PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

OF THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

 

 

 

                                                      

                          The State House,

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                P.O. Box 9120,

Fax. No. 255-22 2113425                                                       DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz                                                      Tanzania.

              ikulupress@yahoo.com

 

                                                                          

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

 

Rais Kikwete ateua majaji

wapya wa Korti ya Rufani

 

 

Rais Jakaya Kikwete amewateua Majaji wanne wa Mahakama Kuu ya Tanzania kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani.

 

Taarifa iliyotolewa leo (Jumatatu, Februari 4, 2008) na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo inasema kuwa majaji walioteuliwa ni Jaji Steven James Bwana, Jaji Bernard Michael Luanda, Jaji Mohammed Chande Othman na Jaji Sauda Mjasiri.

 

Taarifa hiyo iliyotangazwa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais inasema kuwa uteuzi huo umeanza leo hii (Jumatatu, Februari 4, 2008).

 

Uteuzi huo umefanyika kwenye Siku ya Sheria Tanzania, siku ambayo huashiria mwanzo wa kalenda ya mwaka wa shughuli za Mahakama nchini.

 

Kabla ya uteuzi wake, Jaji Bwana alikuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha.

 

Jaji Bwana ambaye aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu mwaka 1999, pia amepata kuwa Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Jaji wa Mahakama Kuu ya Visiwa vya Seychelles, na Katibu Sheria wa Jaji Mkuu wa Tanzania.

 

Jaji Bwana pia alikuwa Jaji Mfawidhi wa kwanza Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara.

 

Naye Jaji Luanda, kabla ya uteuzi wake, alikuwa Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara, mjini Dar es Salaam.

 

Jaji Luanda amepata kuwa Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, na aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2000.

 

Jaji Mjasiri alikuwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Biashara, Dar es Salaam kabla ya uteuzi wake.

 

Jaji Mjasiri ambaye amepata kuwa mwanasheria katika Shirika la Sheria Tanzania (TLC), na mwanasheria wa Benki ya Biashara na Maendeleo ya Mashariki na Kusini mwa Afrika (PTA), aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2002.

 

Kabla ya uteuzi wake, Jaji Othman alikuwa katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam.

 

Jaji Othman amepata kuwa mwanasheria katika Chama cha Msalaba Mwekundu (IRC), amepata kuwa Mwanasheria Mkuu wa serikali ya Visiwa vya Timor Mashariki, na pia kuwa mwendeshaji mashitaka katika Mahakama ya Kimataifa ya Rwanda (ICTR) mjini Arusha.

 

Aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2004.

 

 

Ikulu

Dar es Salaam

 

05/2/2008