MAENDELEO YA UCHUMI JUMLA | UENDELEZAJI WA SEKTA BINAFSI | SUALA MAALUMU KATIKA MAENDELEO |
MAENDELEO KATIKA SEKTA MBALIMBALI

MAENDELEO KATIKA SEKTA MBALIMBALI
 

Kilimo
Maliasili na Utalii
Madini
Viwanda na Biashara
Ujenzi wa Maendeleo ya Ardhi
Mawasiliano na Uchukuzi
Nishati
Maji
Elimu na Mafunzo
Afya
Maendeleo ya Jamii

         
AFYA
 
Hali ya Magonjwa kwa Jumla

274. Kumekuwa na ongezeko la wagonjwa wa kifua kikuu kutoka wagonjwa 63,048 mwaka 2002 hadi wagonjwa 63,211 mwaka 2003, sawa na ongezeko la chini ya asilimia 1. Upande wa ukoma wagonjwa wamepungua kwa asilimia 17.6 kutoka wagonjwa 7,007 mwaka 2002 hadi wagonjwa 5,771 mwaka 2003. Ugonjwa wa malaria unaendelea kuwa tatizo kubwa na unahitaji jitihada za ziada ili kuukabili kikamilifu. Msisitizo umekuwa katika utoaji wa tiba sahihi kwa wagonjwa wa malaria kwa kutumia dawa ya SP (sulfadoxine/pyrimethamine) na kufanya utafiti wa dawa nyingine za kuutibu. Aidha, mpango wa kuongeza matumizi ya vyandarua kwa bei nafuu kwa mama wajawazito na watoto walio chini ya mwaka mmoja umekamilika. Utekelezaji wa majaribio wa mpango huo unaendelea katika wilaya ya Kilosa na Kibaha.

UKIMWI
275. Ugonjwa wa UKIMWI bado unaendelea kuwa tatizo kubwa hapa nchini na katika nchi jirani. Hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2002 watu takribani milioni 2 walikuwa wakiishi na virusi vya UKIMWI. Kati yao, watu 400,000 – 500,000 wapo katika hatua ya ugonjwa ya kuhitaji madawa ya kupunguza makali ya UKIMWI. Tatizo hili la UKIMWI linaongezea mzigo mkubwa kwa huduma za afya nchini kwa vile asilimia 40-50 ya vitanda vya hospitalini vimekaliwa na wagonjwa hao. Mwaka 2002, wagonjwa wa UKIMWI wapatao 12,675 walipata huduma mbalimbali kwenye vituo vya huduma za afya nchini kote.

Elimu ya Afya kwa Wananchi na Afya ya Mazingira
276. Elimu ya afya imeendelea kutolewa kwa wananchi kwa njia ya radio, magazeti na televisheni. Aidha, tafiti zimefanyika juu ya athari ziwapatazo wafanyakazi viwandani, mashambani na katika sekta za ujenzi na kubaini kuwa athari za afya na magonjwa mengi huwapata wafanyakazi ambao hutumia kemikali. Kwa hiyo, miongozo ya utekelezaji wa huduma za afya ya mazingira iliandaliwa ili kuleta changamoto kwa wadau wa afya ya mazingira katika utoaji huduma.

Afya ya Mama na Mtoto
277. Jitihada za kupunguza vifo vya watoto, hasa wenye umri wa chini ya miaka mitano na mama wajawazito ziliendelea. Huduma zilitolewa kwa wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano ikiwemo chanjo na uzazi wa mpango pamoja na kujifungua. Aidha, mafunzo yalitolewa kuhusu afya ya mama na mtoto kwa watoa huduma mbalimbali zikiwepo zile za matibabu ya tahadhari na kutoa kinga kwa wajawazito dhidi ya malaria, matibabu ya dharura kwa wazazi na mafunzo rejea kuhusu uzazi wa mpango ambapo kwenye vituo vya kutolea huduma vya serikali zilitolewa bila malipo. Mafunzo hayo yanalenga kuongeza stadi za matibabu ya magonjwa yale yanayosababisha zaidi vifo kwa watoto ambayo ni malaria, vichomi, kuharisha, surua, upungufu wa damu na utapiamlo. Kufikia mwaka 2003, wilaya 72 zinatekeleza mkakati huo na zaidi ya wahudumu 1,226 katika wilaya 46 walipatiwa mafunzo.

278. Viwango vya chanjo katika mwaka 2003 vilikuwa vya kuridhisha. Chanjo ya kifua kikuu ilifikia asilimia 88, polio asilimia 91, kifaduro, pepopunda na homa ya ini asilimia 89, na surua asilimia 89. Jumla ya majokofu mapya 1,003 yanayotumia gesi yalinunuliwa na kupelekwa mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Singida, Mbeya, Iringa na Ruvuma badala ya majokofu ya zamani yaliyokuwa yanatumia mafuta ya taa.

