MPANGO WA MAENDELEO WA
MWAKA 2003/04
UTANGULIZI
Mpango wa maendeleo wa mwaka
2003/04 unalenga katika kuendeleza utekelezaji wa mikakati ya kupambana na
umaskini pamoja na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi. Mikakati ya kupambana na
umaskini na ufuatuliaji wake vilijumuishwa katika mfumo wa bajeti tangu mwaka
wa fedha ulioishia Juni 2002.
Kwa kuzingatia mapitio ya mwenendo
wa uchumi na bajeti ya mwaka 2002/03 pamoja na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2025 ni dhahiri kwamba jitihada zaidi zitawekwa katika kulinda na
kuendeleza mafanikio yaliyopatikana katika kupunguza umaskini na ukuaji wa
uchumi. Mapitio na matarajio ya makubaliano kati ya serikali na wahisani mbali
mbali pia yamezingatiwa katika kuandaa mpango huu wa maendeleo.
Ili kufanikisha malengo
yaliyowekwa, vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025
vya uendelezaji rasilimali watu, usalama na uhakika wa chakula, kukuza ajira na
kuongeza mapato ya fedha za kigeni vitaendelea kutekelezwa. Aidha, ili
kufanikisha utekelezaji wa vipaumbele hivyo, mkazo umewekwa katika kujenga
mazingira mazuri ili wadau mbalimbali waweze kushiriki kikamilifu katika maeneo
ya huduma za kijamii na kiuchumi na katika maeneo mengine yanayojumuisha,
ardhi, utalawa bora, hifadhi ya mazingira, masuala ya jinsia na vita dhidi ya
ukimwi.
Mgawanyo wa rasilimali kisekta
umezingatia malengo yaliyotajwa hapo juu. Katika kipindi cha mwaka wa fedha
2003/04 kiasi cha sh 807,440,576,900 milioni zinatarajiwa kutumika katika
mpango mzima. Fedha za hapa ni sh. 165,724,798,200 milioni na za nje sh
641,715,778,700 milioni.
Ukuaji wa uchumi kwa jumla
Hali ya uchumi wa Taifa katika mwaka 2002 umekuwa
kama ilivyotarajiwa, ambapo kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa uliongezeka, na
akiba ya fedha za kigeni iliongezeka kutokana na kuongezeka kwa mauzo nje ya
nchi. Kasi ya upandaji bei pia iliendelea kupungua.
Pato
la Taifa
Takwimu zinaonyesha kuwa Pato la Taifa
lilikua kwa asilimia 6.2 mwaka 2002 ikiwa ni zaidi ya lengo la asilimia 5.9
ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 5.7 mwaka 2001. Sekta ya kilimo ilikua kwa
asilimia 5.0 na kutoa mchango mkubwa katika ukuaji wa Pato la Taifa. Sekta
nyingine zilizokua na kuchangia kwa viwango vikubwa katika Pato la Taifa ni
pamoja na biashara na hoteli ikijumuisha utalii (asilimia 7.0) na bidhaa za
viwanda (asilimia 8.0), Mawasiliano na uchukuzi (asilimia 6.4) na huduma za
kibiashara (asilimia 4.8)
Kasi
ya Upandaji Bei
Kasi ya upandaji bei iliendelea kupungua na kufikia
asilimia 4.2 mwezi Machi 2003 ikilinganishwa na asilimia 4.5 mwezi Juni 2002.
Kupungua kwa mwenendo wa kasi ya upandaji bei kunatokana hasa na hali nzuri ya
upatikanaji na ugavi wa chakula pamoja na sera za makusudi za kudhibiti
mwenendo wa mapato na matumizi ya Serikali na ujazi wa fedha nchini.
Deni
la Taifa
Katika kuimarisha usimamizi wa madeni ya
nje na ndani, Mkakati wa Deni la Taifa ulizinduliwa mwezi Agosti 2002. Mkakati
huu unabainisha mwongozo na maelekezo ya ukopaji nje, hususan, muundo wa
usimamizi kiasasi, mamlaka ya kukopa na aina ya mikopo. Lengo kuu la Mkakati
huu ni kuhakikisha kwamba mzigo wa madeni ya nje utakuwa stahimilivu (debt
sustainability). Kwa upande wa madeni ya ndani ubadilishaji wa dhima za ndani
zisizo na dhamana katika hawala zinazouzika unaendelea. Utaratibu huu
umepanuliwa kufuatia kuzinduliwa hatifungani za hazina za miaka 5 na
zilizoorodheshwa katika soko la Hisa la Dar es Salaam. Aidha, hatifungani za
hisa za miaka 10 zimezinduliwa mwezi Oktoba 2002.
Mauzo na Uagizaji Bidhaa Nje
Thamani ya mauzo ya bidhaa nje kwa kipindi
cha mwaka 2002 iliongezeka kwa asilimia 13.0 na kufikia dola 877.0 milioni
ikilinganishwa na dola 776.4 kwa kipindi cha mwaka 2001. Ongezeko hilo la
thamani ya mauzo ilichangiwa hasa na mauzo ya bidhaa zisizo asilia kama madini,
mazao ya samaki na bidhaa za viwandani ambazo zilichangia asilimia 77.16
ikilinganishwa na asilimia 70.1 mwaka 2001. Kwa ujumla thamani ya bidhaa za
asilia karibu zote zilishuka kutokana na kushuka kwa bei katika masoko ya dunia
(kahawa, pamba, katani, korosho, karafuu). Kutokana na bidhaa za asilia
kuendelea kushuka thamani zilichangia asilimia 22.8 tu ikilinganishwa na
asilimia 29.9 mwaka 2001 kwenye Pato la Taifa. Thamani ya uagizaji bidhaa toka
nje ilikuwa dola 1,511.3 milioni mwaka 2002 ikilinganishwa na dola 1,560.5
milioni mwaka 2001. Kupungua huko kulitokana na kupungua kwa uagizaji wa bidhaa
za mitambo na chakula.
Thamani ya Shilingi
Wastani wa thamani ya shilingi ya Tanzania kwa dola
moja ya Marekani ilipungua na kufikia Sh.966.6 mwaka 2002 ikilinganishwa na Sh.
888.9 kwa dola ya Marekani mwishoni mwa mwezi Juni 2001. Kupungua huku kwa
thamani ya shilingi kulisababishwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa fedha za
kigeni katika soko la fedha kulikosababishwa na kupungua kwa mauzo ya bidhaa
nje na kuongezeka kwa mahitaji ya uagizaji bidhaa toka nje. Thamani hii
iliendelea kupungua hadi kufikia shilingi 1040 kwa dola ya Marekani mwezi
Aprili 2003.
Mapato
Uwezo wa serikali wa kukusanya mapato yake
uliongezeka katika kipindi cha mwaka 2001/02 hasa kutokana na kutekelezwa kwa
mikakati mbalimbali ya kukusanya kodi. Ongezeko hili hasa limetokana na
ongezeko la makusanyo ya kodi za mapato pamoja na kodi ya ongezeko la thamani
(VAT). Mapato ya serikali kwa mwaka 2001/02 yalikuwa asilimia 12.2 ya Pato la
Taifa, ambayo yanalingana na ya mwaka uliopita. Mapitio ya miezi mitatu ya
kwanza ya mwaka wa fedha wa 2002/03 yanaonyesha kwamba makusanyo yamevuka na
kuwa juu kidogo ya makadirio. Malengo ya muda wa kati wa sera ya kodi ni
kuongeza uwezo wa serikali wa kukusanya mapato kwa kuongeza vyanzo vya kodi,
kupambana na ukwepaji kodi, kudhibiti misamaha ya kodi pamoja na kuimarisha
usimamizi wa ukusanyaji wa kodi.
Katika kipindi cha mwaka wa fedha
2002/2003 Mpango wa Maendeleo uliidhinishiwa kiasi cha Sh 718,787,933 milioni
kwa ajili ya kutekeleza programu na miradi mbalimbali. Kwa ujumla Mpango wa
maendeleo ulilenga zaidi katika uboreshaji wa huduma za kijamii na uchumi;
ukuzaji wa sekta ya kilimo, mifugo, viwanda, na biashara ya ndani; uimarishaji
wa utawala bora na kukamilisha sensa ya watu na makazi ya mwaka 2002.
Kutokana na Sera ya
Elimu na Mafunzo pamoja na miongozo mbalimbali ya serikali, sekta ya elimu
iliandaa Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Elimu (Education Sector Development
Programme –ESDP) ambao ulianza kutekelezwa mwaka 2001/02 kwa kuanzia na Mpango
wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM). Mpango wa MMEM unalenga katika kuongeza
idadi ya uandikishaji watoto mashuleni, kuongeza ujenzi wa madarasa, kuajiri
kwa awamu walimu na kuwapanga upya kulingana na mahitaji, kuinua ubora wa elimu
kunakojumuisha mafunzo ya walimu walio kazini na tarajali, kutoa vifaa vya
kufundishia na kujifunzia; na kuinua uwezo wa uongozi na usimamizi wa
uendeshaji wa shule.
Katika kipindi cha mwaka 2002/03, Serikali
iliendeleza juhudi zake za kupanua na kuboresha elimu nchini kwa kutekeleza
programu mbalimbali zenye lengo la kuboresha elimu. Programu hizi ni pamoja na
uendelezaji elimu ya awali, elimu ya msingi, elimu ya sekondari, na elimu ya
juu na ufundi. Hivyo mkazo uliwekwa katika:
- Kuongeza idadi ya watoto wanaoandikishwa
kwa kuongeza idadi ya madarasa na walimu
-
Kuinua ubora
wa elimu ya walimu kwa kuendesha mafunzo kazini na tarajali na utoaji wa vifaa
vya kutosha vya kufundishia na kujifunzia, na
-
Kuinua uwezo
wa uongozi na usimamizi wa uendeshaji wa elimu katika ngazi zote.
Utekelezaji
a)
Programu ya Uendelezaji Elimu ya Awali
Kutokana na serikali kuridhia
mfumo wa elimu ya awali, shule za awali za serikali zimeongezeka toka shule
5,234 mwaka 2001 hadi kufikia shule 5,261 mwaka 2002. Kwa nchi nzima kuna jumla
ya shule za awali 9,569 zikijumuisha shule za serikali na za watu binafsi.
Ongezeko la shule za serikali na za watu binafsi limeongeza idadi ya wanafunzi
toka 310,933 mwaka 2001 hadi wanafunzi 581,022 hapo Juni 2002. Hi ni sawa na
ongezeko la asilimia 87.
b)
Programu ya Uendelezaji Elimu ya Msingi
Kukamilika kwa mwaka wa kwanza
(2002) wa utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (PEDP)
unaonyesha ongezeko la uandikishaji wa wasichana na wavulana katika shule za
msingi. Hadi mwezi wa Septemba 2002 wanafunzi 1,659,847 waliandikishwa
ikilinganishwa na wanafunzi 1,100,312 mwaka 2001. Lengo lilikuwa kuandikisha
wanafunzi 1,500,000. Kwa ujumla, idadi ya wanafunzi katika shule za msingi
iliongezeka kutoka wanafunzi 4,842,875 mwaka 2001 hadi 5,972,077 mwaka 2002
sawa na ongezeko la asilimia 23. Uandikishaji wa watoto wote waliopo shuleni
(GER) umefikia asilimia 98.6 wakati uandikishaji wa watoto wa rika ya Elimu ya
msingi (miaka 7-13) walioko shuleni umefikia asilimia 80.7. Mafanikio mengine katika
mwaka husika ni pamoja na kujenga madarasa mapya 8,817 (mengine 7,000 yalikuwa
katika hatua mbalimbali za ujenzi), kujenga nyumba za walimu 3,613 na kuajiri
waalimu 7,277.
c)
Programu ya Uendelezaji Elimu ya Sekondari.
