UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116539

E-mail: press@ikulu.go.tz

Website:  www.mawasilianoikulu.go.tz  

Fax: 255-22-2113425

 

Coat of Arms

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA MHARIRI WA GAZETI LA UHURU

 

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete atakuwa miongoni mwa viongozi wa nchi wanachama wa Jumuia ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) watakaohudhuria mkutano wa dharura wa wakuu wa nchi hizo unaofanyika kesho, Ijumaa, Mei 20, 2011.

 

Rais Kikwete na ujumbe wake wameondoka nchini jioni ya leo, Alhamisi, Mei 19, 2011, kwenda Namibia, Windhoek, kuhudhuria mkutano huo wa siku moja.

 

Mkutano huo utakaofanyika chini ya uenyekiti wa Rais wa Nambia, Mheshimiwa Hifikepunye Pohamba ambaye pia ni mwenyekiti wa sasa wa SADC utajadili ajenda nne.

 

Ajenda hizo ni pamoja na kujadili hali ya kisiasa na kiusalama ya Jamhuri ya Madagascar ambayo ni nchi mwanachama wa SADC.

 

Nchi hiyo imekuwa katika mzozo mkubwa wa kisiasa kufuatia mapinduzi ya uongozi yaliyomwondoa Rais Marc Ravalomanana madarakani. Mapinduzi hayo yaliongozwa na meya wa zamani wa jiji la Antananarivo, Mheshimiwa Andry Rajoelina akisaidiwa na jeshi la nchi hiyo na ambaye anatawala nchi hiyo kwa sasa.

 

Mkutano huo pia utajadili hali ya kisiasa na kiusalama ya nchi nyingine mwanachama wa SADC, Jamhuri ya Zimbabwe, ambayo nayo imekuwa inakumbwa na mzozo wa kisiasa tokea mwanzoni mwa mwaka 2000.

 

Pande zinazovutana katika Zimbabwe zilikubaliana kutia saini makubaliano ya Global Political Agreement (GPA) iliyounda Serikali ya Kitaifa baina ya vyama vitatu vikuu vya siasa nchini humo Septemba 2008.  Vyama hivyo ni ZANU-PF, MDC-T na MDC-M lakini katika siku za karibuni, Serikali hiyo imeanza kukumbwa na vikwazo mbalimbali.

 

Viongozi hao pia watapokea na kujadili ripoti ya kikosikazi cha mawaziri wa nchi za SADC kuhusu uwezekano wa kuundwa kwa eneo moja kubwa huru la biashara katika nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC), COMESA na SADC.

 

Aidha, wakuu hao watapokea na kujadili ripoti ya mawaziri wa Sheria na Wanasheria wakuu wa nchi za SADC kuhusu Baraza la Usuluhishi la SADC. 

 

SADC ina nchi wanachama 15 ambao idadi ya wakazi wake inakadiriwa kufikia milioni 257.7.  Nchi hizo ni Tanzania, Angola, Botswana, Lesotho, Afrika Kusini, Mozambique, Malawi, Madagascar, Namibia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Mauritius, Swaziland, Seychelles, Zambia na Zimbabwe.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

19 Mei, 2011