikiwa chini ya NEPAD ambayo yanajumuisha utawala wa sheria, haki za binadamu, uhuru wa vyombo vya habari, uhuru wa vyama vya siasa, mageuzi katika uchumi yenye kulenga katika ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini na kuendeleza ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi. Haya ni matokeo ya mkataba wa kujiunga na utaratibu unaotoa fursa kwa nchi kujitathmini na kujipima zenyewe kuhusiana na utekelezaji wa vigezo muhimu vya NEPAD, ulioridhiwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Februari,  2005.

 

47.             Mheshimiwa Spika, Kufuatia mageuzi ya kiuchumi yanayoendelea hapa nchini kama ilivyoainishwa kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, serikali iliwasilisha miradi ifuatayo kwa sekretariati ya NEPAD: Ujenzi wa daraja la Umoja linalounganisha nchi za Tanzania na Msumbiji, upanuzi wa bandari ya Dar es salaam, uunganishaji wa umeme kutoka Zambia hadi Kenya, maendeleo ya ukanda wa Mtwara na uboreshaji wa barabara za Jumuiya ya Afrika ya Mashariki.

 

Ushirikiano wa Kiufundi Baina ya Nchi Zinazoendelea

48.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005 Tanzania iliendelea kutumia fursa mbali mbali zilizotolewa na Serikali ya China chini ya mpango wa ushirikiano kwa nchi zinazoendelea zinazosaidiwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa. Wataalam wa Kitanzania kutoka Wizara na Taasisi mbali mbali walihudhuria mafunzo ya Uvunaji wa Maji ya Mvua, Nishati Mbadala na Televisheni  nchini China.

 

MAENDELEO YA SEKTA

Kilimo

 

49.             Mheshimiwa Spika, Mwaka 2005/06, uzalishaji wa mazao ya chakula ulipungua kwa baadhi ya mazao yakiwemo: ngano, mahindi, mtama na ndizi.  Uzalishaji uliongezeka kwa mazao mengine kama muhogo, kunde na mpunga. Kwa upande wa mazao ya biashara uzalishaji uliongezeka kwa mazao ya pareto, tumbaku na pamba, wakati ambapo uzalishaji wa kahawa na korosho ulipungua. Aidha, eneo lililo chini ya kilimo cha umwagiliaji lilipungua kutoka hekta 23,970 mwaka 2004, hadi hekta 22,506, mwaka 2005. Kupungua kwa uzalishaji kwa baadhi ya mazao kulitokana na ukame, huduma duni za ughani, na hali ya bei za mazao kwa wakulima ambazo hazitabiriki. Hivyo kuanzia sasa suala la kilimo cha umwagiliaji kama sehemu ya Mkakati wa Mapinduzi ya kilimo nchini kitapewa msukumo zaidi.

 

50.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, mkazo katika sekta ya kilimo utakuwa ni pamoja na: kuendelea kuboresha upatikanaji wa chakula cha kutosha; kupanua kilimo cha umwagiliaji; na kuongeza Hifadhi ya Taifa ya Chakula.

 

Viwanda

51.             Mheshimiwa Spika, Mwaka 2005/06, mafanikio ya kuridhisha yalipatikana katika sekta ya viwanda yakiwemo kuongezeka kwa uzalishaji wa bidhaa kulingana na mahitaji ya soko la ndani na nje.  Viwanda vya usindikaji wa mazao ya kilimo cha chakula vilihamasika na kuanza kutumia teknolojia sahihi za uzalishaji na usindikaji wa bidhaa mbali mbali kama matumizi ya teknolojia ya ‘‘biogas’’, teknolojia ya kukausha tumbaku kwa usalama zaidi, usindikaji wa mafuta ya kupikia na teknolojia ya kusafisha chumvi katika kiwango cha mataifa; na kuimarishwa kwa maabara ya upimaji ubora wa vyakula za Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

 

52.             Aidha, katika kuhamasisha uwekezaji katika ujenzi wa maeneo mapya ya kuzalisha bidhaa kwa ajili ya mauzo nje (EPZ), viwanda viwili vilianzishwa na kuanza uzalishaji.  Viwanda hivyo ni A-Z kilichopo Kisongo-Arusha, kinachozalisha vyandarua vyenye dawa na Kiwanda cha African Packaging System kilichopo “Millenium Business ParkDar es Salaam.

 

53.             Mheshimiwa Spika, Mpango wa mwaka 2006/07, unalenga katika yafuatayo: kujenga uwezo wa sekta binafsi wa kuongeza thamani na ubora wa bidhaa kwa kuzingatia matakwa ya soko la kimataifa; kuongeza juhudi zaidi za kuhamasisha uanzishaji wa maeneo maalum ya uwekezaji na uzalishaji kwa ajili ya uuzaji nje (EPZ); kuhamasisha uwekezaji katika sekta ya viwanda vya nguo, ngozi na usindikaji mazao ya kilimo na mifugo; kuboresha mazingira ya uzalishaji viwandani; na kuimarisha mahusiano ya kiuchumi kati ya nchi yetu na jumuia za kikanda na kimataifa. Juhudi zitaongezwa katika mwaka 2006/07 kutumia fursa za masoko nafuu ya AGOA, EBA, Canadian PACT pamoja na yale ya Japan, Korea ya Kusini na China.

 

Madini

54.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005/06, sekta ya madini imepata mafanikio ya kuridhisha yakiwemo: kuanza kwa utekelezaji wa mfumo maalumu unaolenga kuimarisha utoaji wa leseni za madini na kuongeza maduhuli ya serikali; kukamilika kwa upimaji wa viwanja vidogo vya madini mkoani Morogoro; kukamilika kwa ufungaji na kuanza kutumika mashine za kuchonga na kusanifu madini kwenye kituo cha uchongaji na usafishaji vito Arusha; na kutoa elimu na mafunzo mbalimbali kwa wachimbaji wadogo. Mapato yatokanayo na madini hayaridhishi hivyo serikali imeunda kamati maalum ya kutathmini suala hili kwa kina.

 

55.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, sekta ya madini inalenga: kuboresha mahusiano kati ya wachimbaji wadogo na wakubwa; kuongeza nafasi za ajira; kuhakikisha uchimbaji salama na unaozingatia utunzaji mazingira; kuunda kitengo cha kuratibu maendeleo ya wachimbaji wadogo; kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza zaidi; na kuhakikisha kwamba madini yanayozalishwa yanaongezewa thamani kabla ya kuzwa nje.

