UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

RAIS Jakaya Mrisho Kikwete ameiomba China kusaidia kuanzisha Benki ya Kilimo nchini ikiwa ni mradi wa pamoja kati ya Serikali za Tanzania na China.

 

Rais Kikwete amesema kuwa ni muhimu kuimarisha sekta ya kilimo nchini kwa kuianzishia sekta hiyo benki, kwa sababu kilimo bora ndicho kitawatoa Watanzania wengi zaidi katika umasikini na kwa haraka zaidi.

 

Kilimo ndicho kitatusaidia kusonga mbele haraka. Tunahitaji mikopo kwa wakulima wetu. Tunawaombeni mwangalie uwezekano wa China kuwekeza katika kilimo chetu. Benki ya pamoja ya kutoa mikopo kwa wakulima wetu,” Rais Kikwete amemwambia Balozi wa China nchini Tanzania Liu Xinsheng katika mkutano uliofanyika leo, Jumatatu, Januari 19, 2009 Ikulu, Dar es Salaam.

 

Balozi Xinsheng amesema kuwa anaelewa fika umuhimu wa benki ya kilimo kwa maendeleo ya kilimo cha Tanzania na akaahidi kuwa atawasilisha maombi hayo ya Rais Kikwete kwa Serikali yake.

 

Balozi Xinsheng pia ametumia mkutano huo kumweleza Rais Kikwete kuhusu maendeleo yaliyopatikana katika maandalizi ya kuanzishwa kwa Eneo la Maendeleo ya Uchumi (Economic Development Area – EDA).

 

Pia amemweleza Rais Kikwete kuhusu mipango ya kutekelezwa kwa awamu nyingine ya usambazaji maji ya Mradi wa Maji wa Chalinze. Mradi huo ulijengwa kwa msaada wa Serikali ya China.

 

Balozi Xinsheng pia amemkabidhi Rais Kikwete ramani ya Kituo cha Mikutano cha Julius Nyerere Convention Centre (JNCC) uliopangwa kujenga mjini Dar es Salaam.

 

Ujenzi wa Kituo hicho utagharimiwa na Serikali ya China, na mkataba wa ujenzi wa Kituo hicho ulitiwa saini wakati wa ziara ya Rais Kikwete nchini China Mei mwaka jana. Kituo hicho kinatarajiwa kugharimu dola za Marekani milioni 11.

 

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

19 Januari, 2009