HOTUBA YA
RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI MHE. AMANI ABEID KARUME
KATIKA MAADHIMISHO YA
SHEREHE ZA MIAKA 38 YA MAPINDUZI
YA ZANZIBAR TAREHE 12 JANUARI, 2002
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Benjamin William Mkapa,
Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Dr. Ali Mohammed Shein,
Makamo Mwenyekiti wa CCM Tanzania Visiwani na
Rais Mstaafu wa Zanzibar, Mheshimiwa Dr. Salmin Amour,
Makamo Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara
Mheshimiwa
John Samuel Malecela,
Waziri Mkuu, Mheshimiwa Fredric Sumaye,
Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
Mheshimiwa
Shamsi Vuai Nahodha,
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mzee Ali Hassan Mwinyi,
Waheshimiwa Mawaziri wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano
na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Katibu Mkuu wa CCM, Mhe. Philip Mangula,
Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa,
Waheshimiwa Mabalozi wa Nchi za Nje,
Ndugu Wananchi,
Mabibi na Mabwana
1.0 UTANGULIZI:
1.1 Kwanza naomba tumshukuru
Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa
kutuwezesha kukutana hapa leo hii tukiwa wazima na wenye afya ili kwa pamoja
tuadhimishe miaka 38 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar yaliyofanyika tarehe 12
Januari 1964.
1.2 Nachukua fursa hii pia
kuwashukuru wananchi kwa jumla kwa kuienzi siku hii kwa kujitokeza kwa wingi
ili tujumuike pamoja kwenye kilele cha maadhimisho haya. Aidha nawapa shukurani nyingi wananchi
wote wa Visiwa vya Unguja na Pemba kwa kuonesha busara na uvumilivu mkubwa
kutokana na hali ngumu za maisha wakati wa kipindi kigumu cha uchumi duni. Serikali yenu ya Awamu ya Sita imeanza
kuchukua hatua za dhati za kuleta marekebisho kadhaa yenye lengo la kujenga
misingi ya maendeleo kwa watu wote.
Shukurani pia ziwafikie wananchi wote kwa jumla kwa kudumisha utulivu,
upendo, amani na usalama nchini mwetu.
1.3 Shukurani
maalum kwa niaba yenu wananchi nazielekeza kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mheshimiwa Benjamin William Mkapa kwanza kwa kujumuika nasi katika
kilele cha maadhimisho haya siku hii ya leo. Kuhudhuria kwako katika sherehe hii ni faraja kubwa
kwetu. Tunakushukuru Mhe. Rais
kutokana na wewe mwenyewe binafsi kuwa karibu sana na watu pamoja na Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar, nyakati zote ziwe za furaha au ziwe za shida. Kwa nafasi zako mbali mbali ukiwa ni
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano, umeyafuatilia
matukio na maendeleo ya Zanzibar kwa karibu sana kwa lengo la kuyafanya maisha
ya Wazanzibari yawe tulivu na bora zaidi.
1.4 Tunakushukuru na kukupa
pongezi Mheshimiwa Rais kwa ujasiri na uongozi wako wa busara, maamuzi na upeo
mkubwa ambao umeiletea nchi yetu ya Tanzania sifa na heshima kubwa
duniani. Uongozi wako usioyumba
umeweza kukuza umoja na upendo baina ya wananchi, amani na kupanuka kwa demokrasia
ya kweli hapa nchini.
2.0 MAANA YA MAADHIMISHO YA LEO:
2.1
Ndugu Wananchi,
tumejumuika kwa wingi leo kwa lengo la kuyakumbuka na kuyaenzi Mapinduzi
Matukufu ya Januari 12, 1964, Mapinduzi yaliyojenga msingi wa ukombozi wa
wanyonge wa nchi hii na ukombozi wa Wazanzibari wote kwa jumla. Tunaikumbuka siku ya leo kwa sababu ni
siku ambayo tofauti baina ya Wazanzibari, tofauti za rangi, asili, uzawa,
kabila, imani na mali ziliondolewa na ni wajibu wetu sote kuhakikisha kuwa
tofauti hizo hazitorejea tena.
2.2
Aidha tunaitukuza siku
ya leo kwa kuwakumbuka mashujaa wote walioshiriki kwa namna moja au nyengine
katika Mapinduzi hayo, kuwaombea kwa Mola wale waliotangulia mbele ya haki na
kuwatakia maisha mema wale ambao bado wako hai. Ni siku ambayo tunawaenzi wale wote ambao kwa vipindi mbali
mbali katika muda wa miaka 38 iliyopita wametoa nguvu zao katika kuyalinda,
kuyaenzi na kuzitekeleza ahadi za Mapinduzi kwa maslahi ya wananchi wote.
2.3 Tunaiadhimisha siku hii ya leo kwa kuzikumbuka, kuzitafsiri
na kuazimia kuendelea kuzilinda na kuzitekeleza ahadi zilizowekwa na waasisi wa
Mapinduzi zenye lengo la kuinua hali za wananchi wote wa Zanzibar kuwa bora
zaidi. Aidha hatuna budi tuitumie
siku ya leo kupima utekelezaji wetu wa ahadi hizo za Mapinduzi.
