HOTUBA YA WAZIRI WA FEDHA
UTANGULIZI:
1.
Mheshimiwa Spika,
naomba kutoa hoja kwamba Bunge likubali kujadili na kupitisha makadirio ya
mapato na matumizi ya serikali kwa mwaka wa fedha wa 2001/2002.
Pamoja na hotuba hii vimetayarishwa vitabu vinne vinavyoelezea kwa
undani takwimu mbalimbali za bajeti. Kitabu
cha kwanza kinahusu makisio ya mapato. Kitabu
cha pili na cha tatu vinahusu makisio ya matumizi ya kawaida kwa Wizara na
Idara pamoja na Mikoa na Halmashauri za Miji na Wilaya.
Kitabu cha nne kinaelezea makadirio ya matumizi ya maendeleo kwa
Wizara, Idara na Mikoa pamoja na Halmashauri.
Aidha, upo Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2001/2002.
2.
Mheshimiwa Spika,
awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa
wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine kufanikisha matayarisho ya
Bajeti hii. Napenda kuishukuru
Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge kwa kazi nzuri iliyofanya ya kuchambua
makisio yote kwa kina. Ushauri
uliotolewa na Kamati hiyo umesaidia sana kuboresha bajeti hii.
3.
Mheshimiwa Spika, maandalizi
ya bajeti yamehusisha washikadau wengi na vyombo mbalimbali.
Kwa msingi huo, nawashukuru pia wafanyakazi wa Ofisi ya Rais Mipango na
Ubinafsishaji, Wizara nyingine zote, Idara zinazojitegemea, Mikoa na
Halmashauri zote, pamoja na Taasisi za Kitaifa kwa michango yao iliyosaidia
kufanikisha utayarishaji wa bajeti hii. Naomba
pia niishukuru Wizara ya Sheria na Mambo ya Katiba kwa kutayarisha miswada na
nyaraka mbalimbali za sheria kama sehemu ya zoezi hili. Aidha, napenda
kuwashukuru wafanyakazi wenzangu wa Wizara ya Fedha, nikianzia na Naibu Waziri
wa Fedha Mhe. Abdisalaam Issa Khatibu (Mb); Katibu Mkuu Peter J. Ngumbullu,
Manaibu Katibu Mkuu Peniel Lyimo na Gray Mgonja, Viongozi wengine wa Hazina na
wafanyakazi wote. Namshukuru
Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali kwa kuchapisha kwa wakati hotuba hii, vitabu vya
bajeti, pamoja na nyaraka nyingine zinazohusu bajeti hii.
Mwisho nawashukuru kipekee wataalamu na wale wote waliotoa mapendekezo
kuhusu sera na namna ya kutoza kodi mbalimbali nchini ambayo yamezingatiwa
sana katika kuandaa bajeti hii.
4.
Mheshimiwa Spika,
tunamaliza mwaka wa fedha wa 2000/2001 tukiwa na majonzi kwa kufiwa na Wabunge
wenzetu kadhaa. Katika kipindi
hiki cha Bunge jipya Wabunge watano (5) waliaga dunia.
Wabunge hao ni Hayati John Ndugulile Mgeja aliyekuwa Mbunge wa Solwa;
Hayati Ernest Nyanda aliyekuwa Mbunge wa Busega; Hayati Biku Mohamed Biku
aliyekuwa Mbunge wa Solwa; Hayati Prof. Chrispin Hauli aliyekuwa Naibu Waziri
wa Fedha na Mbunge wa Ludewa na Hayati Abbas Gulamali aliyekuwa Mbunge wa
Kilombero. Mwenyezi Mungu aziweke
roho za Marehemu hawa mahali pema peponi.
5.
Mheshimiwa Spika,
kikao hiki cha Bajeti ni cha kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge
uliofanyika mwezi Oktoba, mwaka 2000. Chama
cha Mapinduzi kilishinda uchaguzi huo kwa kishindo. Hotuba hii ni ya kwanza katika kutekeleza
Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala cha CCM.
Naomba Waheshimiwa Wabunge muipokee kwa imani na matumaini makubwa.
UTEKELEZAJI WA SERA ZA BAJETI YA MWAKA
2000/2001:
6.
Mheshimiwa Spika,
tathmini inaonyesha kwamba sera na malengo
ya bajeti
ya Serikali ya mwaka wa
fedha unaoisha yamepata mafanikio
ya kuridhisha. Mwaka
wa kalenda
wa 2000,
uchumi ulikua kwa asilimia 4.9 ukilinganishwa
na asilimia 4.7 mwaka 1999. Mfumuko wa bei uliendelea kupungua na kufikia asilimia 5.3
kwa mwaka ulioishia Machi 2001 na unatarajiwa
kuwa asilimia
4.9 ifikapo
mwisho wa
mwezi huu
wa Juni 2001. Akiba ya
fedha za kigeni iliongezeka na kufikia dola za Marekani bilioni moja mwisho wa
mwezi Machi 2001, ambayo inatosha kulipia bidhaa na huduma za kutoka nje ya
nchi kwa kipindi cha miezi mitano. Kiwango
hiki hakijawahi kufikiwa katika historia ya Tanzania.
7.
Mheshimiwa Spika,
makusanyo ya mapato ya Serikali kwa kipindi cha Julai 2000 hadi
mwezi Machi 2001, yalifikia shilingi 686.316 bilioni ikilinganishwa na makisio
ya shilingi 647.209 bilioni, kwa kipindi hicho. Kiasi hicho kinaonyesha
ongezeko la shilingi 39.107 bilioni zaidi ya lengo. Aidha, mwelekeo unaonyesha kwamba hadi Juni 30, 2001,
makusanyo yatafika kiasi cha shilingi 912.906 bilioni yakilinganishwa
na kiasi kilichokisiwa
katika bajeti cha shilingi 861.402 bilioni.
Hili ni ongezeko la shilingi 51.504 bilioni sawa na asilimia 6 zaidi ya
lengo.
8.
Mheshimiwa Spika,
kuhusu matumizi katika mwaka
2000/2001, Serikali imeendelea na utaratibu wa 'Cash
Budget' kwa lengo la kudhibiti matumizi yake. Utaratibu huu umesaidia sana
kuboresha nidhamu ya matumizi katika vyombo vya Serikali.
Katika mwaka huu wa fedha kuanzia Desemba 2000 Serikali ilitoa mgao wa
fedha za matumizi kwa vipindi vya miezi mitatu mitatu badala ya kila mwezi kwa
sekta zinazopewa kipaumbele (Priority
Sectors). Hatua hii imesaidia
sekta hizo kuwa na uhakika wa upatikanaji wa fedha na hivyo kupanga vizuri
matumizi yao. Aidha, katika mwaka
huu wa fedha Bunge lako lilipitisha sheria mbili za kudhibiti mapato na
matumizi. Sheria ya kwanza ni ya
kusimamia fedha za Serikali (Mapato na Matumizi pamoja na Ukaguzi wa Hesabu
za Serikali)
na Sheria
ya pili inahusu taratibu za manunuzi ya vifaa na huduma serikalini.
Sheria hizi mbili mpya ambazo
zitaanza kutumika rasmi mwezi ujao, zimechukua
nafasi ya sheria ya 'Exchequer and Audit
Ordinance' ya mwaka 1961 ambayo imefutwa. Madhumuni ya sheria hizi ni
kuboresha zaidi usimamizi, udhibiti na ukaguzi wa fedha, na ununuzi wa vifaa
na huduma. Aidha, hesabu za Wizara zote sasa zimeingizwa katika mtandao wa
kompyuta ili kudhibiti matumizi. Serikali hivi sasa iko mbioni kuingiza ofisi
zote za Hazina Ndogo zilizoko mikoani katika mtandao huo na tunategemea zoezi
hilo litakamilika katika miezi michache ijayo.
Aidha, Halmashauri za Wilaya 28 zimeshaingia katika mtandao na nyingine
29 zinafanyiwa majaribio ya kuingia katika mfumo huo kwa lengo la kuziingiza
Halmashauri zote upesi iwezekanavyo.
9.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka wa fedha wa 2000/2001, mgao wa fedha za matumizi uliendelea kuzingatia
Sera ya Serikali ya kutoa upendeleo maalumu kwa Sekta za huduma ya jamii
(Elimu, Afya na Maji),na huduma za kiuchumi kama vile barabara. Shughuli za Uchaguzi Mkuu pia zilipatiwa fedha za kutosha na
hivyo hapakuwa na matatizo kama yaliyotokea mwaka 1995.
Aidha, Serikali imeendelea kulipa deni la ndani lililohakikiwa, na hadi
Machi 2001, kiasi cha shilingi 7.630 bilioni kililipwa kwa wazabuni, na
shilingi 45.008 bilioni zililipwa kwa wadai wengine ambao ni pamoja na TANESCO,
DAWASA, na vyombo vya fedha.
10.
Mheshimiwa
Spika, ningependa
kutoa taarifa kwamba madeni yote ya nyuma kati ya Serikali ya Muungano na
TANESCO na DAWASA yamesawazishwa.
Hivyo kuanzia Januari mwaka huu, TANESCO na DAWASA haziidai Serikali
Kuu. Kuanzia Julai 2000, kila
Afisa Mhasibu alitakiwa kulipia matumizi ya umeme, maji, na simu, kinyume na
huko nyuma ambapo HAZINA ilikuwa inabeba mzigo huo kwa niaba ya Maafisa
Wahasibu hao.
11.
Mheshimiwa
Spika, matumizi
halisi kwa kipindi cha Julai 2000
hadi Machi 2001,
yalifikia shilingi 906.905 bilioni
yakilinganishwa na makisio ya
shilingi 985.394 bilioni. Kati ya
fedha hizo shilingi 736.024 bilioni ni matumizi ya kawaida na shilingi 170.881
bilioni ni matumizi ya maendeleo. Mwelekeo
unaonyesha kwamba matumizi yote yatafikia shilingi 1,493.899 bilioni (1.49
trilioni) kwa mwaka mzima wa 2000/2001 ikilinganishwa na makisio ya awali ya
shilingi 1,394.588 bilioni (1.39 trilioni).