 

Nishati

56.             Mheshimiwa Spika, Mafanikio yaliyopatikana mwaka 2005/06, katika sekta ya nishati ni pamoja na: kuanza kwa uzalishaji umeme kwa kutumia gesi ya Songosongo; kusainiwa kwa makubaliano ya makusudio (Agreement of Intent) kati ya Serikali na mwekezaji wa mradi wa gesi ya Mnazi Bay utakaozalisha umeme wa MW 14 kwa Mkoa wa Lindi na Mtwara; na kukamilika kwa ufafiti uliofanyika mkoani Mwanza wa kubaini vikwazo katika kutumia umeme utokanao na jua kama nishati mbadala. Vilevile, TANESCO iliingia mkataba na kampuni ya Wartisila ili kurekebisha mtambo wa IPTL utumie gasi kuzalisha umeme badala ya mafuta ya petroli. Mafanikio mengine ni pamoja na: kukamilika kwa mradi wa umeme wa Lower Kihansi; kukamilika kwa miradi ya kupeleka umeme wilaya za Serengeti na Ukerewe; na kuendelea na mradi wa Urambo.

 

57.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, sekta ya nishati inalenga kuendeleza miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia gesi ya Songosongo. Kiasi cha umeme kinachotegemewa kuzalishwa ni: MW 45 (IPTL-Tegeta), MW 200 (Kinyerezi), MW 60 (Ubungo-Awamu ya Kwanza) na MW 40 (Ubungo-Awamu ya Pili) na MW 100 umeme wa kukodisha (leasing). Aidha malengo mengine ni pamoja na: kununua umeme kutoka Zambia; kuandaa mkakati wa kuboresha uzalishaji na usambazaji umeme mijini na vijijini; kuongeza upatikanaji wa nishati mbadala vijijini ili kupunguza uharibifu wa mazingira; kuendeleza jitihada za utafutaji mafuta ya petroli; na kuongeza matumizi ya nishati itokanayo na mionzi ya jua.  Mradi wa makaa ya mawe Kiwira utapanuliwa na mwekezaji binafsi kwa lengo la kuzalisha MW 200 za umeme. Juhudi za kuongeza vyanzo vingine vya kuzalisha umeme badala ya kutegemea maji, zitapewa msukumo zaidi.

 

Barabara

58.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005/06, kulikuwa na mafanikio yafuatayo katika sekta ya barabara: barabara zenye kilometa 10,062 za mikoa na kilometa 5,968 za barabara kuu zilifanyiwa matengenezo na kuwa na hali nzuri; madaraja 699 yalifanyiwa matengenezo na 17 mapya yalijengwa; na jumla ya makandarasi 315 walipatiwa mafunzo muhimu kwa lengo la kujengewa uwezo zaidi.

 

59.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha 2006/07, Serikali inalenga kutekeleza yafuatayo: kukarabati jumla ya kilometa 15,000 za barabara za mikoa na wilaya; kuendeleza utekelezaji wa mradi maalum wa kuboresha miundombinu katika mikoa sita ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Kigoma, Rukwa na Tabora; kuendelea kuwajengea uwezo makandarasi wazalendo na wadau wengine; na kuzifanyia mapitio sera mbalimbali za sekta hii kwa lengo la kuziboresha.

 

Mawasiliano na Uchukuzi

60.             Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha 2005/06, katika sekta ya uchukuzi na mawasiliano Serikali ilitekeleza yafuatayo: kuendelea na ujenzi wa uwanja mpya wa ndege wa Songwe na kulifikia asilimia 40; kukamilisha ukarabati wa njia za kuruka na kutua ndege katika viwanja vya ndege vya Mwanza, Arusha na Kigoma; kuendelea na matengenezo ya miundombinu katika uwanja wa ndege wa Singida; na kuendelea kukarabati magati katika bandari za maziwa makuu. Vilevile, kazi mbalimbali za ukarabati katika reli ya kati kwa lengo la kuboresha huduma zimeendelea kufanyika.

 

61.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2006/07, Serikali inalenga kutekeleza yafuatayo: kuanza kutekeleza mpango wa kubadilisha mfumo wa reli ya kati ikiwa ni pamoja na kubadilisha na kuweka mataruma ya uzito wa ratili 80; kuendeleza ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya viwanja vya ndege, bandari, magati, reli na mtandao wa mawasiliano; kuendeleza mpango wa kuoanisha viwango vya usafirishaji na mawasiliano vya ndani na vya kimataifa; kuboresha huduma za Mamlaka ya Hali ya Hewa; na kuratibu vyombo vya usafiri wa abiria ili kupunguza ajali.

 

Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA)

62.             Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka 2005/06, iliendelea kutoa kipaumbele katika masuala ya TEKNOHAMA kwa kutekeleza yafuatayo: kufanya tathmini kuhusu uendelezaji wa Mkonga wa Taifa wa Mawasiliano; kuunda Timu ya Waratibu wa TEKNOHAMA; kuanzisha vituo vya mawasiliano katika miji ya Singida, Morogoro, Mtwara, Mpwapwa, Rungwe na Pemba; na kuendelea kutekeleza mradi wa kujumuisha masomo ya TEKNOHAMA kwenye mitaala nchini (e-schools, e-education, e-learning).

 

63.             Mheshimiwa Spika, Malengo ya serikali kwa kipindi cha 2006/07 ni kama ifuatavyo: kuendeleza teknolojia ya TEKNOHAMA; kuratibu utekelezaji wa shughuli za TEKNOHAMA; na kuendeleza ushirikiano wa ki-kanda na kimataifa katika nyanja za TEKNOHAMA

 

Maliasili

64.             Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha 2005/06, katika sekta ya Maliasili Serikali ilitekeleza yafuatayo: Jumla ya miche 66, 182, 502 ilioteshwa iklinganishwa na miche 65,558,138 ya mwaka 2004, ongezeko hilo sawa na asilimia 0.95; kukamilisha upimaji wa misitu ya hifadhi katika maeneo ya Kapingo, Engoma, Mikikagi na Itira katika kisiwa cha Ukerewe; na kukamilisha kazi za kuhesabu rasilimali za misitu  katika wilaya za Morogoro, Mvomero, Kilombero, Ulanga, Handeni, Kilindi, Kilwa, Nachingwea, Liwale, Tunduru, Mpanda na Rufiji.

