PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

Fax. No. 255-22 2113425                                               The State House,                     

Tel: 255-22-2116539/2116913                                        P.O. Box 9120,

                                                                                        DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI SASA KUWA NA MAHAKAMA YA RUFAA

 

 

Na Maura Mwingira

Nairobi, Kenya

15/12/2006

 

 

Jumuia ya Afrika ya Mashariki sasa itakuwa na Mahakama ya Rufaa, kufuatia viongozi wa Jumuia hiyo hapo jana (Alhamisi) kutia saini na kuridhia marekebisho katika  Katiba ya Jumuia hiyo.

 

Marais Jakaya Kikwete, Mwai Kibaki na Yoweri Museveni walisaini marekebisho ya katiba hiyo  wakati wa kikao kidogo (mini summit) cha  viongozi hao kilichofanyika  katika ukumbi wa mikutano wa jengo la Umoja wa Mataifa, hapa Nairobi Kenya.

 

Viongozi hao walikuwa jijini Nairobi kuhudhuria  mkutano wa pili wa kimataifa kuhusu Maziwa Makuu.

 

Pamoja na kuridhia  kuundwa kwa Mahakama ya Rufaa, viongozi hao pia wametia saini marekebisho ya katiba hiyo ya EAC ambapo sasa kutakuwa na kipengele kitakachowapa mamlaka viongozi wa jumuia hiyo kuwachakulia hatua za kidhamu majaji wa mahakama za Jumuia hiyo.

 

Marekebisho  ya katiba ya Jumuia ya  Afrika Mashariki, kunafuatia maagizo yaliyotolewa na viongozi hao kupitia tamko lao la pamoja lililotolewa mara baada ya mkutano wa nane wa kilele wa EAC uliofanyika  Arusha, Tanzania  Novemba 30 mwaka huu.

 

Novemba 27, siku mbili kabla ya kufanyika kwa mkutano wa kilele majaji wa mahakama ya EAC walitoa hukumu  kupinga uteuzi wa wabunge kutoka nchi Kenya kwa kuwatamka si wabunge waliochaguliwa kihalali.

 

Uamuzi huo ulileta sitofahamu na kusababisha wabunge  wa Bunge la Afrika Mashariki kutoapishwa  hadi  sasa.

 

Utiaji saini wa mabadiliko ya katiba ya EAC  ulishuhudiwa pia na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Kenya, Uganda na Katibu Mkuu wa Jumuia ya Afrika Mashariki Juma Mwapachu na baadhi ya maafisa wachache kutoka EAC.

 

Mwisho