HOTUBA YA WAZIRI WA UJENZI MHESHIMIWA JOHN P. MAGUFULI (MB.) WAKATI
AKIWASILISHA BUNGENI MPANGO WA MAENDELEO NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA KWA
MWAKA 2002/03
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge
lako Tukufu sasa likubali kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Ujenzi
kwa mwaka wa fedha 2002/03.
2.
Mheshimiwa Spika, kabla sijaendelea napenda kwanza
kabisa kuipongeza Kamati nzima ya miundombinu ambayo kwa umoja wao wameweza
kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa. Napenda kulihakikishia Bunge lako
Tukufu kuwa Wizara yangu itaendelea kuzingatia na kutekeleza maelekezo
yaliyotolewa na Kamati hiyo, na yatakayotolewa na Bunge lako Tukufu katika
kipindi hiki cha mwaka 2002/03 kwa kadri ya uwezo tutakaopewa tayari kutekeleza
majukumu yaliyopangwa.
3.
Mheshimiwa Spika, Napenda pia kumpongeza Waziri Mkuu
Mheshimiwa Frederick Tluway Sumaye, Mbunge wa Hanang, kwa hotuba yake katika
Bunge hili la Bajeti ambayo kwa kiasi kikubwa imefafanua masuala ya barabara
na imetupa upeo wa majukumu ya Serikali
ya Chama cha Mapinduzi katika kipindi kijacho. Hali kadhalika nawapongeza
Waziri wa Fedha Mheshimiwa Basil P. Mramba, na Mheshimiwa Abdallah M. Kigoda,
Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais (Mipango na Ubinafsishaji) kwa hotuba zao ambazo
sio tu zimechambua na kuelezea kwa kina maendeleo, matatizo na matarajio ya
uchumi wetu, bali pia zimeweka wazi sera, malengo na mikakati ya utekelezaji wa
mipango ya Serikali.
DIRA YA WIZARA
4.
Mheshimiwa Spika, Dira ya Wizara ya Ujenzi ni
kuendeleza Sekta ya Ujenzi ili kuchochea na kuleta ufanisi katika maendeleo ya
kijamii na kiuchumi na hivyo hatimaye kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa
nchi.
Maeneo yanayosimamiwa
na kuendelezwa na Wizara ya Ujenzi ni yale ya Ujenzi, Ukarabati, na Matengenezo
ya Barabara, Madaraja na Majengo ya Serikali.
Maeneo mengine ni ya kutoa Huduma za Ufundi na Umeme na Huduma za Ugavi.
Kwa kuzingatia Dira ya
Taifa ya Maendeleo hadi mwaka 2025 (vision 2025), malengo na matazamio ya
Wizara ifikapo mwaka 2025 ni kama ifuatavyo:
·
Kuwa
na mtandao mzuri na salama wa barabara ambapo nchi zote jirani zitakuwa
zimeunganishwa kwa barabara za lami, makao makuu ya Mikoa yote yatakuwa
yameunganishwa kwa barabara za lami wakati makao makuu ya Wilaya yatakuwa
yameunganishwa na barabara za kuaminika zinazopitika wakati wote.
·
Kuwepo
kwa Makandarasi na Wahandisi Washauri wengi wazalendo watakaokuwa na sifa na
uzoefu wa kutosha wa kuwawezesha kufanya kazi kwa viwango vinavyotakiwa na
kukamilisha kazi katika muda uliopangwa kwa mujibu wa Sheria zetu.
·
Kuwa
na Sekta ya ujenzi inayochangia katika kupunguza utegemezi, kuondoa umaskini na
kutoa ajira kwa wananchi kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya raslimali za
ndani ikiwa ni pamoja na matumizi ya nguvu kazi iliyopo hasa katika matengenezo
ya barabara.
·
Kuandaa
mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji binafsi kuwekeza katika miradi ya
barabara.
·
Kuwa
na maeneo ya miliki ya barabara (Roads Reserve) yanayotambulika na kuheshimika.
·
Kuwa
na ushiriki mkubwa wa wanawake katika kazi za barabara katika ngazi zote za
utungaji sera, upangaji mipango, utekelezaji na ufuatiliaji wa miradi ya
barabara.
·
Kuwa
na Sekta ya Barabara inayotekeleza shughuli zake bila kuathiri mazingira.
MAJUKUMU YA WIZARA
5.
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumekuwa tunalieleza Bunge lako Tukufu, majukumu ya Wizara
ya Ujenzi ni kama ifuatavyo:
·
Kuandaa sera, mipango
na mikakati inayolenga katika ukuzaji, uimarishaji na uendelezaji wa sekta ya
ujenzi nchini katika muda mfupi, wa kati na mrefu.
·
Kusimamia ujenzi,
ukarabati na matengenezo ya Barabara, Madaraja na Majengo ya Serikali.
·
Kusimamia uendeshaji
wa shughuli za Bodi ya Mfuko wa Barabara, Wakala wa Barabara, Wakala wa Nyumba
pamoja na Wakala zingine zinazotarajiwa kuundwa chini ya Wizara zinazohusu
Idara ya Ufundi na Umeme na Idara ya Ugavi na Huduma.
·
Kuratibu shughuli za
Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi ambazo ni Baraza la Taifa la Ujenzi na
Bodi za Usajili wa Makandarasi, Wahandisi, Wasanifu Majengo na Wakadiriaji
Majenzi na Usimamizi wa Vifaa.
·
Kutafuta fedha za nje
na za ndani za kugharamia miradi iliyo chini ya Wizara.
·
Kuandaa na kusimamia
viwango vya ubora wa kazi za ujenzi, ukarabati pamoja na matengenezo ya
barabara.
·
Kuandaa mazingira
yatakayovutia wawekezaji binafsi katika ujenzi wa barabara na madaraja.
·
Kusimamia na kuratibu
shughuli za upembuzi yakinifu wa barabara kuu na za vijijini.
·
Kusimamia shughuli za
Usalama wa Barabara (Road Safety).
·
Kuboresha ufanisi wa
Wahandisi Washauri na Makandarasi wazalendo katika ujenzi na matengenezo ya
barabara nchini kwa kuwapatia mafunzo.
·
Kusimamia na
kuendesha shughuli zote za ununuzi, ukarabati na matengenezo ya magari, vivuko,
mitambo, viyoyozi na vifaa vya elektroniki vya Serikali.
·
Kuhakikisha mali za
Serikali kama Magari, Pikipiki na Mitambo inasajiliwa kwa namba za Serikali kwa
mujibu wa Sheria ya barabarani ya mwaka 1973.
·
Kutekeleza utaratibu
wa kujenga na kuwauzia Watumishi wa Serikali nyumba za kuishi kupitia Wakala wa
Majengo.
·
Kusimamia ukodishaji
wa magari, mitambo ya kokoto na ukodishaji wa mitambo ya Serikali (Road
Workshops).
·
Kusimamia maendeleo
ya Watumishi wa Wizara.
MIKAKATI YA UTEKELEZAJI
6.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza majukumu haya, Wizara imezingatia maelekezo
yaliyotolewa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala ya mwaka 2000-2005, Dira
ya Taifa ya Maendeleo hadi mwaka 2025, mikakati ya kupunguza umaskini na Sera
nyingine za Ujumla za Taifa za kukuza uchumi na kuboresha maendeleo ya Jamii.
Aidha Wizara imejiwekea Mikakati ifuatayo katika kutekeleza majukumu haya:-
·
Kufanya mapitio ya
mfumo wa utendaji ili shughuli za kiutendaji zifanywe na taasisi
zinazojitegemea (Wakala) na Wizara ibaki na majukumu yake ya msingi ya uandaaji
wa sera na mikakati inayolenga katika ukuzaji na uimarishaji wa sekta ya
ujenzi.
·
Kutoa kipaumbele
katika ukarabati na ujenzi wa barabara kwa kufuata Kanda Kuu za usafirishaji,
barabara za Mikoa na za Wilaya ambazo ni muhimu kwa huduma za usafirishaji wa
mazao ya kilimo na huduma nyingine muhimu za kitaifa.
·
Kuweka mazingira
mazuri ya upatikanaji wa zana za ujenzi kwa kuimarisha karakana za Serikali na
kuhamasisha watu binafsi kuanzisha kampuni za kukodisha mitambo.
·
Kuendeleza mafunzo
kwa Wahandisi Washauri na Makandarasi wazalendo ili wasimamie na kutekeleza
vizuri mikataba ya ujenzi na matengenezo ya barabara.
·
Kutafuta vyanzo
vingine vya fedha za Mfuko wa Barabara ili ukidhi mahitaji ya ujenzi na
matengenezo ya barabara.
·
Kuendeleza mazungumzo
na wawekezaji binafsi wanaoonyesha nia ya kuwekeza katika ujenzi wa barabara na
madaraja.
·
Kuhakikisha usanifu
wa barabara mpya unazingatia hifadhi ya mazingira, usalama wa watumiaji wote na
viwango vya mahitaji halisi ya matumizi ya magari.
·
Kuandaa utaratibu
mzuri wa kusimamia Sheria ya Udhibiti wa Uzito wa magari na matumizi bora ya
barabara kwa kuwashirikisha wadau wote.
·
Kushirikiana na
Wizara ya Mambo ya Ndani na Mawasiliano na Uchukuzi katika kuimarisha utaratibu
mzima wa utoaji mafunzo na leseni kwa madereva na kutoa elimu na hamasa ya
Usalama Barabarani.
·
Kuwasaidia wananchi,
mamlaka mbalimbali na Umma kwa ujumla kutambua mipaka ya maeneo ya barabara
(Road Reserve) na kutayarisha ramani za barabara zitakazoonyesha mipaka ya
miliki ya barabara zote za Umma.
·
Kuendeleza teknolojia
ya nguvu kazi ili kuwapa uwezo wananchi wengi zaidi kushiriki katika kazi za
matengenezo ya barabara katika maeneo
yao bila kusubiri msaada kutoka Serikalini.
UTEKELEZAJI
WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA 2001/02 NA MALENGO YA MWAKA 2002/03
7.
Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa maelezo kuhusu Dira, Majukumu na Mikakati ya
utekelezaji ya Wizara, naomba sasa kutoa maelezo kuhusu utekelezaji wa malengo
ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2001/02 na malengo ya mwaka 2002/03.
Mifumo
ya Taasisi zilizo chini ya Wizara
8.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyolieleza Bunge lako Tukufu katika hotuba yangu ya Bajeti
ya mwaka 2001/02 kuhusu uundwaji wa Wakala, nafurahi kutamka kuwa pamoja na
Wakala wa Barabara (Tanzania Roads Agency - TANROADS) ambao umeanzishwa tangu
mwaka 2000, Wakala wa Nyumba za
Serikali (Tanzania Building Agency -TBA) pia umeundwa tangu mwezi Mei mwaka
2002, kwa kutumia Sheria Na. 30 ya mwaka 1997.
Majukumu yake muhimu ni pamoja na:-
·
Kutunza nyumba za
Serikali zinazomilikiwa na Wakala.
