PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

 

 

                                                      

                                           The State House,

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                    P.O. Box 9120,

Fax. No. 255-22 2113425                                                           DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz                                                           Tanzania.

              ikulupress@yahoo.com

 

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Na Maura Mwingira

5/9/2007

MPWAPWA

 

Rais Jakaya Kikwete amezitaka Wizara  za Maendeleo ya  Mifugo  na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba wanafunzi 86 wanaomaliza mafunzo yao katika Chuo cha Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Mifugo wanapata ajira serikalini.

 

Ametoa agizo hilo leo wakati  alipoitembelea Taasisi hiyo ya Taifa ya Utafiti wa Mifugo iliyopo Wilayani Mpwapwa, Mkoani Dodoma kukagua shughuli za Taasisi hiyo ambayo pia inatoa mafunzo ya ngazi ya diploma na cheti  katika maeneo ya tiba za mifugo na  uzalishaji wa mifugo.

 

Mkuu wa  Chuo hicho ambacho kilianzishwa mwaka 1935 , Dkt. Jerome  Bahami, alimweleza Rais kwamba, kwa mwaka huu chuo  hicho kina wanafunzi 86 wa mwaka wa pili na wa mwisho, na  robo tatu yao wakiwa wanajilipia wenyewe, na kwamba   wengi wao hawana uhakika wa ajira baada ya kumaliza masomo yao.

 

“Kwa nini hawa wakose ajira wakati tuna uhaba mkubwa wa wataalam” akahoji Rais na kuendelea “Huku tunasema tunataka kufanya mageuzi katika kilimo na ufugaji, hivi kinachokwamisha hawa wasijariwe ni nini, hata kama wamelipiwa na wazazi wao, lakini mzazi anapomlipia mwanae matumaini yake  si apate ajira baada ya kumaliza masomo yao. Fanyeni utaratibu wa kuwaajiri hawa” akasema Rais huku akimwelekea Naibu Waziri wa Mifugo, Dkt Charles Mlingwa.

 

Pamoja na kuangiza  wizara husika kuwaajiri  wahitimu hao, Rais pia ameshauri kufanyiwa marekebisho au kufutwa kabisa kwa Sheria Namba Nane.

 

Amesema  Sheria hiyo ni kikwazo  katika utoaji wa ajira hasa kwa wataalamu wa kada maalum ambao mahitaji yao ni makubwa lakini ni wachache.

 

“Nchi ina shida kubwa ya wataalamu, leo hii  kwa mfano Wizara au Halmashauri inatangaza nafasi za wataalamu wa mifugo, na wataalamu hao wako 10,  halafu mnasema ni lazima wahojiwe na madiwani, madiwani wenye elimu yao ni ya chini kuliko wataalamu hao, hivi jamani tunakwenda wapi, sheria hii ifanyiwe marekebisho ni ucheleweshaji wa muda tu na kuwapa watu posho,” akasema Rais.

 

Ameongeza kwamba  zinapojitokeza nafasi za ajira kwa kada maalum, badala ya kuzitangaza nafasi hizo magazeti, wahusika waende moja kwa moja vyuoni na kuwatambua watu wanaowataka, na wakimaliza masomo yao na kuthibishwa na vyuo vyao kwamba wamefaulu vizuri basi waajiriwe.

 

 “Haiwezekani, wataalamu mbalimbali wakakosa ajira serikalini, kwa vile tu  eti sheria namba nane inataka kila nafasi ya ajira itangazwe kwa sababu tu wakubwa fulani wamesema huu ndio utaratibu wa uwazi, hapana lazima tufikie mahali maamuzi mengi tuyabadilishe tu” akasisitiza  Rais

 

 

Chuo hicho cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo mwaka huu kinatarajiwa kuchukua wanafuzi 210 ambao watalipiwa na serikali kwa asilimia 100 na baada ya kumaliza masomo yao wataajiliwa na serikali.

 

Akiwa  kwenye taasisi hiyo, Rais Kikwete alitembelea mashamba ya mifugo na kujionea ng’ombe aina ya Mpwapwa wanaozalishwa  katika taasisi hiyo, pamoja na mbuzi aina ya Malya ambao nao huzalishwa hapo.

 

Rais aliwataka wataalamu hao, kuongeza kasi ya uzalishaji wa madume ya kisasa kwa kutumia teknolojia ya chupa, kwa lengo la kupata madume mengi ya kisasa ili kubadili aina ya ng’ombe waliopo ambao hawazalishi nyama ya kutosha, maziwa na hata ngozi bora.

 

Akasema  serikali itakafanya kila lilo ndani ya uwezo wake, kuisaidia Taasisi hiyo na chuo chake ambavyo   amesema ni muhimu sana katika utekelezaji wa mageuzi ya sekta ya mifugo nchini.

 

Awali  Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Dkt Regnald Mbwile, amemweleza Rais kwamba Taasisi hiyo  ilianzishwa mwaka 1905 na Wajerumani. Wakati huo ikiwa kama kliniki ya kutibu magonjwa ya mifugo.

 

Amefafanua kwamba, Tasisi hiyo ambayo ina josho la  kuoshea mifugo likiwa ni la kwanza Afrika Mashariki, lilijengwa  mwaka 1905 na hadi leo hii linafanya kazi, pia kuna   vituo vya utafiti wa mifugo vitatu ambavyo ni vya mabuki kiliochopo kanda ya Ziwa, kituo cha Utafiti wa Mifugo Uyole kilichopo kanda ya Nyanda za Juu Kusini na kituo cha utafiti wa malisho Kongwa.

 

Aidha  ameyaeleza malengo ya Taasisi ni kuchangia katika kujitosheleza kwa chakula na maendeleo ya kiuchumi kwa kufanya tafiti sahihi na endelevu ambazo zinalenga kuongeza tija katika mifugo kwenye kanda mbalimbali za kilimo nchini.

 

Akieleza zaidi shughuli za Taasisi hiyo, Dkt. Mbwile amesemaTaasisi inaendeleza uzalishaji wa ng’ombe wa aina ya Mpwapwa ambao ni chotara kwa ajili ya nyama na maziwa, ambapo ng’ombe mmoja huweza kutoa hadi lita tisa za maziwa kwa siku na kilo 230 za nyama.

 

Mhe. Rais shughuli zenu nyingine ni uendelezaji na uzalishaji wa mbuzi wa aina ya Malya au Blended Goat kwa ajili ya nyama na maziwa, kuchagua na kukoosafu mifugo ya asili, kushirikiana na wadau wengine wanaojishughulisha na uendelezaji wa mifugo na uzalishaji na usambazaji wa mifugo yenye tija vijijiniakasema Dkt Mbwile.

 

Taasisi ya Taifa ya Utafiti  wa Mifugo pia hujishughulisha na  kufanya tathimini na kuboresha vyakula vya mifugo, kutathimini na uboreshaji wa malisho na nyanda za malisho, utoaji wa habari kuhusu teknolojia zilizopo na kufanya tafiti zinazohusu masuala mtambuka kama vile mtizamo wa jinsia, athari za ukimwi, matumizi ya ujuzi asilia na hifadhi ya mazingira.

 

 Mwisho.