HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI

MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) KWENYE SHEREHE YA KUFUNGA MAFUNZO YA UONGOZI DARAJA LA KWANZA CHUO CHA MAGEREZA UKONGA, DAR ES SALAAM TAREHE

13 FEBRUARI, 2004

 

 

*   Kamishna Mkuu wa Magereza,

*   Makamishna wa Magereza

*   Maafisa Waandamizi wa Magereza

*   Mkuu wa Chuo,

*   Wahitimu wa Mafunzo

*   Wageni Waalikwa

*   Mabibi na Mabwana

 

Awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kutoa shukrani zangu nyingi za dhati kwa Uongozi wa Jeshi la Magereza nchini kwa kunipa fursa hii ya kuwa Mgeni Rasmi katika kufunga mafunzo haya ya Uongozi Daraja la Kwanza kozi Na. 5, yanayohitimishwa rasmi leo.  Nawashukuru sana.

 

Kabla ya kutekeleza jukumu lililonileta hapa la kuyafunga rasmi mafunzo haya nataka nizungumze machache kwa wahitimu.  Kwanza nataka niwakumbushe tu mambo mawili ambayo nina uhakika tayari mnayafahamu.

 

Hali ya magereza yetu nchini hivi sasa bado siyo ya kuridhisha.  Tunayo matatizo mengi ikiwa ni pamoja na uchakavcu wa majengo ya magereza na nyumba za askari, uhaba au ukosefu wa vyombo vya usafiri, upungufu katika huduma ya wafungwa na askari, upungufu wa vitendea kazi mbalimbali na kadhalika.  Hali hiyo isiyoridhisha chimbuko lake ni kudorora kwa uchumi wa taifa kwa muda mrefu, suala ambalo lilipelekea kuwepo kwa matatizo kwenye sekta zote nchini.  Hata hivyo hali hiyo imeanza sasa kubadilika katika siku za karibuni baada ya kuanza kuimarika kwa uchumi wa taifa.

 

Wakati huo huo, mwelekeo wa sasa wa kijamii na kisiasa nchini na duniani kote umeegemea katika suala zima la utawala bora, ambapo mambo yanayozingatiwa ni utawala wa sheria, haki za binadamu na uendeshaji wa shughuli za kiserikali kwa uwazi na ukweli.  Mwelekeo huu umepelekea watu kutambua zaidi haki na wajibu wao na hivyo kuleta hali ya uwajibikaji zaidi katika kazi za umma.

 

Mambo haya mawili niliyoyaeleza ndiyo yanayotukabili hivi sasa na nadhani mtakubalina nami kwamba yameifanya kazi ya uaskari magereza kuwa ngumu sana.  Mmeshuhudia wenyewe jinsi vyombo vya habari nchini vinavyofuatilia kwa makini shughuli za chombo hiki ikiwa ni pamoja na kutoa malalamiko na maoni ya wananchi kuhusiana na dosari mbalimbali zinazolihusu Jeshi hili, zikiwa za ukweli au hata za uongo.  Ninachotaka kusema hapa ni kwamba uwezo wetu wa kutoa huduma ipasavyo unakabiliwa na upungufu na wakati huo huo uwajibikaji wetu unafuatiliwa kwa karibu sana.

 

Nimewakumbusha mambo haya ambayo tayari mnayafahamu kwa sababu yana umuhimu mkubwa katika utendaji wenu baada ya mafunzo haya.  Uongozi Daraja la Kwanza ndiyo kiungo baina ya askari wa chini na wafungwa na uongozi wa juu.  Suala la muhimu sana linalohakikisha kwamba mambo niliyoyazungumzia hayaliathiri vibaya Jeshi hili ni kwa uongozi kuwa karibu sana na askari wa chini na wafungwa, kwa maana ya kufuatilia matatizo yao kuwaelewesha juhudi zinazofanyika kuyatatua na kuwaelimisha pia pale tunapokwama.  Njia hii pekee ndiyo itakayoondoa majungu, malalamiko na hata vitendo vya utovu wa nidhamu vinavyoweza kuliaibisha Jeshi la Magereza nchini.  Nataka sasa muelewe kuwa wasimamizi wa kwanza wa nidhamu jeshini ni viongozi wa ngazi yenu.  Kwa misingi hiyo ukali wetu kwa makosa ya nidhamu jeshini utaanzia kwenu pale mtakapozembea wajibu huo wa usimamizi wa nidhamu.

 

Ninafahamu kwamba uongozi wa jeshi hili tayari umekwishaanza kuchukua hatua madhubuti za kuhakikisha uimarishaji wa utawala bora kwa kuandaa nyenzo mbalimbali za kuwawezesha viongozi kutekeleza wajibu wao ipasavyo.  Jeshi limechukua hatua ya kuboresha Prisons Standing Orders ambazo ndiyo mwongozo wa utendaji wa shughuli za kila siku jeshini.  Hali kadhalika, kila askari amepatiwa Code of Conduct for Prisons Officers.  Wakati huo huo wateja wa aina zote wa jeshi hili wameandaliwa utaratibu maalum wa kuwaelimisha kuhusu huduma wanazopaswa kupatiwa na jeshi hili na namna ya kulalamika pale wanapoona mapungufu.  Baadhi ya taratibu hizo ni vipindi vya Radio na waaraka maalum unaoitwa Mkataba wa Huduma kwa Mteja.

 

Wito wangu kwenu wahitimu wa mafunzo haya ni kwamba mzingatie nyenzo zote hizo mlizoandaliwa ili muweze kutimiza wajibu wenu ipasavyo.  Katika hali iliyopo hivi sasa nchini na duaniani kote kama nilivyokwishaeleza hapo awali, kiongozi atakayekiuka maadili yanayosisitizwa katika nyenzo hizo mbalimbali nilizozitaja ni lazima atakaribisha mtafaruku kwake binafsi na kwa Jeshi hili kwa ujumla.

 

Kama ilivyo ada katika shughuli yoyote inayokutanisha watu wengi namna hii, ni muhimu nilizungumzie pia tatizo la janga la UKIMWI ambalo ni tishio kwa uhai wa Taifa na Dunia kwa ujumla.  Nadhani kwa uzoefu wenu wa maisha sitakuwa na haja ya kufafanua kwa kirefu hali halisi ya tishio la ugonjwa huu kwani nina hakika kila mmoja wetu hapa atakuwa tayari ameshaguswa kwa namna moja ama nyingine na athari zake.  Hivyo ninawajibika kukumbusha tu hapa kwamba mapambano dhidi ya UKIMWI ni endelevu na yanamhusu kila mmoja wetu.  Labda niongeze kwa kusema kwamba tunatarajia wahitimu wa mafunzo ya uongozi pia kuonyesha uongozi wao katika mapambano hayo ambayo silaha yake kuu ni kubadili tabia.

 

Baada ya nasaha hizi maalum kwa wahitimu, nataka sasa niwapongezeni wote wale walifanikiwa kumaliza vyema mafunzo haya na kufaulu kustahili kupandishwa cheo kuwa Koplo wa Magereza.  Kwa kuwa cheo kina maana ya kuongezewa majukumu zaidi, ni matumaini yangu kwamba kufuzu kwenu ni ishara ya kwamba sasa mnao uwezo wa kumudu madaraka zaidi.  Nawatakieni utendaji mwema vituoni ili siku zijazo wote muweze kuteuliwa kuhudhuria mafunzo ya uongozi Daraja la Pili.

 

Kwa hayo machache, sasa natamka kwamba Mafunzo ya Uongozi Daraja la Kwanza Kozi Namba 5 yamefungwa rasmi.

 

Asanteni.