2.4
Wakati wa maadhimisho
haya, na ikiwa ni matokeo ya Mapinduzi, tuna wajibu pia wa kuuzungumzia
Muungano kati ya iliyokuwa Tanganyika na Zanzibar - Muungano uliozaa
Tanzania. Tunauzungumza Muungano
kwa madhumuni ya kuulinda na kuuenzi huku tukielewa kuwa bila ya Mapinduzi
tusingelikuwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
2.5
Kadhalika,
tunaiadhimisha siku hii ya leo, ili tuweze kutafakari yale tuliyofanikiwa
kuyatekeleza, tufanye uchambuzi wa yale yaliyotutatiza na sababu zake na hatimae
tupange mkakati wa kipi kifanyike ili tuweze kwa ufanisi zaidi kuziendeleza
azma za Mapinduzi za kuinua hali za wanyonge na kulijengea heshima Taifa letu.
3.0 MAFANIKIO TULIYOYAPATA TANGU MAADHIMISHO YA MIAKA 37
YA MAPINDUZI
3.1 Ndugu Wananchi, leo ni mwaka
mmoja tangu tuadhimishe miaka 37 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, na ni mwaka
mmoja na kidogo tangu muiweke madarakani Serikali ya Awamu ya Sita ambayo mimi
naiongoza. Katika kipindi cha
mwaka mmoja huo tumeweza kupunguza ukubwa wa Serikali Kuu na kuunda Serikali
ndogo ya Wizara 12 tu. Tumeunda
Serikali ndogo ili kupunguza gharama za uendeshaji lakini bila ya kuathiri
huduma za Serikali hiyo kwa wananchi.
Sambamba na marekebisho hayo ya muundo wa Serikali, baadhi ya mashirika
na taasisi nyengine zilifanyiwa marekebisho kwa lengo la kuimarisha utendaji
wake.
3.2 Pamoja
na kufanya marekebisho kwenye muundo wa Serikali na vyombo vyake, tumejitahidi
na tunaendelea kujenga nidhamu na uwajibikaji katika utendaji wa vyombo
hivyo. Katika kulitekeleza hilo,
Serikali yenu imeidhinisha Sheria inayoongoza mambo ya fedha kwa lengo la
kujenga udhibiti wa mapato na matumizi ya Serikali na vyombo vyake. Pia Serikali yenu imeandaa Sheria ya
Zabuni itakayosimamia taratibu zote za uagiziaji na ununuzi wa mahitaji ya
Serikali. Hatua hii ina lengo la
kuondoa ubadhirifu wa rasilimali za Serikali na kuepukana na ununuzi wa mali
holela na kwa bei zisizo za ushindani.
Aidha Serikali imesisitiza ununuzi wa mahitaji yake kutoka kwa wale
wafanyabiashara wanaolipa kodi kihalali Serikalini watakaokuwa na namba maalum
zinazowatambulisha.
3.3
Ndugu Wananchi, katika
kipindi hicho cha mwaka mmoja, Serikali yenu imeongeza juhudi za
kuzishughulikia kero zinazowakabili wananchi walio wengi. Kwa kipindi kirefu, wastaafu Serikalini
na Mashirika ya Serikali, wamekuwa wakilalamika kwa sababu hawakulipwa haki
zao. Kwa taarifa yenu, hivi sasa
Serikali imelishughulikia suala hili, na wastaafu wameanza kupata haki zao kwa
utaratibu unaofahamika. Katika
kipindi cha mwaka mmoja uliopita Serikali imeweza kuwalipa wastaafu 876 viinua
mgongo vya jumla ya Shilingi 770 milioni.
Aidha Serikali imelipa pencheni za wafanyakazi zenye jumla ya Shilingi
784 milioni.
3.4 Suala
la michango ya Serikali katika Mfuko wa Hifadhi ya Jamii pia lilikuwa ni tatizo
kwa muda mrefu. Baada ya
kulifanyia uchunguzi, na kurekebisha kasoro zilizokuwepo, michango hiyo ya
Serikali kwa niaba ya wafanyakazi sasa inalipwa kama kawaida, na mfanyakazi
hana haja ya kuwa na hofu juu ya haki zake pale anapostaafu. Katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita hadi kufikia mwezi wa
Septemba, Serikali ilikwisha kulipa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii jumla ya Shilingi
258 milioni.
3.5
Ili kujenga msingi wa
maendeleo endelevu, Serikali yenu imeandaa mpango utakaoongoza juhudi zake, na
za wananchi katika kukabiliana na tatizo sugu la umasikini. Kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa
Mataifa la Mpango wa Maendeleo (UNDP), Serikali yenu imetengeneza sera na
mikakati ya utekelezaji kwa kila sekta ili kuongoza juhudi zetu katika kupambana
na umasikini na kuzifanya hali za wananchi kuwa bora zaidi. Mpango huu ambao ni tafsiri ya Mpango
wa Maendeleo wa Muda Mrefu wa Dira ya Zanzibar ya 2020 utakuwa ukitekelezwa
katika vipindi vya miaka mitatu mitatu ambapo kila baada ya mwaka mmoja tathmini
ya utekelezaji itafanyika na kufanya marekebisho yanayostahili kufanyika ili
kuimarisha utekelezaji wa mwaka ujao.
3.6 Ndugu
Wananchi, hatua nyengine ambayo Serikali yenu imeipa umuhimu mkubwa katika
mwaka huu uliopita, ni ujenzi wa mazingira yatayopelekea kuondokana na migogoro
ya kisiasa ndani ya jamii yetu na kujenga misingi mizuri zaidi ya
demokrasia. Kwa zaidi ya miaka
sita sasa, nchi yetu imekuwa katika malumbano ya kisiasa baina ya vyama na wafuasi
wa vyama vikuu vya kisiasa hapa nchini.