·
Kuwapatia nyumba bora
za kuishi Watumishi wa Serikali wakiwa kazini na baada ya kustaafu.
·
Kutekeleza utaratibu
wa kujenga na kuwauzia Watumishi wa Serikali nyumba kwa kutumia fedha zitakazolipwa
na waliokopeshwa nyumba, na pia kutokana na mapato mengine.
·
Kutoa huduma za
ushauri (Consultancy Services) kuhusiana na majengo.
·
Kuhakikisha kuwa
majengo ya Serikali yanajengwa na kutunzwa kwa kuzingatia viwango(standards)
vilivyowekwa.
Aidha, hatua mbalimbali zinachukuliwa ili Idara za
Ufundi na Umeme na Ugavi na Huduma nazo ziwe Wakala.
Mpango wa Taifa wa kuendeleza
Mtandao wa Barabara
9.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imekamilisha kuandaa rasimu ya awali ya Mpango wa Miaka
Kumi wa kuendeleza Mtandao wa Barabara hapa nchini kwa kipindi cha
2001-2010. Mpango huu utatumika kama
mwongozo wa kuteua barabara kuu na za vijijini za kufanyiwa ukarabati katika
kipindi hiki. Wizara kwa sasa inafanya
mapitio ya rasimu hiyo ili kuandaa mapendekezo ya mwisho ya mpango. Aidha, Wizara imepanga kufanya mkutano na
wahisani wa sekta ya barabara mwaka 2002/03 ili kuwasilisha Mpango huo kwao kwa
madhumuni ya kuwaomba kugharamia baadhi ya miradi inayopendekezwa.
Ukanda
wa Maendeleo wa Mtwara (Mtwara Development Corridor - MtDC)
10.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu ikiwa ndiyo mratibu wa shughuli za Ukanda wa Maendeleo
wa Mtwara inaendelea kushirikiana na Wizara nyingine nchini ili kusimamia na
kutekeleza malengo yaliyowekwa kwa kushirikiana na nchi wanachama wa Ukanda wa
Maendeleo wa Mtwara (Mtwara Development Corridor – MtDC).
Baada ya mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia Makaa
ya Mawe ya Mchuchuma-Katewaka kupata wawekezaji na kuweka saini Mkataba wa
Makubaliano ya Awali (Agreement of Intent) kati ya Serikali na Wawekezaji mwezi
Julai, 2001, hatua iliyofikiwa mpaka sasa ni kwamba majadiliano ya pamoja kwa
pande zote zinazohusika yanaendelea vizuri.
Aidha, wadau mbalimbali kama vile Wizara ya Nishati na Madini, Wizara ya
Fedha, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, TANESCO na Benki ya Dunia
wanashirikishwa katika majadiliano hayo.
Hadi sasa Mkakati wa utekelezaji (Project Development Programme)
umekwisha tayarishwa na Wizara ya Nishati na Madini, Shirika la Maendeleo la
Taifa (NDC) na kwa ushirikiano na wawekezaji na majadiliano ya jinsi ya kuanza
utekelezaji yanaendelea.
Mradi mwingine unaohusika ni ujenzi wa barabara ya
Mtwara-Masasi-Songea-Mbamba Bay. Mradi
huu umepata fedha za msaada kutoka Mfuko wa Maendeleo wa Kuwait kwa kiasi cha
dola za Kimarekani milioni moja (US.$1.0million). Fedha hizo zitatumika kwa
ajili ya kufanyia upembuzi yakinifu (feasibility study). Kazi hii inatarajiwa kuanza mwaka wa fedha
2002/03 mara baada ya kumpata Mtaalam Mshauri.
11. Mheshimiwa
Spika, mnamo mwezi Machi 2002,
Serikali ya Tanzania kupitia Wizara yangu na Serikali ya Msumbiji kupitia
Wizara ya Ujenzi na Nyumba ziliwekeana saini Mkataba wa Maelewano (Memorandum
of Understanding) juu ya ujenzi wa Daraja la Umoja (Unity Bridge) katika mto
Ruvuma. Daraja hilo litakuwa ni kiungo
muhimu kwani litaweza kuziunganisha nchi hizi mbili kwa njia ya barabara. Katika mkataba huo nchi zote mbili
zinawajibika kutafuta fedha na wawekezaji kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo.
12. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2002/03 lengo kuu
kuhusu maendeleo ya Ukanda wa Maendeleo wa Mtwara ni kukamilisha Rasimu ya
Mkataba wa Maelewano (Memorandum of Understanding) kati ya nchi wanachama. Tunaamini kwamba kusainiwa kwa Mkataba wa
Maelewano kwa nchi wanachama kutakuwa ni kiunganisho chenye nguvu za kisheria
kwa nchi wanachama wa ukanda huu na kuwa kichocheo kikubwa cha kupata
wawekezaji na wahisani katika miradi ya Ukanda huu. Pili, hali hii itawezesha kuandaliwa kwa miradi mama (Regional
Anchor Projects) ambapo nchi zote zitaweza kuiwasilisha kwa pamoja kwenye
makongamano mbalimbali ya wawekezaji.
Ushirikiano
wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)
13. Mheshimiwa Spika, kuhusu Jumuiya
ya Afrika Mashariki ningependa niongelee zaidi miradi ya barabara iliyomo
kwenye ukanda wa Jumuiya hiyo (East African Road Network Projects). Miradi hii iko kwenye kanda tano (five
corridors) ambazo zimeunganisha nchi za Afrika Mashariki. Miradi hiyo na hatua za utekelezaji wake
hadi sasa ni kama inavyoonyeshwa katika Kiambatanisho Na. 1.
14. Mheshimiwa
Spika, ili
kutafuta fedha za kuendeleza barabara kwenye kanda hizo Sekretariati ya Jumuiya
ya Afrika Mashariki inaandaa kongamano/mkutano wa wafadhili (EAC / Development
Partners Road’s Consultative Meeting) Mwezi Oktoba mwaka 2002. Madhumuni ya mkutano huo ni kuwafahamisha
wahisani wa miradi ya barabara kuhusu maendeleo na utekelezaji wa miradi hiyo
pamoja na kuwahamasisha katika kuendeleza sekta hii ya barabara. Vile vile, zimeanzishwa juhudi za pamoja kwa
nchi zote za Afrika ili kuweka mkakati wa pamoja wa kuondoa umaskini (New Partnership for Africa’s
Developemnt-NEPAD). Kwa nchi wanachama
wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, maandalizi haya yamekwishaanza na Wizara yangu
imekwishaainisha miradi ya barabara itakayoingizwa katika mkakati huu kama ilivyofafanuliwa
kwenye Kiambatanisho Na. 2(a).
BODI YA MFUKO WA
BARABARA
15. Mheshimiwa
Spika, katika hotuba yangu ya
bajeti ya mwaka wa fedha 2001/2002 nililiarifu Bunge lako Tukufu juu ya hatua
mbalimbali zilizofikiwa na Bodi ya Mfuko wa Barabara katika utekelezaji wa
majukumu yake pamoja na malengo ya siku zijazo. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2001/2002 Bodi imefanya
yafuatayo:-
·
Bodi imetathimini
upya viwango vya tozo mbalimbali zinazoingia katika mfuko na kutoa mapendekezo
kwa ajili ya kuhakikisha fedha za kutosha zinapatikana za kutunza barabara
zetu. Lengo ni Mfuko wa Barabara uweze
kutosheleza mahitaji ya matengenezo ya barabara Kuu na za Mikoa pamoja na
barabara muhimu za Wilaya na Mijini ifikapo mwaka 2008/2009. Mapendekezo hayo yanaendelea kufanyiwa kazi
na Wizara yangu kwa lengo la kuyawasilisha Serikalini ili yatolewe maamuzi ya
mwisho.
·
Bodi imepitia upya na
kuboresha mikataba ya kazi (Performance Agreements) kati ya Bodi na
watekelezaji kwa kuweka vigezo vya utekelezaji (performance indicators)
vinavyopimika.
·
Bodi imefuatilia
matumizi ya fedha za mfuko kwa kukagua kazi zinazofanywa na taasisi zinazotumia
fedha hizi kwa kutumia wakaguzi wa fedha na ubora wa kazi (Financial and
Technical Audits).
16. Mheshimiwa
Spika, kati ya mwezi Agosti na
Desemba, 2001, Bodi ya Mfuko wa Barabara iliendesha ukaguzi wa hesabu kwa
taasisi zilizopokea fedha kwa mwaka wa fedha 2000/01. Ripoti ya Ukaguzi inaonyesha Bodi ya Mfuko ilipata ripoti safi. Ripoti inaonyesha Wizara ya Ujenzi, TANROADS, Halmashauri za Miji na Wilaya
zilifanyiwa ukaguzi. Hatua
zimekwishaanza kuchukuliwa kwa watendaji waliobainika kutumia vibaya fedha
hizi. Halikadhalika hatua kali zitachukuliwa dhidi ya makandarasi waliobainika
kufanya kazi mbovu kwa mujibu wa Sheria Na.17 ya mwaka 1997. Ili kurekebisha
kasoro zilizojitokeza katika mwaka 2000/01, Bodi imeamua kuwa kuanzia mwaka wa
fedha 2001/02 ukaguzi wa hesabu ufanyike mara mbili kwa mwaka ili kudhibiti
matumizi mabaya ya fedha mapema iwezekanavyo. Taasisi husika zitaendelea kutoa ripoti
za kazi mara nne kwa mwaka.
17.
Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, katika
mwaka wa fedha 2001/02, hadi kufikia tarehe 25/6/2002, Bodi ya Mfuko wa
Barabara ilipokea na kugawa jumla ya Shilingi 48,519.18 milioni ambazo ni asilimia
96 ya lengo la mwaka ambalo ni Shilingi 50,790 milioni. Kati ya fedha hizo, Shilingi 3,352.9 milioni
zimetolewa kwa Wizara ya Ujenzi, Shilingi 30,176.243 milioni kwa TANROADS,
Shilingi 620.384 milioni kwa ajili ya matumizi ya Bodi yenyewe na Shilingi 14,369.639
milioni kwa Serikali za Mitaa.
18.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza majukumu yake, Bodi ya Mfuko wa Barabara imepanga
kutekeleza malengo yafuatayo katika mwaka 2002/03:-
·
Kufuatilia matumizi
ya fedha zilizotolewa kwa kufanya ukaguzi wa hesabu na ubora wa kazi kwa
kutumia Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali, Mhandisi Mshauri na Bodi
yenyewe.
·
Kutayarisha kitabu
cha mwongozo wa Mfuko wa Barabara ambacho kitajumuisha utaratibu wa usimamzi wa
fedha za mfuko na mikataba ya kazi, kuelimisha juu ya mabadiliko yanayoendelea katika sekta ya barabara,
majukumu ya Bodi ikiwemo utaratibu wa kugawa na kufuatilia fedha za mfuko. Sheria iliyoanzisha Bodi nayo itaambatanishwa. Kijitabu hicho kitasambazwa kwa Wabunge
wote, Makatibu Tawala wa Mikoa yote, Wakurugenzi Watendaji na Umma kwa ujumla.
