HOTUBA YA
WAZIRI MKUU, MHESHIMIWA FREDERICK T. SUMAYE (MB)
WAKATI WA
KUAHIRISHA BUNGE, TAREHE 9 APRILI 2003
Mheshimiwa
Spika, kabla sijatoa hotuba yangu ninapenda kuungana na Waheshimiwa Wabunge na
wananchi kwa ujumla kutoa salaam zangu za rambirambi kwa familia ya Jaji Mkuu
Mstaafu Marehemu Francis Lucas Nyalali.
Marehemu Nyalali alikuwa mfano wa kuigwa kwa jinsi alivyosimamia kazi
zake katika misingi ya haki. Amekuwa
Jaji Mkuu kwa miaka 23 na hivyo alikuwa kisima kikuu cha busara na hekima
nchini mwetu. Tunaiombea familia ya
marehemu uvumilivu na subira katika wakati huu mgumu wa majonzi makubwa na
tunamwomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa
Spika, kazi zilizokuwa zimepangwa kwa ajili ya Mkutano wa Kumi na Moja wa Bunge
lako Tukufu zimekamilika. Katika
mkutano huu Waheshimiwa Wabunge wamepitisha miswada sita ya sheria na kuridhia
maazimio matatu. Aidha, Serikali
imejibu maswali ya msingi 102 ya Waheshimiwa Wabunge na mengine mengi ya
nyongeza.
Mheshimiwa
Spika, katika mkutano huu Bunge lako Tukufu limepitisha miswada ya sheria yenye
manufaa mbalimbali kwa maendeleo ya Taifa letu. Moja ya miswada hiyo ni Muswada
wa Sheria ya Nishati ya Atomiki ya mwaka 2003 inayoweka mazingira muafaka ya
uendelezaji wa matumizi salama na ya amani ya nishati ya atomiki, teknolojia ya
nyuklia na pia kuweka mfumo madhubuti wa kinga dhidi ya madhara ya mionzi.
Matumizi
ya nishati ya atomiki yatatuhakikishia kuwepo kwa nishati rahisi na yenye
uhakika na hivyo kutuwezesha kuzalisha mali kwa haraka kwa gharama nafuu na kwa
wingi. Nchi yetu hivi sasa inategemea
umeme unaotokana na maporomoko ya maji, mafuta na baadaye gesi ya Songo
Songo. Vyanzo hivi vya nishati
hutupatia umeme ambao ni aghali na usioaminika sana kutegemeana na hali ya hewa
na upatikanaji wa mafuta katika soko.
Nguvu ya nyuklia itatatua matatizo haya kwa kutupatia nishati ya uhakika
na ya bei nafuu jambo ambalo litasaidia sana kukuza uchumi wetu.
Mheshimiwa
Spika, mbali na kuweka mazingira ya uendeshaji wa matumizi ya nishati ya
atomiki, muswada huu unaweka pia masharti ya kulinda afya za wananchi kwa
kudhibiti matumizi ya vyakula vilivyochafuliwa na mionzi na unaweka kinga dhidi
ya madhara yote yanayotokana na mionzi kwa binadamu, wanyama, mimea na mazingira.
Mheshimiwa
Spika, Bunge lako Tukufu limepitisha pia Muswada wa Sheria ya Ushindani wa Haki
wa Mwaka 2003 (The Fair Competition Bill, 2003). Katika dunia ya leo yenye uchumi huria na
utandawazi, ushindani wa kibiashara mara nyingi sio wa haki kama haudhibitiwi. Mara nyingi makampuni makubwa huweza kuunda
vikundi vya kupanga bei, kufanya makubaliano ya kupunguza uzalishaji, kupanga
bei ya zabuni, n.k. mambo ambayo huathiri mwenendo wa uchumi. Aidha, baadhi ya wafanyabiashara wanayo pia
tabia ya kudanganya kuhusu viwango vya ubora wa bidhaa zao na matumizi yake.
Muswada
huu ni muhimu sana kwa kuwa unaweka utaratibu muafaka wa kusimamia mashindano
katika biashara, unalenga katika kudhibiti matumizi mabaya ya nguvu za soko na
kuhakikisha kwamba maadili mema ya kibiashara yanafuatwa na kila mmoja na
hatimaye kumlinda mlaji. Moja ya
maadili hayo ni pamoja na kuhakikisha kwamba taarifa muhimu zinaonyeshwa kwenye
bidhaa kuhusu usalama wa bidhaa husika.
Masharti haya ya kusimamia ushindani halali wa biashara ni kigezo muhimu
katika kuvutia biashara za kimataifa na uwekezaji kutoka nje. Sheria hii itasaidia sana uchumi wetu katika
nyanja hizi za uwekezaji.
Mheshimiwa
Spika, Bunge lako Tukufu limepitisha pia Muswada wa Sheria ya Mamlaka ya
Kuratibu Mawasiliano Tanzania wa Mwaka 2003 (The Tanzania Communications
Regulatory Authority). Madhumuni ya
Muswada huu ni kuanzisha mamlaka mpya ya udhibiti wa sekta za mawasiliano. Mamlaka hii itasimamia shughuli za watu na
taasisi zinazoendesha biashara ya mawasiliano kwa njia ya simu, matangazo ya
redio na televisheni, utoaji wa huduma za posta na teknolojia ya
elektroniki. Muswada huu unaweka
mamlaka ya udhibiti ili kuwasimamia kwa karibu watoaji huduma hizi za
mawasiliano. Katika kuwasimamia,
mamlaka hii imepewa uwezo wa kutoa leseni na kufuta leseni kwa wale
watakaokwenda kinyume na viwango (standards) vya utoaji huduma
vilivyowekwa na kusimamia upangaji wa bei (rates and charges) za huduma
hizi kwa walaji na kuzingatia kuwa huduma hazileti athari kwa maadili ya jamii.
