DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Rais Kikwete: Toeni pesa tumalize migogoro Afrika

 

Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametoa changamoto tatu kwa Umoja wa Mataifa (UN) katika mahusiano yake na AU, ili kwa pamoja, taasisi hizo mbili ziweze kufanikiwa katika kutatua migogoro ya Afrika.

 

Akizungumza leo (Jumatano, Aprili 16, 2008) katika Baraza la Usalama la UN mjini New York, Marekani, Rais Kikwete amesema kuwa kuna umuhimu wa taasisi hizo mbili kuweka taratibu wa jinsi AU inavyoweza kuingilia migogoro ya Afrika bila kusababisha mgongano na UN.

 

Amesema kuwa kuna wakati AU inaona umuhimu wa kuingilia haraka na kumaliza tatizo katika nchi ya Afrika na inafanya hivyo, hata kama wajibu mkuu wa kumaliza migogoro duniani ni wajibu wa UN. Hili, amesema, linaweza kusababisha mgongano kati yake na AU kama halikuwekewa taratibu na mipaka inayojulikana na kukubaliwa na kila taasisi.

 

Pili, Rais Kikwete amesema kuwa upo umuhimu mkubwa wa UN kuisaidia AU katika kujenga uwezo wake wa kuingilia na kumaliza migogoro ya Afrika haraka na bila ucheleweshaji wowote.

 

Pia Rais Kikwete amesema kuwa suala la kuijengea AU uwezo, hasa linalohusiana na umuhimu wa UN kuruhusu ulinzi wa amani unaoidhinishwa na UN na kuendeshwa na taasisi za kikanda kama AU, kugharimiwa na UN.

 

Kwa sasa taratibu za UN hairuhusu Umoja huo kugharimia shughuli hizo, hata kama zimeidhinishwa na Baraza la Usalama la UN.

 

Rais Kikwete ametoa mapendekezo hayo mahsusi wakati anahutubia kikao maalum cha ngazi ya juu cha pamoja kati ya Baraza la Usalama la UN na Baraza la Amani na Usalama la AU.

 

Kikao hicho kinatafuta njia za jinsi taasisi hizo zinavyoweza kushirikiana katika kutatua migogoro ya kisiasa ya Afrika.

 

Kikao hicho cha aina yake kimeitishwa na Afrika Kusini ambayo ndiyo mwenyekiti wa Baraza la Usalama la UN kwa mwezi huu wa Aprili.

 

Alikuwa ni Rais Thabo Mbeki wa Afrika Kusini ambaye alifungua kikao hicho kabla ya kumkaribisha Naibu Katibu Mkuu wa UN wa masuala ya siasa, B. Lynn Pascoe kuzungumza na kufuatia na Rais Kikwete.

 

Miongoni mwa viongozi wengine maarufu waliozungumza katika kikao hicho ni Waziri Mkuu wa Uingereza, Gordon Brown; Waziri Mkuu wa Italia, Romano Prodi; Rais wa Ivory Coast, Laurent Gbagbo; Rais wa DRC, Joseph Kabila na Rais wa Somalia, Abdullahi Yusuf Ahmed.

 

Wengine ni Waziri Mkuu wa Ethiopia, Meles Zenawi; Makamu wa Rais wa Botswana, Luteni Jenerali Mompati Merafhe na Mwenyekiti wa Tume ya AU, Alpha Omar Konare.

 

Jumla ya viongozi wa serikali na nchi pamoja na wawakilishi wao kutoka nchi 42 wamezungumza katika kikao hicho maalum.

 

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki Moon aliahidi kuwa UN iko tayari kuendelea kushirikiana na AU katika kumaliza migogoro inayoendelea katika Bara hilo.

 

Ban Ki Moon amesema kuwa Afrika ni Bara ambalo limekuwa moyoni mwake hata kabla ya kushika madaraka makubwa ya UN.

 

Amesema kuwa tokea kukamata madaraka ya ukatibu mkuu, ametembelea nchi 11 za Bara hilo na kuwa kuanzia kesho (Ijumaa, Aprili 18, 2008) anaondoka tena mjini New York kutembelea nchi nyingine nne za Afrika.

 

Amempongeza na kumshukuru Mwenyekiti wa Tume ya AU, Konare kwa mchango wake katika AU ambako amekuwa kiongozi wa kwanza tokea kuanzishwa kwa umoja huo. Konare anamaliza muda wake mwishoni mwa mwezi huu.

 

Mwisho.

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais na HabariabariHabar,

NEW YORK.

17/04/2008