PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

 

 

                                                      

                                        The State House,

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                       P.O. Box 9120,

Fax. No. 255-22 2113425                                                              DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz                                                            Tanzania.

              newsikulu@yahoo.com

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

 

Kikwete -  ……….Ufisadi

 

Na Maura Mwingira

10/10/2007

ARUSHA

 

 

 Rais Jakaya Kikwete ameonya tabia inayotaka kujengeka miongoni mwa wananchi na hususani wanasiasa ya kugeuka kuwa wapelelezi, wakamataji, waendesha mashtaka na watoa hukumu, na tena wakizitoa huku hizo bila ya watuhumiwa kuwapo.

 

Amesema tabia hiyo ikiachwa kuendelea siyo tu itaipeleka nchi pabaya, lakini itawatisha wananchi, itawatia hofu na kujenga chuki kati ya mtu na mtu hali ambayo amesema haiendani na  taratibu za kuendesha nchi kwa misingi ya kufuata kanuni, taratibu,  na sheria za nchi.

 

Amebainisha kwamba tabia hiyo ya wanasiasa kujigeuza kuwa wao ndio wapelelezi, wakamataji, waendesha mashtaka na watoa hukumu kuwa  haimtendei haki mtuhumiwa ambaye naye ana haki yake ya msingi ya kulindwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

 

Rais Kikwete ameeleza kuwa kila taarifa  inayohusu rushwa au tuhumu za mtu kutuhumiwa kuhusika na vitendo vya rushwa, zitachunguzwa kwa kuzingatia misingi ya sheria za nchi na vyombo vinavyohusika na si vinginevyo na kuongeza kwamba yeyote atakayethibitishwa na mamlaka halali kwamba ama ametoa rushwa au kupokea rushwa atachukuliwa hatua za kisheria bila ya kujali nafasi na madaraka aliyonayo.

 

Rais kikwete ameyasema  hayo jana usiku (Jumanne) wakati alipokuwa akimshukuru  Askofu  Thomas Laiser wa  Dayosisi Mkoani Arusha ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri la Tanzania, kwa kumpongeza (Kikwete) kwa ujasiri mkubwa wa kupambana na  vitendo vya rushwa na hasa rushwa   katika uchaguzi. 

 

Askofu Laiser alitoa pongezi hizo kwa Rais wakati wa  hafla ya uchangiaji wa ujenzi wa hosteli ya Dayosisi ya KKKT Arusha,  hafla iliyofanyika katika hoteli ya  Kibo Palace,  ambapo Rais Kikwete alikuwa mgeni rasmi. Jumla ya shilingi milioni 363.6 zilipatikana huku Rais akichangia shilingi milioni mbili. Lengo lilikuwa kukusanya shs. 350.0.

 

 

Rais Kikwete amebainisha kwamba nia na dhamira ya serikali ya Chama cha Mapinduzi ya kupambana na vitendo vya rushwa ni ya dhati, na utekelezaji wa vita hivyo umeanzia ndani ya Chama chenyewe.

 

 

Kama sisi wenyewe ndani ya Chama cha Mapinduzi tumeanza kupambana wenyewe kwa wenyewe kwa nini tushindwe kwa watu wengine,  tumedhamiria kwa dhati na wala hatutamuogopa na hatumuugopi mtu yoyote” akasema Rais.

 

 

Akasema  Kikwete “Mhe. Baba Askofu, naomba  nikushukuru kwa kunipongeza kwa juhudi zangu za kupambana na rushwa, nimefarijika sana na pongezi zako. Kwa sababu wapo watu wengine wanaoona hakuna  lolote tunalofanya, wana macho lakini hawaoni, wana masikio lakini hawasikii. Tumedhamiria kupambana na rushwa popote pale na tumeanza ndani ya Chama chetu, hiki ni kielelezo cha juu kabisa cha dhamira yetu ya kupamba na rushwa”.

 

Akizungumzia zaidi juhudi hizo za serikali za kupambana na rushwa ndani ya Chama cha Mapinduzi na taifa kwa ujumla, Rais ameeleza kwa kusema “ Nilitoa ilani na tahadhari kabla ya uchaguzi kuanza katika ngazi za wilaya, maana huko ndiko pesa zinakotembea tembea. Niliwaambia wenzangu jamani taarifa hizi za kwamba viongozi wanapata uongozi kwa kununua hii si heshima nzuri, tuachane na tabia hii”.

 

Akaendelea “Tuliviagiza vyombo vyetu kuifanya kazi hiyo. Lakini  tunafanya hivyo kwa kuzingatia misingi ya kanuni, taratibu na sheria za nchi”. Anasema Kikwete na kuongeza “ Hata wale TAKUKURU wakisema huyu tumemkamata akitoa rushwa au katika mazingira ya kutoa rushwa wao hawana uamuzi wa mwisho wa kutoa hukumu, zipo mamlaka halali zinazohusika na kutoa hukumu baada ya kuridhika na upelelezi na  uendeshaji wa kesi hiyo. Ni  mahakamani ndiko kutakako thibitisha kama mtuhumiwa huyo ametoa au hakutoa rushwa”.