Mheshimiwa
Spika, Bunge lako Tukufu limepitisha Muswada wa Sheria ya Kuifanyia Marekebisho
Sheria ya Mikopo, dhamana na Misaada ya
Mwaka 2003 kwa madhumuni ya kusimamia vizuri zaidi ukopaji kutoka vyanzo vya
ndani na nje ya nchi kwa kuifanyia marekebisho Sheria ya Bunge namba 30 ya
Mwaka 1974 iliyokuwa ikisimamia ukopaji huo.
Muswada
unalenga kuweka sheria ya kusimamia kwa karibu Deni la Taifa na kuandaa
utaratibu mpya wa kusimamia madeni ya Taifa ili Serikali iweze kujua deni
halisi la ndani na la nje kwa wakati wowote.
Muswada pia unampa Waziri wa Fedha mamlaka ya kisheria ya kukopa ndani
na nje na kutoa dhamana kwa niaba ya Serikali na kupiga marufuku mtu mwingine
yeyote kuiingiza Serikali katika madeni.
Katika kutekeleza wajibu wake, Waziri wa Fedha atakuwa anashauriana na
Kamati ya Kitaifa ya Kusimamia Madeni.
Lengo ni kuweka udhibiti madhubuti katika kukopa, matumizi ya mikopo
hiyo na matumizi ya fedha za misaada kutoka nje. Muswada huu ni muhimu sana kwa uchumi wetu na kwa utoaji wa huduma
bora kwa wananchi wetu. Aidha, ni
muswada muhimu sana kwa washiriki wetu katika maendeleo kwa sababu unaweka
udhibiti mzuri katika ukopaji wa Serikali.
Mheshimiwa
Spika, Bunge pia limepitisha muswada wa sheria unaounda Mamlaka ya Udhibiti wa
Usafiri wa Anga (Tanzania Civil Aviation Authority) ili kusimamia huduma
zote za usafiri wa anga. Lengo ni kuwa
na mamlaka itakayosimamia na kuratibu shughuli hii muhimu na kuhakikisha kuwa
usalama wa anga yetu hauathiriki wala usalama wa raia kudhurika. Mamlaka hii ni muhimu kwa uchumi wetu kwa
sababu biashara za mataifa zinategemea sana uwingi na usalama wa usafiri na
usafirishaji katika nchi husika. Bunge
pia limepitisha Muswada wa Kufanya Marekebisho katika Sheria Mbalimbali kwa
lengo la kuziboresha au kuendana na sheria zingine zilizotungwa.
Mheshimiwa
Spika, kama nilivyosema mwanzoni, Bunge lako Tukufu limepitisha pia maazimio
matatu. Moja ya maazimio hayo ni lile
linalohusu Kuridhia Mkataba wa Usafirishaji kwa Njia za Barabara wa Jumuiya ya
Afrika Mashariki uliotiwa saini tarehe 29 Novemba, 2001. Mkataba huu ni muhimu sana katika kuimarisha
Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa vile unahuisha (harmonize) mambo muhimu
kama vile kodi, ada na ushuru vinavyotozwa mipakani, unaweka uwiano wa kisheria
katika matumizi ya barabara, unaondoa ucheleweshaji wa mizigo mipakani na
kurahisisha safari za wananchi kwenda nchi nyingine ya Jumuiya.
Mheshimiwa
Spika, Bunge lako Tukufu limepitisha pia azimio la kuridhia Itifaki ya Mkataba
wa Afrika Mashariki kuhusu ushirikiano katika kuhakiki na kuthibitisha viwango
vya ubora wa bidhaa na vipimo (Protocol on Co-operation in Standardization,
Quality Assurance, Metrology and Testing).
Itifaki ya mkataba huu ilisainiwa tarehe 15 Januari 2001 na Mawaziri wa
nchi zetu tatu ambazo ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Itifaki hii ni muhimu sana katika kuendeleza
biashara baina ya nchi yetu, Kenya na Uganda kwa sababu inaondoa vikwazo vya
biashara vinavyotokana na tofauti katika ubora wa viwango vya bidhaa, mizani na
vipimo. Maendeleo ya biashara mahali
popote duniani yanategemea sana ubora wa bidhaa zinazozalishwa. Bidhaa duni haziwezi kushindana kikamilifu
na kupata bei nzuri katika soko la karne hii.
Mheshimiwa
Spika, Bunge lako Tukufu limepitisha pia azimio la kuridhia Mkataba wa
Ushirikiano wa kiuchumi, kisayansi na kiufundi baina ya Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Korea (Agreement on Economic,
Scientific and Technical Co-operation between the Government of the Republic of
Korea and the Government of Tanzania).
Mkataba huu ulitiwa saini na nchi hizi mbili huko Seoul, Korea tarehe 18
Desemba, 1998. Mkataba huu ni muhimu
sana kwa nchi yetu kwa kuwa unatupa fursa ya kukuza uwezo wetu wa kitaaluma na
utafiti, kupata elimu ya juu na ile ya ufundi kutokana na kubadilishana
wataalam, matokeo ya tafiti mbalimbali, majarida, habari za kitaalam na
kushiriki katika semina, makongamano na mikutano mingine ya aina hiyo baina ya
nchi hizi mbili.
Mheshimiwa
Spika, baada ya kutoa ufafanuzi kwa kifupi wa yale tuliyofanyia kazi Bungeni
kwa manufaa ya wananchi, naomba sasa nizungumzie maeneo mengine muhimu
yafuatayo:
Mheshimiwa
Spika, hivi sasa kuna vita vinavyoendelea Mashariki ya Kati kati ya Marekani na
Washirika wake dhidi ya Iraq. Matumaini
ya kila mmoja wetu ni kuwa vita hivyo vitakwisha haraka ili visilete madhara
makubwa kwa uchumi wa dunia. Pamoja na
juhudi mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali yetu za kupunguza madhara
yanayoweza kuletwa na vita hivi kama alivyoelezea Mheshimiwa Rais Mkapa katika
hotuba yake ya mwishoni mwa mwezi Machi, 2003, ni vema wananchi kwa upande wetu
tukachukua tahadhari muhimu kwa maana hasa ya kupunguza matumizi yasiyo ya
lazima. Kwa mfano, gharama za mafuta
zinaonekana kupanda, tupunguze matumizi ya mafuta yasiyo ya lazima, n.k. Bado hatujajua biashara itaathirika kiasi
gani na hivyo kuathiri mapato ya Serikali kwa sababu athari hii hujitokeza
polepole na kukaa kwa muda mrefu.