Malumbano na mivutano hiyo ilipelekea kuhatarika kwa amani na utulivu wa
nchi na wananchi wake. Aidha
mivutano hiyo imezorotesha juhudi za maendeleo ya nchi yetu. Jina la Zanzibar na Tanzania likaanza
kuchafuka nchi za nje.
3.7 Ili kurekebisha hilo
Serikali yenu ilitoa msamaha kwa wale wote waliokuwa na tuhuma za makosa yenye
mwelekeo wa kisiasa. Aidha
Serikali yenu kwa ushirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
ilitoa kila aina ya msaada kwa vyama vya CCM na CUF ili viweze kufanya mazungumzo
yatakayotupeleka katika hatua mpya ya kujenga maelewano, kuaminiana na
kudumisha amani na utulivu nchini.
3.8
Matokeo ya juhudi hizo
ni kutiwa saini kwa muafaka tarehe 10 Oktoba 2001. Kasoro za kiufundi zilizojitokeza katika utekelezaji wa muafaka
huo, nazo zimeshughulikiwa kwa pamoja na hivi sasa utekelezaji unaendelea.
3.9 Ndugu Wananchi, juhudi
zote hizi za jumla, zimeanza kujenga miongoni mwetu mioyo ya kuaminiana
na hivyo kukuza ushirikiano na amani ndani ya nchi. Kwa mataifa ya kigeni, nayo pia yameanza kurejesha imani juu
ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mazungumzo ya ushirikiano kati ya Serikali yenu na nchi za nje na
mashirika ya kimataifa yanafanyika kila mara, kama mnavyoona na kusikia kutoka vyombo vya habari. Matumaini yetu ni kuukuza ushirikiano
huo kwa faida ya pande zote.
4.0 HATUA MAALUM ZA UTEKELEZAJI - KISEKTA:
4.1
Ndugu Wananchi, pamoja na mafanikio hayo ya jumla tuliyoyapata katika
kipindi cha mwaka mmoja tangu maadhimisho ya miaka 37 ya Mapinduzi, yapo mambo
mahsusi yaliyotekelezwa na Serikali yenu kwenye maeneo mbali mbali. Nitatumia fursa hii kuelezea kwa ufupi
baadhi ya hatua hizo ikiwa ni kipimo cha utekelezaji wa ahadi za Mapinduzi.
4.2 Usafiri
na Usafirishaji:
4.2.1 Kwa lengo
la kuimarisha huduma ya mawasilino na hivyo kuchochea maendeleo, Serikali yenu
katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita imeweza kukamilisha ujenzi wa barabara
zifuatazo Unguja na Pemba:
- Barabara ya
Makunduchi - Mtende
- Barabara ya
Kibuteni - Kizimkazi
- Barabara ya
Kitogani - Paje
- Barabara ya Kaebona - Kaepwani
- Barabara ya Chake -
Vitongoji
- Barabara ya Chake - Wesha inaendelea
kutengenezwa.
- Ujenzi wa Barabara ya Bambi
nao umeanza na unaendelea.
4.2.2 Ndugu
Wananchi, katika kipindi cha mwaka huu baada ya kumalizika ujenzi wa barabara
nilizozitaja, kazi za ujenzi wa barabara zifuatazo zitaanza mara moja tukiwa na
lengo la kuzimaliza kabla ya Januari 2003.
- Barabara ya Mahonda -
Donge - Mkokotoni
- Barabara ya Mtuhaliwa
- Chokocho
- Barabara ya Kidimni -
Kitope
- Barabara ya Kilindini
- Micheweni
4.2.3
Kwa upande wa sekta ya usafiri wa anga, mwaka huu wa 2002, Serikali
ikishirikiana na Benki ya Dunia itaifanyia matengenezo barabara ya kurukia
ndege Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa Zanzibar. Aidha katika sekta ya mawasiliano ya simu mpango wa
kusambaza mtandao wa simu za mkono sehemu zote za Unguja na Pemba
utakamilishwa. Hali hiyo
itawafanya wananchi wa visiwa hivi popote walipo waweze kuwasiliana na sehemu
yoyote ile duniani.
4.2.4
Aidha katika kipindi hicho,
Serikali iliipeleka meli ya
M.V. Mapinduzi ili ifanyiwe matengenezo makubwa. Kazi hiyo iliyogharimu fedha nyingi imekamilika na meli hiyo
imerejea na kuanza kufanya kazi.
4.3 Kilimo:
4.3.1 Kwa kutambua
kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi wetu, Serikali katika mwaka uliopita
ilipania kuimarisha upatikanaji wa uhakika wa zana za kisasa za ukulima. Kwa madhumuni hayo, Serikali
iliyafanyia matengenezo makubwa matrekta 16 ili yaweze kutoa huduma kwa
wakulima Unguja na Pemba. Aidha
ili kuifanya huduma hii itosheleze, Serikali imeagizia matrekta mengine mapya 6
ambayo karibu yatawasili.
4.3.2
Kwa upande wa sekta ya uvuvi Serikali iliendelea na juhudi za kuwapatia
wavuvi nyenzo muhimu kwa kazi zao kwa njia ya mikopo. Napenda kuwakumbusha wananchi wote waliobahatika na mpango
huo wazitumie vizuri nyenzo zao kwa uzalishaji bora. Kwa wale waliokosa vifaa hivyo wakati huu wavute subira
kwani Serikali tayari imeshaagiza vifaa ambavyo vinategemewa kuwasili wakati
wowote mwezi huu.
