DIRECTORATE
OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
UNITED
|
Telephone: 255-22-2114512, 2116898 E-mail: press@ikulu.go.tz Fax: 255-22-2113425
|
|
PRESIDENT’S OFFICE, THE
STATE HOUSE, P.O. BOX 9120, DAR
ES SALAAM. Tanzania. |
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UJERUMANI imeihakikishia Tanzania kuwa itaendelea kutimiza ahadi zake za
misaada kwa
Tanzania pamoja na matatizo makubwa ya kiuchumi na
kifedha yanayozikabili chumi za nchi
mbali mbali duniani, ikiwamo Ujerumani yenyewe.
Nchi hiyo pia imempongeza
Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa jitihada
na mchango wake mkubwa katika kuleta
amani katika Bara la Afrika, na hasa
katika eneo la Maziwa Makuu.
Ujerumani imetoa uhakikisho huo kwa
Tanzania na pongezi hizo kwa Rais
Kikwete leo, Alhamisi, Februari 19, 2009, wakati wabunge wa Kamati ya
Fedha ya Bunge la Ujerumani walipokutana na kufanya mazungumzo
na Rais Kikwete.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar Es
Salaam, Rais Kikwete amewahakikishia wabunge hao kuwa Tanzania inaendelea kuunga mkono jitihada za Ujerumani kupata
kiti cha kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UN).
Rais Kikwete pia ameishukuru
Ujerumani kwa
misaada ambayo wamekuwa wanatoa kwa Tanzania, akiwahakikishia kuwa misaada hiyo
inatumika kama ilivyokusudiwa.
Rais pia amewaelezea wabunge hao kuhusu
jitihada zinazofanywa na Serikali
katika kujenga nidhamu zaidi katika
matumizi ya fedha za umma.
Pia, Rais amewaeleza wabunge hao juu
ya jitihada zinazofanywa kuimarisha Ofisi ya Mdhibiti
na Mkaguzi
Mkuu wa Serikali
(CAG) kuweza kusimamia vizuri matumizi ya Serikali na
kuweza kufanya ukaguzi wa kuthibitisha
kuwa thamani ya miradi nchini
inalingana na fedha inayotumika kwenye miradi hiyo.
Nao wabunge hao wamesisitiza
msimamo wa
Ujerumani wa kuendelea kuunga mkono jitihada za Afrika katika
kupata kiti kimoja ama viwili
vya kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Mwisho
Imetolewa na Kurugenzi
ya Mawasiliano ya Rais
Ikulu
Dar es Salaam.
19 Februari, 2009