DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

Na Mwandishi Maalum,

 

MAELFU ya wakulima wadogo nchini wanatarajiwa kunufaika na mpango wa uwezeshaji, ambako kila mkulima atakopeshwa mahitaji ya kilimo yenye thamani ya zaidi ya sh 200,000 kwa mwaka, ili kumwezesha kuinua uzalishaji na kujiongezea kipato.

 

Chini ya mpango huo unaogharimiwa kwa pamoja na taasisi mbalimbali duniani, ikiwamo ile ya Bill and Melinda Gates Foundation, wakulima hao watapewa mbegu, mbolea na mahitaji mengine ya kuwezesha kuinua kiwango cha uzalishaji.  Wakulima pia watahakikishiwa soko la mazao yao.

 

Ujumbe wa watu 17 kutoka taasisi hizo umemwambia Rais Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatatu, Februari 9, 2009, kwamba mpango huo utawashirikisha wakulima kiasi cha 250,000 wa Tanzania katika awamu ya kwanza ya miaka mitatu.

 

Mbali na Bill and Melinda Gates Foundation, taasisi nyingine zinazoshiriki katika mpango na ambao wajumbe wake wamekutana na Rais Kikwete leo, Ikulu, Dar es Salaam ni Alliance for a Green Revolution in Afrika (AGRA), Standard Bank na Export Trading Group.

 

Wakati wa mazungumzo yake na ujumbe huo, Rais Kikwete ameziomba taasisi zinazoshiriki katika mpango huo kuongeza idadi ya wakulima wa Tanzania watakaonufaika na mpango huo. “Kiasi cha wakulima 250,000 ni kizuri, lakini fikirieni angalau kuanza na wakulima 1,000,000 hivi,” amesema Rais Kikwete.

 

 

Rais amesema kuwa mpango huo ni muhimu sana kwa sekta ya kilimo ya Tanzania ambayo, kimsingi, inakwamishwa na ukosefu wa mikopo midogo midogo ya  kumwezesha mkulima kupata fedha za kununulia mahitaji muhimu ya kilimo.

 

Rais ameshukuru na kusema kuwa katika mazingira ambamo asilimia 80 ya wananchi wote wa Tanzania wanaishi kwa kutegemea kilimo, tena kilimo cha kujikimu, ni jambo lisilofikirika kuwa Serikali inaweza kupuuza mipango kama ule uliobuniwa na taasisi hizo.

 

Amesema kuwa matatizo makubwa ya kilimo cha Tanzania ni kutokutumika maji ya kutosha katika kilimo (umwagiliaji mdogo), kutokutumika mbegu bora na hivyo kusababisha uzalishaji duni, kutokutumika mbolea ya kutosha, kutokutumika madawa ya kuua wadudu wanaoharibu mazao, ukosefu wa mipango mizuri ya ununuzi wa mazao ya wakulima na miundombinu bora vijijini kuwawezesha wakulima kusafirisha mazao yao.

 

“Sisi hapa bado tunatumia kilo nane za mbolea kwa eka moja wakati wenzetu kule Uholanzi wanatumia kilo 500, na hivyo siyo jambo la kushangaza kwamba uzalishaji wetu ni duni na wa chini mno,” Rais Kikwete ameuambia ujumbe huo.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

09 Februari, 2009