HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE,
KATIKA HAFLA YA KUKABIDHI HATI IDHINI KWA VYUO VIKUU NA VYUO VIKUU VISHIRIKI, IKULU, DAR ES SALAAM TAREHE, 18 AGOSTI, 2010
Mheshimiwa Jumanne Maghembe, Waziri wa
Elimu na Mafunzo ya Ufundi;
Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi;
Katibu Mtendaji wa Tume;
Wakuu wa Vyuo Vikuu;
Viongozi Wenzangu;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana:
Nakushukuru
Mheshimiwa Waziri kwa kunishirikisha katika hafla hii
ya kukabidhi Hati Idhini za kuviidhinisha rasmi vyuo vikuu 09 kutoa elimu ya
juu hapa nchini. Hafla hii ni kielekezo dhahiri cha mafanikio tuliyoyapata katika
maendeleo ya elimu ya juu hapa nchini.
Napenda
kuchukua nafasi hii kuvipongeza vyuo vyote ambavyo leo
nimevikabidhi Hati Idhini za kuviruhusu rasmi kutoa elimu ya juu. Hongereni sana. Hii ni hatua kubwa
katika maendeleo ya vyuo vyenu na maendeleo ya elimu nchini. Ni jambo la fahari kubwa kwetu sote na ni jambo la kutia moyo kwamba dhamira yetu ya kuwawezesha
vijana wetu wengi kupata elimu ya juu ina mwelekeo mzuri. Wahenga waliosema elimu ni ufunguo wa maisha hawakukosea, kwani
sisi kama nchi mwelekeo wetu sasa ni kuhakikisha kuwa nchi yetu inakuwa na watu
wengi wenye elimu nzuri ili kufungua milango ya kuliletea taifa maendeleo ya
haraka. Dira ya Maendeleo inalenga nchi
yetu kutoka kuwa nchi maskini na kuwa nchi ya kipato
cha kati ifikapo mwaka wa 2025. Lakini
hatutafika huko kama hatutafanikiwa kuwapata
Watanzania wenye elimu nzuri tangu ya msingi mpaka elimu ya juu.
Mheshimiwa Waziri na Wageni
Waalikwa;
Mtakubaliana nami kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, tumepata mafanikio makubwa
katika kupanua elimu. Tumefanya upanuzi mkubwa wa
elimu katika ngazi zote, kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari, ufundi na
mpaka elimu ya juu. Vile vile, Elimu ya
Watu Wazima na Elimu Maalumu nazo zimepewa msukumo
mkubwa. Mafanikio haya makubwa yamepatikana kwa kushirikisha
wananchi katika kupanga na kutekeleza miradi na programu mbalimbali za
maendeleo ya elimu kama vile MMEM, MMES na MEMKWA.
Ndugu Wageni Waalikwa;
Kwa upande wa maendeleo
ya elimu ya juu pia tumepata mafanikio ya kutia moyo. Tumeongeza idadi ya vyuo vikuu kutoka 26 mwaka 2005 hadi 33 mwaka 2009 ambapo kwa sasa vyuo vikuu vya binafsi vipo 21 na vya Serikali 12. Ongezeko hili la vyuo
vikuu nchini limewezesha idadi ya Wanafunzi wanaojiunga na
vyuo vya elimu ya juu kuongezeka kutoka 55,296
mwaka 2005 hadi 118,000 mwaka 2009.
Tumefanikiwa
kufikisha idadi hiyo kubwa ya wanafunzi katika vyuo vikuu kutokana pia na ufadhili unaotolewa na Serikali kwa wanafunzi. Serikali
iliongeza fedha kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi
kutoka shilingi 56.1 bilioni mwaka
2005 hadi shilingi 243 bilioni mwaka
2010. Ongezeko hili la fedha limewezesha idadi ya wanafunzi wanaonufaika na mikopo kuongezeka kutoka wanafunzi 16,345 mwaka 2005 hadi wanafunzi 69,250 mwaka 2009. Pamoja
na juhudi za kuwezesha wanafunzi wengi kupata mkopo
hiyo, hapana budi hatua zaidi zichukuliwe
kuyapatia ufumbuzi malalamiko yahusuyo utaratibu
wa kukubaliwa kupata mkopo na uchelewashaji wa malipo. Nilishaagiza Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Wizara ya Fedha na Bodi ya
Mikopo kushirikiana kumaliza matatizo hayo.