 

65.             Mheshimiwa Spika, Malengo ya Serikali katika mwaka 2006/07 ni: kuweka misingi madhubuti ya usimamizi wa rasilimali za maliasili ili kuongeza mchango wake katika Pato la Taifa; kuendeleza uhifadhi na uvunaji endelevu wa maliasili kwa kuboresha usimamizi na utendaji kazi unaofuata kanuni na sheria; kujenga mfumo madhubuti wa kiutawala ili kuboresha utoaji wa huduma; na kupanua wigo wa ushiriki wa sekta binafsi,mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau mbalimbali katika mipango inayohusu kulinda, kuhifadhi, na kusimamia matumizi endelevu ya maliasili.

 

UTEKELEZAJI WA  MASUALA MTAMBUKA

66.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, Serikali iliendelea kutekeleza maamuzi mbalimbali ya kisera na yanayozingatia masuala mtambuka.  Nitaelezea kwa kifupi kuhusu utekelezaji wa masuala hayo kama ifuatavyo:-

 

(i)      Utawala Bora

67.             Mheshimiwa Spika, Serikali iliendelea kutathimini hali ya rushwa kwa kutumia viashiria vilivyowekwa. Aidha, Serikali iliunda kamati za maadili makazini pamoja na kuendelea kutayarisha mkakati wa pili wa kupambana na rushwa mahali pa kazi katika ofisi za umma.

 

68.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, mambo yatakayosisitizwa ni: kuendelea kuboresha usimamizi wa fedha za umma na uwajibikaji; kushirikisha wadau mbalimbali katika mchakato wa maandalizi,  ufuatiliaji wa utekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya maendeleo; kuendelea kutekeleza Mpango wa Maboresho ya Serikali za Mitaa; kuimarisha kampeni ya kupambana na rushwa; kupambana na wahalifu; kuendelea kurekebisha kanuni na sheria ikiwa ni pamoja na mfumo wa uendeshaji; na kuimarisha upatikanaji wa taarifa zitakazosaidia kufanya maamuzi sahihi.

 

 

 

(ii) Vita Dhidi ya UKIMWI

69.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, Serikali iliendelea kuchukua hatua mbalimbali zikiwemo uhuishwaji wa shughuli za kudhibiti UKIMWI katika wizara, taasisi za serikali na sekta binafsi; na uandaaji wa mikakati ya kudhibiti UKIMWI kwa lengo la kuainisha shughuli zitakazofanyika katika kupambana na UKIMWI.  Taarifa ya utafiti ya kila mwaka kuhusu UKIMWI na magonjwa ya zinaa (Oktoba 2005) inaonyesha kuwa maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI yameongezeka kutoka watu 188,140 mwaka 2004, hadi watu 188,400 mwaka 2005. Kati ya hao wanawake ni 97,130  sawa na asilimia 51.6

 

70.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mwaka 2005, mafunzo yaliendelea  kutolewa katika ngazi mbalimbali.  Mwongozo wa kudhibiti UKIMWI katika sekta ya umma uliandaliwa ambao  uliweka bayana taratibu za kuzingatia wakati wa kutoa matunzo na msaada kwa watu waishio na virusi vya UKIMWI. Aidha, hadi Desemba 2005, vituo 96 vilikuwa vinatoa dawa za kurefusha maisha kwa watu waishio na virusi vya UKIMWI na watu 25,840 waishio na virusi vya UKIMWI  walisajiliwa katika mpango wa matibabu na matunzo.

 

71.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha 2006/07, Serikali itaendelea kuongeza idadi ya vituo vya kutolea dawa za kurefusha maisha kwa watu waishio na virusi vya UKIMWI na kuendelea kusajili watu waishio na virusi vya UKIMWI  katika mpango wa matibabu na matunzo pamoja na kuendelea na juhudi za kutoa elimu katika ngazi mbalimbai.

 

(iii) Masuala ya Jinsia

72.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali iliendelea kutekeleza sera, mipango na mikakati inayolenga katika kuboresha masuala ya jinsia. Aidha, uwakilishi wa wanawake umeendelea kuongezeka kutokana na marekebisho yaliyofanywa katika katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuendelea kurekebisha sheria za uchaguzi ili kuwa na uwakilishi wa wabunge wanawake unaofikia asilimia 30. Aidha, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Mhe. Rais kwa kuwateua wanawake wengi katika nyadhifa nyeti za kufanya maamuzi makubwa serikalini. Kwa upande wa Waheshimiwa Wabunge wanawake wamefikia asilimia 30.41 ikiwa ni zaidi ya lengo la kiwango cha chini kilichowekwa kwenye katiba ya nchi yetu na makubaliano  ya nchi wanachama wa SADC.

 

73.             Mheshimiwa Spika, Katika kuwawezesha wanawake kupanua uelewa wao kibiashara, wanawake 127 walishiriki maonyesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam kwa kuwezeshwa na Serikali ikishirikiana na Mfuko wa Fursa Sawa kwa Wote (Equal Oppotunities Trust Fund-EOTF) mwaka 2005, ikilinganishwa na wanawake 130 mwaka 2004.

 

74.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, Serikali itaendelea kuhamasisha matumizi ya takwimu zilizochambuliwa kijinsia katika maamuzi mbalimbali pamoja na kuhuisha sheria zinazoendelea kuwakandamiza wanawake. Serikali itahakikisha kiwango cha uwakilishi wa wanawake katika ngazi mbalimbali kinazingatiwa pamoja na kuhakikisha kuwa wanawake wanaendelea kupewa fursa ya kujiendeleza kielimu na kiuchumi ili waweze kufaidika zaidi katika maendeleo ya taifa.

 

(iv)    Idadi ya Watu

75.             Mheshimiwa Spika, Makadirio ya idadi ya watu Tanzania kwa kutumia takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2002 yanaonyesha kwamba kwa mwaka 2005, idadi ya watu ilikuwa 37,267,530, kati ya hao, wanawake ni 19,009,051, sawa na asilimia 51.01 na wanaume 18,258,479, sawa na asilimia 48.99. Tanzania Bara ilikadiriwa kuwa na watu 36,197,313 wakati Tanzania Zanzibar ilikadiriwa kuwa na watu  1,070,217.

 

76.             Mheshimiwa Spika, Kutokana na makadirio hayo Mkoa wa Dar es salaam ulionyesha kuwa na msongamano wa wastani wa watu 2,010 kwa kilomita ya mraba, ukifuatiwa na Mwanza watu 163, na Kilimanjaro watu 108. Mikoa iliyo na msongamano mdogo ilionyesha kuwa ni Lindi yenye watu 12 kwa kilomita ya mraba, ikifuatiwa na Rukwa watu 18. Kwa Tanzania Zanzibar karibu mikoa yote ina msongamano mkubwa wa kati ya watu 117 na 1,919 katika kilomita ya mraba.

