PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

 

Fax. No. 255-22 2113425                                                       The State House,                            

Tel: 255-22-2116539/2116913                                                P.O. Box 9120,

                                                                                           DAR ES SALAAM.

 

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

 

MSIFANYE KAZI KWA MAZOEA-KIKWETE

·        Awataka viongozi kuwa wabunifu

·        Awataka kuachana na ofisi zao na kwenda kwa wananchi

 

 

Na Maura Mwingira

SERENGETI

 

14/8/2006

 

  

Rais Jakaya Kikwete amewataka viongozi wote katika ngazi za utendaji na utawala  kuachana na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea na badala yake wawe na mawazo mapya yatakayosukuma maendeleo ya wananchi.

 

Rais ametoa rai hiyo  jana wakati alipokuwa akizungumza na viongozi wa mkoa wa Mara wakati alipokuwa akitoa majumuisho ya ziara yake ya kikazi ya siku sita Mkoani hapa. Majumuisho hayo yalifanyika katika hoteli ya Kitalii ya Grument wilayani Serengeti

 

“Viongozi tusifanya kazi kama ilivyokuwa zamani, usisema zamani tulikuwa tunafanya hivi, lazima sasa tuwe na mawazo mapya yatakayolenga kusukuma mbele maendeleo ya watu,” alisema.

 

Na kuongeza kuwa ni jambo jema kwa viongozi kutowakemea au kuwakwepa, watu wanaowaletea mawazo mapya kwa kisingizo cha zamani tulikuwa tunafanya hivi, au kuwahoji wameyatoa wapi mawazo hayo.

 

Rais Kikwete alitoa mfano kwa kusema kuwa hata uteuzi wa wakuu wa wilaya ambao ulifanyika hivi karibuni haukuwa na mabadiliko makubwa kwa wakuu wa wilaya wa zamani, karibu  nusu yao walibaki na kuhamishwa vituo vyao vya kazi ili hali 10 wakibakishwa katika vituo vyao vya zamani kwa sababu mbalimbali zikiwamo za kukaribia kustaafu.

 

“Tulifanya hivyo kwa sababu tunataka viongozi hawa waende katika eneo jipya ili wakawe na mawazo mapya”

 

Hata hivyo alibainisha kuwa viongozi hao wa zamani wanaweza kuendelea na staili zao za zamani, lakini  wakatenda kwa kasi mpya, ari mpya na nguvu mpya, huku wakiwa wabunifu wa mambo mapya.

 

“Usiwe kiongozi ambaye ukiamka asubuhi unakwenda ofisini, unasoma mafaili, unauliza kuna barua ngapi, unasoma magazeti kisha huyo unafunga ofisi, siku imekwisha unarudi nyumbani” alisema

 

Na kuwataka viongozi  wajiulize kwa uwazi ndani ya mioyo yao pale wanapoondoka katika vyeo vyao au katika mikoa na wilaya wanazoongoza wakumbukwe kwa jambo lipi jema walilowafanyia wananchi wanaowaongoza.

 

“Jiulize hivi miye Kikwete baadaya  ya uongozi wangu nataka nikumbukwe kwa lipi, ukijiuliza hivyo ndani ya moyo wako basi wakati wote unakuwa na jambo jipya. Tukiwa na moyo huu hata kasi ya maendeleo yetu itakuwa kubwa, lakini tukifanya kazi kwa mazoea hatufiki mbali na hiyo ndiyo sura ya uongozi” alisisitiza.

 

Katika majumisho hayo ambayo yaliwahusisha viongozi wa serikali na chama tawala,  Rais Kikwete aliwataka pia kufanya kazi kwa malengo yanayopimika.

 

Aliwataka pia kuwatembelea wananchi katika maeneo wanayoishi na kufanya kazi, kwa kuwa kwa kufanya hivyo si tu kutawajengea uwezo wa kuyafamu maeneo yao ya utawala lakini pia inakuwa rahisi kwao kufahamu shida za wananchi na wafanyakazi, na vile vile kujiamini.

 

“Acheni kukaa kwenye ofisi zenu kubwa, viti vya kuzunguka na viyoyozi,mkurugenzi wa halmashauri unatumia muda mwingi kukaa ofisini, na matokeo yake unadanganywa na  maofisa wako, wanajaza night na kwenda safari kwa kazi ambazo hawakuzifanya. Na matokeo yake  wakurugenzi wengi mnapata matatizo kwa sababu hamko makini” alifafanua.

 

Rais alisema kuwa wakurugenzi wengi ni warasimu wakubwa na wanaodhani kuwa heshima kubwa kwao ni kukaa ofisi kwao. Wanasubiri hadi Mkuu wa Mkoa au Rais afanya ziara ndipo na wao wanatokea.

 

“Jamani viongozi tuwe wepesi wa kutatua matatizo ya wananchi, tuwajali, tusikilize kero zao, na mara nyingi kero nyingi zinazotolewa na wananchi ufumbuzi wake umo  ndani yenu, vinginevyo wananchi hao wakiyafikisha kwa Rais munaanza oho majungu, oh watu wafitini, badilizi staili zenu za kufanya kazi, kwa sababu watu wa nchini wanateseka sana. Kwa sababu viongozi wa juu hawana interest na matatizo yao”. Alibainisha.

