HOTUBA
YA WAZIRI WA NCHI OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UBINAFSISHAJI, MHESHIMIWA Dk.
ABDALLAH OMARI KIGODA (MB), AKIWASILISHA BUNGENI TAARIFA YA HALI YA UCHUMI WA
TAIFA KATIKA MWAKA 2002, NA MAPENDEKEZO YA MPANGO WA MUDA WA KATI NA MFUMO WA
MATUMIZI YA SERIKALI KWA KIPINDI CHA MWAKA 2003/04-2005/06
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako
Tukufu sasa likae kama kamati ili liweze kupokea na kujadili Taarifa ya Hali ya
Uchumi wa Taifa katika mwaka 2002 na Mapendekezo ya Mpango wa Muda wa Kati na
Mfumo wa Matumizi ya Serikali kwa kipindi cha mwaka 2003/04-2005/06. Pamoja na hotuba hii nawasilisha Kitabu cha
Hali ya Uchumi katika Mwaka 2002 na Kitabu cha Mpango wa Maendeleo wa mwaka
2003/04.
2. Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza
kutoa Taarifa nilizozitaja hapo juu napenda kutoa shukrani zangu kwa Kamati ya
Bunge ya Fedha na Uchumi ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. Njelu Kasaka, Mbunge
wa Lupa kwa mchango mkubwa iliotoa wakati ikijadili Muhtasari wa Hotuba hii
ambao umetuwezesha kuboresha kazi yetu.
Aidha, napenda kuchukua fursa hii kutoa shukrani kwa viongozi na
wafanyakazi wenzetu wa Wizara ya Fedha
pamoja na wadau wengineo ambao tumefanya nao kazi bega kwa bega
kutayarisha Taarifa hii na Mpango wa Maendeleo.
3. Mheshimiwa Spika, mwisho napenda kutoa shukrani zangu kwa Dk. E. S. Bukuku, Katibu Mkuu, Mipango na Ubinafsishaji, Naibu Katibu Mkuu, Bwana O. M. S. Bendera, Wakurugenzi, Viongozi wa asasi na wafanyakazi wote wa Mipango na Ubinafsishaji ambao wamefanya kazi kwa bidii na kufanikisha utayarishaji wa Taarifa hii na mpango huu.
4. Mheshimiwa Spika, sasa naomba kuchukua nafasi hii kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa majina kwa kushinda katika uchaguzi mdogo uliofanyika mwezi Mei, mwaka huu. Mheshimiwa Abu Towagale Kiwanga (Mb.), CCM, Jimbo la Kilombero, Mhe. Nazir Mustafa Karamagi (Mb.), CCM, Jimbo la Bukoba Vijijini, Mhe. Ndeka E. Nziriye (Mb.), CCM, Jimbo la Kigoma Kusini, Mhe. Sumri Abdallah Salum Mohamed (Mb.), CCM, Jimbo la Mpanda Magharibi, Mhe. Karim Said Othman (Mb.), CUF, Jimbo la Chambani, Mhe. Masoud Abdalla Salim (Mb.), CUF, Jimbo la Mtambile, Mhe. Mohamed Juma Khatib (Mb.), CUF, Jimbo la Chonga, Mhe. Ali Said Salim (Mb.), CUF, Jimbo la Ziwani, Mhe. Shoka Khamis Juma (Mb.), CUF, Jimbo la Micheweni, Mhe. Salim Omar Ali (Mb.), CUF, Jimbo la Tumbe, Mhe. Mchande Salim Mchande (Mb.), CUF, Jimbo la Konde, Mhe. Khamis Ali Saleh (Mb.), CUF, Jimbo la Mgogoni, Mhe. Mohamed Ali Said (Mb.), CUF, Jimbo la Wingwi, Mhe. Khalifa Suleiman Khalifa (Mb.), CUF, Jimbo la Gando, Mhe. Khalifa Mohammed Issa (Mb.), CUF, Jimbo la Mtambwe, Mhe. Bakar Shamis Faki (Mb.), CUF, Jimbo la Ole, Mhe. Mwadini Abass Jecha (Mb.), CUF, Jimbo la Utaani, Mhe. Ali Said Juma (Mb.), CUF, Jimbo la Kojani; na, Mhe. Omar Juma Omar (Mb.), CUF, Jimbo la Pandani.
5. Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, Mipango na Ubinafsishaji, imekua ikishughulikia na kufuatilia maeneo makuu matatu ya jumla: Eneo la kwanza ni lile la kuona kuwa uchumi wetu unakua kwa viwango na kasi kubwa ikilinganishwa na mwaka uliopita. Tunaamini kuwa kama sharti moja la kupambana vyema na changamoto ya kupunguza umaskini ni viashiria vya uchumi jumla (macro economic fundamentals) kukua na kuwa tulivu. Tunaelewa hili ni sharti la lazima ingawaje sio ufumbuzi pekee wa kuboresha maisha ya Mtanzania. Katika eneo hili kama tutakavyoona tumepata mafanikio sio tu kwa ukuaji wa Pato la Taifa lakini takwimu zinatuonyesha pia ukuaji umetokea kwa karibu sekta zote.
6. Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni ile changamoto ya kuhakikisha ni jinsi gani mafanikio haya tunayoyapata katika kutekeleza sera za uchumi jumla yanatiririka na kuwanufaisha wananchi hususan vijijini. Hata hivyo jitihada na hatua za Serikali za utekelezaji wa Mkakati wa Kupunguza Umaskini zimeonyesha dalili nzuri za kupunguza umaskini usio wa kipato baina ya wananchi. Aidha programu zilizopangwa kutekelezwa chini ya sekta ya kilimo; kwa mfano, Mkakati wa Kuendeleza Sekta ya Kilimo pamoja na taratibu za kuanzisha skimu za utoaji wa mikopo kwa wale wenye vipato vya chini (micro credit schemes); azma ya Serikali ya kutekeleza Sera ya Uwezeshaji pamoja na Urekebishaji wa Utendaji kazi wa Halmashauri zetu za Wilaya; vitasaidia sana kupunguza umaskini wa kipato baina ya watu hasa vijijini. Changamoto kubwa ni kwa kila mwenye uwezo wa kufanya kazi afanye kazi kwa bidii, tija na ufanisi na Serikali itimize majukumu yake ya utawala bora na uwekaji wa mazingira bora.
7. Mheshimiwa Spika, eneo la tatu pamoja na lile la kuratibu mipango Kitaifa, ni lile la Uwekezaji na Ubinafsishaji. Tunaamini uwekezaji utasaidia sana katika kukuza ujenzi wa mtaji wa taifa na hivyo kukuza uchumi wetu. Mazingira tuliyojiwekea ya kuvutia wawekezaji wa ndani na nje yatabidi yawe endelevu, pamoja na kuimarisha taratibu za kutoa upendeleo wa makusudi kwa Watanzania wazalendo. Takwimu za uwekezaji kama tutakavyoziona zinaonyesha kutuelekeza kwenye upendeleo huo. Zoezi la ubinafsishaji linalenga katika urekebishaji wa utendaji wa viwanda na mashirika yetu. Mafanikio yamepatikana na vile vile yapo matatizo mbali mbali ambayo bado yanabakia ni changamoto kwa Serikali. Medani za uchumi zinaelekeza kuwa zoezi la ubinafsishaji ni asilimia ndogo tu ya hatua za urekebishaji uchumi zinazochukuliwa na nchi. Hivi sasa nchini Tanzania zoezi hili linakaribia hatma, ila changamoto tuliyonayo ni vipi tutahakikisha kuwa mafanikio yaliyokwishapatikana katika zoezi hili yanakuwa endelevu. Ipo haja kwa Serikali kuendelea kuweka mazingira bora ya sera ya fedha (monetary) na sera za kodi (fiscal) ili kuwezesha wamiliki kufanya kazi zao kwa tija na ufanisi. Takwimu zinatuonyesha kuwa kati ya viwanda vilivyobinafsishwa, karibu asilimia 51 vinamilikiwa na Watanzania.
8. Mheshimiwa Spika, hata hivyo tumegundua kwamba kwa baadhi ya Watanzania makini (serious) wanaomiliki viwanda hivi wamekumbwa na matatizo yafuatayo: Kwanza, mtaji mkubwa wa kifedha unaohitajika kubadilisha mitambo na mashine zilizopitwa na wakati zilizokuwa katika viwanda wanavyomiliki ni mzigo mkubwa. Mzigo huu unawafanya wasianze kufanya kazi kwa kuendana na teknolojia ya kisasa hivyo kushindwa kumudu ushindani wa soko. Pili, gharama kubwa za uzalishaji zinazotokana au na madeni yaliyorithiwa au na gharama za uendeshaji hasa zinazotokana na bei kubwa za umeme. Tatu, udhaifu katika menejimenti na ujuzi. Mwisho, udhaifu tuliorithi wa kutohimili utamaduni mpya wa Watanzania wazawa kumiliki viwanda na ule wa kushindwa kutayarisha michanganuo yakinifu ya miradi ambayo inaweza kupata mikopo kutoka mabenki. Inawezekana kabisa ipo haja ya makusudi kwa Serikali kutafuta sasa taratibu za kuwapunguzia mizigo hii, hususan wawekezaji Watanzania ili waweze kuvifufua viwanda hivi kwa ukamilifu ili vifanye kazi, hasa kwa wale wawekezaji Watanzania ambao ni makini. Kwa hiyo, ipo haja ya msingi kwa Serikali kutafakari na kubuni njia na taratibu zinazoweza kuchukuliwa ili kuwapunguzia wawekezaji Watanzania: bei ya manunuzi ya mashirika hayo; kufuta madeni yanayowasibu; kuwaongezea muda wa kulipa madeni yao na mwisho kuwapa uwezo wa kupata mikopo kutoka mabenki au taasisi nyinginezo za fedha ili kuendeshea na kutekelezea mipango yao ya uwekezaji na biashara.