 

77.             Mheshimiwa Spika, Sera ya Taifa ya Idadi ya Watu ilikamilika kuhuishwa katika mwaka 2005, na Mpango wa Utekelezaji ulianza  kuandaliwa. Mafunzo ya namna ya kujumuisha masuala ya idadi ya watu katika mipango ya maendeleo yaliendelea kutolewa katika ngazi za wilaya na kata, mashirika yasiyokuwa ya kiserikali na Wabunge.

 

(v) Mazingira

78.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005/06 Serikali iliandaa Mkakati wa kuhifadhi mazingira ya Ardhi na Vyanzo vya Maji.  Mkakati umelenga kukabiliana na tatizo kubwa la uharibifu wa mazingira utokanao na shughuli za ufugaji na kilimo kwenye maeneo ya vyanzo vya maji.  Pia mkakati huu unalenga kukabiliana na uharibufu wa mazingira utokanao na ukataji miti ovyo kwa ajili ya kuni,  mkaa na  matumizi mengine.

 

79.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07 Serikali inategemea kuchukua hatua zifuatazo: kudhibiti shughuli za kilimo na ufugaji kwenye vyanzo vya maji; kuendelea kuhamasisha wafugaji kuondokana na ufugaji holela na kuhamahama; kuandaa mipango mizuri ya matumizi ya ardhi; kuendeleza kampeni ya kitaifa ya upandaji miti na kuitunza;  kujenga na kuendeleza malambo, visima na mabwawa katika maeneo ya wafugaji na wakulima; kuendeleza  matumzi ya teknolojia sahihi za kuvuna, kuhifadhi na kusambaza maji ya mvua na ya ardhini kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji; kuhamasisha  taasisi, wakulima wa tumbaku na watumiaji wengine wakubwa wa miti, kuni, na mkaa, kwa mfano taasisi za elimu, majeshi na viwanda kuwa na mashamba yao ya miti; kuendelea kudhibiti uchomaji wa misitu na ukataji miti holela, kudhibiti shughuli za umwagiliaji; na kupanda miti ifaayo kwenye vyanzo vya maji.

 

MIPANGO MAALUMU YA MAENDELEO YA KIUCHUMI NA KIJAMII

80.             Mheshimiwa Spika, Katika muda wa kati, Serikali imeandaa kuendelea kutekeleza mipango na mikakati mbalimbali inayojumuisha: MKUKUTA; Mkakati wa Maendeleo wa Sekta ya Kilimo; Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania (MKURABITA); Tanzania Mini-Tiger Plan 2020 (TMTP 2020); Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara Tanzania (MKUMBITA); Mkakati wa Madeni wa Taifa na Mkakati wa Pamoja wa Kusimamia Misaada Tanzania. Aidha, Serikali imetayarisha Mfumo wa ufuatiliaji wa utekelezaji wa MKUKUTA  utakaotumika kufanya tathmini ya matokeo ya utekelezaji katika kipindi chote cha miaka mitano. Mfumo huu pia utabainisha mafanikio na mapungufu yatakayoweza kujitokeza ili kutoa maamuzi ya jinsi ya kuboresha uchumi na maendeleo ya jamii.

 

81.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005/06, Serikali iliendelea kutekeleza mipango na mikakati hiyo kama ifuatavyo:-

 

(i)      Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA)

82.             Mheshimiwa Spika,  MKUKUTA ulianza kutekelezwa mwaka 2005/06  ambapo sekta zote na taasisi mbali mbali zilizo za Serikali na zisizo za Serikali zinahusika katika utekelezaji wa maeneo makuu matatu ya MKUKUTA ambayo ni:- (i) ukuaji wa uchumi na upunguzaji wa umasikini wa kipato; (ii) uboreshaji wa maisha na ustawi wa jamii; na (iii) utawala bora na uwajibikaji. Baadhi ya mambo ya jumla ambayo yametekelezwa hadi sasa ni pamoja na: kuoanisha MKUKUTA na mipango mikakati  pamoja na bajeti ya serikali; kukamilisha   mwongozo wa jinsi ya kuoanisha mipango ya sekta na MKUKUTA na kukamilisha utayarishaji wa Mfumo wa Ufuatiliaji wa Hali ya Umaskini Kitaifa; na kuelimisha mikoa na halmashauri za serikali za mitaa kuhusu mwongozo wa uaonishaji wa mipango ya sekta na MKUKUTA. Aidha, zoezi la kuanisha gharama za utekelezaji wa malengo ya MKUKUTA lilianzishwa.

 

83.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha 2006/07, Serikali itaendelea na zoezi la kuainisha gharama za utekelezaji wa malengo ya maeneo yote ya MKUKUTA na kuendelea na utekelezaji wa mipango, programu na mikakati mbalimbali ya kufanikisha malengo ya jumla ya MKUKUTA. Vilevile, Zoezi la kuainisha gharama za utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2005 litaanzishwa rasmi katika kipindi hicho.

 

(ii)     Utekelezaji wa Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara Tanzania (MKUMBITA)

84.             Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza MKUMBITA kwa lengo la kupunguza gharama za uanzishwaji na uendeshaji wa biashara kwa kuondoa vikwazo vikiwemo vya kisera, kisheria, kanuni, kiutaratibu na kitaasisi ambavyo vinakwamisha ukuaji wa sekta binafsi. Katika mwaka 2005/06 MKUMBITA uliendelea kuboresha mazingira ya biashara nchini.  Hii ilikuwa ni pamoja na:  

·        Kukamilisha mapitio ya sheria na kanuni mbalimbali kwa lengo la kuimarisha mazingira ya biashara nchini.  Sheria na Kanuni hizi ni pamoja na Dhamana ya Ardhi ambazo zilianza kutumika mwezi Agosti, 2005 na Sheria ya Kusajili Shughuli za Biashara ya mwaka 2006; na

 

·        Kutayarisha rasimu za miswada kwa ajili ya sheria mbalimbali kama vile Miswada ya Kuthamanisha Ardhi; Usalama  Kazini; Fidia kwa Wafanyakazi; Hifadhi ya Jamii na Uwakala wa Soko la Ardhi ambayo imekwishawasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali; na kuwezesha maandalizi ya Mkakati wa Kuendeleza Sekta Binafsi.

 

85.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, Serikali itaendelea kuratibu MKUMBITA kwa kutoa msukumo wa pekee na thabiti katika kuendeleza sekta binafsi kwa kuweka mazingira bora ya kufanyia biashara na uwezeshaji nchini hususan kuendelea kuboresha sera, sheria na taratibu zinazokwaza sekta binafsi; kubadilisha mtazamo  wa watendaji wa serikali kwa sekta binafsi, kuimarisha Kituo cha Uwekezaji cha Taifa  na kuleta mageuzi katika Mahakama ya Biashara.