Hivyo, tunahitajika kuwa waangalifu sana katika matumizi ya fedha kwa
sababu kama mapato yataathirika, kwa vyovyote vile matumizi pia yataathirika.
Mheshimiwa
Spika, Mheshimiwa Rais Mkapa katika hotuba yake ya mwishoni mwa mwezi
niliyoitaja alizungumzia kwa kirefu sana juu ya athari za hali ya hewa
inayotukabili nchini hivi sasa. Sitaki kurudia
yote aliyoyasema Mheshimiwa Rais lakini nasisitiza tu kuwa mvua alizotuasa
Mheshimiwa Rais tuzitumie vizuri ndizo hizi zinazonyesha sasa katika baadhi ya
maeneo nchini mwetu. Tunachotakiwa ni
kuzitumia mvua hizi kwa ukamilifu kadri inavyowezekana. Hotuba ya Rais imeweka maelekezo mengi
bayana katika suala hili. Wakuu wa
mikoa na wakuu wa wilaya wote watapelekewa nakala za hotuba hiyo kwa
utekelezaji. Hivyo, utekelezaji huo
uanze mara moja kwa usimamizi wa matumizi ya mvua hizi zinazonyesha sasa na
mengine yafuatie. Kama nyongeza kwa
maelekezo haya ya Rais, Wakuu wa Mikoa pia wamepelekewa maelekezo mengine
kutoka kwa Waziri wa Kilimo na Chakula na kutoka kwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa
Spika, leo mwezi Aprili 2003 ni mwaka wa saba na nusu wa uongozi wa awamu ya
tatu yaani uongozi wa Rais Mkapa na mwaka wa pili na nusu wa kipindi cha pili
cha awamu hiyo ya tatu. Kipindi cha
miaka saba na nusu sio haba lakini siyo kikubwa kwa maana ya uongozi wa nchi. Katika vipindi mbalimbali vilivyopita na
hata hivi sasa kuna baadhi ya watu ambao wamekuwa wakiandika makala mbalimbali
katika vyombo vya habari, hasa baadhi ya magazeti kuilaumu Serikali ya Rais
Mkapa na kwa mjumuiko Chama cha Mapinduzi kuwa hakuna lolote lililofanyika na
hali za wananchi zimeendelea kuwa duni zaidi.
Inawezekana kabisa haya yanasemwa kwa sababu kipindi cha miaka saba na
nusu kwa wengine ni kipindi kirefu sana na huenda watu wamesahau yaliyotokea
tangu wakati huo hadi sasa. Lakini pia
inawezekana sana wengine hawana habari ni nini kimetokea katika miaka hiyo saba
na nusu au hata katika hii miaka miwili na nusu ya kipindi hiki cha pili cha
awamu ya tatu.
Mheshimiwa
Spika, lengo langu siyo kulinganisha awamu zingine na awamu ya tatu, la
hasha! Kwanza awamu zote tatu zilikuwa
chini ya CCM na mzazi wake CCM yaani TANU.
Aidha, kila awamu imeishi chini ya mazingira tofauti na nyingine na kila
awamu imekuwa na mafanikio yake na matatizo yake pia. Na muhimu zaidi, kwa vile zote zilikuwa chini ya CCM, kila awamu
iliyopewa madaraka na wananchi iliendeleza yale yaliyofanywa au kuanzishwa na
awamu iliyotangulia. Nitataja tu baadhi
ya vipengere ili kujibu baadhi ya hoja zinazojitokeza.
Hali ya Uchumi:
Mheshimiwa
Spika, hali ya uchumi wetu imeendelea kukua.
Tangu awamu ya tatu ilipoingia madarakani ukuzaji wa uchumi umeendelea
kwa kuendeleza marekebisho (reforms) katika sekta mbalimbali. Marekebisho hayo yamefanyika katika vyombo
vya fedha na mabenki, utumishi wa umma, sekta binafsi, mashirika ya umma na
hata katika mfumo wa siasa. Matokeo ya juhudi
hizi zote ni mazuri kwani uchumi wetu
umekua kwa wastani wa asilimia 3 hadi kufikia zaidi ya asilimia 5.5. Aidha, sekta binafsi imeweza kuchukua nafasi
yake stahili ya kipaumbele katika kuendesha uchumi wetu. Mapato ya fedha za kigeni nayo yaliongezeka
na mfumuko wa bei uliteremka kutoka wastani wa asilimia 30 mwaka 1995 mpaka
wastani wa asilimia 4.5 hivi sasa. Kwa
ajili ya kufanya vizuri katika kurekebisha na kuendesha uchumi wetu, nchi yetu
ilifanikiwa kukubaliwa kuingizwa katika mpango wa nchi maskini zinazo samehewa
madeni, yaani HIPC na kuwa moja ya nchi nne duniani kufanikiwa kuingia katika
mpango huo. Mpango huu umekuwa na manufaa sana kwa nchi yetu kwa sababu
tumeweza kuwa na uwezo zaidi wa kuhudumia huduma mbalimbali za jamii kwa sababu
HIPC hutupatia unafuu wa fedha katika bajeti yetu, hutuwezesha kukopa fedha kwa
miradi muhimu na husaidia kuwavutia wawekezaji kwa sababu ya kuwa na imani na
jinsi uchumi wetu unavyoendeshwa.
Kuna watu wanaodhani kuwa kigezo cha kuingia HIPC ni umasikini. Hiyo siyo kweli. Kigezo muhimu sana ni jinsi unavyosimamia uchumi wako kwa umakini
kwa kufuata misingi inayokubalika ya kiuchumi.