4.3.3
Serikali pia iliendelea kuihudumia sekta ya ufugaji kwa kuwapatia
wafugaji mafunzo ya utunzaji wa tembe wa kisasa. Wafugaji 75 walipatiwa mafunzo hayo, na kati yao 23
wameshapatiwa mifugo hiyo kwa utaratibu wa kupewa na kurejesha ndama ili
wafugaji wengine waweze kufaidika nao.
4.4 Elimu:
4.4.1 Kwa upande wa sekta ya elimu, Serikali
imeendelea na juhudi za kuimarisha huduma za sekta hiyo. Jumla ya madarasa 95 yalijengwa katika
kipindi cha mwaka uliopita. Aidha
madawati 4,050 yalisambazwa maskulini.
Lengo ni kulimaliza tatizo la madawati hivi karibuni.
4.4.2
Kuhusu uandikishaji wa watoto wapya, jumla ya watoto 28,000
waliandikishwa ikiwa ni jumla ya watoto wote waliofikia umri wa kwenda skuli,
na tutawaandikisha wale wote waliofikia umri wa kwenda skuli kwa mwaka huu.
4.5 Afya:
Utoaji wa huduma za afya na utibabu uliendelea
kuimarishwa kwa kuhakikisha upatikanaji wa dawa muhimu. Kwa wale wagonjwa waliohitaji uchunguzi
zaidi au huduma za mabingwa, ama walipelekwa Tanzania Bara au baadhi yao
walipelekwa nje ya nchi. Watoto
wenye matatizo ya ugonjwa wa moyo wamekuwa wakipelekwa Israel na India kwa
matibabu zaidi.
Pamoja na juhudi hizo, bado hospitali zetu zina upungufu
mkubwa wa madawa muhimu. Kutokana
na hali hiyo maandalizi ya kutafuta uwezo mzuri wa kuagiza madawa
yanafanywa. Lengo kubwa la
Serikali ni kuirekebisha hali hiyo katika kipindi hiki ili wagonjwa wote waweze
kupata huduma kamili ya matibabu na dawa.
Kwa upande wa majengo, Serikali imeweza kuyafanyia
matengenezo majengo ya hospitali ya Mnazi mmoja pamoja na ujenzi wa ukuta wa
hospitali ya wagonjwa wa akili.
Aidha nyumba ya kulelea watoto Forodhani, nyumba za matunzo ya wazee
Dole, Mkwajuni na Kivunge zilifanyiwa matengenezo muhimu.
4.6 Maji:
4.6.1 Kwa
lengo la kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa maji Serikali katika mwaka
uliopita ilichukua hatua kadhaa za kuimarisha upatikanaji wa maji na usambazaji
wake.
4.6.2 Maeneo ya
Chwaka, Charawe, Bwejuu, Paje, Jambiani, Makunduchi, Bumbwisudi na Unguja Ukuu
kwa upande wa Unguja sasa yanapata maji safi na salama. Kwa upande wa Pemba, vijiji vya
Vitongoji, Jamvini, Masipa, Kangani, Kionjo, Chunga na Konde vimewekewa mashine
mpya za kusukumia maji. Aidha
Serikali imefunga jenereta mpya za kusukumia maji kwa ajili ya kijiji cha Weni
- Wilaya ya Wete. Kwa wastani hivi
sasa karibu asilimia 60 ya watu wote wanapata maji safi na salama. Hivi sasa Serikali inaelekeza juhudi
zake katika kulimaliza tatizo la maji kwenye miji ya Unguja na miji ya
Pemba. Kiini cha matatizo hayo kwa
kiasi kikubwa, ni uchakavu wa mtandao wa usambazaji maji, ujenzi holela, na
kasi kubwa ya ongezeko la watu mijini Zanzibar. Kutokana na gharama kubwa ya mradi huo Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar imeiomba Serikali ya Japan kusaidia lakini wakati huo huo juhudi zetu
za ndani za kurekebisha hali hiyo zinaendelea. Kwa hivyo nawaomba wananchi wanaoishi katika maeneo hayo
wawe na subira.
5.0 MATATIZO YALIYOTUKABILI:
Ndugu Wananchi, licha ya mafanikio mengi ya kupigiwa
mfano ambayo nimeyaelezea, mafanikio hayo yamepatikana katika mazingira magumu
ya kiuchumi.
5.1 Ufinyu wa Bajeti:
5.1.1 Moja ya
matatizo hayo ni ufinyu wa bajeti ya Serikali kwa maana ya ukusanyaji mdogo wa
mapato kulingana na mahitaji makubwa ya matumizi, hali inayoipunguzia Serikali
uwezo wa utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo. Hali hii inasababishwa na vianzio duni vya mapato na
matumizi yaliyopanuka kuliko uwezo uliopo.
5.1.2
Mapato ya Serikali kwa jumla kwa kipindi hicho cha mwaka mmoja yalifikia
wastani wa asilimia 59.3 tu ya lengo lililowekwa. Kutokana na kuanguka kwa biashara, mapato yatokanayo na
uagiziaji bidhaa toka nje yalifikia asilimia 55 tu. Makusanyo ya kodi ya VAT yalifikia asilimia 50 tu ya lengo,
ambapo makusanyo ya kodi za ndani kupitia Bodi ya Mapato yalifikia asilimia 67
tu ya lengo.
5.2 Gharama za Uendeshaji
Serikali:
5.2.1 Tatizo jengine linaloikabili Serikali yenu, ni gharama
za uendeshaji wake. Licha ya
kupunguza idadi ya Wizara, bado muundo wa utendaji Serikali ni mkubwa. Serikali ina wafanyakazi wachache wenye
uwezo wa kazi za kitaalam, na idadi kubwa ni ya watendaji wenye ujuzi wa kati
na kati na wahudumu. Ufanisi wa
utendaji Serikalini bado ni mdogo.