9. Mheshimiwa Spika, nilipowasilisha Taarifa ya Hali ya Uchumi kwa mwaka 2001 na Mapendekezo ya Mpango wa Muda wa Kati na Mfumo wa Matumizi ya Serikali kwa Kipindi cha mwaka 2002/03 – 2004/05, nililitaarifu Bunge lako Tukufu juu ya malengo ya uchumi jumla kwa mwaka 2002/03 kama ifuatavyo:
·
Pato la Taifa halisi kukua kwa asilimia 5.9 mwaka
2002 na asilimia 6.3 mwaka 2003;
·
Kuwa na kiwango cha kasi ya upandaji bei kisichozidi
asilimia 4.2 ifikapo Juni, 2003;
·
Kuongeza mapato ya ndani ya Serikali kwa uwiano wa
Pato la Taifa wa asilimia 12.3 mwaka 2002/03;
·
Kukidhi ujazi wa fedha (M2) kwa viwango
vinavyowiana na malengo ya ukuaji wa uchumi na kupunguza kasi ya upandaji bei;
na,
·
Kuongeza akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango cha
kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma toka nje kwa kipindi
kisichopungua miezi minne.
Ukuaji wa Uchumi
10. Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa vigezo na viashirio vya msingi vya
uchumi jumla (macro economic fundamentals) Pato la Taifa lilikua kwa asilimia
6.2 mwaka 2002, ikilinganishwa na asilimia 5.7 mwaka 2001. Ukuaji huu wa uchumi
ni zaidi ya lengo lililowekwa la asilimia 5.9 kwa mwaka 2002.
11. Mheshimiwa
Spika, kiwango tulichofikia cha ukuaji wa uchumi kwa
wastani wa asilimia 5.6 kwa miaka mitatu iliyopita ukilinganisha na kile cha
asilimia 3.4 kwa wastani kwa nchi za Afrika kinatia moyo. Hata hivyo ukuaji huo bado ni mdogo mno
kuweza kukidhi mahitaji yatokanayo na ongezeko la idadi ya watu la asilimia 2.9
kwa mwaka na kutoa ufumbuzi wa matatizo yetu kama vile ukosefu wa ajira na
umaskini. Njia kuu ya kuinua kiwango
cha kukua kwa uchumi wetu ni kuongeza juhudi, maarifa na ubunifu katika ngazi
zote za jamii. Serikali itaendelea
kuweka mazingira bora, lakini tegemeo kuu la kukua kwa uchumi wetu ni pamoja
na: kuongeza kiwango cha uwekaji akiba; kuongeza kasi ya ongezeko la mitaji; kuongeza
kasi ya mauzo nje; na, wananchi wenyewe kufanya kazi kwa bidii.
Kasi ya Upandaji Bei
12. Mheshimiwa
Spika, kasi ya upandaji bei iliendelea kupungua na
kufikia asilimia 4.3 mwezi April 2003,
ikilinganishwa na asilimia 4.5 mwezi Juni 2002. Kupungua kwa mwenendo wa kasi ya upandaji bei kunatokana hasa na
hali nzuri ya upatikanaji wa mapato, mazao na usambazaji wa chakula, pamoja na
sera za makusudi za kudhibiti mwenendo wa mapato na matumizi ya Serikali na
ujazi wa fedha nchini.
13. Mheshimiwa Spika, kushuka kwa kasi ya upandaji bei kutoka asilimia 30 mwaka 1995 na kufikia asilimia 4.3 kumetuletea manufaa makubwa kama vile kutengemaa kwa uchumi; kuvutia wawekezaji, na kuboresha ufanisi wa sekta ya fedha. Kutokana na ongezeko katika ubora wa bidhaa zetu sasa tunaweza kuuza nje baadhi ya bidhaa kama vile saruji, nyaya na transfoma za umeme, bia, sigara, na mablanketi. Hata hivyo, kutokana na kutokuwepo kwa ongezeko linaloridhisha la pato halisi (disposable income) kwa wananchi walio wengi vijijini na mijini, kushuka kwa kasi ya upandaji bei hakujaleta manufaa makubwa kwa wananchi wengi. Kazi kubwa ni kuongeza uzalishaji wa bidhaa na utoaji huduma mbali mbali pamoja na uwezo wa wananchi wa kununua bidhaa na huduma hizo.
14. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha Juni – Desemba 2002 ujazi wa fedha kwa maana pana
(M2) uliongezeka kwa asilimia 13.0 ikiwa karibu sawa na kiwango cha
lengo la asilimia 12.0 katika mwaka 2002/03.
Katika kipindi hicho mikopo kwa Serikali iliongezeka kwa asilimia 30.4,
ikilinganishwa na kupungua kwa asilimia 11.1 katika kipindi kama hicho mwaka
2001. Mwenendo huo ulitokana na ongezeko la mauzo ya dhima za Serikali. Mikopo
kwa sekta binafsi iliongezeka kwa asilimia 18.4, ikilinganishwa na ongezeko la asilimia
6.6 katika kipindi kama hicho mwaka 2001.
Wastani wa riba za mikopo zinazotozwa na mabenki ya biashara ulipungua
kidogo na kufikia asilimia 15.7 mwezi Desemba 2002 kutoka asilimia 16.4 mwezi
Juni 2002. Wastani wa riba inayotolewa
kwa amana ulipungua na kufikia asilimia 3.1 mwezi Desemba 2002 kutoka asilimia
3.5 mwezi Juni 2002.
15. Mheshimiwa
Spika, kiwango cha ujazi wa
fedha kilichofikiwa katika mwaka 2002 cha asilimia 13.0 kinaashiria kwamba uchumi wetu unakaribia kuanza kuwa na
nguvu za kujirekebisha wenyewe na kufanya kazi ipasavyo; yaani uchumi ambao
ujazi wake wa fedha unaendana na ongezeko la uzalishaji na viwango vya huduma
zinazotolewa nchini, mabenki yanayotoa mikopo kwa riba za kadri, sekta za
uzalishaji zinazofanya kazi kwa ufanisi na fedha yenye thamani ndani na nje ya
nchi.
Akiba ya Fedha za Kigeni
16. Mheshimiwa Spika, akiba ya fedha za kigeni iliongezeka kwa asilimia 32.3 na
kufikia dola 1,529.9 milioni mwaka 2002 kutoka dola 1,156.6 milioni mwaka
2001. Kiasi hiki ni sawa na uwezo wa
kuagiza bidhaa kutoka nje kwa miezi 8.9 ikilinganishwa na miezi 6.3 mwaka 2001.
Thamani ya Shilingi
17. Mheshimiwa Spika, thamani ya shilingi ya Tanzania kwa dola moja ya Marekani ilipungua kwa asilimia 7.6 kutoka Sh. 888.9 kwa dola ya Marekani mwishoni mwa Juni 2001 hadi Sh. 956.8 kwa dola ya Marekani mwishoni mwa Juni 2002. Thamani iliendelea kupungua kwa kasi hadi kufikia shilingi 1040 kwa dola ya Marekani mwezi Mei 2003. Kupungua huku kwa thamani ya shilingi kulisababishwa kwa kiasi kikubwa na kasi ndogo ya mauzo nje na kuendelea kushuka kwa bei za bidhaa asilia katika soko la dunia. Njia kuu ya kuimarisha thamani ya shillingi ni kuongeza mauzo nje.
BAJETI
YA SERIKALI
Mapato
18. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka 2001/02 makusanyo ya mapato
ya ndani kupitia kodi za mapato, ushuru wa forodha, kodi ya ongezeko la thamani
(VAT), na mapato kutokana na vyanzo vingine yalikuwa asilimia 12.2 tu ya Pato
la Taifa, ambayo yanalingana na ya mwaka 2000/01. Malengo ya muda wa kati ya sera ya kodi kuendelea ni kuongeza
uwezo wa Serikali wa kukusanya mapato kwa kuongeza vyanzo vya kodi, kupambana
na ukwepaji kodi, kudhibiti misamaha ya kodi pamoja na kuimarisha usimamizi ili
kufikia kiwango cha asilimia 13.2 ya Pato la Taifa kwa mwaka 2003/04.
Matumizi
19. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2001/02 matumizi makubwa ya Serikali
yalielekezwa katika kupunguza umaskini na kukuza uchumi. Sekta na maeneo yaliyopewa kipaumbele
yaligawiwa fedha karibu zote zilizokuwa zimekadiriwa.
Deni la Taifa
20. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwishoni
mwa Desemba 2002, deni la taifa lilikuwa dola za Marekani 8.9 bilioni sawa na
ongezeko la asilimia 7.2 ikilinganishwa na deni la dola 8.3 bilioni mwishoni
mwa mwaka 2001. Kati ya fedha hizo, deni la nje ni dola za kimarekani 8.0 bilioni
au asilimia 89.9, na lile la ndani ni dola 0.9 bilioni sawa na asilimia
10.1. Ongezeko la deni linatokana hasa
na kupevuka kwa madeni ya nyuma.
21. Mheshimiwa
Spika, Mkakati wa Deni la Taifa unaolenga katika
kuimarisha usimamizi wa madeni ya nje na ndani ulizinduliwa mwezi Agosti 2002.
Mkakati huu unabainisha mwongozo na maelekezo ya ukopaji nje, ukiwa na lengo la
kuhakikisha kwamba mzigo wa madeni ya nje utakuwa stahimilivu (debt
sustainability).
22. Mauzo
na Uagizaji Bidhaa Nje
Mheshimiwa Spika, thamani
ya mauzo ya bidhaa nje mwaka 2002 iliongezeka kwa asilimia 16.25 na kufikia
dola 902.55 milioni, ikilinganishwa na dola 776.4 milioni mwaka 2001. Ongezeko hilo lilichangiwa hasa na mauzo ya
bidhaa zisizo asilia kama vile madini, mazao ya samaki na bidhaa za viwandani
ambazo zilichangia asilimia 77.16, ikilinganishwa na asilimia 70.1 mwaka
2001. Kwa ujumla thamani ya bidhaa
asilia karibu zote zilishuka kutokana na kupungua kwa bei katika soko la dunia
na hivyo kuchangia asilimia 22.8 tu ya jumla ya mauzo nje, ikilinganishwa na
asilimia 29.9 mwaka 2001. Thamani ya
uagizaji toka nje ilikuwa dola 1,511.3 milioni mwaka 2002, ikilinganishwa na
dola 1,560.5 milioni mwaka 2001. Kupungua huko kulitokana na kupungua kwa
uagizaji wa bidhaa za mitambo hususan kwenye sekta ya madini na chakula.
