HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI,

MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) KUMKARIBISHA

RAIS WA ZANZIBAR, MHE. AMANI ABEID KARUME KUFUNGUA MKUTANO WA MWAKA WA MAAFISA WAKUU

WA JESHI LA POLISI NCHINI KWENYE UKUMBI WA MIKUTANO WA KIMATAIFA ARUSHA, TAREHE

15 DESEMBA, 2003

 

·        Mheshimiwa Amani Abeid Karume, Rais wa Zanzibar

·        Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mheshimiwa Mohammed Babu

·        Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Omari Mahita

·        Makamishna wa Polisi

·        Naibu Makamishna wa Polisi

·        Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi

·        Viongozi mbali wa Serikali Mkoani Arusha

·        Mstahiki Meya wa Manispaa ya Arusha

·        Wakuu wa Madhehebu mbalimbali ya dini Mkoani Arusha

·        Wageni Waalikwa

·        Mabibi na Mabwana

 

Mheshimiwa Rais

Kazi yangu asubuhi hii ni kukukaribisha rasmi kutufungulia mkutano wa mwaka wa Maafisa Wakuu wa Jeshi la Polisi nchini, unaofanyika hapa mjini Arusha.  Lakini kabla sijafanya hivyo, napenda kuchukua fursa hii kwa niaba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kutoa shukrani zetu nyingi za dhati kwako kwa kukubali kuja Mkoani Arusha kutufungulia mkutano huu.

 

Mheshimiwa Rais

Jana tarehe 14/12/2003 tulikuwa nawe Wilayani Same Mkoa wa Kilimanjaro ambapo ulitufungulia rasmi Kituo cha Polisi Same kilichojengwa kwa nguvu za wananchi, na leo hii tupo nawe hapa Arusha kutufungulia rasmi mkutano wa mwaka wa Maafisa Wakuu wa Jeshi la Polisi nchini. 

 

Mheshimiwa Rais

Hatuna lugha ya kueleza shukrani zetu nyingi za dhati kwako, kwani katika hali ya kawaida, siyo rahisi kuwa na kiongozi mkubwa wa hadhi yako, kwa siku mbili mfululizo, katika mikoa miwili tofauti kwa shughuli mbili tofauti, lakini za idara hiyo hiyo moja.  Kwa kweli tunakushukuru sana.  Jambo hili siyo tu linatupa faraja kubwa kwa jinsi viongozi wetu mnavyoonyesha upendo na moyo wa kutujali, bali pia linatupa changamoto na ari ya kuongeza ufanisi katika utendaji kazi zetu.

 

Mheshimiwa Rais

Mambo mengi kuhusu Jeshi la Polisi, yakiwemo mafanikio na matatizo umeshaelezwa kwa kirefu na ufasaha na Inspekta Jenerali wa Polisi.  Sitapenda kukuchosha kwa kurudia kuzungumzia hayo.  Hata hivyo, napenda kuchukua fursa hii kuishukuru Serikali ya Awamu ya tatu ya CCM kwa kutekeleza kikamilifu ilani yake iliyouza kwa wananchi mwaka 2000 kuhusu vyombo vya ulinzi na usalama likiwemo Jeshi la Polisi.  Serikali ya CCM iliahidi kuimarisha majeshi yetu ya ulinzi na usalama kwa kuyapatia mahitaji yake ya vitendea kazi kwa kadri hali ya uchumi inavyoruhusu, ili majeshi yetu yaweze kutekeleza majukumu yake kwa urahisi.

 

Mheshimiwa Rais

Kama alivyosema IGP Serikali imekuwa ikifanya juhudi kubwa kutatua matatizo mbalimbali ya Jeshi la Polisi, ikiwa ni pamoja na kuongeza bajeti.

 

Mheshimiwa Rais

Juhudi hizo za Serikali zinaonekana, kwani hali ya Jeshi la Polisi ilivyokuwa miaka mitatu iliyopita ni tofauti na ilivyo sasa.  Bajeti ya Jeshi la Polisi imeongezwa kwa asilimia 30 kwa mwaka wa fedha wa 2002/03 na 2003/04.  Pia vitendea kazi mbalimbali vimeboreshwa kwa kadri hali ya uchumi itakavyoruhusu, naamini mazingira ya kazi yataendelea kuboreshwa mwaka hadi mwaka.  Tunaishukuru sana Serikali.

 

Mheshimiwa Rais

Kama nilivyosema awali, kazi yangu ni kukukaribisha tu.  Hivyo naomba kwa heshima na taadhima, nikukaribishe rasmi ili uzungumze na hadhara hii ambao wana hamu kubwa ya kusikia kutoka kwako.

 

 

Karibu sana Mheshimiwa Rais