MISAADA
NA MIKOPO NAFUU YA NJE:
12.
Mheshimiwa Spika,
katika kipindi cha Julai, 2000 hadi Machi, 2001, mwenendo wa upatikanaji wa
misaada kutoka Jumuiya ya Kimataifa, ikiwa ni pamoja na Mashirika ya Fedha na
Nchi Wafadhili, ulikuwa wa kuridhisha kwa ujumla.
Katika kipindi hicho cha miezi tisa, jumla ya misaada iliyopatikana ni
shilingi 353.063 bilioni. Kati ya
misaada iliyopokelewa, shilingi 198.218 bilioni zilikuwa za urari wa malipo ya
nje (balance of payments), msaada wa kulipia madeni ya Mashirika ya Fedha ya
Kimataifa (multilateral debt fund),
msaada wa mpango wa kusaidia bajeti kwa ajili ya kupunguza umaskini (poverty reduction budget support – PRBS) na msaada wa kapu kwa
sekta za afya na serikali za mitaa (basket
funds). Kiasi hicho
kilichopatikana chini ya programu hizi katika kipindi cha Julai 2000 – Machi
2001, ni kikubwa kuliko kile kilichokuwa kimekadiriwa cha shiling 154.456
bilioni. Aidha, shilingi 118.974
bilioni zilipatikana kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika kipindi hicho,
ikiwa ni chini ya makadirio ya shilingi 248.889 bilioni.
Hali kadhalika, chini ya mpango wa kufutiwa madeni wa HIPC, tulipata msamaha wa awali wa kufutiwa madeni (interim
relief) kwa kiasi cha shilingi 46.062 bilioni.
MBINU ZA KUKUZA UCHUMI:
13.
Mheshimiwa
Spika, katika
miaka mitano iliyopita, Serikali ilichukua hatua muhimu mbalimbali za
kurekebisha sera na mfumo wa uchumi na fedha, kwa lengo la kujenga msingi wa
maendeleo ya taifa linalojitegemea. Dira
ya taifa (vision
2025) inaainisha dhamira hiyo, ambayo kwayo, mikakati mingi
imetayarishwa na inaendelea kutekelezwa, ikiwa ni pamoja na mbinu za
kuhamasisha uwekezaji, mkakati wa kuondoa umaskini, na mingine mingi.
14.
Mheshimiwa
Spika, njia kuu
za kuondoa umaskini ni kuongeza kipato cha wananchi, na kuboresha huduma za
msingi za jamii. Njia pekee ya
kuongeza kipato ni uchumi wetu kukua kwa
kiwango kikubwa
kuliko cha
sasa cha
asilimia 5 hivi.
Tunahitaji uchumi ukue kwa
asilimia zaidi ya 8 kwa mwaka, ndipo tuwe na uhakika wa kupata matokeo
endelevu ya kuondoa umaskini. Uchumi
ukikua kwa kiwango cha juu, wigo wa kodi kwa ajili ya mapato ya ndani
utapanuka, na uwezo wa Serikali kugharamia shughuli za kuondoa
umaskini na nyingine za maendeleo ya Taifa, utaongezeka.
15.
Mheshimiwa Spika,
njia kuu kuliko zote ya kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi, ni kufufua
kilimo, ambacho kinabeba asilimia 80 ya Watanzania. Tukiweza kufikia
na kuvuka asilimia 5 ya ukuaji endelevu katika kilimo, umaskini utapungua kwa
kasi kubwa. Mbinu mpya za kufufua
kilimo ziko mbioni kukamilishwa, na Waziri wa sekta husika atazungumzia hili
kwa undani katika maelezo yake hapa Bungeni.
16.
Mheshimiwa Spika,
mbinu nyingine muhimu ya kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi ni kuendeleza
upanuzi na uimara wa sekta binafsi ya ndani na nje.
Serikali imekuwa ikisaidia maendeleo ya sekta binafsi tangu mwaka 1993,
kwa njia mbalimbali, zikiwemo:-
(i)
Marekebisho ya uchumi (macroeconomic
reforms)
(ii)
Sheria ya uwekezaji (1993 na 1997)
(iii)
Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma
(iv)
Uundaji upya wa Kituo cha Uwekezaji (TIC)
(v)
Marekebisho ya Mfumo wa Kodi
(vi)
Ushirikishwaji wa Sekta Binafsi katika kubuni na kutafakari sera za
Serikali za maendeleo, ambazo ni pamoja na sera za sekta muhimu kama fedha
(kodi), mawasiliano na uchukuzi, nishati (umeme), n.k.
17.
Mheshimiwa Spika,
Serikali itaendelea na sera hizo, licha ya kuchukua hatua nyingine zenye lengo
la kuboresha zaidi mazingira ya uwekezaji ili sekta binafsi ikue na itoe
mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya taifa na kupunguza umaskini. Maeneo ambayo utekelezaji wake unaendelea ni pamoja na:-
·
kuboresha zaidi
mfumo wa kodi
·
kuongeza mgao wa
fedha katika bajeti kwa miundo mbinu kama vile barabara,
·
kufanya
mabadiliko ambayo yatapunguza gharama za uzalishaji,
·
kutekeleza kwa
haraka mabadiliko muhimu ya utawala bora,
·
kuweka mazingira
bora yanayoimarisha biashara kubwa, ndogo, za kati, na isiyo rasmi,
·
kuendeleza sera
ya kudhibiti ongezeko la ujazi wa fedha ili kudhibiti mfumuko wa bei,
·
kuweka mazingira
bora ya ushindani katika sekta ya benki ili kupunguza riba, na kuongeza uwezo
wa vyombo vya fedha kutoa mikopo kwa wakopaji wadogo na wakubwa.
Hii ni pamoja na kukamilisha kanuni za usimamiaji wa taasisi za mikopo
kwa wakopaji wadogo wadogo (micro-finance
regulation);
·
kuweka mazingira
yatakayowezesha uanzishwaji wa vyombo vya uwekezaji wa pamoja (collective
investment schemes);
·
kuendeleza
programu za ushirikiano chini ya Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC)
na Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)
ili kupanua soko na kuongeza biashara na uwekezaji.
18.
Mheshimiwa Spika,
Serikali imekamilisha mkakati wa kitaifa wa kupunguza umaskini kwa
kushirikisha jamii ya Watanzania na nchi zinazotufadhili.
Mkakati huo
uliwasilishwa kwa Shirika
la Fedha la Kimataifa na Benki ya Dunia na kupitishwa na Bodi zao mwezi
Novemba mwaka 2000. Wakati
tunatayarisha mkakati huo wa kupunguza umaskini (Poverty
Reduction Strategy Paper - PRSP),
tumekuwa pia tukikamilisha vigezo kadhaa kuhusu vita dhidi ya umaskini,
vikiwemo kuboresha takwimu juu ya hali halisi ya umaskini nchini, kuboresha
uwezo wetu wa kufuatilia mipango yetu, kuhakikisha Bajeti ya Serikali
inaonyesha wazi tunalenga katika kupambana na umaskini, kufanya tathmini ya
mtandao wa shule, kuendeleza chanjo kwa watoto, na vita dhidi ya Ukimwi, na
kuendelea kuzungumza na wadai wetu wengine ili nao washiriki katika
kutupunguzia madeni. Wakati huo
pia, katika kipindi cha mpito, Tanzania imepata msamaha wa awali wa madeni (Interim Debt Relief) kutoka Benki ya Dunia, Shirika
la Fedha
la Kimataifa, Benki ya
Maendeleo ya
Afrika, na
Wadai wa
kundi la nchi
tajiri la
Paris Club.
Hadi kufikia Aprili 2001, msamaha huo wa awali ulifikia dola za
Kimarekani 54.6 milioni, sawa na shilingi 46.062 bilioni, ambazo nimezitaja
hapo awali.
19.
Mheshimiwa Spika,
uamuzi wa mwisho wa kupatiwa msamaha kamili wa madeni (Completion
Point) utafikiwa kabla ya Desemba mwaka huu. Hivi sasa Serikali inakamilisha taarifa ya utekelezaji wa
vigezo mbalimbali vya PRSP kwa ajili
ya kufikia uamuzi huo wa mwisho wa kupunguziwa madeni. Dalili zinaonyesha kwamba, mara uamuzi wa mwisho ukifikiwa,
nchi zinazotudai za kundi la Paris Club, zitatufutia madeni yote,
na Mashirika
ya Fedha ya Kimataifa,
na Benki
ya Maendeleo
ya Afrika
kwa pamoja
yatatupunguazia mzigo
wa madeni kwa zaidi ya
asilimia 70.
20.
Mheshimiwa Spika,
pamoja na utekelezaji wa vigezo muhimu vya programu ya kuondoa umaskini,
tunapaswa tuendelee na sera sahihi za uchumi, fedha, na utawala bora.
Vigezo vya
kuzingatia hapa
ni pamoja
na usimamizi
bora wa
bajeti ya
Serikali, ikiwemo kuendelea kuwa makini na waadilifu katika kukusanya na
kutumia mapato ya Serikali, kuendelea kuboresha mfumo wa kodi, kuboresha
mazingira ya uwekezaji mitaji na biashara, miundo mbinu na huduma nyingine za
uchumi.
21.
Mheshimiwa
Spika, mpango wa
Taifa wa kupunguza umaskini unahitaji kupewa msukumo mkubwa kwa kushirikisha
jamii yote ya Watanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa hususan nchi na
mashirika yanayotufadhili. Katika
kuweka msukumo huo, mambo matatu hayana budi yafanyike:
(i)
Kuweka malengo ya Kitaifa yaliyo wazi,
(ii)
Kubuni mazingira ya kiuchumi ya Kitaifa ambayo
yatachochea maendeleo, na
(iii)
Kujenga mfumo wa usimamizi na tathmini.
Mambo
haya yameainishwa katika Dira ya Taifa (Vision
2025), na katika Mkakati wa
Kuondoa Umaskini (PRSP).
22.
Mheshimiwa Spika,
kwa ujumla, malengo, shughuli na viashirio vya mkakati wetu wa kupunguza
umaskini vinazingatia maeneo matatu makubwa:-
(i)
kupunguza umaskini wa kipato,
(ii)
kuendeleza ubora wa maisha na ustawi wa jamii, na
(iii)
kupunguza madhara yanayoweza kuwapata watu maskini.
