PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

 

 

 

 

                                            The State House,

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                        P.O. Box 9120,

      Fax. No. 255-22 2113425                                                                DAR ES SALAAM.

                                                                                           E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Na Mwandishi Maalum

13/06/07

Ikulu

 

Rais Jakaya Kikwete amesema  anayo nia na dhamira ya dhati ya  kuwaondoa Watanzania katika maisha ya dhiki na umaskini.

 

Ameeleza kuwa   hali ya umaskini  inayowakabili zaidi ya asilimia  39 ya Watanzania hasa wale wa vijijini, ni jambo linalomsumbua sana. na ndio maana  anabuni  mikakati na mipango mbalimbali  ya kuwaibua wajasiriamali wadogo na wakati ili hatimaye waongeze kipato chao na kuboresha maisha yao.

 

Kikwete ameyasema hayo jana jioni ( Jumanne) wakati alipokuwa akibadilishana mawazo na mtaalam maarufu wa uchumi, mwanzilishi wa Benki ya watu maskini  Gramees Bank, na Mshindi wa Tuzo ya Amani ya mwaka 2006 (Nobel Peace Prize Laurette) Professa  Yunus Mohamed, kutoka Bangladesh.

 

Amesema kuanzishwa kwa  mchakato wa utoaji wa mikopo nafuu ambayo kwa sasa imepachikwa jina la mabilioni ya JK, ni  sehemu tu ya mikakati yake ya kutafuta njia muafaka za kuwawezesha wananchi wa kipato cha chini na maskini.

 

Akifafanua zaidi, Rais amesema  kunahitajika ubunifu zaidi, utaalamu na utashi wa kisiasa kutoka kwa viongozi na wananchi wenyewe katika mchakato mzima wa kuondokana na umaskini.

 

“Wakati wote wa kampeni za uchaguzi, nilijitahidi sana kuelezea nia na dhamira yangu  hiyo ya kuinua hali ya maisha ya wananchi kwa kuwapatia fursa ya kupata  mikopo nafuu ili hatimaye waweze kuendesha shughuli za ujasiriamali zitakazowaongezea kipato. Ni dhamira niliyonayo na ni jambo linalonigusa sana”. Amesema.

 

Rais amemweleza ProfessaYunus Mohamed  kwamba, nia yake ya kumwalika kuja hapa nchini ililenga hasa kutaka wabadilishane mawazo, uzoefu na mbinu ambazo zitamuwezesha yeye binafsi kama Rais, lakini na wadau wengine wakiwamo watendaji serikalini, wamiliki wa Mabenki, vyama vya kuweka na kukopa kwa pamoja nini wanaweza kufanya kuharakisha mchakato wa kuwaondoa wananchi katika umaskini.

 

“Ninakushukuru sana professa kwa kuukubali mwaliko wangu, niliona ni bora tukutane  na tuweze kubadilishana mawazo, lakini kubwa zaidi kuchota maarifa yako uliyotumia kuwaondolewa umaskini maelfu ya wananchi wa Bangladesh na kuboresha maisha yao kwa njia  ya mikopo nafuu” amesema Rais.

 

Amebainisha kwamba siku zote amekuwa akiamini kwamba Mabenki ya biashara si rafiki wa watu maskini, hivyo inatakiwa kuundwa mifumo rasmi nje ya mifumo ya benki za biashara ambazo licha ya kutoza riba kubwa lakini zimejaa urasmu mkubwa inapofikia suala la kuwakopesha watu wa kipato cha chini.

 

Hata hivyo Rais amesema kidogo kidogo baadhi ya benki zimeanza kuwaamini na kuwakopesha watu wa kipato cha chini kwa kuwa   wameonyesha uadilifu mkubwa wa kurudisha mikopo hiyo.

 

Akitoa mchango wake wa mawazo ya  nini Tanzania inaweza kufanya kuwaondolea umaskini watu wake, Professa   Yunus  Mohamed amesema Tanzania inao uwezo  na kila sababu ya kuiondoa hali ya umaskini inayowakabili wananchi wake.

 

Amesema tofauti na ilivyo nchi kwake Bangladeshi ambao kuna mamilioni  ya watu maskini, kwa Tanzania  ambayo ina  asilimia 39 sawa na familia milioni 2.5 tu  ina kazi nyepesi zaidi  ya kuwaondolea umaskini watu hao kwa kuwa nchi inazo raslimali nyingi, serikali mathubuti na kinachotakiwa ni ubunifu tu .

