PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

 

 

                                                                           

 

 

 

                                                      

                                  The State House,

                                                                                       Tel: 255-22-2116539/2116913                                                     P.O. Box 9120,

                                                                                       Fax. No. 255-22 2113425                                                             DAR ES SALAAM.

                                                                                        E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Rais Jakaya Kikwete leo amekuwa na mazungumzo na ujumbe wa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) ulioongozwa  na Bw. Zhang De Jiang, mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Kamati Kuu ya CPC akiwa  pia ni  Katibu wa Kamati ya Chama ya Jimbo la Guandong.

 

Katika mazungumzo hayo, Rais na mgeni wake walijadiliana na kubadilishana mawazo kuhusu namna Tanzania na China zinavyoweza kuongeza kasi ya ushirikiano hususani katika sekta za biashara na uchumi.

 

Bw. Zhang De Jiang alimweleza Rais kwamba  ziara yake hapa nchini ina malengo ya  kukuza na kuendeleza uhusiano wa kibiashara na kiuchumi  kati ya Tanzania na jimbo hilo la  Guangon, jimbo ambalo ni moja kati ya majimbo yanayofanya vizuri kiuchumi  na kuchangia katika pato la taifa la China. GDP ya jimbo hilo ni dola za Kimarekani 330 milioni kwa mwaka na inachangia moja ya nane ya pato la China.

 

Bw. Zhang De Jiang amesema,   pamoja na kwamba katika ziara yake hii imefuatana na wajasiriamali 200,  ambao kesho watakutana na wajasiriamali wa Tanzania na kubadilishana nao uzoefu, atatumia ujumbe mwingine wa wafanyabiashara utakaoongozwa na  Mkurugenzi Mkuu wa Jimbo hilo.

 

Amefafanua kwamba kazi ya ujumbe huo itakuwa ni kuchambua sera na vivutio vya uwekezaji vilivyopo hapa nchini ambavyo kwayo vitatumika katika kutoa maamuzi ya maeneo ya kuja kuwekeza hapa nchini.

 

Kiongozi huyo wa ujumbe wa CPC, amesema Tanzania  chini ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete inayo mazingira na fursa nzuri ya kuendelea kiuchumi, kibiashara na kijamii.

 

Amesema  hali ya amani na utulivu iliyopo nchini, ni moja ya vivutio vikubwa vya uwekezaji hasa uwekezaji wa kutoka nje.

 

Aidha amebainisha kwamba  uadilifu wa Watanzania, uhodari wao wa kazi, uwingi wa raslimali ni  moja ya mambo ambayo yanawavutia wawekezaji kuja Tanzania.

Bw. Zhang  De Jiang pia amemweleza Rais kwamba, ikiwa Tanzania itafungua zaidi milango ya uwekezaji kutoka nje,  kama lilivyofanya jimbo hilo ambalo yeye ndiye kiongozi wake, si tu kutachangia katika ukuaji wa uchumi, lakini pia kutaiwezesha reli ya Tazara  kufufuka na kufanya kazi kwa ufanisi na tija.

 

Amesema China imeweza kufanya vizuri katika mageuzi yake ya kiuchumi baada ya kufanya marekebisho makubwa  na kufungua milango ya uwekezaji kutoka nje, huko jimbo hilo la Guandong likiwa la kwanza katika utekelezaji wa mageuzi hayo na kuvutia wawekezaji kutoka nje.

 

Amefafanua kwamba China imefika hapo ilipo na kuwa moja ya mataifa yanayo kuja juu kwa kasi kwa ukuaji wa uchumi  baada ya kupitia vikwazo vingi na machungu mengi lakini ambayo baadaye yamekuja kuipatia neema nchi hiyo.

 

Dhumuni jingine la ujio wa Ujumbe huo wa CPC ni kukidhibitishia uhusiano na ushirikiano endelevu kati yake na Chama cha Mapinduzi.

 

Kwa upande wake Rais Kikwete ameeleza kufurahishwa  kwake na uamuzi wa jimbo hilo la Guandong la kuleta nchini wafanyabiashara na kutaka kupanua  kuwa na uhushirikiano endelevu wa kibiashara na uchumi  kati  yake na Tanzania.

 

Amesema Tanzania inayo mengi ya kujifunza kutoka China, na kuongeza kuwa kupitia mipango mathubuti, sera nzuri na utekelezaji  makini wa maamuzi mbalimbali, Tanzania pia inaweza kuondoka katika umaskini wake na kuwa nchi iliyoendelea kama ilivyofanya china.

 

Amesema serikali inaukaribisha ujumbe huo wa wafanyabishara na kuhakikisha kwamba utapewa   ushirikiano wa kila hali ili hatimaye, waweze kuwekeza na kufanya biashara na Watanzania.

 

Rais aliainisha  mambo kadhaa  yakiwamo  mazingira mazuri ambayo serikali imeyaandaa kwa ajili ya kuvutia wawekezaji wa ndani na nje.

 

Mazungumo kati ya Rais na ujumbe huo wa CPC pia ulihudhuriwa na viongozi wa Chama cha Mapinduzi  wakiongozwa na  Naibu Katibu Mkuu wa Chama, Bw. Jaka Mwambi

 

Mwisho.

 

Ikulu

Dar es Salaam.

 

11 Juni 2007