Njia
ya kupunguza umaskini wa kipato ni kuwezesha shughuli za kuzalisha mapato ya
aina mbalimbali kustawi. Uwezesho
huo utatokana na ukuaji wa kilimo, upanuzi
wa vitega
uchumi vya
asilia na vya kisasa vya
uzalishaji, uimarishaji wa miundo mbinu hasa vijijini, kuendeleza nyenzo za
uchumi mdogo, na kuboresha mfumo wa utawala na sheria ulio thabiti na
unaochochea maendeleo.
Umaskini
wa kutokuwa na kipato unatokana pia na elimu ndogo, afya mbaya, na ustawi wa
jamii ambao ni wa mashaka. Hivyo,
njia ya kuboresha maisha ya watu ni kuhakikisha kwamba kila mtu anapata nafasi
sawa ya kupata elimu angalu ya msingi, anajua kusoma na kuandika, anapata afya
bora, maji salama, chakula bora, lishe bora, na kwa hali ya sasa, kwamba
anajikinga na madhara, hasa ya Ukimwi.
23.
Mheshimiwa Spika,
kwa kuzingatia hali ya umaskini ya wananchi wetu, na kwa kutambua kwamba sekta
ya binafsi bado ni changa, sehemu kubwa ya gharama za kutekeleza mkakati wa
kuondoa umaskini itaendelea kubebwa na Serikali kwa kupitia bajeti yake.
Kiasi kikubwa cha fedha kitatokana na mapato yetu ya ndani, na kingine
kitatokana na misaada ya wafadhili wetu, pamoja na mikopo nafuu kutoka vyombo
vya fedha vya kimataifa. Uwezo wetu wa kugharamia programu hiyo pia utasaidiwa na
kufutiwa madeni chini ya mpango wa HIPC.
24.
Mheshimiwa Spika,
kwa sasa bado hatuna uhakika tutahitaji fedha kiasi gani miaka ijayo kwa
kugharamia za mahitaji muhimu ya kuondoa umaskini.
Hii ni kwa sababu programu kabambe za kufufua kilimo na maendeleo
vijijini hazijakamilishwa vilivyo. Hata
hivyo, ni
wazi kwamba mahitaji yatakuwa makubwa kuliko uwezo wetu, na hivyo, itatubidi
tuimarishe juhudi za kuongeza mapato ya ndani, tutumie mapato yetu kwa uangalifu
mkubwa, na tuendeleze uhusiano mzuri tuliuonao sasa na wafadhili wetu na
wengine wote wanaotuunga mkono katika vita dhidi ya umaskini.
MALENGO YA BAJETI YA MWAKA 2001/2002:
25.
Mheshimiwa Spika,
kama nilivyosema awali, sera ya bajeti ya mwaka 2001/2002 ni ya kutekeleza Ilani
ya Uchaguzi ya Chama Tawala, ambayo kwa ujumla inalenga kuendeleza ustawi wa
uchumi, na wakati huo huo kuongeza matumizi katika sekta na maeneo
yaliyobainishwa ya kupunguza umaskini. Malengo
ya jumla ya uchumi, mapato na matumizi kwa mwaka 2001/2002 ni haya yafuatayo:-
(i)
Kuongeza ukuaji wa uchumi kwa asilimia 5.9, mwaka huu wa 2001 na asilimia
6.2 mwaka 2002. Ongezeko hili
litatokana hasa na hali nzuri ya hewa, na kuchukuliwa kwa hatua nilizozieleza
hapo awali.
(ii)
Kudhitibi mfumuko wa bei yaani upandaji wa gharama za maisha kwa kiasi
cha kufikia asilimia 4.4 badala ya 4.9 kwa mwaka unaomalizika sasa.
(iii)
Kulenga nakisi ya bajeti (bila misaada ya nje) kuwa asilimia 3.1 ya Pato
la Taifa. Nakisi hiyo ni kubwa
kuliko ya mwaka huu wa fedha ya asilimia 1.2 ya Pato la Taifa kutokana na nia ya
Serikali ya kuongeza matumizi chini ya mpango wa kupunguza umaskini.
Matumizi hayo ni kwa ajili ya elimu ya msingi, afya, maji, barabara
vijijini, kilimo, mahakama, na vita dhidi ya Ukimwi.
(iv)
Kuongeza matumizi yote ya Serikali (bila kujumuisha miradi inayogharamiwa
na wafadhili) kutoka asilimia 13 ya Pato la Taifa kwa mwaka wa fedha
unaomalizika na kufikia asilimia 15.2 ya Pato la Taifa mwaka ujao wa fedha.
Matumizi
yasiyo ya mishahara (non-wage) yataongezeka kwa asilimia 28 kwa sekta zinazopewa
kipaumbele. Vile vile gharama za
mishahara (wage bill) zitaongezeka kwa asilimia 10.
(v)
Kupanua wigo wa kodi ili mapato ya kodi yafikie asilimia 12.1 ya Pato la
Taifa.
(vi)
Kuendelea kuhifadhi akiba ya fedha za kigeni katika kiwango kinachoweza
kununua toka ng’ambo mahitaji ya bidhaa na huduma za kutosheleza miezi minne.
Hivi sasa kiasi hiki ni shilingi bilioni takribani 900 sawa na dola
bilioni moja za kimarekani.
SERA ZA MAPATO:
26.
Mheshimiwa Spika,
sera za mapato zinalenga kuendeleza hatua zilizoanza miaka ya hivi karibuni za
kupanua wigo wa kodi, na pia kuboresha mfumo na usimamizi wa kukusanya kodi, ili
kuongeza ari ya wananchi ya kulipa kodi na kuondoa ukwepaji wa kodi wa watu
wasio waaminifu.
27.
Mheshimiwa Spika,
sababu za msingi za nchi yetu kulazimika kuwa
na sera sahihi ya kodi ni pamoja na:-
(i)
Kukusanya mapato ya kutosha kuiwezesha
Serikali kugharamia huduma
za uchumi, jamii, usalama na ulinzi, na kulipa madeni ya Serikali.
(ii)
Kuweka mazingira sahihi ambayo hayaongezi gharama kwa walipa kodi na
wanaokusanya kodi (cost of compliance).
(iii)
Kuweka mazingira yatakayoiwezesha Tanzania kushindana katika ulingo wa
biashara ya Kimataifa, ambayo ni pamoja na kuvutia uwekezaji kutoka nje ya nchi.
(iv)
Kuwa na mfumo wa kodi ambao unatabirika.
(v)
Kutoa upendeleo maalum kwa baadhi ya sekta (kwa mfano kilimo) ambazo
zinapewa kipaumbele cha juu katika maendeleo ya nchi, katika kuondoa umaskini.
28.
Mheshimiwa Spika,
misingi hii ya sera za kodi imeainishwa katika hatua
mpya za mapato nitakazopendekeza hivi punde.
SERA
ZA MATUMIZI:
29.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha wa 2001/2002,
sera za matumizi zinalenga katika kutekeleza azma ya Serikali ya
kupunguza umaskini niliyoielezea hapo awali.
Hata hivyo, kutenga mgao mkubwa wa fedha kwa sekta
zinazopewa kipaumbele kutakuwa na matokeo yanayotarajiwa iwapo tu, fedha hizo
zitasimamiwa vizuri. Kwa
mantiki hii, Serikali kuanzia mwezi Julai itatekeleza kikamilifu Sheria ya Fedha
za Umma (Public Finance Act) na ile ya
Ununuzi wa Vifaa vya Umma (Public
Procurement Act). Aidha,
mianya inayofanya vyombo vya Serikali kukopa bidhaa na huduma bila idhini na
kusababisha Serikali kulimbikiza madeni itazibwa. Mfumo wa Kompyuta wa
IFMS sasa umeanza kutumika kwa kila Wizara na pia umesambazwa hadi Mikoani
ili kuwezesha taarifa za mapato na matumizi kupatikana Hazina moja kwa moja
katika mtandao wa kompyuta. Nia
ni kuwa na mtandao huo hadi ngazi ya Halmashauri za Wilaya.
Aidha, utaratibu wa matumizi kwa fedha taslim 'Cash Budget' utaendelezwa
lakini kwa kutoa fedha kwa vipindi vya miezi mitatu mitatu
badala ya kila mwezi kwa sekta muhimu
(priority sectors) . Sekta nyingine zitaendelea kupewa fedha kila mwezi,
pamoja na maelezo kuhusu matarajio ya miezi mitatu inayofuata. Marekebisho haya
ya utaratibu wa cash budget' yana lengo la kusaidia Maafisa Wahasibu kuwa na
uhakika wa kiasi cha fedha wanazotegemea ili waweze kupanga matumizi yao kwa
ufanisi zaidi na kwa kiasi kile tu cha mgao uliopo.
Utaratibu huu umeongeza sana nidhamu ya matumizi kuliko ilivyokuwa awali
ambapo tabia ya ‘ponda mali’ ilishamiri.
30.
Mheshimiwa
Spika, eneo
lingine ambalo linafuja fedha za serikali na ambalo halina budi kupatiwa
ufumbuzi ni lile la mifuko mbalimbali iliyoundwa kusaidia vikundi au sekta
maalum. Mifuko hiyo ni pamoja na
ule wa pembejeo, mfuko wa vijana, mfuko wa wanawake na mingine.
Sote tunajua kwamba fedha zinazotolewa kupitia mifuko hii hazirudi,
na hivyo matarajio ya
kufanya mifuko hii iwe mifuko endelevu, hayapo.
Utaratibu mpya wa kuendesha mifuko hii unatayarishwa.
Njia nzuri ni kutumia benki za hapa nchini kusimamia mifuko hiyo chini ya
kanuni za huduma za mikopo midogo midogo (microfinance regulations).
Kwa hivyo fedha za mifuko hiyo hazitatolewa mpaka hapo utaratibu mzuri
utakapobuniwa na kuamuliwa.
31.
Mheshimiwa Spika, ili
nchi iweze kupanga mipango yake ya maendeleo kwa uhakika zaidi, ni muhimu kuwa
na takwimu sahihi za idadi ya wananchi wake.