 

Tanzania mnazo raslimali nyingi sana, hamna idadi kubwa ya watu maskini, kinachotakiwa ni kujipanga vizuri, kuwa wabunifu na kuamua kwa dhati kukitekeleza kile mlichoamua, na hapo mtaweza kabisa kuziondoa familia hizo 2.5. milioni katika lindi la umaskini”

 

Ameongeza “kila mtu ni mjasiriamali, hata ombaomba yule wa mtaani anaweza kuwa mjasiriamali, tofauti iliyopo ni kwamba wengine walipata fursa ya kujipambanua na kuwa wajasiriamali, na kundi jingine halijawezeshwa kufanya hivyo” anasema Professa Yunus

 

Professa Yunus  ambaye alikuwa hapa nchini kwa mwaliko maalum wa Rais Jakaya Kikwete, amemweleza Rais  kwamba hakuna njia ya haraka na  ya uhakika ya  kuwaondoa wananchi katika umaskini kama ile ya kuwapatia  fursa na uwezo wa kupata mikopo ama isiyo na riba kabisa au yenye riba ndogo sana.

 

“Wamiliki wengi wa Mabenki na hata wasomi, hawaliamini hili, lakini sisi tumedhihirisha kwamba inawezekana na tumelifanya kupitia benki yetu ya watu maskini, Gramees Bank” anasisitiza.

 

Amefafanua kwamba mkopo anaopewa mtu  maskini unatakiwa kuwa wa bure au riba yake isizidi asilimia 10 kwani ikizidi hapo huo si mkopo wa kumwezesha mtu maskini kujiwezesha na kujinasua na umaskini…… “ ukizidisha riba juu ya asilimia kumi wewe si mkopeshaji bali unafanya biashara ya fedha” anasema.

 

Aidha Professa huyo amepinga ile dhana ya kwamba watu maskini hawalipi mikopo wanayopewa kwani amesema katika Benki ya Grameen ambayo yeye ni mwanzilishi wake, watu maskini na wengi wao wakiwa ni wanawake wameonyesha uadilifu wa hali ya juu katika urejeshaji wa mikopo kwa asilimia 98.

 

Ameelez kuwa Grameen Bank ni benki ambayo inajiendesha kwa amana ya watu hao maskini, na wala haitegemei au kupata fedha yoyote kutoka nje au kwa wafadhili.

 

“Grameen Bank, ni benki ya wananchi wenyewe, wanaimiliki wenyewe kwa amana zao, wala hatuna fedha yoyote kutoka kwa mfadhili, na hili hata nyinyi mnaliweza mkiamua, mkitegemea fedha ya mfadhili hamtafika kokote.

 

Katika mchango wake huo, Profesa Yunus, amemweleza Rais, kwamba katika utekelezaji wa mchakato wa kuwaondoa watu katika umaskini, lengo lisiwe ni watu wangapi wamefikiwa bali ni wangapi hawajafikiwa.

 

“Kila wakati malengo yenu yawe ni watu wangapi hatujawafikia, siyo wangapi tumeshafanikiwa kuwafikia, mkifanya hivyo mtabweteka, daima zingatieni hili, mwezi  huu tunataka kuwafikia wangapi, miezi sita ijayo wangapi, mwakani wangapi hapo  ndipo mtakapoweza kufanikiwa.

 

Aidha Professa huyo ambaye anaheshimiwa sana duniani na hata kwa mataifa yaliyoendelea, amemshukuru sana Rais Jakaya Kikwete kwa kumwalika na kwa kuamini kwamba naye anaweza kutoa mchango wake katika kufanikisha nia ya Rais ya kuwawezesha wananchi kufanya shughuli za ujasiriamali.

 

Amesema yuko tayari na wakati wowote kushirikiana kwa hali na mali katika utekelezaji wa nia hiyo.

 

Akiwa hapa nchini, pamoja na kuwa na mazungumzo na Rais, Profesa Yunus alikutana pia na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha, Gavana wa Benki Kuu, wamiliki wa Mabenki, asasi zisizo za kiserikali zinazojihusisha na utoaji wa mikopo midogo midogo,  watafiti  na wataalamu wa uchumi.

 

Mwisho.