 

(iii)    Mpango Maalum wa Kuharakisha Maendeleo Tanzania (Tanzania Mini-Tiger Plan 2020)

86.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2005 Serikali ilianza kutekeleza Mpango Maalumu wa Kuharakisha Maendeleo ya Tanzania “(Tanzania Mini-Tiger Plan 2020)” kwa kuzingatia uzoefu na mafanikio ya nchi za Kusini Mashariki mwa Asia. Lengo la mpango huu ni kuongeza kasi ya ukuaji uchumi kama msingi wa kuongeza wastani wa kipato cha Mtanzania; kuongeza mauzo ya bidhaa na huduma nchi za nje;  na kuongeza fursa za ajira nchini kwa shabaha ya kukabiliana vizuri zaidi na tatizo la umaskini.

 

87.             Mheshimiwa Spika; Katika harakati za kuendeleza Mpango huu, miradi ifuatayo ilitekelezwa: kuzinduliwa kwa kampuni ya kuagiza na kukarabati magari, mashine na vipuri mbalimbali (Tsubasa Renewcar EA Ltd); na kuanza kwa ujenzi wa eneo maalum la uwekezaji raslimali  katika eneo la Mabibo Dar es salaam linalojulikana kama “The Benjamín William Mkapa Special Economic Zone (BWM-SEZ)”. Vilevile, kamati ya kusimamia ujenzi wa Kituo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT-SEZ) iliundwa na iliendelea na kazi zake chini ya uratibu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

 

88.             Aidha, Wataalam walitembelea India Oktoba 2005, ili kupata uzoefu wa kuanzisha na kuendesha vituo vya aina hiyo hapa nchini.  Katika kufanikisha  Mpango huu, sheria ya kuanzisha Maeneo Maalum ya Uwekezaji Rasilimali (SEZs) imepitishwa na Bunge lako Tukufu Februari, 2006 na kupata kibali cha Rais  Machi, 2006  na kuanza  kutumika rasmi tarehe 1 Mei, 2006.

89.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, Mpango huu utakuwa na malengo yafuatayo: kuendelea na ujenzi na kulitangaza  Eneo Maalum la Uwekezaji la ‘Benjamín William Mkapa Special Economic Zone’ liloko Mabibo ili kuwavutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi; kuunda Mamlaka ya Kusimamia Maeneo Maalum ya Uwekezaji (SEZs Authority); kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa Watanzania kutoka nchi zenye uzoefu wa Maeneo Maalum ya Uwekezaji; na kuanza ujenzi wa kituo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika Eneo Maalum la Uwekezaji liloko  eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (ICT-SEZ).

 

(iv)    Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania (MKURABITA)

90.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha 2005/06, Awamu ya Kwanza ya MKURABITA ilihusu tathmini ya sekta isiyo rasmi na taarifa yake kukabidhiwa Serikalini tarehe 5 Oktoba 2005. Tathmini ilibainisha mtandao, thamani ya sekta isiyo rasmi, kanuni na taratibu zinazo tumiwa na wadau kumiliki mali na kufanya biashara nje ya mfumo rasmi wa sheria. Vilevile, tathmini iliainisha vikwazo vya kisheria vinavyowazuia Watanzania walio wengi kuzingatia sheria kikamilifu wafanyapo biashara na katika kumiliki mali hususan ardhi na majengo.

 

91.             Kazi nyingine zilizofanyika ni pamoja na: uhamasishaji wa viongozi katika ngazi mbalimbali juu ya malengo na madhumuni ya MKURABITA; uhamasishaji kwa walengwa na watendaji kupitia warsha mbalimbali, uhamasishaji wa wafanya biashara ndogo ndogo na za kati juu ya shughuli za MKURABITA; uandaaji wa taratibu za ushirikiano na Wizara na Taasisi za Serikali zinazoweza kufanya shughuli kwa ushirikiano na MKURABITA; na ukamilishaji wa Mpango wa Kazi kwa ajili ya Awamu ya Pili ya MKURABITA.

 

92.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, malengo ya MKURABITA ni pamoja na: kufanya utafiti katika wilaya 26 za Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar ili kuandaa mapendekezo ya awali ya maboresho ya sheria na kanuni zitumikazo katika sekta isiyo rasmi; kutoa mapendekezo ya awali ya muundo wa kitaasisi (institutional arrangement); kutoa mafunzo kwa wataalamu wa Kitanzania ili kuhakikisha umiliki na ushiriki wa Watanzania katika kutengeneza sheria; kutekeleza shughuli zinazoenda sambamba na maandalizi ya maboresho ili kuendeleza nguvu na msukumo wa Watanzania ulitokana na taarifa ya utafiti; na kukamilisha “Concept Document” ya programu ambayo itatumika kama kiongozi cha mpango huu, na kuendeleza utengenezaji wa tovuti ya MKURABITA.

 

 

 

(v)     Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF)

93.             Mheshimiwa Spika, Kutokana na mafanikio yaliyopatikana katika Awamu ya Kwanza ya TASAF, Serikali iliamua kuendelea na Awamu ya Pili ya TASAF. Utekelezaji wa TASAF umetokana na kupata mkopo wa gharama nafuu kutoka Benki ya Dunia wa kiasi cha dola za Kimarekani 129 milioni na ruzuku ya dola za Kimarekani 21 milioni. Fedha hizo zimelenga kufanikisha Malengo ya Maendeleo ya Milenia na ya MKUKUTA.

 

94.             Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha Awamu ya Pili ya TASAF kilichoanza Mei 11, 2005, Serikali imefanikiwa katika: kuhamasisha umma kupitia vipindi vya radio na televisheni, makala katika magazeti na vipeperushi; kuandaa miongozo ya utekelezaji wa mradi katika ngazi za Halmashauri za Wilaya, Manispaa, Jiji na Shehia; na kutafsiri katika lugha ya Kiswahili miongozo mbalimbali.

 

95.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, TASAF imejiwekea lengo la kuwafikia wananchi wote wa Tanzania kwa kutoa mafunzo kuhusu taratibu za utekelezaji wa miradi itakayofadhiliwa na TASAF. Aidha, utaratibu utawekwa kuhakikisha kwamba wananchi wanatekeleza miradi kwa ufanisi, kusimamia kwa karibu utekelezaji na kuhakikisha kwamba taarifa za utekelezaji zinatolewa kwa wakati kwa ajili ya tathimini.

