DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail:  ikulumawasiliano@yahoo.com

              press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Alhamisi, Mei 20, 2010, amekutana na kufanya mazungumzo na Baroness Catherine Ashton, Waziri wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Ulaya (EU) na Makamu wa Rais wa Tume ya Ulaya.

 

Katika mkutano huo uliofanyika Ikulu, Dar es Salaam, viongozi hao wawili wamezungumzia masuala mbalimbali ya kimataifa, na yale yanayohusu uhusiano kati ya Tanzania na EU.

 

Aidha, viongozi hao wawili wamejadiliana kuhusu jinsi gani Tanzania na EU zinavyoweza kushirikiana katika kupambana na uharamia katika eneo la Bahari ya Hindi.

 

Baroness Catherine Ashton ambaye aliwasili nchini jana akitokea Kenya yuko njiani kwenda Seychelles kuhudhuria Mkutano wa Mawaziri wa Mwambao wa Afrika Mashariki utakaojadili jinsi ya kupambana na uharamia wenye chimbuko lake kwenye Pwani ya Somalia.

 

Mkutano huo uliopangwa kuanza kesho, Ijumaa, Mei 21, 2010, umeandaliwa na Serikali ya Seychelles kwa kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Mambo ya Nje ya EU na Ofisi ya Makamu wa Rais wa Tume ya Ulaya.

Katika mkutano wake na Baroness Catherine Ashton, Rais Kikwete amesema kuwa Serikali yake inafurahishwa na kuridhishwa na uhusiano kati ya Tanzania na EU katika maeneo mbalimbali.

 

EU imekuwa inasaidia maendeleo ya Tanzania kupitia msaada wake katika Bajeti ya Tanzania ambako maeneo yanayolengwa ni sekta za usafirishaji, kilimo, utawala bora, nishati, tabianchi, Mpango wa Taifa wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini wa MKUKUTA kwa upande wa Tanzania Bara na MKUZA kwa upande wa Tanzania Visiwani.

 

EU pia imekuwa inatoa misaada yake kwa taasisi na wabia wengine wa shughuli za maendeleo nchini wasiokuwa Serikali.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

20 Mei, 2010