Kwa upande wa elimu ya
sekondari uwezo wa kuingia sekondari umeongezeka toka asilimia 19.5 mwaka 2001
hadi asilimia 21.7 mwaka 2002. Idadi ya wasichana wanaojiunga na kidato cha
kwanza imeongezeka kwa kiasi kidogo toka asilimia 49.9 mwaka 2001 hadi asilimia
50 mwaka 2002 na wale wanaojiunga na kidato cha tano toka asilimia 38 hadi
asilimia 42. Ili kuimarisha uongozi na uendeshaji wa shule, waalimu wakuu wa
shule za sekondari 120 walihudhuria mafunzo mafupi ya uongozi wa elimu (ADEM)
na wengine 239 walifuzu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha, shule 50
zilikarabatiwa na shule 530 zilipatiwa vitabu vya kiada na vifaa vya maabara.
Katika mwaka 2002 serikali
chini ya Mpango wa Elimu ya Sekondari kwa Wasichana (GSES) iliwalipia ada
wasichana 4,291 wa kidato cha I-IV na wasichana 76 wa kidato cha V-VI ambao
wazazi wao hawakuwa na uwezo wa kuwalipia karo na mahitaji mengine.
d)
Programu ya Uendelezaji Elimu ya Juu na Ufundi.
Katika ngazi hii ya Elimu kazi
zilizofanyika ni pamoja na kuendelea kutoa mafunzo mbalimbali katika Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine, Chuo Kikuu cha Mzumbe,
Vyuo Vikuu Vishiriki vya Ardhi na Muhimbili na vyuo vingine vya Elimu ya juu na
vya ufundi. Mengine yaliyoendelea kufanyika ni pamoja na Baraza kuendelea na
kazi ya kutathmini vyuo binafsi ili kusimamia ubora wa elimu itolewayo kwa
kutoa ushauri na miongozo mbalimbali. Aidha, Serikali iliendelea na mpango wake
wa kusaidia vyuo vya elimu ya juu vya binafsi kwa kuanzisha mpango wa kutoa
mikopo kwa wanafunzi katika vyuo hivyo.
Utangulizi
Katika mwaka 2002 serikali iliendelea
kuimarisha utoaji wa huduma za afya na uboreshaji wa afya ya msingi kwa
wananchi wote. Umuhimu mkubwa uliwekwa katika upatikanaji wa dawa, huduma za
mama na mtoto na makundi mengine yanayoathirika zaidi.
Lengo Kuu la Sera ya Afya ilikuwa
kuboresha afya za wananchi wa Tanzania ili waweze kushiriki kikamilifu katika
shughuli za kiuchumi, kijamii na kifamilia. Sera ya afya inahimiza yafuatayo:
-
Wananchi
kushiriki kikamilifu katika mambo yanayohusu afya zao; na kipaumbele kutolewa
kwa makundi ya watu wanaoweza kuathirika zaidi hususan, akinamama, watoto na
jamii maskini zisizo na uwezo. Hii ni pamoja na kuzingatia usafi wa makazi ya
watu na matumizi ya maji na vyakula salama.
-
Pia
upatikanaji wa dawa muhimu na vifaa katika vituo vya kutolea tiba, uendelezaji
wa wataalam na watumishi wa afya pamoja na kuimarisha ubora wa majengo ya
kutolea huduma ya afya.
Kwa mwaka 2002 sekta ya afya imeendelea
kutekeleza programu ambazo zinalenga katika kuimarisha utoaji huduma bora za
afya na uboreshaji wa afya ya msingi kwa wananchi wote. Kwa ujumla matokeo ya
utekelezaji yamekuwa ya kuridhisha. Programu zifuatazo zilitekelezwa:
a) Programu
ya Kinga
Baadhi ya shughuli muhimu
zilizotekelezwa ni pamoja na: huduma za chanjo kwa watoto chini ya miaka mitano
na akina mama waja wazito, udhibiti wa magonjwa ya kuambukiza hususan malaria,
UKIMWI, kifua kikuu na ukoma; ununuzi wa dawa za magonjwa ya milipuko na ya
kuambukiza na kutoa ruzuku kwa Taasisi ya Utafiti wa magonjwa ya Binadamu na
Taasisi ya Chakula na Lishe.
b) Programu
ya Tiba
Katika programu hii shughuli
zilizofanyika ni pamoja na usimamizi na ununuzi wa dawa muhimu na vifaa vingine
katika vituo vya kutolea huduma za tiba; uendeshaji wa Hospitali ya Taifa
Muhimbili, Taasisi ya Mifupa (MOI), Taasisi ya Saratani Ocean Road, KCMC,
Hospitali ya Bugando na Hospitali teule za wilaya; na kutoa ruzuku kwa
hospitali za mashirika ya dini. Pia zilifanyika shughuli za matibabu ya wagonjwa
wa rufaa nje ya nchi na uendelezaji wa mabadiliko juu ya mfumo wa uendeshaji
hospitali za serikali.
c) Programu
ya Utawala na Maendeleo ya Watumishi
Pamoja
na mambo mengine programu hii ilitoa mafunzo kwa wataalam wa afya na Kamati za
Afya za Uendeshaji za mikoa na za wilaya juu ya mabadiliko ya sekta ya Afya.
Aidha, yalifanyika mafunzo ya wataalam wa afya nje ya nchi; na ukarabati wa
majengo ya vyuo 25 vya afya. Uimarishaji wa majengo ya ofisi za Wizara ya Afya,
Wodi ya watoto Muhimbili, hospitali ya Rufaa Mbeya na hospitali ya Mirembe
ulifanyika.
d) Programu
ya Huduma za Mipango, usimamizi Uhasibu na Udhibiti
Mapitio
ya sera ya Afya ni mojawapo ya kazi muhimu zilizofanyika. Pia kulifanyika
mapitio ya mipango na ripoti za fedha kwa halmashauri 113 za wilaya. Aidha,
kulifanyika ukusanyaji wa takwimu kwa ajili ya zoezi la kutathmini matumizi ya
fedha za serikali (Public Expenditure Review). Matayarisho ya Ulingo wa Muda wa
Kati wa Matumizi ya Fedha za Serikali (MTEF) kwa mwaka 2003/04-2005/06
yalifanyika.
Katika
mwaka 2002/03 serikali ilikamilisha na kuridhia utekelezaji wa Sera mpya ya
Maji ambayo inalenga katika kuchangia mkakati wa serikali wa kupunguza
umasikini. Vidhihirishi vya kupungua kwa umaskini vilivyoainishwa kwenye sera
ni pamoja na kutumia muda mchache katika shughuli ya kuteka maji mahudhurio
mazuri shuleni, utumiaji wa muda wa ziada kwenye shughuli nyingine za
uzalishaji mali, pamoja na ubora wa afya za wananchi. Sera ya Maji ya mwaka
2002 inaweka mkazo katika masuala yafuatayo:
-
Maji ni bidhaa muhimu na ina bei, kwa hiyo kama bidhaa zingine ni lazima
inunuliwe
-
Vyanzo vya maji havinabudi kutunzwa na kuhifadhi mazingira yake na wadau
wote hawana budi kushirikishwa katika utoaji wa huduma ya maji vijijini
-
Kubuni na kutumia tekinolojia nyepesi na yenye gharama nafuu ili
kuwezesha watu wengi zaidi kupata maji kwa muda mfupi. Ukuzaji wa uvunaji wa
maji ya mvua unapewa kipaumbele.
-
Ushirikishwaji wa sekta binafsi katika utoaji na usambazaji maji.
Kwa kipindi cha mwaka 2002/03 sekta ya
maji iliweka mkazo katika maeneo yafuatayo:
- Kuhakikisha kuwa mapitio ya Sera ya Maji ya
1991 yanafanyika ili kuboreshwa.
- Kuboresha utoaji wa huduma ya maji safi,
salama na ya kutosha kwa makundi mbalimbali ya kijamii mijini na vijijini.
- Kuimarisha huduma ya mifumo ya uondoaji maji taka mijini.
- Kuimarisha usimamizi na ugawaji wa
rasilimali ya maji ili kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
- Kutunza na kuhifadhi vyanzo vya maji kwa
lengo la kupunguza viwango vya uchafuzi.
- Kuwa
na wataalam wa kutosha wa kuimarisha na kuboresha maendeleo ya Sekta ya Maji.
Utekelezaji
Mapitio
ya utekelezaji kwa mwaka 2002/03 yanaonyesha yafuatayo:
-
Miradi ya maji katika miji ya Morogoro, Tabora, Dodoma, Tanga, Arusha,
na Moshi ilikarabatiwa;
-
Mamlaka ya maji safi na maji taka katika baadhi ya
miji nchini iliimarishwa, kwa kupatiwa zana zinazohitajika;
-
Miradi 13 ya Maji Vijijini ilikarabatiwa na visima
virefu (boreholes) vipatavyo 540 vilichimbwa katika vijiji mbalimbali nchini.
-
Idadi ya kamati za maji imeongezeka na vijiji 4,858 kati ya vijiji
6,767 vilivyoandikishwa vimeunda mifuko ya kuendeshea shughuli za maji;
-
Halmashauri za miji 6 sasa zimeunda Mamlaka za Maji Safi na Majitaka
kwa ajili ya usimamizi wa ugavi wa maji na kuondoa majitaka. Mamlaka hizo pia
zimepewa uwezo wa kuwekeza kwenye huduma za maji na majitaka.
Ardhi ni rasilimali
muhimu katika maendeleo ya Taifa. Utunzaji na uhifadhi wa rasilimali ya ardhi
ni muhimu kwa maendeleo ya Taifa. Ubora wa mipango ya matumizi bora ya ardhi,
uelewekaji wa sheria za ardhi na vijiji na uimarishaji wa uwezo wa utekelezaji
ni muhimu katika utunzaji na uhifadhi wa ardhi.
Katika kipindi cha mwaka 2002/03 malengo ya sekta ya
ardhi yaliyowekwa ni pamoja na:
-
Kuongeza ubora na ufanisi katika kusimamia na kutoa huduma za ardhi.
-
Kuongeza
ufanisi na ubora katika upimaji wa viwanja na uchoraji ramani.
-
Kuwa na
usimamizi mzuri wa sera, mipango na programu.
