UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

BENKI Kuu ya Tanzania (BOT) imesema kuwa inatarajia kuwa mfumuko wa bei uliopanda ghafla mwaka jana, kwa sababu ya kupanda mno kwa bei za mafuta na vyakula (nafaka), utaanza kushuka katika siku za karibuni, na hivyo kuteremsha gharama za maisha.

 

BOT imesema kuwa sababu kubwa ya mfumuko wa bei kubakia juu kwa sasa, baada ya bei ya mafuta kuwa imeshuka, ni gharama kubwa za usafirishaji wa vyakula.

 

Mfumuko wa bei nchini ulikuwa asilimia 13.5 kwa mwezi uliopita wa Desemba kutoka asilimia 8.6, kabla ya kuanza kupanda ghafla na kwa kiasi kikubwa kwa bei ya mafuta na bei duniani na ile ya chakula.  

 

Pamoja na hali hiyo, BOT inabashiri kuwa lengo la ukuaji wa uchumi kwa asilimia 7.5 bado linaweza kufikiwa.

 

Maelezo hayo ya BOT yako katika ripoti ya benki hiyo iliyowasilishwa na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Benno Ndullu, leo, Jumatatu, Januari 19, 2009, katika mkutano kati ya Wizara ya Fedha na Uchumi, na taasisi zake, na Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

 

Mkutano huo uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam ni mfululizo wa mikutano kati ya Rais Kikwete na Wizara mbalimbali za Serikali inayolenga kutathmini utekelezaji wa Serikali yake katika miaka mitatu tokea kuingia madarakani.

 

Tofauti na mikutano aliyoifanya mwanzoni mwa utawala wake ambako Rais alitembelea kila Wizara na kutoa maelekezo yake, mikutano ya sasa inafanyika Ikulu kati ya Rais na viongozi wa juu wa Wizara mbalimbali na taasisi za Wizara hizo.

 

Gavana Ndullu amemwambia Rais Kikwete kuwa utafiti uliofanyika katika miji yote nchini kwa mwaka mzima wa jana, 2008, unaonyesha kuwa mfumuko wa bei ulishuka kwa bidhaa na huduma zote zisizokuwa chakula.

 

Utafiti huo wa BOT unaonyesha kuwa mfumuko wa bei wa chakula uliongezeka kutoka asilimia 10.1 Januari mwaka jana hadi kufikia asilimia 18.6 mwezi uliopita wa Desemba, mwaka jana.

 

Amesema Gavana Ndullu: “Hata hivyo, kutokana na mwenendo wa hivi karibuni wa bei za mafuta katika soko la dunia, ambapo bei ya mafuta imeshuka kiasi kikubwa, mfumuko wa bei unatarajiwa kuanza kushuka katika siku za usoni.”

 

Gavana pia amesema kuwa kumekuwapo na kasi kubwa ya ongezeko la mikopo kwa sekta binafsi kutoka mabenki katika kipindi cha miezi mitano ya mwanzo ya mwaka wa fedha 2008/2009.

 

Amesema kuwa mikopo hiyo imeongezeka kwa kiasi cha sh. bilioni 840.4 ambalo ni ongezeko la asilimia 85 ya ongezeko la sh bilioni 900 zilizokusudiwa kukopesha sekta binafsi kwa mwaka mzima.

 

Gavana Ndullu pia ameeleza kuwa hazina ya fedha za kigeni katika BOT hadi kufikia Desemba mwaka jana ilikuwa ni dola za Marekani bilioni 2,894.42, ambazo zinatosha kuweza kuagiza bidhaa kutoka nje kwa kipindi cha miezi minne 4.3.

 

Kuhusu sekta ya fedha, Gavana amesema kuwa sekta hiyo imeendelea kuimarika mwaka uliopita na kuwa mabenki 31 kati ya mabenki 34 yanayofanya kazi nchini yanakidhi kiwango cha mtaji unaoweza kuhimili madai (capital adequacy ratio) kwa asilimia inayofikia asilimia 17, ikilinganishwa na kiwango kinachokubaliwa kimataifa, yaani asilimia 10.

 

Gavana amesema kuwa kwa jumla mabenki yote nchini yanayo ukwasi (capital) wa kutosheleza malipo kwa wateja wao kwa kiwango cha asilimia 50.7 ikilinganishwa na kiwango kinachokubaliwa kibenki cha asilimia 20.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

19 Januari, 2009