Chakula na Lishe
279. Taasisi ya Chakula na Lishe iliendelea kutoa ushauri wa kitaalam kwa wilaya na kushirikiana na taasisi mbalimbali nchini ili kuboresha afya na lishe ya jamii. Utafiti uliofanyika nchi nzima ulionyesha kwamba, tatizo la uvimbe wa tezi la shingo kwa sasa linaathiri asilimia 8 ya Watanzania. Aidha, utafiti huo pia uliangalia upatikanaji wa chumvi yenye madini joto katika ngazi ya kaya na kuonekana ya kuwa asilimia 83.8 ya kaya zinatumia chumvi yenye madini joto. Kiwango hiki kipo chini ya kigezo cha Shirika la Afya Duniani (WHO) ambacho ni asilimia 90.

UKIMWI na Lishe
280. Mafunzo na ushauri nasaha kuhusu unyonyeshaji na ulishaji watoto kwa wakati huu wa UKIMWI yalitolewa kwa wafanyakazi 39 wa Afya katika mikoa ya Arusha, Manyara na Iringa. Aidha, vijitabu, vipeperushi na mabango vinavyoelezea njia mbadala za ulishaji watoto vilichapishwa na kusambazwa. Vile vile, kutokana na tafiti mbalimbali kuonyesha uhusiano mkubwa kati ya lishe na uambukizo wa virusi vya UKIMWI, mwongozo wa kitaifa wa lishe kwa watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI ulitayarishwa.

Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF)
281. Utaratibu wa kuelimisha na kuhamasisha halmashauri za wilaya kuanzisha CHF unaendelea. Wilaya 88 zimeelimishwa na kuhamasishwa kuunda bodi za afya za halmashauri na kamati mbalimbali za afya kama vyombo vya usimamizi wa huduma za afya wilayani. Halmashauri 23 zinatekeleza utaratibu huu wa CHF na nyingine 17 zinakamilisha taratibu ili waanze utekelezaji. Faida zilizopatikana kwa kuanzisha mfuko huu ni pamoja na upatikanaji wa dawa, ukarabati wa majengo na vifaa vya tiba, ulinzi wa dawa toka kwa wananchi wenyewe, na uimarishaji wa ushirikishwaji wa wananchi kuhusu afya zao.

Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF)
282. Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya uko katika mwaka wake wa tatu wa utekelezaji. Idadi ya wanachama wa mfuko ilifikia 242,508 mwaka 2003 ikilinganishwa na 167,989 mwaka 2002, sawa na ongezeko la asilimia 44.4. Jumla ya wananchama 210,152 kati ya 242,508 tayari walikwisha kamilisha taratibu za ujazaji wa fomu ikiwa ni asilimia 86.7 ya wanachama wote na hivyo kustahili kupatiwa vitambulisho. Aidha, vituo 3,551 vya matibabu vilisajiliwa na Mfuko kuhudumia wanachama, ikiwa ni ongezeko la asilimia 4 ikilinganishwa na vituo 3,415 vilivyokuwepo mwaka 2002. Vituo hivi vinajumuisha vituo 3,060 vya serikali, na 491 vya madhehebu ya dini. Jumla ya maduka ya dawa 33 yamekwisha sajiliwa kutoa huduma za dawa katika mikoa 20 ikilinganishwa na maduka mawili 2 yaliyosajiliwa katika mwaka wa fedha wa 2002/03.

Vituo vya Kutolea Tiba
283. Katika harakati za kuboresha utoaji wa huduma za afya, kumekuwa na mtandao mzuri wa vituo vya kutolea huduma nchi nzima. Katika mwaka 2003, kumekuwa na ongezeko la zahanati 233 na vituo vya afya 16 vilivyojengwa na halmashauri na nguvu za wananchi. Pia, masanduku ya dawa yalipelekwa kwenye vituo hivyo. Jumla ya vituo 87 vilivyo chini ya mashirika ya kujitolea na watu binafsi vimesajiliwa katika mwaka 2003. Aidha, serikali imeongeza ruzuku ya vitanda kwa hospitali za mashirika ya dini kutoka sh. 7,500 mpaka sh.15,000 kwa kitanda kwa mwaka.

Mafunzo ya Afya
284. Katika jitihada za kuongeza ufanisi katika fani mbalimbali za afya, Wizara imepeleka mafunzoni Madaktari Wasaidizi 154, Waganga 694, Wauguzi daraja “A” 454, daraja “B” 429, Wauguzi wakunga 184, Mabwana Afya 11 pamoja na Mabwana Afya Wasaidizi 62.

Jedwali Na.84(VYOMBO VYA AFYA NCHINI)

Jedwali Na.85(WALIOFAULU MAFUNZO)

Jedwali Na.86(MATUMIZI YA VYOMBO VYA AFYA)

Jedwali Na.87(IDADI YA WATAALAM WA AFYA )

Jedwali Na.87A(IDADI YA VITANDA KATIKA HOSPITALI ZOTE NCHINI - 2002)

 
Back Top