Nchi yetu haijafanya
sensa kwa
zaidi ya miaka kumi sasa.
Kwa kuzingatia ukweli huu, mwezi Agosti mwaka 2002, tunategemea kufanya
sensa ya watu nchini kote. Ili
kufanikisha zoezi hilo maandalizi yanatakiwa yaanze sasa.
Kwa hivyo, Bajeti ya 2001/2002 imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni
8.0 kugharamia maandalizi yanayotakiwa.
Nachukua fursa hii kuwaomba wananchi kujiandikisha itakapotangazwa kwani
ni zoezi muhimu sana ambalo limeahirishwa mno.
MASLAHI YA WATUMISHI
32.
Mheshimiwa Spika,
Serikali inatambua hali isiyoridhisha ya maisha ya watumishi wake kutokana na
mishahara midogo. Hali hii
imesababisha baadhi ya watumishi wasio waadilifu kushawishika kujihusisha na
vitendo vya wizi, rushwa au hujuma na pia kuwa na ufanisi mdogo katika sehemu
zao za kazi. Ili kurekebisha hali
hii, Serikali katika mwaka huu wa fedha yaani 2001/2002, imetenga fedha kwa
ajili ya nyongeza
ya mishahara ya watumishi wake. Kiasi
kilichotengwa kwa zoezi hilo ni shilingi bilioni 30.
Idara Kuu ya Utumishi itatoa maelezo kuhusu marekebisho hayo mara
itakapokamilisha uchambuzi. Aidha, kwa upande wa wastaafu, Serikali inatarajia kuongeza
kiwango cha chini cha pensheni kwa asilimia 20. Vile
vile katika mwaka wa fedha wa 2001/2002, Serikali itaanza kutekeleza uamuzi wake
wa kuanzisha bima ya matibabu kwa
watumishi wa umma baada ya kukamilisha taratibu zote zinazotakiwa.
Chini ya
utaratibu huo, mwajiri
atachangia asilimia tatu (3%) ya
mshahara wa mtumishi na mtumishi mwenyewe atachangia kiasi kama hicho.
Utaratibu huu utaanza mwezi Julai, 2001 na tayari shilingi bilioni 11
zimetengwa katika bajeti hii.
33.
Mheshimiwa
Spika, mwezi Aprili, 2001 Bunge lilipitisha sheria ya kuanzisha mfuko wa
elimu wenye lengo la kusaidia kugharamia elimu ya juu.
Pamoja na mambo mengine mfuko huo utatumika kusomesha watoto ambao wazazi
wao hawana uwezo. Waziri mwenye dhamana ya elimu ya juu atatoa kanuni na
taratibu za matumizi ya mfuko huo. Kwa
kuanzia, bajeti hii imetenga shilingi bilioni 5 kwa ajili ya mfuko huo.
MISAADA NA MIKOPO NAFUU YA NJE
34.
Mheshimiwa Spika, ingawa juhudi zitaimarishwa za kuongeza mapato ya
ndani, kiasi kinachotarajiwa kukusanywa bado hakitaweza kutosheleza mahitaji ya
msingi ya bajeti ya Serikali. Serikali
bado itahitaji kupata mikopo nafuu na misaada kutoka nje.
35.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hatua za Serikali za kusimamia sera za kukuza uchumi na
kuondoa umasikini, Wafadhili wana nia ya kuendelea kuisaidia Tanzania. Mpango wa
PRGF unaogharimiwa na Shirika la Fedha
la Kimataifa - IMF
umeingia mwaka wa pili. Katika mwaka 2001/2002, tunategemea kupata jumla ya
dola za Kimarekani 51.6 milioni sawa na shilingi
bilioni 46.440. Fedha
hizo zitasaidia kutunisha akiba ya fedha za kigeni kwa ajili ya uagizaji bidhaa
kutoka nje na kulipa madeni ya nje. Aidha,
Benki ya Dunia - World
Bank, chini ya Mpango wa kurekebisha uchumi, (PSAC) inatarajiwa kutoa mkopo nafuu kiasi cha dola za Kimarekani 80.0
milioni sawa na shilingi bilioni 72.0 katika
mwaka 2001/2002. Tunategemea
pia kupata kiasi cha dola za Kimarekani 25 milioni, sawa na shilingi bilioni
22.5 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AFDB).
36.
Mheshimiwa Spika,
pamoja na mikopo nafuu
tunayotegemea kupata kutoka Mashirika
ya Fedha ya Kimataifa, tukifanikiwa kufikia hatua ya mwisho ya kusamehewa madeni
chini ya mpango wa HIPC (completion
point) wadai wetu watatupa msamaha mkubwa zaidi wa madeni, unaokadiriwa kuwa dola za Kimarekani 100
kwa mwaka, sawa na shilingi 90.0 bilioni. Aidha, tunategemea katika mwaka 2001/2002, Wahisani
marafiki wataendelea kuchangia katika programu mbalimbali kwa ajili ya kupunguza
umaskini.
Makisio
yanaonyesha kwamba Wafadhili wetu, Nchi marafiki, na Jumuiya ya Ulaya
watatupatia misaada (grants) kiasi cha dola za Kimarekani 225 milioni sawa na shilingi
202.5 bilioni, kupitia
kwenye mpango wa kusaidia bajeti kwa ajili ya kupunguza umaskini (PRBS),
na misaada maalum kwa programu za kapu la sekta (basket funding). Tunakadiria
pia kupata dola za Kimarekani 336 milioni sawa na shilingi 302.272 bilioni kwa
ajili ya miradi ya maendeleo.
37.
Mheshimiwa Spika,
naomba Waheshimiwa Wabunge waungane nami kumpongeza kwa dhati, kwa niaba ya
wananchi, hasa maskini, Mheshimiwa Rais Benjam William Mkapa kwa mchango wake
mkubwa wa kutupatia misaada na misamaha hiyo.
Haya ni matokeo ya juhudi zake makini katika kusimamia uchumi, kuinadi
nchi yetu ng’ambo na kuiletea Tanzania sifa kubwa kama nchi inayo piga hatua
nzuri ya maendeleo, inayotawaliwa kwa msingi wa demokrasia, haki za binadamu na
utawala bora, na ambayo mambo yake ni ya ukweli, uwazi na yenye kutabirika.
Tanzania ni miongoni mwa nchi za HIPC nne tu duniani ambazo zimekamilisha
mkakati kabambe unaokubaliwa na jumuiya ya kimataifa na hivyo kuwa na sifa ya
kusamehewa madeni.
MFUMO
WA MAKISIO YA BAJETI YA MWAKA 2001/2002:
38.
Mheshimiwa Spika, kama
nilivyosema hapo awali bajeti
ya mwaka 2001/2002, inalenga kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama
Tawala, ambayo imeweka kipaumbele kikubwa katika kuondoa umaskini uliokithiri
nchini mwetu. Kwa kuzingatia sera
za uchumi zilizoelezwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na
Ubinafsishaji, pamoja na zile nilizoelezea hapo awali, kwa msingi wa mfumo wa
kodi wa sasa bila ya marekebisho yoyote, Serikali
inatarajia kukusanya
mapato ya ndani
ya jumla ya shilingi 991.198 bilioni katika mwaka wa 2001/2002. Kwa upande wa matumizi, Serikali imepanga kutumia jumla ya shilingi
1,764.737 bilioni (trilioni 1.76).
39.
Mheshimiwa Spika,
kwa
kuzingatia makisio ya kukusanya shilingi 991.198 bilioni kulingana na mfumo wa
sasa wa kodi, na matumizi ya jumla ya shilingi 1,764.737 bilioni, (1.76
trilioni) pengo la shilingi 773.539 bilioni
linajitokeza. Kama nilivyoeleza hapo awali, katika mwaka 2001/2002,
Wafadhili mbali mbali wanatarajia kutupatia misaada na mikopo nafuu (ikijumuisha
misamaha ya madeni) ya jumla ya shilingi 649.643 bilioni.
Kati ya fedha hizo, shilingi 283.770 bilioni ni mikopo na misaada
itakayopitia kwenye bajeti chini ya programu mbali mbali, shilingi 63.600
bilioni ni kutokana na misamaha ya madeni, na shilingi 302.272 bilioni ni mikopo
na misaada kwa ajili ya miradi ya maendeleo.
Ni muhimu kueleza hapa kuwa baadhi ya wafadhili bado wameendelea kutoa
misaada kwa ajili ya miradi ya maendeleo nje ya bajeti ya Serikali.
Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa misaada yote toka
kwa wafadhili
itatolewa katika
utaratibu wa
‘exchequer’
yaani kujumuishwa katika bajeti ya Serikali.
Kiwango hiki cha mchango wa wafadhili kinapunguza pengo hadi kufikia
shilingi 123.896 bilioni.
40.
Mheshimiwa Spika,
serikali
inategemea kupunguza akiba yake (reserve) ya
ndani kwa kiasi cha shilingi 69.910 bilioni.
Aidha, Serikali katika mwaka 2001/2002, inatarajia kupata shilingi 20
bilioni kutokana na uuzaji wa sehemu ya hisa katika mashirika ambayo Serikali ni
mbia. Maeneo haya mawili ya vianzio
vya fedha yanapunguza pengo hadi kufikia shilingi 33.986 bilioni ambazo inabidi zipatikane kwa
kuchukua hatua mpya za mapato.
41.
Mheshimiwa Spika, katika
jitihada za kuboresha mfumo wa kodi, ada, na taratibu za kukusanya mapato ya
Serikali, inapendekezwa kufanya marekebisho ya aina mbalimbali katika kodi.
Lengo la marekebisho haya ninayopendekeza ni kufanikisha malengo
niliyoyaeleza hapo awali, ambayo ni pamoja na kuipatia Serikali mapato
yaliyopangwa katika bajeti hii, kuleta uwiano mzuri wa kodi katika uchumi, na
kupunguza adha na kero kwa wananchi, kuweka mazingira mazuri zaidi ya kutumia
nguvu kazi na rasilimali nyingine katika maeneo muhimu ya uchumi kama vile
kilimo, viwanda, utalii, madini, na biashara.