-
Kuweka
mazingira mazuri ya maendeleo endelevu ya makazi, ujenzi wa nyumba za bei nafuu
na matumizi bora ya ardhi.
-
Kuweka
mazingira mazuri ya utendaji kazi na maendeleo ya rasilimali watu.
-
Kuweka
utaratibu mzuri wa kukusanya na kusimamia mapato.
Sekta ya ardhi katika kipindi
cha mwaka 2002/03 ilitekeleza majukumu yafuatayo:
-
Elimu kuhusu
Sheria mpya za Ardhi ilifanyika pamoja na upembuzi yakinifu wa Mradi wa Viwanja
20,000 katika jiji la Dar es Salaam ulikamilika.
-
Mwongozo wa
tathmini ya ardhi ulikamilika na kusambazwa pamoja na upimaji wa viwanja katika
sehemu za Mbezi na Mbweni na hati 2,976 zilisajiliwa na maombi 190
yalikataliwa.
-
Upigaji wa
picha za anga ulifanyika katika miji ya Mtwara, Lindi, Nachingwea, Ruangwa, Tandahimba,
Masasi, Tunduru, Mahenge, Mbinga, Liwale na Newala.
-
Ripoti
inayohusu tathmini ya mali 1,500 ilikamilika na kusambazwa ikiwa ni pamoja na
sheria ya utatuzi wa migogoro ya ardhi ya mwaka 2002 ambayo itaanzisha mabaraza
ya ardhi na nyumba iliandaliwa.
-
Sera ya
Taifa ya maendeleo ya makazi ilichapishwa na kusambazwa na utafiti wa taarifa
zinazohusu vifaa vya ujenzi vya bei nafuu iliandaliwa na kuchapiswa.
-
Idara ya
“Management Information System” ambayo inatumia teknolojia ya kisasa katika
upatikanaji wa habari, takwimu na utunzaji wa kumbukumbu sahihi za ardhi
ilianzishwa; na iliweza kubaini viwanja 76,000 vilivyopimwa na kutambua viwanja
33,000 ambavyo vina hati miliki.
Nishati ni nyenzo muhimu katika kuchochea
ukuaji wa uchumi, kuboresha huduma za jamii na suala zima la kupambana na
umaskini. Tanzania imedhihirisha kuwa na rasilimali kubwa ya vyanzo vya nishati
ya umeme, gesi asilia,, tungamotaka, makaa ya mawe na nishati inayojadidika
(renewable energy). Pamoja na kuwa na vyanzo vingi vya nishati bado
havijaandelezwa licha ya shughuli za kukuza uchumi kuhitaji vyanzo hivi muhimu.
Mapitio ya Mwaka 2002/03
Madhumuni
na Malengo
Katika kipindi cha mwaka 2002/03 sekta ya
nishati ilipanga kutekeleza malengo yafuatayo:
-
Kukamilisha
mapitio ya sera ya nishati ya mwaka 1992, ili iende sambamba na sera za jumla
za kiuchumi zinazotekelezwa hapa nchini
-
Kuendeleza
matumizi ya vyanzo vya nishati kama mionzi ya jua, upepo, nishati inayojadidika
(renewable energy) na makaa ya mawe
-
Usambazaji
umeme vijijini na katika wilaya za Serengeti, Urambo na Ukerewe
-
Kuratibu na
kusimamia biashara ya mafuta ya petroli nchini na kuendeleza utafiti wa mafuta
pamoja na kukamilisha utekelezaji wa mradi wa gesi wa Songosongo
-
Kusimamia
urekebishaji wa sekta ndogo ya umeme, kuimarisha utendaji katika shirika la
TANESCO pamoja na ubinafsishaji wake
Pamoja na majukumu mengine sekta ya
nishati ilitekeleza yafuatayo:
-
Kukamilisha
mapitio ya sera ya nishati ya mwaka 1992 na kupitishwa rasmi na serikali
-
Kazi ya
kumchagua Mkandarasi wa kutekeleza mradi wa Songosongo na kutiliana mkataba na
kampuni ya “Larsen & Toubro Limited, India (L & T) “ imekamilika
-
Kazi ya
kurekebisha Shirika la TANESCO ilikamilka na kuwekwa chini ya manejimenti mpya
ya Net Group Solution kwa nia ya kuongeza ufanisi wa utendaji, hususan katika
kukusanya mapato
-
Mikutano
mbalimbali ilifanyika kwa kushirikiana na nchi wanachama wa jumuiya ya Afrika
Mashariki katika kuweka mikakati ya kuendeleza nishati pia kutangaza maeneo
yenye dalili za mafuta ya petroli na yanayoweza kuvutia wawekezaji
-
Takwimu za
kasi ya upepo zinaendelea kukusanywa ili kuweza kuthibitisha kama kasi ya uepo
huo inaweza kutosheleza kuzalisha umeme
-
Usambazaji
umeme katika vijiji vya wilaya za Serengeti, Urambo, Ukerewe, Ngara na
Biharamulo uliendelea. Aidha, serikali kwa kushirikiana na serikali ya Sweden
iliandaa taratibu za kuanzisha asasi maalum, “Rural Energy Agency” ambayo
itajihusisha na utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini na “Rural Energy Fund”
kwa ajili ya kutekeleza miradi ya nishati vijijini
Utangulizi
Sekta ndogo ya barabara
ni kati ya sekta muhimu katika uendelezaji na ukuzaji wa uchumi. Umuhimu wa
sekta hii hujitokeza katika usafirishaji na uchukuzi wa abiria na mizigo toka
sehemu moja hadi nyingine. Katika nchi yetu asilimia 70 ya uchukuzi wa mizigo
hufanywa kwa njia ya barabara na asilimia 64 ya mizigo ya nchi za jirani.
Katika kipindi cha mwaka 2002/03 sekta ya barabara imekuwa na maendeleo mazuri
ambayo yametokana na kuanzishwa kwa mfuko wa Barabara (Road Fund), Wakala wa
serikali wa Mamlaka ya Barabara (TANROADS) na Bodi inayosimamia uendeshaji
mfuko wa barabara (Road Funds). Kutokana na mabadiliko hayo barabara zote kuu
za mikoa na za vijijini zimeendelea kufanyiwa matengenenzo kama inavyopangwa.
Aidha, sekta binafsi zimeendelea kushirikishwa zaidi katika sekta hii.
Madhumuni makuu ya sekta ya barabara ni
kuwepo kwa mtandao wa barabara kote nchini zinazopitika katika kipindi chote
cha mwaka na zenye muungano mzuri kati ya barabara kuu za mikoa na zile za
vijijini. Hii ni pamoja na kuwa na
barabara kuu bora zenye kuunganisha nchi yetu na nchi jirani.
a)
Ukarabati, Ujenzi na Matengenezo ya Barabara
Katika kipindi cha mwaka wa fedha wa
2002/03 malengo ya ukarabati na matengenezo ya barabara kuu yalikuwa:
-
Matengenezo
maalum (Periodic maintenance) kilometa 165 za matengenezo ya kawaida (routine
maintenance) kilometa 6,382 madaraja na “culverts” 1,279
-
Ukarabati wa
barabara kuu kilometa 297, matengenezo ya dharura (emergency works) kilometa
377, “Backlog maintenance” kilometa 538 na madaraja makubwa 32
-
Kushirikisha
sekta binafsi katika shughuli za ukarabati, ujenzi na matengenezo ya barabara
ikiwa ni pamoja na kuendeleza na kutoa mafunzo kwa makandarasi wazalendo
-
Utekelezaji
wa mpango maalum wa ujenzi wa barabara kuu kwa viwango vya lami kwa kutumia
fedha za ndani
-
Matengenezo
ya kawaida (routine maintenance) kilometa 10,807, madaraja na “culverts” 1,351
pamoja na matengenezo ya dharura kilometa 699
-
Ukarabati wa
kilometa 648.5 na madaraja makubwa 60
-
Matengenezo
ya kawaida kilometa 1,808 na madaraja 157 kwa upande wa barabara Kuu na
kilometa 2,423 na madaraja 101 upande wa barabara vijijini kazi hizo
zilifanyika
-
Ukarabati wa
barabara kuu kilometa 121 zimekamilika ikiwa ni pamoja na kilometa 54.6 za
barabara vijijini na daraja moja.
-
Maandalizi
ya Sera ya Ujenzi yamekamilika na ipo katika hatua za mwisho kupitishwa na
serikali. Pia kazi ya kuandaa mkakati wa ushirikishaji wa sekta binafsi kwenye
shughuli za ujenzi, matengenezo na ukarabati wa barabara imekamilika
-
Baraza la
Taifa la Ujenzi (National Construction Council), Bodi ya Msajili wa makandarasi
(Constractor Registration Board) na Tanzania Civil Engineering and Constructors
Association (TACECA) wameendelea kutoa mafunzo kwa makandarasi wazalendo. Lengo
kuu ni kujenga uwezo wa wazalendo ili washiriki kikamilifu katika kazi za
ujenzi na matengenezo ya barabara. Sambamba na kujenga uwezo wa makandarasi
wazalendo Baraza la Ujenzi la Taifa kwa kushirikiana na wadau wake wameanzisha
mfuko maalum wa kusaidia wakandarasi wazalendo kupata fedha za kununulia vifaa
n.k
-
Kuhusu
mpango wa kuwapa uwezo sekta binafsi ili ishiriki katika shughuli za ujenzi wa
barabara kupitia mfumo wa (BOT) “Build Operate and Transfer” Wizara ya Ujenzi
inaendelea na majadiliano na kampuni binafsi ya PRODECO kuhusu jinsi ya kuingia
mkataba utakaoiwezesha kampuni hiyo binafsi kuanza na eneo walilopewa la ukanda
wa kati. Hususani barabara za Itigi, Manyoni, Tabora na Kigoma.
Pamoja na mafanikio yalionekana katika kipindi cha mwaka 2002/03 kwenye sekta ya barabara yapo matatizo yaliyojitokeza ambayo ni pamoja na:
-
Pamoja na
kuwepo kwa mfuko wa barabara bado fedha zinazopatikana hazijaweza kukidhi
mahitaji halisi. Katika mwaka 2002/03 fedha za matengenezo zilizopatikana ni
asilimia 30 ya mahitaji yote;
-
Uharibifu wa
miundombinu unaosababishwa na uchukuzi wa mizigo usiozingatia viwango
vilivyowekwa pamoja na uharibifu unaosababishwa na mvua; na
-
Makandarasi
Wazalendo hawajaweza kushiriki kikamilifu katika kazi za matengenezo, ukarabati
na ujenzi wa barabara. Sehemu kubwa ya kazi hizi zinafanywa na kandarasi za nje
Utangulizi
Sekta za Mawasiliano na
Uchukuzi zinalinganishwa na umuhimu wa mzungunko wa damu katika mwili wa mwanadamu.
Kukwama kwa sekta hizi ni kielelezo cha kuanguka kwa shughuli za kijamii na
maendeleo ya kiuchumi. Kwa kutambua umuhimu huo sekta hizi zinapewa kipaumbele
katika mgao wa raslimali kitaifa na ushirikishwaji wa sekta binafsi. Aidha,
serikali iliandaa pogramu maalum za ukarabati wa miundombinu ya sekta hizi.