5.2.2
Pamoja na tatizo la ukubwa wa Serikali, mapato ya wafanyakazi ni madogo
na hayakidhi mahitaji yao. Matokeo
ni muda mwingi hutumika kujitafutia maslahi mengine kwa njia ambazo aghlab
zinaambatana na udokozi na ubadhirifu.
5.2.3 Haya
ni mambo ambayo yanahitaji kushughulikiwa kwa haraka.
5.3 Maendeleo ya
Vijana:
5.3.1 Ndugu Wananchi, maendeleo ya
nchi yetu yanategemea sana nguvu za vijana. Ili vijana waweze kutekeleza majukumu yao wanapaswa wajenge
utamaduni wa kujituma na kupenda kufanya kazi. Ingawa safari yetu ya kufikia maendeleo ni ndefu, lakini
tunaweza kufanikiwa iwapo vijana watafanya kazi kwa bidii na maarifa huku
wakipiga vita uzembe, uvivu na ubadhirifu. Tunahitaji vijana wenye uwezo mkubwa wa kitaalam na maarifa. Kama tulivyoahidi katika Ilani ya
Uchaguzi, Serikali ya Awamu ya Sita, itaendelea na juhudi zake za kuongeza vyuo
vya mafunzo ya amali, kwa lengo la kuwapatia vijana taaluma ya ufundi na
hatimae kuweza kujiajiri wenyewe kwa wale watakaokosa ajira Serikalini. Katika kutekeleza azma hii Wizara ya
Vijana, Ajira, Maendeleo ya Wanawake na Watoto pamoja na Wizara ya Elimu,
Utamaduni na Michezo na Wizara ya Fedha na uchumi zimesaini mkataba na Benki ya
Maendeleo ya Afrika (ADB) kuhusu uanzishaji wa vituo viwili vya Amali,
Mkokotoni, Unguja na Vitongoji, Pemba.
5.3.2 Aidha Wizara hiyo inafanya utafiti
kuhusu uwezo na mahitaji ya vifaa katika vituo mbali mbali vya Amali ikiwemo,
Dole, Skuli ya Sekondari ya Mikunguni, Chuo cha Karume, Chuo cha Utalii,
Dodeani na Chuo cha JKU, Mtoni.
Matokeo ya utafiti huu yataisaidia Wizara kujua mahitaji ya kila chuo
ili itakapotoa msaada katika vyuo vya Amali ukidhi mahitaji yao halisi. Kadhalika, Serikali ya Mapinduzi,
itaongeza nafasi za masomo ya juu mara baada ya kuzinduliwa rasmi Chuo Kikuu
cha Taifa cha Zanzibar "State University of Zanzibar" (SUZA) hivi
karibuni kwa madhumuni ya kuongeza
idadi ya wataalamu.
5.3.3 Kwa upande mwengine,
katika juhudi za kujiandaa na utekelezaji wa Mpango
wa Dira ya Maendeleo ya 2020, Serikali yenu imewasiliana na vyombo vya fedha
vya Kimataifa IMF na World Bank na kuwaomba utaalam na hata fedha ikiwezekana,
utakaowasaidia wawekezaji kuanzisha ujenzi wa viwanda mbali mbali ndani ya
Maeneo Huru vitakavyozalisha aina nyingi ya bidhaa zitakazosafirishwa nje ya
nchi kwa kutegemea masoko ya Marekani,
Jumuiya ya Ulaya (EU),
Jumuiya ya SADC na Jumuiya ya Afrika Mashariki. Tukifanikiwa na utekelezaji wa mpango huo, tatizo la ajira kwa vijana
na wengine litamalizika kabisa na kugeuka historia.
5.3.4
Ndugu Wananchi, Serikali itaendelea na juhudi zake za kuimarisha mfumo
wa uajiri Serikalini pamoja na kurekebisha mfumo wa mishahara ili uwe kivutio
kwa vijana wenye taaluma nzuri katika fani zao. Ili kuhakikisha kuwa kila mfanyakazi wa Serikali analipwa malipo
stahiki, Serikali itaendelea na zoezi la kutathmini na kuchunguza idadi halisi
ya watumishi na taarifa zao kuwekwa vizuri katika kompyuta. Zoezi hili litakapofanikiwa litaisaidia
Serikali kupunguza matumizi ya mishahara na hatimaye fedha hizi zitumike katika
miradi ya maendeleo.
5.4 Magendo ya Karafuu:
5.4.1
Ndugu Wananchi, tatizo jengine kubwa ambalo limeikumba nchi yetu katika
miaka ya hivi karibuni ni magendo ya karafuu. Kama tunavyofahamu karafuu ni zao ambalo nchi yetu
inalitegemea sana kwa mapato yake ya fedha za kigeni. Licha ya kwamba uzalishaji wake Zanzibar umepungua na
wazalishaji duniani wameongezeka bado mauzo ya karafuu yanaipatia nchi yetu
sehemu kubwa ya mapato yake ya fedha za kigeni zinazoisaidia nchi kununulia
dawa za hospitali, vifaa vya maskuli, lami ya kujengea barabara, kusafirisha
wagonjwa, ununuzi wa zana za kusukumia maji, kilimo na kadhalika.
