HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI

MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) WAKATI WA

KUFUNGA MAFUNZO YA AWALI YA ASKARI MAGEREZA

KOZI NA. 18, CHUO CHA KIWIRA TUKUYU, MBEYA

TAREHE 30/3/2004

 

 

·       Kamishna Mkuu wa Magereza,

·       Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya,

·       Mkuu wa Chuo,

·       Maafisa wa Majeshi mbalimbali,

·       Wahitimu wa Mafunzo,

·       Wageni Waalikwa,

·       Mabibi na Mabwana.

 

Kwanza, napenda nianze kwa kutoa shukurani zangu za dhati kwa Uongozi wa Jeshi la Magereza nchini kwa kunipa fursa hii ya kuwa Mgeni Rasmi wa kufunga mafunzo haya.  Hii ni mara ya pili mfululizo kwangu kupata fursa kama hii kwani mwezi wa Februari mwaka huu nilikuwa Mgeni Rasmi katika shughuli ya kufunga mafunzo ya Uongozi Daraja la Kwanza Chuo cha Magereza, Ukonga, Dar es Salaam.

 

Napenda kuchukua fursa hii pia kuishukuru Jumuiya ya Chuo hiki kwa ujumla kwa niaba ya waalikwa wote, kwa mapokezi mazuri tuliyoyapata tangu tulipowasili hapa.

 

Aidha, napenda kuchukua fursa hii  kutoa shukrani na pongezi kwa wale wote waliohusika katika maonesho mbali mbali yaliyochangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha shughuli hii ya leo, ikiwa ni pamoja na gwaride rasmi la kuhitimisha mafunzo, onesho la Watoto wa Kituo cha Malezi, Kwaya, Brass Band, Shairi na Taarab.  Mambo hayo yote yamefanywa kwa ustadi mkubwa na kudhihirisha kwamba kulikuwepo na jitihada za hali ya juu katika maandalizi ya shughuli hii ya leo.  Nawapongeza sana.

 

Kabla ya kutekeleza jukumu lililonileta hapa la kuyafunga rasmi mafunzo haya, napenda nizungumze machache kwa Wahitimu.  Kwanza, kama alivyogusia Kamishna Mkuu wa Magereza hivi punde, ni muhimu sana mjue kwamba kumaliza kwenu mafunzo haya ya Awali siyo mwisho wa mafunzo yenu ya kazi hii ya Magereza.  Kiutaratibu, mnapaswa kuendelea na mafunzo yenu kwenye vituo mtakavyopangiwa, kwa kuoanisha nadharia na vitendo na pia kwa kujifunza kutoka kwa wale wenye uzoefu kazini.

 

Suala hili la mafunzo endelevu kazini baada ya Mafunzo ya Awali lina umuhimu wa pekee kwa chombo hiki kwa sababu, kazi ya kuwatunza binadamu ni kazi inayohitaji maamuzi ya busara yanayozingatia mchanganyiko wa sheria, taratibu na hali halisi inayojitokeza kwa wakati husika.  Katika hali hii, ujuzi na uzoefu wa muda mrefu ni hazina kubwa sana katika kufanikisha kazi za Jeshi hili.

 

Pamoja na suala hili la mafunzo endelevu, napenda pia niwaase wahitimu kuhusu umuhimu wa kujiendeleza katika taaluma nyingine zenye manufaa kwenye Jeshi hili.  Ni vyema muelewe kwamba, Jeshi hili linahitaji wasomi wa taaluma mbali mbali ili kufanikisha majukumu yake kisayansi zaidi siku hadi siku. Kwa sababu hii, mnayo fursa ya kujiendeleza katika nyanja zinazohitajika Jeshini, hususan baada ya kukamilisha muda wa mwaka mmoja wa kujijengea ujuzi wa kazi za msingi za Jeshi hili.  Natoa wito kwenu kuhakikisha mnaitumia vyema fursa hii ili mjihakikishie maendeleo kazini katika zama hizi za sayansi na teknolojia.  Msibweteke na ajira hii mliyoipata na kusahau kujiendeleza.

