DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

TANZANIA na Zambia zimekubaliana kushirikiana zaidi katika kutafuta majawabu ya matatizo yanayoikabili Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA).

 

Nchi hizo mbili pia zimekubaliana kushirikiana katika kuboresha huduma nyingine za kiuchumi zinazomilikiwa na kuendeshwa kwa pamoja kati ya nchi hizo mbili.

 

Pia nchi hizo zimekubaliana kuhusu umuhimu wa kurahisisha taratibu za kuvusha malori kwenye mpaka wa pamoja wa Nakonde kati ya nchi hizo mbili.

 

Hayo yalikuwa baadhi ya masuala yaliyozungumzwa na kukubaliwa leo, Jumatatu, Februari 9, 2009, wakati wa mazungumzo rasmi ya Kiserikali kati ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Rais Rupiah Bwezani Banda wa Zambia.

 

Rais Banda amewasili nchini leo kwa ziara ya siku mbili ya kikazi yenye madhumuni ya kujitambulisha rasmi kufuatia kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa nchi hiyo rafiki na jirani ya Zambia miezi mitatu iliyopita. Rais Banda ataondoka nchini kesho kurejea nyumbani.

 

Mazungumzo hayo rasmi yaligusia maeneo kadhaa ikiwa ni pamoja na uhusiano kati ya nchi hizo mbili, masuala ya kikanda na majadiliano kuhusu jinsi tatizo kubwa ya kiuchumi duniani linavyoathiri chumi za nchi hizo mbili.

 

Juu ya uhusiano kati ya Tanzania na Zambia, viongozi hao wawili wamejadili hali ya Reli ya TAZARA inayomilikiwa kwa pamoja na nchi hizo mbili na kukubaliana kuwa yatafutwe majawabu ya matatizo yanayoikabili reli hiyo kwa sasa.

 

Marais hao wawili wamewaelekeza mawaziri wao kukaa chini na kutoa mapendekezo ya jinsi ya kumaliza matatizo yanayoikabili TAZARA.

 

 

Viongozi hao wawili pia wamejadili huduma nyingine za kiuchumi zinazomilikiwa na kuendeshwa kwa pamoja na nchi hizo mbili ikiwemo barabara kuu ya kutoka Dar es Salaam hadi Lusaka ya TAZAM, na bomba la mafuta la TAZAMA linalounganisha miji mikubwa hiyo miwili ya nchi hizo mbili.

 

Marais hao vile vile wamejadili namna ya kurahisisha uvukaji mpaka wa Nakonde hasa kwa malori makubwa ya mizigo na pia wamejadili na kukubaliana namna gani ya kumaliza matatizo ya umeme ambao Zambia inatoa kwa Tanzania kwa miji ya Mbeya na Sumbawanga.

 

Kuhusu masuala ya kanda, viongozi hao wawili wameridhishwa na maendeleo ambayo yamepatikana katika siku za karibuni katika migogoro ya kisiasa ya Zimbabwe na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

 

Rais Kikwete na Rais Banda pia wamekubaliana pia kuhusu umuhimu wa kufufua Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC), ili iweze kutafuta namna ya kuongeza kasi ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

 

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

09 Februari, 2009