HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) WAKATI WA UZINDUZI WA BODI YA TAIFA YA PAROLE UNAOFANYIKA HOLIDAY INN,

DAR ES SALAAM TAREHE 28/8/2003

 

 

*    Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Parole Mama Julie Manning

*    Wajumbe wa Bodi ya Taifa ya Parole

*    Wageni Waalikwa

*    Mabibi na Mabwana

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Awali ya yote napenda kuwashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi wa Bodi mpya ya Taifa ya Parole, na pia kushiriki katika ufunguzi wa kikao chake cha kwanza tokea iundwe upya.  Nimefurahi vile vile kupewa fursa hii kwa sababu kazi hii ya utekelezaji wa Sheria ya Parole ni yetu sote, mimi nikiwa mtendaji wa mwisho katika mtiririko.

 

 

Kufanya kazi vizuri kwa sheria hii ni faraja kwenu na kwangu na Wizara kwa ujumla wake.

 

Napenda kuchukua fursa hii pia, kuwapongeza wajumbe wote wa kuteuliwa wa bodi hii kwa kuteuliwa tena baada ya kumaliza kipindi chao cha kwanza cha miaka mitano.  Nimeambiwa kwamba hata miongoni mwa wajumbe wanaoingia kwenye bodi hii kwa nyadhifa zao ni mmoja tu aliyebadilika.  Nawapongeza pia wajumbe hao kwa kuendelea kuwepo na pia naomba nichukue nafasi ya kipekee kumkaribisha mjumbe mpya aliyejiunga nanyi.  Matokeo ya msimamo wenu wa kutetea mlichoamini kuwa ni sahihi – sheria.  Naamini uzoefu wa miaka mingi mlio nao katika bodi utasaidia kuleta ufanisi zaidi, kwani uzoefu ni suala muhimu katika kuongeza ufanisi wa jambo lolote.  Ninawatakieni wote utendaji wenye ufanisi na wenye heshima na usio na majuto ya kuwepo kwa sheria mnayosimamia.

 

 

 

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Narudi kwenye historia.  Wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa akizundua Bodi za Parole za Taifa na Mikoa kwa mara ya kwanza hapa nchini mwaka 1998 alielezea kwa kina kuhusu dhana nzima ya Parole na umuhimu wake katika mfumo wa utekelezaji wa sheria za kupambana na uhalifu nchini na hivyo kudumisha usalama wa jamii kwa ujumla.  Pamoja na kutoa wito kwa jamii kuielewa na kuikubali dhana ya Parole, Mheshimiwa Waziri Mkuu alisisitiza kwamba kwa kukubali kuanzishwa kwa mfumo wa Parole nchini, haina maana kwamba Serikali imeweka rehani dhamana kuu ya kudumisha usalama wa jamii.  Aliwahakikishia wananchi kwamba parole ni mfumo uliokwishatumika duniani kwa miaka zaidi ya 300 na kuthibitika kwamba ni sahihi katika kuimarisha urekebishaji wa wahalifu na hivyo kuimarisha usalama wa jamii.  Sio vinginevyo.

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Nimelazimika kukumbusha yale aliyoyasema Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu kuu mbili.  Kwanza, ni kutokana na uzoefu tulioupata katika awamu ya kwanza ya miaka mitano ya utekelezaji wa Sheria ya Parole hapa nchini.  Suala kubwa lililojitokeza ni kwamba sheria ya awali ilikuwa na msimamo mkali sana wa kuzuia wafungwa wenye aina fulani za makosa wasihusishwe na parole.  Matokeo ya hali hiyo ni kwamba sheria ilishindikana kutekelezeka.  Ni wafungwa watatu tu kwa nchi nzima walioweza kupata msamaha wa parole katika miaka mitano.  Msimamo huo mkali katika sheria hiyo ulitokana na msimamo wa jamii dhidi ya makosa husika.  Mkutano wenu wa uzinduzi uliofanyika Sea Cliff uliliona tatizo hili na kulielezea kwa kina.  Bodi yako iliiomba sana Serikali, ili iipitie sheria ya Parole upya.

 

Katika hali hii, wito wa Serikali uliotolewa mwaka 1998 kuitaka jamii ya Watanzania kuielewa na kuikubali dhana ya parole ulikuwa na umuhimu wa pekee.  Napenda nichukue fursa hii kuwapongeza na kuwashukuru sana wananchi kwa kuitikia wito wa Serikali na hivyo kuwezesha sheria iliyokuwepo kufanyiwa marekebisho muhimu ambayo kimsingi yamelegeza msimamo mkali uliokuwepo.  Taarifa kwamba kikao hiki cha kwanza kitajadili orodha ya majina 249 ya wafungwa wanaotarajiwa kusamehewa ni dalili nzuri kwamba marekebisho hayo ya sheria yameanza kuleta matunda mazuri.  Lengo la Serikali ni kuona kuwa ni wafungwa sugu na wenye makosa mazito ndio wanaokuwa Magerezani na hivyo kuondoa dhana ya kurundikana kwa wafungwa.

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Sababu kuu ya pili ya kukumbushia wito wa Serikali ni suala zima la ushiriki wa jamii katika kufanikisha urekebishaji wa wale watakaopata msamaha wa parole.  Nataka nichukue fursa hii kusisitiza kwamba, sheria ya parole haitaweza kutekelezeka bila ya ushirikiano wa jamii katika kuwapokea wahusika, kuwakubali, kuwasaidia na pia kufuatilia mienendo yao ili kuhakiki kuwa wanaishi kama raia wema.  Kumtenga au kumkataa mtu aliyetoka gerezani kwa msamaha wa parole ni kumnyima fursa yake ya kibinadamu ya kujirekebisha.  Aidha, kwa upande mwingine, kuficha maovu atakayotenda mfungwa aliyesamehewa kwa parole ni kuharibu ufanisi wa mfumo huo.  Hivyo natoa wito kwa jamii kutimiza wajibu wake bila hofu wala upendeleo katika kufanikisha sheria ya msamaha wa parole nchini.  Ukweli ni ukweli na tusijaribu kuuficha ukweli ili kufurahisha au kutaka kupendwa.  Parole haipo ili kulegeza misingi ya usalama wa raia.

