DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Wadau wakubaliana kumaliza msongamano Bandari ya Dar

 

WADAU wote Wakuu wa Bandari ya Dar es Salaam wamekubaliana kumaliza kabisa msongamano wa mizigo katika Bandari hiyo, haraka iwezekanavyo, na pengine katika mwezi mmoja ujao.

 

Wadau hao, kila mmoja wao, amekubali kutoa mchango wake katika kuhakikisha kuwa mlundikano wa mizigo katika Bandari hiyo unamalizwa ili kuiwezesha Bandari hiyo kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.

 

Wadau hao wamefikia msimamo huo katika majadiliano ya kina na ya wazi wakati walipokutana na Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika mkutano maalum ulioitishwa kujadili na kukubaliana juu ya njia za kupunguza ama kumaliza mlundikano wa bidhaa katika Bandari hiyo.

 

Mkutano huo uliofanyika leo, Ijumaa, Januari 16, 2009 Ikulu, Dar Es Salaam ulikuwa sehemu ya mikutano iliyoanza jana ambako Rais anakutana na Wizara mbali mbali na mashirika yaliyoko chini ya Wizara hizo kutathmini utendaji wa Serikali yake.

 

Mkutano huo uliohudhuriwa na Makamu wa Rais Dk Ali Mohamed Shein, Waziri wa Miundombinu Dk Shukuru Kawambwa na Katibu Mkuu Kiongozi Philemon Luhanjo umehudhuriwa pia na uongozi wa Mamlaka ya Bandari (TPA) na ule wa Bandari yenyewe ya Dar es Salaam.

 

Wengine waliohudhuriwa mkutano huo ni Kampuni ya Kupakua na Kupakia Mizigo katika Bandari ya Dar Es Salaam (TICTS), Mawakala wa Kuondoa Mizigo Bandarini (Clearing and Forwarding Agents), Chama cha Wamiliki Meli Tanzania (Tanzania Shippers Association), Chama cha Wasafirishaji Tanzania (Tanzania Transporters Association) na Chama cha Wamiliki wa Vituo vya Kontena Nje ya Bandari (ICD,s).

 

Miongoni mwa hatua ya kwanza itakayochukuliwa kumaliza mlundikano huo ni kuondoka haraka iwezekanavyo kiasi cha makontena 5,332 ya mizigo ambayo yamelundikana katika Bandari hiyo.

 

Makontena hayo yatahamishiwa katika ICD’s zenye wa kuchukua zaidi ya makontena 8,300 kwa wakati mmoja na ambazo kwa sasa hazina mizigo.

 

Wadau hao wamekubaliana kuwa moja ya matatizo makubwa na yanayosababisha msongamano katika Bandari hiyo ni baadhi ya waagiza mizigo kuigeuza Bandari ya Dar es Salaam kuwa ghala la kuwekea mizigo badala ya Bandari hiyo kuruhusiwa kuwa sehemu ya kupitishia mizigo tu, iwe ya kusafirisha nje ya nchi ama ya kupokelewa nchini kutoka nje.

 

Katika mkutano huo pia imekubaliwa kuchukua hatua za kuzungumza na nchi jirani za Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kutafuta matatizo ambayo ufumbuzi wake unahitaji ushirikiano wa nchi hizo kwa sababu za kupitia mizigo yao katika Bandari hiyo ya Dar es Salaam.

 

Imetolea na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

16 Januari, 2009