HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA
MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA BENJAMIN WILLIAM MKAPA, KWA WANANCHI,
31 JULAI 2004
Ndugu Wananchi,
Juzi nimerejea nyumbani kutoka
Gaborone, Jamhuri ya Botswana, ambapo nilikwenda kutembelea Makao Makuu ya
Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kukagua kazi za Jumuiya, na
kuzungumza na viongozi na wafanyakazi kwa wadhifa wangu wa Mwenyekiti wa
SADC. Nilipata pia fursa ya kufanya
mazungumzo na Rais wa Botswana, Mhe. Festus Mogae na viongozi wengine wa nchi
hiyo.
Mojawapo ya mambo niliyoyafuatilia
ni mipango ya SADC kuhusu sekta ya afya, hususan UKIMWI, Kifua Kikuu na
Malaria, magonjwa ambayo yanaleta matatizo makubwa ya kijamii, kiuchumi na
kimaendeleo katika nchi zetu.
Leo napenda nizungumze nanyi kuhusu
ugonjwa wa malaria. Nafanya hivyo kwa
sababu tumezoea mno kuishi na malaria kiasi kwamba hatuoni au kuzingatia vya
kutosha hatari kubwa sana inayoletwa na malaria. Tunayo kila sababu kuongeza nguvu kwenye
kupambana na UKIMWI, lakini tunayo kila sababu pia kuongeza nguvu kwenye
kupambana na malaria. Ningependa takwimu
zifuatazo zinazoelezea hali ya malaria na athari zake kwenye nchi za SADC, na
pia kwetu Tanzania, zituzindue kuhusu hatari iletwayo na malaria.
Ndugu
Wananchi,
Takwimu zilizopo zinaonyesha kuwa
kwa nchi wanachama wa SADC, kwa ujumla wao, malaria ni chanzo cha pili kwa kuua
watu wengi, baada ya UKIMWI. Watu kati
ya 300,000 – 400,000 hufa kila mwaka.
Asilimia 30 ya wagonjwa wa nje katika hospitali, vituo vya afya na
zahanati, wanasumbuliwa na malaria. Asilimia
40 ya wanaolazwa wanaugua malaria. Hawa
ni watu ambao hawafanyi kazi za familia na za kujenga nchi kwa vile
wanaumwa. Hiyo ni hasara kubwa kwa
familia zao na kwa mataifa yao. Fikiria
pia gharama kubwa kwao wenyewe, na kwa Serikali zao, ya kuwatibu.
Hali ni hiyo hiyo hapa kwetu
Tanzania; tena sisi malaria ndiyo huua watu wengi zaidi kuliko UKIMWI. Tanzania tunaongoza kwa vifo vya malaria katika nchi zote
za SADC. Lakini tunaogopa UKIMWI zaidi kwa vile ni ugonjwa mpya kuliko malaria,
ugonjwa ambao tumekuwa nao kwa karne na karne.
Tunaogopa UKIMWI kwa vile hauna tiba, na hatuogopi malaria kwa vile yana
tiba japo yanaua watu wengi kuliko UKIMWI. Na wengine wanahalalisha mazoea ya
malaria kwa kusema lazima ukiishi hapa uwe na kiasi fulani cha vimelea vya
malaria mwilini wakati wote. Ombi langu
ni kuwa tusiseme hivyo kwa maana ya kupuuzia hatari ya malaria; tuseme hivyo kwa
kujikumbusha wakati wote kuwa kama vile ambavyo vimelea vyake viko nasi wakati
wote, malaria inapaswa kuwa ajenda ya kudumu katika kaya zetu na jamii zetu.
Ndugu
Wananchi,
Hebu tafakarini takwimu
zifuatazo.