Jambo la pili ambalo ni vema mkalizingatia ni kuhusu mwelekeo wa sasa wa kijamii na kisiasa nchini na duniani kote na jinsi unavyoingiliana na shughuli za Jeshi lenu.  Nyote mnafahamu kwamba, ajenda za sasa duniani kote zimeegemea kwenye utawala wa sheria, haki za binadamu na uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa uwazi na ukweli.  Mwelekeo huu umesababisha watu kutambua zaidi haki na wajibu wao na hivyo kuleta hali ya uwajibikaji zaidi katika kazi za umma.  Nyote mnafahamu pia kwamba vyombo vya usimamizi na utekelezaji wa sheria yaani Polisi, Mahakama na Magereza ndivyo vyenye nafasi kubwa zaidi katika kulinda na kudumisha usalama katika jamii.

 

Ni kutokana na ukweli huu ninawajibika kuwaonya kuhusu athari za kutozingatia kikamilifu sheria na taratibu za kazi wakati wote na mahali popote mara mtakapofika kwenye vituo vyenu vya kazi.  Napenda ieleweke kwenu na kwa watumishi wengine wote kwamba, mnawajibika kufanya kazi zenu kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizopo na kwamba unyanyasaji wa wafungwa au ukiukaji wa maadili ya kazi kwa njia yoyote ile ni marufuku.

 

Katika kuimarisha uwezo wa Jeshi hili wa kuzingatia hali halisi iliyopo, Serikali ililiwezesha Jeshi kufanya kazi ya kuziboresha kanuni za kudumu za Magereza, yaani “Prisons Standing Orders” ambazo ndizo mwongozo wa shughuli za kila siku magerezani, vyuoni na kwenye ofisi zote za Magereza nchini.  Kazi hii ilifanywa na Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).  Serikali inaamini kwamba, toleo jipya la “Prisons Standing Orders” ambalo ndilo lilitumika kuendesha mafunzo haya yanayomalizika leo, litasaidia katika kuliweka Jeshi hili kwenye mwelekeo mzuri zaidi kulingana na wakati tulionao sasa.

Katika jitihada hizo hizo za kuboresha huduma za Jeshi hili serikali imesimamia utolewaji wa chapisho la Code of Conduct for Prisons Officers” ambalo licha ya kuwekwa ndani ya “Prisons Standing Orders”, limetolewa pia kwenye vijitabu vidogo vidogo vinavyogawiwa kwa kila askari nchini.  Kijitabu hiki ni maelekezo mahsusi ya maadili yanayopaswa kufuatwa na Askari Magereza ndani na nje ya kazi ili kumwezesha kila askari kufanya rejea ya haraka pale anapohitaji kupata ufumbuzi kwa jambo lolote.  Nadhani ni vyema nieleze hapa kwamba katika “Code of Conduct for Prisons Officers” msisitizo mkubwa umewekwa kuhusu uzito wa kosa la Trafficking, yaani mahusiano yasiyostahili baina ya askari na mfungwa, ambao kimsingi ni rushwa.  Imeelezwa wazi kuwa askari anapotenda kosa la Trafficking ni kwamba amesaliti kiapo chake cha uaminifu na utii moja kwa moja.

 

Hatua hizi za serikali za kusimamia uboreshaji wa PSO na uchapishaji wa “Code of Conduct for Prisons Officers” ni sehemu tu ya mpango kabambe wa serikali wa kuimarisha utoaji huduma wa Jeshi la Magereza, pamoja na taasisi nyingine za usimamizi na utekelezaji wa sheria hapa nchini, yaani Mahakama, Polisi na Magereza.  Katika mpango huo kwa upande wa Magereza, serikali tayari imekwishafanya tathmini ya mahitaji ya Jeshi hili katika kuliwezesha kutekeleza majukumu yake kulingana na viwango vinavyokubalika kimataifa.  Tathmini hiyo ilifanywa na wataalam wa kimataifa walioteuliwa na Umoja wa Mataifa kupitia Shirika lake la Mpango wa Maendeleo (UNDP) na tayari baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa kwenye tathmini hiyo yameanza kutekelezwa na yako katika hatua mbalimbali.