5.4.2
Wimbi lililojitokeza hivi sasa la kusafirisha nchi jirani karafuu kwa
magendo, linawadhulumu Wazanzibari walio wengi huduma hizo. Serikali kwa msimu uliopita imejitahidi
sana kuudhibiti usafirishaji huo wa magendo na jitihada hizi zitaendelea kwa
nguvu zaidi. Nachukua fursa hii
kuvishukuru vyombo vyote vya ulinzi vilivyohusika katika zoezi hili la
kupambana na magendo ya karafuu pamoja na wananchi wema waliosaidiana
navyo. Aidha nawapa shukurani za
dhati wale wananchi wote waliofuata taratibu zilizowekwa katika uuzaji wa
karafuu. Serikali kama ilivyo
kawaida yake, itajitahidi kila inapowezekana kuzirekebisha bei za ununuzi wa
karafuu toka kwa wakulima pamoja na kuongeza huduma kwa wakulima hao.
5.5 Masuala ya Muungano:
5.5.1 Ndugu
Wananchi, mwezi Aprili mwaka huu Muungano wa iliyokuwa Tanganyika na Zanzibar
utatimiza miaka 38 tangu uasisiwe.
Katika miaka 38 hiyo mafanikio mengi yamepatikana, kubwa ikiwa ni kudumu
kwa Muungano wenyewe.
5.5.2 Muungano
kama chombo chengine chochote kinachokutanisha watu na kuwaweka pamoja hakikosi
misukosuko. Katika maisha ya
Muungano huu, imejitokeza misukosuko ya hapa na pale katika nyanja mbali mbali
zikiwemo:-
- Uwezo wa Zanzibar
kufanya mashauriano na nchi za nje;
- Uwezo wa Zanzibar kukopa nchi za
nje;
- Uwakilishi wa Zanzibar kama sehemu ya
Tanzania kwenye vyombo vya nje na Jumuiya mbali mbali za kiuchumi;
- Ugharimiaji wa kazi za Muungano
- Sehemu ya Zanzibar katika misaada
inayoingia Tanzania;
- Gawio la
mapato kutoka vyombo vya Muungano na kadhalika;
- Uendeshaji wa
biashara baina ya Zanzibar na Tanzania Bara.
5.5.3 Haya na mengineyo ni baadhi ya
masuala ambayo yamekuwa yakizungumzwa mara kwa mara kama kero za Muungano. Hata hivyo kwa kupitia vikao vya
mashauriano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar ufumbuzi wa matatizo hayo hatua kwa hatua umekuwa
ukipatikana.
5.5.4 Aidha, Serikali zenu mbili zimeshaweka mikakati ya kuzishughulikia
kero hizo kwa matayarisho ya kuunda Tume ya Pamoja ya Fedha itakayoshughulikia
mambo yote yanayohusu mapato na matumizi ya mambo ya Muungano. Kadhalika Kamati ya Wataalamu wa Fedha
kutoka Serikali zote mbili imeshaundwa na hivi sasa itashughulikia matokeo ya
siku hadi siku.
6.0 HATUA ZA USONI:
6.1 Ndugu Wananchi, nimejaribu kuyabainisha
baadhi ya matatizo ambayo Serikali yenu imekabiliana nayo katika kipindi cha
mwaka mmoja uliopita. Kuyataja
matatizo si udhaifu, bali ni kujenga tabia ya ukweli na uwazi katika utendaji
wa kazi zetu. Kuyajua matatizo
ndio mwanzo wa kupanga mikakati ya kutafuta ufumbuzi wake.
6.2
Serikali yenu katika mwaka ujao na siku za usoni imepanga kutekeleza
mambo kadhaa ili kukabiliana na matatizo niliyoyataja, kupunguza kero
zinazowakabili wananchi na kuendelea na kutekeleza ahadi za Mapinduzi Matukufu
ya Zanzibar ya kuinua hali za maisha za watu wetu.
6.3 Katika mwaka ujao, Serikali yenu itaziendeleza kwa nguvu zaidi
juhudi za uimarishaji wa mapato yake.
Serikali itaangalia vianzio vipya vya upatikanaji wa mapato, kuziba
myanya ya uvujaji kwa sehemu mbali mbali na papo hapo kuimarisha udhibiti wa
matumizi yake. Katika kufanya
hivyo Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
itaiimarisha Ofisi ya Mamlaka ya
Mapato Zanzibar (TRA) kiujuzi na
vifaa ili ifanye kazi zake kwa ufanisi zaidi. Aidha kwa mapato ya ndani, Serikali itauimarisha utendaji wa
Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) ili iongeze uwezo wake wa ukusanyaji wa mapato
na kupiga vita ukwepaji wa kodi.
6.4 Kuhusiana na ajira ya vijana
Serikali ingependa kuwatanabahisha wananchi wake kwamba huko twendako, ajira
itatokana na kuongezeka kwa harakati za sekta binafsi na Jumuiya za wananchi
wenyewe.
6.4.1 Serikali
kwa upande wake itaendelea na uhamasishaji wa wawekezaji kutoka nje kwa kuweka
mazingira mazuri ya uwekezaji.
Vitega uchumi vikiongezeka, ndivyo ajira itakavyoongezeka. Ili kuwatayarisha vijana kwa ajira hizo,
Serikali itapanua zaidi fursa zilizopo za mafunzo ya amali, ufundi na elimu
mbadala.
6.4.2
Kwa upande wa wananchi, Jumuiya ya wananchi, Jumuiya zisizo za
Kiserikali zitaendelea kuhamasishwa ili zipanue shughuli zao na hivyo kukuza
uwezo wa ajira.
6.5
Muundo wa Utumishi Serikalini hivi sasa hauridhishi, gharama za uendeshaji ni kubwa. Serikali inaandaa hatua ya kuurekebisha
muundo huo ili kuongeza ufanisi.