Tanzania tumefikia na kuvuka kigezo hicho. Ninapenda kumpongeza sana Rais Mkapa kwa juhudi kubwa aliyoiweka
katika kukuza na kusimamia uchumi wetu.
Mapato na matumizi ya Serikali:
Mheshimiwa
Spika, hali ya mapato ya Serikali mwaka 1995 ilikuwa ni duni sana. Serikali yetu ilikuwa inakusanya wastani wa
shilingi bilioni 27 hadi 30 kwa mwezi.
Hali hii hivi sasa imebadilika na wakati mwingine mapato yetu yanafikia
shilingi bilioni 100 kwa mwezi. Aidha,
kabla ya mwaka 1996 nchi yetu ilikuwa imenyimwa misaada na mikopo kutoka nje
kwa sababu ya mazingira ya uchumi tuliyokuwa nayo. Hivi leo kwa sababu ya kufanya vizuri katika uchumi sasa tunapata
misaada na mikopo. Katika kipindi cha
miaka mitatu ya mwanzo hali yetu ya mapato bado ilikuwa ngumu hivyo matumizi
yetu yalikuwa kwa misingi ya kutumia kile tunachopata, yaani Cash Budget. Kwa hiyo, hatukuwa na fedha za maendeleo na
wakati mwingine hata fedha za matumizi ya kawaida hazikupatikana kwa vipindi
virefu hali iliyoathiri sana ufanisi katika utendaji wa Serikali. Matumizi ya Cash Budget pia huathiri
sana usafi wa taarifa za ukaguzi wa hesabu za Serikali. Hii hutokana na kuwa fedha zinazopatikana
katika siku au mwezi wa mwisho wa mwaka wa fedha wa Serikali, taarifa zake ni
vigumu sana kuwahi ukaguzi hasa kama fedha hizo zimepelekwa katika wilaya za
pembezoni. Aidha, uduni wa mawasiliano
kati ya mikoa na wilaya hizo na mikoa na Dar-es-Salaam huzidisha pia tatizo
hili. Kwa sababu hii, wapo baadhi ya
watu ambao hutumia taarifa hizi kuishambulia Serikali kana kwamba fedha hizo
zote zimeibiwa. Baada ya taarifa za
ukaguzi kutoka, maafisa wahasibu hujibu hoja mbalimbali za Mkaguzi na Mdhibiti
Mkuu wa Serikali na kwa sehemu kubwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu ameridhika sana
na majibu yanayotolewa na Serikali.
Huduma za Jamii na kupambana na
umasikini:
Mheshimiwa
Spika, moja ya kigezo muhimu cha kupima hali ya umasikini ni jinsi huduma za
jamii zinavyopatikana. Penye umasikini
uliokithiri huduma hizi huwa duni sana.
Lakini uboreshaji wa huduma za jamii nayo ni nyenzo muhimu ya kupambana
na umasikini. Kwa mfano, kama una taifa
lenye elimu nzuri, lenye wananchi wenye afya nzuri, kuna njia nzuri za
mawasiliano, n.k. ni nyenzo muhimu sana kwa taifa hilo kusonga mbele na
kuachana na umasikini. Kwa sababu ya
umuhimu huo, Serikali ilitoa kipaumbele katika kuelekeza rasilimali chache
ilizonazo katika sekta za huduma za jamii.
Kipaumbele hicho kilihusiana na fedha zetu wenyewe na fedha za washirika
wetu katika maendeleo. Kwa mfano, fedha
za mfuko wa madeni na fedha za HIPC, sehemu kubwa zilielekezwa katika sekta za
huduma za jamii kama mbinu za kupambana na umasikini. Kwa sababu hiyo, kumekuwa na mafanikio makubwa katika sekta hizo
kama nitakavyozielezea:
ELIMU:
(i) Elimu ya Msingi
Mheshimiwa
Spika, ilani za uchaguzi za CCM ya mwaka 1995 na ya mwaka 2000 zote zimeweka
msisitizo sana katika elimu ya msingi kama haki ya mtoto wa Tanzania. Katika kutekeleza ilani hizo Serikali
imefanya kila juhudi kufikia malengo yaliyokusudiwa. Sote tunaelewa mapungufu makubwa yaliyokuwepo katika elimu yetu
ya msingi. Vyumba vya madarasa vya
kutosheleza havikuwepo, na vilivyokuwepo vingi vilikuwa katika hali mbaya,
nyumba za walimu, vyoo vya wanafunzi vilikuwa na upungufu mkubwa, vifaa vya
kufundishia na vitabu vilikuwa havipo, n.k.
Ili kukabiliana na hali hii maamuzi muhimu ilibidi yachukuliwe na
Serikali; kwa mfano:
·
Operation ya utengenezaji madawati nchi nzima;
·
Ujenzi wa majengo muhimu ya shule;
·
Ajira ya walimu wenye sifa;
·
Kuwafunza walimu
waliokuwa kazini upya (upgrading courses);
·
Kuwaandikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule;
·
Kuondoa ada na michango kwa shule za msingi ili kusiwe na
kisingizio cha watoto kutokwenda shule;
·
Kuanzisha mradi wa maendeleo
wa shule za msingi (MMEM);
·
Kuendelea kuongeza bajeti katika sekta.
Mheshimiwa
Spika, juhudi hizi zimezaa matunda mengi na mazuri. Hadi leo zaidi ya vyumba vya madarasa vya kisasa 40,000 vimekwishajengwa,
nyumba za walimu zaidi ya 17,000 zimejengwa, madawati zaidi ya 880,000
yametengenezwa, idadi kubwa ya walimu wameajiriwa na vitabu na zana zingine za
kufundishia kupelekwa shuleni. Matokeo
ya juhudi hizi ni kuwa hivi leo pamoja na alama za kufaulu mtihani wa darasa la
saba kupandishwa, sasa tuna tatizo la watoto waliofaulu kubaki nyumbani tofauti
na huko nyuma ambapo shule za sekondari zilikuwa zinakosa wnafunzi waliofaulu
na hivyo kuchukua hata walio na alama za chini.
