KIKWETE AFADHAISHWA NA MIGOGORO ISIYOKWISHA AFRIKA
· ahimiza utashi wa kisiasa kuimaliza
· awashukuru viongozi wenzie kwa kumpongeza
· ahimiza kuutokomeza umaskini

KhartoumSudan         24 Januari, 2006

Na Maura Mwingira       

Rais Jakaya Mrisho amesema  inasikitisha kuona baadhi ya maeneo ya bara la Afrika yakiwa bado yakabiliwa na migogoro hata baada ya miaka mingi ya  uhuru wa nchi hizo.

Ameyasema hayo  wakati alipokuwa akitoa hotuba ya shukrani wakati wa ufungaji wa mkutano wa sita wa kawaida wa viongozi wakuu wa nchi na serikali uliomalizika leo hapa Khartoum Sudan.

Rais ambaye huu ulikuwa ni mkutano wake wa kwanza kuhudhuria akiwa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alieleza kwamba licha ya migogoro hiyo kuwapo katika nchi hizo, utatuzi wake  umekuwa ukichukua muda mrefu  kwa kile alichosema ni ushirikiano mdogo kutoka kwa wadau.

Rais ambaye alizungumza kwa lugha ya Kiswahili, alisema  kuwapo kwa migogoro hiyo pia kunaziathiri siyo tu nchi zinazohusika bali pia hata zile zinazopakana nazo.

Wimbi la wakimbizi, matatizo ya usalama, kudidimia kwa uchumi na kudodora kwa huduma za kijamii ni baadhi tu ya athari zinazozikabili nchi zinazopakana na zile zenye migogoro.

"Hata kwa zile nchi ambazo ziko mbali na nchi zenye migogoro, nazo zinaathiriwa na taswira mbaya inayotokana na migogoro hiyo.  Hivi ni lini viongozi wenzangu taarifa za migogoro ya Afrika zitaacha kupamba vichwa vya habari katika nchi zetu na dunia? akahoji Rais.

Na kuongeza kuwa ni vigumu kwa bara la Afrika kujinasua na kujiendeleza kiuchumi na kijamii kama juhudi za makusudi za kukomesha migogoro hazitafanyika. Na  kusisitiza kuwa anaamini kwamba viongozi hao kwa ushirikiano wao wanaweza kuimaliza migogoro hiyo kama wakitaka iwe hivyo.

Rais akawaeleza viongozi wenzie kwamba Tanzania hivi sasa inashikilia kiti kimoja kati ya viti vitatu visivyo vya kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambavyo Afrika imetengewa.

Akasema kuwa mwezi huu, Tanzania inakuwa mwenyekiti wa Baraza hilo na inaamua kutumia uenyekiti huo kuandaa na kuendesha majadiliano ya wazi kuhusu hali ya kanda ya maziwa makuu.

Akabainisha kuwa nchi nyingi za Afrika ambazo zinahusika  moja kwa moja na machakato wa amani na maendeleo katika kanda hiyo zimealikwa kushiriki kwenye majadiliano hayo. Ambayo alisema yatawahusisha Mawaziri wa Mambo ya Nchi za Nje.

"Napenda kuhimiza nchi zilizoalikwa kuhudhuria majadiliano haya ya wazi yatakayofanyika New York  Januari 27 mwaka huu. Afrika inapaswa kutumia fursa hii kuhamasisha jumuia ya kimataifa kuunga mkono mchakato wa amani na maendeleo katika kanda ya maziwa makuu na kuongeza juhudi za kuandaa mkutano wa pili wa kimataifa wa kanda ya Maziwa Makuu.


Aidha Rais Kikwete alisema kuwa jambo jingine ambalo alipenda kulizungumza katika mkutano huo ni namna ya kushughulikia tatizo la umaskini katika  Bara la Afrika.

Amesema kuwa tafiti mbalimbali zimefanywa juu ya kiini cha umaskini  barani Afrika, na mambo mengi  yamependekezwa juu ya namna ya kupata ufumbuzi wa tatizo hilo.

Akasema Rais, "Kimsingi, Afrika inaendelea kugubikwa na  umaskini, lakini suala la kujiuliza ni kwa nini Afrika, ambayo inautajiri mwingi wa raslimali kama vile watu, ardhi yenye rutuba, mafuta, madini ya thamani, mbao na mazao mengine ya biashara inabaki maskini?.

Akabainisha kuwa ili kuondokana na umaskini huo, Afrika inatakiwa kutekeleza mkakati wa pamoja uliopendekezwa na Jeffrey Sachs, mshauri wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Mkakati unaozihusisha nchi tajiri na maskini.

Akasema mkakati huo unalenga kusaidia nchi maskini angalau kutekeleza kwa wakati Malengo ya Maendeleo ya Milenia, yanayohusu programu za kutokomeza umaskini.

Akasisitiza kuwa mkakati huo unajumuia pia ufutaji wa madeni, kuandaa sera za biashara za kimataifa zinazofaa nchi maskini sana, kuzipatia nchi hizo  uwezo wa sayansi na teknolojia na  maendeleo endelevu.

"Umoja wa Afrika na nchi zetu kwa ujumla ni vema zikatambua wajibu wake  katika jambo hili na kuutumiza ipasavyo, pamoja na kuyahimiza mataifa makubwa  kutumiza wajibu wao",akasisitiza Rais.

Akizungumzia kuhusu Mkutano wa sita wa AU, Rais alisema kuwa amefarijika sana na namna mkutano huo ulivyoendeshwa, lakini amefarijika zaidi na mapokezi mazuri na pongezi alizopewa na viongozi wenzake kwa kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akasema, salamu hizo za pongezi zimedhihirisha urafiki na upendo wao kwake na kuthibitisha mahusiano mazuri yaliyojengeka kati ya Tanzania na nchi zao.

"Napenda kuwathibitishia nia yangu na ya serikali yangu ya kuendeleza mahusiano hayo mazuri, pamoja na kuendeleza mchango wetu katika kuimarisha  Umoja wa Afrika.

Akawashukuru kwa kumchagua yeye kutoka hotuba ya shukrani  kwa niaba ya viongozi wenzie.

Rais pia alimpongeza Rais wa Liberia Mama Ellen Johnson Sirleaf kwa kuchaguliwa kwake kuliongoza taifa hilo.

Akasema Rais "kwa niaba yangu na wananchi wa Tanzania  tumefurahishwa na ushidi wako wa kihistoria kwa nchi yako na bara letu la Afrika. Na kuhakikishia ushirikiano wangu na ule wa serikali na nchi yangu".

Aidha Rais alimpongeza Rais wa Sudan Omar El Bashir na viongozi wa SPLA chini ya marehemu John Garang na sasa Mhe. Salva Kiir, Makamu wa Ris wa Sudan kwa ujasiri wao na moyo wao wa  uzalendo kwa nchi yao na huruma wa raia wao waliokuwa wakiteseka kwa madhara ya vita.

Sudan inasherehekea mwaka mmoja tangu kusainiwa kwa mkataba wa amani baina ya Serikali ya Sudan na Wapiganaji wa SPLM.

Rais na Ujumbe wake anarejea nyumbani kesho (Jumatano)

Mwisho.
 

Maura Mwingira