Mkakati wa Kuongeza Mauzo Nje
23. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002 mwenendo wa mauzo na uagizaji bidhaa nje
umeendelea kuonyesha nakisi katika urari wa biashara ya nje japokuwa
imepungua. Ili kupunguza nakisi serikali
inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga katika kukuza mauzo ya
bidhaa nje. Itakumbukwa kwamba mnamo
Julai 2002, Bunge lilipitisha sheria ya kuanzisha maeneo huru ya uzalishaji
bidhaa kwa ajili ya kuuza nje (EPZ).
Baada ya sheria hiyo kupitishwa na Bunge, Serikali ilikamilisha
utayarishaji wa kanuni zinazoongoza uanzishaji na usimamizi wa maeneo
hayo. Kutokana na jitihada hizi Kiwanda
cha nguo cha NIDA-Tabata, Dar-es-Salaam kimepata usajili wa EPZ na
kuzinduliwa. Aidha viwanda vya Nguo vya
Urafiki na kile cha Ubungo Millennium vinaendelezwa ili kusajiliwa. Ili kukuza mauzo nje ni muhimu kuendelea
kutekeleza kwa dhati mkakati wa kukuza mauzo nje kwa kuboresha miundo mbinu,
ujuzi, masoko, utangazaji wa bidhaa, ubora wa viwango, n.k.
SEKTA YA NJE
HALI YA UCHUMI DUNIANI NA
USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
Ukuaji wa Uchumi:
24. Mheshimiwa Spika, licha ya misukosuko mingi duniani, pato la dunia lilikua kwa
asilimia 3.0 katika mwaka 2002, ikilinganishwa na asilimia 2.3 katika mwaka
2001. Kwa nchi zilizoendelea pato
lilikua kwa asilimia 1.8 mwaka 2002 ikilinganishwa na asilimia 0.8 katika mwaka
2001. Nchi zinazoendelea pato lake liliongezeka kwa asilimia 4.6, kutoka
ongezeko la asilimia 3.6 mwaka 2001 wakati ongezeko la pato la bara la Afrika
lilipungua kutoka asilimia 3.6 mwaka 2001, hadi asilimia 3.4 mwaka 2002. Aidha, katika baadhi ya nchi za Afrika,
kutozingatiwa kwa suala la usimamizi mzuri wa uchumi; migogoro ya kisiasa
katika nchi nyingi za Afrika, tatizo la magonjwa na ukame wa 2002 vilichangia
kulegalega kwa uwekezaji na shughuli za kiuchumi barani Afrika.
Mwelekeo wa Ukuaji wa
Uchumi Duniani katika Kipindi cha Mwaka 2003/04
25. Mheshimiwa
Spika, mwelekeo wa ukuaji wa uchumi duniani kwa kipindi
cha muda mfupi ujao siyo wa kuridhisha kutokana na matatizo ya kiusalama na
afya kwa maana ya kuongezeka kwa wasiwasi wa ugaidi, machafuko ya kisiasa
katika maeneo ya Mashariki ya Kati, Bara la Afrika na baadhi ya nchi za Amerika
Kusini; na kuongezeka kwa athari za UKIMWI na kuibuka kwa ugonjwa wa Severe Acute Respiratory Syndrome
(SARS). Matatizo haya mawili yanaweza
kuathiri biashara yetu ya utalii na uwekezaji.
Serikali inachukua hatua zinazostahili ili kukabiliana na matatizo haya
na kutoa taarifa sahihi ndani na nje ya nchi.
Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)
26. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002,
Jumuiya ya Afrika Mashariki iliendelea na: maandalizi ya itifaki ya ushuru wa
pamoja wa forodha ambayo imepangwa kukamilika mwezi Novemba 2003; jitihada za
kukuza biashara na uwekezaji rasilimali; na, taratibu za kufungua masoko ya
mitaji na mizania ya malipo na nchi za nje hususan kwenye masoko ya mitaji ya
Dar es Salaam, Nairobi na Kampala. Rasimu ya Sera na Mkakati wa Sekta ya Kilimo
na Maendeleo Vijijini ilikamilishwa kwa lengo la kuendeleza ushirikiano katika
kilimo, usalama na uhakika wa chakula na mchanganuo wa fursa za Bonde la Ziwa
Victoria kama Eneo Maalum la kukuza Uchumi ulikamilishwa (Economic Growth
Zone). Katika mpango wa muda wa kati
maeneo haya yataendelea kupewa kipaumbele.
JUMUIYA YA MAENDELEO YA
NCHI ZA KUSINI MWA AFRIKA (SADC)
27. Mheshimiwa
Spika, Tanzania ilikuwa mwenyeji wa mkutano wa mawaziri
wa SADC uliofanyika Zanzibar mwezi Februari, 2002 ambao pamoja na mambo mengine
uliazimia kufanyika kwa mkutano wa kutathmini fursa za uwekezaji vitega uchumi
kusini mwa Afrika unaotarajiwa kufanyika mjini London Uingereza mwezi Julai,
2003.
28. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002, SADC ilikamilisha rasimu ya kwanza ya Mkakati wa
Mpango wa Maendeleo ya Ushirikiano (Regional Indicative Strategic Development
Plan – RISDP). Mpango huu unalenga:
kuondoa umaskini; ushiriki sawa wa maendeleo; utandawazi; maendeleo endelevu;
pamoja na, masuala yanayohusu jinsia ili yapatiwe ufumbuzi wa pamoja.
29. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Azimio na Mkataba wa Jumuiya ya nchi za Kusini mwa Afrika (Declaration and Treaty) mwaka 2002, Serikali ya Tanzania iliridhia itifaki zinazohusu Maendeleo ya Utalii; Afya; Kulinda na Kuhifadhi Wanyamapori; Siasa na Ushirikiano katika Ulinzi; Udhibiti wa Silaha Ndogo Ndogo; pamoja na itifaki ya Taratibu za Kuendesha shughuli za Jumuiya. Aidha, kwa mwaka 2003/04 SADC itakamilisha zoezi la muundo wake kulingana na majukumu yake mapya.
MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA
SEKTA MUHIMU
SEKTA ZA UZALISHAJI
Sekta ya Kilimo
30. Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa ukuaji
kisekta (sectoral growth) katika mwaka 2002, sekta ya
kilimo ilikua kwa asilimia 5.0 ikiwa ni pungufu kidogo, ikilinganishwa na
ukuaji wa asilimia 5.5 mwaka 2001.
Ukuaji huo ulitokana zaidi na ukuaji katika sekta ndogo ya mifugo
(asilimia 3.5), misitu na uwindaji (asilimia 3.0) na uvuvi (asilimia 6.5).
Sekta ndogo ya mazao ya kilimo, ilikua kwa asilimia 6.2 mwaka 2002 ikiwa ni
chini ya ukuaji wa asilimia 7.3 mwaka 2001.
31. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka 2002/2003 Serikali iliendelea kuweka msingi
utakaowezesha sekta ya kilimo kuongoza katika kukuza uchumi, kuongeza nafasi za
ajira na kupunguza umaskini nchini kupitia:-
·
Kukamilisha programu ya kutekeleza mkakati wa
kuendeleza sekta ya kilimo;
·
Mpango kamambe wa kuimarisha kilimo cha umwagiliaji
nchini uliokamilishwa mwezi Oktoba, 2002.
Ili mpango huu uwe wa manufaa hapana budi kuziwezesha wilaya, kata na
vijiji kuandaa mipango shirikishi ya utekelezaji katika ngazi hizo ili kujenga
dhana ya umiliki (ownership);
·
Kuainisha mfumo wa kodi wa Serikali kuu na Serikali
za mitaa kwa nia ya kupunguza kodi wanazotozwa wakulima;
·
Kukarabati barabara na madaraja vijijini yaliyopewa
kipaumbele chini ya mkakati wa kupunguza umaskini, ili kupunguza gharama za
uzalishaji katika sekta ya kilimo;
·
Kueneza kwa mtandao wa simu katika vijiji vingi
mwaka 2002 kwa lengo la kurahisisha mawasiliano kwa wakulima wanapotafuta
masoko kwa ajili ya mazao yao, pembejeo na zana za kilimo;
·
Kuelimisha wawekezaji juu ya kufutwa kwa malimbikizo
ya madeni ya kodi ya ardhi iliyokuwa inatozwa kwa shillingi 600 kwa ekari hapo
awali ikilinganishwa na kiwango cha sasa cha shilingi 200 tu kwa ekari;
·
Taasisi za kifedha zimehimizwa kutoa mikopo kwa
wakulima wakubwa na wadogo nchini na kuhamasisha wananchi kuungana ili
kuanzisha benki za ushirika na jamii.
Aidha azma ya Serikali, ni kuhamasisha uanzishaji wa Benki ya Maendeleo
itakayohudumia kilimo;
·
Kuongeza bajeti kwa ajili ya kukusanya takwimu
muhimu katika sekta ya kilimo, kwa hiyo kuwezesha kufuatilia mwenendo wa sekta.
32. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2003/04 ni azma ya Serikali kuendelea na jitihada zake za
kuweka mazingira mazuri yatakayowezesha taifa kufanya mageuzi katika kilimo.
