DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

TRL yaahidi kuongeza ufanisi katika kuendesha Reli ya Kati

 

Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) imeahidi kuongeza ufanisi wake katika uendeshaji wa Reli ya Kati, ili kuhakikisha kuwa Reli hiyo inatoa mchango mkubwa zaidi katika uchumi wa Tanzania, na kuboresha usafiri kwa Watanzania.

 

Kampuni hiyo imetoa ahadi hiyo leo, Ijumaa, Januari 16, 2009 wakati uongozi wa TRL ulipokutana na kufanya mazungumzo na Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika mfululizo wa mikutano yake na viongozi wa Wizara mbalimbali na mashirika yake ili kutafakari utendaji wa Serikali yake.

 

Mkutano wa leo, kama ilivyokuwa mikutano iliyoanza jana (Alhamisi, Januari 15, 2009) umehudhuriwa na Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein, Waziri wa Miundombinu Dk. Shukuru Kwambwa na Katibu Mkuu Kiongozi Philemon Luhanjo.

 

Katika mkutano huo uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam, uongozi huo wa TRL imesema kuwa ni kweli yamekuwepo matatizo katika uendeshaji wa kampuni hiyo, lakini hayo ni matatizo ya mwanzo tu na kuwa ufanisi wa Kampuni hiyo utaongezeka kwa kadri muda unavyokwenda.

 

TRL ni kampuni tanzu inayomilikiwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania inayomiliki hisa asilimia 49 na Shirika la Rites la India ambalo linamiliki asilimia 51.

 

Kampuni hiyo iliundwa mwaka juzi, 2007, kwa ajili ya kuendesha Reli ya Kati baada ya RITES kuwa imeshinda zabuni ya kuendesha Reli hiyo ya kati kwa miaka 25.

 

Uongozi huyo wa TRL umetoa ahadi hiyo ya kuongeza ufanisi baada ya kikao cha leo kuwa kimejadili hali ya utendaji ya kampuni hiyo, na matatizo ambayo yamekuwa yanaikwamisha kampuni hiyo kutoa huduma bora zaidi kwa wateja.

 

Baada ya mkutano huo wa leo kuwa umejadili masuala mbali mbali ya Reli hiyo ya Kati ikiwa ni pamoja na utunzaji wa reli hiyo, usalama wake, hali yake ya kifedha na mambo mengine, uongozi wa TRL umeahidi kuongeza ufanisi wake ili kutoa huduma bora zaidi kwa Watanzania.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

16 Januari, 2009