MAENDELEO YA UCHUMI JUMLA | UENDELEZAJI WA SEKTA BINAFSI | SUALA MAALUMU KATIKA MAENDELEO |
MAENDELEO KATIKA SEKTA MBALIMBALI

               
MAENDELEO YA UCHUMI JUMLA

Hali ya Uchumi wa Taifa
Hali ya Uchumi na Ushirikiano wa Kimataifa
Sekta ya Nje
Fedha za Serikali
Fedha na Taasisi za Fedha
Rasilimali Watu

     
FEDHA ZA SERIKALI
MAPATO

72. Sera za bajeti ya mwaka 2003/04 zililenga kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na Mkakati wa Kupunguza Umaskini na kuchochea maendeleo ya nchi kwa ujumla. Kwa kuzingatia sera hizo, bajeti ya Serikali ililenga kukusanya mapato ya ndani ya sh. 1,393,026 milioni, sawa na asilimia 13.3 ya Pato la Taifa, ikilinganishwa na asilimia 12.3 mwaka 2002/03. Mapato yatokanayo na kodi yalikadiriwa kufikia jumla ya sh. 1,264,161 milioni na yale yasiyo ya kodi sh. 128,865 milioni. Misaada na mikopo kutoka nje ikijumuisha mapato yanayotokana na msamaha wa deni la nje kwa utaratibu wa HIPC, ilikadiriwa kufikia jumla ya sh. 1,014,911 milioni.

Mapato ya Ndani
73. Mapato halisi ya ndani kwa kipindi cha Julai – Desemba 2003 yalifikia sh. 713,511 milioni, ikilinganishwa na makisio ya sh. 699,354 milioni, na hivyo kuzidi makisio ya kipindi hicho kwa asilimia 2. Kiwango hiki cha makusanyo ni sawa na asilimia 51.2 ya makisio ya mapato yote ya ndani katika mwaka 2003/04. Kati ya mapato hayo, sh. 653,296 milioni zilikuwa ni mapato yaliyotokana na kodi, ikiwa ni zaidi ya makisio ya sh. 634,838 milioni kwa asilimia 3, na sh. 60,216 milioni zilitokana na mapato yasiyo ya kodi, sawa na asilimia 6.6 chini ya makisio ya sh. 64,516 milioni.

74. Katika kipindi cha Julai – Desemba 2003, mwenendo wa mapato ya ndani ulikuwa wa kuridhisha kutokana na kuongezeka kwa ufanisi katika ukusanyaji wa kodi, hususan kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa bidhaa ya petroli inayoagizwa kutoka nje ya nchi na kodi ya mapato. Pia, makusanyo ya kodi katika kipindi hicho nayo yalikuwa ya kuridhisha kutokana na mabadiliko ya mfumo na usimamizi wa kodi yaliyotokana na kuboreshwa kwa mazingira ya ulipaji wa kodi kama ilivyoainishwa katika Mpango wa mwaka 2003 – 2008 wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA). Aidha, makusanyo ya kodi za ushuru wa forodha na bidhaa zinazozalishwa nchini yaliongezeka katika kipindi cha Julai – Desemba 2003 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliotangulia kutokana na ongezeko kubwa la uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi katika kipindi hicho. Makusanyo ya mapato yasiyotokana na kodi hayakuwa ya kuridhisha katika kipindi hicho kutokana na kupungua kwa shughuli zinazochangia mapato hayo kwa baadhi ya wizara, idara za serikali na mikoa.

75. Hadi kufikia mwisho wa Machi 2004, mapato ya ndani kwa mwaka 2003/04 yalifikia sh. 1,089,260 milioni, sawa na asilimia 78.2 ya makisio ya mwaka. Mapato hayo ni zaidi ya makisio ya sh. 1,050,866 milioni kwa kipindi hicho kwa asilimia 3.7. Kutokana na mwenendo huo, lengo la mapato ya ndani kwa mwaka 2003/04 linatarajiwa kupitwa na kufikia sh. 1,400,605 milioni ifikapo Juni 2004, sawa na asilimia 0.54 juu ya makisio ya mwaka. Kiwango hicho cha makusanyo kitakuwa sawa na asilimia 14 ya Pato la Taifa kwa makadirio ya mwaka 2003/04, ikiwa ni zaidi ya lengo la kukusanya asilimia 13.3 ya Pato la Taifa katika kipindi hicho.

