DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

MHESHIMIWA Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amewaagiza Wakuu wa wilaya zote nchini kuendesha zoezi la msako wa nyumba kwa nyumba, ili kubaini watoto waliofaulu kuingia sekondari mwaka huu lakini mpaka sasa wameshindwa kuanza masomo yao.

 

Aidha, Mheshimiwa Rais, ameagiza kuwa katika zoezi hilo, wazazi wote ambao wanawazuia watoto wao kuanza masomo ya sekondari kwa sababu yoyote ile wahojiwe kwa nia ya kuhakikisha kuwa wanawapeleka watoto wao shule mara moja.

 

Rais Kikwete alitoa maagizo hayo juzi, Jumanne, Mei 11, 2010 mjini Masasi wakati akipatiwa maelezo ya Maendeleo ya Mkoa wa Mtwara baada ya kuwa ameambiwa kuwa asilimia 35.6 ya watoto wote 12,843 walioshinda mtihani wa darasa la saba mwaka jana na kuchaguliwa kuingia sekondari katika mkoa wa Mtwara, hawajaripoti shuleni mpaka sasa.

 

Rais Kikwete aliambiwa kuwa ni asilimia 64 tu, yaani watoto 8, 278 walioripoti na kuanza masomo ya sekondari wakati watoto 4,565 hawajaripoti shuleni na hawajulikani waliko.

 

Katika idadi hiyo, Wilaya ya Mtwara ndiyo inayoongoza kwa asilimia 54, ikifuatiwa na Nanyumbu asilimia 48, Masasi asilimia 35, Tandahimba asilimia 32, Mikindani asilimia 22 na Newala asilimia 21.

Rais Kikwete aliambiwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali (mst) Anatoli Tarimo kuwa baadhi ya sababu zilizowazuia watoto hao kupiga ripoti shuleni ni pamoja na baadhi yao kupata mimba, kuozwa ama kuzuiwa na wazazi wao kwenda shule.

 

Mara baada ya kupewa takwimu hizo, Rais Kikwete aliagiza:  “Hizi takwimu ni za juu sana.  Haiwezekani tukaendelea kuwadhulumu watoto wetu maisha bora kwa kuwazuia wasiende shule wakati shule zipo, nafasi zipo na kila kitu kipo.”

 

Aliendelea kutoa maelekezo Mheshimiwa Rais: “Tafuteni majina ya watoto hawa wote, wazazi wao waitwe, wajieleze na kama hawana majibu wawajibishwe. Afuatwe mtoto mmoja baada ya mwingine bila kumwacha yoyote. Na njia rahisi ufanywe msako wa nyumba kwa nyumba, kama ilivyokuwa zamani wakati wa kukusanya kodi,” alisema Rais Kikwete na kuongeza:

 

“Wazazi wa watoto hao wahojiwe siyo kwa nia ya kutaka kujua sababu gani zinazuia wasiwapeleke watoto shule, bali kwa nia ya kuhakikisha kuwa watoto wanapelekwa shuleni mara moja. Kazi hii ifanyike katika kila wilaya nchini na isimamiwe na mkuu wa wilaya katika kila wilaya ambako yapo matatizo ya namna hii.”

 

Rais Kikwete alipewa ripoti hiyo ya maendeleo ya Mkoa wa Mtwara, ikiwa sehemu ya shughuli zake wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani humo ambako miongoni mwa mambo mengine jana, Jumatano, Mei 12, 2010, alishirikiana na Rais wa Mozambique, Mheshimiwa Emilio Armando Guebuza, kufungua rasmi daraja jipya na zuri linalounganisha Tanzania na Mozambique kwenye Mto Ruvuma.

 

Daraja hilo lenye urefu wa mita 720, na lililogharimu kiasi cha shilingi bilioni 34 zilizotolewa kwa usawa na Serikali za Tanzania na Mozambique, limejengwa kutoka eneo la Mtambaswala kwa upande wa Tanzania kwenda eneo la Negomane upande wa Mozambique.

 

Mkataba wa ujenzi wa daraja hilo ulisainiwa Oktoba 16, 2005, na ujenzi wenyewe ulianza rasmi Novemba 10, 2005 na kukamilika Novemba 2009.

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

13 Mei, 2010