HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI MHE. OMAR RAMADHAN MAPURI (MB) WAKATI WA KUFUNGA SEMINA YA WADAU WA MPANGO WA HUDUMA KWA JAMII ILIYOFANYIKA KUNDUCHI BEACH HOTEL, DAR ES SALAAM TAREHE

12 DESEMBA 2003

 

·       Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Mpango wa  Huduma kwa Jamii na Mwenyekiti wa Semina hii Mhe. Jumanne Mangara

·       Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Huduma kwa Jamii Mhe. Omar Kwaangw

·       Katibu MkuuWizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi Bw. Bakari Mahiza

·       Wawakilishi kutoka nchi za Kenya, Malawi, Namibia na Uganda

·       Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya Mpango wa Huduma kwa Jamii

·       Wageni Waalikwa

·       Mabibi na Mabwana

 

Ndugu Mwenyekiti

Ninayo furaha kujumuika nanyi tena leo katika siku hii ya kufunga Semina ya Wadau wa Mpango wa Huduma kwa Jamii.

 

Ndugu Mwenyekiti

Ni imani yangu kuwa, kutokana na mada mbalimbali zilizowasilishwa, wadau wote mmepata elimu kubwa na ya kutosha kuhusu mpango mzima wa huduma kwa jamii na umuhimu wake kwa nchi yetu.  Aidha, mmepata uzoefu, ikiwa ni pamoja na kufahamu mafanikio na matatizo ya mpango huu kutoka kwa wenzetu wa nchi za jirani zilizoanzisha mpango huu kitambo sasa ambao mlikuwa nao katika semina hii.  Hivyo, nchi yetu ina bahati kuwa, inatarajiwa kuanza mfumo huu kwa ufanisi kutokana na kurekebisha makosa mbalimbali ambayo wenzetu walianza nayo.

 

Ndugu Mwenyekiti

Kama mjuavyo,  lengo la semina hii ni kuwakutanisha  wadau wote muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Mpango wa Huduma kwa Jamii ili kuwaelimisha juu ya wajibu na majukumu ya kila mmoja katika mfumo mzima wa huduma hii.  Naamini lengo hilo limetimia, kwani kwa siku mbili mlizokaa hapa, mmepata elimu ya kutosha kuhusu utekelezaji wa mpango huu, na ninyi mtakuwa waalimu kwa wadau wengine ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria semina hii.

 

Ndugu Mwenyekiti

Kwa ruhusa yako naomba ninukuu kwa lengo la kusisitiza maneno aliyosema Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa akifungua semina hii jana.  Mheshimiwa Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa elimu kwa jamii ili jamii iuelewe vizuri mpango huu na kutoa ushirikianao unaotakiwa.  Katika hotuba yake alisema, nanukuu; “Ni wajibu wetu sote kuwaelimisha wananchi ili waone umuhimu wa wahalifu wa makosa madogo madogo kama vile ugomvi mdogo mdogo, wazururaji, wanaotoa matusi, n.k kutumikia vifungo vyao nje ya Magereza kwa kufanya kazi kwenye jamii, ili Magereza machache tuliyonayo yabaki kwa ajili ya wahalifu sugu wenye makosa makubwa kama vile mauaji, ujambazi, ubakaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya na makosa mengine yanayohatarisha usalama na maisha ya jamii”.  Mwisho wa kunukuu.  Hivyo, ni imani yangu kuwa kazi hii ya kuelimisha jamii kutokana na ujuzi mlioupata hapa mtaifanya kwa uaminifu na ukamilifu.

 

Ndugu Mwenyekiti

Matarajio ya Serikali kwenu kuhusu utekelezaji wa mpango huu kwa ufanisi ni makubwa.  Nafurahi kuwa wadau wote muhimu katika utekelezaji wa mpango huu wameshirikishwa kikamilifu.  Michango mliyotoa wakati wa kujadili mada mbalimbali zilizotolewa itasaidia kupata mikakati na mbinu madhubuti za kukabiliana na changamoto zote zitakazojitokeza.  Serikali haitarajii mpango huu kuwa wa majaribio kwa kipindi kirefu  katika mikoa sita tu iliyochaguliwa (yaani, Dar es Salaam, Dodoma, Kilimanjaro, Mbeya, Mwanza na Mtwara) bali utakuwa ni mpango wa kudumu utakaoenea kwa haraka katika mikoa yote nchini.  Endapo nchi jirani na nchi yetu zimefanikiwa, tena wataalam wao tulikuwa nao hapa hapa katika semina hii wametupa ujuzi na uzoefu wao, hakuna sababu yoyote mpango huu usienee kwa haraka nchi nzima katika kipindi kifupi kijacho.

 

 

 

 

Ndugu Mwenyekiti

Nina ujasiri wa kusema hayo kwa sababu faida za mpango huu wa Huduma kwa Jamii  kwa wananchi na kwa Serikali ziko wazi.  Wananchi watafaidika kwa wahalifu kufanya kazi za kutengeneza barabara, kujenga shule na zahanati, kusafisha na kutunza mazingira, n.k.  Kwa upande wa vijijini, wananchi watapata msaada wa wahalifu katika kufanya kazi za maendeleo ya kijiji, hali ambayo siyo tu itatoa nafuu kwa wanakijiji bali pia itaharakisha kazi hizo.  Kwa upande wake Halmashauri za Miji na Wilaya, fedha ambazo zingetumika kulipa vibarua wa kutengeneza barabara, kujenga shule na zahanati, kusafisha na kutunza mazingira, sasa zitatumika katika shughuli nyingine za maendeleo.  Na kwa upande wa Serikali Kuu, itapata unafuu wa gharama za kumhudumia na kumlisha mfungwa na unafuu wa gharama za kuendesha Magereza.  Aidha, kwa upande wa mhalifu mwenyewe, atapata faida ya kuendelea kuishi na familia yake uraiani na hivyo kuepukana na adha mbalimbali za jela, ikiwemo uwezekano wa kuambukizwa magonjwa mbalimbali kama vile kifua kikuu.

 

 

 

Ndugu Mwenyekiti

Naamini mlikuwa na muda mzuri wa kujadiliana kwa kina na ufasaha mada mbalimbali zilizowasilishwa mbele yenu na mmetumia vizuri na kwa ukamilifu muda huo  mliokaa hapa kujadiliana mambo hayo, na mna hamu kubwa ya kwenda kuyafanyia kazi yote mliyojifunza.  Hivyo, sipendi kuwachosha kwa hotuba ndefu. 

 

Ndugu Mwenyekiti, ndugu wana semina, mabibi na mabwana, baada ya kusema hayo, ninayo furaha kutamka kwamba semina yenu ya wadau wa mpango wa huduma kwa jamii imefungwa rasmi.

 

 

Asanteni sana kwa kunisikiliza