Serikali ina lengo la kuwa na wafanyakazi wenye ujuzi wa kazi zao. Kwa hiyo mafunzo kazini na nje ya kazi
yatasisitizwa. Nidhamu na
uwajibikaji vitapewa umuhimu mkubwa.
6.6 Ili kukabiliana na tatizo la huduma
za jamii kwa jumla, na kwa lengo la kuharakisha maendeleo, Serikali itaendelea
na mipango yake ya kusaidia nguvu za wananchi katika kujijengea mabanda ya
skuli, vituo vya afya, maji, umeme na kadhalika. Sambamba na hatua hizo, Serikali kupitia Afisi ya Waziri
Kiongozi itaendelea kuwahamasisha wananchi Mijini na Vijijini ili waweze kuutumia
vizuri Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ambao umeshaanza kutumika na umetoa
mchango mkubwa katika huduma za jamii. Aidha, kwa mwaka huu wa fedha Serikali
itahakikisha kuwa jumla ya Shs. 150 milioni zilizotengwa kwa ajili ya miradi
hiyo zitatolewa zote kama ilivyoahidiwa.
6.7
Nimeeleza hapo awali, kwamba moja ya fanikio kubwa tulilolipata katika
mwaka uliopita ni kuandaa mpango wa kupunguza umasikini Zanzibar. Kwa mwaka huu tuliouanza Serikali
inaandaa mikakati ya kuanza kuitekeleza awamu ya kwanza ya miaka mitatu ya
mpango huo. Kipaumbele katika
mkakati huo wa miaka mitatu ni kuelekeza nguvu zaidi kwenye sekta ya afya,
maji, barabara, kilimo, elimu na utawala bora. Serikali kwa kushirikiana na Mashirika ya Kimataifa ya UNDP
na Benki ya Dunia yanaandaa mkutano wa mashauriano na wahisani wengine kuona
jinsi gani wahisani hao wanaweza kutusaidia katika utekelezaji wa mpango huo wa
kupunguza umasikini.
6.8
Ndugu Wananchi, mipango ya maendeleo inawahusu wananchi. Ili kuwa na mipango mizuri ni vyema
kujua idadi ya walengwa wanaokusudiwa.
Idadi ya watu wa Zanzibar inakadiriwa kufika milioni moja. Uhakika wa idadi hiyo, imegawika vipi
kimikoa, kijinsia, watoto na watu wazima, itafahamika wakati litakapofanyika
zoezi la kuhesabu watu mwezi wa Agosti mwaka huu. Maandalizi ya zoezi hili la sensa yapo mbioni
kukamilika. Zoezi la majaribio
limefanyika na matokeo ni mazuri.
Ni haki na wajibu wetu sote kujitokeza bila ya kukosa wakati wa
utekelezaji wa zoezi lenyewe.
Sensa ni jambo linalofanyika katika nchi zote duniani kila baada ya
miaka kumi. Madhumuni ni
kuipa Serikali uwezo wa kupanga
vizuri mipango ya kuwahudumia watu wake.
Sensa haitafuti wakorofi, wala haitafuti majambazi. Ni jukumu la watu wote na hasa viongozi
kuwahamasisha wananchi washiriki zoezi hili kwa faida yetu sote.
6.9
Ndugu Wananchi, ongezeko la idadi ya watu linaambatana sana na uzito juu
ya mazingira ya nchi. Jinsi idadi
ya watu inavyoongezeka ndivyo msongamano wa watu kwenye eneo dogo la ardhi
unavyozidi. Matokeo yake ni
kuharibika kwa mazingira na kupungua kwa rasilimali za asili. Inakadiriwa kuwa kwa wastani takriban
hekta 1,000 za misitu ya asili hukatwa kila mwaka kwa ajili ya matumizi mbali
mbali. Ili kukabiliana na tatizo
hili nchi haina budi iwe na mipango mahususi ya kuhifadhi mazingira ya
asili. Kila mwaka tumekuwa
tukipanga siku maalum za upandaji wa miti hapa visiwani. Kampeni hii ya upandaji wa miti haina
budi iimarishwe na kuendelezwa kila mwaka. Kutokana na haja hiyo, Serikali itasimamia kwa ukamilifu na
kuwahusisha wananchi wote mijini na vijijini.
6.10
Ndugu Wananchi, mafanikio ya maandalizi yote ya maendeleo ya nchi yetu
na watu wake, yatategemea kuwepo kwa watu waliohai na wenye afya nzuri kwa
kufanya kazi. Wakati Serikali
inayashughulikia hayo, ni wajibu wetu sote kuelewa vyema kwamba UKIMWI ni
tatizo linaloathiri jamii yetu kwa kasi kubwa. Hadi sasa watu zaidi ya 2,000 wameathirika na virusi
vya ukimwi, na karibu watu 500 wameshapoteza maisha. Makisio ni kwamba idadi ya walioathirika inafikia watu 7,000
au zaidi.
6.11
Ukimwi, tunaambiwa kwamba hadi sasa hauna tiba. Kwa bahati nzuri kinga yake kubwa ni
kujiepusha na tabia ya kufanya mapenzi nje ya ndoa. Wakati umefika wa kuelimishana na kuhamasishana ili
tuondokane na tabia zinazosambaza maradhi hayo. Tuzungumze juu ya ukimwi kila tunapojumuika, kwenye mikutano
ya kijamii, kisiasa, michezo, mikusanyiko ya kidini na kadhalika. Tusione haya wala vibaya kuuzungumza
ukimwi, kwani tukiuonea haya utatumaliza.
