.

Dira Jukumu

Dira ya Wizara hii ni kufikia maelewano baina ya waajiri na waajiriwa, kuwa na mazingira ya kazi yanayozingatia afya na usalama wa wafanyakazi na watu wengine,  kuweka mazingira ya kuwezesha matumizi ya nguvu kazi, na kujenga jamii ya vijana wenye kuwajibika

Jukumu la Wizara hii ni kuinua viwango vya kazi, ajira, ustawi wa jamii na maendeleo ya vijana pamoja na michezo.

 

Kazi za Wizara

  •  Kuratibu sera ya kazi, Sera ya Taifa ya Ajira, Vyama vya Wafanyakazi, Mipango ya maendeleo ya nguvukazi, Vyama vya  Kimataifa vya Wakanyakazi, Kuratibu na kusaidia Sekta isiyo rasmi, maendeleo ya vijana,  ajira na miradi ya kujitegemea ya vijana,  Mafunzo ya kiufundi, Vyama vya Vijana, Sera ya Ustawi wa jamii,  kuwaandaa na kuwarudisha makwao ombaomba, Sera juu ya maendeleo  ya michezo na utekelezaji wake.

  • Kuendeleza nguvukazi chini ya Wizara 

  • Kusimamia shughuli za Idara za Serikali, Mashirika ya Umma na Miradi iliyo chini ya Wizara 

  • Kuhakikisha maendeleo ya michezo yote katika ngazi za Kitaifa na Kimataifa.

Taasisi na Mashirika

Mfuko wa Huduma za Jamii (NSSF)
 

Mfuko wa Huduma za Jamii (NSSF) ulianzishwa chini ya Sheria ya Bunge Na. 28 ya mwaka 1997 ambayo imeanza kutumika kuanzia Tarehe 1 Julai mwaka 1998.

 

Mfuko huu unahudumia sekta yote binafsi nchini, waliojiajiri na kila mtu ambaye hana mpango mwingine wa mafao.

 

Kwa mujibu wa Sheria iliyoanzisha mfuko huu, mfuko huu unatoa mafao ya aina mbili; mafao ya muda mfupi na ya muda mrefu. Mafao ya mudamfupi ni pamoja na msaada wa mazishi, uzazi, kuumia kazini na huduma za matibabu. Mafao ya muda mrefu ni mafao ya uzee, kutojiweza kutokana na maradhi, malipo kwa wafiwa na malipo maalum yanayotolewa kwamkupuo.  Wakati mafao yote ya muda mrefu yanatolewa na Mfuko hivi sasa, mafao ya muda mfupi yanayotolewa ni misaada ya maziko na uzazi tu. Hata hivyo matayarisho yapo katika hatua za mwisho kwa ajili  ya kutoa mafao ya kuumia kazini na huduma za afya.

 

Mamlaka ya Vyuo vya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA)

 

Sheria mpya ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi ilipitishwa bungeni mwaka 1994. Chini ya sheria hii mpya, taratibu za kutoa mafunzo ya ufundi stadi zimeimarishwa kwa kuanzishwa Mamlaka ya Vyuo vya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) ambayo kazi yake ni kusimamia maendeleo ya mafunzo ya ufundi stadi nchini.  Mamlaka hii inaongozwa na bodi ambayo ina wawakilishi kutoka serikalini, waajiri, vyama vya wafanyakazi na taasisi zisizo za kiserikali.

 

Taasisi ya Uongezaji Tija (NIP)

 

Taasisi hii imeanzishwa ili kuinua huduma za ushauri, na kusimamia mafunzo kwa nia ya kuongeza tija. Taasisi hii imeanzishwa chini ya Sheria ya Mashirika ya Umma ya mwaka 1969 na Tangazo la Serikali Na 124 la tarehe 10 Mei, 1974.

 

Hivi karibuni, Taasisi hii imeanza kuzisaidia sekta binafsio hasa zile zinazoendeshwa na watu wenye kiwango kidogo cha elimu kama vikundi vya akina MAMA LISHE na wafanyakazi na wamiliki wa migahawa midogo midogo na kantini.

 

Taasisi ya Taifa ya Mafunzo ya Ustawi wa Jamii

 

Taasisi hii imeanzishwa kwa ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Uholanzi kupitia Shirika la Maendeleo la nchi hiyo (NVIB). Taasisi hii imeanzishwa chini ya sheria ya Bunge Na. 26 ya mwaka 1873. 

Chuo kinaendesha mafunzo na kozi za aina mbalimbali kama ifuatavyo;

  • Stashahada ya Juu ya Ustawi wa Jamii

  • Stashahada ya Juu ya Usimamizi Kazini

  • Cheti cha Ustawi wa Jamii

  • Cheti cha Usimamizi Kazini