HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) WAKATI WA KUFUNGA MKUTANO WA MWAKA WA MAAFISA WAKUU WA JESHI LA POLISI NCHINI KATIKA UKUMBI WA AICC, ARUSHA TAREHE 17/12/2003

 

·       Inspekta Jenerali wa Polisi

·       Makamishna wa Polisi

·       Naibu Makamishna wa Polisi

·       Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi

·       Wageni Waalikwa

·       Mabibi na Mabwana

 

Ndugu Mwenyekiti

Ninayo furaha kubwa kujumuika nanyi tena leo katika siku hii ya kufunga rasmi mkutano mkuu wa mwaka wa MaafisaWakuu wa Jeshi la Polisi nchini.

 

Naamini kwa siku tatu mlizokaa hapa, mmepata fursa nzuri ya kupima utendaji kazi wenu kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita, mmebadilishana uzoefu na mbinu za utendaji kazi na mmepanga mikakati mbalimbali ya kukabiliana kikamilifu na changamoto zilizoko mbele yenu kwa lengo la kuboresha zaidi utendaji kazi wenu, katika kuhakikisha ulinzi na usalama wa watu na mali zao unadumishwa.

 

Ndugu Mwenyekiti

Nimepitia ratiba yenu na kuona mada mbalimbali mlizojifunza na kujadili.  Hakika ni mada nzuri zilizochaguliwa vizuri na zinafaa kwa wakati tulionao sasa.  Kinachotarajiwa kwenu ni kuyazingatia na kuyafanyia kazi yale yote mliyojifunza, kwani hilo ndilo lengo hasa la mkutano huu, kwamba mkitoka hapa kwenda katika vituo vyenu vya kazi, mkayatekeleze kwa vitendo yale yote mliyojadili na kukubaliana kwa pamoja.

 

Ndugu Mwenyekiti

Nafahamu katika siku tatu mfululizo mlizokaa hapa, mmepata fursa ya kujadiliana kikamilifu, kwa kina na ufasaha mambo yote muhimu yanayolihusu Jeshi la Polisi na utendaji kazi wake kwa ujumla.  Hata hivyo, napenda kugusia machache kwa lengo la kuzidi kukumbushana na kusisitiza umuhimu wa mambo hayo.

 

Ndugu Mwenyekiti

Suala la ushirikiano na raia wema ni suala ambalo linapaswa kupewa umuhimu wa pekee kabisa.  Nafurahi kuwa suala hili lilisisitizwa pia na Mgeni rasmi Mhe. Amani Abeid Karume, Rais wa Zanzibar, wakati wa ufunguzi wa mkutano wenu juzi na pengine mlipata fursa ya kulijadili pia wakati wa kujadili hotuba ya mgeni rasmi.  Hata hivyo, nami pia napenda kusisitiza jambo hili kutokana na umuhimu wake.

 

Ndugu Mwenyekiti

Popote pale duniani, iwe ni kwa nchi tajiri au maskini, Jeshi la Polisi haliwezi kufanikiwa bila kuwa na ushirikiano wa kweli na madhubuti na raia wema.  Kama mjuavyo, askari Polisi siyo malaika.  Hawawezi kujua mipango mbalimbali ya uhalifu inayofanywa, kuwajua wahalifu na mbinu zao; n.k. bila kupata taarifa kutoka kwa raia wema.  Hivyo, raia wema ni muhimu sana katika kutekeleza kazi za Polisi, na pengine raia wema ndiyo uti wa mgongo wa ufanisi wa kazi za Polisi

 

Ndugu Mwenyekiti

Siku chache zilizopita, nilikuwa katika ziara ya kikazi mkoani Mwanza na katika baadhi ya wilaya za mkoa huo.  Katika mojawapo ya wilaya, nilimuona mahabusu aliyekamatwa wakati akiuza silaha aina ya bastola iliyokuwa na risasi 6 kutokana na taarifa za raia mwema.  Pia nilielezwa tukio la raia mmoja mwema kugundua silaha aina ya SMG iliyofichwa na majambazi shambani kwake na kutoa taarifa Polisi.  Sote tunafahamu matokeo, endapo raia hao wema wasingetoa taarifa Polisi na silaha hizo kuangukia mikononi mwa majambazi.  Huo ni mfano mmoja tu katika wilaya moja, naamini ninyi mnayo mifano mingi zaidi ya namna raia wema walivyosaidia kuepusha maafa makubwa kwa nchi yetu na mtakubaliana nami kuwa taarifa kutoka kwa raia wema ni uti wa mgongo wa ufanisi wa kazi za Polisi .  Hivyo, mtakaporudi katika vituo vyenu vya kazi, mkalipe umuhimu wa pekee suala hili na mkalisisitize pia katika mabaraza yenu.  Kama mnavyosisitiza suala la ukimwi na rushwa, na suala la uhusiano mzuri na raia wema mkalisisitize pia.