6.12
Kwa upande mwingine wapo wenzetu ambao tayari wameathirika na wengine
wamekufa. Tuwatunze walioathirika
bila ya ubaguzi na tuwahudumie mayatima wa waliokufa kwa ukimwi kama watoto
wetu.
6.13
Wale ambao wanashaka, wajitokeze, wapime damu zao na wapate ushauri
nasaha ili waweze kuishi kwa matumaini.
Aidha, Serikali imo katika hatua za mwisho za ukamilishaji wa sheria ya
kuanzishwa kwa Tume ya Ukimwi Zanzibar (ZACAIDS). Kazi kubwa ya Tume ya Ukimwi Zanzibar itakuwa ni kuhakikisha
utayarishaji na utekelezaji wa mikakati na sera za kupambana na ukimwi pamoja
na kuzuia kuenea kwa virusi na athari za ukimwi kwa jamii na kuwasaidia
walioathirika na janga hilo.
6.14
Napenda kuitumia fursa hii pia kuvipongeza vyombo, mashirika na watu
binafsi ambao wanajihusisha na kazi ya kupunguza kasi ya kuenea kwa
ukimwi. Jumuiya ya Umoja wa NGO -
Cluster, ZACP, Africare, USAID, UNICEF, UNDP na wengineo ni baadhi ya vyombo
tunavyosaidiana navyo katika vita hii.
6.15 Ndugu Wananchi,
niliyoyataja ni baadhi ya mambo machache ambayo
Serikali yenu imepanga kuyatekeleza katika mwaka ujao. Mafanikio ya utekelezaji yatategemea
sana mazingira ya kiuchumi na kijamii yatakavyokuwa. Mipango ya kiuchumi imetayarishwa. Kubwa ni kujenga mazingira ya kisiasa na kiutawala
kuhakikisha utekelezaji mzuri.
6.16 Ndugu Wananchi, nchi hii ni yetu sote kila
mmoja wetu ana haki na wajibu sawa na mwenziwe. Tafauti zote zilizokuwepo huko nyuma ziliondoshwa tarehe 12
Januari, 1964, siku ambayo nchi
yetu ilipata uhuru wa kweli na jamhuri na ndio tunaisherehekea hivi leo. Katika kipindi cha miaka 38, nchi yetu
imeshuhudia mabadiliko mengi ya maendeleo yakiwemo maendeleo ya kisiasa,
kiuchumi, kijamii na kadhalika.
6.17
Kwa upande wa siasa tumepiga hatua kubwa zaidi kwa vile hivi sasa Taifa
letu limefikia pahala ambapo tuna mfumo wa vyama vingi vya siasa unaosimamiwa
na Katiba yenyewe na Sheria zinazohusika na kadhalika. Hatua hii imetufanya Watanzania kuwa na
utajiri mkubwa wa vyama vya siasa lakini sio utajiri wa uchumi. Wamarekani wana vyama viwili tu vya
siasa, Chama cha "Democrats na Republican". Wenzetu hao wana umasikini wa vyama vya
siasa ukiwalinganisha nasi wenye zaidi ya vyama 12 lakini kwa upande wa uchumi
wamepiga hatua kubwa kushinda nchi zote nyengine duniani.
6.18
Naamini wakati umefika kwa Watanzania kuutumia vizuri utajiri wetu wa
vyama vya siasa kwa kuunganisha nguvu zetu na kuzielekeza kwenye juhudi za
kutafuta maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa nchi yetu na watu wake wote. Kwa hivyo natoa changa moto kwa viongozi
wa vyama, wafuasi wote na wananchi wote kwa jumla tuutumie wakati wetu vizuri
kwa kujenga maisha yetu sote na vizazi vijavyo. Inawezekana kila mmoja wetu atimize wajibu wake.
6.19
Tukijenga ushirikiano, na ushindani kwa misingi ya kuheshimiana na
uzalendo tutaweza kudumisha umoja, utulivu, amani, upendo na maendeleo kwa watu
wetu.
7.0 HITIMISHO:
7.1 Kwa
kumalizia, naomba tena nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
ujumbe wake kwa kuwa nasi siku hii ya leo. Pia nawashukuru viongozi wengine wote wa Kitaifa kwa kuungana
nasi katika kilele cha sherehe ya Mapinduzi mwaka huu.
7.2 Nawashukuru
mabalozi wa nchi za nje, wahisani mbali mbali waliopo na wasiokuwepo hapa leo
hii. Nazishukuru Serikali zote za nje zilizotusaidia wakati huu mgumu zikiwemo
Marekani, Uingereza, Ufaransa, Belgium, Sweden, India, Oman, Saudi Arabia,
Kuwait, UAE, Egypt, Libya, Tunisia, Japan na kadhalika. Shukurani maalum nazitoa kwa Serikali
ya ndugu zetu wa China, kwa misaada ya hali na mali pamoja na msamaha wa madeni
kwa Zanzibar na Tanzania. Kadhalika
nazishukuru taasisi za Kimataifa, World Bank, IMF, UNDP, UNESCO, UNIDO, WFP,
FAO, ILO, WHO, ADB, OPEC, BADEA, KUWAIT FUND na SAUD FUND kwa mashirikiano
mazuri tuliyonayo pamoja na misaada yao muhimu ya maendeleo kwetu. Mwisho kabisa nawashukuru sana wananchi wote kwa kunisikiliza kwa
makini.
7.3 Nawatakieni
nyote kheri za mwaka mpya.
Ahsanteni.
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
MAPINDUZI DAIMA