 

Na kwa sababu hiyo aliwataka wakurugenzi wa halmashauri za miji kuwa macho na masikio yao yawe wazi ,kwa kuwa hakuna mkubwa mwingine zaidi yao.

 

Akasisitiza kuwa kwakiongozi  wa kuchaguliwa na kuteuliwa mtaji wao ni wananchi na si vinginevyo.

 

Aidha Rais aliwataka viongozi hao kuimarisha utawala bora kwa kuwa heshima ya serikali ni  kutenda vema.

 

“Fanyeni vizuri katika utawala, ongozeni vizuri katika uchumi, simamieni ulinzi na usalama, zingatieni maadili ya kazi na utumishi. Maana heshima ya serikali ni kuzingatia maadili, kujali taratibu za kazi , kuheshimu sheria na kuheshimu haki za binadamu”.

 

Rais aliwaambia viongozi hao kuwa katika ziara yake hiyo yako mambo mengi mazuri aliyojifunza. Miongoni mwa hayo ni kwamba wananchi wa mkoa wa Mara wana ari kubwa ya kujiletea maendeleo yao.

 

Karibu wilaya zote au zimekamilisha ujenzi wa shule za sekondari katika kila kata, na ama nyingine ziko katika hatua za ukamilishaji.

 

Rais alisema amegundua pia kwamba mkoa huo una ardhi nzuri inayofaa kwa kilimo katika baadhi ya wilaya, inazo raslimali za utalii na madini, na kuna ari ya viongozi katika  kuleta maendelo ya kukuza uchumi wa mkoa huo..

 

Aidha Rais alizitaja baadhi ya changamoto zinazowakabili viongozi wa mkoa huo, kuwa ni pamoja na kupambana na umaskini.

 

Alisema kuwa kielelezo kikubwa cha hali ya umaskini wa wakazi wa mkoa huo ni hali ya nyumba zao, ambazo alisema hazifanani na utajiri mkubwa uliomo mkoani humo ukiwamo wa ng’ombe.

 

Na kwa sababu hiyo aliwataka kupambana na mila zinazokinzana na dhana nzima ya maendeleo, kuwapatia elimu watoto wa kike, kuongeza kasi katika ukusanyaji wa mapato, kukabiliana na vitendo vya uhalifu, mauaji ya watu, wizi wa mifugo, uharamia kwenye ziwa, kupambana na magendo ya uuzaji wa chakula na mapambano dhidi ya ugonjwa wa ukimwi na kilimo cha bangi.

 

Alisema kuwa serikali imejipanga vema katika utekelezaji na kuyapatia ufumbuzi baadhi ya matatizo sugu yanaoukabili mkoa huo, hususani upatikanaji wa maji safi na salama, barabara na huduma madhubuti za afya na kuchangia katika sekta ya elimu hususani katika upatikanaji wa walimu, vifaa vya maabara, mabweni na vitabu.

 

Katika hatua nyingine Rais Jakaya Kikwete amesema yeye binafsi na kwa kushirikiana na Mkewe Mama Salma Kikwete watafuta wahisani watakao saidia ujenzi wa mabweni ya kulala wanafunzi wa shule ya sekondari ya Natta iliyoko wilayani Serengeti.

 

Rais alitoa ahadi hiyo mara baada ya kufungua bweni la wasichana lenye uwezo wa kulaza wanafunzi  wa kike 48. Bweni ambalo limepewa jina la Mama Salma Kikwete.

 

Rais alisema kuwa watajadiliana na mke wake namna ya kuwapata wafadhili hao ambao alisema kuwa baadhi yake ni marafiki zao, ili kuwawezesha watoto  hasa wa kike kwa kuanzia na baadaye wa kiume ili wapate malazi yanayoeleweka shuleni hapo.

 

Shule hiyo imejengwa kwa ushirikiano wa wananchi wa eneo  hili, halmashauri, wadau mbalimbali akiwamo mbunge wa jimbo hilo, Mhe. Wanyancha.

 

“Nitakwenda kumweleza mke wangu, kwamba kuna bweni huko limepewa jina lako, lakini si wanafunzi wote wa kike wamepata mahali pa kulala hivyo atafute njia ya kufanikisha ujenzi kwa ajili ya wanafunzi waliobakia. Lakini nitamwambia yeye si mama wa wanafunzi wa kike peke yake, bali hata wa kiume ni mama yao hivyo nao asiwasahau,” alisema Rais, kauli iliyowafurahisha wananchi.

 

Kuhusu ombi la kuipatisha shule hiyo umeme, Rais alisema kuwa atakwenda kuzungumza na Waziri wa Nishati na Madini kuangalia uwezekano wa kutenga fedha kutoka fungu la umeme vijiji ili kuiwezesha shule hiyo kupata umeme.

 

Jumla ya shilingi milioni 48 zinahitaji kuvuta umeme na kuupeleka shuleni hapo. Umeme wa gridi ya taifa unapita karibu kabisa na shule hiyo, lakini unahitajika kubadilishwa nguvu zake ili uweze kutumika shuleni hapo.

 

Rais amerejea jijini Dare s Salaam leo baada ya kumaliza ziara yake mkoani hapa.

 

mwisho