 

Ndugu Mwenyekiti

Kwa upande mwingine wa shilingi, raia wema wamekuwa mstari wa mbele kushirikiana na Jeshi la Polisi kutoa taarifa mbalimbali za uhalifu.  Hata hivyo, wamekuwa wakikatishwa tamaa na baadhi ya askari wachache wasiokuwa waaminifu ambao huvujisha siri za watoa taarifa.  Kitendo hicho siyo tu ni cha hatari kwa raia wema, bali ni cha hatari pia kwa Jeshi la Polisi, kwani bila taarifa za uhalifu Jeshi haliwezi kufanya chochote.  Aidha, kwa upande wa raia wema, mbali ya askari hao wasio waaminifu kujenga uhasama miongoni mwao, lakini pia wanasabisha baadhi ya raia wema kuumizwa, kujeruhiwa vibaya na hata wengine kuuawa kutokana na waliowataja kulipiza kisasi.  Ni wazi kuwa hatutakubali baadhi ya askari watuharibie sifa yetu njema.  Hivyo, askari yeyote wa cheo chochote atakayebainika kuvujisha siri za watoa taarifa, hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yake, ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi kwa fedheha.

 

Ndugu Mwenyekiti

Kama mjuavyo, kipindi hiki cha mwezi wa Disemba ajali nyingi za barabarani hutokea na kupoteza maisha ya watu wengi na wengine kubaki na ulemavu wa kudumu.  Ipo imani potofu kuwa kipindi hiki cha mwisho wa mwaka Mwenyezi Munguhufunga mahesabu yakendiyo sababu ajali nyingi hutokea.  Hata hivyo, jambo hilo siyo la kweli kwani hakuna ajuaye kama mwisho wa mwaka kwa Mwenyezi Mungu ni Disemba (Calenda Year) au Juni (Financial Year) au mwezi mwingine wowote.  Ukweli ni kuwa ajali nyingi kipindi hiki husababishwa na kuongezeka kwa wasafiri wanaoenda makwao kusherehekea sikukuu za Krismas na Mwaka mpya. 

 

Ndugu Mwenyekiti

Kutokana na ongezeko hilo la abiria na pilika pilika za mwisho wa mwaka, baadhi ya madereva wa magari ya abiria huenda kwa mwendo wa kasi ili waende safari nyingi zaidi na hivyo kupata faida kubwa.  Hali hii huonekana zaidi kwa mabasi yanayokwenda mikoa jirani, mfano Dar es Salaam – Morogoro, Kilimanjaro – Arusha, na mabasi madogo yanayotoka mikoani kwenda wilaya za jirani.  Ni vyema makamanda wote wa mikoa mhakikishe kuwa askari wa usalama barabarani wanasimamiwa kikamilifu ili kuhakikisha ajali zinazosababishwa na uzembe na mwendo kasi zinapungua.  Mtakapowasimamia kikamilifu askari wa usalama barabarani, mtasaidia kuokoa maisha ya abiria wasio na hatia ambao wamekuwa wakipoteza maisha yao bure.  Mbali ya tatizo la ukimwi kusabisha yatima, ajali za barabarani pia zimekuwa zikisababisha yatima kutokana na wazazi au walezi kupoteza maisha yao katika ajali.

 

Ndugu Mwenyekiti

Kama nilivyosema awali, naamini katika siku tatu mfululizo mlizokaa hapa, mlikuwa na muda mzuri wa kujadiliana kwa kina na ufasaha mada mbalimbali zilizowasilishwa kwenu na mna hamu kubwa ya kwenda kuyafanyia kazi yote mliyoazimia.  Hivyo, sipendi kuwachosha kwa hotuba ndefu.  Aidha, napenda kutumia fursa hii pia kuwatakieni wote safari njema kurudi vituo vyenu vya kazi, na pia nawatakia kheri na baraka kwa sikukuu ya Christmas na mwaka mpya wa 2004. 

 

Ndugu Mwenyekiti, ndugu Makamanda, Mabibi na Mabwana, baada ya kusema hayo, ninayo furaha kutamka kwamba, mkutano wenu wa mwaka wa Maafisa Wakuu wa Jeshi la Polisi nchini umefungwa rasmi.

 

Asanteni sana kwa kunisikiliza.