TAARIFA YA WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA
NCHI KUKEMEA VITISHO VINAVYOFANYWA DHIDI YA WATANZANIA WENYE ASILI YA TANZANIA BARA
WANAOISHI ZANZIBAR
1.
Kule Zanzibar
limezuka wimbi la uhuni wa kuwatisha Watanzania wenye
asili ya Tanzania Bara wanaoishi huko.
Vitisho hivyo vinavyotolewa kwa njia za kauli
na vipeperushi vinawataka Watanzania wenye asili ya Tanzania Bara waondoke Zanzibar kabla ya zoezi la uandikishaji wapiga kura kuanza
vyenginevyo watadhuriwa.
2.
Napenda kuchukua
fursa hii kukemea vikali vitendo
hivyo ambavyo siyo tu ni vya kihuni na kihalifu, bali
pia ni vya kuvunja Katiba zetu zote mbili; yaani Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania ya Mwaka 1977 na Katiba ya Zanzibar ya 1984.
3.
Ibara ndogo ya
kwanza ya ibara ya 17 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano inasomeka ifuatavyo:-
“17.-(1) Kila
raia wa Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kwenda
kokote katika Jamhuri ya Muungano na kuishi katika sehemu yoyote, kutoka nje ya
nchi na kuingia, na pia haki ya kutoshurutishwa
kuhama au kufukuzwa kutoka katika Jamhuri ya Muungano.”
4.
Aidha, ibara
ndogo ya kwanza ya ibara ya 16 ya Katiba ya Zanzibar inasomeka ifuatavyo:-
“16.-(1)
Hakuna mtu atakayenyimwa uhuru wake wa kwenda, na kwa madhumuni ya kifungu hiki uhuru uliotajwa
humu maana yake ni haki ya kwenda popote katika Zanzibar, haki ya kuishi
katika sehemu yoyote ya Zanzibar, haki ya
kuingia Zanzibar, haki ya
kuondoka Zanzibar na haki ya kutofukuzwa Zanzibar.”
5.
Vitendo hivyo vya
kihuni vilivyojitokeza Zanzibar havina nguvu ya kisheria wala kimantiki kuweza
kumkatiza mtu yeyote, Mtanzania na hata asiyekuwa
Mtanzania, haki yake ya kuishi na kutofuzwa Zanziba; haki ambayo imetolewa
kikatiba.
6.
Vitendo hivyo si
vya kihuni tu bali pia ni vya kijinga, vya kipumbavu,
vya ufinyu wa mawazo na si vya kuona mbali.
Hii ni kwa sababu si Watanzania wenye asili ya
Bara tu ndio wanaoishi Zanzibar, bali wapo pia Wazanzibari kwa maelfu wanaoishi
Tanzania Bara. Vitisho dhidi ya
Watanzania wa Bara wanaoishi Zanzibar vinaweza kabisa kuchochea vitisho dhidi ya
Wazanzibari wanaoishi Tanzania Bara.
Hali hiyo haitokuwa kwa manufaa ya yeyote
isipokuwa labda kwa maadui wa Muungano wetu.
7.
Vitisho dhidi ya
“Wabara” vilikuwa vikisikika huko Zanzibar wakati wa mapambano ya
kutafuta uhuru, na vilikuwa ni sera ya msingi ya chama cha Hizbu kilichokuwa kikitetea
Usultani. Pamoja na
kwamba tulikuwa tunatawaliwa, vitendo kama hivyo vya
vitisho havikuvumiliwa. Iweje vivumiliwe
na kuachiwa viendelee leo wakati tunajitawala na tuko
huru? Hiyo haiwezekani hata kidogo.
8.
Naliagiza Jeshi la Polisi kuvikomesha mara moja
vitendo hivyo kwa nguvu zake zote za kisheria. Na agizo hili nitalifuatilia kwa karibu.
9.
Kwa upande
mwingine, nawataka Watanzania wote wanaoishi Zanzibar, Wazanzibari na wasiokuwa
Wazanzibari, waishi kwa amani bila ya kubughudhiana kwa asili zao. Wenye asili ya Bara Afrika, wenye asili ya
Bara Arabu, wenye asili ya Bara Hindi na wengineo wote,
wamekutana huko kwa matakwa ya historia.
Wapo waliopelekwa huko na harakati za kutafuta riziki kwa uvuvi; wapo
walijikuta Zanzibar wakikimbia vita makwao; wapo waliopelekwa Zanzibar na
biashara halali; wapo pia waliopelekwa huko na biashara haramu ya utumwa. Leo wakianza kufukuzana nani atabaki? Kwani, kama mwenye asili ya Bara Afrika hana haki ya kuishi Zanzibar, yule mwenye asili ya Bara Arabu au Bara Hindi
ataipata wapi haki hiyo?
10.
Wakati wa kupigania uhuru, Wazanzibari wa asili zote
walishirikiana. Hivyo hivyo katika
Mapinduzi ya 1964. Iweje leo wabaguane kwa asili zao?
11.
Nawataka wananchi
wote huko Zanzibar waendelee na shughuli zao
bila ya hofu wala woga. Wala wasikubali
kutishwa kwani sera za vitisho zimekwisha pitwa na
wakati. Kila ataetishiwa atoe taarifa
Polisi au hata kwa Sheha aliye karibu naye. Nawataka Polisi
na Masheha wazishughulikie taarifa hizo kwa uzito
mkubwa tena bila ya ajizi.
12.
Daftari la kudumu
la wapiga kura kamwe lisitumiwe kama
kisingizio cha kuhalalisha vitendo vya kihuni na vya kutishia amani na
utulivu. Sheria za Uchaguzi zimeweka
utaratibu mzuri wa kuweka pingamizi dhidi ya mtu
asiyestahiki kuandikishwa kwa ajili ya kupiga kura. Wala kustahiki au kutostahiki kupiga kura hakuambatani na kabila la mtu wala asili yake.
13.
Napenda
kuwahakikishia Watanzania wote, Bara na Zanzibar, kwamba Jeshi la Polisi litasimamia haki za raia wote
kwa uadilifu mkubwa. Wakati wa uandikishaji katika daftari la wapiga kura, Jeshi la
Polisi litasaidia kuhakikisha kwamba hakuna mwenye kustahiki ataenyimwa haki
yake. Natoa wito utapofika wakati, wote
wenye kustahiki kisheria wakajiandikishe.
Kama kutakuwa na wasiotahiki
wataojipeleka kujiandikisha, watashughulikiwa wakati huo kwa majibu wa sheria,
na siyo hivi sasa kwa vitisho.
14.
Kuna tuhuma
kwamba vitisho hivyo vinavyofanywa hivi sasa vinaendeshwa na
chama fulani cha siasa. Ni juu ya
Msajili wa Vyama vya Siasa kufuatilia hilo. Lakini upande
wetu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, vitendo hivyo si vya kisiasa na hivyo havistahiki hifadhi ya kisiasa. Kwetu sisi hivyo ni
vitendo vya kihalifu na tutavishughulikia kwa mtazamo huo. Kwa hivyo tutapokuwa tunaviandama,
hatutokubali lawana kwamba tunaandama chama cha siasa au tunaandama
wanasiasa. Kazi yetu ni
kupambana na uhalifu popote unapofanywa na mtu yeyote anayeufanya. Hatujali kama ni
mwanasiasa, mkulima, mfanyabiashara, mhubiri wa dini, mweusi, mweupe, mwanaume
au mwanamke n.k.
15.
Naomba ushirikiano
wenu wote katika kuendeleza amani na utulivu nchini.
Omar R. Mapuri
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI
10 /2/2004