·
Kuelimisha wadau juu
ya fomula mpya ya kugawa fedha kwenye Halmashauri na kusisitiza umuhimu wa
ushirikishwaji wa jamii katika kutunza barabara kwa njia ya kuchangia gharama.
·
Kushirikiana na wadau
ili waunge mkono juhudi za kupanua wigo wa Mfuko wa Barabara na juhudi za
kupambana na tatizo la magari kuzidisha uzito kwenye barabara.
·
Kushirikiana na Bodi
nyingine za nchi mbalimbali ili kujifunza kutokana na uzoefu wao.
19. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha 2002/03
Serikali imeweka malengo ya kukusanya jumla ya Shilingi 64,341 milioni kwa
ajili ya Mfuko wa Barabara ambazo zitagawiwa kwa TANROADS Shilingi 40,154.866
milioni, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa
na Serikali za Mitaa Shilingi 19,070.02 milioni, Wizara ya Ujenzi Shilingi
4,449.67 milioni na Bodi ya Mfuko wa Barabara Shilingi 674.27 milioni.
WAKALA WA BARABARA (TANROADS)
20. Mheshimiwa
Spika, miaka miwili imetimia tangu
Wakala wa Barabara, (TANROADS) uliopoanzishwa hapo tarehe 1 Julai, 2000. Katika miaka hii miwili, TANROADS imekuwa
ikiweka na kuendeleza mifumo ya kisasa ya menejimenti na mawasiliano katika
ngazi zote za Makao Makuu ya Mikoa ili kuweza kukabili majukumu yake katika
karne hii ya Sayansi na Teknolojia.
Matokeo ya juhudi hizo yanadhihirishwa na dalili za kuboreka kwa
utendaji wa kazi za barabara na nidhamu katika matumizi ya fedha.
Aidha, Wakala umeongeza kasi ya kufanya kazi kwa
kutumia makandarasi na kupunguza mfumo wa kufanya kazi kwa kutumia vikosi vyake
(Force Account). Uamuzi wa kutumia
makandarasi umewezesha kuwepo kwa ongezeko la kandarasi za matengenezo ya
barabara zinazotekelezwa kutoka wastani wa kandarasi 50 -100 kwa kila robo
katika mwaka 1999/2000 hadi kufikia kandarasi 500-700 kwa robo katika mwaka
2001/2002. Aidha, katika kipindi cha
2002/03 Wizara itapitia muundo wa TANROADS ili kuwa na Wakala wenye Watumishi
wachache lakini wenye ufanisi zaidi na hii itasaidia kuelekeza fedha nyingi za
Mfuko wa Barabara kwenye matengenezo ya barabara badala ya fedha nyingi kuishia
kwenye matumizi ya uendeshaji/utawala.
21. Mheshimiwa
Spika, napenda kusisitizia tena
mwito wangu kwa Waheshimiwa Wabunge na Viongozi wa Mikoa na Wilaya kuendelea
kufuatilia kwa karibu utendaji wa TANROADS katika maeneo yao na kuzipa taasisi
hizi mbili (TANROADS na Bodi ya Mfuko wa Barabara) ushirikiano wa karibu ili
ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.
22.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2001/02
Wizara ilipanga kukusanya jumla ya Shilingi 4,789.636 milioni kupitia idara
zake zinazokusanya maduhuli ambazo ni Bohari Kuu, Ufundi na Umeme, Majengo na
Utawala. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Juni, 2002, jumla ya Shilingi 3,528.56
milioni zilikusanywa sawa na asilimia 73.7 ya malengo yaliyowekwa.
Katika mwaka 2002/03
Wizara ya Ujenzi inatarajia
kukusanya jumla ya shilingi 2,089,985,000 kutokana na vianzio vyake mbalimbali.
Wakala wa Nyumba, Idara ya Ufundi
na Umeme pamoja na Bohari Kuu ziko chini ya “Retention Scheme” hivyo huruhusiwa
kutumia kiasi fulani cha makusanyo yao kugharamia matumizi ya kawaida na kiasi
kingine kinachobakia hupelekwa HAZINA.
23. Mheshimiwa
Spika, Wizara yangu inaendelea
kutekeleza miradi ya ukarabati na ujenzi wa barabara kuu katika mfumo wa kanda
kuu za usafirishaji kama zilivyofafanuliwa kwenye Kiambatanisho
Na.2(b). Katika mwaka wa fedha
2001/2002 Wizara ilitengewa jumla ya Shilingi 91,799 milioni kwa miradi ya
maendeleo ambapo Shilingi 16,554 milioni zilikuwa fedha za hapa na Shilingi
75,245 milioni zilikuwa fedha za kigeni zilizotokana na michango ya wahisani
mbalimbali. Aidha, Wizara ilitengewa
jumla ya Shilingi 3,488 milioni toka Mfuko wa Barabara kwa ajili ya miradi ya
maendeleo. Kwa hiyo jumla ya fedha zote
za hapa zilizotengwa kwa miradi ya maendeleo ni Shilingi 20,042 milioni. Hadi
kufikia mwishoni mwa mwezi Juni, 2002 jumla ya Shilingi 19,906.92 milioni fedha
za hapa zilikwishatolewa. Viambatanisho Na. 3 na 4
vinaonyesha utekelezaji halisi wa miradi ya maendeleo kwa mwaka 2001/02.
Katika mwaka 2001/02 Wizara yangu
ilitengewa jumla ya Shillingi milioni 58,908.162 kwa ajili ya matengenezo ya
barabara. Kati ya fedha hizo, Shilingi
milioni 31,390.28 ni za hapa toka Mfuko wa Barabara na Shilingi 27,517.882 ni
za nje toka kwa wahisani mbalimbali.
Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Juni 2002, jumla ya kandarasi 1,365 za
kazi za matengenezo zilitolewa kama Kiambatanisho Na. 2(c)
kinavyoonyesha.
24. Mheshimiwa
Spika, katika kutekeleza mipango
ya mwaka 2001/02, utekelezaji wa kazi za barabara uliathirika kutokana na
sababu zifuatazo:
·
Ufanisi duni wa
baadhi ya Makandarasi katika kutekeleza kazi za barabara.
·
Upungufu wa mitambo
ya kuwawezesha Makandarasi wazalendo kumudu utekelezaji wa kazi za barabara.
·
Baadhi ya Wahisani
kuchelewa kutoa fedha kufuatana na ratiba iliyowekwa hivyo kuchelewesha miradi
kuanza ama kuchelewesha malipo kwa makandarasi kwa muda uliokubaliwa katika
mikataba.
·
Upungufu wa fedha
kulinganisha na mahitaji halisi ya miradi ya maendeleo na kazi za matengenezo
ya barabara.
·
Utaratibu mrefu wa
kutoa zabuni (hasa kwa miradi ya Wahisani) umechelewesha kuanza kwa utekelezaji
wa baadhi ya miradi.
25.
Mheshimiwa Spika, ili kuongeza kasi ya ujenzi wa barabara nchini, Serikali imeanzisha
Mpango Maalum wa kutekeleza miradi ya barabara kwa kutumia fedha za ndani kama
Waraka wa Baraza la Mawaziri Na.5 wa 2001 unavyoeleza. Katika Mpango huu Serikali itakuwa inatenga
Shilingi 1,840 milioni kila mwezi kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Wizara yangu imeanza kutekeleza miradi
ifuatayo katika mwaka wa fedha wa 2001/02 mpaka 2005/06 kupitia mpango huu
maalum:-
·
Barabara ya Somanga¾Masaninga na Daraja la Matandu (km.33)
·
Barabara ya
Nangurukuru¾Mbwemkulu (km. 95)
·
Barabara ya Mbwemkulu¾ Mingoyo (km 95)
·
Barabara ya Dodoma¾Manyoni (km 124)
·
Barabara ya Manyoni¾Singida (km122)
26.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2001/2002 Shilingi 12,000 milioni zilitengwa kwa
ajili ya kuanza kutekeleza mradi huu. Kazi ambazo zilipangwa kufanyika ni
kuteua Mkandarasi wa ujenzi wa Barabara ya Somanga¾Masaninga kwa kiwango cha lami na daraja la
Matandu, kufanya usanifu, kuitisha zabuni na kuanza ujenzi sehemu ya
Nangurukuru¾Lindi¾Mingoyo na Dodoma ¾ Manyoni na Manyoni¾Singida. Mkandarasi wa sehemu ya Somanga-Masaninga
pamoja na daraja la Matandu ameteuliwa.
Mkataba kati ya Wizara ya Ujenzi na Kampuni ya Ujenzi inayoitwa China
Geo Engineering kwa ujenzi wa barabara ya Somanga¾Masaninga
ulitiwa saini tarehe 22/2/2002. Kazi
hiyo itagharamu Shilingi 12,286,602,742.00. Hivi sasa Mkandarasi anaendelea na
kazi ya kupeleka vifaa katika eneo la mradi.
Maandalizi ya kuanza ujenzi yanatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe
9/7/2002 na ujenzi rasmi kuanza. Tarehe 11/06/2002 Mkataba wa usimamizi wa
ujenzi wa barabara hiyo ulisainiwa kati ya Wizara na Kampuni ya Parkman Limited
ya Uingereza inayoshirikiana na Kampuni ya M-Konsult ya Tanzania kwa gharama ya
Shilingi 1,041,952,476.00 Mhandisi Mshauri huyu anatazamiwa kuanza kazi ya
usimamizi mara moja.
Tarehe 3/6/2002 Wizara ya Ujenzi iliingia Mkataba
na Kampuni ya BKS Group ya Afrika ya Kusini inayoshirikiana na Kampuni ya
Co-Architecture ya Tanzania kama Mhandisi Mshauri kwa ajili ya kuandaa nyaraka
za zabuni hadi kumpata Mkandarasi wa kujenga barabara ya Nangurukuru¾Mingoyo baadaye kusimamia ujenzi wa sehemu ya
barabara hiyo ya Nangurukuru hadi Mbwemkulu (95 km). Kazi hiyo itagharimu Shilingi 1,038,144,000.00
Tarehe 12/06/2002 Wizara ya Ujenzi imeingia pia
Mkataba na Kampuni iitwayo Roughton International ya Uingereza ambayo inashirikiana
na Kampuni iitwayo Data Consult Ltd ya Tanzania kuwa Mhandisi Mshauri kwa ajili
ya kuandaa nyaraka za zabuni hadi kumpata Mkandarasi wa kujenga barabara ya
Dodoma¾Singida na baadaye kusimamia ujenzi wa sehemu ya
Dodoma hadi Manyoni. Mkataba huu utagharimu
Paundi za Kiingereza 500,978.00 na Shilingi 426,412,500.00 za Tanzania.
27.