Naamini tutaanza mwaka mpya wa masomo na mambo
mapya mazuri. Aidha, ofisi yangu kupitia
kwa Katibu Mkuu Kiongozi itafuatilia kwa karibu
mchakato huo.
Ndugu Wageni waalikwa
Sisi
serikalini tumejipanga vyema kupitia Mpango wa
Maendeleo ya Elimu ya Juu (MMEJU) ambao tumeanza kuutekeleza. Ni mategemeo yetu
kuwa utekelezaji wa Mpango huo utasaidia kuimarisha na
kuboresha elimu ya juu kwa kiwango kikubwa. Napenda
kuwahakikishia kuwa Serikali itasimamia kwa ukamilifu
utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Juu (MMEJU) ili malengo yake
yaweze kufikiwa. Chini ya mpango huu tunategemea kufanya yafuatayo:
1. Kukarabati, kupanua na
kuimarisha miundombinu ya vyuo vikuu na vyuo vikuu vishiriki ili viweze
kuhimili ongezeko kubwa la wanafunzi watakaomaliza elimu ya sekondari.
2. Kuongeza udahili wa wanafunzi
kwenye vyuo vya elimu ya juu na kuhamasisha
wanafunzi wa kike idadi ifikie asilimia 40 ya wanavyuo wanaodahiliwa kila mwaka.
3. Kuandaa wahadhiri wa kutosha
na wenye sifa za kufundisha kwenye vyuo vya elimu ya juu.
4. Kuunganisha vyuo vikuu na
taasisi za utafiti kwenye mtandao mmoja ili kuimarisha utafiti wa pamoja,
kupanua elimu katika kiwango cha uzamili na uzamivu.
5. Kuratibu na kusimamia utoaji
wa Elimu ya Juu iliyo bora na kufanyika kwa utafiti ili ziweze kutatua matatizo
ya kijamii na kiuchumi.
6. Kuimarisha mazingira ya utoaji wa
Elimu ya Juu na maslahi yanayoendana nayo ili wahadhiri wavutiwe kujiunga na
kubaki katika vyuo vya Elimu ya Juu na Vyuo Vikuu.
7. Kuimarisha utoaji wa Elimu ya
Juu kwa njia ya Masafa na Elimu Mtandao.
8. Kuimarisha uwezo wa watendaji
katika usimamizi na menejimenti ya programu za elimu katika ngazi zote.
Tukitekeleza
malengo haya, kama taifa tutakuwa tumepiga hatua
kubwa. Ni mategemeo yangu kwamba vyuo na taasisi
husika vitajipanga vyema katika kufanikisha utekelezaji wa Mpango huu wa maendeleo
ya elimu ya juu.
Mheshimiwa Waziri na Ndugu
Wakuu wa Vyuo;
Upanuzi
wa elimu ya juu umeleta changamoto zake kama ilivyo
kwa sekondari na msingi. Kubwa kati ya
changamoto hizo ni uhaba wa wakufunzi wenye sifa
stahiki wa kufundisha katika vyuo hivyo. Natambua na kuwapongeza kwa jitihada kubwa mnazozifanya
za kukabiliana
na changamoto hii kubwa. Napenda kutumia
nafasi hii kurudia ushauri wangu nilioutoa siku za nyuma kuwa vile vyuo vyetu
vyenye Wahadhiri na Maprofesa wa kutosha katika fani mbalimbali kama vile Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine, Morogoro, na Chuo
Kikuu cha Tiba cha Muhimbili, wapanue, waimarishe na waboreshe programu zao za
uzamili na uzamivu. Kwa
kufanya hivyo tutapata wahitimu wengi wenye sifa stahiki za kufundisha kwenye
vyuo vyetu vikuu.
Naomba
niwakumbushe na kusisitiza umuhimu wa vyuo vikuu kujikita
katika masuala ya utafiti. Sifa moja nyingine kubwa ya Chuo Kikuu zaidi ya ile
ya kufundisha ni kufanya utafiti. Naomba vyuo vikuu kuhakikisha kwamba vinatoa
kipaumbele cha juu kwa shughuli za utafiti. Vyuo viwe na mikakati
maalum na mipango kazi mizuri ya kufanya tafiti za namna mbalimbali
zitakazonufaisha vyuo kitaaluma na kuliwezesha taifa letu kusonga mbele
kimaendeleo.
