DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

 

Telephone: 255-22-2114512, 2116898

E-mail: press@ikulu.go.tz             

Fax: 255-22-2113425

 

 

PRESIDENT’S OFFICE,

      THE STATE HOUSE,

       P.O. BOX 9120,  

DAR ES SALAAM.

Tanzania.

 

 

 

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 

Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amesema kuwa ni dhamira ya Serikali yake kuendelea kuongeza bajeti ya kupambana na ukimwi nchini, ili kuiwezesha Serikali kuwa na uwezo wa kutosha kuhudumia wahanga na waathirika wote wa ugonjwa huo.

 

Aidha, Rais Kikwete ameishukuru Serikali ya Marekani kwa misaada na juhudi zake kubwa kuisaidia Tanzania kupambana na ugonjwa wa ukimwi kupitia Mpango wa Dharura wa Rais Kupambana na Ukimwi (PEPFAR).

 

Rais Kikwete ameeleza msimamo huo wa Serikali yake wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mratibu wa Kimataifa wa Serikali ya Marekani wa Mapambano dhidi ya Ukimwi, Mheshimiwa Balozi Dk. Eric Goosby, Ikulu, Dar es Salaam, leo, Jumatatu, Mei 17, 2010.

 

Rais Kikwete amemwambia Balozi Goosby kuwa Serikali ya Tanzania imedhamiria kuhakikisha kuwa inaongeza uwezo wake wa kifedha na kibajeti katika kupambana na ukimwi.

 

Kikwazo cha kuongeza bajeti ya kupambana na ukimwi siyo matokeo ya dhamira ya kisiasa. Dhamira ya kisiasa ni kubwa sana. Tatizo ni uwezo mdogo wa taifa letu tu na umasikini wa nchi yetu,” amesema Rais Kikwete na kumweleza kwa undani hatua ambazo Serikali imechukua kukabiliana na ugonjwa wa ukimwi na hatua zilizochukuliwa kuongeza bajeti ya sekta ya afya ambayo sasa inashikilia nafasi ya tatu kwa ukubwa baada ya sekta za elimu na miundombinu.

 

Naye Balozi Goosby amemhakikisha Rais Kikwete msimamo wa Rais Barack Obama wa Marekani na Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo,  Mama Hillary Clinton kwa kuendelea kuinga mkono Tanzania katika mapambano yake dhidi ya ukimwi kwa sababu nchi hiyo imekuwa mfano katika Afrika katika kupambana na ugonjwa huo.  Marekani pia inaisaidia Tanzania kupambana na ugonjwa wa malaria kupitia Mpango wa Rais dhidi ya Malaria (PMI).

 

Nimekuja kuthibitisha dhamira ya Rais Obama na Waziri Clinton ya kuendelea kuunga mkono jitihada za Tanzania katika kupambana na ukimwi. Chini ya PEPFAR kiasi cha Watanzania 200,000 wanapata dawa za kurefusha maisha.”

 

Balozi Goosby ambaye alifuatana na Balozi wa Marekani katika Tanzania, Mheshimiwa Alfonso E. Lenhardt, yuko nchini kuhudhuria Mkutano wa Mwaka wa PEPFAR ambao umepangwa kufanyika kwenye Kituo cha cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC) kuanzia keshokutwa, Jumatano, Mei 19, 2010.

 

Mkutano huo umepangwa kumalizika Ijumaa, Mei 21, 2010, umetanguliwa na mikutano mingi ya wataalam ambayo ilianza tokea Alhamisi iliyopita, Mei 13, 2010.

 

Mkutano huo wa Arusha unawakutanisha kiasi cha maofisa 400 wa Serikali ya Marekani ambao wanashiriki katika shughuli za kupambana na ugonjwa wa ukimwi katika nchi 31 duniani.

 

Balozi Goosby ambaye amekuwa katika shughuli za kupambana na ukimwi kwa miaka 25 sasa, amemwambia Rais Kikwete: “Mkutano huu wa mwaka unalenga kujadili, kutafakari na kutangaza mafanikio ya mpango wa PEPFAR siyo tu katika Tanzania lakini katika nchi nyingine za Afrika na dunia ambako yamekuwepo mafanikio makubwa ya mpango huu. Pia mkutano huo utaonyesha mafanikio ya ushirikiano wa Tanzania na Marekani katika kupambana na ugonjwa huu.”

 

Imetolewa na:

 

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,

Ikulu,

DAR ES SALAAM.

 

17 Mei, 2010