Mheshimiwa Spika, malengo ya mwaka wa fedha 2002/03 ni kuendelea na ujenzi wa sehemu
ya Somanga-Masaninga na Daraja la Matandu na kukamilisha nyaraka za Zabuni na
kuteua Makandarasi kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara za
Nangurukuru¾Mbwemkulu, Mbwemkulu¾Mingoyo,
Dodoma¾Manyoni na Manyoni-Singida. Jumla ya Shilingi 22,000 milioni za ndani
zimetengwa katika mwaka wa fedha wa 2002/03 kwa ajili ya kuendelea na
utekelezaji wa mpango huu kama Kiambatanisho Na.5 (b)
kinavyoonyesha.
28. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2002/03 jumla ya
Shilingi 160,169.32 milioni zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Kati
ya fedha hizo Shilingi 38,968.67 milioni ni fedha za hapa na Shilingi 121,200.9
milioni ni fedha za kigeni.
Aidha, katika fedha za hapa, jumla
ya Shilingi 4,449.67 milioni zinatoka Mfuko wa Barabara na Shilingi 34,519
milioni zinatoka kwenye bajeti ya maendeleo. Muhtasari wa Mpango huu
umeonyeshwa katika Viambatanisho Na. 5 na Na.6.
Mpango wa matengenezo ya Barabara
mwaka 2002/03
29. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002/03 jumla ya Shilingi milioni 51,445.913 zimetengwa
kwa ajili ya matengenezo ya barabara Kuu na za Mikoa. Kati ya fedha hizo,
Shilingi milioni 40,154.866 ni fedha za hapa toka Mfuko wa Barabara na Shilingi
milioni 11,291.047 ni fedha za nje.
Muhtasari wa kazi zote za matengenezo zilizopangwa kwa mwaka 2002/03 ni
kama zilivyoonyeshwa katika
Kiambatanisho Na.7.
30.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2002/03 Wizara ya Ujenzi imetengewa jumla ya
Shilingi milioni 9,075.9569 fedha za hapa kwa ajili ya Matumizi ya
Kawaida. Fedha hizi zinajumuisha,
mishahara ya Wizara, mishahara ya TANROADS, mishahara ya Taasisi nyingine na
fedha za retention.
Muhtasari wa makisio ya Matumizi ya Kawaida pamoja
na mapato ya fedha za Mfuko wa Barabara kwa mwaka 2002/03 umeonyeshwa katika Kiambatanisho Na.8.
31.
Mheshimiwa Spika, katika harakati za kupambana na hali ngumu ya upatikanaji wa nyenzo
na vitendea kazi, Wizara yangu inatekeleza mradi huu wenye lengo la kuendeleza
teknolojia inayoruhusu na kutilia mkazo matumizi ya nguvu kazi na nyenzo
zinazopatikana kwa urahisi hususan hapa hapa nchini (Labour Based Technology)
katika ukarabati, matengenezo na ujenzi wa barabara. Katika mwaka wa fedha wa
2001/02, Wizara yangu iliendelea kufuatilia, kutathmini na kuratibu matumizi ya
teknolojia hii katika kazi za barabara kwenye miradi mbalimbali mikoani na
wilayani. Aidha, Wizara imeendelea kusambaza vitabu vya miongozo na maelekezo
ya matumizi ya teknolojia hii kwa watumiaji na watendaji mbalimbali ikiwa ni
pamoja na Wakandarasi na Wahandisi Washauri.
32.
Mheshimiwa Spika, Wizara ina Chuo kinachotoa mafunzo ya matumizi sahihi ya teknolojia
hii (Appropriate Technology Training Institute – ATTI) ambacho kipo Kiwira
mkoani Mbeya. Wizara inaendelea na juhudi zake za kuhakikisha Chuo hiki
kinaimarishwa ili kiendelee kutoa mafunzo na huduma nyinginezo kwa walengwa
wote hususan ofisi za Halmashauri za Wilaya na Miji, Wakala wa Barabara
(TANROADS), Makandarasi na Wahandisi Washauri kwa kuchangia gharama kiasi
kidogo.
33.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa
2002/03, Wizara yangu imepanga kutekeleza yafuatayo:-
·
Kuendelea
kutoa miongozo na maelekezo ya utumiaji wa teknolojia ya nguvu kazi kwa
walengwa na kutathmini mwenendo mzima wa utekelezaji wa kazi za barabara kwa
kutumia teknolojia hii.
·
Kuchapisha
na kusambaza kitabu cha mwongozo (Labour Based Technical Manual Volume IV).
·
Kukiendeleza
na kukipatia nyenzo na vitendea kazi chuo cha ATTI kwa kushirikiana na
wataalamu kutoka ILO ili kiweze kutoa mafunzo kwa watu wote ikiwa ni pamoja na
Makandarasi.
·
Kuhamasisha
kupatikana kwa mwelekeo mmoja (National Framework) utakaofuatwa na watu wote
wanaojihusisha kwa njia moja au nyingine na matumizi ya teknolojia hii katika
kazi za barabara.
·
Kuiendeleza
‘Labour Based Documentation Center’ kwa kukusanya na kusambaza takwimu na
taarifa mbalimbali zinazohusiana na matumizi ya teknolojia hii katika kazi za
barabara.
USHIRIKISHWAJI WA WANAWAKE KATIKA
KAZI ZA BARABARA
34.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu kupitia Kitengo cha Wanawake inaendelea kuhamasisha na
kuwaelimisha wanawake ili waweze kushiriki kwa wingi zaidi katika kazi za
barabara. Lengo kuu la kuanzishwa kwa Mpango huu ni kuhakikisha kuwa wanawake
nao wanashiriki katika kazi za ukarabati na matengenezo ya barabara kwa ajili
ya kujipatia pato, kuchangia maendeleo nchini na kujikwamua na umasikini.
Wizara kupitia mikoa inayotekeleza mpango huu inaendelea kuhamasisha na
kuwaelimisha wanawake ili waweze kushiriki kwa wingi zaidi katika kazi hizi.
Mpango huu umekuwa ukikua mwaka hadi mwaka kutoka mikoa 5 ya majaribio katika
mwaka 1993 hadi mikoa 14 hivi sasa. Hadi sasa mikoa inayotekeleza Mpango huu ni
Mtwara, Lindi, Mbeya, Iringa, Ruvuma, Morogoro, Dar es Salaam, Pwani, Kagera,
Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Shinyanga na Mbeya. Katika mikoa hii asilimia 20 ¾ 35 ya nguvu kazi za barabara ni wanawake.
35.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2001/2002 Wizara yangu
ilitoa mafunzo ya upangaji mipango yenye mtazamo wa kijinsia kwa washika dau wa
Wizara, Mikoa na Wilaya ili kujenga msingi imara wa ushirikishwaji wanawake
katika sekta ya ujenzi. Aidha ili kujenga msingi imara wa ushiriki wa wanawake
katika kazi za barabara, Wizara yangu kwa kushirikiana na vyombo vingine
itaendelea kufanya uhamasishaji kwa wanawake waweze kuunda vikundi vya
ukandarasi ili kuweza kufaidika na zabuni za barabara ikiwa ni pamoja na
kuongeza ajira ya nguvu kazi kwa wanawake. Pia, Wizara yangu kwa kushirikiana
na Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD) imeweza kutoa mafunzo ya jinsia na
uongozi kwa viongozi wa ngazi za juu wa Wizara (Wakurugenzi na Wakurugenzi
wasaidizi) wapatao 35. Lengo la mafunzo haya ni kuwawezesha kupanga mipango
yenye mtazamo wa kijinsia, kuelewa mikataba mbalimbali ambayo imeridhiwa na
Serikali yetu kwa lengo la kumwendeleza mwanamke katika nyanja mbalimbali,
usawa wa kijinsia na kuangalia/kuweka mikakati ya kuendeleza dhana ya
ushirikishwaji wa wanawake katika sekta ya ujenzi. Kwa kushirikiana na mikoa ya
Mtwara na Lindi, inayofadhiliwa na Finnida, Morogoro (SDC), Pwani (DANIDA),
Iringa na Ruvuma (EDF) na Mwanza (UNDP), kitengo cha ushirikishwaji wa wanawake
cha Wizara yangu kimeweza kuunda vikundi vya makandarasi wadogowadogo hivyo
kuhamasisha wanawake kujiunga na kuongeza ajira ya nguvu kazi kwa asilimia 35%.
36.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2002/2003 Wizara yangu itaendelea kutoa
mafunzo ya upangaji mipango yenye kuzingatia jinsia katika ngazi mbalimbali ili
kuongeza kasi ya ushirikishwaji wanawake katika sekta ya ujenzi kutoka asilimia
35% ya sasa hadi 50%. Aidha, Kitengo cha wanawake cha Wizara yangu kwa
kushirikiana na Mameneja wa Mikoa wa Wakala wa Barabara kitaendelea kufanya
uhamasishaji kwenye Mikoa ile ambayo haijaanza utekelezaji wa mpango huu ili
mpango uweze kutekelezwa nchi nzima kama ilivyokusudiwa.
KITUO
CHA USAMBAZAJI WA TEKNOLOJIA KATIKA SEKTA YA USAFIRISHAJI (TANZANIA TECHNOLOGY
TRANSFER (T2) CENTRE)
37.
Mheshimiwa
Spika, Kituo hiki kilianzishwa mwaka 1997 kutokana na juhudi za Wizara yangu kwa kushirikiana na Chuo
Kikuu cha Dar es salaam pamoja na msaada wa Shirika la Barabara la Marekani (US FHWA). Madhumuni ya
kituo hiki ni kuimarisha/kuboresha
sekta ya usafirishaji kwa kutumia mbinu ya usambazaji wa Teknolojia. Kwa
kuanzia kituo kinajihusisha na usambazaji wa teknolojia katika sekta ya barabara.
38.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2001/2002, Wizara yangu kwa kupitia Kituo
hiki iliendelea kusambaza Teknolojia katika sekta ya usafirishaji hapa nchini
kwa kusambaza kwa wadau makala zinazoelezea teknolojia mbalimbali katika sekta
ya usafirishaji na kuendelea na utekelezaji wa mradi wa kuhamasisha wanafunzi
wa shule za Sekondari kuchukua masomo ya Sayansi (TRAC Programme) kwa shule za
Sekondari za Jangwani, Mzizima na Azania ziliziko jijini Dar es Salaam. Aidha, Kituo kimefanya utafiti unaolenga
kuboresha utendaji kazi wake, kukiwezesha kuwa endelevu na kutayarisha Mpango
wa muda mfupi na mrefu kuhusu usambazaji wa teknolojia hapa nchini. Pia,
kiliandaa na kukamilisha makubaliano ya ushirikiano (Memorandum of
Understanding) na Shirikisho la Barabara Duniani (World Road Association)
litakalowezesha kituo kupata misaada na kubadilishana teknolojia katika masuala
ya sekta ya barabara, na kuimarisha huduma za kituo kwa kununua vifaa
mbalimbali.