(ii) Elimu zingine
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa hatua zingine zinazofuata za elimu hali ni hiyo hiyo. Kumekuwepo na mafanikio makubwa sana. Idadi ya shule za sekondari imeongezeka hasa
zinazojengwa na wananchi na kukabidhiwa serikalini na zinazoendeshwa na
taasisi, madhehebu au watu binafsi.
Jumla ya sekondari zaidi ya 450 zimejengwa katika kipindi hicho. Aidha, elimu ya wasichana imetiwa mkazo
katika ngazi zote. Kwa upande wa
mafunzo ya ufundi, vyuo vinavyotoa elimu hiyo vimeongezeka. Zaidi ya vijana 20,000 wamefaidika na
mafunzo hayo kati ya 1995 – 2000. Kwa
upande wa vyuo vikuu, kuna maendeleo makubwa na vyuo vikuu sasa viko zaidi ya
kumi na vingine vinaendelea kuandikishwa.
AFYA:
Mheshimiwa
Spika, utoaji wa huduma za afya ni muhimu ili kuwa na taifa lenye watu wenye
afya. Tangu mwaka 1995 juhudi kubwa
zimefanyika kuboresha huduma hiyo.
Tutakumbuka kuwa hali ya huduma za matibabu haikuwa nzuri na ilikuwa ni
vigumu hata kupata madawa ya kawaida katika hospitali za umma. Vifaa vingine vya upasuaji havikuwepo na
mara nyingi ilibidi mgonjwa au ndugu zake wavitafute. Hali hiyo hivi sasa haipo.
Leo madawa muhimu yanapatikana katika hospitali zote mpaka zahanati za
vijijini. Wazee, wakina mama wajawazito
kwa huduma za uzazi na watoto wadogo wanatibiwa bure. Aidha, majengo ya kutolea huduma hizi za afya na vifaa muhimu
vimeboreshwa. Zahanati zaidi ya 1180
ama zimejengwa au kukarabatiwa, vituo vya afya 183 vimejengwa na hospitali
kadhaa kujengwa ama kukarabatiwa. Hali
ni hivyo hivyo kwa nyumba za madaktari, waganga na watumishi wengine wa
afya. Uboreshaji wa huduma umeendelea
kwa kununulia hospitali na vituo vya afya vifaa muhimu. Kwa upande wa hospitali za wilaya na mikoa
karibu zote sasa zina vifaa vya kisasa vya X-ray, Ultrasound machines, darubini
za kisasa, vifaa vingine muhimu vya maabara, n.k. Aidha, huduma muhimu za chanjo kwa watoto zimeendelea kutolewa
kwa mafanikio makubwa, na vivyo hivyo kwa huduma zingine za kinga na tiba. Aidha, matatizo ya milipuko ya magonjwa
yameshughulikiwa mara yalipojitoleza.
MAJI:
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa maji juhudi kubwa zimefanyika kuboresha utoaji wa huduma
hiyo muhimu. Visima vifupi na virefu
zaidi ya 8,600 vimechimbwa, visima vingi vya zamani vimekarabatiwa, mifuko ya
maji vijijini zaidi ya 2,200 imeanzishwa na bodi za maji safi na majitaka
kuanzishwa katika karibu miji yote nchini.
Haya yote yameboresha kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa maji kwa
wananchi.
BARABARA:
Mheshimiwa
Spika, sekta ya barabara ni sekta muhimu sana kwa maendeleo ya uchumi na upatikanaji
wa huduma kwa wananchi. Ili kuleta
ufanisi katika eneo hili muhimu Serikali ilianzisha wakala wa barabara ili
kusimamia ujenzi na ukarabati wa barabara kuu na kutumia halmashauri za wilaya,
miji, na jiji kusimamia ujenzi wa barabara zilizoko chini ya milki yao kwa
kupewa asilimia 30 ya fedha zinazokusanywa na mfuko wa barabara. Barabara kuu ambazo zimejengwa au zipo
katika hatua mbalimbali za ujenzi wa kiwango cha lami ni kama, Ubungo-Mlandizi,
Chalinze-Melela, Kawawa Road Dar-es-Salaam, Makuyuni-Ngorongoro Gate, Mutukula-Muhutwe-Kagoma, barabara za Mwanza mjini hadi
Airport, Nyanguge-Mwanza, Bagamoyo-Wazo Hill, Mwanza-Mto Magogo,
Songwe-Tunduma, Makutano-Butiama-Kiabakari, Tunduma-Sumbawanga, Nzega-Shellui,
Ndundu Somanga, Morogoro-Dodoma, Dodoma-Manyoni, Dar-es-Salaam – Kibiti, daraja la Mto Rufiji, barabara ya
Kitonga escarpment, na nyingine nyingi fupifupi. Aidha, barabara nyingi zimetengenezwa kwa
viwango vya changarawe na udongo hasa kwa kutumia fedha zinazotolewa kwa
Halmashauri za Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa
Spika, Waheshimiwa Wabunge watakubaliana nami kuwa kabla ya mwaka 1995 barabara
katika manispaa zetu ikiwa ni pamoja na jiji la Dar-es-Salaam zilikuwa
hazipitiki kabisa. Mradi wa Urban
Sector Rehabilitation Project ulikarabati barabara na mifumo ya maji safi na
maji taka katika manispaa za Tanga, Moshi, Arusha, Morogoro, Iringa, Mbeya,
Mwanza na Tabora. Jiji la
Dar-es-Salaam nalo lilishughulikiwa chini ya utaratibu tofauti na barabara hizo
zote zimeboreshwa. Hali ya manispaa zetu
sasa zinapendeza.
MASLAHI
YA WATUMISHI:
Mheshimiwa
Spika, mwaka 1995 mshahara wa kima cha chini serikalini ulikuwa shilingi
17,500/= kwa mwezi. Leo kima hicho
kimepanda hadi shilingi 55,000/= kwa mwezi.