Lakini ni dhahiri kwamba jitihada pekee zinazofanywa na Serikali haziwezi kuongeza
tija na kuleta mageuzi yanayotarajiwa katika kilimo. Ninaamini tunaweza kufanikiwa katika kuleta mageuzi katika sekta
ya kilimo kwa muda mfupi iwapo wadau katika sekta ya kilimo watatimiza wajibu
wao kikamilifu. Serikali kwa upande
wake itaendelea kuweka mazingira ya kuvutia uwekezaji katika sekta ya kilimo
kwa kuimarisha ugani, kuainisha na kupunguza kodi, kuhimiza taasisi za kifedha
kutoa mikopo, kutoa motisha, kusaidia wakulima kupata masoko na kurahisisha
upatikanaji wa zana na pembejeo; na kwa upande mwingine kama mabenki na taasisi
za kifedha zitatoa mikopo; wakulima wataanzisha vyama vya ushirika
vitakavyorahisisha upatikanaji wa pembejeo kwa bei nafuu; sekta binafsi
zitaanzisha viwanda vidogo vya kusindika mazao ya wakulima; mikoa na wilaya
zitasimamia kikamilifu utayarishaji na utekelezaji Mipango ya Maendeleo ya
Sekta ya kilimo; na Mashirika yasiyo ya kiserikali na madhehebu ya dini na
yatahamasisha wananchi kwa bidii kwa nia ya kubadilisha fikra zao kuhusu
kilimo.
33. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
mwaka 2002 sekta ya viwanda ilikua kwa asilimia 8.0 ikilinganishwa na ukuaji wa
asilimia 5.0 mwaka 2001. Kufufuliwa kwa baadhi ya viwanda na ongezeko la
uzalishaji na tija ni miongoni mwa sababu za ukuaji huu.
34. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002 sekta ya viwanda iliongoza kwa kuvutia wawekezaji
wengi zaidi wa ndani na nje ikilinganishwa na sekta nyingine ambapo jumla ya
miradi ya viwanda 103 iliidhinishwa na Kituo cha Uwekezaji yenye thamani ya
shilingi 195,072 milioni, ikilinganishwa na miradi 82 iliyopitishwa mwaka 2001
yenye uwezo wa kutoa nafasi za ajira kwa watu 15,685. Ni jambo la kutia moyo kuona kuwa sekta binafsi nchini inakua na
kuwekeza kwani kati ya miradi ya viwanda iliyoidhinishwa miradi 35 ilikuwa ya wawekezaji
binafsi wa ndani, miradi 42 ya wawekezaji wa nje na miradi 26 ikiwa ni ya ubia
ya wawekezaji wa ndani na nje.
35. Mheshimiwa
Spika, Serikali inakusudia kwa mwaka 2003/04 kutekeleza Sera ya Viwanda
Vidogo na vya Kati ili kuongeza nafasi za ajira; kuboresha mazingira ili
kuvutia wawekezaji kwenye viwanda vinavyoongeza thamani ya bidhaa na mauzo nje
hususan kwenye sekta ya nguo, ngozi na usindikaji wa matunda na mboga na
vifungashio.
Sekta ya Madini
36. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002 sekta ya madini ilikua
kwa asilimia 15.0, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 13.5 katika mwaka
2001. Mchango wa sekta ya madini katika
Pato la Taifa mwaka 2002, uliongezeka na kufikia asilimia 2.7, ikilinganishwa
na asilimia 2.5 mwaka 2001. Katika
mpango wa muda wa kati na mrefu Sekta ya madini inatarajiwa kuongeza nafasi za
ajira, mapato zaidi kwa Serikali, kuendeleza sekta ya viwanda, kuchangia katika
Pato la Taifa na upatikanaji wa fedha za kigeni, na hatimaye kuchangia katika
kupunguza umaskini.
37. Mheshimiwa Spika, mauzo ya madini nchi za nje mwaka 2002
yalifikia kiasi cha dola 372.8 milioni, ikilinganishwa na dola 302.2 milioni
mwaka 2001, sawa na ongezeko la asilimia 23.3. Mchango mkubwa wa zaidi ya
asilimia 88.5 ulitokana na mauzo ya dhahabu ambayo yameongezeka kutokana na
wawekezaji wengi wa nje na ndani wenye mitaji na teknolojia ya kisasa.
38. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2003/04 sekta ya madini itaendelea na
jitihada za kutekeleza sera ya madini ya mwaka 1997, na sheria ya madini ya
mwaka 1998 vyote vikilenga katika kutoa nafasi za ajira na kuongeza uzalishaji
wa madini. Aidha, Serikali itahakikisha
kwamba amani na utulivu kati ya wawekezaji wakubwa na wadogo vinadumishwa, na
kuwa jamii zilizopo karibu na migodi ya madini zinafaidika na miundo mbinu na
huduma za kijamii muhimu kama vile barabara, shule, huduma za afya, maji, na
umeme. Serikali pia itaendelea kuimarisha utoaji wa huduma muhimu za uchimbaji
na uuzaji wa madini kwa wachimbaji wadogo.
39. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002 sekta ya uuzaji jumla, reja reja na
mahoteli ikijumuisha utalii ilikua kwa asilimia 7.0, ikilinganishwa na ukuaji
wa asilimia 6.7 mwaka 2001. Ongezeko hili limetokana na maendeleo ya kuridhisha
ya upatikanaji wa bidhaa hapa nchini. Aidha, hali ya biashara ya utalii nayo
ilichangia kwa kiasi kikubwa kwenye ongezeko hili hasa kutokana na jitihada za
utangazaji wa vivutio vya utalii ndani na nje ya nchi. Pia, Serikali iliandaa
kongomano la kwanza kimataifa la wawekezaji kwenye sekta ya utalii mwezi
Oktoba, 2002.
40. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2003/04 Serikali
itaendelea kuweka mkazo katika utangazaji wa vivutio vya utalii ndani na nje
katika masoko asilia na mapya, ikiwa ni pamoja na kuhimiza uwekezaji katika
sekta ya utalii, kuboresha huduma za utalii, kuimarisha miundo mbinu muhimu ya
utalii na kudumisha usalama wa wageni na mali zao.
Sekta ya
Ujenzi
41. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002, sekta ya ujenzi ilikua kwa asilimia 11.0,
ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 8.7 mwaka 2001. Ukuaji huu ulitokana na ujenzi, matengenezo na ukarabati wa
barabara kuu na za vijijini, madaraja madogo, ujenzi wa majengo ya nyumba za
kuishi na ya biashara na majengo ya shule za msingi na kukamilika kwa daraja la
mto Rufiji.
Barabara
na Madaraja
42. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa 2002 Serikali ilikamilisha
na kuanza utekelezaji wa sera ya ujenzi pamoja na mpango kamambe wa miaka kumi
wa maendeleo ya sekta ya barabara nchini. Aidha, Serikali imeanza utekelezaji
wa miradi mingi ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya barabara kuu kwa kiwango
cha lami kwa kutumia zaidi fedha zake za ndani. Waheshimiwa Wabunge watakumbuka
kwamba Mheshimiwa Rais William Benjamin Mkapa hivi karibuni amefungua miradi
hiyo ikiwemo barabara za Mtukula – Muhutwe – Kagoma (136 km), Songwe – Tunduma
(70 km), Shelui – Nzega ( 108 km), Chalinze _ Melela (129 km), Mkuranga –
Kibiti (60 km), Somanga – Masaninga (33 km) na daraja la mto Matandu.
43. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa barabara za vijijini, jumla
ya madaraja 180 na kilometa 3,780 zilifanyiwa matengenezo mwaka 2002
ikilinganishwa na madaraja 73 na kilometa 3,573 zilizofanyiwa matengenezo mwaka
2001. Pia, Serikali ilikamilisha maandalizi ya taarifa ya mkakati wa
utekelezaji wa barabara za Jumuiya Afrika Mashariki mnamo mwezi Novemba, 2002,
na kuiwasilisha kwenye mkutano wa wahisani uliofanyika Arusha tarehe 29 Aprili,
2003. Tanzania itafaidika sana na programu hii ambayo zaidi ya asilimia 75 ya
barabara zilizopewa kipaumbele zipo nchini. Mfano, barabara kuu ambazo zipo
katika mpango huu ni :
44. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2003/04 Serikali itaendelea
kuweka mkazo katika ujenzi, matengenezo na ukarabati wa madaraja na barabara
kuu na zile za vijijini zilizopewa kipaumbele chini Mkakati wa Kupunguza Umaskini
na wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Utekelezaji wa shughuli hizi
utaishirikisha sekta binafsi kwa kiwango kikubwa.
45. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002 sekta ya mawasiliano na
uchukuzi ilikua kwa kiwango cha asilimia 6.4 ikilinganishwa na asilimia 6.3
mwaka 2001. Viwango hivi vinaonyesha
kuanza kuimarika kwa huduma za mawasiliano kwa njia ya simu na uchukuzi kwa
njia za barabara na anga ambazo sasa zinamilikiwa kwa kiwango kikubwa na sekta
binafsi hivyo kufanya utoaji wa huduma kuwa wa ufanisi. Hali hii imechangia kuongezeka kwa mchango
wa sekta hii katika Pato la Taifa kutoka asilimia 5.4 mwaka 2001 hadi asilimia
5.5 mwaka 2002.
46. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2003/2004 sekta
hii itaendelea kuboresha usafiri wa abiria na uchukuzi wa mizigo kwa pande zote
za mijini na vijijini. Aidha, usafiri
kwa njia za reli na majini na taratibu bora za usalama kwa usafiri wa vyombo
vyote utaimarishwa.
Sekta ya Nishati
47. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2002 Serikali iliendelea
kufanya marekebisho ya kisera na urekebishaji wa muundo na uendeshaji wa
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). Aidha, Serikali itaendelea na jitihada za
kuendeleza na nishati mbadala ambazo zinaendelea kutumika na kufanyiwa utafiti
zaidi za micro-hydro, upepo tungamotaka, bayogesi, mionzi ya jua na
makaa ya mawe.
48. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa sekta ndogo ya gesi,
Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia na wahisani wengine imekamilisha
makubaliano ya uendelezaji wa Mradi wa Gesi ya Songosongo. Utekelezaji wa Mradi huu ulioanza mwezi
Oktoba 2002 utajenga mtambo na bomba la kupitisha gesi kutoka Songosongo hadi
Dar es Salaam. Mradi huu utakamilika ifikapo
mwishoni mwa mwaka 2004.