Kwa kutambua umuhimu wa
utafiti na kwa nia ya kusaidia kuendeleza shughuli za utafiti, sisi katika
Serikali tumetenga shilingi bilioni 30 kwa ajili ya utafiti katika maeneo
mbalimbali. Huu ni mwanzo tu, tutaendelea kuongeza
fedha hizo hatua kwa hatua mpaka tufikie lengo letu la kutenga asilimia moja ya
bajeti ya Serikali kwa ajili ya shughuli za utafiti. Ni jukumu lenu sasa kujipanga
vizuri ili
muweze kutumia fursa hiyo kwa manufaa ya vyuo vyenu na taifa.
Mheshimiwa Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Ufundi na Wageni Waalikwa
Kabla
sijamaliza hotuba yangu, napenda nichukue nafasi hii kuipongeza Tume ya Vyuo
Vikuu Tanzania kwa jinsi inavyokabiliana na changamoto
mbalimbali katika kuboresha elimu ya juu katika nchi yetu. Nafurahi kusikia kwamba mmekamilisha mfumo wa kutambua viwango vya elimu na taaluma mbalimbali, ziwe za
ndani au nje ya nchi unaojulikana kama National
Qualifications Framework. Nawapongeza
kwa kuanza kutumia mfumo wa mtandao kudahili wanafunzi
katika vyuo vya elimu ya juu nchini. Natambua mwanzo ni
mgumu, kutakuwepo na mapungufu yake. Kinachotakiwa
ni kuondoa kasoro hizo na kuuboresha. Ni matumaini yangu kuwa mahitaji maalum ya kujali makundi
mbalimbali katika jamii yatazingatiwa.
Si busara kuwa na mfumo ambao hautajali
mazingira maalum ya jamii na nchi yetu na kusababisha makundi fulani kukosa
fursa ya elimu ya juu.
Nimefarijika sana kusikia kuwa
mmeweza kutoa mafunzo mbalimbali kwa viongozi wa vyuo vikuu ili kuwajengea
uwezo wa kuweza kuvisimamia na kuviendeleza vyuo vyao ili kukidhi mahitaji ya
Taifa kielimu. Nawasihi muendelea na
juhudi zenu hizo
maradufu. Katu msirudi nyuma na wala msikubali kukatishwa tamaa. Uboresheni mpango huu na
kama hapana budi siku za usoni tuangalie uwezekano wa kufanya mafunzo haya kuwa
sharti la kupewa nafasi ya uongozi katika vyuo au kuendelea nao.
Mheshimiwa Waziri, Wakuu wa Vyuo na Wageni Waalikwa;
Mwisho
kabisa, nachukua fursa hii kwa mara nyingine, kuwashukuru
wenzetu wa sekta binafsi kwa jinsi walivyoitikia wito wa kuanzisha vyuo vya
elimu ya juu nchini. Mmeonyesha mfano
mzuri kwa kuiunga mkono Serikali katika kuendeleza
elimu hapa nchini. Napenda tu nitoe tahadhari kwamba mjiepushe kusukumwa na tamaa na kupata faida kubwa bali kutoa huduma kwa
jamii. Elimu ikigeuka
biashara ya kumpatia mtu faida nono itakuwa hatari. Viwango vyetu vya
ada vitakuwa vikubwa mno na havitaendana na hali
halisi ya uwezo wa wananchi wengi kumudu kuipata. Elimu kuwa kwa
wachache ni hatari kwa jamii kwani hata Serikali itashindwa kuwasaidia wengi
kupitia Bodi ya Mikopo. Kama suala la
viwango vya ada lipo kenye mamlaka ya TCU basi lisimamamieni ipasavyo na, kama halina chombo cha kulisimamia, nadhani wakati
umefika litafutiwe chombo. Lazima
tufanye hivyo, vinginevyo tutakosa mwelekeo mzuri katika masuala ya elimu, kitu
ambacho ni hatari kwa maendeleo yetu kama taifa.
Mheshimiwa Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Ufundi na wageni waalikwa
Baada
ya kusema hayo, naomba kuwatakia kila la heri katika shughuli zenu za kutoa na kusimamia elimu.
ASANTENI KWA KUNISIKILIZA