PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

 

Fax. No. 255-22 2113425                                                  The State House,                               

Tel: 255-22-2116539/2116913                                           P.O. Box 9120,

                                                                                           DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Rais Jakaya Kikwete amelitaka shirika la ndege la  Qatar  ambalo limeanza shughuli zake hapa nchini, kuitumia nafasi hiyo kuitangaza  Tanzania kama kituo kikuu  cha utalii na mapumziko.

 

Pamoja na kulitaka shirika hilo kuitumia nafasi hiyo kuitangaza Tanzania, Rais pia ameitaka serikali ya Doha ambako ndiko makao makuu ya shirika hilo la ndege kuangalia uwezekano wa kuwekeza katika ujenzi wa hoteli za kitalii katika  ngazi nyota tano (five star hotel).

 

Ameyasema hayo leo wakati alipokutana na Mwenyekiti  na Mtendaji Mkuu  wa  Shirika hilo na ndege, Bw. Akbar Al Baker, Ikulu jijini Dar es Salaam.

 

Rais amesema amefurahishwa na  uamuzi wa shirika hilo kuichagua Tanzania kuwa moja ya  kituo  chake cha  utoaji wa huduma hiyo ya usafiri wa anga.

 

Alisema  kwa   Qatar airways kuanzisha safari za moja kwa moja kuja nchini Tanzania, kutaongeza idadi ya watalii  wanaokuja nchini kutokana na kuwapo kwa usafiri wa uhakika na wa moja kwa moja.

 

Hata hivyo Rais alisema kuwa  uhaba wa  hoteli za kitalii unakwamisha shughuli zima za utalii, kwa kile alichosema hivi sasa kuna vitanda vipatavyo 957 tu katika hoteli zote za kitalii ambavyo haviendani na wingi wa watalii wanaokuja kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii hapa nchini.

 

Alisema idadi ya watalii inatarajiwa kuongezeka  maradufu na hasa baada ya Serengeti kutangazwa kama moja ya maajabu saba ya dunia.

 

Aidha Rais Kikwete alimtaka Mwenyekiti na mtendaji wa  Qatar Airways, kuangalia pia uwezekano wa kuanzisha safari za moja kwa moja  kupitia Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro na vilevile kuangalia uwezekano wa kusafirisha maua yanazozalishwa katika mikoa ya Arusha na kuuzwa Ulaya.

 

Alisema kuwa hivi sasa wafanyabiashara wa maua wanasafirisha bidhaa hiyo kupitia Kenya, hali inayofanya bidhaa hiyo ionekane kwamba inazalishwa  nchini Kenya.

 

Kwa upande wake, Mwenyekiti huyo wa Qatar Airways, alisema  moja ya kazi kubwa ambayo shirika lake litafanya ni hiyo ya kuitangaza Tanzania kupitia taarifa mbalimbali ikiwa ni pamoja na  kuandaa majarida (inflight magazine) yatakayowekwa katika ndege za shirika hilo.

 

Bw. Akbar Al Baker alisema  kwa kuanzia wamekuja na kundi la waandishi wa habari ambao leo wamekwenda Serengeti kujionea na kuchukua habari mbalimbali zinazohusu vivutio vya utalii na kwenda kuvitangaza.

 

Alieleza kuwa shirika lake lilikuwa limekusudia kuanzisha safari zake za moja kwa moja kutoka Doha kuja Tanzania, miaka mitatu iliyopita lakini lilikwama kutokana na kuchelewa kupata ndege kubwa na za kisasa.

 

 

Aliongeza kuwa shirika hilo lina mpango wa kuleta nchini ndege kubwa na za kisasa zaidi zenye hadhi ya VIP na zenye uwezo wa kukaa angani kwa saa nyingi.

 

Alisema kuwa akirejea kwao Doha, atazungumza na Kiongozi wa nchi hiyo,  ili kuangalia uwezekano wa kuja nchini na kuwekeza katika ujenzi wa hoteli za  kisasa za kitalii ili kukidhi mahitaji ya watalii yanayoongezeka kila mwaka.

 

 

Kuhusu  kupeleka ndege  katika uwanja wa KIA, Bw. Baker alisema shirika hilo litafanya utafiti  wa kuanzisha safari hizo na vilevile kuangalia uwezekano wa kusafirisha maua kwenda nchi za ulaya.

 

Akielezea utendaji kazi wa shirika lake, Bw. Baker alisema Shirika hilo linasafirisha abiria  milioni nane  na nusu  kwa mwaka na linatarajiwa kufikisha milioni 10 mwakani. Qatar Airways inatoa huduma ya usafiri wa anga katika nchi za kimataifa 70.

 

Qatar Airways ilianzishwa mwaka  1993 na ni  moja ya mashirika ambayo yanainukia kwa kasi kibiashara. Aidha Shirika hilo ni moja kati ya mashirika manne ya ndege ambalo ndege zake zina hadhi ya nyota tano (fivestars airline).

 

Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete leo ameagana na Balozi wa Zimbabwe Mhe.Chipo Zindoga ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

 

Katika mazungumzo hayo. Rais alimshukuru na kumpogeza Balozi huyo kwa kazi kubwa na nzuri ya uwakilishi aliyoifanya akiwa hapa nchini.

 

Alisema kuwa katika kupindi hicho cha uwakilishi wake, uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Zimbabwe umeendelea kukua na kuimarika.

 

Naye Balozi Chipo Zindoga alitoa shukrani zake kwa Rais Jakaya Kikwete , serikali na Watanzania kwa ushirikiano mkubwa waliompatia pamoja na upendo waliomuonyesha.

 

Alisema kuwa ushirikiano huo, ulimpatia fursa ya kuelezea kwa kina, kwa uwazi na kwa ufasaha yale yaliyokuwa yakijitokeza nchini mwake, lakini pia ulitoa fursa nzuri ya kuendelea ushirikiano mzuri uliopo kati ya mataifa hayo mawili.

 

Mwisho

 

Ikulu

Dar es Salaam

 

10/01/2007