Aidha, hatua hizi za kodi zitasaidia sana mkakati wetu wa kupiga vita
umaskini.
42.
Mheshimiwa Spika,
Serikali inapendekeza kufanya marekebisho katika maeneo yafuatayo:-
(a)
Mfumo wa ushuru wa forodha;
(b)
Mfumo wa kodi ya mapato;
(c)
Mfumo wa kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT);
(d)
Mfumo wa kodi ya ushuru wa bidhaa;
(e)
Kuanzisha kodi
mpya katika michezo ya kubahatisha;
(f)
Kodi za Serikali za Mitaa;
(g)
Marekebisho ya baadhi ya sheria;
(h)
Marekebisho ya kodi ya huduma za viwanja vya ndege;
(i)
Kodi ya pango la ardhi kwa mashamba;
(j) Kodi na ada zinazokusanywa na Serikali Kuu.
Mfumo
wa Ushuru wa Forodha
43.
Mheshimiwa Spika,
kuhusu mfumo wa ushuru wa forodha, marekebisho yafuatayo yanapendekezwa:-
(a) Viwango vya ushuru wa forodha (tariff bands) vipunguzwe kuwa vitatu (ukiacha cha sifuri) badala ya vinne vya sasa. Kutokana na pendekezo hili, viwango vipya vya ushuru wa forodha vikilinganishwa na vya sasa vitakuwa kama ifuatavyo:-
|
Viwango |
Viwnago |
Husika |
| 0% |
0% | (i)
Pembejeo na zana za kilimo, ufugaji, uvuvi,
madawa ya mifugo na binadamu, malighafi za kutengeneza madawa. |
| 5% | 0% | (ii) Malighafi,
bidhaa za uzalishaji na ukarabati |
| 10% | 10% | (iii)
Malighafi zilizosindikwa kiasi na vipuri mbali ya vile vya magari
(semi-processed input and spares) |
| 20% |
15% |
(iv) Malighafi zilizosindikwa kikamilifu yaani (fully processed inputs) na vipuri vya magari |
| 25% |
25% | v) Bidhaa
za walaji (consumer goods) |
44.
Mheshimiwa Spika,
matokeo ya marekebisho haya ni kwamba ushuru wa forodha sasa utatozwa katika viwango
vitatu tu – yaani asilimia 10, 15 na 25. Bidhaa ambazo sasa hivi zinatozwa asilimia 5 ya ushuru,
hazitalipa ushuru wa forodha. Matumaini
ya Serikali ni kwamba hatua hii itapunguza gharama za uzalishaji hasa kwa
viwanda na wawekezaji wengine wanaoagiza kutoka nje malighafi na bidhaa za
uzalishaji.
45.
Mheshimiwa Spika,
marekebisho haya ya mfumo wa ushuru wa forodha yanakadiriwa kupunguza mapato ya
Serikali kwa kiasi cha shilingi 18.791 bilioni.
Sambamba na punguzo hilo la mapato, mfumo mpya wa viwango vya ushuru
unategemewa kupunguza mapato ya VAT, kwa kiasi cha shilingi 1.939 bilioni kwa
bidhaa zinazoagizwa kutoka nje.
46.
Mheshimiwa Spika, kwa
kuzingatia marekebisho ya mfumo wa ushuru wa forodha niliyoyaelezea hapo juu,
hakuna haja ya kuendelea kuwa na Tangazo la Serikali Na. 433 (Government Notice
No. 433). Tangazo hilo liliweka viwango tofauti na vile vilivyomo katika kitabu
cha Ushuru (Tariff Book) kwa baadhi ya malighafi za viwanda vya ndani ili kuvipa
upendeleo maalum. Viwango vipya vya
ushuru vinavyopendekezwa tayari vimezingatia azma hiyo.
Hatua hii inategemewa kupunguza mapato kwa kiasi cha shilingi 3.5
bilioni.
Kutoza
Ushuru wa Muda (Suspended Duty) kwa Baadhi ya Bidhaa Zinazoagizwa Kutoka Nje
47.
Mheshimiwa Spika,
Ili kuhakikisha kuwa kuna ushindani wa haki katika soko la ndani kati ya bidhaa
zinazozalishwa hapa nchini na zile zinazotoka nje, inapendekezwa kutoza ushuru
wa muda (suspended
duty) kwa baadhi ya bidhaa kutoka nje.
Bidhaa hizo zimeorodheshwa katika Muswaada wa sheria ya Fedha ya mwaka
2001. Hatua hii itaongeza
mapato ya Serikali kwa shilingi 2.4 bilioni.
Utaratibu
Mpya wa Kutathmini Bidhaa kutoka Nje:
48.
Mheshimiwa
Spika, ili kuzingatia matakwa ya Shirika la Biashara la Kimataifa (World
Trade Organisation) ambako Tanzania ni mwanachama, utaratibu wa kutathmini
bidhaa kutoka nje kwa ajili ya kutoza kodi, umebadilika. Utaratibu
ujulikanao kama "Agreement on Customs Valuation" (ACV) ndio unatumika
sasa. Kutokana na badiliko hili
hakuna tena matumizi ya mtindo wa “bei ya chini ya kukadiria kodi” (minimum
dutiable value -MDV) isipokuwa kwa Sukari
inayoagizwa kutoka nje ambayo inatawaliwa na mkataba maalum kati ya
Serikali na wawekezaji.
49.
Mheshimiwa
Spika,
napendekeza kulifanyia marekebisho Tangazo la Serikali No. 133 la mwaka
1996 ili kuweka ukomo (Cap) wa kiwango cha ushuru wa forodha wa asilimia 5 kwa
mwezi kitakachotozwa waingizaji kwa muda mfupi wa vifaa na zana za uwindaji wa
kitalii. Hatua hii inalenga kuondoa
kero na lawama zilizokuwa zinatolewa na sekta ya utalii, na haina madhara kwa
mapato ya Serikali.
Marekebisho
ya Mfumo wa Kodi ya Mapato
50.
Mheshimiwa
Spika, inapendekezwa pia kufanya marekebisho kadhaa katika eneo la kodi
ya mapato kama ifuatavyo:-
(a)
Kodi ya zuio kwenye bidhaa na huduma (withholding
tax) on goods and services) inafutwa kwa wale wote ambao wana kitambulisho cha walipa kodi
(tax payer identification number - TIN). Hatua
hii inatarajiwa kupunguza
mapato kwa kiasi cha shilingi 12.179 bilioni.
(b)
Kwamba kipengele cha "additional 15% capital allowance on unredeemed
qualifying capital expenditure" kwenye
Sheria ya Madini ya mwaka 1998 (The Mining Act, 1998) sasa kitumike kwa
wawekezaji wa zamani tu. Wawekezaji wapya wasipewe unafuu huo. Hatua hii inafuatia ukweli
kwamba, sehemu ya 17 ya
Sheria hiyo tayari inaruhusu punguzo la asilimia 100 (100% capital allowance). Aidha, hatua hii itasaidia pia kurahisisha usimamizi wa
kodi katika sekta ya madini. Pendekezo hili halitaathiri
mapato ya Serikali.
(c)
Kurekebisha kifungu cha 87(1) cha Sheria ya madini ya mwaka 1998 ambacho
kinaruhusu mchimbaji madini kuahirisha ulipaji wa mrahaba (royalty) au
kurejeshewa mrahaba aliolipa endapo atakuwa na matatizo ya ukwasi.
Napendekeza kwamba kifungu hiki cha sheria kiwahusu wawekezaji wa zamani tu.
Marekebisho haya hayategemewi kuipatia au kuipotezea Serikali mapato.
(d)
Napendekeza kuunganisha
kodi za “Housing Levy” na ile ya
“VETA” na kuwa kodi moja ya kuendeleza ufundi stadi (skills
development levy). Kiwango cha
kodi hiyo
kitakuwa asilimia
sita (6%) ya gharama za mishahara (wage bill).
Kadhalika, kodi hii sasa itakusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
na kugawanywa kama ifuayavyo: theluthi mbili ya kodi itawasilishwa Hazina, na
theluthi moja itawasilishwa Taasisi ya VETA.
Hatua hii itapunguza gharama kwa waajiri (cost of labour) na haipunguzi
mapato ya Serikali wala ya VETA.
(e)
Napendekeza kuondoa kodi ya zuio kwenye riba (interest) kwa mikopo
iliyokopwa nje ya nchi. Pendekezo
hili lina lengo la kuhuisha kodi hiyo ya riba na kuboresha mazingira ya
uwekezaji. Hatua hii itapunguza mapato kwa
shilingi 378 milioni.
(f)
Napendekeza kufuta
kipengele cha gawio hisia (deemed dividend) kwenye Sheria ya Kodi ya
Mapato. Pendekezo hili linalenga kumwondolea mamlaka Kamishna wa Kodi ya Mapato
ya kujitangazia gawio endapo kampuni haitafanya hivyo ili kuondoa kero iliyopo
hivi sasa kwa kampuni zinazolipa kodi.
(g)
Napendekeza kufuta
malipo ya awali ya kodi ya mapato ambayo mfanya biashara hutakiwa kulipa kabla
hajaanza biashara. Pendekezo hili linalenga kuwawezesha hasa
wafanyabiashara ndogo ndogo kupata leseni na kuanza biashara halali,
badala ya utaratibu wa sasa ambao wengi wanashindwa kulipa kodi hiyo ya awali na
hivyo kulazimika kufanya biashara bila leseni. Hatua hii inategemewa
kupunguza mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi 3.179 billioni.
Kodi
ya Ongezeko la Thamani (VAT)
51.
Mheshimiwa
Spika, katika eneo la kodi ya VAT, napendekeza kufanya marekebisho
yafuatayo:-
(i)
Nafuta
msamaha wa kodi ya VAT kwa Serikali na taasisi zake.
Kwa maana hiyo basi, Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na Taasisi
zinazotegemea Serikali Kuu kwa bajeti zao sasa zitalipa
Kodi ya
Ongezeko la
Thamani (VAT).