 

(vi)    Ubinafsishaji na Maendeleo ya Sekta Binafsi

96.             Mheshimiwa Spika,  Katika mwaka 2005/06, Serikali kwa kupitia Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) imeanzisha mabaraza ya biashara ya mikoa kwa lengo la kupanua wigo wa mashauriano kati ya Serikali na Sekta Binafsi ili kuboresha mazingira ya uzalishaji na biashara katika mikoa na wilaya. Mabaraza hayo yameanzishwa katika mikoa 12 ifuatayo: Kilimanjaro, Arusha, Manyara, Tanga, Mwanza, Kagera, Morogoro, Iringa, Mbeya, Ruvuma, Mtwara, na Dodoma. Aidha, Baraza la Biashara la Zanzibar limeanzishwa chini ya uenyekiti wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

 

97.             Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) iliendelea na juhudi za kuhamasisha na kuratibu wawekezaji wa ndani na nje katika sekta mbalimbali kwa lengo la kukuza sekta binafsi. Katika mwaka 2005, Kituo kiliandikisha miradi 550 yenye thamani ya sh. 1,876,063 milioni ambayo ilitoa fursa za ajira kwa watu 55,663 ikilinganishwa na miradi 454 yenye thamani ya sh. 1,246,040 milioni mwaka 2004.  Aidha, TIC inatekeleza mikakati ya kuibua fursa za uwekezaji mikoani. Ili kutimiza azma hiyo, tayari kituo kimefungua ofisi katika Kanda ya Ziwa mkoani Mwanza, na Kanda ya Kaskazini mkoani Kilimanjaro.

98.             Mheshimiwa Spika, Thamani ya uwekezaji wa mitaji ya kigeni ya moja kwa moja (FDIs) ilikuwa dola za Kimarekani 325 milioni mwaka 2005, ikilinganishwa na dola za Kimarekani  470 milioni mwaka 2004, sawa na upungufu wa asilimia 30.8.  Upungufu huo ulisababishwa hasa na kushuka kwa uwekezaji katika sekta ya madini.

 

99.             Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, malengo ya TIC ni pamoja na kufungua ofisi katika Kanda ya Kusini; kuendelea kuhamasisha wawekezaji wa nje kwa mtindo wa “Investor Targeting’’ ili kuongeza mitaji ya moja kwa moja (FDIs); kuwasaidia wawekezaji wadogo na wa kati (SMEs); kuanda miradi inayouzika (Bankable Projects); na kusaidiana na mikoa katika kuandaa na kuratibu warsha za uwekezaji.

 

100.         Mheshimiwa Spika, Mwaka 2005, jumla ya mashirika 11 yalibinafsishwa na mali 126 ziliuzwa na  kufanya jumla ya mashirika yaliyobinafsishwa kuwa 322 na mali za mashirika kuwa 647 tangu zoezi hili lianze miaka 13 iliyopita. Mashirika hayo yalibinafsishwa kwa Watanzania na wawekezaji kutoka nje kwa utaratibu wa kuuza hisa, kuuza mali, na kukodisha. Aidha, Tume ya Rais ya Urekebishaji wa Mashirika Umma iliongezewa muda wa miaka minne kuanzia Januari 2004 hadi Desemba 2007 ili kukamilisha ubinafsishaji wa mashirika  yaliyobaki.

 

101.         Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2006/07, mashirika 36 yaliyobaki   yataendelea na hatua mbalimbali za marekebisho, yakiwemo TAZARA, vitengo vya kibiashara vya Mamlaka ya Bandari Tanzania (ukiondoa kitengo cha makontena ambacho kimeshakodishwa) na Shirika la Bima la Taifa.   PSRC itafikia mwisho Desemba 2007, ambapo zoezi hili linatakiwa liwe limekamilika. Baada ya hapo, azma ya Serikali ni kubakiza Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini (Monitoring & Evaluation) ya mashirika yaliyobinafsishwa na kuratibu shughuli za mamlaka za udhibiti.

 

(vii)   Utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.

102.         Mheshimiwa Spika, Uwezeshaji wa Watanzania kiuchumi umekuwa moja ya ajenda ya muda mrefu katika sera za Taifa letu. Jitihada za uwezeshaji wa wananchi kiuchumi zimekua zikifanywa na vyombo mbalimbali hata kabla ya Sera ya Uwezeshaji kuundwa. Bunge lako Tukufu lilishuhudia uzinduzi wa Sera ya Taifa ya Uwezeshaji Juni 2004 na kupitisha Sheria ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Novemba 2004, ambayo ilianza kutumika rasmi Februari 2005. Lengo kuu la Sera ni kuwawezesha wananchi kushiriki katika shughuli mbali mbali za kiuchumi na kutoa mwongozo wa jumla utakaohakikisha kwamba, wananchi wanapata fursa za kiuchumi katika sekta mbali mbali. Aidha, Baraza la Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi liliundwa na kuzinduliwa rasmi Novemba 2005. Vilevile, Mhe. Rais alimteua Katibu wa Baraza la Uwezeshaji tarehe 3 Aprili 2006 akiwa na dhamana ya kusimamia utekelezaji wa Sera ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi. Pamoja na kuteuliwa kwa Katibu wa Baraza shughuli za Sekretariati ya Baraza la Uwezeshaji zitaanza kutekelezwa rasmi mwaka wa fedha 2006/07 ambapo sh.1.4 bilioni zimetengwa kwa ajili hiyo. 

 

103.         Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza sera hii, kila sekta inawajibika kuendelea kubuni mikakati yake, kufafanua na kuchanganua jinsi ya kuitekeleza.  Mikakati ya kisekta inaendelea kujikita zaidi katika kuwaendeleza wananchi kwa kuwapa upendeleo maalumu, na kuwawezesha kwa kuwapatia huduma bora za elimu na mafunzo ya ujasiriamali, kujenga miundombinu na kuwapa fursa za kushiriki katika kubuni, kupanga na kutekeleza sera na mikakati ya kisekta ya uwezeshaji wananchi kiuchumi.

 

104.         Mheshimiwa Spika,  Katika mwaka 2006/2007 baadhi ya kazi zitakazofanywa na Serikali ni:- kuajiri watumishi wa sekretariati ya Baraza; kufanya utafiti wa kuainisha mambo muhimu ya kipaumbele (quick wins) katika kutekeleza Sera; kuandaa mwongozo wa jinsi wananchi watakavyoshiriki katika kutekeleza Sera; na  kuandaa mfumo wa kuhakikisha kwamba sera ya uwezeshaji inafahamika zaidi kwa wananchi wote.