39.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2002/03, Wizara yangu ina mpango wa
kukiendeleza kituo hiki ili kiweze kusambaza teknolojia katika sekta ya
barabara na usafirishaji, kukamilisha utafiti kuhusu uboreshaji wa huduma za
Kituo na kuanza utekelezaji wa mapendekezo yake, kuandaa kozi, semina na warsha
zinazohusu sekta ya usafirishaji, kwa wadau. Pia kituo kitaendelea kutekeleza
mradi wa kuhamasisha wanafunzi wa shule za Sekondari kuchukua masomo ya Sayansi
na Teknolojia (TRAC Programme). Aidha
kituo kitaendelea kuboresha njia za kisasa ya upashanaji habari na nyaraka
mbalimbali kitaalamu kupitia mtandao wa kompyuta (Website), uboreshaji wa
huduma za maktaba ya Kituo na kukiimarisha kwa kununua vifaa mbalimbali.
CHUO CHA UJENZI MOROGORO
40.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu ina Chuo cha Ujenzi Morogoro kilichoanzishwa kwa
madhumuni ya kuwapa mafunzo kazini Mafundi Sanifu (Technicians) na Wahandisi wa
Wizara ya Ujenzi na Halmashauri za Miji/Wilaya. Katika mwaka wa fedha 2001/02
Chuo kilipanga kutoa mafunzo kwa Mafundi Sanifu na Wahandisi 75. Hadi kufikia
Juni 2002, Mafundi Sanifu 87 wamepata mafunzo mbalimbali chuoni. Aidha, Chuo
kimeweza kukarabati baadhi ya majengo yake.
41.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2002/03 Chuo kimepanga kutoa mafunzo kwa idadi
ya Wahandisi na Mafundi Sanifu 90 kutoka Idara na Wakala mbalimbali. Aidha,
Chuo kimepanga kuendelea kuyafanyia ukarabati majengo ya Chuo pamoja na ununuzi
wa samani na gari kwa ajili ya kurahisisha mafunzo.
42.
Mheshimiwa Spika, ajali za barabarani limekuwa tatizo kubwa hapa nchini. Taifa
limekuwa likipoteza watu wengi kutokana na ajali za barabarani. Aidha Serikali
hutumia fedha nyingi zikiwemo za kigeni katika ununuzi wa dawa, vipuri kwa
ajili ya kutengeneza magari yaliyopata ajali au kununua mengine mapya baada ya
kuharibika kabisa. Tathmini inaonyesha kuwa gharama hizi hufikia asilimia kati
ya 1 na 2 ya pato la Taifa kwa mwaka.
43.
Mheshimiwa Spika, kutokana na utafiti, ajali nyingi husababishwa na mambo yafuatayo;
uendeshaji mbaya wa magari, baadhi ya magari kuendeshwa yakiwa mabovu na uzembe
wa watumiaji wengine wa barabara. Aidha uzidishaji wa uzito katika magari
makubwa huchangia sana uharibifu wa barabara kabla ya muda wake uliokadiriwa
wakati wa kusanifiwa na hivyo kuongeza gharama za matengenezo.
44.
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimekuwa nikilieleza Bunge lako Tukufu, Wizara imekuwa ikichukua
hatua mbalimbali zinazolenga kupunguza ajali pamoja na uharibifu wa barabara
unaotokana na uzidishaji uzito. Katika mwaka wa 2001/02, Kitengo cha Usalama
Barabarani kimeweza kutekeleza kazi zifuatazo: -
·
Kuimarisha mfumo wa
kisasa wa uwekaji takwimu za ajali kwenye kompyuta kwa kuwapa mafunzo zaidi
wataalam husika ili iwe rahisi kufahamu sehemu sugu za ajali na kuzirekebisha
ipasavyo.
·
Wizara kwa
kushirikiana na Wizara ya Elimu na Utamaduni na Taasisi ya Elimu Tanzania
inalenga kuendeleza elimu ya usalama barabarani katika shule zote za msingi na
sekondari pamoja na vyuo vya Walimu hapa nchini. Mitaala ya Elimu ya Usalama
Barabarani imeshaandaliwa na majaribio ya kufundisha somo hili yanafanywa
katika baadhi ya shule za msingi na sekondari katika mikoa ya Pwani, Dar es
salaam na Morogoro.
·
Wizara imeandaa mfumo
bora wa ukaguzi wa magari unaoendana na mapendekezo ya Umoja wa Nchi za Kusini
mwa Afrika (SADC) na Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC).
·
Wizara kwa kupitia
redio, magazeti na televisheni imekuwa ikiendesha kipindi cha “Barabara zetu”,
ili kuwaelemisha wananchi juu ya utumiaji bora na salama wa barabara zetu na
ubebaji wa mizigo.
·
Ili kudhibiti uzito
na kuondoa tatizo la rushwa, Wizara kupitia Wakala wa Barabara imekuwa
ikiwashirikisha wadau wote kuanzia wanaoagiza na wanaosafirisha mizigo mfano
Mamlaka ya Bandari, Mamlaka ya Mapato (TRA), Shirika la Viwango (TBS), Mamlaka
ya Leseni za Usafirishaji, Taasisi ya Kuzuia Rushwa (PCB) pamoja na Kitengo cha
Vipimo (Weights and Measures) ili kuhakikisha kwamba mizigo inayoagizwa na
kusafirishwa katika barabara zetu inakuwa katika viwango vinavyoruhusiwa kwa
mujibu wa Sheria ya Road Traffic Act.
Na. 30 ya mwaka 1993, Regulation 2001 – Section 114.1P. (Max. Vehicle Weight) na
hivyo kupunguza mianya ya rushwa.
45.
Mheshimiwa Spika, Mpango wa mwaka wa fedha 2002/03 ni :-
·
Kujenga vituo vipya
vya mizani za kisasa katika maeneo ya Mikese (Morogoro), Mpemba (Tunduma) na
Mutukula (Kagera).
·
Kuendelea
kuwaelimisha wananchi, madereva, wamiliki wa vyombo vya usafiri umuhimu wa
kuzingatia kanuni bora za utumiaji wa barabara.
·
Wizara itaendelea
kusimamia majaribio ya elimu ya usalama barabarani katika baadhi ya shule za
msingi, sekondari na vyuo katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro na
kupanua majaribio haya katika kanda nyingine.
·
Kutoa mafunzo kwa
Askari wa Usalama barabarani na Wahandisi mbalimbali juu ya uingizaji wa
takwimu za ajali kwenye kompyuta na uchambuzi wake wa vyanzo vya ajali.
·
Kukamilisha rasimu ya
mfumo wa shule za udereva, upimaji na utoaji wa leseni kwa madereva.
·
Mapendekezo yaliyo
kwenye mifumo ya Ukaguzi wa magari, uendeshaji wa kozi za madereva pamoja na
utoaji leseni kwa madereva itawasilishwa katika vyombo husika kuomba ridhaa ya
Serikali kuanza kutekelezwa.
·
Kuendelea kutoa
mafunzo kwa Wahandisi na Watumishi wengine wa Wizara jinsi ya kufanya Road
Safety Audit.
IDARA YA
UFUNDI NA UMEME
46.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2001/02
Idara ya Ufundi na Umeme iliendelea kutekeleza majukumu yake ya kuratibu,
kutathmini, kusajili, kufuta, kukodisha na kufanya matengenezo ya magari na
mitambo ya Serikali, uendeshaji wa Vivuko na Mitambo ya kusaga mawe, ushauri,
usimamizi wa miradi, usimikaji na matengenezo ya mitambo ya umeme, majokofu,
viyoyozi na vifaa vya Elektroniki.
47.
Mheshimiwa Spika, katika kuboresha huduma
zitolewazo na Idara hii, Wizara yangu
katika mwaka 2001/02 ilitekeleza yafuatayo:
·
Zabuni
zimetangazwa kwa lengo la kumpata Mhandisi Mshauri wa kufanya upembuzi yakinifu
na baadaye kuandaa zabuni kwa ajili ya matengenezo ya vivuko vitano kwa
kugharimiwa na fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia (IDA). Vivuko hivyo ni MV.
Sengerema, MV. Pangani, MV. Kigamboni, MV. Rufiji, MV. Ulanga.
·
Ununuzi
wa vifaa vya kisasa na uimarishaji wa huduma za utengenezaji wa magari na
mitambo katika karakana zote za Idara ya Ufundi na Umeme.
·
Magari
madogo (Saloon) mapya kumi (10)
yamenunuliwa kwa nia ya kuimarisha kitengo cha kukodisha magari ya Serikali
yaani GTA. Aidha magari manne ya kuimarisha ukaguzi wa kazi yamenunuliwa.
Vilevile gari moja maalum (Bucket Wagon) limenunuliwa kwa lengo la kuboresha
huduma za ubadilishaji taa za kuongozea magari pamoja na taa za barabarani.
·
Kivuko
kipya chenye uwezo wa kubeba tani 50 kimenunuliwa kwa ajili ya mto Kilombero.
·
Ukarabati
wa mitandao ya umeme (Electrical systems) ulifanyika katika majengo ya Wizara
ya Ulinzi na Mahakama ya Rufaa Dar es Salaam.
Aidha ukaguzi wa mtandao wa umeme ulifanyika kwenye majengo ya Wizara ya
Elimu na Utamaduni na Wizara ya Afya.
·
Kusajili magari ya Serikali yenye namba za
kiraia.
Kwa
muda mrefu sasa, Serikali imekuwa ikiingia gharama kubwa kutokana na kulipia
Bima na matumizi mabaya ya magari ya Serikali ambayo yamesajiliwa kwa namba za
kiraia. Katika kutekeleza Sheria ya
Usalama Barabarani ya mwaka 1973 na Waraka Na.1 wa Rais wa mwaka 1998 unaohusu
kubana matumizi ya Serikali, Wizara imetekeleza zoezi maalum la kusajili magari
3,139; pikipiki 1,407; na mitambo 120 iliyokuwa na namba za kiraia kuanzia
Februari, 2002 hadi tarehe 29/6/2002.
Zoezi hili linaendelea hadi magari, mitambo na pikipiki zote
zitakaposajiliwa na tunategemea kuokoa zaidi ya Shilingi bilioni 10 za
Serikali.
48.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002/03 Wizara
yangu kupitia Kitengo cha Ufundi na Umeme kitatembelea Mikoa yote, Wilaya zote
na miradi yote ya Serikali ili kufanya uhakiki wa kusajili mali za Serikali
ikiwa ni pamoja na Magari, pikipiki na Mitambo na hii itasaidia kujua Mitambo
halisi ya Serikali. Ningeomba
Waheshimiwa Wabunge na Wananchi kwa
ujumla waisaidie Idara hii katika kupata taarifa ya vifaa hivi vya Serikali
katika maeneo yao. Katika mwaka wa
Fedha wa 2002/03 Idara hii inalenga kutekeleza kazi zifuatazo:-
·
Ununuzi
wa kivuko kipya chenye uwezo wa kupakia tani 25 kwa ajili ya Bugolora¾Ukara (Mwanza).
