DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameondoka nchini asubuhi ya leo, Jumamosi, Januari 31, 2009, kwenda Addis Ababa, Ethiopia, kuhudhuria Mkutano wa 12 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa AU.

 

Mkutano huo wa 12 utafanyika kwa siku mbili kuanzia keshokutwa, Jumatatu, Januari 2, 2009, kwenye Ukumbi wa UNCC-EAC mjini Addis Ababa.

 

Mkutano huo utatanguliwa na Kikao Maalum cha wakuu hao wa nchi wanachama wa AU kitakachofanyika kesho, Jumapili, Februari Mosi, 2009, kujadili maendeleo ya kuanzishwa kwa Serikali ya Umoja wa Afrika.

 

Kikao hicho maalum kitafanyika chini ya uenyekiti wa Rais Kikwete, katika nafasi yake kama Mwenyekiti wa AU, na ni mwendelezo wa majadiliano ya suala hilo kama ilivyoamuliwa katika kikao kilichopita cha AU kilichofanyika Sharm El Sheikh, Misri, Juni, mwaka jana.

 

Kikao hicho maalum kitapokea na kujadili ripoti ya Kamisheni ya AU juu ya mapendekezo ya jinsi ya kuanzishwa kwa Serikali hiyo.

 

Kikao hicho kitafuatiwa na Mkutano wenyewe wa 12 wa wakuu wa nchi hizo utakaofanyika kwenye ukumbi huo huo wa UNCC-ECA.

 

 

 

Rais Kikwete ataufungua Mkutano huo ambao pia utamchagua mwenyekiti mpya wa AU, ambaye atachukua nafasi ya Rais Kikwete, anayemaliza muda wake kwenye nafasi hiyo.

 

Miongoni mwa wazungumzaji kwenye ufunguzi huo, mbali na Rais Kikwete mwenyewe, watakuwa ni pamoja na Waziri Mkuu wa Ethiopia Ato Meles Zenawi, Mwenyekiti wa Kamisheni ya AU Jean Ping, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon, na Katibu Mkuu wa Umoja wa Nchi za Kiarabu (Arab League) Amr Moussa.

 

Kwenye siku ya pili ya Mkutano huo, Jumanne, Februari 3, 2009, wakuu hao watajadili zahama ya kifedha inayoikabili dunia baada ya kuwa wamewasikiliza wataalam mbalimbali wa masuala ya fedha katika Afrika na duniani.

 

Kwenye siku hiyo ya pili na ya mwisho ya Mkutano huo, Tanzania inatarajiwa kuwasilisha mapendekezo ya mfumo wa kisheria wa kuwalinda masikini katika Afrika.

 

Mbali na mkutano huo, Rais Kikwete pia atahudhuria Mkutano wa 20 wa Kamati ya Utekelezaji ya Wakuu wa Nchi za NEPAD uliopangwa kuanza asubuhi la leo, Jumamosi, Januari 31, 2009.

 

Baadaye mchana, Rais Kikwete atahudhuria mkutano maalum wa eneo la Maziwa Makuu ambao utapokea na kujadili ripoti kuhusu hali ilivyo katika Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

 

Ripoti hiyo itawasilishwa na marais wa zamani, Olusegun Obasanjo wa Nigeria na Benjamin Mkapa wa Tanzania ambao wameombwa na Umoja wa Mataifa na Wakuu wa Nchi za Maziwa Makuu kuongoza jitihada za kuleta amani Mashariki mwa DRC.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

31 Januari, 2009