PRESS SECRETARY TO THE PRESIDENT

 

Fax. No. 255-22 2113425                                   The State House,                         

Tel: 255-22-2116539/2116913                          P.O. Box 9120,

                                                                                DAR ES SALAAM.

E-mail:  press@ikulu.go.tz

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Na Mwandishi maalum

22/9/2006

NewYork

 

 

 

Tanzania ni  moja  kati ya nchi tano zitakazonufaika na msaada wa Dola za Kimarekani milioni 250 zitakazo tolewa  kupitia  Mpango wa Rais Billi  Clinton  unaoshughulikia matatizo mbalimbali yanayoikabili dunia hususani nchi zinazoendelea, maarufu kama  Clinton Global Initiative (CGI).

 

Rais Mstaafu wa Marekani, Bill Clinton  ambaye ndiye mmiliki wa mpango huo, alitangaza  mbele ya Rais Jakaya Kikwete na  viongozi mbalimbali wa serikali, mashirika mkubwa na biashara na taasisi zisizo za kiserikali, kwamba Tanzania  ni nchi mojawapo itakayonufaika na fedha hizo.

 

Aliyasema hayo wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa mwaka  wa siku tatu wa taasisi yake,  ulioanza juzi hapa NewYork , Marekani.

 

Rais huyo Mstaafu wa Marekani, alisema kuwa fedha hizo ambazo zimetolewa na  Bangladesh Royal Advancement Committee (BRAC), kama mchango wake kwa taasisi yake, zitaelekezwa  katika uendelezaji wa sekta ya kilimo, upatikanaji wa huduma  za afya na udhibiti wa malaria, uendelezaji wa elimu, kukuza ujasiriamali kwa  kupitia mipango endelevu ya huduma za fedha.

 

Nchi nyingine zitakazonufaika na fedha hizo ni  Kenya, Nigeria, Uganda na Sudani.

 

Katika mkutano huu wa siku tatu wa taasisi hiyo ya Bill Clinton,  ambao pia ulihudhuriwa na Mke wa Rais wa Marekani Laura Bush na kutangaza mikakati ya upatikani wa maji safi na salama kwa nchi za Afrika.

 

Wajumbe  wa mkutano huo ambao   walipata  muda wa kujadiliana  na kubadilishana mawazo kuhusu kuhusu mada kuu nne zilizowasilishwa kwa nyakati tofauti mbele yao .

 

Mada hizo ni  pamoja na  mabadiliko  ya hali ya hewa na uhifadhi  wa  mazingira, afya, maji safi na maji taka, upunguzaji wa umaskini, na tofauti za mitazamo ya kidini.

 

Rais Jakaya Kikwete alishirikia katika mjadala uliozungumzia  afya, upatikanaji  wa maji safi na salama, na athari za maji taka na changamoto zake katika kukabiliana na matatizo hayo.

 

Akitoa mchango wa mawazo yake kuhusu mada hiyo, Rais Jakaya Kikwete alisema kwamba, suala la upatikanaji wa maji safi na salama, ni moja ya mambo yanayopewa umuhimu wa peke na serikali yake.

 

Aliwaeleza wajumbe waliokuwa wakiijadili mada hiyo, kwamba serikali ya Tanzania chini ya uongozi wake, imejiwekea mipango na sera za kukabiliana na uhaba mkubwa wa matatizo ya upatikanaji wa maji safi na salama hususani kwa wananchi wa vijijini.

 

Alisema kuwa changamoto kubwa kwa serikali yake iko  katika upatikanaji wa raslimali kwa maana ya fedha na rasilimali watu.

 

Rais Kikwete alibainisha kwamba, upatikanaji wa raslimali za kutekeleza mikakati ya kuwapatia  Watanzania maji  safi na salama zikipatikana ni wazi kwamba  idadi ya wananchi watakaopata huduma hiyo itaongezeka.

 

Alitoa mfano kuwa wanawake na watoto wa kike ndio ambao wakitumia muda wao mwingi katika kutafuta maji  kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

 

“Tatizo letu sisi haliko katika mpango mkakati na sera, hivyo vyote tunavyo, kinachotukwamisha ni uwezo wa kifedha na kimtaji wa kukabiliana na changamoto hiyo, na ndio maana tumekuwa tukiomba nchi wahisani na wadau wa maendeleo watusaidie.

 

Alisema kuwa ikiwa uwekezaji  katika sekta hiyo utakuwa ni mkubwa ni wazi kwamba utatoa nafuu kubwa kwa wanawake na watoto wa kike ambao wamekuwa wakitumia muda wao mwingi kutafuta maji.

 

Aidha Rais Kikwete alisema kuwa utolewaji wa elimu kuhusu matumizi bora na endelevu ya maji inahitajika.

 

Rais Kikwete alifafanua kwamba, ni jambo lisilo na mjadala kwamba, lazima kuwapo na ushirikiano miongoni mwa wadau wote wanaotumia raslimali maji, yaani wale wanaoitumia raslimali hiyo kwa matumizi ya majumbani na wale wanaotumia kwa kilimo.

 Alibainisha kwamba  moja ya changamoto kubwa inayoikabili serikali yake na nchi zinazoendelea kwa ujumla ni katika kuwashawishi nchi wahisani na wafadhili kuwekeza katika sekta ya maji.

 

Alisema kuwa wadau wengi wa maendeleo wamekuwa wakikazania kuwekeza katika sekta za afya, elimu na miundombinu na kusahau au kutoipa umuhimu wa pekee sekta ya maji.

 

Alisema kuwa changamoto kubwa zinazozikabili nchi zinazoendelea, Tanzania ikiwamo, ni ukosefu wa mitaji, na raslimali watu inayoweza kutoa mchango wa kukabiliana na tatizo la uhaba wa maji safi, salama na uhifadhi wa maji taka.

 

 

 

Nao washiriki wengine wa mjadala huo wa afya, maji safi na salama na maji taka, walibainisha kwamba huu ni wakati muafaka kwa wadau mbalimbali, wakiwamo viongozi wa seriakali ya Marekani na mashirika makubwa ya biashara kukubali kubadilika kimawazo na kuwekeza katika sekta ya maji,

 

Washiriki wa mdahalo huo, walibainisha umuhimu wa sekta ya umma na sekta binafsi kushirikiana  katika kulitafutia ufumbuzi tatizo la uhaba wa maji safi na salama, kwa  nchi zinazoendelea.

 

Walionya kwamba kutokana na taarifa mbalimbali za utafiti, kuwa vita kuu ya dunia inayoweza kutokea haitahusu kugombea mafuta bali itahusu vita  vya kugombea maji.

 

Jumla ya Dola za Kimarekani milioni 350 zimeahidiwa kutolewa na makampuni mbalimbali ya kimataifa kusaidia taasisi ya Bill Clinton ili iweze kutekeleza majukumu yake ya kuzisaidia nchi maskini.

 

Naye mshiriki mmoja wa mjadala wa ajenda hiyo, alisema kuwa wakati umaefika sasa wa kuzitaka nchi zilizoendelea, Marekani ikiwamo, kubadilika kifikra na kuwekeza  katika usambazaji wa raslimali maji katika maeneo ya vijijini na mijini.

 

Alibainisha kwamba kama  juhudi za makusudi hazitafanyika katika  usimamizi wa utoaji wa huduma hiyo ya maji, basi vita kuu nyingine itakayofuata haitakuwa ya mafuta bali maji.

 

 

Mwisho