·
Kuendelea
na ukarabati wa vivuko na kununua vifaa vya uokoaji majini kwa ajili ya vivuko
(Life Saving Equipments and Life Jackets).
Aidha mafunzo ya uokoaji kwa wafanyakazi wa vivuko vyote nchini
yataendeshwa.
·
Kuimarisha
Karakana za viyoyozi, majokofu na elektroniki zilizopo katika Mikoa ya Dodoma,
Arusha na Tanga ili ziweze kutoa huduma nzuri zaidi.
·
Kuendelea
kununua vitendea kazi vya kisasa (Workshop Tools) zaidi ili kuboresha huduma
zitolewazo na Wizara hii.
·
Kuendelea
kukagua na kukarabati mitambo ya umeme kwenye majengo na Taasisi za Serikali
kwa nia ya kuepusha majanga yatokanayo na hitilafu za umeme kama vile moto.
·
Kuendelea
kujiandaa ili Kitengo hiki nacho kiwe Wakala kwa mujibu wa Sheria Na. 30 ya
Mwaka 1997.
49.
Mheshimiwa Spika, Idara ya Ugavi na Huduma chini ya Wizara yangu inalenga katika
kuhakikisha kunakuwepo na mfumo imara wa kuendesha shughuli za ununuzi na Ugavi
Serikalini zenye ufanisi unaolenga matumizi bora ya fedha za Serikali. Umuhimu
wa fani ya Ugavi hasa katika mazingira ya sasa ya uchumi unaotegemea nguvu za
soko unaendelea kudhihirika kwani utaalamu wa fani hii huleta thamani kwa kila
Shilingi inayotumika katika ununuzi.
50.
Mheshimiwa Spika, Wataalamu wa Ugavi wanahusika na shughuli za
kupanga kwa ufanisi upatikanaji wa mahitaji mbalimbali kwa ajili ya shughuli za
Wizara, Idara na Taasisi za Serikali.
Ili kufanikisha shughuli hizi Idara husimamia wataalamu ili kuhakikisha
kuwa ununuzi wa vifaa, kazi na huduma, utunzaji wa vifaa na mali za Serikali
pamoja na kumbukumbu zake unafanywa kwa ufanisi.
51.
Mheshimiwa Spika, Idara pia husimamia shughuli za Bohari Kuu ya Serikali, Wakala wa
Ugomboaji na Usafirishaji wa mizigo ya Serikali pamoja na maendeleo ya
Watumishi wa kada ya Ugavi Serikalini.
52.
Mheshimiwa Spika, takwimu mbalimbali zinaonyesha kuwa, kati ya asilimia 60 hadi 70 ya Bajeti
ya Serikali hutumika kila mwaka katika ununuzi wa vifaa, kazi na huduma (goods,
works & services). Hii ina maana
kwamba wataalamu hawa wanapaswa kuwajibika zaidi kusimamia matumizi ya fedha za
Serikali na kwa ufanisi. Kutokana na jukumu hilo watumishi hao wanapaswa
kuzingatia maadili ya taaluma yao ili kuepuka hasara ambazo hutokea kutokana na
usimamizi dhaifu katika shughuli za Ugavi. Wizara yangu ikizingatia hasara
ipatikanayo kutokana na udhaifu huo haiwezi kuacha hali hii iendelee, hasa
ikizingatiwa kwamba Serikali ina jukumu la kujenga uchumi imara ili kuleta
maendeleo kwa wananchi wake kwa kuondoa umaskini na kuongeza pato la Taifa.
53.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002/03 Wizara yangu inalenga katika
kuongeza ufanisi ili Serikali ipate vifaa na huduma zenye ubora ambao
utalingana na thamani ya fedha zinazotumika. Ili kufanikisha azma hii wizara
yangu inatarajia kufanya yafuatayo:-
·
Kuandaa
orodha ya viwango (standard specifications) ya vifaa ambavyo vitatumika
Serikalini kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
·
Kuhakikisha
kuwa Watumishi wa Ugavi Serikalini wanafanya kazi zao kwa kuzingatia sheria,
kanuni na taratibu kama zilivyoainishwa na Sheria ya Ununuzi ya Umma ya mwaka
2001 na Sheria Namba 9 ya NBMM ya mwaka 1981.
·
Kuhakikisha
kwamba watumishi wa Ugavi wanapewa mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi katika
taaluma yao ili wafanye kazi zao kwa ufanisi.
·
Kuimarisha
shughuli za Wakala wa Ugomboaji na Usafirishaji wa shehena za Serikali ili
iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kwa gharama nafuu.
·
Kuendelea
kuboresha mfumo wa Ununuzi na Utunzaji wa vifaa (Procurement and Supply
Management Systems) katika Wizara, Idara, kuhakikisha kuwa Taasisi na Mikoa ili
kuleta ufanisi katika uagizaji, upokeaji, utunzaji na utoaji wa vifaa.
54.
Mheshimiwa Spika, ili kuleta ufanisi, Wizara yangu katika mwaka 2002/03
itafuatilia suala la ajira ili kuhakikisha kuwa Taasisi zote za Serikali Kuu na
Serikali za Mitaa zinaajiri wataalamu wa Ugavi ambao wamesajiliwa na Bodi ya
Taifa ya Usimamizi wa Vifaa kama Sheria inavyotaka. Ni matarajio ya Wizara
yangu kuwa utekelezaji wa mkakati huu utaweza kuleta ufumbuzi kwa matatizo ya
upotevu wa fedha na mali za Serikali katika harakati za kupunguza umaskini ili
kuleta maendeleo ya nchi .
56.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa
2001/02, Baraza lililenga kutoa msukumo katika kukamilisha Sera ya Taifa ya
Ujenzi, kuendelea na shughuli za mafunzo kwa Makandarasi, Washauri, Watendaji
Wakuu hasa wa Serikali za Mitaa kuhusu sheria mpya ya Manunuzi ya Umma (Public
Procurement Act No. 3 of 2001), usimamizi wa mikataba ya ujenzi; kuboresha
upatikanaji wa takwimu za shughuli za ujenzi; utayarishaji wa miongozo ya
kiufundi; huduma za ushauri, ukaguzi wa miradi, na usuluhishi wa migogoro. Aidha Baraza lilipanga kukamilisha uundaji
wa Mfuko wa fedha wa Maendeleo ya Sekta ya Ujenzi (Construction Industry Development Fund – CIDF).
57.
Mheshimiwa Spika, huduma ya mafunzo imeendelea
kuwa miongoni mwa mambo muhimu yaliyoshughulikiwa na Baraza katika mwaka huu wa
fedha. Mafunzo yafuatayo yalitolewa:-
·
Matengenezo
na ujenzi wa barabara kwa kutumia nguvu kazi (labour based technology)
yalitolewa kwa wahandisi na mafundi 21 wa mradi wa kilimo wa “Participatory
Irrigation Development Programme (PIDP)” na pia kwa makandarasi 6 wa Wilaya ya
Muheza.
·
Kanuni za zabuni na mikataba ya ujenzi yalitolewa kwa
wahandisi kutoka Halmashauri za Wilaya 29.
·
Udhibiti wa mikataba na sheria mpya ya Manunuzi ya Umma ya
mwaka 2001 yalitolewa kwa makandarasi 30 na wahandisi 18 wa mikoa ya Lindi na
Mtwara.
·
Baraza lilishiriki katika kutoa mafunzo kwa Kamati ya Bunge
ya Fedha na Uchumi juu ya sheria mpya ya Manunuzi ya Umma. Mafunzo haya
yaliandaliwa na Wizara ya Fedha.
·
Tathmini za zabuni
(tender evaluation), ukaguzi wa kiufundi (technical audit), mambo ya kisheria
yahusuyo zabuni na mikataba na masuala ya madai katika kandarasi za ujenzi kwa
washiriki wapatao 140.
·
Matengenezo na ujenzi
wa barabara kwa Kanda ya Kati na Nyanda za Juu Kusini yameendelea kutolewa kwa
makandarasi 32. Zabuni na usimamizi wa mikataba ya ujenzi yalitolewa kwa
wahandisi 30 wa TANROADS wa mikoa ya Iringa na Ruvuma.
58.
Mheshimiwa Spika, Baraza limepiga hatua kubwa katika kuanzisha Mfuko
wa Fedha wa Maendeleo ya Sekta ya Ujenzi.
Mfuko huu umeshaanzishwa na Kamati ya Uendeshaji imeshateuliwa. Mfuko huu unategemewa kutoa huduma za
dhamana na ukopeshaji wa fedha kwa walengwa ambao ni wadau wote wa Sekta ya
Ujenzi.
59.
Mheshimiwa
Spika,
nafurahi kulitangazia Bunge lako kwamba Baraza lilitoa huduma za ushauri
zipatazo 34 ikiwa ni pamoja na usuluhishi wa migogoro mitano. Aidha Baraza
limetengeneza miongozo ya taratibu za zabuni kwa miradi ya Wizara za Afya Ofisi
ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Wizara ya Kilimo –
Mradi wa Programu ya kilimo (Agricultural Sector Programme Support).
60.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2002/2003 Baraza litaendelea kutoa Huduma za
Ushauri wa Kiufundi kwa wateja wake kuhusiana na tathmini za zabuni, uteuzi wa
washauri, utayarishaji wa makabrasha ya zabuni, madai, usuluhishi wa migogoro,
usimamizi wa miradi na uchapishaji wa majarida.
BODI YA
TAIFA YA USIMAMIZI WA VIFAA (NBMM)
61.
Mheshimiwa
Spika, Bodi ya Taifa ya
Usimamizi wa Vifaa (National Board for Materials Management – NBMM) ni Taasisi
ya Serikali iliyoanzishwa kwa Sheria ya Bunge Na 9 ya mwaka 1981 kwa lengo la
kukuza na kuendeleza taaluma ya Ugavi. Bodi katika kutekeleza majukumu yake
hutoa miongozo mbalimbali, mafunzo na ushauri wa kitaalamu kwenye taaluma ya
Ugavi, aidha huratibu mafunzo na kuendesha mitihani ya taaluma ya Ugavi. Bodi
pia, husimamia na kudhibiti mienendo ya wataalamu wafanyao kazi za Ugavi
kupitia njia ya usajili, ambapo hadi mwezi Juni 2002 wataalamu wapatao 1,379
wameshasajiliwa na Bodi.