Programu hizi zilihusu ukarabati wa njia za reli, simu, barabara, posta na
bandari. Ukarabati wa miundombinu kupitia programu zilizotanjwa hapo juu
umesaidia kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji katika sekta hizi; na
ushirikishwaji wa sekta binafsi katika utoaji wa huduma.
Mapitio
ya mwaka 2002/03
Madhumuni
na Malengo
Katika mwaka wa 2002/03
malengo makuu ya sekta za mawasiliano na uchukuzi yalikuwa kama ifuatavyo:-
-
Kuratibu na
kuhuisha sera, mikakati na sheria ili kuhakikisha kwamba huduma za mawasiliano
na uchukuzi zinatolewa kwa ufanisi;
-
Kuratibu
shughuli zote za ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundo mbinu ya sekta za
mawasiliano na uchukuzi;
-
Kujenga
uwezo wa kiutendaji wa wafanyakazi wa taasisi zote zilizo chini ya sekta za
mawasiliano na uchukuzi;
-
Kushirikiana
na asasi za kitaifa na kimataifa kwa madhumuni ya kuendeleza na kuboresha
huduma za mawasiliano na uchukuzi;
-
Kuweka
taratibu nzuri zitakazosaidia uratibu wa usalama wa vyombo vya usafiri wa
abiria ili kupunguza ajali;
-
Uratibu wa
huduma za sekta za mawasiliano na uchukuzi ili kuhakikisha kwamba hazileti
athari kubwa katika mazingira; na
-
Uboreshaji
wa huduma za utabiri wa hali ya hewa.
Utekelezaji wa malengo ya sekta ya
mawasiliano na uchukuzi kwa mwaka 2002/03 ni kama ifuatavyo:
-
Wizara
imeandelea na kuhuisha sera za sekta za mawasiliano na uchukuzi. Sera ya
uchukuzi imekamilishwa katika mwaka huu wa 2002/03 na kupitishwa na serikali.
Mkakati wa utekelezaji wa sera hiyo unaendelea kukamilishwa. Sera ya Posta na
ya “Information Communication Tecknology” zinaendelea kukamilishwa
-
Utaratibu wa
shughuli za ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya sekta za
mawasiliano na uchukuzi zinaendelea vizuri. Kazi zilizopangwa za ujenzi,
ukarabati na matengenezo ya viwanja vya ndege, vituo vya hali ya hewa na
mitandao ya simu zinaendelea vizuri
-
Mafunzo
yenye lengo la kujenga uwezo wa kiutendaji (rasilimali watu) katika sekta za
mawasiliano na uchukuzi yameendelea kutolewa kupitia vyuo vya mafunzo vilivyopo
chini ya sekta hii pamoja na vingine kama chuo cha watumishi wa umma, vyuo vya
elimu ya juu n.k
-
Sheria
inayomtaka kila mwenye chombo cha usafiri kuwa na vifaa vyote muhimu vya
kuokolea imekwishaandaliwa na ipo kwenye hatua za utekelezaji
-
Kuhusu
kuboresha huduma za hali ya hewa, taratibu zakuendeleza sekta hii zinaendelea
kitaifa na kupitia ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Mchango wa sekta ya kilimo na chakula
kwenye uchumi wa Taifa unabakia kuwa wa muhimu na wa kipekee kwani ndiyo chanzo
kikuuu cha chakula na malighafi ya viwanda, nafasi za ajira na soko la bidhaa
za viwandani.
Madhumuni na malengo ya sekta ya kilimo na
chakula ya mwaka 2002/03 yaliendelea kulenga katika kutekeleza Sera ya kilimo
na mifugo ya mwaka 1997 kupitia mkakati wa kuendeleza sekta ya Kilimo ya mwaka
2001 ambao unalenga katika masuala makuu yafuatayo:
-
Kuhakikisha
upatikanaji na usalama wa chakula kwa wakati na kwa watu wote
-
Kuongeza
kipato cha wakulima kwa kutumia mbinu za kisasa za kilimo, usindikaji na masoko
imara
-
Kuongeza
mapato ya fedha za kigeni kwa kuongeza wingi wa bidhaa zenye ubora unaokubalika
kikanda na kimataifa na kuendeleza matumizi ya teknolojia sahihi na rahisi na
yenye tija
-
Kutoa
msukumo wa matumizi endelevu ya rasilimali za asili kama ardhi na maji pamoja
na kuimarisha maingiliano ya sekta ya kilimo na sekta nyingine za kiuchumi
-
Jukumu la
kutoa huduma shirikishi za ughani nchini kupitia National Agriculture Extension
Project II (NAEPII) katika mikoa yote nchini zimehamishiwa kwenye Halmashauri
za Wilaya kwa kuhamisha wataalam kutoka Wizara ya Kilimo na Chakula na
kutayarishwa kwa uwiano wa majukumu ya Wizara ya Kilimo na Chakula na Ofisi ya
Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
-
Jumla ya
majaribio 114 yalifanyika katika mashamba ya wakulima na watafiti 80 walipatiwa
mafunzo ya rejea ya utafiti husishi. Aidha, huduma za utafiti zinalenga katika
kupata mbegu zinazo zaa kwa wingi, zinazostahimili ukame na kumudu kupambana na
mashambulizi ya wadudu na magonjwa kwa kutumia mbinu shirikishi inayolenga
matakwa ya wadau ambao huchangia sehemu kubwa ya gharama za utafiti. Matokeo ya
tafiti shirikishi zilizofanyika ni kuwepo kwa mbegu mpya za mazao ya mahindi,
maharage, mtama, pamba na ngano.
-
Mpango
Kabambe wa Kilimo cha Umwagiliaji umekamilika na umeonyesha kuwepo kwa hekta
29.4 milioni zinazofaa kwa kilimo cha umwagiliaji kati ya hizo hekta 2.3
milioni zina uwezekano mkubwa, hekta 4.5 milioni zina uwezekano wa wastani na
zilizobaki zina uwezekano mdogo. Baadhi ya mikakati ya kuhakikisha kuwa kilimo
cha umwagiliaji maji kinaendelezwa ni: ufufuaji na uboreshaji wa miundo mbinu
katika skimu za asili za umwagiliaji; kuanzishwa miradi mipya ya gharama ndogo
ambayo wakulima watachangia nguvu na gharama za uendeshaji; kuongeza uvunaji wa
maji ya mvua kwa kujenga mabwawa na kuchimba visima na kuwepo kwa mfumo mzuri
wa usimamizi na uratibu wa kazi ya umwagiliaji.
-
Katika kuhakikisha kuwa uagizaji na usambazaji wa pembejeo unafanikiwa
kwa kumpatia mkulima pembejeo kwa wakati unaofaa, kwa kiasi kinachohitajika na
kwa bei nafuu Mfuko wa Pembejeo za Kilimo ulikopesha jumla ya shilingi 1.2
bilioni kati ya shilingi 1.5 bilioni zilizokuwa zimetengwa. Pia benki za
ushirika zikiwemo Benki ya Ushirika Kilimanjaro (KCB) na Benki ya Ushirika wa Wakulima Kagera (KFCB) zilizokopesha jumla ya shilingi 19.81 bilioni kwa ajili ya kununulia na
kusambaza zana na pemebejeo za kilimo.
Sekta ndogo ya mifugo ni muhimu katika
uchumi kwa vile huchangia upatikanaji wa chakula na lishe, nguvu kazi wanyama,
usafirishaji, biashara na nishati.
-
Kuhakikisha upatikanaji wa chakula cha kutosha na kuinua kiwango cha
lishe kwa kudhibiti magonjwa ya mifugo;
-
Kuboresha uzalishaji, ubora na usambazaji wa mazao na pembejeo za
mifugo;
-
Kuendeleza hali ya maisha vijijini kwa kuongeza kipato kitokanacho na
uzalishaji, usindikaji na mauzo ya mazao ya mifugo;
-
Kuongeza mapato ya fedha za kigeni kwa kutoa msukumo wa uzalishaji na
kuongeza mauzo ya mifugo na mazao ya mifugo nchi za nje ;
-
Kuendeleza na kutumia teknolojia za kisasa zinazoongeza uzalishaji wa
mifugo, nguvukazi na ardhi;
-
Kuhakikisha matumizi na maendeleo endelevu ya malisho na maji ili
kupunguza athari za mazingira;
-
Kuendeleza rasilimali watu walioko katika sekta ili kuongeza tija,
uwezo, hamasa na moyo wa kujituma;
-
Kuendeleza nguvukazi katika sekta ya mifugo kwa kuzingatia matakwa ya
kijinsia ili kuongeza uzalishaji wa nguvukazi na uwiano wa kijinsia; na
-
Kuweka mazingira bora katika kutoa huduma kwa ufanisi.
Majukumu yaliyotekelezwa katika mwaka
2002/3 ni pamoja na:
-
Kuandaa mafunzo ya kanda ya magonjwa ya maumbikizo ya mifugo;
-
Kufanya mikutano kujadili
sheria za mifugo;
-
Kufanya majaribio ya chanjo ya magonjwa ya mifugo kama vile New Castle;
-
Kuendesha mafunzo juu ya
uzalishaji bora wa mifugo katika wilaya 36;
-
Ujenzi wa mabwawa ya mifugo;
-
Kukarabati Vituo vya Uchunguzi wa Mifugo na kuvipatia madawa muhimu;
-
Kuendesha mafunzo ya ukaguzi wa nyama na mifugo;
-
Kuratibu na kutathmini maendeleo ya mbuzi wa maziwa;
-
Kuanzishwa kwa vikundi vya
ushirika wa wafugaji; na,
-
Kufanyika kwa mafunzo ya ughani kwa wafugaji 1000 na Maafisa wa Ughani
40.
Utangulizi:
Sekta ya Maliasili na Utalii
inajumuisha sekta ndogo za Misitu, Nyuki, Uvuvi, Wanyamapori, Mambo ya Kale na
Utalii. Katika kufanikisha majukumu yake, sera na sheria zinaendelea kuhuishwa
na mikakati ya kutekeleza inaendelea kuandaliwa kwa nia ya kuhakikisha hifadhi,
usimamizi na matumizi endelevu ya maliasili, na kukuza utalii pamoja na kulinda
maeneo ya kihistoria na kutoa mchango mkubwa kwa pato la Taifa.
Sekta ya Maliasili ililenga
kutekeleza yafuatayo:-
-
Kuongeza mchango wa sekta za maliasili na Utalii katika Pato la Taifa
na katika kuongeza ajira na kuondoa umaskini nchini.
-
Kuhakikisha uhifadhi, usimamizi bora na matumizi
endelevu ya maliasili zetu.
-
Kuboresha utendaji, uwezo wa kusimamia na kuongeza
ufanisi wa utoaji huduma katika shughuli zinazohusu sekta za maliasili na
utalii.
-
Kuimarisha na kuendeleza utalii wa ndani na nje ya nchi.