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Ninazo taarifa kwamba kutokana na sheria hii mpya, tofauti na tulikotoka, walipatikana wafungwa 2,098 wenye sifa za kufikiriwa katika mpango wa parole lakini wengi wao majina yao hayataweza kufikishwa kwenye kikao hiki cha kwanza kwa sababu mbalimbali.  Sababu zilizotajwa ni:-

 

(i)                Majalada yao kutokamilika kwa wakati.

 

(ii)              Matokeo ya uchunguzi wa alama za vidole kuchukua muda mrefu kupatikana kutoka kitengo cha utambulisho (IB).

 

(iii)            Nakala za hukumu kuchelewa kupatikana kutoka mahakama husika.

 

(iv)            Kuchelewa kwa taarifa kutoka kwenye vijiji wanakotarajia kwenda kuishi kutokana na umbali wa Magereza walipo wafungwa husika.

 

Nachukua fursa hii kuwataka watendaji Wakuu wa Idara zinazohusika na vipengele hivi muhimu vinavyowawezesha wafungwa kujadiliwa kwenye Bodi za Parole, kuongeza ushirikiano wa karibu ili mpango huu uweze kutekelezeka kwa ufanisi zaidi.  Ni mategemeo yangu kwamba idadi hiyo kubwa ya wafungwa wenye sifa itajadiliwa na Bodi hii mapema iwezekanavyo.  Napenda kusisitiza kuwa, ni ushirikiano wa karibu wa vyombo vyote husika tu ndiyo utakaowezesha utekelezaji wa sheria hii kuwa na ufanisi uliokusudiwa.  Vinginevyo tutakuwa na utaratibu mzuri lakini ambao utendaji unafanya matunda yake yachelewe au yasipatikane kabisa.  Uamuzi wa Parole wakati mfungwa ameshamaliza kifungo ni jitihada zisizo na matunda.

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Kabla sijatekeleza kazi mliyonituma kuifanya hapa asubuhi ya leo, naomba nichukue fursa hii kuzungumza japo kwa muhtasari kuhusu suala zima la adhabu mbadala wa kifungo hapa nchini.  Nataka kukumbusha kwamba wakati tunaanzisha Parole hapa nchini tulijadili matatizo yaliyoukumba mfumo wa Magereza duniani ikiwa ni pamoja na hapa Tanzania.  Mtindo wa kumpeleka kila mkosaji gerezani umesababisha magereza mengi kufurika na kuwa na msongamano usioruhusu utekelezaji wa programu za urekebishaji, achilia mbali matatizo mengineyo mengi yatokanayo na hali ya msongamano.  Hali hii iliilazimu Jumuiya ya Kimataifa kupitisha Maazimio mawili ambayo kimsingi yanahimiza matumizi ya adhabu mbadala wa kifungo kama njia nzuri ya kuwarekebisha wahalifu wa kawaida na kuyaacha magereza yatumike tu kwa wahalifu wenye kutishia usalama wa jamii.

 

Ndugu Mwenyekiti

 

Tangu Maazimio hayo yapitishwe na Umoja wa Mataifa mwaka 1990 Tanzania imekwishachukua hatua kadha za kuimarisha utekelezaji wake, ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa mfumo huu wa Parole.  Katika hatua nyingine, Tanzania imepitisha Sheria ya “Community Service” ambayo ina lengo la kuwapa wahalifu wenye makosa yasiyo ya hatari katika jamii adhabu za kufanya kazi za huduma za jamii kwa kipindi fulani huku wakiishi majumbani kwao.  Hawa hata hawapelekwi magerezani.

 

Huu ni utaratibu mzuri zaidi wa kuwaadhibu wakosaji has wenye makosa madogo madogo, kwani kufungwa gerezani kumekuwa na athari nyingi siyo kwa anayeadhibitiwa tu, bali hata kwa familia yake na wale wote wanaomtegemea; watu ambao kwa namna fulani wanaadhibiwa bila kuwa na hatia yoyote.  Kufungwa gerezani kuna athari nyingi, kama vile kuvunja ndoa, kusambaratisha familia, kusababisha ongezeko la watoto wa mitaani na pia kuandaa wahalifu wapya wa baadaye kutokana na watoto wa mitaani ambao baadae wanakuwa wazee wa mitaani mara nyingi waliobobea kwenye fani ya uhalifu.  Ni aibu kwa wazee wazima kuvizia magari yanayopata ajali na kasha badala ya kusaidia majeruhi kazi yao inakuwa ni kuwamalizia ili wapate nafasi ya kuvuna wasichopanda.

 

Napenda kutoa wito kwa wananchi, waupokee kwa dhati mfumo huo wa “Community Service” kwa umuhimu unaostahili na washirikiane ipasavyo na wale watakaokuwa wanasimamia utekelezaji wake.  Mratibu wa mfumo huo amekwisha kuteuliwa na Mhe. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

 

 

 

 

 

Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe

 

Baada ya kusema hayo, ninayo furaha kutamka kwamba, Bodi ya Taifa ya Parole kwa mwaka 2003 hadi 2008 imezinduliwa rasmi na pia kikao chake cha kwanza cha Bodi hiyo kimefunguliwa rasmi.

 

Asanteni sana kwa kunisikiliza.