62.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa 2001/02 Bodi imefanya ukaguzi katika
sehemu mbalimbali za kazi kwenye Serikali na Taasisi zake pia Mashirika
mbalimbali ya Umma na binafsi kwa mikoa ya Dar es salaam na Mbeya kwa madhumuni
ya kuwaelimisha na kufuatilia utekelezaji wa Sheria ya Bunge Namba 9, ya mwaka
1981. Aidha katika ukaguzi huo Waajiri walitakiwa kuajiri Wataalamu wenye sifa
katika fani ya Ugavi na ununuzi na kusisitiza juu ya uzingatiaji wa miiko ya
maadili (ethical code of conduct) ili kuepuka hasara kwa Taasisi na Mashirika
hayo na Taifa kwa ujumla kutokana na ununuzi usiokuwa wa kitaalamu. Bodi imepanga kuwachukulia hatua kali za
kisheria wale wote watakaobainika kukiuka utekelezaji wa sheria hiyo. Kwa
kipindi cha mwaka huu wa fedha Bodi imesajili wataalamu wapya wapatao 220, pia
ni azma ya Bodi kuwafutia usajili wataalamu watakaobainika kukiuka miiko ya
maadili ya taaluma. Katika kipindi hiki Bodi haikuwasajili waombaji wawili
waliokuwa na vyeti vya kughushi na wamefikishwa kwenye vyombo vya dola kujibu
mashtaka hayo. Aidha, Bodi imetahini watahiniwa 1996 katika ngazi mbalimbali za
taaluma, kati yao watahiniwa 502 sawa na asilimia 25.1 walifaulu mitihani yao,
42 wamefutiwa matokeo ya mitihani yao kutokana na kukiuka taratibu na kanuni za
mitihani na waliosalia ama wanarudia mtihani au baadhi ya masomo. Hadi kufikia
Juni 2002 jumla ya watahiniwa 10,108 sawa na asilima 40.6 ya watahiniwa wote
24,896 wamefuzu mitihani yao katika ngazi mbalimbali.
63.
Mheshimiwa Spika, Bodi imeanza kufanya marekebisho makubwa katika mtaala wa
kufundishia ili kwenda na wakati. Aidha Bodi inaandaa utaratibu utakaowezesha
kuimarisha kitengo cha Ushauri na Utafiti wa kitaalamu (Research and
Consultancy Unit) ili kuboresha ushauri unaotolewa kwenye Serikali na Taasisi
zake hasa katika masuala yote yanayohusiana na shughuli za Ugavi.
64.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2002/03, Bodi imeweka majukumu
yafuatayo kwa ajili ya utekelezaji:-
·
Kusajili wataalam 200
na kuwatahini watahiniwa 2,500 katika ngazi mbalimbali.
·
Kwa kushirikiana na
Waajiri, kuwachukulia hatua mbalimbali za kinidhamu Wataalamu wote
watakaobainika wanakiuka miiko ya maadili ya taaluma, kusababisha matumizi
mabaya ya fedha katika ununuzi na utunzaji vifaa, kwa lengo la kuongeza ufanisi
wa kazi katika njia ya uwazi na ukweli na kupambana na rushwa.
·
Kuendelea kutoa
mafunzo kwa njia ya warsha na makongamano juu ya umuhimu wa matumizi ya njia
bora za kisasa katika ununuzi na ugavi.
·
Kuendelea na ukaguzi
na kuwachukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha kwenye vyombo
vya dola Waajiri na Wataalamu mbalimbali Serikalini, kwenye Taasisi na
Mashirika ya Umma na binafsi wanaoajiri Wataalam ambao hawajasajiliwa na Bodi.
Ukaguzi huo utahusu mikoa yote ya Tanzania bara.
·
Kufanya marekebisho
katika mtaala wa kufundishia kwa lengo la kupata wataalamu wenye sifa na upeo
mkubwa zaidi hasa wakati huu wa utandawazi na mabadiliko ya tekinolojia.
·
Kushirikiana na Bodi
zingine pamoja na taasisi mbalimbali katika kuyatafutia ufumbuzi matatizo
yanayoathiri utendaji bora wa wataalamu wa ugavi.
·
Kuendelea
kuwaelimisha waajiri juu ya namna bora za utunzaji na usimamizi wa vifaa na
uwekaji sahihi wa kumbukumbu za manunuzi, pia taratibu bora za ununuzi.
·
Kubuni mbinu
mbalimbali za kuwezesha kuongeza idadi ya wanaofaulu mitihani kwa kiwango
kikubwa zaidi.
65.
Mheshimiwa Spika, majukumu ya Bodi hii ni pamoja na kusajili, kuendeleza ubora na kudhibiti
mwenendo wa kitaaluma wa Wahandisi na Makampuni ya ushauri wa kihandisi. Aidha katika kipindi cha mwaka 2001/02 Bodi
ya Usajili wa Wahandisi imetekeleza yafuatayo:-
·
Hadi mwishoni mwa
Juni 2002, Bodi ilikuwa imesajili Wahandisi 447 na Makampuni ya ushauri wa
kihandisi 13, hivyo kufanya idadi ya Wahandisi waliosajiliwa nchini kufikia
4,435 na Makampuni ya ushauri wa kihandisi kufikia 84 yakiwemo makampuni 20 ya
kigeni.
·
Bodi ilitembelea
mikoa ya Dar es Salaam, Iringa, Mbeya Ruvuma, Kilimanjaro na Arusha ili kukagua
shughuli za kihandisi viwandani, kwenye miradi na mashirika ya Umma.
·
Bodi iliandaa
mitihani ya kitaalamu kwa ajili ya kuwapandisha daraja “Technician Engineers”
kufikia kiwango cha “Professional Engineers”. Jumla ya Technician Engineers 58
walifanya mitihani hiyo na watahiniwa 35 kufaulu.
·
Bodi imechapisha
majarida, kuandaa miongozo ya mafunzo kwa vitendo (Internship) kwa fani 11 za
uhandisi, mihadhara ya kitaalam (Professional Lectures) na kozi fupi za ujenzi.
66.
Mheshimiwa Spika, Bodi imewafuta kwenye orodha Wahandisi 189 na Makampuni mawili (2)
ya ushauri wa kihandisi kutokana na kukiuka miiko ya taaluma hii. Narudia wito
wangu wa siku zote kwamba wataalamu wote wa Sekta ya Ujenzi lazima watekeleze
kazi zao kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za taaluma husika. Huu ni
msingi muhimu wa kujenga na kuendeleza wazalendo.
67.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2002/03 Bodi inakusudia kufanya yafuatayo:
·
Kuendelea kusajili
Wahandisi.
·
Kuhakikisha
kuwa Wahandisi wote wa kigeni pamoja na Makampuni ya kigeni ya ushauri wa
kihandisi yanayofanya kazi katika miradi iliyofadhiliwa na nchi zao
wanasajiliwa na Bodi.
·
Kutoa
mafunzo kwa vitendo (internship) kwa wahandisi wanaomaliza mafunzo yao vyuoni.
·
Kuendelea
kuuelimisha Umma juu ya athari za kutumia wataalam wasio na sifa za kihandisi.
·
Kuendelea kufanya
kaguzi za mara kwa mara juu ya mienendo na shughuli za kihandisi.
·
Kuendeleza mikakati
ya kupambana na rushwa katika fani ya uhandisi.
BODI YA USAJILI WA WABUNIFU MAJENGO
NA WAKADIRIAJI MAJENZI (AQSRB)
68.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2001/02 Bodi ya AQSRB
ilipanga kutekeleza majukumu yafuatayo:-
·
Kuendelea kusajili
Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi.
·
Kuendeleza kuimarisha
ukaguzi katika maeneo ya ujenzi
·
Kuendelea kuhamasisha
watu wote waone umuhimu wa kutumia Wataalam waliosajiliwa na Bodi.
·
Kushirikiana na
Serikali, Bodi nyinginezo na Taasisi mbalimbali katika kutafuta ufumbuzi wa
matatizo yanayoathiri utendaji bora wa kazi katika sekta ya ujenzi.
69.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2001/02 Bodi ilifanya ukaguzi katika maeneo ya
Ujenzi katika mikoa 13 ambayo ni: - Kilimanjaro, Arusha, Mwanza, Shinyanga,
Dodoma, Ruvuma, Iringa, Morogoro, Pwani, Singida, Mbeya, Kagera na DSM. Katika
ziara hii, pamoja na ukaguzi, Bodi iliwakumbusha Wajenzi umuhimu wa kufuata
sheria Aidha Bodi, iliendelea kutoa elimu kwa Umma kuhusu umuhimu wa kutumia
wataalam waliosajiliwa na Bodi.
70.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwishoni mwa Juni 2002, Bodi ilikuwa imeshasajili jumla
ya wataalam 270 katika fani za Wabunifu Majengo (Wazalendo) 133, Wakadiriaji
Majenzi (Wazalendo) 83, Wabunifu Majengo (Wageni) 41 na Wakadiriaji Majenzi
(Wageni) 13. Aidha, makampuni 95 yalikuwa yamesajiliwa na yanafanya kazi.
Katika mwaka huo huo wataalam 92 waliomba kufanya mitihani na 81 walitahiniwa.
Ili kuimarisha nidhamu ya wataalam waliosajiliwa Bodi iliwafutia usajili
wataalam wake kumi(10) na kampuni moja.
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002/03 Bodi
itaendelea kutekeleza majukumu yake ya msingi ikiwa ni pamoja na :
·
Kusajili wataalam
wapya
·
Kufanya ukaguzi wa
maeneo ya majenzi
·
Kusimamia kwa makini
sheria Na. 16 ya mwaka 1997 pamoja na taratibu zake
·
Kuendelea kuuelimisha
Umma kuhusu umuhimu wa kutumia Wataalam wa majenzi katika kazi za ujenzi
·
Kuboresha utaratibu
wa mitihani ya Bodi
·
Kuanzisha maktaba kwa
ajili ya kuweka kumbukumbu za rejea na habari nyingine muhimu kwa wataalam.
·
Bodi itatoa miongozo
ya mara kwa mara, yenye lengo ya kufafanua na kuelekeza mfumo wa utendaji kazi
za kila siku za kitaalam.
·
Bodi itaendelea na
mpango wa kutayarisha Sheria ya Majengo ambayo itakuwa sheria mama.
·
Kuanzisha mpango wa
Elimu Endelevu (CPD) ambao lengo lake kuu ni kuwanoa wataalam waliosajiliwa.
BODI YA
USAJILI WA MAKANDARASI (CRB)
71.
Mheshimiwa
Spika, kwa mujibu wa sheria ya Bunge
Na. 17 ya mwaka 1997, Bodi ya Usajili wa Makandarasi ina jukumu la kusajili
Makandarasi wa aina zote za ujenzi. Aidha Bodi inawajibika kuhakikisha kwamba
Makandarasi wote wanasajiliwa baada ya kuthibitisha kuwa wana sifa, uwezo wa
kitaalam na fedha za kufanyia kazi za ujenzi katika madaraja (class of
registration) watakayosajiliwa. Aidha Bodi ina jukumu la kujenga uwezo wa
Makandarasi wazalendo.
72.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha 2001/02 Bodi ilisajili Makandarasi 551 katika fani
na madaraja mbalimbali na kufanya jumla ya Makandarasi waliosajiliwa kuwa
2,428.
73.
Mheshimiwa
Spika, katika kutekeleza jukumu lake la msingi, Bodi ilifanya ukaguzi katika
miradi ya ujenzi 160 na kutathmini utendaji wa Makandarasi katika miradi
hiyo. Hadi mwishoni mwa Juni 2002, Bodi
ilifuta makandarasi 301 na kufanya jumla ya Makandarasi waliofutwa tangu mwaka
1998 kwa kushindwa masharti ya sheria na utendaji mbaya wa kazi kuwa 1,195. Aidha Bodi imepeleka Makamani Kampuni 20
zilizofanya kazi ya Ukandarasi bila kusajiliwa na Bodi.