-
Kuongeza mapato ya Serikali yatokanayo na sekta za
maliasili na utalii.
-
Kuwezesha wananchi, sekta binafsi, vikundi vya kijamii
na mashirika yasiyo ya kiserikali na wadau wengine wote kuweza kushiriki
kikamilifu katika mipango yote inayohusu kulinda, kuhifadhi, kusimamia na
matumizi endelevu ya maliasili na utalii.
Utekelezaji:
Ili kufikia malengo yaliyotajwa,
utekelezaji kwa mwaka 2002/2003 ni kama ifuatavyo;
-
Wizara ilihuisha sheria na kuboresha kanuni zinazotawala
Sekta ya Uvuvi.
-
Wananchi na sekta binafsi walishirikishwa katika kuandaa
mipango ya hifadhi na usimamizi wa Misitu na Nyuki.
-
Utambuzi wa maeneo ya Hifadhi za Misitu na Nyuki
ulifanyika katika mikoa ya Morogoro, Pwani na Manyara.
-
Ili kuboresha mazao ya samaki ukaguzi ulifanyika katika
sehemu mbalimbali hususani kwenye vyombo vya kuvulia samaki na viwanda
vinavyotengeneza samaki.
-
Ukaguzi na tathmini ya maeneo yaliyotengwa na hifadhi za
misitu zilifanyika.
-
Wizara iliandaa Mkutano wa Wawekezaji kwenye Sekta ya
Utalii na ilishiriki katika Maonyesho ya Kibiashara na mikutano ya kimataifa
inayohusu maliasili.
-
Utekelezaji wa mikakati ya kupambana na rushwa na
uelimishaji wa wananchi katika kuhifadhi rasilimali za asili na utamaduni
zilifanyika.
-
Jumla ya miche 9,256,289 ilikuzwa.
-
Jumla ya hekta 2,368 za ardhi ziliandaliwa na hekta
6,460 za mashamba ya miti na mashamba 16 ya miti yalitunzwa.
-
Ujenzi na ukarabati wa miundombinu katika mashamba na
maeneo ya uwindaji ulifanyika.
-
Ukaguzi na usimamizi wa uwindaji wa kitalii, wakala wa
utalii na ukusanyaji wa mapato vilifanyika.
-
Kutangaza vivutio vya kitalii nje ya nchi na kukuza
uwekezaji katika sekta ya maliasili.
-
Ukarabati wa majengo, sehemu za kihistoria, vifaa vya
kufanyia kazi na ajira kwa wafanyakazi watakaoshughulikia uhifadhi na tathmini
ya rasilimali za asili na utamaduni zilifanyika.
-
Programu na kampeni za kuzuia uvuvi haramu, ujangili na
uchomaji moto ovyo wa misitu zilitekelezwa.
-
Programu ya hifadhi ya samaki katika ziwa Viktoria na
Tanganyika zilitekelezwa.
Utangulizi
Sekta ya viwanda na biashara katika mwaka 2002
ilikuwa na mafanikio ya kuridhisha. Majukumu makuu ambayo sekta imejiwekea ni
kuweka mazingira mazuri ya uwekazaji ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa
kuridhisha wa nyezo muhimu kama vile umeme na maji, na kuhakikisha ubora wa
bidhaa zinazozalishwa ili ziweze kuhimili ushindani wa ndani na nje.
Mwaka 2002/03 shughuli zifuatazo
zilipangwa kutekelezwa:
-
Kuimarisha
uwezo wa sekta katika kuhudumia wawekezaji na washikadau mbalimbali;
-
Uimarishaji
wa taasisi za utafiti na teknolojia;
-
Kuhakikisha
upatikanaji wa bidhaa na huduma bora nchini;
-
Kuongeza
uzalishaji na mchango wa sekta katika uchumi;
-
Kuwa na
ushindani halali wa kibiashara, kumlinda mlaji na kuongeza mauzo ya bidhaa nje.
Utekelezaji
Hali ya utekelezaji wa shughuli
zilizopangwa katika sekta hii ulikuwa mzuri ingawa kwa kiasi kikubwa uliathiriwa
na ukosefu wa fedha.
-
Mazingira
mazuri ya uwekezaji pamoja na upatikanaji wa nyezo muhimu kama vile umeme na
maji umewahamasisha wawekezaji wengi kuendelea kufanya ukarabati wa viwanda na
kuanza uzalishaji kwenye miradi mipya ya viwanda iliyokamilika
-
Wizara
ilifanya ukaguzi wa viwanda katika mikoa mbalimbali kwa madhumuni ya kuhimiza
maendeleo ya viwanda na kuelewa matatizo yanayokabili viwanda na pia kupata
picha halisi ya ufanisi katika viwanda mbalimbali
-
Sekta ya
viwanda na biashara ndogo imeendelea kutoa ajira na kuchangia Pato la Taifa.
Inakisiwa sekta hii ilichangia kiasi cha 1/3 ya Pato la Taifa;
-
Katika hatua
za kupambana na umaskini, mafunzo ya usindikaji wa vyakula yalitolewa kwa kina
mama 1700 chini ya mradi wa UNIDO kupitia SIDO
-
Hadi kufikia
Desemba 2002 mfuko wa wafanyabiashara wadogo ulitoa mikopo yenye thamani ya sh.
4.64 bilioni kwa wananchi;
-
Marekebisho
ya “tariff” za umeme, urekebishaji wa viwango vya kodi na ukaguzi wa bidhaa ni
hatua zilizochukuliwa na serikali ili kuongeza ufanisi katika uzalishaji na
kumudu ushindani wa bidhaa katika soko la ndani na nje.
Kutokana na utekelezaji mzuri wa sera na
majukumu iliyojiwekea sekta ya viwanda kwa mwaka 2002 ilikua kwa asilimia 8.0
ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 5.0 mwaka 2001. Sekta hii imeongoza kwa
kuvutia wawekezaji wengi zaidi ikilinganishwa na sekta nyingine kwani miradi ya
viwanda 103 yenye thamani ya shilingi 198,245 milioni iliidhinishwa mwaka 2002
ikilinganishwa na miradi 82 iliyopitishwa mwaka 2001. Aidha, miradi hii ina uwezo
wa kutoa nafasi za ajira kwa watu 16,010.
Matatizo
Pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha
mwaka 2002 bado sekta ya viwanda na biashara inaendelea kukabiliwa na matatizo
kadhaa ikiwa ni pamoja na kodi kubwa, gharama kubwa za umeme, ushindani wa
bidhaa kutoka nje, mitambo mibovu kwa baadhi ya viwanda na miundombinu hafifu
hasa barabara za mikoani. Aidha, kwa upande wa viwanda vidogo matatizo makubwa
yaliyoendelea kukwamisha ukuaji wake ni pamoja na tatizo la kupata mitaji,
udhaifu wa huduma za kuendeleza biashara, na ushirikiano mdogo uliopo kati ya
taasisi mbalimbali na sekta hii.
Utangulizi
Sekta ya madini ina mchango mkubwa katika pato la
Taifa na mapato ya fedha za kigeni na pia sekta hii ni chanzo cha ajira katika
sekta isiyo rasmi. Katika mwaka 2002/03 Serikali iliendeleza jitihada zake za
kuweka mazingira bora ya kuwezesha ushiriki wa sekta binafsi kuweka sera,
sheria, taratibu, vivutio, huduma za ughani na ukusanyaji maduhuli ya Serikali.
Aidha, mkazo uliwekwa pia katika kuendeleza wachimbaji wadogowadogo na uhifadhi
wa mazingira katika machimbo ya madini.
Madhumuni na malengo kwa sekta ya madini kwa mwaka
2002/03 yalikuwa haya yafuatayo:
-
Kuongeza mchango wa sekta ya madini katika Pato la Taifa na fedha za
kigeni;
-
Kuongeza ajira na kuchangia kuondoa umaskini kwa wananchi kwenye maeneo
yenye migodi;
-
Kukuza na kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika shughuli za
utafutaji, uchimbaji na uuzaji wa madini nchini na nchi za nje;
-
Kuendeleza na kuhamasisha uanzishaji na ukuzaji wa viwanda
vitakavyoongeza thamani (value added) ya madini yanayochimbwa hapa nchini kabla
ya kuyauza nje;
-
Kupunguza au kuzuia athari za uharibifu wa mazingira zinazotokana na
uchimbaji madini kwenye maeneo mbalimbali nchini hasa kwenye machimbo; na
-
Kuimarisha usimamizi, udhibiti na uratibu katika sekta ya madini ikiwa ni
pamoja na kuimarisha ukusanyaji mapato.
Utekelezaji
Kazi zilizofanyika katika mwaka 2002/03 ni pamoja na:
-
-
Kuanzishwa kwa kituo cha mafunzo ya uchongaji wa vinyago kwa kutumia
miamba cha Arusha;
-
Kukamilika kwa uanzishaji wa kituo cha mafunzo ya teknolojia bora ya
uchimbaji na uchenjuaji wa madini ya dhahabu huko Matundas Wilayani Chunya;
-
Kuendelea kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo wa madini kuhusu njia bora za
uchimbaji wa madini (mfano dhahabu) na unaozingatia hifadhi ya mazingira hususan matumizi bora ya zebaki;
-
Kukamilika kwa ukarabati wa nyumba na ofisi za kanda mbalimbali;
-
Kukamilika na kuanza kutumika kwa muundo mpya wa sekta ya madini
unaotarajiwa kuimarisha usimamizi wa sera, sheria na taratibu. Katika muundo
huo vitengo vya idara ya Jiolojia na maabara vimeundwa upya; na
-
Mtaala mpya wa mafunzo ya ufundi mchundo yalikamilishwa na kuanza
kutumika katika chuo cha madini Dodoma.
Utangulizi
Ushirika na Maendeleo ya Masoko ni msingi imara wa
kuongeza akiba na mitaji hivyo kuinua kipato na kupunguza umaskini kwa wananchi
walio wengi hasa wale waishio vijijini. Aidha, uendelezaji ushirika na masoko
unatoa fursa pana kwa wananchi hasa wanachama wa ushirika kuunganisha nguvu zao
kwa pamoja na kupata bei nzuri ya mazao.
Wizara ya Ushirika na Masoko katika kutekeleza azma
ya kufufua, kuimarisha na kuendeleza Ushirika nchini, imeendelea kusimamia
jukumu la uwekaji wa mazingira ya maendeleo ya vyama vya ushirika endelevu
vinavyomilikiwa na wanachama wenyewe pamoja na mfumo wa Masoko wenye ufanisi,
kwa kutunga sera, sherie na taratibu za usimamizi.
-
Kuweka mazingira mazuri katika kuendeleza sera, sheria na kanuni
zinazohusiana na ushirika na masoko.
-
Kusimamia maendeleo endelevu na ya kiuchumi ya vyama vya ushirika na
mfumo wa masoko ya mazao ya kilimo.
-
Kuratibu, kuimarisha na kusimamia shughuli zinazohusiana na ushirika na
maendeleo ya masoko ya kilimo.