Hata hivyo, misamaha hii ya kodi itaendelea kutolewa kwa vifaa na huduma
kwa ajili ya miradi inayofadhiliwa na wafadhili na mashirika na taasisi za
kujitolea, kulingana na sheria na mikataba maalum iliyopo.
Hatua hii inategemewa kuipatia
Serikali jumla ya shilingi 56.0 bilioni kwa mwaka 2001/2002.
(ii)
Kwa kuzingatia pendekezo
nitakalotoa hivi punde la kuanzisha kodi mpya ya michezo ya kubahatisha (gaming tax), napendekeza pia kuondoa
kodi ya ongezeko la thamani kwenye michezo yote ya kubahatisha ili
kurahisisha utozaji wa kodi hiyo mpya. Hatua hii inategemewa kupunguza
mapato ya Serikali kwa kiasi cha shilingi 2.0 bilioni, ambayo yatafidiwa
na kodi mpya inayopendekezwa.
(iii)
Naondoa kodi ya VAT kwa usafiri wa barabara (ground
transport) kwa watalii (tour operators). Lengo la hatua hii ni kuleta usawa na haki katika biashara ya
utalii. Hatua hii itapunguza mapato ya
Serikali kwa kiasi cha Shs. 500 milioni.
(iv)
Napendekeza kuondoa kodi ya VAT kwa vifungashio vya maziwa (milk
packaging materials). Hatua hii ina
lengo la kusaidia kupunguza gharama
za viwanda vya kutengeneza maziwa ili yaweze kuuzwa kwa bei nafuu na pia
kumpatia mfugaji soko la maziwa ghafi. Pendekezo
hili litapunguza
mapato ya Serikali kwa kiasi cha Shs. 400 millioni. Aidha, inapendekezwa
kufuta uingizaji wa maziwa ya unga na kuweka ushuru wa
ziada "suspended duty" wa
asilimia ishirini na tano (25%) kwa aina nyingine zote za maziwa kutoka nje isipokuwa
maziwa ya watoto (infant formula).
(v)
Napendekeza kuondoa
kodi ya VAT katika ‘Computers’, ‘Printers’ zake na ‘Accessories’
zake. Hatua hii
inalenga kuharakisha kasi ya Tanzania kuingia katika karne ya 21 ya mawasiliano
na uchumi unaotegemea mtandao wa kompyuta katika zama za sasa za utandawazi.
Hii ni pamoja na kutoa motisha kwa vijana washawishike kujihusisha na
shughuli za Kompyuta, kama wenzao wanavyofanya ulimwenguni kote.
Ni tegemeo langu kuwa shule, vyuo na taasisi za elimu zitachukua fursa
hii kuanza kufundisha masomo ya kompyuta na hasa kutumia kompyuta zaidi kuliko
sasa. Hatua hii itapunguza mapato ya
Serikali kwa kiasi cha shilingi 1.544 bilioni.
(vi)
Napendekeza kuondoa
kodi ya VAT kwenye vifaa vya hospitali, na kodi zote kwa madawa ya
walioadhirika na ukimwi, malaria na kifua kikuu. Pendekezo hili linalenga kuongeza idadi na aina ya mashine na
vifaa vya kuchunguza magojwa na kutibu wagonjwa ili kutoa unafuu kwa sekta ya
tiba na hivyo kusaidia kupunguza gharama ya vifaa hivyo na madawa ambavyo hata
bila ya kodi bado ni aghali sana. Hatua
hii pia inajibu lawama ambazo zimetolewa kwa Serikali kutoka mashirika na
taasisi za kujitolea kwamba kodi katika vifaa vya kuokoa maisha ya binadamu ni
kero kubwa. Hatua hii pia
itapunguza gharama kubwa mno za kupeleka watu kutibiwa nje ya nchi na haitegemewi kupunguza mapato
ya Serikali. Aidha, pendekezo kuhusu dawa za ukimwi lina lenga kumwongezea uhai
mgonjwa na linaenda sambamba na fikra za kitaifa na kimataifa.
Ieleweke kuwa bado hakuna dawa za kuponyesha kabisa ugonjwa huu na kuwa
zilizopo bado ni aghali sana sana.
(vii)
Napendekeza kuondoa kodi ya VAT
kwa nyuzi (yarn) zinazosokotwa nchini.
Pendekezo hili linalenga kupunguza gharama ya nyuzi hizi na kuongeza
ajira kwa wafumaji wadogo wadogo wanaotumia mikono (hand
looms). Hatua hii itapunguza
mapato ya Serikali kwa kiasi cha Sh.9 milioni.
(viii)
Napendekeza kuondoa kodi ya VAT kwenye vifaa vya uwekezaji katika miradi
ya elimu. Pendekezo hili linalenga
kuvutia wawekezaji wa shule, vyuo na taasisi zenye hadhi ya kimataifa badala ya
kupeleka wanafunzi nje ya nchi, hasa nchi jirani.
Hatua hii pia inajibu malalamiko yanayotolewa kwamba sera ya kodi
inakwamisha uwekezaji katika elimu ya kisasa.
Hatua hii itapunguza mapato ya Serikali kwa Sh.88.7 milioni.
Mfumo
wa Kodi ya Ushuru wa Bidhaa (Excise)
52.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu mfumo wa Ushuru wa Bidhaa inapendekezwa kufanya
marekebisho yafuatayo:
(a)
Napendekeza
kufanya marekebisho ya viwango vya
ushuru wa bidhaa kwenye bidhaa za mafuta ya petroli ili viwe kama ifuatavyo:
| Shs. Kwa Lita |
||
| (i) Liquified Petroleum Gas (LPG) | 228.0 |
|
| (ii) Motor Spirit Premium (MSP) | 146.0 | |
| (iii) Motor Spirit Regular (MSR) | 135.0 |
|
| (iv) JET A I | 56.0 | |
| (v) Illuminating kerosine (IK) | 122.0 |
|
| (vi) Gas Oil (GO) | 127.0 |
|
| (vii) Industrial Diesel Oil (IDO) | 201.0 |
|
| (viii) Heavy Furnace Oil (HFO) | 35.0 |
Hatua hii ina lengo la kulinda mapato yatakayopotea kutokana na kufuta
ushuru wa forodha wa asilimia tano (5) kufuatia marekebisho niliyotaja awali ya
mfumo wa ushuru wa forodha. Kutokana
na marekebisho hayo, mafuta ya petroli sasa yatakuwa na kodi tatu tu, ambazo ni
ushuru wa bidhaa (excise duty), VAT na ada ya barabara
(fuel levy). Hatua hii italinda mapato ya Serikali
kwa kiasi cha shilingi
8.311 bilioni. Napenda kusisitiza kwamba pendekezo
hili haliongezi kodi katika bidhaa za mafuta ya petroli, ila linapunguza
idadi ya kodi hizo.
(b)
Napendekeza pia kupunguza
ushuru wa bidhaa (excise duty)
kwa
mvinyo unaotengenezwa kwa
zabibu za hapa nchini kutoka shilingi
700 kwa lita za sasa hadi shilingi 350 kwa
lita. Pendekezo hili lina nia ya
kuhamasisha upya kilimo cha zabibu na kupanua viwanda vya mvinyo Mkoani Dodoma
na hivyo kuondoa umaskini humo. Hatua
hii itapunguza mapato ya Serikali kwa kiasi kidogo sana cha
shilingi milioni moja na nusu tu.
(c)
Sambamba na hatu hii, napendekeza pia kuanzisha
utaratibu wa kuweka stampu ya kodi ‘tax stamp’ kwenye mvinyo
unaoagizwa kutoka nje ili kudhibiti ukwepaji kodi katika bidhaa hii na kulinda
viwanda vya mvinyo nchini. Utaratibu
huo wa kuweka ‘tax stamp’ kwenye mvinyo
kutoka nje utaanza kutekelezwa mwezi Januari 2002.
(d)
Napendekeza kurekebisha ushuru wa bidhaa ‘excise
duty’ kwa asilimia 5 (5%) kwenye bidhaa za sigara, bia na soda ili kuhuisha
kodi hiyo kulingana na mfumuko wa bei. Pendekezo
hili linategemewa kuipatia
Serikali mapato ya ziada ya shilingi 3.624 bilioni katika mwaka
2001/2002.
Kodi
Mpya kwenye Michezo ya Kubahatisha:
53.
Mheshimiwa
Spika, kutokana na
uzoefu ambao Serikali sasa inao kuhusu michezo ya kubahatisha, napendekeza kuanzisha
kodi ya michezo ya kubahatisha (gaming tax). Napendekeza kodi hiyo mpya iwe katika viwango vifuatavyo:-
(i)
Casino:
(a) shilingi 500,000 kwa
meza moja kwa mwezi.
(b)
shilingi 100,000 kwa mashine kwa mwezi.
(ii)
Bahati nasibu binafsi (private
lotteries) – asilimia 60 ya mauzo yote (gross sales)
(iii)
Mashine
za Sloti (slot
machines) shilingi 20,000 kwa mashine kwa mwezi.
Kodi
hii mpya inatarajiwa kuipatia Serikali mapato
ya kiasi cha shilingi 7.0 bilioni katika mwaka 2001/2002.
Napendekeza kwamba asilimia 92 ya mapato hayo iingie Serikalini na
asilimia 8 iliyobaki iende kwa chombo cha usimamizi (regulator).
Kodi
za Serikali za Mitaa:
54.
Mheshimiwa
Spika, katika eneo hili, nakumbushia na kusisitizia:
(i)
Utekelezaji wa dhati wa sheria inayotaka Waziri mwenye dhamana ya
Serikali za Mitaa kushauriana na Waziri wa Fedha kabla ya kufanya marekebisho
katika sheria za kodi na ada mbalimbali za Serikali za Mitaa.
Hii ni kutokana na kudhihirika kuwa bado kuna mgongano kati ya Sera za
Kodi Kitaifa ambazo hutangazwa na Waziri wa Fedha na kodi au ada mbalimbali
zinazoanzishwa na Serikali za Mitaa. Hatua
hii ina lengo la kuondoa kero ya kuwepo kwa kodi nyingi mno na hasa kwa
wakulima, wafanya biashara na wenye viwanda.