Kila mwaka Watanzania karibu milioni
18 wanaugua malaria. Maana yake ni kuwa karibu
kwa kila Watanzania wawili, mmoja anaugua malaria kila mwaka. Takwimu za mwaka
2002 zinaonyesha kuwa matukio ya malaria yaliyoripotiwa kwenye sehemu za huduma
za afya yalikuwa mara tano zaidi ya matukio ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Surua na
Ukoma kwa pamoja. Malaria huua wastani
wa Watanzania 100,000 kila mwaka, yaani sawa na kuua mtu mmoja katika kila
dakika 5. Na wote hao hawana sababu ya
kufa, maana malaria ni ugonjwa unaozuilika kwa gharama ndogo, na kwa kiasi
kikubwa unatibika ukiwahiwa. Lakini bado kwa kuzoea malaria, hatutaki kukubali ukweli
kuwa ugonjwa huu ni hatari kubwa kwa uhai, maendeleo na ustawi wa taifa letu,
na ni sababu mojawapo kubwa ya kutupunguzia sana maksi za maendeleo ya kijamii
tunapolinganishwa na nchi nyingine.
Kinachosikitisha zaidi ni kuwa wengi
wa wanaougua na kufa kwa malaria ni watoto wetu wadogo wenye umri wa chini ya miaka
5. Kitakwimu, tangu nimeanza kuzungumza
nanyi, dakika tano zilizopita, watoto zaidi ya 300 wameambukizwa malaria na
wanaweza kufa. Kila mwaka tunapoteza watoto 70,000 wanaokufa kwa malaria. Yaani, kwa kila vifo 10 kutokana na malaria,
7 ni vya watoto hao chini ya umri wa miaka 5.
Narudia. Malaria huathiri zaidi kina mama wajawazito
na watoto wadogo chini ya miaka 5. Kipindi kinachoongoza kwa maambukizo ya
malaria ni Oktoba-Desemba, na Februari-Aprili.
Kwa hiyo, kwa uchungu mkubwa, naomba kuanzia mwaka huu tukubaliane
kitaifa kuibua upya nia na moyo wa ushupavu wa kupambana na malaria ili kuokoa
watoto wetu tunaowapenda sana.
Ndugu
Wananchi,
Leo napenda nipendekeze kwenu hatua
zifuatazo ambazo mimi naziona ni muhimu sana katika kupambana na malaria.
·
Kwanza, kila mmoja wetu atambue na
kukubali kuwa malaria ni tatizo kubwa sana. Tusilipuuze wala kulifanyia mzaha.
·
Pili, kila mmoja wetu akubali yeye
mwenyewe kuwa askari katika mapambano dhidi ya malaria. Mzigo huu ni wetu sote, Serikali na kila
mwananchi.
·
Tatu, kila mmoja wetu ajiandae kwa
mapambano hayo kwa kujifunza mbinu zake, kuzielewa na kuzizingatia. Kila mtu, mkubwa kwa mdogo, ajue malaria
inavyoenea, inavyoweza kuzuiliwa, na inavyoweza kutibiwa.
·
Nne, wenye wajibu wa kuelimisha
jamii, kuanzia Wizara ya Afya, Asasi Zisizokuwa za Serikali, Halmashauri na
Serikali za Mitaa katika ngazi zote, na hata viongozi wa kijamii, wote waongeze
kasi na usahihi wa elimu ya afya kuhusu kuzuia na kutibu malaria.
·
Tano, tujenge ushirikiano na
ushirikishwaji miongoni mwa wadau wote, kwenye ngazi zote. Ugonjwa wa malaria utadhibitiwa vizuri zaidi
kila mwanajamii akishiriki. Haisaidii
sana, kwa mfano, kwa kaya moja kuharibu mazalio ya mbu, kama jirani zao nao
hawafanyi hivyo.
·
Sita, wanasiasa na viongozi wa
dini watumie majukwaa yao kuelimisha jamii na kuhimiza utekelezaji wa mikakati
ya kupambana na malaria, si UKIMWI peke yake.
·
Saba, watoto wadogo, chini ya
miaka 5, na akina mama wajawazito, wapewe kipaumbele cha pekee kwenye kuzuia na
kutibu malaria.