-
Kuweka mazingira mazuri na yenye ufanisi katika utoaji wa huduma na
ushauri
-
Kuwapa uwezo wanachama wa Vyama vya Ushirika kuendesha vyama vyao kwa
njia ya kidemokrasia
Katika kipindi
cha mwaka 2002/03 Wizara ya Ushirika na Masoko ilitekeleza yafuatayo:-
-
Rasimu ya Sheria ya Vyama vya Ushirika, Mkakati wa Kuendeleza Ushirika na
programu ya Marekebisho ya Ushirika viliandaliwa.
-
Tafsiri ya Sera ya Maendeleo ya Ushirika ya mwaka 2002 katika lugha ya
kiswahili ilikamilika na kuanza kusambazwa kwa wadau.
-
Vyama vya ushirika 123-vinavyojumuisha wakulima, wavuvi, wanawake na
wafanyabiashara wadogowadogo vilianzishwa.
-
Mafunzo ya kuanzisha na kusimamia vyama vya ushirika vya wakulima, wavuvi
pamoja na vyama vya ushirika vya wanawake yalitolewa.
-
Ukaguzi wa vyama vya ushirika 16 katika mikoa ya Mbeya, Dodoma, Morogoro
na Dar es salaam na ushauri wa jinsi ya kuviboresha na kuanzisha vingine
ulitolewa.
-
Bei za jumla za mazao ya chakula na masoko ya mifugo zilikusanywa na
kutangazwa.
-
Wasimamizi wa masoko 51 kutoka mikoa 10 walipewa mafunzo na takwimu
zinazohusiana na tafiti za masoko ya mazao ya mifugo, pamba, pareto, sigara na
vifaranga.
Utangulizi.
Mapitio ya mwaka 2002/03
Madhumuni/Malengo:
Utawala bora ni jibu la
moja kwa moja katika kufikia uwajibikaji wa kijamii, uwazi na ushirikishwaji wa
wadau wote. Kwa misingi hiyo, madhumuni na malengo ya sekta hii kwa mwaka
2002/03 yalikuwa:
-
Kuendelea na
utekelezaji wa programu ya kurekebisha na kuboresha mfumo wa sheria (Legal
Reform Programme) na kusimamia na kuendeleza utawala bora wa sheria na haki ili
kujenga amani na utulivu, hivyo kuchochea ukuaji wa uchumi;
-
Kuimarisha
idara ya Sheria na mifumo ya utendaji kwa lengo la kupunguza mlundikano wa kesi
katika Mahakama na vyombo vingine vya sheria;
-
Kutayarisha
na kuchapisha miswada 2,600 na sheria za Bunge 2,500;
-
Kuimarisha
na kuhuisha mfumo wa upangaji na usimamizi wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi;
-
Kusimamia
utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025 pamoja na sera mbalimbali za
kupambana na umaskini;
-
Kuendeleza
ukusanyaji na uchambuzi wa Takwimu za kiuchumi na kijamii pamoja na kuchambua
sera na kuwianisha masuala muhimu katika kusimamia uchumi; na
-
Kuratibu na
kuhakiki mapato na matumizi ya rasilimali za Taifa.
Utekelezaji
Katika mwaka 2002/03 serikali iliweza kutekeleza
malengo yaliyowekwa katika sekta hii ambayo ni pamoja na:
-
Sensa ya
watu na makazi ilifanyika kwa mafanikio mwezi August, 2002. Aidha, takwimu
muhimu zinaendelea kukusanywa na kuzalishwa kwa wakati ili ziweze kutumiwa na
wadau mbalimbali;
-
Mikakati ya
kuongeza uwazi, na nidhamu katika matumizi ya fedha na rasilimali za umma,
inaendelea kuzingatiwa, kwa mfano matumizi ya mfumo wa sasa wa bajeti ya
serikali, (Medium Term Expenditure Framework (MTEF);
-
Jengo la
Mahakama Kuu lilifanyiwa ukarabati na ujenzi wa Mahakama Kuu Bukoba ulianza.
Aidha, Mahakama za Mwanzo 2 zimeimarishwa katika mikoa ya Arusha na Manyara
chini ya mradi wa Quick Start;
-
Wizara na
Taasisi mbalimbali za serikali ziliendelea kutekeleza mikakati na ratiba za
kazi za kupambana na rushwa;
-
Sekta ya
sheria iliendelea kutoa ushauri wa kisheria kwa Wizara na Taasisi za Serikali;
-
Utaratibu wa
kushirikisha asasi za vikundi vya jamii zisizo rasmi katika mfumo wa sheria
ulianzishwa;
-
Wanasheria 6
walipata mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi. Aidha, Mahakimu 59 walipelekwa
kuchukuwa mafunzo ya Stashahada ya sheria na 14 cheti cha sheria;
-
Huduma za
mahakama zimeboreshwa kwa nia ya kupunguza msongamano wa kesi. Hii ni pamoja na
kuimarisha kitengo cha Polisi na Magereza kwa kuwaongezea fungu la fedha na
kuwapatia polisi vitendea kazi; na
-
Kutekeleza
mfumo wa kisheria na utafiti, pamoja na programu ya urekebishaji wa sekta ya
sheria.
Utangulizi
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
katika kipindi cha mwaka uliyopita imeendelea kutekeleza majukumu mbalimbali
iliyopewa kwa kutumia mikakati mbalimbali. Majukumu ya kiutendeji ya Ofisi ya
Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ni pamoja na kuratibu na kusimamia
tawala za mikoa ili ziweze pia kuzisaidia halmashauri katika kutekeleza wajibu
na majukumu yake; kusimamia na kutayarisha sera za maendeleo vijijini;
kuboresha miundo, hali ya watumishi na mifumo ya kazi ndani ya ofisi yenyewe,
mikoa na halmashauri; na kusimamia taasisi na miradi inayotekelezwa chini ya
ofisi.
Katika kipindi cha mwaka
2002/03, miradi iliyopangwa kutekelezwa chini ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa
na Serikali za Mitaa ni pamoja na:
-
Programu ya Uboreshaji mfumo wa Serikali za Mitaa (Local Government
Reform Programme) na Programu ya uimarishaji huduma Mijini;
-
Programu ya ukarabati wa vituo vya kutolea huduma za afya na Shirika la
Elimu Kibaha;
-
Programu ya usafiri na usafirishaji vijijini na mfuko wa pamoja wa sekta
ya afya (Health Sector Programm Support); na
-
Programu ya uboreshaji wa sekta ya Elimu pamoja na Programu ya
uimarishaji wa sekretarieti za mikoa.
Katika kipindi cha mwaka 2002/03, kanuni
za utumishi wa serikali za mitaa katika manispaa, halmashauri za miji na wilaya
zimeandaliwa zikiwa katika lugha ya kiingereza na kiswahili na kusambazwa kwa
wadau. Aidha, halmashauri 25 kati ya 38 zilizo katika awamu ya kwanza ya mpango
wa kuboresha serikali za mitaa zimeandaa na kukamilisha mipango ya mikakati
(strategic plans) ya halmashauri zao.
Hadi kufikia Septemba 2002, ukarabati wa
miundo mbinu katika miji ya Arusha, Moshi, Morogoro, Iringa, Mbeya, Mwanza,
Dodoma na Tanga ulikuwa umefanyika. Aidha, Utekelezaji wa programu na miradi
mbalimbali ya mikoa na halmashauri, umefikia hatua mbalimbali za kuridhisha
ikiwa ni pamoja na ukarabati na ujenzi wa nyumba za serikali, madarasa, nyumba
za walimu, zahanati/vituo vya afya na barabara; uimarishaji wa huduma za afya
na maji; uendeshaji na usimamizi wa mfuko wa miradi ya kujitegemea n.k.
Kwa ujumla utekelezaji wa miradi
mbalimbali umekabiliwa na matatizo ya kutokupatikana au kuchelewa kutolewa kwa
fedha za maendeleo kama zilivyoombwa. Aidha, hata fedha za nje hazikuweza
kupatikana kutokana na kukosekana kwa “counterpart fund”.
Hifadhi na usimamizi wa Mazingira ni
muhimu katika kuhakikisha kuwepo kwa maendeleo endelevu nchini. Hivyo katika
mwaka 2002/2003 sera na mipango ya maendeleo iliendelea kuelekezwa katika
kupambana na matatizo sugu sita ya mazingira nchini ambayo yamepewa kipaumbele
katika Sera ya Mazingira ya mwaka 1998. Matatizo hayo ni uharibifu wa ardhi,
kutopatikana kwa maji safi na salama kwa wananchi wengi wa mijini na vijijini,
uchafuzi wa mazingira kwa jumla, upotevu wa makazi ya viumbe hai na bioanuwai,
uharibifu wa makazi ya viumbe wa majini na uharibifu na uchomaji ovyo wa
misitu. Azma hii inaendana na malengo ya jumla ya nchi ya kutengemaza uchumi,
kuboresha afya na maisha ya wananchi na vilevile kuondoa umaskini.
Mapitio
ya mwaka 2002/03
Katika mwaka 2002/2003 malengo na
madhumuni kuhusu hifadhi na usimamizi wa mazingira yalikuwa ni:
-
Kuoanisha masuala ya hifadhi na usimamizi wa mazingira na kuyazingatia
katika maandalizi ya program, bajeti na mipango ya maendeleo ya kitaifa na
ki-sekta.
-
Kuzuia na kudhibiti uharibifu wa ardhi, mimea na uchafuzi wa maji na hewa
nchini.
-
Kuhifadi baioanuwai na kuhakikisha matumizi endelevu na sawa ya
rasilimali zilizopo
-
Kukuza weledi kwa wananchi kuhusu masuala ya hifadhi na usimamizi wa
mazingira.
Ili kufikia malengo yaliyotajwa juu ya
hifadhi na usimamizi wa mazingira kwa mwaka 2002/2003 shughuli zifuatazo
zilitekelezwa:-
-
Awamu ya pili ya kuelimisha na kuhamasisha viongozi wa ngazi za juu wa Wilaya, Miji na Manispaa
kuhusu Sera mpya ya Mazingira ilifanyika katika Halmashuri za Manispaa, Miji na
Wilaya zipatazo 45.
-
Rasimu ya Mkakati wa Taifa wa Hifadhi ya Bioanuwai na Mpango wake wa
utekelezaji ulikamilishwa.
-
Awamu ya kwanza ya utekelezaji wa miradi ya Hifadhi ya Ziwa Victoria na
Tanganyika ilikamilika ambapo protocol/ convention za kuhifadhi maziwa haya
zimekamilika. Zaidi ya hayo, na Wadudu milioni 10 wanaokula magugu maji
walizalishwa na kusambazwa kwenye Ziwa Victoria na vilevile miti milioni moja
ilipandwa na utekelezaji wa miradi kadhaa ulifanyika katika kipindi hicho
katika maziwa haya.