 

105.         Mheshimiwa Spika, Licha ya Tanzania kupata mafanikio makubwa katika uchumi jumla, changamoto kubwa iliyopo ni  kuendeleza na kuhakikisha kwamba mafanikio hayo yanawafikia wananchi wengi, hususan wananchi masikini walio vijijini. Aidha, kukamilika na kutekelezwa kwa kikamilifu miradi ya: Vitambulisho vya Taifa; Upimaji na Utoaji Hatimiliki  na Utayarishaji wa Ramani Maalum za Maeneo zinazosomeka kwa Kompyuta (Geographical Information System - GIS & National Spatial Data Infrastructure - NSDI) kutafanikisha kupatikana takwimu sahihi na katika muda muafaka.  Takwimu hizi zitasaidia katika tafiti mbalimbali zinazohusu jamii na maendeleo. Aidha, katika kuendeleza juhudi za kuwawezesha wananchi kiuchumi Serikali imeanzisha mfuko wa dhamana kwa SMEs, na  inaendelea  kutekeleza mipango na mikakati mbalimbali iliyoanzishwa ikiwemo: MKURABITA; MKUMBITA; Tanzania Mini Tiger 2020; na TASAF.

 

MISINGI NA MALENGO YA MPANGO WA MUDA WA KATI NA BAJETI KWA MWAKA 2006/07-2008/09

106.         Mheshimiwa Spika, Mpango huu na Bajeti hii ni ya kwanza kutayarishwa na Serikali ya Awamu ya Nne katika kutekeleza MKUKUTA. Misingi na Malengo ya Mpango wa Muda wa Kati na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2006/07-2008/09 inazingatia utekelezaji wa ahadi ya Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, inayolenga katika kuyafikia malengo makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ikijumuisha kuwapo maisha bora ya kila Mtanzania na kupunguza kabisa umasikini wa kipato ifikapo 2015.

 

107.         Mfumo wa Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka 2006/07 utatolewa na Waziri wa Fedha ambapo atabainisha kwa kina mwenendo wa mapato na matumizi ya Serikali katika mwaka 2005/06 na makadirio kwa mwaka 2006/07 pamoja na kufafanua maeneo makuu yaliyotengewa fedha.

 

108.         Mheshimiwa Spika, Misingi ya malengo mapana ya Mpango na Bajeti kwa kipindi cha muda wa kati 2006/07–2008/09 ni kama ifuatavyo:

                    i)      Kuendelea kutengemaza uchumi mkuu au uchumi jumla ( Macro economic stability);

                  ii)      Kuendelea kutekeleza MKUKUTA kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na kuendelea kutekeleza miradi mikubwa kama MKURABITA, Mpango Maalum wa Kuharakisha Maendeleo Tanzania, Mradi wa Maji kutoka Ziwa Victoria kwenda Kahama-Shinyanga, ujenzi wa barabara na madaraja pamoja na miundombinu ya umwagiliaji maji;

                iii)      Kuendelea kubuni na kutekeleza mipango na mikakati ya kuharakisha ukuaji wa uchumi kwa mfano mradi wa Vitambulisho vya Taifa, mradi wa upimaji ardhi na utoaji hatimiliki, na utayarishaji wa ramani maalum za maeneo zinazosomeka kwa kompyuta (Geographical Information System–GIS and National Spatial Data Infrastructure–NSDI);

                iv)      Kuimarisha na kusaidia sekta isiyo rasmi, ili ipanuke na kutengemaa kwa lengo la kuingizwa kwenye mfumo rasmi wa uchumi;

                  v)      Kuimarisha mifumo ya uratibu na usimamizi wa miradi ya maendeleo katika ngazi zote;

                vi)      Kuendelea kutekeleza sera ya Serikali ya kupeleka madaraka kwa wananchi kupitia Programu ya Maboresho ya Serikali za Mitaa;

              vii)      Jamii kuwa na mwamko, nidhani, na tabia ya kujituma katika shughuli za maendeleo; na

            viii)      Kupatikana kwa rasilimali na kuzitumia ipasavyo.

 

109.         Mheshimiwa Spika, Kufuatia misingi niliyoitaja hapa juu, matarajio ya malengo ya uchumi jumla katika kipindi cha mwaka 2006/07-2008/09 ni kama ifuatavyo:

                    i)      Pato halisi la taifa kukua kwa asilimia 5.9[4] mwaka 2006, asilimia 7.3 mwaka 2007, asilimia 7.7 mwaka 2008, na asilimia 7.9 mwaka 2009;

                  ii)      Kiwango cha kasi ya upandaji bei kisichozidi asilimia 4.0 (kwa bei za 2001) kufikiwa ifikapo mwezi Juni 2007;

                iii)      Mapato ya ndani kuongezeka kufikia asilimia 14.5 ya Pato la Taifa mwaka 2006/07, asilimia 14.7 mwaka 2007/08 na kuongezeka hadi asilimia 14.8 mwaka 2008/09;

                iv)      Ujazi wa fedha kwa tafsiri pana (M2) kudhibitiwa kwa viwango vinavyowiana na malengo ya ukuaji wa uchumi na kasi ya upandaji bei; na

                  v)      Akiba ya fedha za kigeni itakayokidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi kisichopungua miezi saba.

MAJUMUISHO

110.         Mheshimiwa Spika, Baada ya kuelezea hali ya uchumi wa taifa, misingi na malengo ya mpango na bajeti kwa kipindi cha 2006/07–2008/09, nachukua fursa hii kusisitiza mambo muhimu ambayo kama taifa tunahitaji kuyapa kipaumbele katika utekelezaji na ufuatiliaji wa karibu kwa mwaka 2006/07 kama ifuatavyo: -

                    i)      Kuhakikisha kwamba wananchi wanaelewa masuala muhimu yote yaliyobainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, na Mkakati wa Kukuza uchumi na Kupunguza Umasikini Tanzania, kupitia vyombo mbalimbali vikiwemo Televisheni, Radio, Tovuti ya Taifa na magazeti mbalimbali;

                  ii)      Kuendelea kuhakikisha kwamba mipango, mikakati na malengo tunayojiwekea yanalenga katika kukuza uchumi, kuongeza nafasi za ajira, kuongeza tija, na kuongeza mapato ya fedha za kigeni na ya ndani;

