PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

 

 

                                                      

                                           The State House,

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                    P.O. Box 9120,

Fax. No. 255-22 2113425                                                           DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz                                                           Tanzania.

              ikulupress@yahoo.com

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

LIMENI MAZAO YA BIASHARA MUONDOKANE NA UMASKINI - KIKWETE

 

Na Maura Mwingira

3/9/2007

KONGWA

 

 

Rais Jakaya Kikwete amewataka wananchi wa wilaya ya Kongwa, kulifufua na kutilia mkazo zao la karanga na  ili liwe zao lao la biashara.

 

Amesema  umaskini  utaondokana na maisha bora yatapatikana ikiwa wataelekeza nguvu zao katika kulima mazao ya biashara kama karanga na ufuta, badala ya kuelekeza nguvu zao kwa mazao ya chakula pekee.

 

Rais Kikwete ametoa wito huo leo kwa nyakati tofauti wakati alipokuwa akisalimiana na wananchi wa vijiji vya wilaya ya Kongwa  katika siku yake ya tatu ya ziara ya kikazi mkoani dodoma .

 

“Mlilima sana karanga kwa kusimamiwa na wakoloni, mlifanya kazi kwa wakoloni, leo wakoloni wameondoka tumeacha kulima karanga kwa nini” akahoji Rais na kuongeza “lifufueni zao hili kwani ndio litakalo waondoa kwenye umaskini na kuwapatia maisha bora” akatitiza.

 

Amefafanua kwamba wilaya au mkoa ambao hauna zao la biashara, ni wazi umaskini katika eneo hilo hautatoweka na wananchi hawatakuwa na maisha bora. Na hivyo akawasisitizia kujielekeza katika utafutaji wa mazao ya biashara.

 

Amewaeleza wananchi hao kwamba serikali inaposema maisha bora kwa kila Mtanzania haimanishi kuwajaza fedha mikononi bali ni kwa wananchi wenyewe  kujishughuliza katika kazi zitakazowapatia kipato na kuboresha maisha yao .

 

“Nimekwisha kuzungumza na mkoa, kwamba wakati umefika sasa wa kutillia mkazo mazao ya biashara, na kwa mkoa wenu mazao hayo ni karanga, mtama,  na zabibu, la sivyo Yesu atakapokuja kutuhukumu atatukuta bado  tu maskini na tukiishi katika nyumba za tembe.

 

Amewataka wananchi hao kuzingatia maelekezo ya wataalamu na kanuni bora za kilimo na ufugaji kwa kuwa ndiyo hasa mambo yatakayobadilisha maisha yao kwa haraka.

 

Aidha Rais amewaeleza wananchi ambao waliojitokeza kwa wingi kumwona na kumsikiliza kwamba serikali imejipanga vema kuwatumikia na kuwaondolea kero zao, na kwa wilaya hiyo kero kubwa ni maji na barabara.

 

Kuhusu tatizo la maji katika wilaya hiyo, Rais amewahakikisha wananchi kwamba tatizo hilo litakwisha kabla ya mwisho wa mwaka huu, baada  kukamilika kwa mradi unafadhailiwa  na Benki ya dunia.

 

Tayari asilimia 60 ya utekelezaji wa mradi huo ambao ni ujenzi wa matanki ya kuhifadhi maji na utandikaji wa mabomba umekwisha kukamilika.

 

Kuhusu barabara, Rais  amesema Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya barabara za wilaya hiyo.

 

 

Akiwa katika wilaya ya Kongwa,   Rais alifungua jengo la wagonjwa wa nje katika hospitali ya Wilaya hiyo  ambalo limeghalimu shilingi milioni 86. Kukamilika kwa jengo hilo kutasaidia sana kupunguza msongamano na wagonjwa na kuboresha huduma kwa wananchi.

 

Aidha Rais aliweka jiwe la msingi katika shule ya sekondari ya  Sagara, shule hiyo ambayo ni ya kata imejengwa kwa michango ya wananchi Serikali Kuu, Halmashauri na wafadhili imegharimu shilingi milioni 91, kati ya hizo milioni 42 zimetumika kwa jengo la utawala na milioni 49 kwa ujenzi wa  madarasa saba.

 

Kwa kufurahishwa na majengo mazuri ya shule hiyo ambao ina walimu 11 na wanafunzi 197, Rais alichangia shillingi milioni mbili, wanafunzi wa shule hiyo wanapatiwa huduma ya kifungua kinywa na chakula cha mchana ili kuwaepusha na utoro.

 

Kuhusu ukimwi, Rais amewahimiza kujitokeza kwa wingi Septemba 22 kupima kwa hiari ili wajue hali ya afya zao huku akiwasisitizia kutumia kinga ili kujiepusha na maambukizo mapya. Wilaya ya Kongwa ina maambukizo ya asilimia 9.

 

Mwisho.