-
Taasisi mbal imbali zilishiriki katika kukuza weledi kwa wadau mbalimbali
na wananchi wote kwa ujumla kuhusu umuhimu wa hifadhi na usimamizi bora wa
mazingira hapa nchini kwa kutumia mbinu mbalimbali kama vile semina, warsha,
midahalo, makongamano, vipindi maalum kwenye vyombo vya habari (Redio,
Television, magazeti, vipeperushi, n.k), na kuandaa mafunzo mbalimbali na
upashanaji habari kwa kutumia mawasiliano na teknolojia ya kisasa.
-
Vyombo na asasi mbalimbali za Serikali na zisizo za Kiserikali zilitoa
mafunzo na kuwahamasisha wenye viwanda kuhusu matumizi ya teknolojia sahihi zenye kupunguza/kuzuia
uzalishaji wa taka za viwanda na majumbani na zenye kuzingatia maendeleo
endelevu ya viwanda.
-
Mikakati ya kitaifa inayohusu utekelezaji wa maazimio na mipango ya
maendeleo ya Umoja wa Mataifa kuhusu mikataba ya UNCCD, CBD, UNFCC na RAMSAR
iliandaliwa na kutekelezwa.
-
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira liliendelea na
utekelezaji wa program zake mbalimbali ikiwa ni pamoja na programu maalum ya
kutunza mfumo ikolojia wa korongo la Kihansi unaolenga kuhifadhi bioanuwai
iliyopo hasa vyura wa manyunyu.
Utangulizi
Utekelezaji wa malengo ya jumla ya Dira ya
Taifa ya Maendeleo 2025 kuhusu kuondoa umaskini uliokithiri nchini na kufikia
ubora wa hali ya juu, unaofanywa na Mkakati wa Taifa wa Kupunguza Umaskini
(PRSP), umebainisha maeneo mbalimbali ya utekelezaji. Baadhi ya maeneo hayo
yatatekelezwa na sekta za elimu, afya, kilimo, jinsia pamoja na maswala ya
kijamii. Aidha, mkakati huu unaendelea kutekelezwa katika ngazi mbalimbali kwa
kushirikisha wadau mbalimbali.
Katika kipindi cha 2002/03-malengo makuu
yalikuwa yafuatayo:
-
Kuondoa
umaskini uliokithiri miongoni mwa wananchi na kufikia ubora wa juu wa maisha ifikapo
mwaka 2025
-
Kuimarisha
taasisi zote zinazohusika na usimamizi na uratibu wa mipango ya kuondoa
umaskini.
-
Kuimarisha
rasilimali watu, mawasiliano, ushirikiano na ushirikishwaji wa wadau wote wa
ndani na nje katika mapambano ya kuondoa umaskini nchini.
-
Kuelimisha
na kuhamasisha Sera za kupunguza umaskini.
Programu ya umaskini katika kipindi cha
2002/03 ilitekeleza yafuatayo:
-
Taarifa ya
maendeleo ya Makakati wa Kupunguza Umaskini (PRS) ya mwaka 2001/02
ilitayarishwa na kusambazwa;
-
Taarifa ya
hali ya umaskini na maendeleo (PHDR 2002) imechapishwa;
-
Taarifa za
tafiti za matumizi kikaya (HBS 2000/01) na hali ya ajira (intergrated Labour
Force Survey 2000/01) nchini imetayarishwa na kusambazwa;
-
Zoezi la
kukusanya maoni kutoka vijijini yanayohusu uwiano wa idadi ya watu na mkakati
mzima wa kuondoa umaskini lilifanyika (Participatory Poverty Assessment);
-
Mikutano na
warsha mbalimbali iliyowahusisha wadau mbali mbali kuhusu umaskini, ikiwemo
uendeshaji wa wiki ya Umaskini ilifanyika; na
-
Utayarishaji
pamoja na usambazaji wa mwongozo wa kutathmini (Poverty Monitoring Master Plan)
makakati wa kupunguza umaskini umefanyika.
Utangulizi
Tanzania inatambua
athari kubwa inayokumba juhudi zake za maendeleo kutokana na janga la UKIMWI.
Hali hii imefanya serikali kuchukua hatua madhubuti kwa kuhusisha sekta
mabimbali ambazo zimekuwa zikifanya kazi kwa utaratibu wa pamoja. Pia mwitikio
wa wananchi umepata nguvu zaidi kutokana na kujihusisha kikamilifu kwa Serikali
na Jumuiya ya Kimataifa katika kushughulikia janga hili.
Madhumuni na Malengo
Katika kutekeleza Sera ya
kudhibiti UKIMWI shughuli zifuatazo zilipangwa kutekelezwa katika kipindi cha
mwaka 2002/03.
-
Kuzuia
kuenea kwa UKIMWI kunatokana na tabia isiyo salama ya kujamiana
-
Kupunguza
tabia ya kujamiana kama mkakati wa kuondoa umaskini
-
Kuhamasisha
kukubalika kwa watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI ili kupunguza unyanyapaa
-
Kuhakikisha
usalama wa huduma ya damu wanazopewa wagonjwa
-
Kutoa tiba
ipasavyo kwa watu walioathirika kwa magonjwa ya zinaa
-
Kutoa elimu
ya UKIMWI katika mashule yote na sehemu zote za kazi
-
Kuchukua
hatua madhubuti za kuelimisha umma kuhusu kuachana na mila ambazo zinaendeleza
kusambaa kwa UKIMWI
Katika kipindi cha 2002/03 Programu ya
Ukimwi imetekeleza yafuatayo:
-
Uzinduzi na
usambazaji wa nakala zaidi ya milioni 15 za Sera ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI
ambazo zimetafsiriwa katika lugha ya Kiswahili kwa wadau mbalimbali
-
Kukamilishwa
kwa wigo wa kitaasisi kwa ajili ya mkakati wa uongozi, kuratibu sekta
mbalimbali, kufanya ufuatiliaji na tathmini kuhusiana na virusi vya UKIMWI
(VVU/UKIMWI)
-
Kuhakikisha
kuwa kila sekta na jumuiya zimejihusisha kikamilifu katika utengenezaji na
utekelezaji wa mbinu za kupambana na VVU/UKIMWI
-
Kuchapisha
vijitabu karibu 700,000 na kusambazwa mashuleni kama njia ya kuimarisha kampeni
dhidi ya VVU/UKIMWI
-
Kutoa elimu
ya afya kwa umma juu ya kinga dhidi ya UKIMWI pamoja na mbinu za huduma ya
matibabu kwa wagonjwa
-
Kuhimiza
wananchi kupima hali zao ya kiafya kwa hiari na kutoa ushauri nasaha wa
kitaalam
-
Kuratibu
utafiti kuhusiana na ugonjwa huu wa UKIMWI
-
Kuhakikisha
usalama wa damu wanazopewa wagonjwa.
Madhumuni makuu ya serikali katika masuala
ya Jinsia ni kuwa na sera ambayo inaleta usawa wa kinjisia pamoja na usawa
katika mgawanyo wa rasilimali. Usawa unasaidia katika kusukuma ukuzaji wa
uchumi na maendeleo ya watu kwa ujumla.
Kufuatana na sensa ya watu na makazi
iliyofanyika Agost mwaka 2002, Idadi ya Watanzania wote ni 34,568,609 millioni
na kati ya hawa wanawake ni 12,558,530 millioni sawa na asilimia 51.1 na wengi
wao wanaishi vijijini na ni wazalishaji wakuu wa mazao ya chakula na biashara.
Karibu asilimia 88 ya wanawake wote wanafanya shughuli mbalimbali ambazo hazina
kipato kinachotambulika.
Serikali kwa kushirikiana na mashirika
yasiyo ya kiserikali yanayoshughulikia masuala ya jinsia inaendelea kuhimiza
uingizaji wa masuala ya jinsia katika sera, mipango na bajeti.
Mapitio ya Mwaka 2002/03
Malengo makuu ya serikali kuhusu masuala
ya jinsia kwa mwaka 2002/03 yalikuwa kama ifuatavyo:
-
Kuwa na
mipango ya makusudi ya kuwapa uwezo wanawake waliopo katika utumishi wa
serikali na mashirika yake fursa sawa za ajira na upandishaji wa vyeo
-
Kufundisha
na kuelekeza wizara, Mikoa, na wilaya kuweza kupanga mipango na kuandaa bajeti
zinazozingatia masuala ya jinsia
-
Kufanya
utafiti wa kuwa na vitengo vya jinsia katika ofisi za serikali na mashirika ya
umma
Utekelezaji
-
Wizara Mikoa
na Wilaya zote zilipewa mafunzo ya jinsi ya kupanga mipango na bajeti
zinazozingatia masuala ya jinsia sambamba na mafunzo ya Mfumo wa Bajeti wa Muda
wa Kati (Medium Term Expenditure Framework-MTEF).
-
Utafiti wa
kuwa na vitengo vya jinsia maofisini umekamilika (Gender focal points)
Katika mwaka 2003/04
shabaha ya mpango ni kuendeleza utekelezaji wa mkakati wa kupambana na umaskini
pamoja na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi. Mkakati wa kupambana na umaskini
pamoja na kufuatilia utekelezaji wake vilijumuishwa katika mfumo wa bajeti
tangu mwaka wa fedha ulioishia Juni 2002.
Kwa kuzingatia mapitio ya mwenendo wa
uchumi na bajeti ya mwaka 2002/03 ni dhahiri kwamba jitihada zaidi zinatakiwa
ili kuimarisha mafanikio yaliyopatikana katika kupunguza umaskini na kuongeza
kiwango cha ukuaji wa uchumi. Aidha, mapitio na matarajio ya makubaliano kati
ya serikali na wahisani mbali mbali yamezingatiwa.
Mpango wa mwaka 2003/2004 umezingatia
vipaumbele vilivyoainishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 vya
uendelezaji rasilimali watu, usalama na uhakika wa chakula, kukuza ajira na
kuongeza mapato ya fedha za kigeni. Ili kufanikisha utekelezaji wa vipaumbele
hivyo, mkazo umewekwa katika kujenga mazingira mazuri kwa wadau ikiwa ni pamoja
na wawekezaji mbalimbali katika maeneo ya huduma za jamii na za kiuchumi na
nyanja nyinginezo zinazojumuisha, ardhi, utawala bora, usalama na amani,
hifadhi ya mazingira, masuala ya jinsia na vita dhidi ya UKIMWI.
Malengo ya jumla ya mpango na bajeti kwa
mwaka 2003/04 ni kama ifuatavyo:
-
Kukuza
uchumi kwa kiwango cha asilimia 6.3 mwaka 2003, hadi asilimia 7.4 mwaka 2006;
-
Kupunguza
kasi ya upandaji bei kufikia kiwango cha asilimia 4.0 ifikapo Juni 2004 na
kuendelea kulingana na viwango vya nchi tunazoshirikiana nazo kibiashara;
-
Kuongeza
ukusanyaji wa mapato ya ndani ya serikali kwa kiwango cha asilimia 13.2 ya Pato
la Taifa la mwaka 2003/04 asilimia 13.5 mwaka 2004/05 na asilimia 13.7 mwaka
2005/06;
-
Kudhibiti
ujazi wa fedha (M2) kwa viwango vinavyowiana na malengo ya ukuaji wa uchumi na
kupunguza kasi ya upandandaji bei; na
-
Kuongeza
akiba ya fedha za kigeni kwa kiwango cha kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa
na huduma toka nje ya nchi kwa kipindi kisichopungua miezi mitano.