Bado kima hiki hakitoshelezi mahitaji ya mtumishi na familia yake,
lakini kuna unafuu mkubwa na utumishi wa umma sasa una heshima ndani ya
jamii. Fedha hizi zimeleta unafuu hasa
kwa vile mfumko wa bei (inflation) umeteremka sana. Maslahi haya yataendelea kuboreshwa kadri
uchumi wetu unavyokua.
UBINAFSISHAJI,
UWEKEZAJI NA AJIRA:
Mheshimiwa
Spika, sera ya ubinafsishaji na kuvutia wawekezaji ni sera ya msingi katika
marekebisho ya uchumi. Sera hii pia ipo
katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 1995 na ya mwaka 2000. Katika sera hiyo na maelekezo ya ilani ya
CCM, ubinafsishaji utaendelea kwa mashirika ya umma yaliyobaki ili yaweze
kuchangia katika uchumi kwa ufanisi zaidi.
Hivi sasa idadi kubwa ya mashirika na makampuni ya umma yamebinafsishwa
na zoezi hilo linaendelea. Kwa yale yaliyo binafsishwa, mengi yemeonyesha
mabadiliko makubwa ya heri katika uzalishaji, na yapo yanayoendelea kutafuta
mtaji wa kuwekeza.
Mheshimiwa
Spika, katika siku za karibuni kumekuwa na baadhi ya watu na hasa baadhi ya
magazeti ambayo yamekuwa yakiandika kuwa ubinafsishaji umeleta umasikini zaidi
hasa kwa kuondoa ajira kwa Watanzania.
Hii siyo kweli. Kabla ya
utekelezaji wa sera ya ubinafsishaji tujiulize mashirika yetu yalikuwa katika hali
gani! Ninatoa mifano michache tu. Makampuni na mashirika yetu yaliyokuwa na
ajira kubwa ni pamoja na viwanda vya nguo na mashamba makubwa. Kwa upande wa viwanda, kiwanda cha Mwanza
Textiles, Kilimanjaro Textiles, Musoma Textiles, Sungura Textiles, Mbeya
Textiles, Morogoro Polytex na vinginevyo vilikwisha funga uzalishaji. Hivi na hapo tulikuwa tunahesabu kulikuwa na
ajira? Nina hakika kama vyote hivi
vingebinafsishwa mapema ajira nzuri, japo inaweza isiwe kubwa kama huko nyuma
ingepatikana.
Kwa
upande wa mashamba, mashamba ya miwa ya Kilombero, Mtibwa na TPC (Arusha chini)
yalikuwa yanazalisha kwa shida sana na mengine yalikuwa hayajawalipa
wafanyakazi wao kwa zaidi ya miezi sita.
Mengine yaliwalipa wafanyakazi kwa kutumia sukari badala ya fedha. Shamba la Kagera lilikwisha funga shughuli
zake. Leo viwanda hivi vinazalisha kwa
zaidi ya mara mbili ya viwango vyake vya kabla ya ubinafsishaji na kutoa ajira
na huduma ya bidhaa za uhakika kwa Watanzania.
Mashamba mengine ya umma kama mashamba ya Ngano – Hanang, mashamba ya
Mahindi na Kahawa Mbozi, mashamba ya mpunga Mbarali, Ruvu, Dakawa na mengineyo
ama hayazalishi kabisa au yanazalisha kidogo sana kwa kukodisha ardhi zao. Watumishi waliokuwepo wanaishi kwa utaratibu
wanaoujua wenyewe. Hali hii wala
haitofautiani sana ukienda katika sekta ya mahoteli. Hoteli kama Kilimanjaro, Bahari Beach, Kunduchi Beach, Dodoma
Hotel, Tabora Hotel na Moshi Hotel zilikwisha funga shughuli zao kabla ya
ubinafsishaji. Hali ni hivyo hivyo kwa
mashirika kama Shirika la Usagishaji la Taifa (NMC), mashamba ya ng’ombe wa
maziwa ya DAFCO, mashamba ya ng’ombe wa nyama, mashamba ya mkonge, mashamba ya
chai na viwanda vyao.
Mheshimiwa
Spika, ningeweza kusema hivi kwa sekta zote na hali isingelikuwa tofauti
sana. Nakubali kuna mashirika
yaliyokuwa yanaonekana yanafanya vizuri machoni pa watu. Mashirika hayo yalipobinafsishwa, baadhi ya
wafanyakazi walipunguzwa, na baadhi ya watu walilalamika. Tukumbuke baadhi ya mashirika na makampuni
hayo yalionekana hivyo kwa sababu yalikuwa yanafanya kazi katika mazingira ya
ukiritimba. Katika mazingira ya sasa ya
ushindani mkali nina hakika hali ingelikuwa tofauti. Katika hali ya ushindani mkali, wafanyakazi watakaoajiriwa ni
wale tu wanaohitajika.
Mheshimiwa
Spika, siyo kweli kuwa ubinafsishaji umeua ajira. Sehemu kubwa ya ajira yetu ilikwishajifunga. Ubinafsishaji katika baadhi ya mashirika
yaliyokuwa yanafanya kazi ni kweli imeua ajira isiyohitajika na umeboresha
ajira inayohitajika katika uzalishaji.
Haya ni mambo mema kwa uchumi wetu na kwa watu wetu. Tukitaka kupata ajira nzuri ya uhakika ni
lazima kwanza, makampuni ya kutuajiri yawepo na pili, kampuni
hizo zifanye kazi vizuri. Ninaamini
kabisa katika hili sera ya CCM na ilani ya CCM ni sahihi na utekelezaji wa
Serikali ni makini.
Mheshimiwa
Spika, wapo wanaosema ubinafsishaji haufanywi kwa uwazi. Tumeunda Tume ya Rais ya Kurekebisha
Mashirika ya Umma (PSRC) kwa Sheria ya Bunge na Tume inafanya kazi zake kwa
uwazi kwa kutangaza katika magazeti yote mashirika yanayouzwa. Barua za maombi hufunguliwa hadharani na
baada ya hapo makamishna wa Tume hushughulikia ubinafsishaji na kuwasilisha
mapendekezo yao kwa wizara husika ambayo huleta mapendekezo ya wizara
serikalini kwa uamuzi. Hivi hapo siri
ipo wapi? Napenda kuuthibitishia umma
wa Watanzania kuwa hakuna siri yoyote katika ubinafsishaji wa mashirika na
makampuni ya umma.
