PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

 

                                                 

 

 

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                        P.O. Box 9120,

Fax. No. 255-22 2113425                                                           DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

     

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 Rais Jakaya Kikwete leo amekuwa na mazungumzo na Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw.  Murilo Portugal.

 

Katika mazungumzo yao, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa IMF alielezea kufurahishwa na hatua ambazo Rais Jakaya Kikwete ameanza kuchukua katika kuhakikisha kwamba kuna kuwa na uwajibikaji katika udhibiti wa mapato na matumizi katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.

 

Nimesoma katika magazeti ya leo juu ya kauli yako kuhusu matumizi mabaya ya fedha za serikali na hatua unazokusudia kuchukua, huu ni mwanzo mzuri, na ninaamini kwamba  kutakuwa na matokeo boraamesema Bw. Portugal.

 

Ameongeza kuwa hatua hiyo pia imepokelewa vema na wabunge wa Kamati ya Fedha wakiongozwa na Mbunge wa  UDP. John Cheyo  ambao alikutana nao leo, na wamemwelezea kwamba sasa wana imani  kwamba na wana Rais ambaye anaunga mkono uwajibikaji.

 

Naibu Mkurugenzi Mkuuhuyo wa  IMF amesema  tatizo la matumizi mabaya ya fedha za serikali haliko Tanzania peke yake bali  ni tatizo linalozikumba karibu nchi zote duniani.

 

Amebainisha kwamba wakati Serikali Kuu zinajitahidi kurekebisha makosa yao, hali bado ni mbaya katika Serikali za Mitaa.

 

Amemweleza  Rais kwamba  fedha za serikali katika nchi yoyote ni lazima zitumike vizuri ile kuleta matokeo yaliyotarajiwa na kwamba udhibiti wa fedha hizo na uhakiki wa matumizi yake ni  jambo la msingi sana.

 

Katika mazungumzo hayo, Naibu Mkurugenzi Mkuu alitaka, pamoja na mambo mengine kupata maelezo kutoka kwa Rais kuhusu  mipango mbalimbali  ya maendeleo na kiuchumi inayofanywa na serikali.

 

Aidha amesema kuwa IMF inaridhika na hali ya mambo ilivyo nchini pamoja na juhudi mbalimbali zinazofanywa na serikali, na kuahidi kwamba itendeleza ushirikiano wake na Tanzania pamoja na kutoa misaada ya kiufundi, na kimawazo wakati wowote Tanzania itakapohitaji  msaada wa aina  hiyo.

 

Kwa upande wake, Rais Jakaya Kikwete , amesema  bado Tanzania itendelea kuhitaji kusaidiwa na IMF katika mambo mbalimbali yanayohusu uchumi, maendeleo ya jamii na uendelezaji wa miundombinu na nishati. Na kwamba inaridhika na uhusiano na ushirikiano uliopo hivi sasa kati ya serikali na IMF.

 

Rais amesema kuwa tatizo la udhibiti mbaya ya mapato ya matumizi ya fedha za serikali ni tatizo ambalo kwa muda mrefu limekuwa likimkosesha amani, na ambalo alikuwa akilitafutia mahali pa kuanzia.

 

Ripoti hii ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali imenipa mahali pa kuanzia, kwani ni tatizo ambalo limekuwa likininyima raha, na maneno niliyoyasema jana kwenye mkutano wangu na watendaji wa serikali za mitaa, si maneno ya vitisho tu bali ninamaanisha yale niliyoyasema. Sitasita kuzivunja halmashauri zitakazoendelea kufanya vibaya na kuitisha uchaguzi mwingine,.

 

Rais amesisitiza kuwa serikali yake  itaendelea kuweka mkazo katika  uendelezaji wa kilimo ili kiwe cha kisasa na hivyo kuongeza tija kwa mkulima na kuboresha maisha yake.

 

Aidha amesema mchakato za kupanua na kuboresha  huduma za elimu, afya, nishati na miundombinu,  ni mchakato endelevu, na kwamba  ukusanyaji wa mapato na uwezeshaji wa chombo kinachohusika na ukusanyaji wa mapato hayo ni jambo linalopewa kipaumbele na serikali.

 

Mazungumzo kati ya Rais na Naibu Mkurugenzi wa IFM, Bw. Murilo Portugal yalihuduhiriwa pia na  Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, Gavana wa Benki Kuu, Daudi Balali na Katibu Mkuu Fedha, Bw. Gray Mgonja.

 

Mwisho.

 

Ikulu

DAR ES SALAAM

 

30/04/2007