74.
Mheshimiwa
Spika, kama nilivyokuwa nalieleza Bunge lako Tukufu, Bodi ya kusajili
Makandarasi ina jukumu kubwa la kujenga uwezo wa Makandarasi wazalendo. Bodi imeshaendesha warsha
16 kwa kushirikisha Makandarasi 2,423.
Katika mwaka 2001 Bodi ilitekeleza Mpango wake wa Mafunzo Endelevu
(Sustainable Structured Training Programme – SSTP). Kozi 10 zimeshafanyika na Makandarasi 291 wameshiriki katika
mafunzo mbalimbali ikiwemo misingi
ya biashara, uandaaji wa zabuni na jinsi ya kutekeleza vema mikataba.
Aidha, Bodi imeanzisha Mfuko wa
kusaidia Makandarasi wadogo (daraja v ¾ vii) kwa kuwadhamini katika benki ili
waweze kupewa dhamana zinazotakiwa bila kuwa na haja ya kuweka rehani kitu
chochote. Kwa kuanzia mpango huu utatoa dhamana kwa ajili ya zabuni (Bid Bonds)
na malipo ya awali (Advance Payment Guarantees).
Utaratibu huu utawawezesha Makandarasi wadogo ambao ndio
wengi kupata dhamana na pesa za kuanzia kazi kwa urahisi zaidi. Vile vile Bodi
inajenga uwezo wa uwakilishi wa Makandarasi kwa kuratibu uanzishwaji wa Chama
cha Kitaifa cha Makandarasi ambao utalenga kujenga mfumo mzuri wa ushirikiano
katika kutatua matatizo yanayowakabili Makandarasi.
75.
Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2002/03 Bodi itaendelea kusajili, kuratibu na kujenga uwezo wa
Makandarasi kwa kufuata sheria. Lengo
ni kuwa na Makandarasi wa Tanzania wenye uwezo kimitambo, ujuzi, mtaji,
wanaozingatia sheria, usalama, kanuni na maadili ya ujenzi ili kulinda haki na
usalama wa watumiaji wa Makandarasi hapa nchini na kufanya kazi nzuri kwa muda
uliopangwa.
UBINAFSISHAJI
WA PEHCOL
76.
Mheshimiwa Spika, PEHCOL ni
Shirika la Umma lililoundwa chini ya Wizara yangu kwa madhumuni ya kuboresha
upatikanaji wa mitambo na magari kwa ajili ya shughuli za ujenzi na matengenezo
ya barabara. Idara na Taasisi za
Serikali na Makandarasi binafsi ambao hawana uwezo wa kununua mitambo hutumia
mitambo na magari kutoka kwenye Shirika hili kwa kukodi.
Mheshimiwa
Spika, kama nilivyolieleza Bunge lako Tukufu
katika Hotuba yangu ya mwaka 2001/2002, taratibu za kuibinafsisha PEHCOL bado
zinaendelea chini ya PSRC.
MAENDELEO YA WATUMISHI
77.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa Fedha 2001/02 Watumishi 511 wa kada
mbalimbali wamepandishwa vyeo, 80 wamethibitishwa kazini na 6 wameajiriwa. Wizara yangu itaendelea
na zoezi hili kwa Watumishi watakaostahili kutokana na miundo ya Utumishi ya
kada zao. Katika mwaka wa fedha 2001/02 Watumishi 40 walihudhuria mafunzo ya
muda mrefu na Watumishi 222 walihudhuria mafunzo ya muda mfupi katika fani
mbalimbali. Lengo la kuwapatia mafunzo Watumishi ni kuwaongezea ujuzi na
ufanisi katika kazi zao. Wizara yangu itaendelea na juhudi za kuwapatia mafunzo
zaidi Wafanyakazi wake katika mwaka wa fedha 2002/03.
78.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2001/02 Wizara yangu imeunda na kuzindua rasmi
Baraza la Wafanyakazi tarehe 06/05/2002 ambalo limeshajadili na kupitisha
Miundo ya Utumishi ya Kada zilizo chini ya Sekta ya Ujenzi.
79.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2002/03 Wizara yangu itaendeleza azma yake ya
kuboresha mazingira ya kazi kwa wafanyakazi wake. Aidha, Watumishi 293 wa kada
mbalimbali watapata mafunzo ya ndani katika fani mbalimbali. Watumishi 1,247 watapandishwa vyeo.
80.
Mheshimiwa Spika, kutokana na maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano ni muhimu
Watumishi wote hasa viongozi wakuu wawe na elimu ya kompyuta.
81.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu imechangia juhudi za Kitaifa za
kupambana na kudhibiti maambukizo ya ukimwi.
Katika kipindi cha mwaka 2001/02 Wizara ilizindua
rasmi mkakati wa kupambana na ukimwi katika Wizara ya Ujenzi Makao Makuu na
Mikoani.
Aidha, Wizara imeanzisha kitengo maalum cha kubuni,
kusimamia na kuratibu utekelezaji wa mikakati ya kupambana na ukimwi kwa
watumishi wake na wananchi kwa ujumla waliopo kwenye maeneo ambayo shughuli za
ujenzi zinaendelea. Ni matarajio yetu
kuwa mkakati tulioanzisha wa kupambana na ukimwi utasaidia kwa kiwango kikubwa
kudhibiti maambukizo ya ugonjwa wa ukimwi.
82.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyolieleza Bunge lako Tukufu katika Hotuba yangu ya mwaka 2001/02,
Watumishi wa kada mbali mbali wakiwemo Wahandisi, Makandarasi, Wabunifu
Majengo, Wakadiriaji Majenzi, Wahandisi Washauri, Wahasibu na kadhalika
walihudhuria Semina juu ya kupiga vita rushwa katika Sekta ya Ujenzi. Aidha kutokana na Semina hiyo wajumbe
walitoa maazimio ya mikakati ya kupiga vita rushwa katika Sekta ya Ujenzi
ambayo Wizara yangu inaendelea kuyatekeleza.
Mheshimiwa
Spika, kama njia mojawapo ya
kupiga vita rushwa, Wizara yangu inatekeleza kikamilifu Sheria Na. 3 ya mwaka
2001 (Public Procurement Act. No. 3)
ambayo inapunguza sana mianya ya rushwa katika utoaji zabuni za ujenzi, ushauri
na ununuzi wa vifaa.
Vile vile katika kupunguza rushwa kwenye vituo vya
Mizani, Wizara inabadilisha mizani ya kizamani na kuweka mipya ambayo inatumia kompyuta
na imeongeza idadi ya mizani inayohamishika (Portable Weigh Bridges).
Aidha, Wizara yangu inaelimisha Umma matumizi bora ya barabara na haki
za watumiaji barabara kwa njia ya vipeperushi na matangazo magazetini.
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa usimamizi wa
ubora wa kazi za barabara Wizara imeimarisha maabara ya vifaa vya ujenzi
mikoani na kusisitiza matumizi yake katika kudhibiti ubora wa kazi. Pia Wizara inashirikiana na Idara ya Ukaguzi
(Technical Audit) ya Wizara ya Fedha katika kukagua miradi inayoendelea na
iliyokamilika.
83.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyokwisha eleza hapo awali, Wizara yangu
inatekeleza malengo yake kwa kutumia Bajeti ya Serikali, kushirikiana na
wananchi pamoja na misaada ya Wahisani mbalimbali. Napenda nitumie nafasi hii
kuzishukuru Serikali za nchi za Denmark, Finland, Italia, Japan, Kuwait,
Marekani, Norway, Saudi Arabia, Switzerland, Uholanzi, Uingereza na Ujerumani
ambazo kwa kiasi kikubwa zimesaidia sana sekta ya Ujenzi. Pia nayashukuru mashirika ya kimataifa ya
ADB, EU, IDA na Mfuko wa Maendeleo wa OPEC kwa kuendelea kusaidia sekta ya
ujenzi. Jitihada zao wote zimechangia katika mafanikio na maendeleo ya Wizara
yangu. Tunawashukuru sana kwa msaada wao.
84.
Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru tena Kamati ya Bunge ya
Miundo Mbinu chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Prof. Daimon Mwaga, Mbunge wa
Kibakwe, kwa ushauri mzuri waliotupa katika kuandaa bajeti hii. Nawashukuru pia
viongozi wenzangu katika Wizara ya Ujenzi ambao ni Naibu Waziri, Mheshimiwa
Hamza Mwenegoha (Mb), Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini, Katibu Mkuu, Eng.
John Kijazi, Mwenyekiti wa RFB Mama Mang’enya, Wenyeviti wa Bodi za NCC, CRB,
ERB, AQSRB, NBMM na PEHCOL. Aidha,
nawashukuru Wakurugenzi na Watendaji Wakuu wa Wakala zote zilizo chini ya
Wizara yangu pamoja na Wahandisi na Watendaji wote wa Wizara.
Makadirio ya Bajeti ya Wizara 2002/03
85. Mheshimiwa
Spika, ili Wizara yangu iweze kutekeleza majukumu na malengo yake ya mwaka
2002/03, naliomba Bunge lako Tukufu liidhinishe Bajeti ya jumla ya Shilingi
221,365.084 milioni ambapo kati ya hizo Shilingi 88,873.763 milioni ni za hapa
na Shilingi 132,491.321 milioni ni za nje.
Fedha za
hapa zinajumuisha:
(i) Shilingi 45,278.80 milioni za Mfuko wa
Barabara ambapo Shilingi 40,154.866 milioni ni kwa ajili matengenezo ya
barabara, Shilingi 4,449.67 milioni ni kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa
barabara Kuu na za Mikoa na Shilingi 674.27 milioni ni kwa ajili ya gharama za
usimamizi na uendeshaji Bodi ya Mfuko wa Barabara.
(ii) Shilingi 9,075.96 milioni kwa ajili ya
mishahara (Personal Emoluments) na matumizi mengineyo (Other Charges).
(iii) Shilingi 22,000.0 milioni kwa ajili ya mradi
maalum wa barabara kuu (Special Trunk Roads Project).
(iv) Shilingi 12,519.0 milioni kwa ajili ya miradi
ya maendeleo ya Barabara Kuu na za Mikoa.
Fedha za nje zinajumuisha:
(i) Shilingi 121,200.9 milioni za miradi ya
maendeleo ya Barabara Kuu na za Mikoa.
(ii) Shilingi 11,291.047 milioni za matengenezo ya
Barabara Kuu na za Mikoa.
85.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
Viambatisho
Kiambatisho 1
Kiambatisho 3
Kiambatisho 4
Kiambatisho 5
Kiambatisho 7, 7A na 7B, 7C na 7D, 7E, 7F na 7G, 7H, 7I, 7J, 7K, 7L, 7M, 7N
Kiambatisho 8