Kupambana na Kero Mbalimbali:
Mheshimiwa
Spika, Serikali imeendelea kupambana na kero mbalimbali za wananchi zikiwemo za
huduma za jamii kama nilivyokwishaelezea, kero za rushwa, kero za kutokuwa na
chakula, ukosefu wa ajira, ukosefu wa mitaji, usalama wa raia, madhara
yanayosababishwa na wakimbizi, n.k. Kwa
upande wa uboreshaji wa utawala na kupambana na tatizo la rushwa, juhudi kubwa
pia zimechukuliwa. Taasisi ya kupambana
na rushwa imeimarishwa, hatua za kisheria na kiutawala zimeendelea kuchukuliwa
dhidi ya wanaopatikana na rushwa, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
imekwisha undwa na utawala unaendelea kuimarishwa katika ngazi mbalimbali hasa
kwa kuendelea kuimarisha maboresho katika mfumo wa Serikali za Mitaa. Kwa upande wa kilimo, juhudi kubwa
zimefanyika hasa kwa mazao ya chakula.
Kwa miaka mitatu mfululizo wakati hali ya hewa ilipokwa nzuri, nchi yetu
siyo tu imejitegemea kwa chakula bali iliweza kuwasaidia chakula majirani zetu
wa kusini waliokuwa na shida ya chakula.
Kwa muda sasa tumepata tatizo la bei kushuka sana katika masoko ya dunia
kwa mazao yetu makuu ya biashara. Hili
ni tatizo nje ya uwezo wetu. Hata
hivyo, juhudi zinafanywa kupambana na tatizo hili kwa kuzalisha zaidi, kuongeza
ubora na kusindika mazao kuongeza thamani kwa mazao hayo.
Mheshimiwa
Spika, baada maelezo haya mafupi kwa sekta hizi chache, sijui kama bado
watakuwepo wanaosema Serikali ya Rais Mkapa haijafanya kitu. Hata jana kuna makala katika gazeti moja
yaliyosema “Tutarajie nini uchaguzi wa 2005? Wananchi wanazidi kuwa fukara kila siku.” Makala kama haya siyo ya kwanza wala hayako
tu katika gazeti hili. Lakini mimi
ninataka kusema hivi sasa:
·
Watanzania hivi sasa wanakula vizuri zaidi kwa sababu kwa
sehemu kubwa tunajitosheleza wenyewe kwa chakula.
·
Watoto wenye umri wa kwenda shule kwa kiwango kikubwa,
zaidi ya asilimia 85 wanakwenda shule bila gharama ya mzazi moja kwa moja, na
ifikapo mwaka 2005 watoto wote watakuwa wanasoma elimu ya msingi.
·
Huduma za afya ni nzuri zaidi na madawa yanapatikana hadi
zahanati za vijijini.
·
Makundi yasiyo na uwezo yanahudumiwa matibabu bila kulipia.
·
Hali ya upatikanaji wa maji mijini na vijijini ni nafuu
sana.
·
Hali ya barabara zetu za vijijini na barabara kuu na hali
ya mawasiliano mengine ni bora zaidi.
·
Elimu kwa ujumla imeboreka kuanzia ngazi za chini hadi chuo
kikuu.
·
Mapato ya Taifa (GDP) yameongezeka na kiwango cha ongezeko
la pato hilo kwa mwaka imekuwa ikiongezeka.
·
Mfumko wa bei umeshuka sana.
·
Pato la mwananchi limeongezeka kutoka kiasi cha US $ 120
mwaka 1995 hadi US $ 280 – 300 kwa mwaka hivi sasa (2003).
Mheshimiwa
Spika, hivi kwa haya yote bado kuna wanaoona Mtanzania sasa ana hali ngumu
kuliko huko nyuma? Labda tafsiri yao ya
umasikini ni tofauti na tafsiri rasmi ya kitaalam. Kama siyo tatizo la tafsiri, basi labda ni tatizo la watani wa
jadi ambapo mtani anaweza tu akakataa kuwa marehemu hajafa na akajidai anaongea
naye na kuchekeshwa sana na aliyoambiwa na marehemu. Mimi ninaamini maisha ya Mtanzania yamekuwa bora zaidi na umasikini
umepungua sana hasa kwa wale wanaojituma kufanya kazi. Kwa wale wasiotaka kufanya kazi ni kweli
umasikini utawaelemea kwa sababu wao wanaukumbatia!
Mheshimiwa
Spika, sikatai kuwa bado kazi ni kubwa mbele yetu na wala haitakuwa rahisi hata
kama tungekuwa na pato la Mtanzania la US $ 2,500 ambayo tumepanga kuifikia
mwaka 2025 kama Dira ya Taifa ya maendeleo inavyoelekeza. Lakini tutaendelea kujitahidi kuboresha
kadri tunavyopata uwezo wa kiuchumi kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya mwaka
2000 ya CCM.
Mheshimiwa
Spika, kabla sijamalizia hotuba yangu naomba nikiri kuwa kuna maeneo mawili
ambayo ni tatizo kwa ufanisi wa shughuli za Bunge na Wabunge. Maeneo hayo ni ufinyu wa ukumbi wa Bunge. Aidha, ukumbi huu kwa vile haukujengwa kwa
ajili ya Bunge, haukidhi sana haja ya Bunge. Bado tunakumbuka sakata iliyowapata Waheshimiwa
Wabunge wakati wa dharura ya tetemeko la ardhi. Serikali inaliangalia jambo hili kwa lengo la kulitatua. Eneo la pili ni la Ofisi za Waheshimiwa
Wabunge katika majimbo yao. Hili nalo
Serikali imelitolea maagizo mapya na taarifa rasmi zinatarajiwa ofisini kwa
Waziri Mkuu mwishoni mwa mwezi huu ili hatua zinazoweza kuchukuliwa
zichukuliwe.
