PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

Fax. No. 255-22 2113425                                              The State House,                                  

Tel: 255-22-2116539/2116913                                      P.O. Box 9120,

                                                                                           DAR ES SALAAM.

 

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

 

RAIS KIKWETE APOKEA HATI ZA UTAMBULISHO

 

 

Rais Jakaya Mrisho Kikwete leo 16 Oct. 2006 amepokea hati za utambulisho za mabalozi wanne watakaowakilisha nchi zao hapa Tanzania.

 

Mabalozi hao ni Mabwana Leandre Amuri Bagenwanubusa wa Burundi,  Boaz Kidiga Mbaya wa Kenya, Francesco Katania wa Italia na  Makoto Ito wa Japan.

 

Mara baada ya kupokea hati zao, Rais amefanya mazungumzo na mabalozi hao na kueleza azma yake ya kushirikiana na nchi hizo katika nyanja za kisiasa, kiuchumi na kibiashara.

 

“Burundi ni nchi jirani, ni lazima tuishi kwa pamoja kwa kushirikiana, napenda pia mjue kuwa barabara, bandari na anga la Tanzania ni vyenu pia, tutahakikisha mnapata fursa ya kuzitumia ili muwe na uhakika wa kuijenga Burundi” Rais amemweleza Balozi Bagenwanubusa ambaye naye ameishukuru Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika kutatua mgogoro wa Burundi.

 

Amewataka pia mabalozi wa Italia na Japan kudumisha ushirikiano baina ya nchi hizi na kueleza kuwa Tanzania imefaidika na misaada ya nchi zao katika sekta mbalimbali.

 

Amezitaka nchi hizi kuendelea kuisaidia Tanzania hasa katika kipindi hiki  ambapo Tanzania imeazimia kuleta mabadiliko katika kilimo, barabara, maji  umeme, na Afya

 

“Nchi yetu bado inahitaji misaada, Tanzania ingependa nchi zetu zishirikiane zaidi katika biashara na hasa vitega uchumi, kwani nia yetu ya kuleta maendeleo ni kubwa sana” Rais amesema na kumweleza balozi wa Japan kwamba nchi hii inaagiza magari na vifaa mbalimbali vya umeme kutoka Japan lakini kiwango cha uwekezaji cha Japan hapa Tanzania ni kidogo sana.

 

“Sekta ya uwekezaji ndiyo pekee nionayo kuwa Japan haijajitokeza sana hapa Tanzania.  Ingekuwa vyema mkatilia mkazo eneo hili ambalo ni muhimu sana kwetu.  Nakushauri ulitizame kwa makini zaidi eneo hili.”  Rais amemwasa balozi huyo mpya wa Japan, Bwana  Ito na kueleza kuwa sekta zingine ambazo nchi hiyo inaweza kuanzisha vitega uchumi ni pamoja na utalii, madini na miundo mbinu.

 

Mwisho

 

Ikulu

16/10/2006