HUDUMA ZA JAMII
49. Mheshimiwa
Spika, katika jitihada za Serikali za kuhakikisha kuwa mafanikio ya ukuaji
wa uchumi jumla yanatiririka kwa wananchi wengi vijijini, imeanzisha kwa
makusudi Mpango wa Kupunguza Umaskini kupitia uboreshaji wa huduma za
jamii. Lengo la Serikali ni kupunguza
umaskini usio wa kipato, pamoja na ule wa kipato.
Sekta
ya Elimu
50. Mheshimiwa
Spika, katika
kipindi cha 2002/03 Serikali iliendelea kuimarisha mazingira ya elimu kwa
kushirikisha asasi mbalimbali. Aidha, mashirika na watu binafsi wamejitokeza
zaidi katika kujenga na kutoa elimu ya awali, elimu ya msingi, sekondari na
elimu ya juu.
51. Mheshimiwa Spika, kutokana na
utekelezaji wa
Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) mwaka 2002, madarasa 15,991
yalijengwa kutokana na juhudi kubwa zilizofanywa na wananchi na kupita lengo
lililopangwa la madarasa 13,868. Uandikishaji wa watoto wote walioko shuleni
umefikia asilimia 98.6 na watoto wa rika ya elimu ya msingi (miaka 7-13),
walioko shuleni umefikia asilimia 80.7 ikiwa inakaribia lengo la asilimia 85
lililowekwa kwa mwaka 2003. Aidha, takwimu zinaonesha kwamba, idadi ya
wanafunzi katika shule za msingi za Serikali na za binafsi iliongezeka kwa
asilimia 23, kati yao waliokuwa wanasoma shule za binafsi waliongezeka zaidi ya
mara tatu. Ili kukidhi mahitaji ya
wanafunzi, shule za Serikali ziliongezeka kwa asilimia 4.8 na walimu nao kwa
asilimia 5.8.
52. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa elimu ya sekondari
uwezo wa kuingia sekondari umeongezeka toka asilimia 19.5 mwaka 2001 hadi
asilimia 21.7 mwaka 2002. Idadi ya wasichana wanaojiunga na kidato cha tano pia
imeongezeka toka asilimia 38 hadi asilimia 42 na Serikali chini ya Mpango wa
Elimu ya Sekondari iliwalipia ada wasichana 4,367 wa kidato cha I-VI ambao
wanajiweza kimasomo lakini wazazi wao hawana uwezo wa kulipa karo. Aidha, kazi zilizoendelea kufanyika katika
ngazi ya elimu ya juu na ufundi, ni pamoja na kuboresha utoaji wa mafunzo
mbalimbali katika vyuo vya elimu ya juu na kuvipandisha hadhi baadhi ya vyuo.
53. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2003/04, mpango wa maendeleo katika sekta
ya elimu utaendelea kuweka mkazo katika kuimarisha mazingira ya kutoa elimu na
mafunzo katika ngazi zote. Jitihada zaidi zitawekwa katika kuongeza
uandikishaji wa wanafunzi unaoenda sambamba na kujenga na kukarabati madarasa
na nyumba za walimu na kuajiri walimu wapya.
Sekta ya Maji
54. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002
Serikali iliridhia utekelezaji wa sera mpya ya maji yenye lengo la kupatikana
maji kwa urahisi ili wananchi wapate
muda wa kujishughulisha na uzalishaji maji ili kuboresha maisha yao na
hivyo kupiga vita umaskini.
55. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
mwaka 2002, jumla ya vyanzo vya
kuchepua maji 4849 vilitambuliwa katika mabonde ya mto Rufiji, Mto Pangani na
Ziwa Victoria. Kati ya hivyo 1773
vimetolewa hati, na 3076 havijapata hati za haki ya kumiliki maji. Aidha, hadi Desemba, 2002 jumla ya visima
virefu 369 vilichimbwa katika maeneo mbalimbali nchini, na vyombo 1278 vya
kuchimba na kutafuta maji viliundwa.
56. Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa
majisafi na salama kwa wananchi waishio vijijini katika mwaka 2002 ulifikia
asilimia 53 ikiwa ni ongezeko la asilimia 3 ikilinganishwa na mwaka 2001.
Huduma ya majisafi mjini iliongezeka na kufikia asilimia 73 ikilinganishwa na
asilimia 70 ya mwaka 2001. Ongezeko hili linatokana na kukamilika kwa mradi
mkubwa wa maji wa mji wa Dodoma ambao ulizinduliwa Desemba 2002 pamoja na
utekelezaji wa mradi wa dharura wa maji wa mji wa Shinyanga. Pia, ukodishaji wa DAWASA umekamilika chini
ya Kampuni ya Dar es Salaam City Water Services kwa kipindi cha miaka kumi na
inatarajia kuanza kazi rasmi mwezi Julai 2003.
57. Mheshimiwa
Spika, ili kuongeza ufanisi, Serikali itaendelea kuhamasisha mashirika ya
kitaifa na kimataifa, mashirika yasiyo ya kiserikali, watu binafsi na wananchi
wenyewe kuchangia, na kushiriki katika ujenzi na ukarabati wa miradi ya maji
vijijini. Lengo la sekta ya maji ni kutoa huduma ya maji safi, salama na ya
kutosha kwa sehemu za mijini na vijijini ili kuongeza idadi ya watu wanaopata
maji toka asilimia 50 mwaka 2002/03 hadi asilimia 55 mwaka 2003/04. Sekta ya maji pia inalenga kuimarisha na
kulinda vyanzo vya maji.
60. Mheshimiwa
Spika, kwa kipindi
cha mwaka 2003/04 sekta ya afya itaanza kutekeleza mpango wa pili wa Mkakati wa
Sekta ya Afya. Mpango huu unalenga
katika kuboresha utoaji wa huduma, na umuhimu utawekwa katika kukarabati vituo
vya afya, kutoa tiba na kuhakikisha kuwa watu wengi zaidi wanapata kwa urahisi zaidi
wa huduma za afya ya msingi. Pia mkazo
utaendelea kuwekwa kwenye kutoa huduma za mama, watoto na watu wasiojiweza
pamoja na udhibiti wa magonjwa ya kuambukiza na milipuko.
UKUAJI WA SEKTA BINAFSI NA UWEKEZAJI
61. Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2002/03 Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji Rasilimali imeendelea kuhamasisha
na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kwa kuzidi kujenga mazingira bora
ya uwekezaji na kuboresha huduma mbali mbali kwa wawekezaji kwa mtindo wa “One
stop Centre”. Aidha katika kipindi cha
mwaka 2002 Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji na kwa kushirikiana na Shirika
la Maendeleo ya Viwanda la Umoja wa Mataifa (UNIDO) kilianzisha mpango maalumu
wa kuwawezesha wawekezaji wa ndani (Domestic Investors Capacity Building)
kuboresha nyaraka za mipango ya biashara (Bankable Business Plans) na kuinadi
kwa wawekezaji wa ndani na nje ili waweze kupata aidha mikopo, wabia au
teknolojia. Kwa sasa zaidi ya miradi 60
ya wawekezaji wa ndani inatangazwa duniani kote kwa ajili hiyo.
62. Mheshimiwa Spika,
katika kutekeleza majukumu yake ya kuwapatia wawekezaji ardhi kama
ilivyoainishwa katika kifungu cha 20 cha Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999, Kituo
cha Uwekezaji na kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Makazi na Maendeleo
Mijini kimeainisha ardhi inayofaa kwa uwekezaji. Tayari ekari milioni 4 zimepatikana na uhakiki wa aina ya umilikaji wa maeneo hayo unaendelea
kufanywa na maafisa wa Serikali katika mikoa yote ya Tanzania bara. Napenda kusisitiza ya kwamba hakuna
Mtanzania atakayenyang’anywa ardhi ili apewe mgeni bali Mtanzania husika ndiye
atakayeitumia ardhi hiyo kumwezesha kuwekeza.
63. Mheshimiwa Spika, Aidha
katika mwaka 2002 Kituo cha Uwekezaji kiliandikisha miradi 311 yenye thamani ya
Sh. 1,024.5 milioni. Kati ya miradi
hiyo, 126 ni ya wawekezaji wa ndani, 104 ni ya wawekezaji wa nje, na 81 ni
wawekezaji wabia. Vile vile, katika
kipindi hicho (2002) idadi ya wawekezaji waliohudumiwa kwa kupatiwa vibali
mbali mbali ni 260 kwa masuala ya kodi, 243 kwa masuala ya uanzishaji makampuni
na 214 leseni za biashara, 926 walipatiwa vibali vya kufanya kazi nchini
(Resident Permit Class “B”), 976 walipatiwa vibali vya kuishi nchini na 61 kwa
masuala ya ardhi.
64. Mheshimiwa Spika,
katika kutekeleza Mkakati wa kukuza ushiriki wa sekta binafsi katika uchumi
Serikali kwa mwaka 2002/03 ilishughulika na:-
65. Mheshimiwa Spika, katika
kipindi cha mwaka 2002/2003, Serikali kwa kushauriana na sekta binafsi chini ya
Baraza la Biashara la Taifa (TNBC) imepitia sera na sheria mbalimbali za
kibiashara na uwekezaji. Masuala
yaliyoshughulikiwa ni pamoja na:-
§
Kuandaa mapendekezo ya kurekebisha Sheria za Ardhi ili kurahisisha
utolewaji wa mikopo;
§
Kuanzisha mfumo wa Hazina ya Ardhi (Land Bank) ili kukuza uwekezaji
katika kilimo;
§
Kuhuisha Sheria za Ajira;
§
Kurekebisha mfumo wa kodi ili kuondoa adha ya utozaji wa kodi nyingi na
kupunguza kero kwa wazalishaji; na,
§
Kupunguza urasimu katika kutoa leseni na kushirikisha sekta binafsi
katika majadiliano ya mikataba ya kimataifa inayohusiana na biashara na
uwekezaji.