 

Mojawapo ya mapendekezo hayo ni umuhimu wa Jeshi hili kuunda upya mfumo wake wa mafunzo ya watumishi na kuboresha vyuo vyake, ili hatimaye kuwe na watumishi wenye uwezo unaotambulika kote duniani na pia kuwa na vyeti vinavyokubalika kote duniani.  Tayari Jeshi limekwishaunda upya mfumo wa Mafunzo ya Awali kwa kushirikiana na wataalam kutoka Kitivo cha Sheria, Chuo Kikuu cha D’Salaam na Taasisi ya Technikon ya Afrika Kusini.  Jitihada zinaendelea ili mafunzo ya uongozi ya madaraja yote nayo yapitiwe upya.  Tunategemea Jeshi hili litakuwa na watumishi wenye elimu ya ngazi ya vyeti (Certificates), Diploma na Shahada za ngazi mbalimbali, katika taaluma ya “Correctional Services”.  Zote hizo zitatolewa hapa nchini na kutambulika duniani kote.

 

Yapo mambo mengi katika mapendekezo hayo ya kuboresha hali ya Jeshi hili lakini nadhani hili la uboreshaji wa mfumo wa mafunzo na viwango vya taaluma kwa watumishi ndilo lenye umuhimu wa kuzungumziwa hapa.  Ni matumaini yangu kwamba mtakuwa mmepata dira ya mwelekeo wa kazi hii mliyoamua wenyewe kujiunga nayo.  Kwa ufupi tu ni kwamba, katika muda mfupi ujao taaluma hii ya “Correctional Service” kwa hapa nchini itapata hadhi ya kutambulika kimataifa na hivyo kuwapeni fursa za kuweza kujinadi pale Umoja wa Mataifa unapotangaza nafasi za vikosi vya kulinda usalama maeneo mbalimbali duniani.  Vile vile mtaweza kwenda kokote duniani na kuweza kupata ajira kwa taaluma hii.  Hii ni changamoto ambayo mnapaswa kuifanyia kazi tangu sasa kwa kuzingatia nidhamu, uadilifu na ari ya kujiendeleza.

 

Napenda kutumia fursa hii pia kuzungumzia machache kuhusu matatizo yaliyopo hapa chuoni kama ilivyoelezwa kwenye risala ya Mkuu wa Chuo.

Serikali inatambua ukweli kwamba chuo hiki bado kipo katika ujenzi na hakijakamilika.  Shughuli za ujenzi wa chuo hiki zilikumbwa na tatizo la kutokuwepo kwa fungu la maendeleo (yaani Development Fund) katika bajeti ya Jeshi la Magereza na hivyo kusimama kwa muda mrefu.  Kwa hali hiyo napenda kuwathibitishia kwamba, serikali inafahamu kikamilifu upungufu uliopo chuoni hapa na kuwa ina lengo la kuhakikisha kwamba, chuo hiki kinakamilishwa kwa hadhi inayostahili utekelezaji wa majukumu yake ipasavyo siku za usoni.  Kwa kuwa tayari Serikali imekwisharudisha fungu la maendeleo, utekelezaji wa lengo hilo utaanza hivi karibuni.  Pamoja na hayo, naomba kuwapongeza na kuwashukuru wahitimu kwa kuielewa hali halisi ya upungufu waliokumbana nao.  Nawapongeza pia kwa moyo wao wa kujitolea kwa kuchanga Tshs.733,000/= ili zisaidie ununuzi wa samani za madarasani.

 

Kama ilivyo ada katika shughuli yoyote, ni muhimu nilizungumzie japo kwa ufupi, tatizo la janga la UKIMWI ambalo ni tishio kwa uhai wa Taifa na dunia kwa ujumla.  Naamini kwa umri wenu na uzoefu wenu wa maisha sitakuwa na haja ya kufafanua kwa kirefu hali halisi ya tishio la ugonjwa huu kwani naamini pia kuwa kila mmoja wetu hapa atakuwa tayari ameshaguswa kwa namna moja au nyingine na athari za gonjwa hili hatari.  Napenda tu kukumbusha kwamba mapambano dhidi ya UKIMWI ni endelevu na yanamhusu kila mmoja wetu, hivyo sote tushiriki kwenye mapambano hayo ipasavyo.  Kama inavyosemwa hivi sasa kuwa “usione soo sema naye”

 

Ndugu Wahitimu, Mabibi na Mabwana, narudia tena kuwapongeza kwa kufanikiwa kwenu kumaliza mafunzo haya salama na pia kuwapa hongera wale wote waliofikia kutunukiwa tuzo za ubora katika maeneo mbali mbali.

Baada ya kusema hayo, ninayo furaha kutamka kwamba Kozi hii Namba 18 ya Mafunzo ya Awali ya Askari Magereza imefungwa rasmi.

 

Ahsanteni.