·
Nane, tusisahau kuwa kinga ni bora
na nafuu zaidi kuliko tiba. Serikali
imeondoa kodi kwenye vyandarua na dawa za kuzuia malaria. Tanzania imesifiwa
sana kwa hatua hizo. Lakini sifa hizo hazitakuwa na maana iwapo wananchi hawataongeza
sana matumizi ya vyandarua vilivyotiwa dawa.
·
Tisa, tiba ni muhimu na inabidi
iwe ya haraka kwa wagonjwa. Kila mtu, na
hasa kila mzazi, ajue vizuri dalili za malaria, na afanye nyumba yake kuwa kituo
cha kwanza cha kutibu malaria.
Upatikanaji wa dawa bora za malaria nyumbani unaweza kuokoa maisha ya
mtoto wako mpendwa. Maeneo yote
yanayotoa huduma za afya yaimarishe uwezo wa kupima haraka na kwa usahihi
vimelea vya malaria na kutibu. Wafanyao
kazi hapo wachukulie malaria, si kama kitu cha kawaida, bali kama jambo la
hatari kwa uhai wa mgonjwa husika, hasa mgonjwa mwenyewe akiwa mtoto
mdogo. Watoto wadogo wengi hufa katika
muda wa saa 48 tu iwapo hawatapata tiba haraka na sahihi tangu waonyeshe dalili
za kwanza za malaria.
·
Kumi, tiba asilia zilizokubalika
na wataalam kuwa zinatibu malaria zitumike, lakini kamwe tusidanganyike kuwa
degedege ni ugonjwa; degedege ni dalili za homa kali ya malaria. Ugonjwa ni malaria. Degedege ni dalili. Tusipoteze muda kupambana
na degedege ambayo ni dalili badala ya kumkimbiza mtoto hospitali ili ugonjwa
wenyewe, ambao ni malaria, utibiwe haraka.
Na kama lipo tatizo lingine litabainika hospitalini, si kwa mganga wa
kienyeji, au kwa kutafuta mchawi. Tupambane na malaria kisayansi, si ki-imani.
Ndugu
Wananchi,
Serikali yenu itajitahidi kuongeza
matumizi ya fedha kukabiliana na magonjwa kama haya ya malaria. Lakini yapo
mengi yanayoweza kufanywa katika ngazi ya familia ili kujikinga na malaria, na
kuyatibu. Tusingoje Serikali kila mara.
Uwezo wa Serikali nao ni mdogo. Ndio maana tunawashukuru wahisani wote –
Serikali za nje, mashirika ya kimataifa, na Asasi Zisizokuwa za Serikali,
wanaotusaidia katika kupambana na malaria.
Nawashukuru sana. Lakini kazi
bado ni kubwa. Utafiti wa chanjo ya
malaria lazima uendelee, tena kwa kasi kubwa zaidi maana huo utakuwa ufumbuzi
wa kudumu. Nafurahi kuwa Tanzania imo
mstari wa mbele katika utafiti huo, kwa kushirikiana na wengine. Nawapongeza
sana watafiti wetu ambao wanasifiwa sana duniani, na ninawatia shime.
Dawa mpya, zenye uwezo wa kudhibiti usugu wa vimelea vya malaria, nazo
lazima zitafitiwe, na zipatikane kwa bei nafuu.
Duniani, fedha nyingi zaidi
hutumika kutafiti magonjwa na dawa kwa magonjwa yanayosumbua wakubwa, yaani
matajiri. Magonjwa yanayoshamiri kwenye
nchi maskini, na ambayo yanazidisha umaskini wetu kama malaria, hayafanyiwi
utafiti wa kutosha, ati kwa vile hata dawa mpya zikipatikana hatuna uwezo wa
fedha wa kununua dawa hizo. Matokeo yake
fedha zinazotumika duniani kote kutafiti malaria kwa mwaka ni chini ya sh.100
bilioni, ambazo hazitoshi kununua hata ndege moja tu aina ya Jumbo Jet! Fedha
zinazohitajika kudhibiti malaria kwa mwaka ni sh.300 bilioni, ambazo ni sawa na
gharama ya kujenga barabara ya njia nne ya urefu wa kilometa 24 tu katika nchi
tajiri. Nusu ya vifo vyote barani Afrika
husababishwa na magonjwa yanayozuilika na kutibika kama ilivyo malaria. Barani Ulaya ni asilimia 2 tu ya vifo
husababishwa na magonjwa hayo.