66. Mheshimiwa Spika, kiwango cha uwekezaji rasilimali kimeongezeka kutoka asilimia 14.8 ya
Pato la Taifa mwaka 1997, na kufikia asilimia 17.4 mwaka 2002. Hata hivyo,
uwekezaji rasilimali nchini bado ni mdogo ikilinganishwa na mahitaji ya
ongezeko la haraka la ukuaji wa uchumi.
Uwiano unaohitajika wa uwekezaji akiba na Pato la Taifa kwa nchi changa
kama Tanzania ili ipate kuendelea kwa kasi zaidi ni asilimia 25. Kwa mwaka 2003, Serikali itaendelea kuweka
mazingira mazuri ya uwekezaji na taratibu zitakazowezesha shughuli ndogo ndogo
za uzalishaji na biashara zipate mikopo.
Uwekaji
Akiba
67. Mheshimiwa Spika,
licha ya ongezeko dogo la uwekezaji rasilimali nchini, bado maendeleo yetu kwa
ujumla ni madogo kutokana na ukosefu wa utamaduni wa kujiwekea akiba. Uwiano
kati ya uwekaji akiba nchini na Pato la Taifa kwa mwaka 2002 ni asilimia 11.1
tu, ambapo katika nchi nyingine kama
Kenya ni asilimia 17, Uganda asilimia 14.7, Nigeria na Afrika Kusini
asilimia 18, Korea na China zaidi ya asilimia 30. Ni wajibu wetu Waheshimiwa
Wabunge, kuhamasisha wananchi kwenye Majimbo yetu kujiwekea akiba na kuanzisha
vitega uchumi vitakavyowawezesha kuondokana na umaskini. Aidha ni wajibu wetu pia kuwahamasisha
wananchi kujenga utamaduni na nidhamu katika kukopa, kutumia vizuri na
kurejesha mikopo hiyo.
UREKEBISHAJI NA UBINAFSISHAJI WA MASHIRIKA YA UMMA
68. Mheshimiwa
Spika,
hadi Machi
2003 mashirika ya umma yaliyobinafsishwa, yakijumuisha 47 yaliyopelekwa LART ni
266. Kati ya mashirika hayo mashirika
134 yamenunuliwa na Watanzania kwa asilimia 100, mashirika 16 yamepata
wawekezaji wa nje kwa asilimia 100 na mashirika 116 yamebinafsishwa kwa njia ya
ubia kati ya wawekezaji wa nje na wawekezaji wa ndani. Mashirika 16 kati ya
mashirika yaliyonunuliwa na Watanzania yamebinafsishwa kwa njia ya kuwauzia
wafanyakazi wa mashirika husika. Hali kadhalika mali nyinginezo
(Non-core-assets) 265 ziliuzwa.
69. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2002, kazi zaidi ilielekezwa katika kuandaa mikakati
mbalimbali ya kubinafsisha au kurekebisha mashirika ya miundombinu na huduma
yakiwemo DAWASA, ATC, TANESCO, THA, TRC, NIC na NMB. Hadi Februari 2003 Serikali iliweza kubinafsisha shirika la Ndege
la Tanzania (ATC) kwa njia ya ubia na DAWASA kwa njia ya ukodishaji.
70. Mheshimiwa Spika, katika
kudhibiti mashirika makubwa yanayotoa huduma na ya miundombinu, Serikali
imechukua hatua ya kuanzisha mamlaka nne za udhibiti: Mamlaka ya udhibiti wa nishati
na maji – EWURA, Mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa nchi kavu na majini -
SUMATRA, Mamlaka ya udhibiti wa mawasiliano na utangazaji – TACRA, na Mamlaka
ya udhibiti wa usafiri wa anga - TCAA. Aidha, kwa mwaka 2003/04
Serikali itaendelea na ubinafsishaji wa mashirika makubwa ya huduma na
miundombinu na mashamba makubwa ya kilimo na mifugo. Serikali pia itaendelea
kufuatilia mashirika yaliyobinafishwa kuhakikisha kuwa mashirika hayo yanafanya
kazi kwa ufanisi kulingana na mikataba ya mauzo.
Mkakati wa Kupunguza Umaskini
71. Mheshimiwa
Spika, uchambuzi wa takwimu na taarifa zilizotokana na
tafiti za mapato na matumizi ya kaya (HBS 2000/01) na tafiti za nguvukazi (ILFS
2000/01) umebainisha kuwa hali ya umaskini wa kipato na maendeleo ya jamii
(elimu, afya, maji, ajira, nyumba) haijabadilika sana. Matokeo ya tafiti hizo yanaonyesha kuwa
asilimia 19 ya watu wana umaskini uliokithiri (food poverty) mwaka 2000/01,
ikilinganishwa na asilimia 22 mwaka 1991/92. Vile vile, asilimia 36 ya watu ni
maskini kutokana na kukosa mahitaji muhimu (basic needs poverty) mwaka 2000/01
ikilinganishwa na asilimia 39 mwaka 1991/92.
Bado lindi la umaskini liko vijijini.
Aidha, tofauti ya kipato imeongezeka sana Dar es Salaam. Utekelezaji wa
Mkakati wa Kupunguza Umaskini umeanza kuonyesha mafanikio hasa katika sekta ya
elimu na katika baadhi za viashirio katika sekta ya afya, maji mijini, na
barabara vijijini.
72. Mheshimiwa Spika, changamoto iliyoko
mbele yetu katika suala zima la kupunguza umaskini ni:-
73. Mheshimiwa
Spika, sensa ya watu na makazi ilifanyika kuanzia tarehe
25 Agosti 2002 hadi 4 Septemba 2002 kama ilivyopangwa. Ripoti ya kwanza ya jumla ilitolewa rasmi
mwezi wa Januari, 2003. Kwa mujibu wa
ripoti hiyo ya jumla, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa na idadi ya watu
wapatao 34.6 milioni iliyoongezeka kwa asilimia 2.9 kwa mwaka kati ya mwaka
1988 na 2002. Katika jumla hiyo karibu
watu 17.7 milioni ni wanawake na watu 16.9 milioni ni wanaume. Aidha katika jumla yote watu milioni 33.6
walikuwapo Tanzania Bara (wakiwemo wanawake 17.2 milioni na wanaume 16.4) na
watu 985,000 walikuwepo Tanzania Visiwani (wakiwemo wanawake 502,000 na wanaume
483,000). Matokeo ya sensa pia
yamedhihirisha kwamba Tanzania Visiwani ina kiwango kikubwa cha ukuaji wa idadi
ya watu wa asilimia 3.1 kwa mwaka kuliko Tanzania bara ambayo kiwango cha
ukuaji wa idadi ya watu kilikuwa ni asilimia 2.9 kwa mwaka.
74. Mheshimiwa
Spika, kufanikiwa kwa zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2002,
kumetokana na ushirikiano wa hali ya juu pamoja na juhudi za viongozi wote
kwenye ngazi mbali mbali za Serikali, taasisi, wafadhili na wananchi wote kwa
jumla. Napenda kuchukua nafasi hii
kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge, Watanzania wote, na wafadhili wetu UNFPA, DFID,
UNDP, USAID, SIDA, na Serikali ya Japan kwa kuwa mstari wa mbele katika
kusaidia zoezi la sensa. Kwa mwaka
2003/04, Serikali itaendelea kukamilisha ripoti 11 zenye takwimu na taarifa
mbali mbali za sensa na kuhakikisha kuwa zinawafikia watumiaji katika ngazi na
nyanja mbali mbali.
Nguvukazi na Ajira
75. Mheshimiwa
Spika, matokeo ya Utafiti wa Nguvukazi wa mwaka 2000/01
yanaonyesha kuwa kati ya watu 17.8 milioni wenye uwezo wa kufanya kazi,
walioajiriwa kwa tafsiri ya kitaifa walikuwa 15.5 milioni. Tafsiri hii
inazingatia mazingira ya ajira katika Tanzania ambapo sehemu kubwa ya watu
wanafanya kazi za kujiajiri badala ya kuajiriwa, na kazi nyingi ni za msimu
kwenye sekta ya kilimo na sekta isiyo rasmi. Kati ya hao walioajiriwa, watu
13.0 milioni walikuwa katika kilimo cha asili, 0.9 milioni katika sekta isiyo
rasmi, 0.6 milioni katika sekta binafsi, 0.5 milioni katika kazi za nyumbani,
0.4 milioni Serikalini na 0.1 milioni katika mashirika ya umma.
76. Mheshimiwa Spika, watu wasio na kazi walikuwa 2.3 milioni, sawa na asilimia
12.9 kwa nchi nzima. Kati ya hao, wanawake walikuwa 1.3 milioni na wanaume 1.0
milioni. Karibu nusu ya wasiokuwa na kazi walikuwa wakiishi mijini. Katika Jiji
la Dar es Salaam peke yake, asilimia 46.5 ya wenye uwezo wa kufanya kazi
walikuwa hawana kazi, ambapo katika miji mingine ni asilimia 25.5 na vijijini
asilimia 8.4. Pia, matokeo yameonyesha kuwa ukosefu wa ajira unawaathiri zaidi
vijana wenye umri kati ya miaka 10 na 34. Kijinsia vijana wa kike ndio
wanaoathirika zaidi kuliko wanaume.
77. Mheshimiwa
Spika, matokeo haya yanabainisha wazi kuwa sekta ya kilimo,
sekta isiyo rasmi na sekta binafsi ndizo zinazoajiri watu wengi zaidi. Hivyo
juhudi za Serikali zitaendelea kulenga katika kuboresha kilimo na kuwezesha
uwekezaji katika viwanda vya kusindika mazao ili kuyaongezea thamani. Aidha, Vyuo vya Majaribio ya Ufundi
vitahimizwa kutoa mafunzo yanayohitajika katika soko la ajira. Kwa kuwa viwanda vya nguo vina fursa ya
kuajiri watu wengi, Serikali itaendelea kutoa motisha kwa viwanda kama hivyo
vitakavyoajiri watu wengi.