(ii)
Ukomo wa kiwango cha asilimia 5 cha ushuru wa mazao ya mkulima, na
mfugaji uzingatiwe ili kuondoa utata uliopo sasa wa baadhi ya Halmashauri za
Wilaya kutoza viwango zaidi ya hicho na hivyo kuleta lawama kutoka kwa wananchi
wa vijijini na vyama vya ushirika.
(iii) Napendekeza kuhamisha utoaji leseni za biashara zifuatazo kutoka Serikali za Mitaa kwenda Serikali Kuu:-
(a)
Biashara za uingizaji bidhaa (import trade)
(b)
Wakala wa kulipwa (commission agents)
(c)
Uwakilishi wa Wana-viwanda (manufacturers’
representatives)
(d)
Wakala wa Wasafiri (travel agents)
(e)
Kambi za Watalii (tourist camps)
(f)
Wauza Magari (motor vehicle dealers)
(g)
Wahudumu
kwa Watalii (tour operators); na mwisho
(h)
Masonara
(goldsmith)
Leseni hizo zitatolewa na
mamlaka zinazosimamia maeneo husika. Hatua
hii ina lenga kuhuisha usimamizi (regulation) wa maeneo hayo ambayo yana upeo wa
kitaifa na wa kimataifa.
(iv)
Napendekeza kuhamishia Halmashauri za Wilaya uandikishaji na utozaji
leseni za biashara na viwanda vidogodogo,
na shughuli zote ndogo ndogo (micro
enterprises). Lengo la hatua hii ni kuoanisha (rationalise) leseni mbali mbali kati ya Serikali Kuu na Serikali za
Mitaa na pia kuondoa usumbufu na gharama kwa walipa kodi husika.
Inalenga pia kupunguza gharama na usumbufu kwa wahusika.
(v)
Napendekeza pia kwamba masharti ya kutoa leseni za biashara yapunguzwe sana.
Njia moja ya kupunguza masharti hayo na kuondoa kero ni kuwa na kituo
kimoja (one stop centre) cha kuandikishia na kutolea leseni za biashara
vijijini, wilayani, mikoani, na wizarani.
(vi)
Napendekeza kuwa leseni za utaalam (professional licence) kwa watu
walioajiriwa zifutwe,
kwani ni kero, zinaongeza gharama za ajira, na kupunguza ajira hasa za wananchi
wasomi.
(vii)
Inapendekezwa pia kwamba sheria ya Uhamiaji ihuishwe na ile ya Biashara
ili kuondoa kero na utata uliopo
sasa hasa kuhusu wawekezaji.
Marekebisho
Mengine ya Baadhi ya Sheria
55.
Mheshimiwa
Spika, katika eneo hili, napendekeza kufanya marekebisho yafuatayo:-
(i)
Kuhusu Sheria ya Ushuru wa Barabara yaani, (Road
Toll Act, 1985). Napendekeza
kubadilisha jina la kodi ya “road toll” liwe “fuel
levy”. Madhumuni ya
hatua hii ni kuondoa utata uliojitokeza kwa baadhi ya walipa kodi hiyo ambao
hutumia mafuta ya petroli katika vyombo visivyotumia barabara kama vile reli na
vyombo vya majini au katika mitambo. Hawa
wanadai kwamba wasingetakiwa kulipa kodi isiyo wahusu.
Kwa hiyo sheria ya “road toll” (Road Toll Act, 1985) irekebishwe ili
kuondoa utata huo na kila anayetumia “fuel” alipe kodi hiyo.
(ii)
Napendekeza kufanya marekebisho katika Sheria ya Ushuru wa
Stempu (Stamp Duty Act No. 20 of
1972) kama ifuatavyo:
(a)
Ushuru wa Stempu kwa mikataba
ya ukodishaji (lease agreements) uwe asilimia 0.96 au shilingi 10.0
milioni kutegemea ipi ni ndogo. Lengo
la hatua hii ni kupunguza gharama za mikataba ya ukodishaji ambazo
zimelalamikiwa sana na washika dau kwamba zinaathiri uwekezaji.
(b)
Ushuru
wa Stempu kwa mapato yatokanayo na mazao
ya kilimo unafutwa. Ushuru
huu umekuwa kero kubwa kwa
wakulima. Kuondolewa kwake
kutalinda pato la mkulima na kusaidia kupunguza umaskini.
(c)
Ushuru wa stempu kwa mapato yanayotokana na kodi ya pango (rental
income) unapunguzwa na kuwa asilimia 1.5. Lengo ni kuweka mazingira mazuri ya kuvutia uwekezaji
katika sekta ya makazi, na
kuzuia ukwepaji
wa kodi
hiyo. Hatua hii itapunguza
mapato kwa kiasi cha shilingi 896 milioni.
Marekebisho
ya Kodi ya Huduma za Viwanja vya Ndege (Airport
Departure Charges):
56.
Mheshimiwa Spika,
katika eneo hili
inapendekezwa kufanya marekebisho yafuatayo:
(i)
Kuongeza
kidogo kiwango cha kodi kwa wasafiri waendao nje ya nchi kuwa dola za Kimarekani
30 badala ya 20 za sasa.
(ii)
Kuongeza kiwango cha kodi kwa wasafiri wa ndani kutoka shilingi 3,000/=
hadi shilingi 5,000/=.
Hatua
hii inategemewa kuipatia Serikali jumla ya
shilingi 2.64 bilioni. Lengo la hatua hii ni kuvihuisha viwango hivyo ili
viwiane na hali halisi ya sasa.
57.
Mheshimiwa
Spika, napendekezwa kurekebisha
kodi ya Pango la Ardhi (Land Rent) kwa
Mashamba ya kibiashara
kutoka shilingi 600 kwa ekari hadi shilingi 200
kwa ekari kwa
mwaka, kwa
mashamba ya
kilimo, mifugo na misitu. Hatua
hii haitegemewi kupunguza mapato ya Serikali kwa sababu hivi sasa kodi hii
haikusanywi – kwani wenye mashamba wanasema hawaimudu.
Lengo ni kuhimiza upanuzi wa mashamba makubwa kwa kutohodhi ardhi na
kusisitiza umuhimu wa kulipia kodi raslimali hiyo.
Kodi
na Ada Zinazokusanywa na Serikali Kuu
58.
Mheshimiwa
Spika, inapendekezwa
kufanya marekebisho ya mfumo wa ada mbali mbali zinazokusanywa na Serikali Kuu.
Madhumuni ya marekebisho hayo ni kuhuisha viwango vya ada hizo ili
viwiane na hali halisi ya sasa. Maelezo
kuhusu viwango hivyo vya ada yapo kwenye muswaada wa sheria ya fedha wa mwaka
2001.
Biashara ya Mipakani
59.
Mheshimiwa
Spika, hivi karibuni Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki walikubaliana kuweka mazingira bora zaidi ya kuhamasisha uwekezaji
kwenye sekta za uchumi, miundo mbinu, na biashara kati ya nchi na nchi ndani ya
Jumuiya hiyo. Moja ya maeneo
yaliyopewa msukumo ni kurahisisha biashara ya mipakani ili wananchi wa nchi hizi
waongeze biashara kati yao kwa njia halali.
Kwa mantiki hiyo, ushuru wa forodha mipakani umepunguzwa sana.
Bidhaa kutoka Tanzania na Uganda kwenda Kenya zinapata punguzo la ushuru
wa forodha kwa asilimia 90. Kwa
maneno mengine, kama ushuru Kenya ni asilimia 25, Mtanzania akiuza Kenya analipa
asilimia 2 tu. Bidhaa za Tanzania
zikiingia Uganda zinapata punguzo la ushuru la asilimia 80.
Maana yake ni kwamba kama ushuru Uganda ni asilimia 25, Mtanzania akiuza
Uganda analipa ushuru asilimia 5 tu. Kwa
upande mwingine, chini ya makubaliano hayo, bidhaa za Kenya zikiingia Tanzania
na Uganda zinapata punguzo la ushuru la asilimia 80.
60.
Mheshimiwa
Spika, punguzo hili la ushuru ndani ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ni
changamoto kubwa kwa wananchi wetu. Nimeagiza
ofisi za Idara ya Forodha mikoani kuwaelimisha wananchi kuhusu changamoto hii,
kwa kuweka matangazo kwa njia ya mabango na nyingine, na pia wao wenyewe
kurahisisha taratibu za forodha, na kuhamasisha watu wafanye biashara halali,
kwa kulipa huo ushuru mdogo sana.
61.
Mheshimiwa
Spika, hatua hizi za kodi zitaanza kutumika tarehe 1 Julai, 2001
isipokuwa pale ilivyoelezwa vinginevyo.
Majumuisho
62.
Mheshimiwa Spika, mapendekezo haya ya marekebisho ya kodi na tozo nyingine,
yamelenga katika kuboresha mfumo wa kodi, ili kupanua wigo kwa kuongeza utii
(compliance), kuondoa kero hasa katika eneo la kilimo na mifugo, kuboresha
mazingira ya ushindani, kuweka mazingira bora na ya wazi ya uwekezaji, kusaidia
kusukuma maendeleo ya jamii kulingana na programu ya kupunguza umaskini, na
mengine mengi. Kwa ufupi,
mapendekezo haya ni ya kuchochea uchumi ukue kwa kasi na kupunguza umaskini.
MUHTASARI
63.
Mheshimiwa
Spika, muhtasari wa hatua zinazopendekezwa na matokeo yake kimapato ni
kama ifuatavyo:
| Shilingi
bilioni |
|
| (i) Mfumo wa Ushuru wa Forodha | -21.830 |
| (ii)
Marekebisho ya Mfumo wa |
-15.737 |
| (iii)
Mfumo wa Kodi ya Ongezeko la |
51.458 |
| (iv) Mfumo wa Ushuru wa Bidhaa | 11.934 |
| (v)
Kodi Mpya ya Michezo ya |
6.417 |
| (vi)
Marekebisho ya Kodi ya Viwanja vya |
2.640 |
| (vii) Mfumo wa Ushuru wa Stempu | -0.896 |
| Jumla | 33.986 |
Mapato
haya ya shilingi 33.986 bilioni yanaziba pengo la bajeti ya mwaka 2001/2002
lililoelezwa hapo awali.