Misaada na Mikopo ya Nje
76. Katika kipindi cha Julai – Desemba 2003 cha mwaka 2003/04, upatikanaji wa fedha za misaada na mikopo kutoka nje ikijumuisha misamaha ya deni la nje kwa utaratibu wa HIPC ulifikia sh. 605,616 milioni. Kati ya fedha hizo, sh. 378,818 milioni, zilitokana na ruzuku na sh. 226,798 milioni zilitokana na mikopo kutoka nje katika kipindi hicho. Jumla ya mapato yaliyotokana na misamaha ya madeni kwa utaratibu wa HIPC yalifikia jumla ya sh. 30,418 milioni. Kwa upande wa misaada na mikopo kwa ajili ya bajeti ya maendeleo ilifikia jumla ya sh. 263,661 milioni katika kipindi hicho. Upatikanaji wa fedha zilizoahidiwa na wahisani ulikuwa wa kuridhisha kwani uliweza kuzidi lengo lililowekwa kwa asilimia 8.1 katika kipindi hicho.

77. Hadi mwezi Machi 2004 jumla ya fedha kutoka nje ya nchi ikijumuisha misamaha ya madeni yaliyo katika mpango wa HIPC zilifikia sh. 964,338 milioni. Kati ya fedha hizo, sh. 612,697 milioni zilitokana na ruzuku na sh. 351,641 milioni zilikuwa ni mikopo kwa ajili ya programu na miradi. Fedha zilizotokana na misamaha katika utaratibu wa HIPC zilifikia sh. 56,687 milioni. Kutokana na mwenendo huo, mapato ya misaada na mikopo ikijumuisha misamaha ya madeni kwa utaratibu wa HIPC, yanatarajiwa kufikia sh. 1,076,748 milioni, ifikapo Juni 2004.

Mikopo ya Ndani na Mapato ya Ubinafsishaji
78. Katika kipindi cha Julai – Desemba 2003, serikali ilikadiria kutumia sh. 137,634 katika kulipa madeni yake katika mabenki ya ndani na taasisi za fedha zisizo mabenki Hata hivyo, katika kipindi hicho, serikali ililipa madeni hayo kwa kiasi cha sh. 246,264 milioni. Aidha, katika kipindi hicho serikali ilipata jumla ya sh. 6,067 milioni kutokana na ubinafishaji wa mashirika yake. Ifikapo Juni 2004 serikali inatarajia kupata jumla ya sh. 38,357 milioni kutokana na mikopo ya mabenki na taasisi zisizo za benki na ubinafsishaji.

MATUMIZI

79. Sera za bajeti kwa upande wa matumizi ya fedha za serikali kwa mwaka 2003/04 zililenga katika kuendeleza na kuimarisha usimamizi mzuri wa matumizi ya fedha za serikali ili kufikia malengo yaliyowekwa katika kukuza uchumi na kuondoa umaskini. Kwa kuzingatia sera hizo, serikali ilikadiria kutumia jumla ya sh. 2,418,337 milioni, sawa na asilimia 24.2 ya Pato la Taifa. Kati ya fedha hizo, matumizi ya kawaida yalikadiriwa kuwa sh. 1,610,897 milioni na matumizi ya maendeleo kuwa sh. 807,440 milioni. Mgawanyo wa matumizi ulikuwa kama ifuatavyo : sh. 464,061 milioni, sawa na asilimia 28.8 ya matumizi ya kawaida, zilitengwa kwa ajili ya kulipia mishahara ya watumishi wa umma; sh. 334,497 milioni, sawa na asilimia 20.8 ya matumizi ya kawaida zilitengwa kwa ajili ya sekta zilizopewa kipaumbele katika Mkakati wa Kupunguza Umaskini na matumizi mengineyo yalitengewa jumla ya sh. 424,141 milioni sawa na asilimia 26.3 ya matumizi yote ya kawaida.