Mheshimiwa
Spika, baada ya maelezo hayo, naomba nimalizie kwa kukushukuru wewe binafsi,
Naibu Spika, Mheshimiwa Juma Jamaldini Akukweti, Mbunge wa Tunduru, Wenyeviti
Mheshimiwa Eliachim Simpasa, Mbunge wa Mbozi Magharibi na Mheshimiwa Anne
Makinda, Mbunge wa Njombe Kusini kwa uongozi wenu mzuri ambao umeliwezesha
Bunge lako Tukufu kukamilisha kazi zote zilizopangwa katika Mkutano huu. Nawashukuru pia wafanyakazi wote wa Ofisi ya Bunge chini ya
uongozi wa Mheshimiwa Kipenka Msemembo Mussa, Katibu wa Bunge, kwa huduma zao
kwa Waheshimiwa Wabunge.
Mheshimiwa
Spika, baada ya mkutano uliopita ulizivunja Kamati za Kudumu za Bunge ili
kuunda kamati zenye muundo na portfolio mpya za kiwizara. Ninapenda kukupongeza wewe na wajumbe wako
wa Tume ya Bunge na wajumbe wa Kamati ya Uongozi kwa uamuzi huo mzuri. Hizi kamati sasa kwa vile zinahusiana na
wizara, zitakuwa na nafasi nzuri zaidi ya kuzamia na kuweza kuishauri Serikali
vizuri zaidi katika maeneo ya portfolio zao. Ninapenda kuwapongeza sasa wenyeviti wapya waliochaguliwa
kuongoza kamati hizo, nao ni:
1.
Mheshimiwa Pius Msekwa, Kamati ya Uongozi;
2.
Mheshimiwa Njelu M. Kasaka, Kamati ya Fedha na Uchumi;
3.
Mheshimiwa Athumani Janguo, Kamati ya Katiba, Sheria na
Utawala;
4.
Mheshimiwa Dakta Amani W. Kabourou, Kamati ya Hesabu za
Serikali;
5.
Mheshimiwa William Shellukindo, Kamati ya Uwekezaji na
Biashara;
6.
Mheshimiwa Dr. William Shija, Kamati ya Mambo ya Nchi za
Nje;
7.
Mheshimiwa Pius Msekwa, Kamati ya Kanuni za Bunge;
8.
Mheshimiwa Dakta John Malecela, Kamati ya Ulinzi na
Usalama;
9.
Mheshimiwa Eliakim Simpasa, Kamati ya Haki, Maadili na
Madaraka ya Bunge;
10.
Mheshimiwa Omar S. Kwaang’w, Kamati ya Huduma za Jamii;
11.
Mheshimiwa Sophia Simba, Kamati ya Maendeleo ya Jamii;
12.
Mheshimiwa Anne Makinda, Kamati ya Maliasili na Mazingira;
13.
Mheshimiwa Mgana Msindai, Kamati ya Hesabu za Serikali za
Mitaa;
14.
Mheshimiwa Prof. Henry Mgombelo, Kamati ya Miundombinu;
15.
Mheshimiwa Eliakim Simpasa, Kamati ya Kilimo na Ardhi.
Mheshimiwa
Spika, napenda niwashukuru sana Wenyeviti hao na Wajumbe wa Kamati zao
waliopitia miswada ya sheria ya Serikali kwa ushirikiano wao na hoja mbalimbali
walizozitoa katika kuboresha miswada hiyo. Serikali imepokea michango hiyo na
pale ilipowezekana imeifanya kuwa sehemu ya marekebisho ya miswada husika. Vikao vya Kamati vilianzia Dare-es-Salaam na
baadhi kumalizikia Dodoma.
Mheshimiwa
Spika, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imefanya kazi kubwa na nzuri
katika kuhakikisha kwamba maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge ambao
umekubaliwa umezingatiwa katika hatua za kupitisha miswada ndani ya Bunge lako
Tukufu. Naomba nimshukuru kwa dhati
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mheshimiwa Andrew Chenge (MB) na watalaam wa
Ofisi yake kwa kazi yao nzuri. Napenda
pia kuwashukuru wafanyakazi wa Serikali na Mashirika ya Umma ambao wameiwezesha
Serikali kujibu hoja mbalimbali na kutoa maelezo ya ziada ndani ya Bunge lako
Tukufu.
Mheshimiwa
Spika, napenda kwa niaba yenu na kwa niaba ya Serikali kuvishukuru vyombo vyote
vya habari kwa kazi yao nzuri ya kutoa habari na kuwaelimisha wananchi kuhusu
hoja zilizokuwa zinatolewa na Waheshimiwa Wabunge katika mkutano huu.
Mheshimiwa
Spika, naomba katika majimbo yetu tukasaidiane na wananchi katika shughuli zao
za maendeleo. Jambo kubwa ambalo hatuna
budi kulizingatia kikamilifu katika kipindi hiki ni kuwahamasisha wananchi
kuzitumia vema mvua za masika katika maeneo ambayo mvua hizo zinanyesha kwa
kupanda mazao yanayokomaa haraka ili taifa liweze kulikabili tatizo la uhaba wa
chakula ikiwa litajitokeza. Aidha,
katika kipindi hiki tulizindua matumizi ya takwimu za sensa hapa Bungeni. Tafadhali nawaomba Waheshimiwa Wabunge mkasaidie
kuhimiza matumizi ya takwimu hizo katika mipango yetu ya maendeleo katika
majimbo, kata na hata vijiji vyetu kwa sababu takwimu zipo hadi ngazi ya
vijiji.
Mheshimiwa
Spika, baada ya maelezo hayo naomba kutoa hoja kuwa Bunge lako Tukufu sasa
liahirishwe hadi tarehe 10 Juni 2003,
siku ya Jumanne, saa 3.00 asubuhi litakapokutana hapa mjini Dodoma.
Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa hoja.