                iii)      Kuendelea kukasimu baadhi ya madaraka ya Serikali kuu kwa Serikali za Mitaa pamoja na kuzipatia rasilimali kwa lengo la kuwapa wananchi uwezo wa kuchambua, kupanga, kutekeleza, kufuatilia na kutathimini mipango na mikakati yao inayolenga katika kuwaondolea umasikini;

                iv)      Kuendelea kuboresha na kuoanisha mifumo ya ufuatiliaji na tathimini ya utekelezaji wa mipango na mikakati ya maendeleo kama ilivyoainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2005 na malengo ya Dira ya Maendeleo 2025 na Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Tanzania;

                  v)      Kuendelea kuhamasisha sekta zote zibuni mikakati madhubuti na endelevu ili kuboresha hali ya maisha ya wananchi;

                vi)      Kuendelea kuboresha na kurasimisha sekta isiyo rasmi ili ipate kupanuka na kutengemaa kwa lengo la kuongeza nafasi za ajira nchini;

              vii)      Kuendelea kuhimiza wawekezaji wa ndani kuwekeza katika viwanda vidogo na vya kati vya kusindika mazao ya kilimo ili kuongeza thamani yake na kuchangia katika kupanua nafasi za ajira;

            viii)      Kuendelea kubuni na kutekeleza mipango na mikakati ya kuwawezesha wananchi kiuchumi ili waweze kuboresha na kuendeleza shughuli zao za kijamii na kiuchumi; na

                ix)      Kuendelea kuhuisha mikakati ya kitaifa ya kujitosheleza kwa chakula kwa lengo la kukuza uchumi na kuondoa umasikini nchini.

 

111.         Mheshimiwa Spika, Ili kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 hatuna budi kulinda mafanikio yaliyopatikana wakati wa Serikali ya Awamu ya Tatu na kulenga katika kuendelea kupata mafanikio zaidi kwa nia ya kuondoa kero zinazowasibu wananchi walio wengi. Katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Nne hatuna budi kuwa makini zaidi katika kubainisha vipaumbele vyetu vya kukuza uchumi na kuondoa umasikini. Kwa hiyo, kwa kutambua kwamba rasilimali zetu ni finyu ni lazima tuelekeze rasilimali za kutosha katika maeneo machache yatakayochochea maendeleo yetu kwa haraka zaidi uamuzi ambao utafanya tuahirishe shughuli nyingine au kuzipa rasilimali chache za kukidhi gharama za uendeshaji tu. Changamoto tuliyo nayo ni kukubaliana ni maeneo gani yapewe kipaumbale zaidi katika mgao wa rasilimali na pia kuheshimu maamuzi yetu. Aidha, ili kuongeza ufanisi zaidi katika utekelezaji wa sera, mipango na mikakati yetu kuna haja ya kuboresha mifumo ya kutekeleza na kuendelea kusimamia, kufuatilia na kutathimini malengo kwa makini zaidi ili uchumi wa taifa letu ukue kwa haraka zaidi.

 

112.         Mheshimiwa Spika, Napenda kuelezea kuwa rasilimali zetu bado ni kidogo ukilinganisha na matatizo mengi ya kijamii na kiuchumi yanayotukabili kitaifa. Tunaweza kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kwa haraka zaidi ikiwa tutatumia rasilimali tulizonazo kwa ufanisi na makini zaidi. Hivyo, wito wangu ni kwa kila mmoja wetu kutumia fursa zilizopo kwa lengo la kuongeza tija kwa kasi kubwa na kukuza uchumi wetu kwa nguvu zaidi ili tuondokane na umasikini uliokithiri.

 

113.         Aidha, ni lazima jamii iwajibike kudhibiti, kufuatilia, kusimamia kwa karibu utekelezaji wa mipango na mikakati na kutathimini malengo.  Serikali itaendelea na jukumu la kuwawezesha na kuunga mkono juhudi za wananchi kwa kuelekeza rasilimali, pamoja na kuendelea kuandaa sera na mikakati na kutoa miongozo ya kuratibu, kusimamia pamoja na kufuatilia kwa karibu na kutathmini utekelezaji ili tuwe na maendeleo yenye kuwiana katika kila ngazi. Hivyo basi, kila mmoja wetu anatakiwa kutimiza wajibu wake ili kufikia azma ya taifa ya ukuaji wa uchumi unaopanda mwaka hadi mwaka na kwa haraka zaidi na kufikia malengo ya MKUKUTA na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025.

 

114.         Mheshimiwa Spika, Mwisho napenda nitambue juhudi za washirika mbalimbali wa maendeleo yetu kwa misaada na michango yao ambayo imekuwa chachu kwa maendeleo. Naomba sasa nitumie fursa hii kuwashukuru wote waliotusaidia na kutoa pongezi zetu za dhati kwa kuzitaja nchi, taasisi na mashirika kama ifuatavyo:- Serikali za Uswisi, Uholanzi, Ujerumani, Denmark, Ufaransa, Uingereza, Hispania, Ubelgiji, Canada, China, Afrika ya Kusini, Japan, Kuwait, Italia, Ireland na nchi nyingine marafiki. Benki ya Dunia, Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Mashirika mbali mbali ya Umoja wa Mataifa kama vile UNDP, UNESCO, UNFPA, UNHCR, UNICEF, UNIFEM, FAO, IFAD, WFP na WHO, Jumuiya ya nchi za Ulaya (EU), Mfuko wa Fedha wa Nchi Wanachama wa Uzalishaji Mafuta (OPEC Fund), Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo la Uingereza (DFID), Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD), Shirika la Maendeleo la Marekani (USAID), Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA), Shirika la Maendeleo la Finland (FINNIDA), Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA), Shirika la Maendeleo la Japan (JICA), Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC), Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) na mashirika mbali mbali ya Kimataifa yasiyo ya kiserikali (NGOs). 

 

Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja.



[1]  Takwimu za ukuaji wa Pato la Taifa zilipitiwa upya kwa kuzingatia matokeo ya takwimu zilizokusanywa na Idara Kuu ya Takwimu.

 

[2]   Mni fedha zilizo kwenye mzunguko nje ya mabenki; M = M+ amana za hundi; M = M + amana za muda maalum + amana za akiba; M= M+ amana za fedha za kigeni.

[3] Kiasi hiki ni kikubwa zaidi ya kile kinachoonyeshwa katika machapisho ya Benki kuu kutokana na tarakimu zao kutojumuisha baadhi ya madeni ya serikali yakiwemo ya Mashirika yaliyobinafsishwa au kufilisika.

[4]   Ukuaji wa Pato la taifa unatarajia kupungua kutokana na ukame, kuchelewa kwa mvua na kupanda kwa bei za mafuta ya petroli.