Lazima sasa dunia iamue: ama sisi wote ni binadamu sawa, tunaohitaji
haki ya msingi ya kuishi na kuwa na afya bora, au sivyo.
Ndugu
Wananchi,
Wakati tukisubiri wakubwa watafakari
swali hilo, naomba sisi wenyewe tusisahau kamwe kuwa malaria inaua watoto wa
Kitanzania 70,000 wenye umri chini ya miaka 5 kila mwaka, au karibu watoto 200
kila siku. Lakini dawa ya chandarua ya sh.300/= tu inaweza kuokoa uhai wa mtoto
wako. Kumwahisha hospitali mtoto wako kunaweza
kuokoa maisha yake. Namwomba kila baba,
na kila mama, ahakikishe mtoto wake analala ndani ya chandarua kilichotiwa
dawa, na auguapo ahakikishe anamfikisha mara moja kwenye zahanati, kituo cha
afya au hospitali iliyo karibu.
Kuchelewa, hata kwa siku moja tu, kunaweza kugharimu uhai wa mwanao. Shirika la Kimataifa la UNICEF linakadiria
kuwa mambo haya mawili: kulala ndani ya
chandarua chenye dawa, na kuwahi hospitali, yanaweza kupunguza malaria kwa
asilimia 60, na kupunguza vifo vya watoto kwa asilimia 20! Na hizi si takwimu tu, ni maisha ya watoto
wetu wa Kitanzania ambayo tunaweza kuyaokoa.
Naomba tusisahau kamwe kuwa malaria
inazidisha umaskini wetu. Malaria
hufikia kilele chake wakati wa msimu wa mvua, ambao ni wakati wa kilimo. Hivyo malaria ni adui wa kilimo
tunachokitegemea kwa chakula na mapato kwenye ngazi ya kaya na taifa. Malaria hupunguza kipato cha wakulima kwa
karibu asilimia 40 kwa familia zenye wagonjwa wa malaria. Kwa wastani, familia ya Kitanzania inatumia
asilimia 20 ya mapato yake kutibu malaria. Kupambana na malaria ni kupambana na
umaskini. Tusilegeze kamba maana sasa
malaria inanyemelea hata maeneo ambayo zamani yalikuwa hayana ugonjwa huu.
Naomba tusisahau kuwa malaria
hupunguza kasi ya kukua kwa uchumi wa taifa na maendeleo yetu. Tanzania inapoteza sh.122 bilioni kila mwaka
kutokana na ugonjwa wa malaria. Hiyo ni
hasara kubwa kwa nchi maskini kama yetu.
Na inawezekana kupunguza sana hasara hiyo kama tukizingatia yote niliyoyaeleza
leo.
Namalizia kwa kukuombeni sana, Ndugu
Wananchi, kila mmoja, kila kaya, kila jamii, tutoe kipaumbele kipya kwenye vita
dhidi ya malaria. Watoto wetu wengi wanakufa
bila sababu; vifo vyao vinazuilika tukiamua hivyo. Taifa linapata hasara kubwa,
inayoepukika. Mapato ya familia
yanaathirika, na si lazima iwe hivyo.
Mwaka mpya wa fedha umeanza. Naomba Wizara ya Afya, wahisani mbalimbali,
asasi zisizokuwa za kiserikali, Halmashauri za Miji na Serikali zote za Mitaa,
na kila mwananchi, tushirikiane upya kuongeza kasi ya vita dhidi ya
malaria. Inawezekana. Okoa watoto wako. Jiokoe mwenyewe. Okoa uchumi wa familia na taifa. Timiza wajibu wako.
Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibariki Tanzania!
Ahsanteni kwa kunisikiliza.