Makadirio ya mapato na matumizi ya Mpango
na Bajeti ya Serikali yanaonyesha mwelekeo ufuatao:
Tsh (‘000’)
|
|
2001/02 Halisi |
2002/03 Makadirio |
2002/03 Mwelekeo |
A.MAPATO YA NDANI
|
1,042,945 |
1,172,297 |
1,183,743 |
|
1.Mapato yatokanayo na kodi |
938,478 |
1,066,899 |
1,097,643 |
|
Ushuru wa Forodha |
88,708 |
109,440 |
160,126 |
|
Kodi za Mauzo ya nje na ndani |
177,615 |
203,927 |
193,267 |
|
Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) |
351,893 |
394,300 |
409,564 |
|
Bidhaa toka nje |
208,674 |
243,505 |
241,009 |
|
Bidhaa za ndani |
143,219 |
150,794 |
168,555 |
|
Kodi ya Mapato |
219,852 |
240,920 |
298,289 |
|
Kodi nyingine |
100,410 |
118,313 |
36,397 |
|
2.Mapato yasiyotokana na Kodi |
104,467 |
105,398 |
86,100 |
|
B.JUMLA YA MATUMIZI |
1,462,767 |
2,106,290 |
1,844,160 |
|
1.Matumizi ya Kawaida |
1,118,156 |
1,386,163 |
1,401,423 |
|
2.Matumizi ya Maendeleo |
344,611 |
720,127 |
447,737 |
|
Fedha
za ndani |
50,236 |
95,662 |
95,662 |
|
Fedha za
nje |
294,375 |
624,465 |
347,075 |
|
Mfuko wa
Songosongo |
- |
- |
- |
|
C.NAKISI/SALIO (A-B) |
-419,823 |
-933,993 |
-660,417 |
|
D. KUZIBA NAKISI |
|
|
|
|
1.Fedha kutoka nje |
503,670 |
890,738 |
719,154 |
|
Ruzuku |
385,200 |
542,298 |
472,348 |
|
Mikopo
ya kibajeti (Programme/Budget Support Loan |
33,171 |
110,801 |
134,566 |
|
Mikopo ya miradi |
154,184 |
340,561, |
198,200 |
|
Kulipia madeni ya nje (amortization) |
-68,885 |
-102,922 |
-85,960 |
|
2.Fedha
za ndani |
-83,849 |
43,254 |
-58,736 |
|
Mikopo isiyo ya mabenki |
36,574 |
9,000 |
9,000 |
|
Mikopo ya mabenki |
-59,181 |
21,254 |
21,655 |
|
Mapato ya Ubinafsishaji |
0 |
18,000 |
0 |
|
Kulipa madeni ya nyuma (arrears) |
-59,107 |
0 |
0 |
|
Kuongeza mitaji ya mabenki Mashirika |
- |
- |
- |
|
Marekebisho (Adjustment to Cash) |
33,564 |
- |
- |
|
Kulipa madeni ya ndani (amortization) |
-1,552 |
-10,000 |
-10,000 |
|
Expenditure float |
-34,147 |
- |
-79,391 |
|
Recovery of NBC Bond |
- |
5,000 |
- |
Shabaha kuu ya mpango
na Bajeti ni kusaidia ufuatiliaji na utekelezaji wa mkakati wa kupambana na
umaskini katika ngazi ya taifa na halmashauri. Aidha, Mpango na Bajeti wa mwaka
2003/04 unalenga katika maeneo yafuatayo:
-
Kudumisha
haki na amani – kwa kuhakikisha kwamba vyombo vya sheria na usalama
vimejumuishwa kikamilifu katika mipango na bajeti ili kupambana na uhalifu
-
Kutengemaza
na kukuza uchumi – kwa kutumia sera madhubuti za uchumi ili kuzuia mfumuko wa
bei, kuvutia wawekezaji na kushiriki kikamilifu katika ushindani wa kimataifa
-
Kuimarisha
serikali za mitaa na halmashauri kwa kuzipa madaraka zaidi na kuziwezesha
kuandaa na kutekeleza mipango na bajeti na kuweka taratibu zilizowazi za kutoa
ruzuku kwa halmashauri hizo
-
Kukuza sekta
binafsi – kwa kuweka mazingira mwafaka kwa kuzingatia marekebisho katika sera
na taratibu, kuimarisha miundombinu na kuelekeza taasisi na vyombo vya fedha
kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha watu kuweka akiba na kukopa toka vyombo
hivyo
-
Kubuni
mipango na bajeti ambazo ni kamilifu – kwa kuzingatia masuala ya usawa,
mazingira, na kupiga vita rushwa
-
Mfumo
unaofaa wa kufuatilia utekelezaji wa mkakati wa kupambana na umaskini – kuwa na
vigezo bayana kuhusu maendeleo ya sekta ya vijiji, kilimo, ushirikishwaji wa
wananchi na kupungua kwa umaskini katika ngazi za wilaya na halmashauri
-
Kuimarisha
mageuzi katika sekta ya umma - kwa kuhakikisha uwajibikaji, kuendesha shughuli
za serikali ki-uwazi na kushirikisha jamii pamoja na kupiga vita rushwa
-
Kuongeza
mishahara ya wafanyakazi kwa awamu ili kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa
jamii.
Sekta
zilizopewa nafasi muhimu kwa ajili ya kuchukua hatua za kisera na kupewa
kipaumbele katika mgawanyo wa rasilimali ni pamoja na:
a)
Elimu – Kuboresha Elimu kwa kuongeza ubora na idadi ya shule za
msingi na sekondari, matumizi bora ya rasilimali na kuijengea jamii uwezo wa
kushiriki katika kuzihudumia shule
b)
Afya – Kukarabati miundombinu ya afya, kuhamasisha ushirikiano
kati ya serikali na sekta binafsi na kuboresha uongozi wa huduma za bima ya
afya
c)
Ukimwi – Kutekeleza sera kamilifu ya kupambana na maambukizi ya
ukimwi na kuboresha huduma za msingi za afya
d)
Maji – Kujenga, kukarabati na kuongeza skimu za maji, kuvuna
maji ya mvua, kufanya utafiti juu ya rasilimali za maji na kutoa mafunzo
maalumu kwa ajili ya wataalam katika sekta;
e)
Kilimo - Kuongeza tija na uzalishaji kwa kuboresha huduma za ugani,
umwagiliaji, utafiti na masoko pamoja na kuboresha mazingira ili kuvutia
ushiriki wa sekta binafsi
f)
Barabara - Kukarabati na kuboresha mtandao wa barabara,
kuzifanyia ukarabati barabara za wilaya na mikoa pamoja na kuhamasisha jamii
kushiriki katika uboreshaji wa barabara zao
g)
Utawala bora – Kuimarisha na kuboresha vyombo vya sheria na usalama,
kutekeleza mikakati ya kupiga vita rushwa na kuboresha matumizi ya fedha za
umma
h)
Takwimu muhimu – Kutoa takwimu sahihi na kwa wakati kwa ajili ya
kuboresha sera, sheria, mikakati na mipango.
Maeneo
mengine muhimu:
Ili
kufanikisha juhudi za kupiga vita umaskini na kuimarisha ukuaji wa uchumi
maeneo yafuatayo pia yatapewa kipaumbele:
a)
Nishati - Upanuzi wa uzalishaji na
usambazaji wa umeme, upanuzi wa matumizi ya umeme sehemu za vijijini pamoja na
kuhamasisha matumizi ya vyanzo mbadala vya nishati ikiwa ni pamoja na mionzi ya
jua, upepo, makaa ya mawe, n.k.
b)
Viwanda – Kushawishi sekta binafsi kuwekeza katika usindikaji
wa mazao, kuzalisha nishati, maji, mawasiliano, usafirishaji, utafiti (R&D)
kwa kuzifanyia mapitio sheria na taratibu ili kuvutia uwekezaji wengi zaidi
c)
Ardhi - Kuweka mazingira yatakayohakikisha miliki ya ardhi na
kuepusha matumizi mabaya ya ardhi ikiwa ni pamoja na ujenzi holela
d)
Madini – Kujenga uwezo wa wachimbaji wadogo kwa kuwapatia mafunzo,
teknolojia na taarifa za Masoko
e)
Utalii - Kuboresha na kukarabati miundombinu pamoja na kuvitangaza
vivutio vya utalii vilivyopo.
f)
Maendeleo Vijijini – Kuchukua hatua za kuhakikisha
upatikanaji wa mikopo, masoko ya nje, kufufua viwanda vya kusindika mazao,
kuondoa kodi mbali mbali ambazo ni kero kwa wakulima na wafugaji, kurahisisha
biahsara na nchi jirani pamoja na kusambaza mbegu bora za mazao na mifugo kwa wakulima.
Muhtasari
wa Bajeti ya Mpango:
Katika
kipindi cha 2003/04 mpango na Bajeti ya Maendeleo umelenga katika kuimarisha
mafanikio yaliyokwisha patikana katika kuongeza ukuaji wa uchumi na kuondoa
umaskini uliokithiri. Bajeti ya
Maendeleo inakisiwa kufikia Tsh 807,440,576,900 kati ya hizo Tsh
165,724,798,200 zitapatikana toka vyanzo vya ndani na Tsh 641,715,778,700 ni za
kutoka nje. Kwa upande wa fedha za ndani Tsh 771,949,619,700 ni kwa ajili ya
kutekeleza miradi na programu za wizara na Tsh 35,490,957,700 ni kwa ajili ya
kutekeleza programmu na miradi mbali mbali ya mikoa na halmashauri za wilaya na
miji.
MUHTASARI
WA BAJETI YA MPANGO WA MAENDELEO WA MWAKA 2003/04 KWA SEKTA KUU
Tsh ‘000’
|
|
Fedha
za Hapa |
Fedha
za Nje |
Jumla |
HUDUMA ZA JAMII |
|
|
|
|
Elimu |
4,633,718.2 |
70,863,356.1 |
75,497,074.3 |
|
Afya |
3,552,448.2 |
24,148,846.6 |
27,701,294.8 |
|
Maji na Mifugo |
7,096,856 |
43,657,350 |
50,754,196 |
HUDUMA ZA KIUCHUMI
|
|
|
|
|
Barabara na Mawasiliano |
46,369,000 |
104,201,683 |
150,570,683 |
|
Nishati na Madini |
5,119,552.3 |
96,892,000 |
102,091,552.3 |
|
Ardhi |
600,000 |
- |
600,000 |
HUDUMA ZA UZALISHAJI
MALI
|
|
|
|
|
Kilimo |
6,436,433.2 |
25,081,541 |
31,517,964.2 |
|
Maliasili na Biashara |
952,586,3 |
30,341,201.5 |
31,477,787.8 |
|
Viwanda na BiasharaI |
200,000 |
1,620,469 |
1,820,469 |
UTAWALA
|
|
|
< |