SURA
YA BAJETI YA MWAKA 2001/2002:
64. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia mfumo wa bajeti kama ulivyoelezwa hapo juu, sura ya bajeti kwa mwaka 2001/2002 inakuwa kama ifuatavyo
Mapato
Shilingi
bilioni
A.
Mapato ya Ndani
1.025184 trilioni
| (i) Mapato ya Kodi | 892.228 |
|
| (ii) Mapato
yasiyo ya |
98.970 |
|
| (iii) Mapato Mapya | 33.986 |
| B. Mikopo na Misaada ya Nje ikijumuisha HIPC | 649.643
bilioni |
| C. Kupunguza akiba (Reserve) | 69.910 bilioni |
| D. Mapato kutokana na uuzaji Hisa | 20.000 bilioni |
|
Jumla ya Mapato yote |
1.764737 trilioni |
Matumizi
E.
Matumizi ya Kawaida
1.412225 trilioni
(i)
Deni la Taifa
332.590
(ii)
Wizara
625.610
(iii)
Mikoa
20.519
(iv)
Matumizi Maalum
232.387
(a)
Bima ya Afya
(10.973)
(b)
Marejesho ya Kodi (56.000)
(c)
Kampeni ya Ukimwi (4.443)
(d)
Karo za Shule za Msingi (11.000)
(e)
Malipo ya Wazabuni
(41.900)
(f)
Mengineyo
(108.071)
(v)
Serikali za Mitaa 201.119
(a) Miji
37.039
(b) Wilaya
164.080
F.
Matumizi ya Maendeleo
352.512 bilioni
(a)
Fedha za Ndani 47.240
(b)
Fedha za Nje 302.272
(c) Songosongo 3.000
Jumla ya Matumizi yote 1.764737 trilioni
65.
Mheshimiwa Spika,
sura hii ya bajeti inaonyesha kwamba nchi yetu bado ni tegemezi kwa kiwango
kikubwa. Mapato yetu wenyewe
yanatosha kugharamia asilimia 58 tu ya matumizi yote.
Hii ina maana kwamba karibu asilimia 42 ya bajeti yetu inategemea
wafadhili, na mikopo nafuu kutoka nje. Huu
ni ushahidi tosha kwamba uchumi wetu haujakua kwa kiwango kinachotakiwa.
Tunahitaji kukuza uchumi kwa kiwango cha asilimia 8 na zaidi kwa mwaka
ili kuongeza uwezo wetu wa kujitegemea na kuondoa umaskini.
66.
Mheshimiwa Spika,
bajeti ninayo pendekeza leo ni bajeti ya kuelekeza juhudi za taifa kwenye
kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi wa taifa na hivyo kupambana na umaskini
wa mali; ambapo kwa mujibu wa Dira ya Maendeleo ya taifa, ifikapo mwaka
2010 idadi ya watu maskini
kupindukia nchini
itakuwa imepungua kutoka
asilimia 48
ya sasa
hadi asilimia 24.
Maskini
vijijini watapungua toka asilimia 57 sasa hadi asilimia 29 ifikapo mwaka 2010.
Njia ya uhakika ya kufikia viwango hivyo ni kutekeleza kwa nguvu zote
sera na mikakati iliyowekwa katika kilimo, mifugo, utalii, viwanda vya msingi na
uchimbaji madini. Aidha, wananchi
wenyewe ndio pekee watakaoweza kujikwamua kwa kufanya
kazi hasa
za kilimo
kwa juhudi
na maarifa
makubwa. Hii
ni kutokana na
ukweli kwamba
umaskini uko
katika kaya
moja moja
na wala
si jambo la kinadharia.
Tujikumbushe tena kwamba ili tuendelee tunahitaji watu, ardhi na siasa
bora. Bajeti hii imeweka mazingira
bora ya kila mtu kufanya kazi kwa kujipatia maendeleo katika hali ya utulivu na
amani.
67.
Mheshimiwa
Spika, bajeti hii, kama itakavyo dhihirika katika kamati za kisekta
wakati Mawaziri mbalimbali watakapofafanua sera na mikakati ya Wizara zao, ni
mwanzo wa kupambana kwa dhati na umaskini
wa hali. Mpango wa HIPC
ukitekelezwa inavyokusudiwa utaleta unafuu mkubwa kwenye kuelimisha watoto wetu;
utaongeza chakula na lishe bora; utapunguza makali ya madhara ya gonjwa hatari
la ukimwi, na utaimarisha haki za binadamu na utawala bora wenye kuzingatia
demokrasia na sheria. Bilevile
mpango huo utapunguza vifo vya watoto chini ya miaka 5 na vya mama wajawazito.
Utaongeza kasi ya kuwapatia wananchi maji safi na salama mijini na
vijijini, utaongeza idadi ya barabara za lami na morum zenye kupitika wakati
wote kwa faida ya wakulima, wazalishaji mali wengineo na wafanyabiashara.
68.
Mheshimiwa
Spika, yote hayo yatawezekana kama watekelezaji watafanya kazi kwa
ufanisi na uadilifu mkubwa, jambo ambalo linahitaji kuangaliwa tena na tena,
kwani bado lipo tatizo la uwezo “capacity” katika Wizara na Halmashauri za
Wilaya. Bado upo ubadhirifu na wizi
wa mali za umma; bado wapo wavivu na wazembe katika utumishi wa umma.
Natoa rai kwa viongozi na hasa Waheshimiwa Wabunge, kuwa makini na wakali
katika kusimamia na kuchunguza matumizi ya fedha na mali za umma.
Haipendezi kusikia kazi hii ikifanywa na mabalozi wanapokagua miradi
wakati sisi tupo.
69.
Mheshimiwa
Spika, hali kadhalika
bajeti hii imejitahidi kuwasaidia wanyonge, wakiwemo wafanyakazi, wakulima
wadogo wadogo, wafanyabiashara ndogo ndogo na masikini wasio na uwezo wa
kusomesha watoto wao. Imewapa fursa
wasomi, wahitimu walio tayari kuingia kwenye usomi na biashara za kompyuta na
mtandao wake ambazo zinasisimua vijana wengi kote duniani leo.
Imetoa nafuu kwa viwanda vidogo vidogo na biashara
ndogo ndogo kwa
ujumla hasa
pale wanapoweza kuanza
biashara bila kwanza kutanguliza
kodi kama
ilivyokuwa. Imepunguza
sana ushuru kwa biashara za mipakani ili kuondoa aibu ya kutumia “njia
za panya”, ambazo natumaini sasa zitaota nyasi kwa kukosa watumiaji, wapita
njia!
70.
Mheshimiwa
Spika, bajeti hii imesikiliza sana mawazo na mapendekezo ya wataalamu
mbalimbali, wafanyabiashara wa kati na wakubwa, imewasikiliza wana-utalii hasa
wasafirishaji wa ndege na magari ya kitalii na wawindaji; imewasikiliza sana
wana-viwanda, na wakulima wakubwa na imewasikiliza hata wafadhili na washauri wa
kimataifa. Na imewasikiliza sana
Waheshimiwa Wabunge, hasa wakati wa kikao cha Kamati ya Fedha na Uchumi.
Nawashukuru wote hao walionipa mawazo na ushauri ulioniwezesha kufikia
hatua hii ya bajeti.
71.
Mheshimiwa
Spika, naomba kuchukua fursa hii kukiri kwamba ingawa tumepiga hatua
kubwa sana na ya kujivunia katika
kukusanya kodi na ushuru wa aina aina, hadi kufikia wastani wa shilingi
76 bilioni kwa mwezi, bado kodi
nyingi haikusanywi kutokana na ukwepaji wa makusudi.
Si siri kwa mfano, kwamba wenye maduka wana bei kwa VAT na bei bila VAT
ambayo ni ya chini. Wateja wengi
hawadai risiti wanaponunua mali, kwa kutotambua kuwa wanashiriki katika kukwepa
kodi. Napenda kuwakumbusha wananchi wote kwamba wanaponunua bidhaa
madukani wasisitize kupewa risiti, kwani huo ndio utaratibu wa kisheria
unaotakiwa kuzingatiwa. Hivi sasa
Serikali imefanikiwa kwa kiasi kuziba mwanya uliokuwepo kwenye mafuta ya petroli
ambapo udanganyifu umeanza kutoweka na ambapo adhabu kali sana zitawakabili
watakao kamatwa wakiuza mafuta yasiyo na alama ya siri.
Serikali inayafanyia kazi maeneo mengine ya ukwepaji kodi kwa lengo la
kuziba mianya iliyopo. Kama nilivyoeleza, kuifanya Serikali yenyewe kulipia kodi
manunuzi yake ni hatua ya kupambana na wakwepa kodi waliokuwa wakitumia vibaya
mianya ya manunuzi ya mahitaji ya Serikali.
72.
Mheshimiwa Spika,
tatizo la pili ni katika sera za kodi; kuwepo kwa mamlaka tofauti za
utozaji na ukusanyaji kodi, yaani Serikali za Mitaa, Waziri wa Fedha na Bunge.
Malalamiko mengi
kuhusu wingi wa kodi na leseni yanatokana na mgongano huo ambapo baada ya
Waziri wa Fedha na Bunge kuidhinisha viwango vya kodi, hutokea eneo hilo
likawekewa tena viwango vya ziada kutokana na maamuzi ya Halmashauri za Wilaya. Nakusudia kusawazisha hali hii mwaka ujao wa fedha na
nitafurahi kupata maoni ya Waheshimiwa Wabunge.
73.
Mheshimiwa
Spika, eneo lingine lenye utata katika kodi ni la misamaha.
Baada ya kuyumba yumba miaka ya karibuni, Serikali sasa imeamua kurejesha
tena misamaha ya kodi kwa mashirika ya dini na taasisi za kujitolea yanayotoa
huduma bila faida (not for profit; NGO).
Uamuzi huu utatangazwa kisheria kwa njia ya Tangazo la Serikali
(Government Notice) na hivyo kuondoa kero iliyojitokeza kuhusiana na misamaha
kwa makundi hayo. Lakini
utakuwepo udhibiti zaidi, kwa nia ya kuondoa udanganyifu.
74
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.