80. Matumizi yote ya Serikali katika nusu ya kwanza ya mwaka 2003/04 (Julai-Desemba 2003) yalifikia jumla ya sh. 1,044,510 milioni, sawa na asilimia 93.1 ya makadirio ya sh. 1,121,774 milioni katika kipindi hicho. Kiwango hiki cha matumizi ni sawa na asilimia 43.2 ya bajeti yote ya matumizi katika mwaka 2003/04. Matumizi ya kawaida katika kipindi hicho yalifikia sh. 768,593 milioni, sawa na asilimia 96.5 ya makadirio ya sh. 796,733 milioni kwa kipindi hicho na matumizi ya maendeleo yalifikia sh. 275,916 milioni, sawa na asilimia 84.9 ya makadirio ya sh. 325,041 milioni. Katika kipindi hicho, Serikali ilitumia sh. 229,781 milioni kulipa mishahara ya watumishi wa umma na sh. 159,390 milioni zilitumika kwa ajili ya sekta zilizopewa kipaumbele katika Mkakati wa Kupunguza Umaskini. Kwa ujumla, kiwango cha matumizi ya bajeti ya kawaida kilikuwa chini ya lengo katika kipindi hicho kutokana na kushindwa au kuchelewa kufanya ununuzi kutokana na kutozoeleka vya kutosha kwa sheria mpya ya manunuzi ya mwaka 2001. Hata hivyo, ikilinganishwa na mwaka 2002/03, matumizi ya bajeti ya kawaida yamekuwa ya kuridhisha kutokana na kuanza kueleweka kwa sheria mpya ya ununuzi ya mwaka 2001.

81. Matumizi ya maendeleo, katika kipindi cha Julai – Desemba 2003 yalifikia sh. 275,916 milioni, sawa na asilimia 85 ya makadirio kwa kipindi hicho. Kutofikiwa kwa lengo la matumizi ya maendeleo, kwa kiwango kikubwa kumetokana na ucheleweshaji wa taarifa za matumizi, hususan kwa miradi inayotekelezwa kwa fedha za wafadhili wa nje.

82. Matumizi yote ya serikali hadi kufikia mwisho wa Machi 2004 katika mwaka 2003/04 yalifikia sh. 1,875,690 milioni, sawa na asilimia 77.6 ya bajeti ya mwaka. Kutokana na mwenendo huo, ifikapo Juni 2004, matumizi yote ya serikali yanatarajiwa kufikia sh. 2,559,090 milioni, sawa na asilimia 105.8 ya makadirio ya bajeti ya mwaka.

83. Katika mwaka 2003/04 serikali iliendelea kuimarisha usimamizi na nidhamu katika matumizi ya serikali kwa madhumuni ya kuongeza ufanisi katika uwajibikaji. Katika kupanga matumizi ya fedha kwa mwaka 2003/04, mgao mkubwa wa fedha za serikali ulielekezwa kwenye sekta zilizopewa kipaumbele katika Mkakati wa Kupunguza Umaskini (afya, elimu, barabara vijijini, maji, kilimo na utawala bora). Aidha, kutokana na upungufu wa chakula uliojitokeza, serikali ilitenga fungu la fedha kwa ajili ya ununuzi wa chakula kwa maeneo ya nchi yaliyohitaji chakula cha msaada.

84. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya afya katika mwaka 2003/04 ilikuwa asilimia 7 kama ilivyokuwa katika mwaka 2002/03. Hata hivyo, kiwango cha fedha za bajeti kilichoelekezwa sekta ya afya kiliongezeka kutoka sh. 148,437 milioni mwaka 2002/03 hadi sh. 182,704 milioni mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa sekta ya elimu ilipungua kutoka asilimia 19.2 mwaka 2002/03 hadi asilimia 17.3 mwaka 2003/04, ingawa fedha zilizoelekezwa sekta hiyo ziliongezeka kutoka sh. 409,362 milioni mwaka 2002/03 hadi sh.446,247 milioni mwaka 2003/04. Katika sekta ya kilimo, misitu, uvuvi na uwindaji; sehemu ya bajeti iliongezeka kutoka asilimia 3 mwaka 2002/03 hadi asilimia 3.5 mwaka 2003/04. Bajeti ya utafiti wa kilimo ilikuwa asilimia 2.8 ya bajeti yote iliyoelekezwa katika sekta hiyo. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya madini, viwanda na ujenzi iliongezeka kutoka asilimia 4 mwaka 2002/03 hadi aslimia 6 mwaka 2003/04, kutokana na kuongezeka kwa miradi ya ujenzi nchini. Fungu la bajeti lililoelekezwa kwenye miradi ya maendeleo ya ujenzi pekee lilikuwa asilimia 83.5 ya bajeti iliyotengwa katika sekta hiyo. Kwa upande wa usafirishaji na mawasiliano, sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta hiyo iliongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2002/03 hadi asilimia 8.3 mwaka 2003/04.

85. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta za huduma za kawaida ilipungua kutoka asilimia 19.2 mwaka 2002/03 hadi asilimia 17.7 mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya usalama iliongezeka kutoka asilimia 4.4 mwaka 2002/03 hadi asilimia 4.5 mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye matumizi mengineyo ilipungua kutoka asilimia 20.4 mwaka 2002/03 hadi asilimia 18 mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya huduma za uchumi (biashara, utalii, huduma za kazi nk.) iliongezeka kutoka asilimia 3.2 mwaka 2002/03 hadi aslimia 4.4 mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa katika sekta ya usalama wa jamii, ustawi na huduma za jamii ilipungua kutoka asilimia 1.7 mwaka 200/03 hadi asilimia 1.6 mwaka 2003/04. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya ulinzi na huduma ilishuka hadi asilimia 6 mwaka 2003/04 kutoka asilimia 6.8 mwaka 2002/03. Sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye sekta ya mafuta na umeme ilipungua kutoka asilimia 0.15 mwaka 2002/03 hadi asilima 0.14 mwaka 2003/04. Na sehemu ya bajeti iliyoelekezwa kwenye huduma nyingine za jamii ilikuwa sawa na kiwango cha mwaka 2002/03 cha asilimia 0.1.

Deni la Taifa
86. Hadi kufikia mwisho wa Desemba 2003, deni la taifa (ikijumuisha la nje na ndani) lilikuwa dola za Marekani 8,755.0 milioni, sawa na ongezeko la asilimia 5.8 ikilinganishwa na dola 8,277 milioni kipindi cha kuishia Desemba 2002. Kati ya deni hilo, dola 7890.7 milioni zilikuwa deni la nje, sawa na asilimia 90.1 ya deni lote, na dola 864.3 milioni zilikuwa deni la ndani, sawa na asilimia 9.9 ya deni lote.

87. Sheria mpya ya kusimamia mikopo na misaada ya mwaka 2003, iliyorekebisha sheria iliyokuwepo ya mwaka 1974 ilianza kutumika mwezi wa Julai, 2003. Makusudi ya sheria hiyo ni kuimarisha usimamiaji wa mikopo na misaada kwa taifa. Pamoja na sheria hiyo, hatua mbalimbali zimechukuliwa kuimarisha na kukijengea uwezo kitengo cha madeni kilichopo Wizara ya Fedha kwa kukiongezea wataalam na vifaa. Aidha, serikali iliendelea na juhudi zake za kuhamasisha na kushawishi nchi wahisani kuipunguzia na/au kuifutia Tanzania madeni chini ya taratibu za HIPC.

Deni la Nje
88. Kati ya deni la nje la dola 7,890.7 milioni, kiasi cha dola 1,159.9 ni riba na dola 6,730.8 milioni ni kiasi cha mikopo halisi iliyotolewa (disbursed outstanding debt). Kati ya fedha za mikopo iliyotolewa, kiasi cha dola 4,520 milioni (asilimia 67.2) zilitoka kwenye mashirika ya kimataifa ya fedha, kiasi cha dola 1,587.5 milioni (asilimia 23.6) zilitoka kwa nchi wahisani, dola 390.4 milioni (asilimia 5.8) zilitokana na mikopo ya kibiashara. Mikopo iliyotokana na vyanzo vingine ilikuwa na thamani ya dola 231 milioni (asilimia 3.4)

89. Deni la nchi wahisani lilipungua kutokana na misamaha ya madeni, wakati ambapo deni la mashirika ya kimataifa ya fedha liliongezeka kutokana na serikali kupokea mikopo nafuu mipya inayotolewa na mashirika hayo kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

90. Katika jumla ya mikopo halisi iliyotolewa kufikia Desemba 2003, serikali ilikuwa imekopa kiasi cha dola 6,089.9 milioni, sawa na asilimia 90.5, ambapo mashirika ya umma yalikuwa yamekopa dola 154 milioni, sawa na asilimia 2.3, na sekta binafsi ilikopa jumla ya dola 487 milioni, ambazo ni sawa na asilimia 7.2 ya jumla ya mikopo yote ya nje.