 

Anaonya Rais kwa kusema. “ Lakini tusifike  mahali tukageuka sisi ndio wapelelezi, wakamataji, waendesha mashtaka na watoa hukumu. Wako wenzetu ambao wameamua kuwa wapelelezi wao, wakamataji wao, waendesha mashitaka wao na watoa hukumu wao, tena wanatoa hukumu wakati mtuhumiwa hayupo.Tusijipeleke huko na tukifanya hivyo tunaipeleka nchi pabaya, nchi itayumba na hili si jambo nzuri na wala si sawa”.

 

Anasisitiza kwa kusema “ tabia hii ya watu kujifanya wao ndio wapelelezi, wakamataji na watoa hukumu ni tabia  ambayo ikiendekezwa itawatisha wananchi, itawatia hofu,  na itajenga chuki kati ya mtu na mtu, hii si haki na wala si sawa, hii si nchi isiyokuwa na utawala wa sheria (law of the jungle). Ni nchi yenye utawala halali na unaozingatia sheria za nchi na ina mamlaka ya kutekeleza majukumu yake kwa  kuzingatia misingi ya haki, nje  ya hapo ni ukiukwaji wa misingi hiyo.”

 

Akasema  haiwezekani kauli ya mwanasiasa mmoja ya kumtuhumu fulani ndio mla rushwa ikawa ndiyo hukumu, au serikali ikalazimishwa kumchukulia hatua mtu yule kwa kutumia kauli ya mwanasiasa tu, lazima taratibu za kisheria zifuatwe, lakini kubwa na la msingi hapa hata yule anayetuhumiwa naye anayo haki yake ya msingi ya  kutendewa haki.

 

“Baba Askofu ninashukuru umeyasema haya na mimi nimeamua kuyaeleza haya niliyosema” akafafanua Rais.

 

Awali katika pongezi zake, Askofu Laiser alimweleza Rais kuwa, Dayosisi Mkoani Arusha ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania kupitia kwake linampongeza Rais Kikwete kwa moyo wa dhati, kwa ujasiri mkubwa aliochukua hivi karibuni wa kupambana na rushwa katika uchanguzi ndani ya Chama cha Mapinduzi.

 

Akasema Askofu Laiser “tunajua katika mapambano yoyote wataathirika waliomo na wasiokuwako katika jambo lenyewe, lakini afadhali waathirike wachache wasiokuwamo maana bila ya mapambano hayo wale wengi waliomo wataendelea  kuendeleza uovu  na dhambi hiyo”

 

Akasisitiza kwa kusema “Mhe. Rais tunajua mapambano hayo yana gharama zake kijamii na kisiasa, lakini gharama hizo ni ndogo ukilinganisha na athari zitakazolikumba taifa hili, rushwa za aina hii na aina nyingine zote zitakapoendelea kufumbiwa macho. Neno la Mungu linasema ila wanawe hawakuenda njia zake  bali waliziacha ili wapate faida wakapokea rushwa na kupotosha hukumu”.

 

Dayosisi Mkoani Arusha ya Kanisa la Kiijili la Kilutheri Tanzania inajenga hoteli itakayoitwa Arusha Springs Hotel mkoani Arusha kama kitega uchumi kitakachosaidia uendelevu wa miradi ya Dayosisi hiyo.

 

Hoteli hiyo inayotarajiwa kukamilika mwezi Februari mwakani itagharimu Tshs. Bilioni  3.6 sawa na dola za Kimarekani milioni 3.5.

 

Askofu Laiser amemweleza mpango wa maendeleo wa Dayosisi hiyo ambayo inahusisha ujenzi wa shule za sekondari, hospitali ya rufaa ni juhudi za Dayosisi hiyo la upunguzwaji  wa umaskini na kuisaidia serikali ya awamu ya nne iweze kufikia lengo lake la maisha bora kwa kila Mtanzania.

 

Kabla ya kuongoza harambee hiyo, Rais Jakaya Kikwete alitembelea na kukagua miradi mikubwa ya shule ya sekondari ya watoto yatima Peace House Secondary School ambayo ujenzi wake utagharimu Tsh.  Bil.8.7 sawa na dola za kimarekani  milioni 8.  mradi wa ujenzi Hospitali ya Rufaa, Arusha Lutheran Medical Centre ambayo ujenzi wake utagharimu dola za Kimarekani milioni 5.6 sawa na Tsh Bil 5.8

 

Mwisho.