JINSIA
78. Mheshimiwa
Spika, sensa ya watu na makazi ya
mwezi Agosti/Septemba 2002 ilibainisha kwamba idadi ya wanawake nchini ni
17,156,905 sawa na asilimia 51.1 ya watu 33,584,607 waishio Tanzania Bara. Kwa
kuzingatia mchango mkubwa unaotolewa na wanawake katika kukuza uchumi na kuleta
maendeleo, Serikali ikishirikiana na taasisi isiyo ya kiserikali ya mtandao wa
jinsia nchini (TGNP) katika mwaka 2002 ilishughulikia masuala yafuatayo:-
·
Kuhakikisha kwamba masuala
ya jinsia yanazingatiwa katika utayarishaji na utekelezaji wa mipango na katika
usimamizi wa uchumi katika ngazi zote;
·
Kutathimini idadi ya
wanawake walio katika ngazi ya uongozi katika ngazi zote za wizara, mikoa na
Serikali za mitaa kwa lengo la kuleta usawa; na,
·
Kutoa mafunzo kwa wanawake
katika nyanja mbali mbali.
79. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi kijacho, Serikali ikishirikiana na taasisi mbalimbali
zinazoshughulikia masuala ya jinsia itaendelea na zoezi la kujenga uwezo wa
kitaalam wa kuandaa, kuchambua na kutekeleza mipango kwa kuzingatia masuala ya
jinsia katika ngazi mbalimbali.
80. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2002
idadi ya wananchi walioambukizwa, iliendelea kuongezeka na kufikia watu 2.2
milioni. Idadi hii ni sawa na asilimia
6.5 ya wananchi wote. Kati ya idadi hiyo ya watu walioambukizwa, theluthi moja
ambayo ni zaidi ya watu 700,000 tayari ni wagonjwa. Kinachotisha zaidi ni kwamba kasi ya maambukizi hayo haijapungua
kutoka ile ya mwaka jana ambayo ni asilimia 7 hadi 10 kwa maeneo ya mashambani
na asilimia 20 hadi 24 katika sehemu za mijini. Takwimu zinazonyesha kwamba
maambukizi mijini yako juu. Mwaka 2002
pia umeshuhudia utekelezaji wa sera na Mkakati wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI
pamoja na kupanua mtandao wa wadau katika vita dhidi ya UKIMWI.
81. Mheshimiwa
Spika, kwa mwaka 2003/04 Serikali itaendelea kusisitiza
na kulifanya suala la kupambana na UKIMWI kuwa agenda ya kudumu katika sehemu
zote za kazi ili kupunguza athari ya kuangamia kwa nguvukazi nchini.
MATARAJIO KWA MWAKA
2003/04
Misingi na Malengo ya
Mpango na Bajeti
82. Mheshimiwa
Spika, malengo ya uchumi jumla katika mwaka 2003/04 – 2005/06 yatakuwa kama
ifuatavyo:-
SHABAHA NA MAENEO YATAKAYOPEWA KIPAUMBELE KATIKA MPANGO NA BAJETI YA
MWAKA 2003/04
83. Mheshimiwa Spika, shabaha kuu ya mpango na bajeti ya mwaka 2003/04 ni
kutekeleza Mkakati wa Kupunguza Umaskini, kuendeleza mafanikio ya uchumi jumla
yaliyopatikana hadi sasa, kukuza sekta binafsi na kuimarisha Serikali za Mitaa
kwa kuzipatia madaraka na rasilimali zaidi.
Ili kufikia malengo ya uchumi jumla na ya kisekta Serikali imeweka
mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na:-
·
Kukuza uzalishaji na uboreshaji huduma katika sekta
za viwanda, madini, utalii na sekta isiyo rasmi;
·
Kutolegeza sera ya udhibiti wa ujazi wa fedha;
·
Kukuza na kuendeleza sekta binafsi ili iweze
kuchangia kwa kiasi kikubwa katika Pato la Taifa;
·
Kuweka mazingira mazuri ya kibiashara kwa kuimarisha
sera pamoja na taratibu mbalimbali; na
84. Mheshimiwa Spika, maeneo yaliyopewa kipaumbele
katika Mpango na Bajeti ya Mwaka 2003/04 ni pamoja na:-
i)
Kuboresha huduma za kijamii na kuimarisha
Miundombinu Sekta zilizopewa kipaumbele ni:- Elimu,
afya, maji, barabara na madaraja vijijini na huduma za ardhi;
ii)
Kilimo
Mkazo umewekwa
kwenye kilimo cha umwagiliaji kwa kufufua skimu za asili za kisasa za
umwagiliaji wa wakulima wadogo wadogo na uvunaji wa maji ya mvua na kutekeleza
kwa nguvu mikakati yote ya kuendeleza kilimo;
MAJUMUISHO
85. Mheshimiwa
Spika, naomba nimalizie kwa kusisitiza kwamba licha ya dalili kadhaa za
mafanikio kuonekana kama vile: uchumi wetu kukua kwa asilimia 6.2 katika mwaka
2002; kasi ya upandaji bei kushuka hadi kufikia asilimia 4.3; akiba ya fedha
zetu za kigeni kuongezeka na kutosha kulipia bidhaa na huduma kutoka nje ya
nchi kwa kipindi cha zaidi ya miezi sita; na kiwango cha uwekezaji rasilimali
kuongezeka na kufikia asilimia 17.4 ya Pato la Taifa mwaka 2002; bado uchumi unakabiliwa
na changamoto na matatizo mbali mbali ambayo hatuna budi kuyatatua. Matatizo yanayokabili uchumi wetu hivi sasa
ni pamoja na Bajeti tegemezi, umaskini vijijini na mijini, ukosefu wa utamaduni
wa kujiwekea akiba, uwekezaji mdogo wa rasilimali, ukosefu wa ajira,
miundombinu hafifu na huduma duni za kijamii.
86. Mheshimiwa
Spika, ili tuweze kuondokana na matatizo niliyoyataja,
hatuna budi kutekeleza yafuatayo:-
(i) Kubaini
fursa zote za kuongeza ukusanyaji wa aina mbalimbali za mapato katika ngazi
zote ili kupunguza utegemezi na kutuwezesha kugharamia maendeleo yetu wenyewe
kwa kiasi kikubwa;
(ii) Kufanya
kazi kwa juhudi na maarifa kwa kutumia rasilimali zinazopatikana katika maeneo
yetu. Hivyo, Taifa, kila kijiji, kata, tarafa, Wilaya hadi ngazi ya mkoa,
walenge katika kubainisha yale wanayoweza kuyafanya kwa kutumia fursa na
rasilimali zilizoko katika maeneo yao;
(iii) Kujenga
utamaduni wa kujiwekea akiba ambayo itawezesha wananchi kuwekeza katika miradi
mbalimbali ya kuzalisha mali na kutoa huduma. Suala la uhamasishaji wa wananchi
kujiwekea akiba ni la msingi;
(iv) Kuelekeza
juhudi katika kujenga na kuendeleza shughuli ndogo ndogo za uzalishaji na
biashara zinazojumuisha usindikaji wa bidhaa asilia, viwanda vidogo na vya kati
na utoaji wa huduma mbalimbali. Ili
kufanikisha azma hii, hapana budi kuanzishwa vikundi mbalimbali vya uzalishaji
mali, kuvisaidia kupata mikopo na kujenga na kuendeleza ujasirimali;
(v) Kuboresha
mazingira ya uwekezaji wa sekta binafsi wa ndani na nje pamoja na kuweka
mkakati thabiti wa kuuza nje bidhaa zilizosindikwa na zisizo asilia kwa kutumia
fursa zote zilizopo kama vile AGOA, EBA na New Canadian Initiative ; na,
(vi) Serikali
itaendelea na utaratibu wa kuboresha mfumo wa ushuru na kodi mbali mbali kwa
Wakulima Vijijini ili kuwaondolea kero na usumbufu ili wajizatiti zaidi katika
uzalishaji na kuongeza viwango vya ubora ili kuongeza viwango vya mapato yao.
87. Mheshimiwa Spika, kama Waheshimiwa
Wabunge wajuavyo, azma ya Serikali ni kujenga na kudumisha ushirikiano mzuri na
wenye manufaa kwa maendeleo ya Taifa letu na nchi zote pamoja na mashirika na
taasisi za kimataifa. Zipo nchi,
mashirika na taasisi za kimataifa ambazo tumeendelea kushirikiana nazo na
zinastahili pongezi zetu. Hivyo, naomba
nitumie fursa hii kuwashukuru wote walioshirikiana nasi na kutusaidia. Baadhi ya nchi na mashirika ya kimataifa
yanayostahili pongezi zetu ni pamoja na:- Benki ya Dunia, Shirika la Fedha la
Kimataifa (IMF), Mashirika mbali mbali ya Umoja wa Mataifa kama vile UNDP,
UNESCO, UNFPA, UNHCR, UNICEF, UNIFEM, FAO, IFAD, WFP na WHO, Jumuiya ya nchi za
Ulaya (EU), mfuko wa fedha wa nchi wanachama wa uzalishaji mafuta (OPEC Fund),
Shirika la Maendeleo la Norway (NORAD), Shirika la Maendeleo la Marekani
(USAID), Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA), Shirika la Maendeleo la Finland
(FINNIDA), Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA), Shirika la Maendeleo la
Japan, Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB), Serikali za Uswisi, Uholanzi,
Ujerumani, Ufaransa, Uingereza, Hispania, China, Afrika ya Kusini, Japan,
Kuwait, Italia, Ireland na nchi nyingine marafiki na mashirika mbali mbali ya
Kimataifa yasiyo ya kiserikali (NGOs).
Tumeendelea kupata mchango mkubwa sana katika maendeleo yetu kutoka nchi
hizo na mashirika hayo. Napenda kutoa
shukrani zetu za dhati kwa nchi Wahisani na mashirika na taasisi mbali mbali za
kimataifa zinazotusaidia katika harakati zetu za maendeleo. Tunawaomba waendelee kushirikiana nasi na
kutusaidia katika juhudi zetu za kujenga uchumi imara na kuboresha maisha na
maendeleo ya wananchi wetu. Aidha,
mashirika hayo na nchi hizo, zinakubaliana na azma yetu na dhana ya kujenga national
capacity and local ownership katika uandaaji sera, mipango, mikakati na
miradi. Napenda pia nitumie nafasi hii
kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote kwa ushauri na ushirikiano wao
wanaoendelea kutupatia katika kutekeleza majukumu ya Ofisi ya Rais, Mipango na
Ubinafsishaji.
88. Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa Hoja.
|
Vigezo |
1995 |
1996 |
1997 |
1998 |
1999 |
2000 |
2001 |
2002 |
|
Ukuaji Halisi wa Pato la Taifa (%) |
3.6 |
4.2 |
3.3 |
4.0 |
4.7 |
4.9 |
5.7 |
6.2 |
|
Mfumuko wa bei
|
27.1 |
21.0 |
16.1 |
12.9 |
7.8 |
6.0 |
5.2 |
4.5 |
|
Kiwango cha wastani cha kubadilisha Sh/Dola |
574.8 |
580.0 |
612.1 |
664.7 |
744.8 |
808.4 |
876.4 |
978.9 |
|
Mauzo ya nje ya
bidhaa (mil. US$) |
682.9 |
763.8 |
752.6 |
588.5 |
543.3 |
663.3 |
776.4 |
877.0 |
|
Uagizaji wa bidhaa (mil. US$) |
1340.5 |
1212.6 |
1148.0 |
1382.2 |
1497.9 |
1366.3 |
1560.5 |
1506.5 |
|
Uwiano wa mauzo nje/ uagizaji bidhaa (%) |
50.9 |
63.0 |
65.6 |
42.6 |
39.7 |
49.6 |
52.0 |
58.7 |
|
Uwiano wa uwekezaji rasilimali /Pato la Taifa (%) |
19.7 |
16.5 |
14.7 |
16.0 |
15.4 |
17.5 |
17.2 |
- |
|
Akiba ya fedha za kigeni (Miezi ya Uagizaji Bidhaa) |
1.6 |
2.4 |
3.8 |
3.0 |
4.1 |
5.6 |
6.3 |
8.9 |
|
|
1995/96 |
1996/97 |
1997/98 |
1998/99 |
1999/00 |
2000/01 |
2001/02 |
2002/03 |
|
Nakisi ya Bajeti kabla ya ruzuku (% Pato la Taifa) |
0.1 |
-1.7 |
-2.3 |
-2.3 |
-5.8 |
-4.6 |
-6.6 |
|
|
Wastani wa riba za Amana za akiba |
12.0 |
11.0 |
10.0 |
7.9 |
7.1 |
4.2 |
3.5 |
3.1 |
|
Wastani wa riba za mikopo |
28.0 |
26.5 |
24.0 |
24.5 |
22.1 |
19.6 |
16.4 |
15.
7 |
Jedwali
Na 2: Ukuaji Halisi wa Pato la Taifa Kisekta na Malengo 1996 – 2006
|
Sekta |
1996 Halisi |
1997 Halisi |
1998 Halisi |
1999 Halisi |
2000 Halisi |
2001 Halisi |
|
Kilimo |
3.9 % |
2.4 % |
1.9 % |
4.1 % |
3.4 % |
5.5 % |
|
Uchimbaji wa Madini na mawe |
9.6 % |
17.1 % |
27.4 % |
9.1 % |
13.9 % |
13.5 % |
|
Bidhaa za Viwandani |
4.8 % |
5.0 % |
8.0 % |
3.6 % |
4.8 % |
5.0 % |
|
Umeme na Maji |
11.1 % |
2.2 % |
5.5 % |
3.9 % |
5.9 % |
3.0 % |
|
Ujenzi |
7.6 % |
35.5 % |
-12.3 % |
8.7 % |
8.4 % |
8.7 % |
|
Biashara , Uuzaji Jumla, Rejareja na Mahoteli |
3.5 % |
5.0 % |
4.7 % |
6.0 % |
6.5 % |
6.7 % |
|
Mawasiliano na Uchukuzi |
1.1 % |
-16.1 % |
32.8 % |
5.8 % |
6.1 % |
6.3 % |
|
Fedha, Bima na Huduma za Kibiashara |
0.4 % |
7.7 % |
5.6 % |
4.1 % |
4.7 % |
3.3 % |
|
Uendeshaji Serikali na Huduma Nyingine |
1.6 % |
3.2 % |
2.7 % |
3.5 % |
3.6 % |
3.5 % |
|
Ukuaji wa Pato la
Taifa kwa mwaka unaohusika |
4.2 % |
3.3 % |
4.0 % |
4.7 % |
4.9 % |
5.7 % |
|
Mwaka wa Fedha |
1995/96 |
1996/97 |
1997/98 |
1998/99 |
1999/00 |
2000/01 |
|
Ukuaji wa Pato la
Taifa kwa Mwaka wa Fedha |
3.9% |
3.7% |
3.7% |
4.4% |
4.8% |
5.3% |
|
Ukuaji wa Pato la
Taifa kwa Mwaka wa Fedha |
3.9% |
3.7% |
3.7% |
4.4% |
4.8% |
5.3% |
Linaendelea
Jedwali Na 2: Ukuaji Halisi wa Pato la Taifa Kisekta na
Malengo 1996 – 2006 – (linaendelea)
|
Sekta |
2002 Halisi |
2003 Malengo |
2004 Malengo |
2005 Malengo |
2006 Malengo |
|
Kilimo |
5.0 % |
5.3 % |
5.5 % |
5.4 % |
5.7 % |
|
Uchimbaji wa Madini na mawe |
15.0 % |
11.1 % |
10.2 % |
9.6 % |
9.5 % |
|
Bidhaa za Viwandani |
8.0 % |
6.9 % |
7.1 % |
8.1 % |
9.0 % |
|
Umeme na Maji |
3.1 % |
6.9 % |
7.1 % |
8.1 % |
7.9 % |
|
Ujenzi |
11.0 % |
4.8 % |
5.3 % |
6.7 % |
8.0 % |
|
Biashara , Uuzaji Jumla, Rejareja na Mahoteli |
7.0 % |
8.9 % |
9.6 % |
10.4 % |
10.8 % |
|
Mawasiliano na Uchukuzi |
6.4 % |
7.9 % |
8.3 % |
9.2 % |
9.9 % |
|
Fedha, Bima na Huduma za Kibiashara |
4.8 % |
6.3 % |
6.6 % |
7.0 % |
7.4 % |
|
Uendeshaji Serikali na Huduma Nyingine |
4.1 % |
4.1 % |
4.2 % |
4.2 % |
4.6 % |
|
Ukuaji wa Pato la
Taifa kwa mwaka unaohusika |
6.2 % |
6.3 % |
6.6 % |
7.0 % |
7.4 % |
|
Mwaka wa Fedha |
2001/02 |
2002/03 |
2003/04 |
2004/05 |
2005/06 |
|
Ukuaji wa Pato la
Taifa kwa Mwaka wa Fedha |
6.0% |
6.1% |
6.5% |
6.8% |
7.2% |
Chanzo:
Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Ofisi ya Rais Mipango na Ubinafsishaji
|
Bidhaa |
1999 |
2000 |
2001 |
2002 |
Badiliko 2001/02 |
|
Bidhaa Asilia |
|
|
|
|
|
|
Kahawa |
76.63 |
83.7 |
57.05 |
35.14 |
-38.4% |
|
Pamba |
28.46 |
38 |
33.7 |
28.15 |
-16.5% |
|
Katani |
7.26 |
5.6 |
6.68 |
6.65 |
-0.4% |
|
Chai |
24.65 |
32.7 |
29.03 |
29.35 |
1.1% |
|
Tumbaku |
43.44 |
38.4 |
35.69 |
50.50 |
41.5% |
|
Korosho |
100.89 |
84.4 |
56.58 |
46.26 |
-18.2% |
|
Karafuu |
19.86 |
10 |
12.32 |
5.40 |
-56.2% |
|
Jumla ndogo ya Bidhaa asilia |
301.18 |
292.8 |
231.05 |
201.46 |
-12.8% |
|
Bidhaa zisizo asilia |
|
|
|
|
|
|
Madini |
73.26 |
178.2 |
302.23 |
372.78 |
23.3% |
|
Bidhaa za Viwandani |
30.05 |
43.4 |
56.17 |
67.10 |
19.5% |
|
Samaki na Bidhaa zake |
56.75 |
76.3 |
96.77 |
116.76 |
20.7% |
|
Mazao ya mboga na Maua |
8.88 |
9.7 |
11.01 |
10.86 |
-1.4% |
|
Bidhaa nyinginezo |
72.74 |
62.9 |
79.34 |
108.09 |
36.2% |
|
Jumla ndogo ya bidhaa zisizo Asilia |
241.67 |
370.5 |
545.52 |
675.58 |
23.8% |
|
Jumla ya Mauzo ya Bidhaa Nje |
542.85 |
663.3 |
776.37 |
877.04 |
12.9% |
Chanzo: Benki Kuu ya Tanzania, Ofisi ya Rais,
Mipango na Ubinafsishaji
Jedwali Na. 4. Mizania ya Malipo na Nchi za Nje
USD mill.
|
|
1995 |
1996 |
1997 |
1998 |
1999 |
2000 |
2001 |
2002 |
|
|
Halisi |
Halisi |
Halisi |
Halisi |
Halisi |
Halisi |
Halisi |
Makisio |
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Urari wa biashara |
-657.6 |
-448.8 |
-395.4 |
-793.7 |
-954.6 |
-703.1 |
-784.1 |
-629.46 |
|
Bidhaa zilizouzwa |
682.9 |
763.8 |
752.6 |
588.5 |
543.3 |
663.2 |
776.4 |
877.04 |
|
Bidhaa zilizonunuliwa |
1340.5 |
1212.6 |
1148.0 |
1382.2 |
1497.9 |
1366.3 |
1560.5 |
1506.5 |
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Urari wa Huduma |
-216.9 |
-278.8 |
-317.9 |
-463.1 |
-158 |