91. Mgawanyo wa mikopo iliyopokelewa toka nje (bila riba) kisekta hadi kufikia Desemba 2003, ni kama ifuatavyo: - kusaidia mizania ya malipo na nchi za nje, dola 1,219.1 sawa na asilimia 18.1; mawasiliano na usafirishaji dola 1,113.6 sawa na asilimia 16.5; kilimo dola 978.0 sawa na asilimia 14.5; madini dola 931.0 sawa na asilimia 13.8; viwanda dola 360.5 sawa na asilimia 5.4; elimu dola 326.9 sawa na asilimia 4.9; sekta ya fedha dola 90.3 sawa na asilimia 1.3; utalii dola 91.1 sawa na asilimia 1.4 na sekta nyinginezo dola 1620.2 sawa na asilimia 24.1.

Mpango wa Kuzipunguzia Madeni Nchi Maskini zenye Madeni Makubwa (HIPC)
92. Serikali imeendelea kupata misamaha ya deni la nje chini ya utaratibu wa HIPC. Hadi kufikia mwaka ulioishia Desemba 2003, serikali ilikuwa imepata misamaha ya deni la nje la kiasi cha dola 26.6 milioni, kutoka mashirika ya kimataifa ya fedha, kwa viwango vinavyoonyeshwa katika mabano kama ifuatavyo : Benki ya Dunia (dola 21.9 milioni), Shirika la Fedha la Kimataifa – IMF (dola 4.4 milioni), Benki ya Maendeleo ya Afrika - ADB (dola 0.2 milioni), na nchi wahisani ambazo ni wanachama wa Paris Club isipokuwa Japan na Brazil, ziliifutia Tanzania madeni yenye thamani ya dola 749.7 milioni. Aidha, katika kipindi hicho hicho, msamaha wa madeni uliotolewa na nchi zisizo wanachama wa Paris Club ulifikia dola 52.8 milioni. Nchi zilizotoa misamaha hiyo ni China, dola 37.7 milioni na Bulgaria dola 15.1 milioni. Fedha zilizotokana na msamaha wa madeni zilitumika kwenye baadhi ya sekta zinazopewa kipaumbele katika Mkakati wa Kupunguza Umaskini, kama vile elimu, maji, afya, kilimo, barabara za vijijini, na utawala bora.

Deni la Ndani
93. Hadi mwisho wa Desemba 2003, deni la ndani lilifikia dola 864.3 milioni, sawa na sh. 919.3 bilioni, ikiwa ni pungufu kwa asilimia 3.1 ikilinganishwa na deni la dola 891.6 milioni, sawa na sh. 870.5 bilioni katika kipindi kilichoishia Desemba 2002. Kati ya deni hilo, asilimia 98.2 lilitokana na dhamana za serikali, ikijumuisha hawala za hazina (Treasury Bills) za muda wa siku 35, 91, 182 na 364, hatifungani (Treasury Bonds) za muda wa miaka 2, 5, 7, na 10 na dhamana nyingine. Kiasi cha deni kilichosalia cha asilimia 1.8, kilitokana na madeni ya nyumba za kulala za NSSF zilizokodishwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

94. Mabenki ya biashara nchini yaliendelea kuwa wakopeshaji wakubwa wa serikali, kwa kuikopesha kiasi cha dola 295.4 milioni, sawa na sh. 314,186.3 milioni, ikiwa ni asilimia 34.2 ya deni la serikali la ndani. Benki Kuu ilikuwa inaidai serikali kiasi cha dola 224.2 milioni, sawa na sh. 238,478.5 milioni, au asilimia 25.9 ya deni lote la ndani. Mikopo kutoka mashirika ya umma ilichangia kiasi cha dola 2.7 milioni, sawa na sh. 2,862.5 milioni au asilimia 0.3 ya deni lote na dola 33.4 milioni, sawa na sh. 35,543.3 milioni au asilimia 3.9 ya deni lote lilitokana na mikopo kutoka sekta binafsi.

Jedwali Na. 25(MWENENDO WA MAPATO NA MATUMIZI YA SERIKALI)MWENENDO WA MAPATO NA MATUMIZI YA SERIKALIl

Jedwali Na. 26(MGAWANYO WA HUDUMA ZA SERIKALI )

 
Back Top